MAKALA YA 25
WIMBO 96 Kitabu cha Mungu Ni Hazina
Mambo Tunayojifunza Kutokana na Unabii wa Yakobo—Sehemu ya 2
“Alimpa kila mmoja wao baraka inayomfaa.”—MWA. 49:28.
JAMBO KUU
Mambo hususa tunayojifunza kutokana na unabii wa Yakobo kuhusu wanawe wanane aliotoa alipokuwa akikaribia kufa.
1. Katika makala hii tutazungumzia sehemu gani ya unabii wa Yakobo aliotoa alipokuwa akikaribia kufa?
WANA wa Yakobo wamemzunguka baba yao aliyezeeka wakimsikiliza kwa makini anapombariki kila mmoja wao. Kama tulivyozungumzia katika makala iliyotangulia, maneno ya Yakobo kwa Rubeni, Simeoni, Lawi, na Yuda yaliwavutia—na hata huenda yaliwashangaza—wanawe. Hivyo, ni lazima wanajiuliza sasa Yakobo atawaambia nini wanawe wanane waliobaki. Acheni tuone tunaweza kujifunza nini kutokana na maneno yake kwa Zabuloni, Isakari, Dani, Gadi, Asheri, Naftali, Yosefu, na Benjamini.a
ZABULONI
2. Yakobo alimwambia nini Zabuloni, na maneno hayo yalitimizwaje? (Mwanzo 49:13) (Tazama pia sanduku.)
2 Soma Mwanzo 49:13. Yakobo anaonyesha kwamba wazao wa Zabuloni wangeishi kwenye ufuo wa bahari, kaskazini mwa Nchi ya Ahadi. Zaidi ya miaka 200 baadaye, kabila la Zabuloni lilipokea eneo lao la urithi lililokuwa kati ya Bahari ya Galilaya na Bahari ya Mediterania. Musa alitabiri hivi: “Shangilia, Ee Zabuloni, unapotoka nje.” (Kum. 33:18) Huenda hilo lilimaanisha kwamba kabila la Zabuloni lingekuwa na uwezo wa kufanya biashara kwa njia rahisi kwa sababu lilikuwa katikati ya bahari mbili. Vyovyote vile, wazao wa Zabuloni walikuwa na sababu ya kuwa na furaha.
3. Ni jambo gani linaloweza kutusaidia tuwe wenye kuridhika?
3 Tunajifunza nini? Tuna sababu za kuwa na furaha, haidhuru mahali tunapoishi au hali zetu. Ili tuendelee kuwa na furaha, ni lazima turidhike na kile tulicho nacho. (Zab. 16:6; 24:5) Nyakati nyingine, huenda ikawa rahisi zaidi kukazia fikira vitu ambavyo hatuna, badala ya kukazia fikira vitu vizuri ambavyo tunavyo. Hivyo, unapokabili hali mbalimbali, jitahidi kukazia fikira mambo mazuri.—Gal. 6:4.
ISAKARI
4. Yakobo alimwambia nini Isakari, na maneno hayo yalitimizwaje? (Mwanzo 49:14, 15) (Tazama pia sanduku.)
4 Soma Mwanzo 49:14, 15. Yakobo anampongeza Isakari kwa kuwa mfanyakazi mwenye bidii kwa kumlinganisha kwa njia nzuri na punda mwenye mifupa migumu—mnyama anayeweza kubeba mizigo mizito. Yakobo alisema pia kwamba Isakari angepata nchi inayopendeza. Kupatana na maneno ya Yakobo, wazao wa Isakari walipata ardhi yenye rutuba na inayozaa iliyo kando ya Mto Yordani. (Yos. 19:22) Hapana shaka kwamba walifanya kazi kwa bidii ili kuilima ardhi yao. Lakini pia, walifanya kazi kwa bidii ili kuwanufaisha wengine. (1 Fal. 4:7, 17) Kwa mfano, kabila la Isakari lilikuwa tayari kuunga mkono taifa lao katika kupigana vita, kama walivyofanya wakati wa Mwamuzi Baraka na nabii wa kike Debora.—Amu. 5:15
5. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kufanya kazi kwa bidii?
5 Tunajifunza nini? Yehova anathamini tunapofanya kazi kwa bidii katika utumishi wake kama tu alivyothamini bidii ya kabila la Isakari. (Mhu. 2:24) Fikiria mfano wa akina ndugu wanaofanya kazi kwa bidii ili kulitunza kutaniko. (1 Tim. 3:1) Ndugu hao hawahitaji kupigana katika vita halisi, lakini ni lazima wafanye jitihada ili kuwalinda watu wa Mungu dhidi ya hatari za kiroho. (1 Kor. 5:1, 5; Yuda 17-23) Pia, wanafanya kazi kwa bidii ili kutayarisha na kutoa hotuba zenye kutia moyo ambazo zitaliimarisha kutaniko.—1 Tim. 5:17.
