Jitahidi Kuwahubiria Wanaume
1. Kuna uhitaji gani mkubwa kuhusiana na kushughulikia mambo ya Ufalme?
1 Kazi ya kuhubiri Ufalme inaposonga mbele katika siku hizi za mwisho, kuna uhitaji mkubwa wa ndugu wenye sifa zinazowastahilisha kuongoza. (Marko 4:30-32; Mdo. 20:28; 1 Tim. 3:1-13) Hata hivyo, katika maeneo fulani wanaume wachache zaidi kuliko wanawake wanakubali ujumbe wa Ufalme. Katika tamaduni fulani, wanaume wanawaachia wake zao majukumu ya kushughulikia mambo ya kiroho na kuwafundisha watoto mambo ya dini. Tunawezaje kuwasaidia wanaume wengi zaidi kutambua uhitaji wao wa kiroho na kujiunga nasi katika ibada ya kweli?
2. Jitihada za Paulo na Petro kuwahubiria wanaume zilikuwa na matokeo gani mazuri?
2 Zingatia Kuwahubiria Wanaume: Kichwa cha familia anapokubali kweli, mara nyingi anawavutia watu wengine wa familia yake wajiunge naye katika ibada safi. Kwa mfano, Paulo na Sila walimhubiria mlinzi wa jela walipokuwa wamefungwa kwa sababu ya kazi yao ya kuhubiri. Mwanamume huyo na watu wote wa nyumba yake walibatizwa. (Mdo. 16:25-34) Paulo alipohubiri jijini Korintho, “Krispo ofisa-msimamizi wa sinagogi akawa mwamini katika Bwana, na ndivyo na watu wote wa nyumba yake.” (Mdo. 18:8) Petro alitumwa na Yehova amhubirie Kornelio, ambaye alikuwa ofisa-jeshi ‘aliyemheshimu na kumwogopa Mungu.’ Kornelio, watu wake wa ukoo, na marafiki wake wa karibu walibatizwa.—Mdo. 10:1-48.
3. Kama Filipo, unaweza kumhubiria nani mwenye “cheo cha juu”?
3 Kuwahubiria wanaume wenye “cheo cha juu” kunaweza kuwa na matokeo mazuri sana. (1 Tim. 2:1, 2) Kwa mfano, malaika wa Yehova alimhimiza Filipo aongee na ‘mwanamume mwenye mamlaka’ ambaye alikuwa amewekwa juu ya hazina zote za malkia wa Waethiopia. Filipo alimsikia yule mwanamume ‘akisoma kwa sauti kubwa nabii Isaya,’ naye akamweleza habari njema kumhusu Yesu. Baada ya Mwethiopia huyo kuwa mwanafunzi, yamkini alihubiri habari njema alipokuwa njiani kurudi nchini kwao. Labda alimhubiria pia malkia na wale waliofanya kazi katika makao yake, watu ambao hawakuwa na fursa nyingi za kusikia habari njema.—Mdo. 8:26-39.
4. Tunawezaje kuwapa wanaume wengi zaidi fursa ya kusikia habari njema?
4 Jinsi ya Kuwapata Wanaume Wengi Zaidi: Kwa kuwa wanaume wengi wanafanya kazi mchana, je, ungeweza kupanga kuhubiri saa za jioni, mwishoni mwa juma, au katika sikukuu? Ukihubiri katika maeneo ya biashara kwa ukawaida huenda ukapata fursa za kuwahubiria wanaume ambao si rahisi kuwapata nyumbani. Ndugu wanaweza pia kujitahidi zaidi kuwahubiria wafanyakazi wenzao wa kiume. Akina ndugu wanaohubiri nyumba kwa nyumba, hasa katika eneo linalohubiriwa mara nyingi, labda wanaweza kuomba kuzungumza na mwanamume mwenye nyumba.
5. Dada anapaswa kufanya nini akimpata mwanamume anayependezwa na ujumbe wa Ufalme?
5 Dada anayempata mwanamume ambaye anapendezwa hapaswi kumrudia akiwa peke yake. Anaweza kuandamana na mume wake au ndugu au dada mwingine. Ikiwa yule mwanamume anayependezwa anafanya maendeleo, inafaa kumwomba ndugu anayestahili aendelee kumtembelea.
