Warudie Wote Wanaopendezwa kwa Kadiri Fulani
1 Wengi wetu tumejifunza kweli kwa sababu mtu fulani aliona kwamba tunapendezwa na ujumbe wa Ufalme na akarudi bila kuchoka, pengine mara kadhaa ili kuchochea upendezi huo. Sisi pia tunapaswa kuwa na bidii ya kuwarudia wote wanaopendezwa kwa kadiri fulani. Kwa kweli, kufanya ziara za kurudia ni sehemu ya kazi yetu ya ‘kufanya wanafunzi.’—Mt. 28:19, 20.
2 Uwe Mtambuzi: Hata kama mtu hatakubali kichapo chochote, huenda uso wake, sauti, na maneno anayotumia yakaonyesha kwamba anapendezwa kwa kadiri fulani na ujumbe wa Ufalme. Hiyo ni sababu nzuri ya kumrudia mtu huyo. Ndugu mmoja alimrudia mtu fulani kwa majuma matano mfululizo pasipo mtu huyo kukubali kichapo chochote. Katika ziara ya sita, mtu huyo alikubali kichapo, na hatimaye funzo la Biblia likaanzishwa.
3 Ukiona mtu anapendezwa, mrudie haraka, pengine siku chache baadaye. Usimpe “yule mwovu” nafasi ya kunyakua kile ambacho kimepandwa moyoni mwa mtu huyo. (Mt. 13:19) Hakikisha kwamba umerudi wakati hususa ulioahidi kurudi.—Mt. 5:37.
4 Mahubiri ya Barabarani: Je, wewe hujitahidi kuwarudia wale waliopendezwa ulipowahubiria barabarani au isivyo rasmi? Unaweza kusema hivi baada ya mazungumzo yenu: “Nimefurahia mazungumzo yetu. Naweza kukupata wapi ili tuendeleze mazungumzo haya?” Inapofaa, huenda wahubiri fulani wakampa aliyependezwa namba yao ya simu nao wakamwomba yake. Huenda watu wasisite kukupa namba ya simu au anwani yao ikiwa wao hukuona ukihubiri mahali palepale kwa kawaida. Hata kama watakataa kukupa anwani yao, jaribu kuchochea upendezi wao unapokutana nao tena barabarani.
5 Sisi hufurahi tunapoona mimea ambayo tulimwagilia maji na kupalilia ikisitawi. Vivyo hivyo, tunaweza kupata furaha nyingi tukifanya ziara za kurudia na kuwasaidia watu wafanye maendeleo ya kiroho. (1 Kor. 3:6) Azimia kuwarudia wote wanaopendezwa kwa kadiri fulani.