DANI
6. Kabila la Dani lilipokea mgawo gani? (Mwanzo 49:17, 18) (Tazama pia sanduku.)
6 Soma Mwanzo 49:17, 18. Yakobo anamfananisha Dani na nyoka anayepambana na maadui walio wakubwa zaidi kuliko yeye, kama vile farasi wa vita na mpandaji wake. Kabila la Dani lingethibitika kuwa hatari kwa maadui wa Israeli. Wakati wa safari yao kuelekea Nchi ya Ahadi, kabila la Dani lililinda taifa la Israeli likiwa “kikosi cha nyuma cha kulinda.” (Hes. 10:25) Huo ulikuwa mgawo muhimu, ingawa kabila la Dani halikuonwa na taifa lote lilipokuwa likitimiza mgawo huo.
7. Tunapaswa kukumbuka nini kuhusu mgawo wowote wa kitheokrasi ambao tunatimiza?
7 Tunajifunza nini? Je, umewahi kutimiza mgawo fulani ambao ni kana kwamba wengine hawakuutambua? Huenda ulisaidia kusafisha na kudumisha Jumba la Ufalme, ulijitolea kufanya kazi kwenye kusanyiko la mzunguko au la eneo, au kufanya kazi fulani nyingine. Ikiwa ndivyo, unastahili kupongezwa! Sikuzote kumbuka kwamba Yehova anatambua na anathamini kila jambo unalofanya kwa ajili yake. Anathamini hasa unapomtumikia, si kwa sababu unataka kusifiwa na wengine, bali kwa sababu unataka kumwonyesha kutoka moyoni jinsi unavyompenda.—Mt. 6:1-4.
GADI
8. Ni jambo gani lililofanya iwe rahisi zaidi kwa kabila la Gadi kushambuliwa katika Nchi ya Ahadi? (Mwanzo 49:19) (Tazama pia sanduku.)
8 Soma Mwanzo 49:19. Yakobo alitabiri kwamba Gadi angevamiwa na kundi la wavamizi. Zaidi ya miaka 200 baadaye, kabila la Gadi liliishi katika eneo lililo mashariki ya Mto Yordani—eneo lililopakana na mataifa adui. Hivyo, ilikuwa rahisi zaidi kwa kabila hilo kushambuliwa. Hata hivyo, kabila la Gadi lilitaka kuishi hapo kwa sababu kulikuwa na malisho mazuri kwa ajili ya mifugo yao. (Hes. 32:1, 5) Inaonekana kwamba watu wa kabila la Gadi walikuwa jasiri. Zaidi ya hilo, walikuwa na uhakika kwamba Yehova angewasaidia kulinda ardhi aliyowapa dhidi ya kikundi chochote cha wavamizi. Hata walituma majeshi yao kwa miaka mingi kwenda kuyasaidia makabila mengine kumiliki sehemu iliyobaki ya Nchi ya Ahadi magharibi ya Mto Yordani. (Hes. 32:16-19) Walikuwa na uhakika kwamba Yehova angewalinda wake zao na watoto wao wakati wanaume hao walipokuwa vitani. Yehova aliwabariki kwa sababu ya ujasiri wao na roho yao ya kujidhabihu.—Yos. 22:1-4.
9. Ikiwa tunamtumaini Yehova, tutafanya maamuzi gani maishani?
9 Tunajifunza nini? Ili tumtumikie Yehova licha ya changamoto, ni lazima tuendelee kumtumaini. (Zab. 37:3) Wengi leo wanaonyesha kwamba wanamtumaini Yehova kwa kujidhabihu ili kuunga mkono miradi ya ujenzi ya kitheokrasi, kutumikia kwenye maeneo yenye uhitaji mkubwa, au kushughulikia migawo mingine. Wanafanya hivyo kwa sababu wana uhakika kwamba sikuzote Yehova atawatunza.—Zab. 23:1.
