Ni Nini Hutuchochea Kuhubiri?
1. Kuna uhusiano gani kati ya upendo na huduma yetu?
1 Kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu ndiyo kazi ya maana zaidi tunayoweza kufanya leo. Kwa kweli, kwa kufanya kazi hiyo, tunaonyesha kwamba tunatii amri mbili kuu zaidi, yaani, kumpenda Yehova na jirani zetu. (Marko 12:29-31) Upendo ndiyo sifa yenye nguvu zaidi inayoweza kutuchochea kuwa wahudumu wenye bidii.—1 Yoh. 5:3.
2. Kazi yetu ya kuhubiri inaonyeshaje kwamba tunampenda Yehova?
2 Upendo kwa Yehova: Kumpenda Rafiki yetu wa karibu zaidi Yehova, hutuchochea kumtetea. Kwa karibu miaka 6,000, Shetani amekuwa akimchongea Yehova. (2 Kor. 4:3, 4) Kwa hiyo, watu wanaamini kwamba Mungu huwatesa watu kwenye moto, kwamba yeye ni Utatu usioeleweka, na kwamba hapendezwi na wanadamu. Wengi hata wamekata kauli kwamba hakuna Mungu. Tunatamani sana watu wajue ukweli kumhusu Baba yetu wa mbinguni! Jitihada zetu zenye bidii za kuwa mashahidi wa Mungu zinamfurahisha sana Yehova na kumkasirisha Shetani.—Met. 27:11; Ebr. 13:15, 16.
3. Ni katika njia gani tunaonyesha kwamba tunampenda jirani kupitia huduma yetu?
3 Upendo kwa Jirani: Kila mara tunapomhubiria mtu fulani tunaonyesha kwamba tunampenda mtu huyo. Katika nyakati hizi za hatari watu wanahitaji sana kusikia habari njema. Watu wengi ni kama Waninawi wa siku za Yona ambao ‘hawakujua hata kidogo tofauti kati ya mkono wao wa kuume na wa kushoto.’ (Yona 4:11) Huduma yetu huwasaidia watu waishi maisha yenye furaha na mafanikio. (Isa. 48:17-19) Huwapa tumaini. (Rom. 15:4) Ikiwa watasikiliza na kutenda kulingana na mambo wanayojifunza, ‘wataokolewa.’—Rom. 10:13, 14.
4. Ni kitu gani ambacho Yehova hatasahau kamwe?
4 Watoto wazuri hawawaonyeshi wazazi wao upendo katika nyakati fulani tu hususa. Wanajitahidi kuwapenda wazazi wao nyakati zote. Vilevile, kumpenda Mungu na jirani kutatuchochea tuwe macho kutambua nafasi za kuhubiri nyakati zote, si tu nyakati ambazo tumepangiwa kuhubiri. Tutahubiri bila kuacha. (Mdo. 5:42) Yehova hatasahau kamwe upendo kama huo.—Ebr. 6:10.