“Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
1. Kitabu “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu” kilichapishwa kwa kusudi gani?
1 Tunatamani sana kujifunza kitabu kipya “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu” kwenye Funzo la Biblia la Kutaniko kuanzia juma la Februari 23! Barua ambayo Baraza Linaloongoza lilimwandikia kila mtu anayempenda Yehova ilimalizia kwa maneno haya: “Tunatumaini kwamba kitabu hiki kitakusaidia kuendelea kutumia kweli maishani mwako na hivyo kujitunza mwenyewe ‘katika upendo wa Mungu . . . kwa kutazamia uzima wa milele.’—Yuda 21.”
2. Kitabu hiki kipya kitatusaidia katika mambo gani maishani?
2 Mambo Tunayotarajia: Kanuni za Biblia zinatumiwaje katika mambo kama vile burudani, urafiki, kuheshimu mamlaka, mazoea ya kibinafsi, ndoa, usemi, na desturi? Dhamiri zetu zitafinyangwa kulingana na viwango vya juu vya uadilifu vinavyoonyeshwa katika Neno la Mungu. (Zab. 19:7, 8) Kadiri tunavyoelewa njia ya Yehova ya kufikiri, ndivyo tunavyochochewa kumpendeza kwa kumtii katika sehemu zote za maisha yetu.—Met. 27:11; 1 Yoh. 5:3.
3. Kwa nini tunapaswa kufanya yote tuwezayo kutoa maelezo katika funzo la kila juma?
3 Jitahidi Kutoa Maelezo: Unapotayarisha, uwe na mradi wa kumsifu Mungu kati ya watu wake waliokutanika pamoja. (Ebr. 13:15) Kutaniko zima litajifunza kitabu hiki kipya pamoja. Kwa sababu sehemu tutakazojifunza zitakuwa fupi, hilo litatuwezesha sisi sote kutayarisha vizuri, na tutakuwa na uhakika tunapotoa maelezo kuhusu yale tuliyojifunza. Maelezo yetu mafupi yaliyotayarishwa vizuri yatawachochea wengine katika upendo na matendo mazuri, na yatatusaidia kuzungumzia habari hiyo kwa uchangamfu na kwa njia inayojenga. (Ebr. 10:24) Pia, tutafurikwa na shangwe tunapotoa maelezo kuhusu imani yetu.
4. Kwa nini ni muhimu tuzishike amri za Yehova?
4 Katika usiku wake wa mwisho duniani akiwa mwanadamu, Yesu alihusianisha kushika amri za Yehova na kukaa katika upendo wa Mungu. (Yoh. 15:10) Kitabu “Upendo wa Mungu” kitatuchochea tuazimie hata zaidi kutumia kanuni za Biblia kila siku maishani na ‘kujitunza katika upendo wa Mungu.’—Yuda 21.