Kujengana Tunapokuwa Katika Huduma
1 Sote tunathamini kupokea kitia-moyo kutokana na “neno linalosemwa wakati unaofaa.” (Met. 25:11) Tunaposhirikiana na wengine katika huduma, tunaweza kuhakikishaje kwamba mazungumzo yetu yanawatia moyo wengine?
2 Mazungumzo Yanayojenga: Kuzungumzia mambo ya kiroho tunaposhiriki katika kazi ya kuhubiri ni jambo lenye kujenga kama nini! (Zab. 37:30) Tunaweza kuzungumza kuhusu utangulizi wetu au kusimulia mambo yaliyoonwa yenye kutia moyo ambayo tulipata hivi karibuni katika utumishi wa shambani. (Mdo. 15:3) Je, tulijifunza jambo fulani lenye kupendeza katika usomaji wa Biblia wa kibinafsi, magazeti ya karibuni, au mkutano wa kutaniko? Tunaweza kuzungumzia habari iliyotolewa katika hotuba ya watu wote ambayo tulisikiliza hivi karibuni katika Jumba la Ufalme.
3 Huenda tukavunjika moyo mwenye nyumba fulani akitokeza kipingamizi tusichoweza kutatua. Tungenufaika kwa kutumia dakika chache baada ya kutoka katika nyumba hiyo kuzungumzia pamoja na mhubiri mwenzetu jinsi ya kushughulikia kipingamizi hicho wakati ujao, labda kwa kuchunguza kitabu Kutoa Sababu. Na ikiwa tulipendezwa na jambo fulani katika utangulizi wa mhubiri mwenzetu, tukimpongeza kwa unyoofu atatiwa moyo.
4 Chukua Hatua: Je, kuna wahubiri fulani katika funzo letu la kitabu ambao hatujahubiri pamoja nao hivi karibuni? Tukiwaomba waandamane nasi katika huduma tunaweza kuwa na “ubadilishanaji wa kitia-moyo.” (Rom. 1:12) Mapainia wa kawaida na wasaidizi wanathamini kufanya kazi pamoja na wengine hasa asubuhi na mapema na pia jioni, wakati ambapo wahubiri wengi hawashiriki katika huduma. Tunaweza kuwaunga mkono mapainia kwa kuandamana nao katika huduma. Je, kuna mhubiri fulani aliye na udhaifu wa kimwili unaomzuia asishiriki sana katika huduma? Kufanya mipango ili mhubiri huyo aandamane nasi, labda katika funzo la Biblia, kunaweza kuwa na manufaa.—Met. 27:17.
5 Nyakati zote pongezi na shukrani zinatia moyo, hata inapohusu mambo madogo. Tunapaswa kukumbuka jambo hilo tunaposhiriki pamoja na wengine katika huduma, kwa kuwa tunataka ‘kuendelea kujengana.’—1 The. 5:11.