MAKALA YA 24
WIMBO 98 Maandiko—Yaliongozwa na Roho ya Mungu
Mambo Tunayojifunza Kutokana na Unabii wa Yakobo—Sehemu ya 1
“Kusanyikeni pamoja niwaambie yatakayowapata katika kipindi cha mwisho cha zile siku.”—MWA. 49:1.
JAMBO KUU
Mambo hususa tunayojifunza kutokana na unabii wa Yakobo kumhusu Rubeni, Simeoni, Lawi, na Yuda ambao alitoa alipokaribia kufa.
1-2. Yakobo alifanya nini alipokaribia kufa, na kwa nini? (Tazama pia picha.)
MIAKA 17 hivi imepita tangu Yakobo, mtumishi mwaminifu wa Yehova, aliposafiri kutoka Kanaani hadi Misri pamoja na watu wa nyumba yake. (Mwa. 47:28) Katika kipindi hicho, alijionea shangwe kubwa ya kuungana tena na mwana wake mpendwa Yosefu na hatimaye kuona familia yake ikiwa pamoja tena. Lakini sasa, Yakobo anahisi kwamba amekaribia kufa. Hivyo, anapanga kuwe na mkutano muhimu wa familia.—Mwa. 49:28.
2 Katika siku hizo, lilikuwa jambo la kawaida kwa kichwa cha familia aliyekuwa akikaribia kufa, kuwakusanya watu wa familia yake pamoja ili kuwapa maagizo yake ya mwisho. (Isa. 38:1) Pia, huenda katika mkutano huo akachagua yule ambaye angekuwa kichwa cha familia baada ya kifo chake.
Yakobo akiwa kitandani, akitoa unabii kuhusu wanawe 12 (Tazama fungu la 1-2)
3. Kulingana na Mwanzo 49:1, 2, kwa nini maneno ya Yakobo yalikuwa muhimu?
3 Soma Mwanzo 49:1, 2. Lakini huu haukuwa mkutano wa kawaida wa familia kwa kuwa Yakobo alikuwa nabii. Katika mkutano huo, Yehova alitumia roho yake kumwongoza mtumishi wake azungumze kuhusu matukio muhimu ya wakati ujao ambayo yangewaathiri kwa njia kubwa wazao wake. Kwa sababu hiyo, nyakati fulani maneno ya Yakobo yanarejelewa kuwa unabii aliotoa alipokuwa akikaribia kufa.
4. Tutachunguza nini katika makala hii? (Tazama pia sanduku “Familia ya Yakobo.”)
4 Katika makala hii, tutachunguza mambo ambayo Yakobo aliwaambia wanawe wanne: Rubeni, Simeoni, Lawi, na Yuda. Katika makala inayofuata, tutazungumzia maneno ya Yakobo kwa wanawe wengine wanane. Kama tutakavyoona, Yakobo hakuzungumza tu kuhusu wanawe, bali pia kuhusu wazao wao, ambao hatimaye walitokeza taifa la Israeli la kale. Tutakapochunguza historia ya taifa hilo, tutajionea wazi jinsi maneno ya kinabii ya Yakobo yalivyotimia. Na kwa kuchunguza maneno yake, tutajifunza mambo muhimu yanayoweza kutusaidia kumfurahisha Baba yetu wa mbinguni, Yehova.
RUBENI
5. Huenda Rubeni alitarajia nini?
5 Yakobo alizungumza kwanza na Rubeni. Alisema hivi: “Wewe ndiye mzaliwa wangu wa kwanza.” (Mwa. 49:3) Akiwa mzaliwa wa kwanza, inaelekea Rubeni alitarajia kupata urithi maradufu wa mali ya baba yake. Pia, huenda alitarajia angekuwa kichwa cha familia baada ya kifo cha baba yake na kwamba wazao wake wangepata pia pendeleo hilo.
