Jumapili, Novemba 2
Tusiendelee kulala usingizi kama wengine wanavyofanya, bali tukae macho na kutunza akili zetu.—1 The. 5:6.
Tunahitaji upendo ili tukae macho na kuendelea kutunza akili zetu. (Mt. 22:37-39) Kumpenda Mungu kunatusaidia kuendelea kuhubiri licha ya changamoto zozote ambazo huenda tukakabili. (2 Tim. 1:7, 8) Kwa kuwa tunawaonyesha upendo hata watu ambao hawamtumikii Yehova, tunaendelea kuhubiri, hata kutoa ushahidi kupitia simu na barua. Tunaendelea kutumaini kwamba siku moja jirani zetu watafanya mabadiliko na kuanza kutenda mambo yanayofaa. (Eze. 18:27, 28) Pia, tunawapenda ndugu na dada zetu. Tunaonyesha upendo huo kwa “kutiana moyo na kujengana.” (1 The. 5:11) Kama wanajeshi wanaotumikia vitani bega kwa bega, sisi pia tunatiana moyo. Hatuwezi kamwe kuwaumiza kimakusudi ndugu na dada zetu au kulipa ubaya kwa ubaya. (1 The. 5:13, 15) Pia, tunaonyesha upendo kwa kuwaheshimu ndugu wanaoongoza kutanikoni.—1 The. 5:12. w23.06 10 ¶6; 11 ¶10-11
Jumatatu, Novemba 3
[Yehova] akisema jambo, je, hatalitenda?—Hes. 23:19.
Njia moja tunayoweza kuimarisha imani yetu ni kwa kutafakari kuhusu fidia. Fidia inatuhakikishia kwamba ahadi za Mungu zitatimia. Tunapotafakari kwa makini kwa nini fidia ilitolewa na mambo yaliyohusika, tunaimarisha imani yetu kwamba ahadi ya Mungu kuhusu kuishi milele katika ulimwengu bora itatimizwa kwa uhakika. Kwa nini tunaweza kusema hivyo? Fidia ilihusisha nini? Yehova alimtuma Mwana wake mpendwa mzaliwa wa kwanza, mwandamani wake wa karibu zaidi, atoke mbinguni na kuzaliwa akiwa mwanadamu mkamilifu. Alipokuwa duniani, Yesu alivumilia hali ngumu mbalimbali. Kisha akateswa na kufa kifo chenye maumivu. Yehova alilipa bei kubwa sana! Mungu wetu mwenye upendo hangeruhusu kamwe Mwana wake ateseke na kufa ili tu kutuandalia maisha bora lakini ya muda mfupi. (Yoh. 3:16; 1 Pet. 1:18, 19) Kwa kuwa alilipa bei kubwa sana, Yehova atahakikisha kwamba tutaishi milele katika ulimwengu mpya. w23.04 27 ¶8-9
Jumanne, Novemba 4
Ewe Kifo, yako wapi maumivu yako makali?—Hos. 13:14.
Je, Yehova anatamani kuwafufua wafu? Bila shaka, anatamani kuwafufua. Aliwaongoza baadhi ya waandikaji wa Biblia kuandika kuhusu ahadi ya ufufuo wa wakati ujao. (Isa. 26:19; Ufu. 20:11-13) Na Yehova anapotoa ahadi sikuzote yeye huitimiza. (Yos. 23:14) Kwa kweli, Yehova anatamani kuwafufua waliokufa. Fikiria maneno ambayo Ayubu alisema. Alikuwa na uhakika kwamba hata akifa, Yehova angekuwa na hamu kubwa ya kumwona akiishi tena. (Ayu. 14:14, 15, maelezo ya chini) Bado Yehova anahisi hivyo kuelekea waabudu wake wote waliokufa. Anatamani kuwafufua, wakiwa na afya nzuri na furaha. Namna gani mabilioni ya watu ambao walikufa bila kupata nafasi ya kujifunza ukweli kumhusu Yehova? Mungu wetu mwenye upendo anataka kuwafufua pia. (Mdo. 24:15) Anataka wawe na nafasi ya kuwa rafiki zake na kuishi milele duniani.—Yoh. 3:16. w23.04 9 ¶5-6