Barua Kutoka kwa Ofisi ya Tawi
Wahubiri wa Ufalme Wapendwa:
Tulitiwa moyo sana kuona kwamba wakati wa msukosuko wa kisiasa uliotukia nchini Kenya hivi karibuni, ndugu wa makabila mbalimbali waliendelea kuonyesha upendo wao wa kindugu na baadhi yao waliwaficha ndugu wenzao wa makabila mengine. Ripoti zinaonyesha kwamba ingawa ndugu wachache walijeruhiwa katika ghasia hizo, hakuna ndugu aliyeuawa. Mliunga mkono kabisa jitihada za kutoa misaada. Kufikia sasa ndugu wengi ambao walikuwa wakimbizi wamerudi nyumbani kwao. Tunamshukuru Yehova kwa sababu ya kutusaidia kudumisha msimamo wetu wa kutounga mkono upande wowote ule, na kuendelea kushiriki kwa ukawaida katika huduma, kuhudhuria mikutano na makusanyiko.—Yoh. 15:19; Isa. 48:17, 18.
Ripoti ya Burundi inaonyesha kwamba katika mwaka uliopita wa utumishi nchi hiyo ilikuwa na kipindi kizuri sana cha utendaji wa kitheokrasi. Idadi ya wahubiri iliongezeka kwa asilimia 9 katika miezi tisa ya kwanza ya mwaka wa utumishi. Mnamo Aprili, asilimia 22 ya wahubiri wote walishiriki katika utumishi mbalimbali wa upainia. Majumba mawili ya Ufalme yanayoweza kutumiwa pia kwa ajili ya makusanyiko yalijengwa huko Rushubi na Kinyinya. Sasa kuna majumba manne ya aina hiyo. Lakini bado kuna kazi nyingi inayohitaji kufanywa katika utumishi wa Yehova.
Nchini Sudan, kazi ya kujenga makao ya wamishonari huko Juba inaendelea vizuri sana. Idadi kubwa ya ndugu waliokuwa wakimbizi sasa wamerudi Sudan na wamekaribishwa vizuri na makutaniko. Tunamshukuru Yehova kwa ajili ya uhuru wa ibada ambao tunaendelea kufurahia nchini Sudan.
Nchini Tanzania, akina ndugu walifurahi sana kuhamia kwenye ofisi mpya ya tawi katika miezi ya mwisho ya mwaka wa utumishi. Hapana shaka kwamba ofisi hiyo mpya itachangia ongezeko kubwa nchini humo.
Nchini Uganda, akina ndugu walifurahi sana kupokea toleo la watu wote la gazeti la Mnara wa Mlinzi linalochapishwa mara nne kwa mwaka katika lugha ya Kiganda, na linatoa ushahidi mzuri katika eneo. Ofisi za kutafsiri lugha ya Kiacholi na Kinyankore ambazo ziko katika maeneo zimewanufaisha sana watafsiri na makutaniko yanayotumia lugha hizo.
Tunafurahi kuwajulisha habari hizo. Pokeeni salamu zetu changamfu za upendo wa Kikristo, na tunawatakia mema.
Ndugu zenu,
Ofisi ya Tawi ya Burundi, Kenya, Tanzania, na Uganda