Yehova Huona Nini Anaponitazama?
1. Ni katika njia gani Biblia ni kama kioo?
1 Unajiangalia kwenye kioo mara ngapi? Wengi wetu hufanya hivyo kila siku kwa sababu jambo hilo hutusaidia kuona marekebisho tunayohitaji kufanya. Biblia ni kama kioo. Kusoma Neno la Mungu kutatusaidia kuona jinsi tulivyo moyoni, yaani kujiona kama Yehova anavyotuona. (1 Sam. 16:7; Yak. 1:22-24) Neno la Mungu linaweza “kutambua fikira na makusudio ya moyo.” (Ebr. 4:12) Kusoma na kutafakari Biblia kila siku kunawezaje kutusaidia kutambua mambo tunayopaswa kufanyia kazi ili tuweze kuwa waeneza-injili wenye matokeo zaidi?—Zab. 1:1-3.
2. Biblia inawezaje kutusaidia tujichunguze?
2 Tumia Biblia Kama Kioo: Masimulizi ya Biblia kuhusu watumishi waaminifu wa Yehova hutufundisha sifa zinazompendeza Yehova. Kwa mfano, Daudi alitetea jina la Mungu kwa bidii. (1 Sam. 17:45, 46) Kwa ujasiri, Isaya alijitolea kuhubiri katika eneo lililokuwa na hali ngumu. (Isa. 6:8, 9) Kwa kuwa Yesu alimpenda sana Baba yake wa mbinguni, aliuona utumishi kuwa chanzo cha burudisho na uradhi badala ya kuwa mzigo wenye kuchosha. (Yoh. 4:34) Wakristo wa karne ya kwanza walihubiri kwa bidii, walimtegemea Yehova, na waliazimia kutokata tamaa. (Mdo. 5:41, 42; 2 Kor. 4:1; 2 Tim. 4:17) Kutafakari mifano kama hiyo hutusaidia kujichunguza kwa lengo la kuboresha utumishi wetu mtakatifu.
3. Kwa nini hatupaswi kuahirisha-ahirisha kunapokuwa na uhitaji wa kufanya marekebisho?
3 Fanya Marekebisho: Bila shaka, hakuna faida za kujiangalia kwenye kioo ikiwa hatutafanya marekebisho yanayohitajika. Tunaweza kumwomba Yehova atusaidie tujichunguze kwa unyoofu na kisha atusaidie tujirekebishe. (Zab. 139:23, 24; Luka 11:13) Kwa sababu muda uliobaki ni mfupi na uhai unahusika, hatupaswi kuahirisha-ahirisha kufanya mabadiliko.—1 Kor. 7:29; 1 Tim. 4:16.
4. Inakuwaje kwa mtu ambaye hulichunguza Neno la Mungu na kutenda kulingana na anayosoma?
4 Yehova hutazama mtu wa siri wa moyoni, na sifa hizo ni muhimu kuliko tunavyoonekana kwa nje. (1 Pet. 3:3, 4) Inakuwaje kwa mtu ambaye hulichunguza Neno la Mungu na kutenda kulingana na anayosoma? Yeye ‘amekuwa, si msikiaji msahaulifu, bali mtendaji wa kazi, na atakuwa mwenye furaha katika kuitenda.’ (Yak. 1:25) Ndiyo, tutakuwa wahudumu wenye furaha na matokeo kwa sababu tunatoa ‘kama vioo, mrudisho wa utukufu wa Yehova.’—2 Kor. 3:18.