ASHERI
10. Kabila la Asheri lilishindwa kufanya mambo gani? (Mwanzo 49:20) (Tazama pia sanduku.)
10 Soma Mwanzo 49:20. Yakobo alitabiri kwamba kabila la Asheri lingekuwa na ufanisi mwingi, na hivyo ndivyo ilivyokuwa. Eneo la urithi la kabila la Asheri lilikuwa na baadhi ya maeneo yenye ardhi yenye rutuba zaidi katika Israeli yote. (Kum. 33:24) Pia, lilipakana na Bahari ya Mediterania na lilitia ndani bandari ya biashara ya Wafoinike yenye ufanisi iliyokuwa Sidoni. Hata hivyo, kabila la Asheri lilishindwa kuwaondoa Wakanaani kutoka kwenye nchi hiyo. (Amu. 1:31, 32) Huenda ufanisi wa kabila la Asheri, pamoja na kuathiriwa vibaya na Wakanaani, kulisababisha kabila hilo lipunguze bidii yake kwa ajili ya ibada safi. Kabila la Asheri halikuwa tayari kusaidia wakati Mwamuzi Baraka alipoomba watu wajitolee kupigana dhidi ya majeshi ya Wakanaani. Matokeo ni kwamba kabila hilo lilikosa kushiriki katika ushindi wa kimuujiza “kando ya maji ya Megido.” (Amu. 5:19-21) Ni lazima watu wa kabila la Asheri waliaibika walipowasikia Baraka na Debora wakiimba wimbo wa ushindi ulioongozwa na roho, uliotia ndani maneno haya: “Watu wa kabila la Asheri waliketi kizembe kando ya bahari.”—Amu. 5:17.
11. Kwa nini tunahitaji kudumisha mtazamo wenye usawaziko inapohusu vitu vya kimwili?
11 Tunajifunza nini? Tungependa kumpa Yehova kilicho bora. Ili kufanya hivyo, tunahitaji kukataa mtazamo wa ulimwengu kuelekea vitu vya kimwili na mali. (Met. 18:11) Tunajitahidi kudumisha usawaziko inapohusu pesa. (Mhu. 7:12; Ebr. 13:5) Haturuhusu kufuatia vitu vya kimwili visivyo vya lazima kutuzuie kumtumikia Mungu. Badala yake, tunajitahidi kumpa Yehova kilicho bora sasa, inapohusu muda wetu na nguvu zetu, tukijua kwamba tutakuwa na maisha yenye kustarehesha kikweli na salama wakati ujao.—Zab. 4:8.
NAFTALI
12. Huenda maneno ya Yakobo kwa Naftali yalitimizwaje? (Mwanzo 49:21) (Tazama pia sanduku.)
12 Soma Mwanzo 49:21. “Maneno yanayovutia sana” ambayo Yakobo alitaja huenda yanarejelea njia ambayo Yesu alizungumza wakati wa huduma yake. Yesu, ambaye alijulikana kwa njia yake ya kufundisha yenye matokeo, alifanya jiji la Kapernaumu lililo katika eneo la Naftali kuwa “jiji lake.” (Mt. 4:13; 9:1; Yoh. 7:46) Isaya alitabiri kwamba watu wa Zabuloni na Naftali wangeona “nuru kuu.” (Isa. 9:1, 2) Kupitia mafundisho yake, Yesu alikuwa “nuru ya kweli inayowaangazia watu wa aina zote.”—Yoh. 1:9.
13. Tunaweza kuhakikishaje kwamba usemi wetu unamfurahisha Yehova?
13 Tunajifunza nini? Mambo tunayosema na jinsi tunavyoyasema ni muhimu kwa Yehova. Tunawezaje kutumia “maneno yanayovutia sana” ambayo yanamfurahisha Yehova? Tunaweza kusema ukweli. (Zab. 15:1, 2) Tunaweza kuwajenga wengine kwa kuwa wepesi wa kuwapongeza na kuepuka kuwachambua au kulalamika. (Efe. 4:29) Na tunaweza kujiwekea lengo la kuwa na ustadi zaidi wa kuanzisha mazungumzo ambayo yanaweza kutupatia fursa za kutoa ushahidi.
YOSEFU
14. Unabii kuhusu Yosefu ulitimizwaje? (Mwanzo 49:22, 26) (Tazama pia sanduku.)
14 Soma Mwanzo 49:22, 26. Ni lazima Yakobo alijivunia sana mwanaye Yosefu. Yehova alikuwa “[amemchagua] kutoka kati ya ndugu zake.” Yakobo alimwita Yosefu “chipukizi la mti unaozaa matunda mengi.” Yakobo ndiye aliyekuwa mti, na Yosefu alikuwa chipukizi lake. Yosefu alikuwa mzaliwa wa kwanza wa Raheli, mke wake mpendwa. Yakobo alionyesha kwamba Yosefu angepokea urithi maradufu ambao Rubeni—mzaliwa wa kwanza wa Yakobo kwa Lea, mke wake—alipoteza. (Mwa. 48:5, 6; 1 Nya. 5:1, 2) Katika utimizo wa unabii huo, wazao wa Efraimu na Manase, wana wa Yosefu, walipokea urithi wa ardhi kama makabila mawili tofauti.—Mwa. 49:25; Yos. 14:4.