6. Kwa nini Rubeni alipoteza haki yake ya mzaliwa wa kwanza? (Mwanzo 49:3, 4)
6 Hata hivyo, Rubeni alipoteza haki yake ya mzaliwa wa kwanza. (1 Nya. 5:1) Kwa nini? Miaka kadhaa mapema, Rubeni alilala na Bilha, suria wa Yakobo. Bilha alikuwa kijakazi wa Raheli, mke mpendwa wa Yakobo ambaye alikuwa amekufa. (Mwa. 35:19, 22) Rubeni alikuwa mwana wa Lea, mke mwingine wa Yakobo. Huenda Rubeni alichochewa na tamaa alipolala na Bilha. Au inawezekana alifanya hivyo ili Yakobo amchukie Bilha na kumpenda zaidi mama yake. Vyovyote vile, jambo alilofanya lilimchukiza sana Yehova na Yakobo, baba yake.—Soma Mwanzo 49:3, 4.
7. Matokeo yalikuwaje kwa Rubeni na wazao wake? (Tazama pia sanduku “Unabii wa Yakobo Aliotoa Alipokuwa Akikaribia Kufa.”)
7 Yakobo alimwambia Rubeni hivi: “Hutafanikiwa.” Maneno hayo yalitimia. Hakuna rekodi yoyote inayoonyesha kwamba mzao yeyote wa Rubeni alikuja kuwa mfalme, kuhani, au nabii. Hata hivyo, Yakobo hakumkana mwanaye, bado alimpa Rubeni urithi, na wazao wake wakawa mojawapo ya makabila katika Israeli. (Yos. 12:6) Rubeni alikuwa ameonyesha sifa nzuri katika pindi nyingine, na hakuna rekodi yoyote inayoonyesha kwamba alifanya uasherati tena.—Mwa. 37:20-22; 42:37.
8. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Rubeni?
8 Tunajifunza nini? Tunahitaji kujitahidi sana kusitawisha sifa ya kujizuia na kuepuka mwenendo mpotovu wa kingono. Ikiwa tutashawishiwa kufanya dhambi, tunapaswa kutua na kufikiria jinsi ambavyo matendo yetu yatamuumiza Yehova, familia yetu, na wengine. Tunapaswa kukumbuka pia kwamba “lolote analopanda mtu, ndilo atakalovuna pia.” (Gal. 6:7) Kwa upande mwingine, jambo lililompata Rubeni linatukumbusha kuhusu rehema za Yehova. Ingawa Yehova hatazuia tusipatwe na matokeo mabaya ya makosa yetu, atabariki jitihada zetu tunapofanya yaliyo sawa.
SIMEONI NA LAWI
9. Kwa nini Yakobo hakufurahishwa na Simeoni na Lawi? (Mwanzo 49:5-7)
9 Soma Mwanzo 49:5-7. Kisha, Yakobo akazungumza na Simeoni na Lawi. Hata hivyo, alichosema kilionyesha kwamba hakufurahishwa nao. Miaka mingi mapema, Dina, binti ya Yakobo alibakwa na mwanamume Mkanaani aliyeitwa Shekemu. Inaeleweka kwamba wana wote wa Yakobo walikasirishwa sana na kilichompata dada yao, lakini Simeoni na Lawi walitenda kwa ukatili. Kwa hila, waliahidi kufanya amani na wanaume wa Shekemu ikiwa wangekubali kutahiriwa. Wanaume hao walikubali kufanya hivyo. Walipokuwa bado wana maumivu ya kutahiriwa, Simeoni na Lawi “wakachukua kila mmoja wao upanga wake, wakaenda ghafla katika jiji hilo na kumuua kila mwanamume.”—Mwa. 34:25-29.
10. Maneno ya kinabii ya Yakobo kuwahusu Simeoni na Lawi yalitimizwaje? (Tazama pia sanduku “Unabii wa Yakobo Aliotoa Alipokuwa Akikaribia Kufa.”)
