Unaweza Kupata Utajiri!
1. Kwa nini ufikirie kufanya upainia wa kawaida?
1 Je, unajitahidi kupata uradhi na shangwe zaidi maishani? Je, unapata furaha na uradhi kwa kuwasaidia wengine? Je, unatamani kupanua utumishi wako kwa Yehova? Ikiwa umejibu ndiyo kwa swali lolote kati ya maswali hayo, basi unapaswa kufikiria upainia wa kawaida. Bila shaka, majukumu ya kutunza familia na majukumu mengine ya Kimaandiko, vilevile hali za kiafya na za kimwili zinapaswa kuzingatiwa.
2. Taja baadhi ya utajiri wa kiroho ambao mapainia wa kawaida wanapata.
2 Maandishi ya Sulemani yaliyoongozwa na roho yanaonyesha kwamba baraka ya Yehova inahusiana na utajiri wa kimwili. (Met. 10:22) Leo, baraka ya Yehova inaleta hasa utajiri wa kiroho. Mapainia wa kawaida wana utajiri mwingi sana wa kiroho. Kwa mfano, wanapata furaha kubwa zaidi ya kutoa ‘wanaponunua wakati’ kutoka kwa mambo yao ya kibinafsi ili kuwasaidia wengine. (Kol. 4:5; Mdo. 20:35) Yehova anaona na kuthamini kazi yao ya jasho na ya upendo. ‘Hazina hizo zilizo mbinguni’ hazitapoteza thamani kamwe. (Mt. 6:20; Ebr. 6:10) Zaidi ya hayo, mapainia wanapokuwa na ‘jicho rahisi’ na kumtegemea Yehova ili atosheleze mahitaji yao, uhusiano wao pamoja naye unaimarika zaidi.—Mt. 6:22, 25, 32; Ebr. 13:5, 6.
3. Kuna tofauti gani kati ya kufuatilia utajiri wa kiroho na kufuatilia utajiri wa kimwili?
3 Mara nyingi kufuatilia utajiri wa kimwili kunaongoza kwenye “tamaa nyingi za kijinga na zenye kudhuru.” (1 Tim. 6:9, 10; Yak. 5:1-3) Baraka ya Yehova haileti kamwe madhara. Kutumia kiasi kikubwa cha wakati wao katika huduma kunawasaidia mapainia wa kawaida kudumisha usawaziko wa kiroho na kukazia uangalifu mambo yaliyo ya maana zaidi. (Flp. 1:10) Ndugu mmoja aliacha kazi ya uinjinia iliyochukua wakati wake mwingi akawa painia. Alisema hivi: “Kazi yangu ya kimwili ilikuwa na mikazo mingi sana. Lakini upainia hauna mikazo yoyote. Sasa ninawasaidia watu na kuwafundisha kweli. Kuwafundisha watu kweli kumeniletea furaha na uradhi zaidi.”
4. Mapainia wa kawaida wanapata baraka gani wanapowapelekea wengine baraka?
4 Baraka kwa Wengine: Leo, kila mtu anakabili “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Watu kila mahali wanahitaji sana tumaini. Watangazaji wa Ufalme wanashangilia kuona kwamba watu waliokata tamaa wanaweza kupata tumaini wanapokubali habari njema. Mapainia wa kawaida wanapata shangwe kubwa hata zaidi kwa kuwa wanatumia saa zaidi ya 800 kila mwaka katika kazi hiyo inayookoa uhai!—1 Tim. 4:16.
5, 6. Unaweza kufanya nini ili uwe painia wa kawaida?
5 Je, umefikiria kwa uzito kutumika ukiwa painia wa kawaida? Huenda ukahitaji ‘kununua wakati unaofaa’ kutoka kwa mambo yasiyo ya maana sana. (Efe. 5:15, 16) Wengi wamefanya hivyo na kurahisisha maisha yao, na hilo limewawezesha kupunguza wakati wanaotumia katika kazi ya kimwili ili watumie wakati zaidi katika kazi ya Ufalme. Je, unaweza kupanga mambo yako ili ujiunge nao?
6 Mwombe Yehova akupe hekima ya kupanga ratiba inayofaa. (Yak. 1:5) Ni baraka gani unazoweza kutarajia ukifanya hivyo? Utapata utajiri mwingi sana wa kiroho! Yehova atakubariki pia kimwili kwa kukutimizia mahitaji yako. (Mt. 6:33) Wale wanaomjaribu Yehova kwa njia hiyo watapata “baraka hata kusiwe na uhitaji tena.”—Mal. 3:10.