Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w25 Mei kur. 14-19
  • Litafute Jiji Litakalodumu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Litafute Jiji Litakalodumu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • MTUMAINI YULE AMBAYE HATAKUACHA KAMWE
  • WATIINI WALE WANAOONGOZA
  • ONYESHA UPENDO WA KINDUGU NA UKARIBISHAJI WAGENI
  • MAMBO YATAKAYOTUKIA WAKATI UJAO
  • Barua Inayoweza Kutusaidia Kuvumilia kwa Uaminifu Mpaka Mwisho
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2024
  • Maamuzi Yanayoonyesha Unamtegemea Yehova
    Daftari la Mkutano wa Huduma na Maisha Yetu ya Kikristo—2023
  • Uwe Mwenye Kiasi Inapohusu Mambo Usiyoyajua
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
  • Kusitawisha Urafiki wa Karibu na Waabudu Wenzetu Ni Jambo Jema Kwetu!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2025
w25 Mei kur. 14-19

MAKALA YA 21

WIMBO 21 Endeleeni Kuutafuta Kwanza Ufalme

Litafute Jiji Litakalodumu

“Tunatafuta kwa bidii [jiji] litakalokuja.”—EBR. 13:14.

JAMBO KUU

Jinsi Waebrania sura ya 13 inavyoweza kutunufaisha leo na wakati ujao.

1. Yesu alitabiri jiji la Yerusalemu lingepatwa na nini katika karne ya kwanza?

SIKU chache kabla ya kifo chake, Yesu Kristo alitoa unabii uliotaja mambo hususa, ambao utimizo wake wa kwanza ulikuwa wakati wa siku za mwisho za mfumo wa mambo wa Kiyahudi. Alionya kwamba siku moja, jiji la Yerusalemu ‘lingezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi.’ (Luka 21:20) Yesu aliwaambia wafuasi wake kwamba mara tu walipoona majeshi hayo—ambayo yalikuja kuwa majeshi ya Roma—walipaswa kuondoka eneo hilo mara moja.—Luka 21:​21, 22.

2. Mtume Paulo aliwapatia Wakristo walioishi Yudea na Yerusalemu kikumbusho gani?

2 Miaka michache tu kabla ya majeshi ya Roma kulizingira jiji la Yerusalemu, mtume Paulo aliandika barua yenye ujumbe muhimu ambayo ilikuja kuitwa kitabu cha Waebrania. Katika barua hiyo, Paulo aliwapa Wakristo wa Yudea na Yerusalemu ushauri muhimu ambao ungewasaidia wajitayarishe kwa ajili ya jambo ambalo lingetokea wakati ujao. Jambo gani hilo? Jiji la Yerusalemu lingeharibiwa. Ili Wakristo hao waokoke, walipaswa kuwa tayari kuacha nyumba na biashara zao. Hivyo, Paulo aliandika hivi kuhusu jiji la Yerusalemu: “Hapa hatuna jiji linalodumu.” Kisha akaongezea hivi: “Bali tunatafuta kwa bidii lile litakalokuja.”—Ebr. 13:14.

3. “Jiji lililo na misingi ya kweli” ni nini, na kwa nini tunalitafuta?

3 Huenda Wakristo walioamua kuondoka Yerusalemu na Yudea walidhihakiwa, lakini uamuzi huo uliokoa uhai wao. Leo, tunadhihakiwa kwa sababu hatuweki tegemeo letu katika pesa au kuwategemea wanadamu wasuluhishe matatizo ya ulimwengu huu. Basi, kwa nini tunafanya hivyo? Tunajua kwamba mfumo huu wa mambo hautadumu. Hivyo, tunalitafuta “jiji lililo na misingi ya kweli,” yaani, “lile litakalokuja,” Ufalme wa Mungu.a (Ebr. 11:10; Mt. 6:33) Kila kichwa kidogo katika makala hii kitazungumzia: (1) jinsi ushauri wa Paulo ulioongozwa na roho ulivyowasaidia Wakristo wa karne ya kwanza kuendelea kulitafuta “[jiji] litakalokuja,” (2) jinsi Paulo alivyowatayarisha kwa ajili ya matukio ya wakati ujao, na (3) jinsi ushauri wake unavyotusaidia leo.