10 Yakobo alihuzunishwa sana kwa sababu ya matendo ya kikatili ya Simeoni na Lawi. Alitabiri kwamba wangetawanywa na kusambazwa katika Israeli. Maneno hayo ya kinabii yalitimia zaidi ya miaka 200 baadaye, taifa la Israeli lilipoingia katika Nchi ya Ahadi. Kabila la Simeoni lilirithi baadhi ya majiji katika eneo la kabila la Yuda. (Yos. 19:1) Urithi wa Lawi ulitia ndani majiji 48 yaliyotawanywa kotekote katika Israeli.—Yos. 21:41.
11. Makabila ya Simeoni na Lawi yalifanya mambo gani mazuri?
11 Wazao wa Simeoni na Lawi hawakurudia makosa ya mababu zao. Na Walawi wengi walimwabudu Yehova kwa ushikamanifu. Musa alipopokea Sheria kutoka kwa Yehova katika Mlima Sinai, Waisraeli wengi walijihusisha na ibada ya sanamu ya ndama, lakini Walawi walimuunga mkono Musa na kumsaidia kuwaangamiza wale walioabudu sanamu. (Kut. 32:26-29) Yehova aliamua kulitenga kando kabila la Lawi, na kulipatia pendeleo lenye thamani la ukuhani. (Kut. 40:12-15; Hes. 3:11, 12) Baadaye, wakati wa kumiliki Nchi ya Ahadi, kwa ujasiri kabila la Simeoni lililisaidia kabila la Yuda kupigana na Wakanaani, kulingana na kusudi la Yehova.—Amu. 1:3, 17.
12. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Simeoni na Lawi?
12 Tunajifunza nini? Kamwe usiruhusu hasira iongoze maamuzi na matendo yako. Ikiwa wewe au mpendwa wako ametendewa isivyo haki, ni jambo la kawaida kukasirika. (Zab. 4:4) Ingawa hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova hapendezwi na maneno au matendo yanayochochewa na hasira kali. (Yak. 1:20) Tunashughulikia visa vya ukosefu wa haki—iwe ni ndani au nje ya kutaniko—kwa kutumia kanuni za Biblia, hivyo tunaepuka madhara yanayotokana na hasira isiyodhibitiwa. (Rom. 12:17, 19; 1 Pet. 3:9) Hata ikiwa wazazi wako wanafanya mambo ambayo hayamfurahishi Yehova, kumbuka kwamba huhitaji kufuata mfano wao mbaya. Usifikie mkataa kwamba huwezi kumfurahisha Yehova na kwamba huwezi kupata baraka zake. Yehova atakuthawabisha kwa sababu ya jitihada zako za kufanya yaliyo sawa.
YUDA
13. Kwa nini huenda Yuda alikuwa na wasiwasi zamu yake ilipofika ya kusikia maneno ya baba yake?
13 Kisha Yakobo akazungumza na Yuda. Baada ya kusikia maneno ya Yakobo kwa ndugu zake wakubwa, huenda Yuda alikuwa na wasiwasi, kwa kuwa yeye pia alikuwa amefanya makosa fulani mazito. Inaonekana kwamba alishiriki katika kulipora jiji la Shekemu. (Mwa. 34:27) Aliwaunga mkono ndugu zake walipomuuza Yosefu kama mtumwa na kumdanganya baba yao kuhusu jambo hilo. (Mwa. 37:31-33) Baadaye, alilala na Tamari, binti mkwe wake, akidhani kwamba ni kahaba.—Mwa. 38:15-18.
14. Yuda alikuwa amefanya mambo gani mazuri? (Mwanzo 49:8, 9)
14 Hata hivyo, akiongozwa na roho, Yakobo alimbariki tu Yuda na kumpongeza. (Soma Mwanzo 49:8, 9.) Yuda alikuwa ameonyesha kwamba anajali sana hisia za baba yake aliyezeeka. Pia, alikuwa amemwonyesha huruma Benjamini, ndugu yake mdogo zaidi.—Mwa. 44:18, 30-34.
