GEORGIA
Upendo wa Kweli wa Kikristo Haushindwi Kamwe
Igor: Sote tulishirikiana na kikundi cha Mashahidi mjini Tkvarcheli, Abkhazia. Kwa kuwa kutaniko ambalo kikundi hicho kilishirikiana nalo lilikuwa kilomita 85 hivi jijini Jvari, kila mwezi nilisafiri kwenda Jvari ili kuchukua machapisho ya Biblia kwa ajili ya kikundi hicho. Mara tu baada ya Muungano wa Sovieti kuvunjika mwaka 1992, watu wa eneo la Abkhazia walitaka kugawanya jimbo hilo. Vita kati ya waasi na jeshi la Georgia vilianza, ambavyo vilifanya hali ziwe ngumu sana.
Gizo Narmania na Igor Ochigava
Ndugu hawa wawili walishirikiana kuwasaidia waamini wenzao wakati wa vita huko Abkhazia.
Gizo: Nilibatizwa nikiwa na umri wa miaka 21, mwaka mmoja tu kabla ya mapigano hayo kuanza. Vita vilipoanza, kwa muda mfupi akina ndugu waliogopa sana na hawakujua la kufanya. Hata hivyo, Igor, ambaye sikuzote amekuwa mchungaji mzuri, alitutia moyo kwa kusema hivi: “Huu ndio wakati ambao watu wanahitaji faraja. Tutaendelea kuwa imara kiroho ikiwa tu tutaendelea kuhubiri.” Hivyo, kwa uangalifu mkubwa, kila siku tulijitahidi kuzungumza na jirani zetu kuhusu ujumbe wenye kufariji katika Neno la Mungu.
Igor: Kwa sababu ya vurugu, hatungeweza kutumia njia tuliyozoea ya kwenda na kurudi kutoka Jvari kuchukua machapisho. Kwa kuwa nililelewa katika eneo hilo, nilifanikiwa kupata njia nzuri iliyopitia kwenye mashamba ya chai na milimani. Lakini bado kulikuwa na hatari ya kukutana na kikundi cha watu wenye silaha au kukanyaga bomu la ardhini. Hata hivyo, sikutaka kuhatarisha uhai wa ndugu zangu, kwa hiyo nilisafiri peke yangu kila mwezi. Kwa msaada wa Yehova, nyakati zote nilifanikiwa kupata machapisho yaliyotuwezesha kubaki imara kiroho.
Ingawa hakukuwa na mapigano katika mji wa Tkvarcheli, baada ya muda mfupi mji huo ulizingirwa, na tukaanza kupata hali ngumu zinazosababishwa na vita. Majira ya baridi kali yalipokaribia, chakula kilianza kupungua na tukawa na wasiwasi ikiwa tungeweza kubaki hai. Tulifurahi sana kusikia kwamba ndugu zetu huko Jvari walifanya mipango ili kutusaidia!
Gizo: Siku moja, Igor aliniuliza ikiwa nyumba yetu ingeweza kutumiwa kwa ajili kutunza na kugawanya chakula kilichoandaliwa na ndugu zetu. Alikuwa anapanga kuleta chakula kutoka jiji la Jvari. Tulihofia usalama wake kwa kuwa tulijua kwamba angehitaji kupita kwenye vituo kadhaa vya ukaguzi, na huenda angekutana na watu wenye silaha au wezi.—Yoh. 15:13.
Tulifurahi sana Igor aliporudi salama salimini siku chache baadaye, akiendesha gari lililojaa chakula ambacho kingetutosha sote kwa miezi yote ya majira ya baridi kali! Katika kipindi hicho kigumu, tulijionea waziwazi kwamba upendo wa kweli wa Kikristo haushindwi kamwe.—1 Kor. 13:8.