MTUMAINI YULE AMBAYE HATAKUACHA KAMWE

4. Kwa nini jiji la Yerusalemu lilikuwa muhimu kwa Wakristo?

4 Jiji la Yerusalemu lilikuwa muhimu kwa Wakristo. Kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza lilianzishwa hapo mwaka wa 33 W.K., na baraza linaloongoza lilikuwa katika jiji hilo. Isitoshe, Wakristo wengi walimiliki nyumba na walikuwa wamejikusanyia mali katika jiji hilo. Hata hivyo, Yesu aliwaonya wafuasi wake kwamba wangehitaji kuondoka Yerusalemu na hata kuondoka Yudea.—Mt. 24:16.

5. Paulo aliwatayarishaje Wakristo kwa ajili ya jambo ambalo lingetukia?

5 Ili kuwatayarisha Wakristo hao kwa ajili ya jambo ambalo lingetukia, Paulo aliwasaidia kukazia fikira maoni ya Yehova kuhusu jiji la Yerusalemu. Paulo aliwakumbusha kwamba kwa maoni ya Yehova, hekalu, ukuhani, na dhabihu zilizokuwa zinatolewa Yerusalemu hazikuwa takatifu tena. (Ebr. 8:13) Watu wengi katika jiji hilo walikuwa wamemkataa Masihi. Hekalu la Yerusalemu halikuwa tena kituo cha ibada safi ya Yehova, na lingeharibiwa.—Luka 13:​34, 35.

6. Kwa nini kikumbusho cha Paulo kinachopatikana katika Waebrania 13:​5, 6 kiliwafaa kabisa Wakristo?

6 Paulo alipowaandikia Waebrania, jiji la Yerusalemu lilikuwa na ufanisi mwingi. Mwandishi Mroma wa kipindi hicho alisema kwamba jiji la Yerusalemu lilikuwa “jiji maarufu zaidi la Mashariki.” Wayahudi kutoka maeneo mbalimbali walisafiri huko kila mwaka ili kushiriki katika sherehe mbalimbali, jambo lililochangia ukuzi wa kiuchumi. Bila shaka, baadhi ya Wakristo walinufaika kutokana na hali hiyo nzuri ya kiuchumi. Huenda ndiyo maana Paulo aliwaambia hivi: “Njia yenu ya maisha iwe bila upendo wa pesa, huku mkiridhika na vitu mlivyo navyo.” Kisha, akanukuu uhakika huu thabiti unaopatikana katika Maandiko, na unaoonyesha ahadi hii ya Yehova kwa kila mmoja wetu: “Sitakuacha wala kukutupa kamwe.” (Soma Waebrania 13:​5, 6; Kum. 31:6; Zab. 118:6) Wakristo walioishi Yerusalemu na Yudea wangehitaji uhakikisho huo. Kwa nini? Kwa sababu muda mfupi baada ya kupokea barua hiyo, wangelazimika kuacha nyumba zao, biashara zao, na sehemu kubwa ya mali zao. Kisha, wangehitaji kuanza maisha mapya katika eneo lingine, jambo ambalo halikuwa rahisi.

7. Kwa nini tunapaswa kujifunza kumtumaini kabisa Yehova sasa?

7 Jambo tunalojifunza: Ni jambo gani litakalotukia hivi karibuni? Mwisho wa mfumo huu wa mambo katika “dhiki kuu.” (Mt. 24:21) Kama Wakristo katika karne ya kwanza, ni lazima tuendelee kukesha na kuwa tayari. (Luka 21:​34-36) Wakati wa dhiki kuu, huenda tukahitaji kuacha baadhi au mali zetu zote, tukitumaini kabisa kwamba Yehova hatawaacha kamwe watu wake. Hata sasa, kabla ya dhiki hiyo kuu kuanza, tuna nafasi ya kuonyesha tunamtumaini nani. Jiulize hivi: ‘Je, matendo na malengo yangu yanaonyesha kwamba ninamtegemea Mungu anayeahidi kunitunza, badala ya kutegemea utajiri?’ (1 Tim. 6:17) Kwa kweli, ingawa tunaweza kujifunza kutokana na mambo ambayo yalitokea katika karne ya kwanza, “dhiki kuu” inayokuja haijawahi kutukia kamwe. Hivyo, tutajuaje kihususa jambo la kufanya dhiki kuu itakapoanza?

