Karne Moja ya Kuutangaza Ufalme!
1 “Tazameni, Mfalme anatawala! Ninyi ndio mawakili wa kumtangaza. Kwa hiyo, mtangazeni, mtangazeni, mtangazeni, Mfalme na ufalme wake.” Ndugu Rutherford alisema maneno hayo yenye kuchochea karibu karne moja iliyopita, na hivyo kuwatia moyo watu wa Yehova kutangaza ujumbe wa Ufalme duniani kote. Na hivyo ndivyo tumefanya! Kama Wakristo wa karne ya kwanza, tumehubiri habari njema ya Ufalme “katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.” (Kol. 1:23) Tumefanya nini ili kuutangaza Ufalme katika karne iliyopita? Tunawezaje kuendelea kuutangaza tunapokaribia miaka 100 tangu Ufalme huo uzaliwe?
2 Mambo Tuliyotimiza: Kwa miaka mingi, machapisho yetu yametangaza Ufalme wa Mungu. Tangu mwaka 1939 gazeti letu kuu limekuwa na kichwa: Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova. Mara nyingi gazeti hilo linazungumzia Ufalme na mambo ambayo Ufalme huo utatimiza. Pia, gazeti la Amkeni! huzungumzia Ufalme wa Mungu kuwa tumaini pekee la wanadamu. Hivyo basi, inafaa kabisa kwamba sasa magazeti hayo mawili yanatafsiriwa na kusambazwa zaidi kuliko magazeti mengine ulimwenguni!—Ufu. 14:6.
3 Watu wa Yehova wametumia mbinu mbalimbali kuutangaza Ufalme. Mwanzoni, tulitumia magari yenye vipaza-sauti, vipindi vya redio, na gramafoni. Mbinu hizo zilitusaidia kueneza habari njema kwa watu wengi kulipokuwa na watangazaji wachache wa Ufalme. (Zab. 19:4) Katika miaka ya karibuni, tumetumia Tovuti ya jw.org kutangaza Ufalme kwa mamilioni ya watu, kutia ndani wanaoishi katika nchi ambazo kazi yetu iko chini ya vizuizi.
4 Pia, watu wa Yehova wameanzisha mipango ya pekee ili kueneza ujumbe wa Ufalme. Kwa mfano, kwenye miaka ya 1990, tulipanua kazi yetu ya kuhubiri nyumba kwa nyumba kwa kuhubiri kwenye bustani za umma, maegesho ya magari, na maeneo ya biashara. Hivi karibuni, tumeanzisha mpango wa pekee wa kuhubiri hadharani katika miji mikubwa ulimwenguni pote. Kwa kuongezea, makutaniko mengi yanashiriki kuhubiri hadharani katika maeneo yao kwa kuweka meza na vigari vya kukokotwa vyenye machapisho katika sehemu zenye wapita njia wengi. Bila shaka, kwenda nyumba kwa nyumba bado ndio njia yetu kuu ya kuhubiri Ufalme.—Mdo. 20:20.
5 Mambo Tunayotarajia Kutimiza: Tutakapoanza mwaka mpya wa utumishi mwezi wa Septemba, wengi wataanza kutumikia wakiwa mapainia wa kawaida. Je, unaweza kuwaunga mkono? Ikiwa haiwezekani, je, unaweza kufanya upainia msaidizi mara kwa mara? Iwe unaweza kufanya upainia au la, uwe na hakika kwamba Yehova atakubariki kwa jitihada zako za kushiriki kikamili katika kuutangaza Ufalme.—Mal. 3:10.
6 Kufikia Oktoba 2014, Ufalme utakuwa umetimiza miaka 100 tangu uzaliwe. Kwa kufaa, toleo la watu wote la Mnara wa Mlinzi la mwezi huo litakazia Ufalme wa Mungu. Jitahidi kuwapa watu wengi iwezekanavyo nakala ya gazeti hilo. Tunapofikiria wakati ujao, acheni tuendelee ‘kutangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu’ kwa wote watakaosikiliza.—Mdo. 8:12.