Kutafuta Amani Licha ya Vita na Ukatili
Gary ambaye alikuwa akitumikia jeshini alisema hivi: “Kabla ya kujifunza Biblia, sikujua kwa nini kulikuwa na ukatili, ukosefu wa haki, na matatizo mengi ulimwenguni. Lakini sasa nina amani ya akili. Ninajua kwamba Yehova Mungu ataufanya ulimwengu kuwa mahali salama.”
Watu wengi wamekuwa na hisia kama za Gary. Chunguza jinsi ambavyo Biblia imewasaidia watu wengine.
BIBLIA INASEMA: “Wewe, Ee Yehova, ni mwema na uko tayari kusamehe.”—Zaburi 86:5.
JINSI MSTARI HUO UNAVYOSAIDIA: “Mstari huo unanihakikishia kwamba Yehova ni mwenye rehema. Ninajua kwamba yuko tayari kunisamehe kwa mambo yote niliyofanya zamani niliposhiriki katika vita.”—Wilmar, Kolombia.
BIBLIA INASEMA: “Ninaumba mbingu mpya na dunia mpya; na mambo ya zamani hayataingia tena akilini, wala hayataingia tena moyoni.”—Isaya 65:17.
JINSI MSTARI HUO UNAVYOSAIDIA: “Nilikuwa nikisumbuliwa na ugonjwa wa mfadhaiko unaosababishwa na tukio lenye kutisha na mkazo kwa sababu ya mambo niliyopitia nilipokuwa jeshini. Lakini andiko hilo linanikumbusha kwamba hivi karibuni Yehova atanisaidia kuondoa mawazo na kumbukumbu mbaya nilizo nazo. Na mambo hayo hayataingia tena akilini au moyoni mwangu. Hilo ni jambo lenye kupendeza sana!”—Zafirah, Marekani.
BIBLIA INASEMA: “Katika siku zake mwadilifu atasitawi, na amani itakuwa nyingi mpaka mwezi utakapokuwa haupo tena.”—Zaburi 72:7.
JINSI MSTARI HUO UNAVYOSAIDIA: “Mara nyingi, mimi hufikiria kuhusu maneno hayo. Hivi karibuni, vita na mambo mabaya yanayosababishwa na vita yatakwisha, na hatutahitaji tena kuogopa kuhusu usalama wa wapendwa wetu.”—Oleksandra, Ukrainia.
BIBLIA INASEMA: “Wafu wako wataishi. . . . Amkeni na mpige vigelegele kwa shangwe, enyi mnaokaa mavumbini!”—Isaya 26:19.
JINSI MSTARI HUO UNAVYOSAIDIA: “Karibu watu wote wa familia yangu waliuawa wakati wa mauaji ya kimbari dhidi ya Watutsi. Lakini mstari huo unanihakikishia kwamba nitawaona tena. Ninatazamia kwa hamu kusikia sauti zao wakiwa na furaha watakapofufuliwa!”—Marie, Rwanda.
BIBLIA INASEMA: “Bado muda mfupi tu, na watu waovu hawatakuwepo tena. . . Lakini wapole wataimiliki dunia, nao watafurahia kwelikweli wingi wa amani.”—Zaburi 37:10, 11.
JINSI MSTARI HUO UNAVYOSAIDIA: “Ingawa vita vimeisha, bado kuna ukosefu wa haki na watu waovu. Mistari hiyo imeniimarisha sana. Yehova anaona kila kitu na anaelewa hali yangu. Anaahidi kwamba hivi karibuni mateso hayo yote yataisha na hayatakumbukwa tena.”—Daler, Tajikistan.
Watu ambao wamenukuliwa katika gazeti hili ni miongoni mwa mamilioni ya Mashahidi wa Yehova ambao Biblia imewasaidia kupata amani. Wamejifunza jinsi ya kushinda ubaguzi wa rangi, utaifa, ukabila, na ubinafsi. (Waefeso 4:31, 32) Mashahidi wa Yehova hawaungi mkono upande wowote inapohusu mambo ya kisiasa na wanakataa kujihusisha na ukatili.—Yohana 18:36.
Pia, Mashahidi wa Yehova hutegemezana kupitia undugu wao wa ulimwenguni pote wenye upendo. (Yohana 13:35) Kwa mfano, Oleksandra, aliyenukuliwa mapema, alilazimika kukimbilia nchi nyingine pamoja na dada yake kwa sababu ya vita. Anasema: “Tulipovuka mpaka, mara moja tuliwaona Mashahidi wenyeji waliokuwa hapo ili kutukaribisha. Utegemezo wao ulitusaidia kuzoea kuishi katika nchi ya kigeni tukiwa wakimbizi.”
Tunakukaribisha kwa uchangamfu ujiunge nasi kwenye mikutano yetu ambako tunajifunza kuhusu ujumbe wa amani unaopatikana katika Biblia na jinsi tunavyoweza kuutumia. Tembelea jw.org ili upate eneo lililo karibu nawe au uombe funzo la Biblia bila malipo na mmoja wa Mashahidi wa Yehova, kwa kutumia chapisho Furahia Maisha Milele!