WATIINI WALE WANAOONGOZA

8. Yesu aliwapatia wanafunzi wake mwongozo gani?

8 Miaka michache baada ya kupokea barua ya Paulo kwa Waebrania, Wakristo waliona majeshi ya Roma yakilizingira jiji la Yerusalemu. Hiyo ilikuwa ishara ya kwamba wakati wa kukimbia ulikuwa umefika; jiji la Yerusalemu lingeharibiwa. (Mt. 24:3; Luka 21:​20, 24) Lakini wangekimbilia wapi? Yesu alikuwa amewaambia tu hivi: “Wale walio Yudea waanze kukimbilia milimani.” (Luka 21:21) Eneo hilo lilikuwa na milima mingi. Hivyo, wangejuaje mlima wa kukimbilia?

9. Kwa nini huenda Wakristo walijiuliza wangekimbilia milima gani? (Tazama pia ramani.)

9 Fikiria baadhi ya milima ambayo Wakristo wangeweza kukimbilia: milima ya Samaria, milima ya Galilaya, Mlima Hermoni na milima ya Lebanoni, na milima iliyo ng’ambo ya Mto Yordani. (Tazama ramani.) Huenda baadhi ya majiji katika milima hiyo yalionekana kuwa mahali salama pa kuishi. Kwa mfano, jiji la Gamla, lilikuwa katika safu zenye miamba za mlima mrefu, na ilikuwa vigumu sana kulifikia. Baadhi ya Wayahudi waliliona jiji hilo kuwa mahali pazuri pa kukimbilia. Hata hivyo, jiji la Gamla lilikuja kuwa eneo ambalo kulikuwa na pambano kali kati ya Wayahudi na Waroma, na wakaaji wengi wa jiji hilo walikufa.b

Ramani inayoonyesha baadhi ya milima na majiji ya Israeli katika karne ya kwanza. Kaskazini ya Yerusalemu kuna milima ya Lebanoni, Galilaya, Samaria, na Gileadi, pamoja na Mlima Hermoni na Mlima Tabori. Majiji yaliyo kaskazini ya Yerusalemu ni Gamla, Kaisaria, na Pela. Kusini ya Yerusalemu kuna milima ya Yudea na Abarimu, pamoja na jiji la Masada. Ramani pia inaonyesha njia zilizotumiwa katika kampeni za kijeshi za Roma na maeneo waliyopoteza Wayahudi kuanzia mwaka wa 67 W.K. hadi 73 W.K.

Kulikuwa na milima mingi ambayo Wakristo wa mapema wangeweza kukimbilia, lakini si yote iliyokuwa salama (Tazama fungu la 9)


10-11. (a) Huenda Yehova aliwaongozaje Wakristo? (Waebrania 13:​7, 17) (b) Wakristo walinufaikaje kwa kuwatii wale walioongoza? (Tazama pia picha.)

10 Inaonekana kwamba Yehova aliwaongoza Wakristo hao kupitia wale waliokuwa wakiongoza kutanikoni. Mwanahistoria Eusebio aliandika hivi baadaye: “Watu katika Kutaniko la Yerusalemu, kupitia mwongozo wa Mungu, walipokea ufunuo ambao walipewa wanaume waliokubaliwa; waliagizwa . . . wahame kutoka katika jiji kabla ya vita na waende kuishi katika jiji fulani la Perea lililoitwa Pela.” Inaonekana jiji la Pela liliwafaa kabisa Wakristo. Jiji hilo lilikuwa karibu na Yerusalemu, hivyo ilikuwa rahisi zaidi kulifikia. Wakaaji wengi wa jiji hilo walikuwa Watu wa Mataifa na kwa sehemu kubwa hawakuathiriwa na Wayahudi wapigania-uhuru wenye msimamo mkali na mapambano yao dhidi ya Waroma.—Tazama ramani.

