Tumia Wakati Wako kwa Hekima Katika Huduma
Mwaka wa utumishi wa 2014, Mashahidi wa Yehova walitumia saa 1,945,487,604 katika huduma na hilo linaonyesha wazi kwamba tumeazimia kuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wa Yehova! (Zab. 110:3; 1 Kor. 15:58) Kwa kuwa “wakati uliobaki umepungua,” je, tunaweza kutumia wakati wetu wenye thamani katika huduma ili kuwafikia wengi zaidi?—1 Kor. 7:29.
Tunahitaji kubadilikana ili tuweze kutumia wakati wetu kwa hekima katika huduma. Kwa mfano, ikiwa kwa kawaida saa moja au zaidi hupita bila kuzungumza na mtu yeyote katika aina fulani ya huduma, je, unaweza kufanya mabadiliko ili uweze kuwapata watu wengi zaidi na kuzungumza nao? Hali hutofautiana eneo moja hadi lingine. Hata hivyo, madokezo yafuatayo yanaweza kukusaidia kutumia wakati kwa hekima na hivyo kuepuka ‘kupiga hewa.’—1 Kor. 9:26.
Kuhubiri Nyumba kwa Nyumba: Kwa miaka mingi, wahubiri wamekuwa na kawaida ya kuanza utumishi asubuhi kwa kuhubiri nyumba kwa nyumba. Hata hivyo, kwa sababu watu wengi huwa kazini muda huo, kwa nini usijaribu kuhubiri nyumba kwa nyumba alasiri au jioni, wakati ambapo watu wengi zaidi wanapatikana nyumbani na wanapumzika? Kuhubiri barabarani au kwenye maeneo ya biashara wakati wa mchana kunaweza kuwa na matokeo mazuri zaidi.
Kuhubiri Hadharani: Meza na vigari vyenye machapisho vinapaswa kuwekwa katika eneo lenye wapita-njia wengi lililo katika eneo la kutaniko. (Ona Huduma Yetu ya Ufalme ya Julai 2013, uku. 5.) Ikiwa wapita njia wanapungua katika eneo lililopangwa, Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko inaweza kuamua kwamba meza au vigari vyenye machapisho vihamishiwe kwenye eneo lingine lenye wapita-njia wengi zaidi.
Ziara za Kurudia na Mafunzo ya Biblia: Je, unaweza kupanga kufanya ziara za kurudia na kuongoza mafunzo ya Biblia, nyakati ambazo hupati matokeo unaposhiriki katika aina nyingine za utumishi? Kwa mfano, ikiwa unapata matokeo mazuri unaposhiriki utumishi wa nyumba kwa nyumba Jumamosi asubuhi, je, unaweza kufanya mipango ya kuongoza mafunzo yako ya Biblia mchana au jioni?
Ingawa ni kweli kwamba tunaweza kuhesabu muda tunaotumia wakati wowote tunapohubiri, shangwe yetu huongezeka tunapopata matokeo mazuri. Ikiwa unaona kwamba hupati matokeo unaposhiriki aina moja ya utumishi, katika muda fulani hususa, jaribu aina nyingine ya utumishi. Sali kwa Yehova, “Bwana wa mavuno,” ili akupe mwongozo wa jinsi ya kutumia wakati wako kwa hekima katika huduma!—Mt. 9:38.