Onyesha Unawajali Watu Kikweli —Kwa Kuhubiri Bila Ubaguzi
1 Katika maono, nabii Yohana aliona malaika anayeruka katikati ya mbingu akitangaza habari njema kwa watu wa “kila taifa na kabila na lugha na watu.” (Ufu. 14:6) Je, tunafuata mwongozo wa malaika huyo kwa kuhubiri bila ubaguzi? Bila kujua, huenda tukawa na maoni yenye ubaguzi. Mtazamo wetu kuhusu watu tunaokutana nao unaweza kuathiri jinsi tunavyowahubiria habari njema. Hivyo, tunapaswa kudhihirisha sifa ya upendo na kuwajali watu kikweli tunapowahubiria wale walio na malezi tofauti.
2 Fikiria Eneo Lenu: Je, kuna wahamiaji au wakimbizi katika eneo lenu? Ni rahisi kuwapuuza. Chukua hatua ya kuwatafuta na ujitahidi kuwafahamu zaidi. Wana mahitaji na mahangaiko gani, wana mapendezi gani, wanaogopa na kuchukia nini? Jitahidi kubadili njia yako ya kuhubiri habari njema kulingana na hali yao. (1 Kor. 9:19-23) Sawa na mtume Paulo, tunapaswa kuhisi tuna wajibu wa kumhubiria habari njema kila mtu katika eneo letu kutia ndani wale wanaotoka nchi za kigeni, wale wenye utamaduni tofauti na wetu, wale wanaozungumza lugha tofauti, na wale walio matajiri sana.—Rom. 1:14.
3 Hata hivyo, unaweza kumhubiriaje mtu anayezungumza lugha ya kigeni? Kitumie vizuri kijitabu Good News for People of All Nations. Pia unaweza kubeba trakti na broshua za lugha zinazozungumzwa katika eneo lenu. (Ona Huduma Yetu ya Ufalme ya Julai 2003, uku. 4, fu. 2-3.) Isitoshe, wahubiri fulani wamejifunza salamu na utangulizi mfupi katika lugha nyinginezo. Mara nyingi watu hufurahi kumsikia mtu akijaribu kuzungumza nao katika lugha yao wenyewe, hata kama anajua maneno machache tu, na hilo linaweza kuwafanya wapendezwe na habari njema.
4 Mwige Yehova: Tunapowahubiria watu wa malezi mbalimbali, tunamwiga Mungu wetu asiye na ubaguzi, Yehova, “ambaye mapenzi yake ni kwamba watu wa namna zote waokolewe na kupata ujuzi sahihi wa kweli.”—1 Tim. 2:3, 4.