Usijiwekee Vizuizi—Kushughulika na Ratiba Yenye Mambo Mengi
1. Kwa nini wengine husita kuanzisha funzo la Biblia?
1 Wahubiri fulani husita kuanzisha funzo la Biblia kwa sababu wana ratiba yenye mambo mengi. Kushughulikia mahitaji ya mwanafunzi wa Biblia kunachukua wakati. Wakati unahitajika ili kujitayarisha kwa ajili ya funzo, kuliongoza, na kumsaidia mwanafunzi ashinde vizuizi anavyopata. Mtume Paulo alisema kwamba aliitoa nafsi yake ili awasaidie Wathesalonike kumjua Yehova. (1 The. 2:7, 8) Tunaweza kuongozaje funzo la Biblia hata tukiwa na ratiba yenye mambo mengi?
2. Upendo wetu kwa Yehova unaathirije jinsi tunavyotumia wakati wetu?
2 Wakati Unahitajika Ili Kumtumikia Yehova: Ukweli wa mambo ni kwamba wakati unahitajika ili kumtumikia Yehova. Kwa mfano, kwa kawaida sisi hutumia wakati kuhudhuria mikutano, kushiriki katika huduma, kusoma Biblia, na kusali. Kwa kupenda, mtu aliyefunga ndoa na mwenye mambo mengi hupanga kutumia wakati pamoja na mwenzi wake wa ndoa. Je, hatupaswi kufurahia zaidi ‘kununua wakati’ kumtumikia Yehova kwa sababu tunampenda? (Efe. 5:15-17; 1 Yoh. 5:3) Kulingana na Yesu, sehemu muhimu ya ibada yetu ni kazi ya kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Kutafakari jambo hilo kutatusaidia tusisite kukubali jukumu la kuongoza funzo la Biblia.
3. Tunaweza kufanya nini ili kuongoza funzo la Biblia hata wakati ambapo hali zinavuruga ratiba yetu ya utumishi wa shambani?
3 Lakini namna gani ikiwa ratiba yetu inavurugwa na kazi ya kuajiriwa, matatizo ya afya yasiyo na tiba, au migawo ya kitheokrasi? Wahubiri wengine ambao mara kwa mara hulazimika kuwa mbali na nyumbani huongoza funzo la Biblia kupitia simu au kupitia kompyuta zilizounganishwa pamoja. Wale ambao ratiba yao huvurugika kwa sababu ya matatizo ya afya yasiyo na tiba wamepanga ili mwanafunzi awatembelee nyumbani. Wengine wamefanya mipango ili mhubiri mwenye kutegemeka ajifunze na mwanafunzi wao wa Biblia wakati ambapo hawapatikani.
4. Ni baraka gani tunazopata tunaposhiriki katika kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia?
4 Paulo alipata shangwe nyingi kwa sababu alitumia wakati wake na nguvu zake kuwasaidia wengine kujifunza kweli. (Mdo. 20:35) Alipotafakari kuhusu wale wote ambao alikuwa amefanikiwa kuwasaidia huko Thesalonike, alichochewa kumshukuru Yehova. (1 The. 1:2) Tunaweza kuridhika na kuongeza shangwe yetu katika huduma iwapo hatutaruhusu ratiba yenye mambo mengi ituzuie kushiriki katika kazi ya kuongoza mafunzo ya Biblia.