11 Wakristo waliokimbilia milimani walifuata shauri la Paulo la ‘kuwatii wale wanaoongoza’ katika kutaniko. (Soma Waebrania 13:​7, 17.) Matokeo ni kwamba watu wa Mungu waliokoka. Historia inathibitisha kwamba Mungu hakuwaacha wale ‘waliokuwa wakingojea jiji lililo na misingi ya kweli’—Ufalme wa Mungu.—Ebr. 11:10.

Kikundi cha Wakristo wa karne ya kwanza wanatembea kwenye eneo lenye milima wakiwa na mali zao.

Pela lilikuwa jiji salama na lililokuwa karibu (Tazama fungu la 10-11)


12-13. Yehova amewaongozaje watu wake wakati wa hali ngumu?

12 Jambo tunalojifunza: Yehova anawatumia wale wanaoongoza kuwapa watu wake mwongozo hususa. Biblia ina mifano mingi ya jinsi Yehova alivyotumia wachungaji kuongoza watu wake wakati wa hali ngumu. (Kum. 31:23; Zab. 77:20) Leo pia tunajionea wazi jinsi ambavyo Yehova anaendelea kuwatumia wale wanaoongoza.

13 Kwa mfano, wakati wa janga la COVID-19, “wale wanaoongoza” walitoa mwongozo tuliohitaji. Wazee walipokea miongozo ya jinsi ambavyo ndugu na dada kutanikoni wangefanya mikutano na kuendelea kumwabudu Yehova. Muda mfupi baada ya janga hilo kuanza, tulikuwa na kusanyiko la eneo la kihistoria katika lugha zaidi ya 500 kupitia Intaneti, televisheni, na redio. Chakula cha kiroho kiliendelea kupatikana. Matokeo ni kwamba tuliendelea kuwa na umoja. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba haidhuru ni majaribu gani ambayo huenda tukapata wakati ujao, Yehova ataendelea kuwasaidia wale wanaoongoza kufanya maamuzi ya hekima. Zaidi ya kumtumaini Yehova na kutii amri zake, ni sifa gani nyingine zitakazotusaidia kujitayarisha kwa ajili ya dhiki kuu na kutenda kwa hekima katika kipindi hicho kigumu sana?

ONYESHA UPENDO WA KINDUGU NA UKARIBISHAJI WAGENI

14. Kulingana na Waebrania 13:​1-3, ni sifa gani ambazo Wakristo walihitaji kuonyesha wakati wa siku za mwisho za mfumo wa mambo wa Kiyahudi?

14 Dhiki kuu itakapoanza, tutahitaji kuonyeshana upendo kuliko wakati mwingine wowote. Hivyo, tutahitaji kufuata mfano wa Wakristo waliokuwa wakiishi Yerusalemu na Yudea. Sikuzote walikuwa wameonyeshana upendo. (Ebr. 10:​32-34) Lakini miaka michache kabla ya mwisho wa mfumo wa mambo wa Kiyahudi, Wakristo walihitaji kuonyesha “upendo wa kindugu” na “kuwakaribisha wageni” kwa kiasi kikubwa hata zaidi.c (Soma Waebrania 13:​1-3.) Hali itakuwa hivyo kwetu pia, kadiri mwisho wa mfumo huu wa mambo unavyokaribia.

15. Kwa nini Wakristo Waebrania walihitaji kuonyesha upendo wa kindugu na ukaribishaji wageni baada ya kukimbia?

15 Majeshi ya Roma yalipolizingira jiji la Yerusalemu na kuondoka kwa ghafla, Wakristo walikimbia na vitu vichache vya kimwili. (Mt. 24:​17, 18) Walihitaji kusaidiana walipokuwa wakisafiri kwenda milimani na walipoanza kuishi katika makao yao mapya. Bila shaka, kulikuwa na pindi nyingi “[kulipokuwa] na uhitaji wa dharura,” na pindi hizo zingewapa Wakristo nafasi za kuonyesha upendo wa kindugu wa kweli na ukaribishaji wageni kwa kutegemezana na kushiriki vitu vyao pamoja na wengine.—Tito 3:14.