15. Yosefu alitendaje alipokabili ukosefu wa haki?
15 Pia, Yakobo anataja kuhusu wapiga mishale ambao “[walimpiga Yosefu] kwa mishale na kuendelea kuwa na uadui dhidi yake.” (Mwa. 49:23) Hao walikuwa ndugu zake waliomwonea wivu, ambao walimsababishia ukosefu mwingi wa haki aliopitia. Hata hivyo, Yosefu hakuwachukia ndugu zake au kumlaumu Yehova. Badala yake, kama Yakobo alivyosema, “Upinde [wa Yosefu] ulibaki mahali pake, na mikono yake ikaendelea kuwa na nguvu na myepesi.” (Mwa. 49:24) Yosefu alimtegemea Yehova wakati wa majaribu yake, na hakuwasamehe tu ndugu zake, bali pia aliwatendea kwa fadhili. (Mwa. 47:11, 12) Yosefu aliruhusu majaribu aliyopitia yaboreshe utu wake. (Zab. 105:17-19) Matokeo ni kwamba Yehova aliweza kumtumia kwa njia kubwa.
16. Tunawezaje kumwiga Yosefu tunapokabili majaribu?
16 Tunajifunza nini? Kamwe tusiruhusu majaribu yatutenganishe na Yehova au waabudu wenzetu. Kumbuka kwamba huenda Yehova akaruhusu majaribu ya imani yawe sehemu ya mazoezi yetu. (Ebr. 12:7, maelezo ya chini) Mazoezi hayo yanaweza kutusaidia kusitawisha na kuboresha sifa za Kikristo, kama vile kuonyesha rehema na kusamehe. (Ebr. 12:11) Yehova atatuthawabisha kwa sababu ya uvumilivu wetu kama alivyomthawabisha Yosefu.
BENJAMINI
17. Unabii kumhusu Benjamini ulitimizwaje? (Mwanzo 49:27) (Tazama pia sanduku.)
17 Soma Mwanzo 49:27. Yakobo alitabiri kwamba Wabenjamini wangekuwa na uwezo mkubwa wa kupigana kama mbwamwitu. (Amu. 20:15, 16; 1 Nya. 12:2) Ilikuwa “asubuhi” katika ufalme wa Israeli wakati kabila la Benjamini lilipotoa mfalme wa Israeli wa kwanza, Sauli. Alithibitika kuwa mpiganaji hodari dhidi ya Wafilisti. (1 Sam. 9:15-17, 21) Miaka mingi baadaye, wakati wa ile “jioni,” Malkia Esta na Waziri Mkuu Mordekai, ambao wote walikuwa Wabenjamini, waliwaokoa Waisraeli ili wasiangamizwe na Milki ya Uajemi.—Esta 2:5-7; 8:3; 10:3.
18. Tunawezaje kuiga ushikamanifu wa Wabenjamini inapohusu mipango ya Yehova?
18 Tunajifunza nini? Bila shaka, Wabenjamini walijivunia kuona mmoja wao akiwa mfalme na kutimiza unabii. Hata hivyo, Yehova alipohamisha ufalme kwa Daudi wa kabila la Yuda, mwishowe Wabenjamini waliunga mkono badiliko hilo. (2 Sam. 3:17-19) Miaka mingi baadaye, wakati makabila mengine yalipoasi, Wabenjamini waliendelea kuwa washikamanifu kwa kabila la Yuda na mfalme aliyewekwa rasmi na Yehova. (1 Fal. 11:31, 32; 12:19, 21) Acheni sisi pia tuwaunge mkono kwa ushikamanifu wale ambao Yehova anawachagua kuongoza watu wake leo.—1 The. 5:12.
19. Tunaweza kunufaikaje kutokana na unabii wa Yakobo aliotoa alipokuwa akikaribia kufa?
19 Unabii wa Yakobo aliotoa alipokuwa akikaribia kufa unaweza kutunufaisha. Kuchunguza jinsi unabii huo ulivyotimizwa kunaimarisha imani yetu kwamba unabii mwingine mbalimbali katika Neno la Yehova utatimizwa pia. Na kuchunguza jinsi wana wa Yakobo walivyopata baraka kunatusaidia kuelewa vizuri zaidi jinsi tunavyoweza kumfurahisha Yehova.
WIMBO 128 Kuvumilia Mpaka Mwisho
a Yakobo alipowabariki wanawe wanne wa kwanza, Rubeni, Simeoni, Lawi, na Yuda, alitoa baraka akianzia kwa mkubwa hadi mdogo. Hata hivyo, alipowabariki wanawe wengine wanane hakufuata mfuatano wao wa kuzaliwa.