6. Tunawezaje kumwiga mtume Paulo ili ‘tuwapate watu wengi zaidi’?
6 Chagua Habari Zinazowapendeza Wanaume: Mtume Paulo aliwafikiria wasikilizaji wake na alibadili mazungumzo yake ili ‘awapate watu wengi zaidi.’ (1 Kor. 9:19-23) Hali kadhalika, sisi tunapaswa kujitahidi kutambua habari zinazoweza kuwavutia wanaume katika eneo letu na kujitayarisha kuzizungumzia. Kwa mfano, mahangaiko ya wanaume wengi yanahusu mambo kama vile matatizo ya uchumi, serikali bora, na usalama wa familia zao. Labda wanataka pia kujua kusudi la maisha, mambo yatakayoipata dunia yetu, na kwa nini Mungu anaruhusu kuteseka. Tukichagua kuzungumzia mambo yanayowahangaisha watu, wengi zaidi watakubali kusikiliza ujumbe wa Ufalme.—Met. 16:23.
7. Wote kutanikoni wanawezaje kuwasaidia waume wasio waamini wanaohudhuria mkutano?
7 Jitahidi Kuwasaidia Waume Wasio Waamini: Ingawa ni mwenendo mzuri wa dada zetu Wakristo ambao hasa unawavutia waume wao wasio waamini, ndugu kutanikoni wanaweza kuwasaidia pia. (1 Pet. 3:1-4) Mume asiye mwamini anapoandamana na mkewe mkutanoni, anapata ushahidi anapokaribishwa kwa uchangamfu. Yaelekea anapendezwa na kweli kwa kadiri fulani, na huenda akakubali kujifunza Biblia.
8. Ndugu wanawezaje kuwasaidia waume wasio waamini ambao hawapendezwi sana na kweli?
8 Kwa upande mwingine, baadhi ya waume hawapendezwi sana na Biblia mwanzoni, lakini hatimaye huenda wakakubali kuzungumzia Biblia pamoja na ndugu ambaye wanajihisi huru kuongea naye. Akina ndugu katika kutaniko moja, walipotembelea familia fulani mara kwa mara, walijitahidi kuongea na mume asiye mwamini kuhusu mambo ambayo walijua yanampendeza. Hatimaye waliweza kuzungumzia mambo ya Biblia pamoja naye, na sasa amebatizwa. Katika kisa kingine, ndugu alimsaidia mume asiye mwamini kujenga ukuta kuzunguka nyumba yake. Kwa sababu ndugu huyo alimsaidia kwa njia hiyo, yule mume alianza kujifunza Biblia. (Gal. 6:10; Flp. 2:4) Wewe ndugu Mkristo, je, unaweza kuwasaidia baadhi ya waume wasio waamini?
9. Kuzoezwa kwa wanaume Wakristo kunaweza kuwa na matokeo gani?
9 Kuwazoeza Wanaume Wakristo Wastahili Kupata Mapendeleo: Wanaume wanaokubali ujumbe wa Ufalme na kujitahidi kupata mapendeleo katika utumishi wa Yehova, huenda wakawa “zawadi katika wanadamu,” yaani, wazee Wakristo wanaotumia uwezo na nguvu zao kutumika katika makutaniko ya watu wa Yehova. (Efe. 4:8; Zab. 68:18) Wanaume hao wanachunga kutaniko kwa kupenda na kwa hamu. (1 Pet. 5:2, 3) Ndugu ulimwenguni pote wanafaidika sana na utumishi wao!
10. Jitihada za Anania za kumsaidia Paulo ziliwanufaishaje wengi zamani, na wengi wananufaikaje leo?
10 Kwa mfano, ijapokuwa Sauli alikuwa amewatesa Wakristo hapo awali, baadaye akawa “mtume kwa mataifa.” (Rom. 11:13) Kwa sababu ya kusikia habari mbaya kumhusu Sauli, mwanafunzi Anania alisita kumhubiria mwanzoni. Hata hivyo, Anania alitii maagizo ya Bwana na alizungumza na yule mwanamume ambaye baadaye akawa mtume na kuitwa Paulo. Kwa miaka mingi, maelfu ya watu walinufaika na huduma ya Paulo, na mamilioni ya watu wanaendelea kunufaika na barua katika Neno la Mungu alizoandika akiongozwa na roho takatifu.—Mdo. 9:3-19; 2 Tim. 3:16, 17.
11. Kwa nini tufanye mabadiliko yoyote yale yanayohitajika ili tuwahubirie wanaume?
11 Na tufanye mabadiliko yoyote yale yanayohitajika ili tuwahubirie wanaume wengi zaidi. Tunapojitahidi kufikia lengo hilo, tuna hakika kwamba Yehova atabariki jitihada zetu za kufanya mapenzi yake na kushughulikia ifaavyo mambo ya Ufalme.