16. Tunawezaje kuwaonyesha upendo waabudu wenzetu wanaohitaji msaada wetu? (Tazama pia picha.)

16 Jambo tunalojifunza: Upendo unatuchochea kuwasaidia waabudu wenzetu wanapohitaji msaada wetu. Watu wengi wa Mungu wamekuwa tayari kuwaandalia mahitaji ya kiroho na kimwili ndugu na dada zao ambao wamekuwa wakimbizi kwa sababu ya vita na majanga ya asili. Dada kutoka nchini Ukrainia, aliyekimbia kwa sababu ya vita alisema hivi: “Tumeuona mkono wa Yehova ukituongoza na kutusaidia kupitia ndugu zetu. Wametukaribisha na kutusaidia kwa njia nzuri sana nchini Ukrainia, Hungaria, na sasa hapa Ujerumani.” Wale wanaowakaribisha ndugu na dada zao na kuwaandalia mahitaji yao ni vyombo mikononi mwa Yehova.—Met. 19:17; 2 Kor. 1:​3, 4.

Wenzi wa ndoa wenye umri mkubwa wakiikaribisha kwa uchangamfu familia ya wakimbizi nyumbani mwao. Familia hiyo ina sanduku moja na mifuko michache.

Leo, Wakristo walio wakimbizi wanahitaji msaada wetu (Tazama fungu la 16)


17. Kwa nini ni muhimu kusitawisha upendo wa kindugu na ukaribishaji wageni sasa?

17 Bila shaka, msaada huo utahitajika hata zaidi wakati wa dhiki kuu, kuliko ilivyo sasa. (Hab. 3:​16-18) Yehova anatuzoeza sasa kusitawisha upendo wa kindugu na kuwa wakaribishaji wageni, sifa tutakazohitaji sana wakati huo.

MAMBO YATAKAYOTUKIA WAKATI UJAO

18. Tunawezaje kuwaiga Wakristo Waebrania wa karne ya kwanza?

18 Kama historia inavyothibitisha, Wakristo waliokimbilia milimani waliweza kuepuka uharibifu uliolipata jiji la Yerusalemu. Waliliacha jiji hilo, lakini Yehova hakuwaacha kamwe. Namna gani leo? Hatujui kihususa jinsi matukio ya wakati ujao yatakavyokuwa. Lakini Yesu alituonya tuwe tayari kutii. (Luka 12:40) Pia, tuna himizo la Paulo katika barua yake kwa Waebrania, ushauri unaotufaa leo, kama ulivyowafaa Wakristo katika karne ya kwanza. Na tuna ahadi hii ya Yehova kwa kila mmoja wetu kwamba hatatuacha wala kututupa kamwe. (Ebr. 13:​5, 6) Acheni tutafute kwa bidii lile jiji litakalodumu—Ufalme wa Mungu—na tufurahie baraka za milele za jiji hilo.—Mt. 25:34.

UNGEJIBUJE?

  • Kwa nini tunahitaji kumtumaini zaidi Yehova sasa?

  • Kwa nini itakuwa muhimu sana kuonyesha utii wakati wa “dhiki kuu”?

  • Kwa nini ni muhimu kusitawisha upendo wa kindugu na kuwa wakaribishaji wageni sasa?

WIMBO 157 Amani Milele!

a Katika nyakati za Biblia, mara nyingi majiji yalitawaliwa na mfalme. Jiji la aina hiyo lingeweza kuitwa ufalme.—Mwa. 14:2.

b Hilo lilitukia mwaka wa 67 W.K., muda mfupi baada ya Wakristo kukimbia kutoka Yudea na Yerusalemu.

c Neno linalotafsiriwa ‘upendo wa kindugu’ linaweza kumaanisha upendo kuelekea watu wa karibu wa ukoo, lakini Paulo alilitumia kurejelea upendo wenye nguvu tulio nao kuelekea ndugu na dada zetu wote kutanikoni.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki