Sisi Ni Wahubiri Nyakati Zote
1. Tunajuaje kwamba waeneza-injili wa karne ya kwanza walikuwa tayari kuhubiri nyakati zote?
1 Katika karne ya kwanza, waeneza-injili wenye bidii walitangaza habari njema “bila kuacha,” popote ambapo wangepata watu. (Mdo. 5:42) Kwa hiyo, hatuwezi kuwazia kwamba walipokuwa wakihubiri nyumba kwa nyumba wangewapita watu waliokutana nao barabarani bila kuwahubiria pia. Wala hawangepoteza nafasi ya kuhubiri isivyo rasmi walipokuwa wakinunua vitu sokoni baada ya kumaliza utumishi wa shambani. Kama Yesu, walikuwa tayari kuhubiri nyakati zote.—Marko 6:31-34.
2. Kuishi kulingana na jina letu kunahusisha nini?
2 Tayari Sikuzote: Jina letu, Mashahidi wa Yehova, linaonyesha kazi tunayofanya; na pia linaonyesha sisi ni akina nani. (Isa. 43:10-12) Hivyo, tuko tayari sikuzote kutetea tumaini letu, hata wakati ambapo hatuhubiri nyumba kwa nyumba. (1 Pet. 3:15) Je, unafikiria mapema nyakati unazoweza kuhubiri isivyo rasmi, kisha kutayarisha yale utakayosema? Je, unabeba machapisho ili kuwapa wale wanaopendezwa? (Met. 21:5) Je, unahubiri tu nyumba kwa nyumba, au pia unawahubiria watu habari njema mahali pengine ikiwa hali zinaruhusu?
3. Kwa nini neno “badala” halifai kutumiwa kurejelea kuhubiri barabarani, bustanini, kwenye maegesho ya magari, mahali pa biashara, na kadhalika?
3 Si Mahubiri ya “Badala”: Wakati uliopita, mara kwa mara tulitumia usemi mahubiri ya “badala” tuliporejelea kuhubiri barabarani, bustanini, kwenye maegesho ya magari, mahali pa biashara, na kadhalika. Hata hivyo, neno “badala” linaweza kumaanisha mahubiri yaliyo tofauti na yale ya kawaida, au yasiyo ya lazima. Mtume Paulo alisema kwamba alihubiri “hadharani” na nyumba kwa nyumba. (Mdo. 20:20) Basi, kuhubiri “hadharani” ni usemi unaofaa kuliko mahubiri ya “badala.” Ni kweli kwamba kuhubiri nyumba kwa nyumba ndiyo njia yetu ya msingi na yenye matokeo zaidi ya kuwapelekea watu ujumbe wa Ufalme. Hata hivyo, waeneza-injili wa karne ya kwanza walikazia fikira watu, bali si nyumba. Walitumia kila nafasi kuwaeleza wengine kuhusu kweli, wakifanya hivyo hadharani, isivyo rasmi, na nyumba kwa nyumba. Na tuwe na mtazamo kama huo ili tutimize huduma yetu kikamili.—2 Tim. 4:5.