Je, Wewe Huangalia Ubao wa Matangazo kwa Ukawaida?
Wazee, watumishi wa huduma, na wengine wenye madaraka kutanikoni huangalia ubao wa matangazo kwa ukawaida ili wajue ni lini wana mgawo. Hata hivyo, wote kutanikoni watapata habari muhimu kwenye ubao wa matangazo. Je, unajua zamu yenu ya kusafisha Jumba la Ufalme itakuwa lini? Je, kutaniko limetumiwa barua muhimu kutoka kwa mwangalizi wa mzunguko au ofisi ya tawi? Je, unajua kichwa cha hotuba ya watu wote juma hili ili uweze kumwalika mwanafunzi wako wa Biblia? Je mabadiliko yamefanywa katika ratiba ya mikutano au katika kikundi chako cha utumishi? Nyingi kati ya habari hizo hazitangazwi tena wakati wa mikutano, na huenda isiwezekane kwa wazee kuwajulisha wahubiri mmoja mmoja. Kwa hiyo, tunapaswa kuangalia ubao wa matangazo kwa ukawaida. Ikiwa tutahakikisha kwamba tunaangalia ubao wa matangazo kwa ukawaida, basi mambo yote yatatendeka “kwa adabu na kwa mpango.”—1 Kor. 14:40.