Wameweka Mfano Mzuri wa Uaminifu
1 Utumishi wa upainia wa pekee ulianzishwa ukiwa sehemu ya utumishi wa wakati wote katika mwaka wa 1937. Wanaume na wanawake wenye uwezo na uzoefu katika huduma ya Kikristo walikubali kwa hiari kutumikia mahali popote ambapo tengenezo lingewaomba waende. Sasa, baada ya miaka mingi, mapainia wa pekee wanaendelea kuweka mfano wa uaminifu unaopaswa kuigwa.—Ebr. 6:12.
2 Waliongoza: Mwanzoni, mapainia wa pekee waliongoza katika kazi ya kuhubiri kwa kutumia kinanda cha gramafoni kwenye mlango wa mwenye nyumba. Pia walitumia habari iliyorekodiwa kuwa msingi wa mazungumzo ya Biblia walipofanya ziara za kurudia. Hilo lilifanywa katika majiji makubwa ambako tayari kulikuwa na makutaniko. Baadaye, mapainia wa pekee walitumwa katika maeneo yaliyo na uhitaji mkubwa wa wahubiri wa Ufalme. Waliwafuatia watu wote waliopendezwa na wakaongoza mafunzo ya Biblia. Kwa sababu ya jitihada zao, mamia ya makutaniko yalianzishwa. Kazi yao ya kueneza habari njema ilichangia sana upanuzi wa tengenezo unaoonekana leo. (Isa. 60:22) Mapainia wa pekee wanaendelea kutimiza fungu muhimu katika kueneza habari njema “katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.”—Kol. 1:23.
3 Wanastahili Kuigwa: Kuna mapainia wa pekee ambao wamekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa makumi ya miaka. Katika miaka hiyo, imani ya wanaume na wanawake hao waaminifu imeboreshwa kupitia hali mbalimbali. (1 Pet. 1:6, 7) Wamekuwa tayari kudhabihu mali zao ili watumike katika maeneo yenye uhitaji wa pekee. Wengine wao sasa wana umri mkubwa na wanakabili matatizo ya afya, au wanakumbwa na matatizo mengine. (2 Kor. 4:16, 17) Hata hivyo, wanaendelea “kusitawi wakati wa kuwa na kichwa chenye mvi.” (Zab. 92:14) Wanamtumaini Yehova nao wanapokea baraka zake.—Zab. 34:8; Met. 10:22.
4 Kwa kweli, mapainia wa pekee wanastahili kupongezwa kwa uchangamfu. Ikiwa una pendeleo la kuwa na mapainia wa pekee katika kutaniko lenu, tumia nafasi hiyo kushirikiana nao na unufaike kutokana na uzoefu wao. Onyesha unathamini utumishi wao wakiwa wahubiri wa Ufalme wenye uaminifu. Msimamo wao imara na ukutie moyo. Wote wanaoiga imani yao wanaweza kufurahia upendeleo wa Yehova na baraka zake kwa kuwa wale “wanaotenda kwa uaminifu ni furaha kwake.”—Met. 12:22.