15. Yuda alithawabishwa kwa njia gani?
15 Yakobo alitabiri kwamba Yuda angekuwa kiongozi miongoni mwa ndugu zake. Hata hivyo, ilichukua miaka mingi kabla ya unabii huo kutimizwa. Kwa mara ya kwanza Yuda anatajwa kuwa akiongoza miaka 200 hivi baadaye. Baada ya kutoka Misri kabila hilo liliongoza taifa la Israeli nyikani na kuingia katika Nchi ya Ahadi. (Hes. 10:14) Miaka mingi baadaye, kabila la Yuda liliongoza katika jitihada za kumiliki Nchi ya Ahadi. (Amu. 1:1, 2) Na Daudi, mmoja kati ya wazao wa Yuda, alikuwa mfalme wa kwanza kati ya wafalme wengi kutoka katika kabila hilo. Lakini unabii huo ulitimizwa pia kwa njia nyingine.
16. Unabii unaopatikana kwenye Mwanzo 49:10 ulitimizwaje? (Tazama pia sanduku “Unabii wa Yakobo Aliotoa Alipokuwa Akikaribia Kufa.”)
16 Yakobo alifunua kwamba Mtawala wa kudumu wa wanadamu angetoka katika uzao wa Yuda. (Soma Mwanzo 49:10 na maelezo ya chini.) Mtawala huyo ni Yesu Kristo, ambaye Yakobo alimwita Shilo. Malaika alisema hivi kumhusu Yesu: “Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake.” (Luka 1:32, 33) Yesu anaitwa pia “Simba wa kabila la Yuda.”—Ufu. 5:5.
17. Tunawezaje kumwiga Yehova inapohusu jinsi tunavyowaona wengine?
17 Tunajifunza nini? Yehova alimbariki Yuda ingawa alifanya makosa fulani mazito. Lakini je, inawezekana kwamba ndugu zake walijiuliza Yehova aliona sifa gani nzuri ndani yake? Vyovyote vile, Yehova aliona sifa nzuri za Yuda na akambariki. Tunawezaje kuiga mfano wa Yehova? Mkristo mwenzetu anapopata pendeleo la pekee, mwanzoni huenda tukashawishiwa kukazia fikira udhaifu wake. Lakini ni vema tukumbuke kwamba kwa hakika Yehova anafurahishwa na sifa zake nzuri. Yehova anakazia fikira sifa nzuri za waabudu wake. Acheni tujitahidi kumwiga.
18. Kwa nini tunahitaji kuwa na subira?
18 Jambo lingine tunalojifunza kutokana na kisa cha Yuda ni umuhimu wa kuwa na subira. Sikuzote Yehova hutimiza ahadi zake, lakini hafanyi hivyo kwa njia au wakati tunaotarajia. Uzao wa Yuda haukuanza papo hapo kuongoza watu wa Mungu. Lakini kwa ushikamanifu uliwaunga mkono wale ambao Yehova aliwaweka rasmi kuongoza, iwe ilikuwa ni Musa Mlawi, Yoshua Mwefraimu, au Mfalme Sauli Mbenjamini. Acheni sisi pia tumuunge mkono mtu yeyote ambaye Yehova anamchagua kuongoza miongoni mwetu leo.—Ebr. 6:12.
19. Tunaweza kujifunza nini kumhusu Yehova kutokana na mazungumzo yetu kuhusu unabii wa Yakobo aliotoa alipokuwa akikaribia kufa?
19 Kufikia sasa tumejifunza nini katika mazungumzo yetu kuhusu unabii wa Yakobo aliotoa alipokuwa akikaribia kufa? Ni wazi kwamba “Mungu haoni kama mwanadamu anavyoona.” (1 Sam. 16:7) Yehova ni mwenye subira sana na mwenye kusamehe. Ingawa haendekezi mwenendo mpotovu, hatarajii ukamilifu kutoka kwa waabudu wake. Hata anaweza kuwabariki watu ambao walifanya makosa mazito zamani ikiwa wanatubu kikweli na kutenda yaliyo sawa. Katika makala inayofuata, tutachunguza mambo ambayo Yakobo aliwaambia wanawe wanane waliobaki.
WIMBO 124 Washikamanifu Sikuzote