Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 7/1 kur. 5-8
  • Je! Serikali ya Kibinadamu Yaweza Kutimiza Mahitaji Hayo?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Serikali ya Kibinadamu Yaweza Kutimiza Mahitaji Hayo?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JITIHADA ZA WANADAMU ZAENDELEA
  • JE! JITIHADA ZA SASA ZINAFANIKIWA?
  • MAMBO WASIYOWEZA WANADAMU KUFANYA
  • NAMNA AMBAYO UFALME WA MUNGU UTAKUJA
  • Ufalme wa Mungu—Tumaini Peke Yake
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Serikali
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Serikali ya Mungu—Tumaini Pekee La Wanadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Ufalme wa Mungu Utafanya Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 7/1 kur. 5-8

Je! Serikali ya Kibinadamu Yaweza Kutimiza Mahitaji Hayo?

WAKATI mmoja ilidhaniwa “kwamba Kanisa duniani ndilo lililokuwa Ufalme wa Mungu.”a Fundisho hilo lilitokea kwa sababu Kanisa Katoliki la Rumi ndilo lililokuwa lenye nguvu zaidi ulimwenguni. Kufikia wakati uliojulikana kama Enzi za Katikati (karne ya 5 mpaka ya 15) mapapa walikuwa na mamlaka ya kisiasa iliyolingana na ya wafalme. Walikuwa na amri juu ya majeshi yenye nguvu. Katika kitabu chake History of the Christian Church, John F. Hurst anaeleza hivi: “Mapapa walikuwa na mamlaka kama ya wafalme, nao waling’ang’ana kwa kadiri walivyoweza kusudi wawe waamuzi katika mambo ya kiserikali.”

Viongozi wa Kanisa hilo walidai kwamba walitawala kwa mamlaka waliyopewa na Mungu. Baadaye, wafalme wa mataifa mbalimbali pia walidai haki ya kimungu ya kutawala. Kitabu New Catholic Encyclopedia chasema hivi: “Wazo la haki ya kimungu liliwaweka wafalme wa mataifa katika hali ya kutetea mamlaka yao kuwa ya kimungu sawa na ile ya papa.”

Walakini je! mapapa na watawala wengine waliodai kutawala kwa haki ya kimungu walitimiza mahitaji ya watu ya kutoa serikali nzuri? Je! raia zao walifurahia maisha, uhuru na furaha?

Sivyo, haikuwa hivyo kwao! Mahali pake, tawala hizo zilikuwa zenye udhalimu na uonezi mbaya sana. Watu walikusanywa wapigane vita vya kipumbavu na kushiriki katika vita vya kidini vyenye umwagaji wa damu ambavyo viliharibu maisha na furaha ya mamilioni ya watu. Vilevile, baraza kuu za kuhukumu wazushi wa dini zilifanywa, na maelfu ya watu kuteswa mpaka kufa katika njia zenye kuchukiza sana. Hakika, namna ilivyo kumvunjia Mungu heshima kwa kuhusianisha ufalme wake na utawala wa kanisa, au na utawala wa wafalme waliodai kuwa na haki ya kimungu!

JITIHADA ZA WANADAMU ZAENDELEA

Katika nyakati za karibuni zaidi, maoni ya kidini yalibadilishwa. “Wazo la wataalamu wengine wa kidini wa kisasa,” chaeleza kitabu The Dictionary of the Apostolic Church kilichochapwa katika mwaka 1916, ni “kwamba ulimwengu huu kama tuujuavyo utasitawi chini ya uongozi wa Kikristo mpaka uwe Ufalme huo.” Lakini je! umekuwa hivyo?

Wakati wa maisha ya mamilioni ambao wangali wanaishi, yanayoitwa mataifa ya Kikristo yamekuwa na daraka la umwagaji mkubwa zaidi wa damu katika historia ya kibinadamu. Mwanahistoria ya Kanisa Roland H. Bainton alisema hivi: “Makanisa katika United States (Amerika) sana sana yalikuwa na maoni ya kuwa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilikuwa ni vita ya kidini.”

Kulingana na wanakanisa Waamerika, Bainton akaeleza, “hivyo vilikuwa vita vitakatifu. . . . Wajeremani walikuwa Waharabu Wabaya. Kuwaua kulikuwa ni kuisafisha dunia kutokana na wanyama wenye kutisha.” Vivyo hivyo, askofu wa London (Uingereza), A. F. Winnington-Ingram, alisihi Waingereza hivi: “Waueni Wajeremani—waueni . . . Kama ambavyo nimesema mara elfu, naiona kuwa ni vita ya kutakasa.”

Hali Wajeremani walidai pia kuwa Wakristo! Hivyo, wakati uo huo, askofu mkuu wa Kikatoliki wa Cologne, Ujeremani, alikuwa akiwaambia askari Wajeremani hivi: “Mungu yu pamoja nasi katika kupigania haki huku ambako tumelazimishwa kufanya. Twawaamuru ninyi katika jina la Mungu, mpigane hata mpaka tone la mwisho la damu yenu kwa ajili ya utukufu na heshima ya nchi hii.”

Miaka zaidi ya 20 baadaye, mwaka 1939, mataifa yaliingia katika vita ya ulimwengu ya pili. Kwa mara nyingine mataifa yaliyoshiriki yalidai kuwa ya Kikristo. Kwa wazi, ulimwengu kama tuujuavyo haukusitawi ukiwa chini ya uongozi wa Ukristo kufikia kuwa ufalme wa Mungu.

Hata hivyo, namna gani miaka yapata 35 tangu kumalizika kwa Vita ya Ulimwengu ya Pili mwaka 1945? Je! inaonekana sasa kwamba mwishowe serikali za kibinadamu zinatimiza mahitaji ya wanadamu?

JE! JITIHADA ZA SASA ZINAFANIKIWA?

Mahali pa kuona matumaini yao ya fanaka yakitimizwa, leo watu wanaona kuenea kwa matatizo ya ulimwengu pote. Kwa kweli, kushindwa kwa wanadamu kumezidi sana hata kufikia kadiri mpya inayohatirisha ustaarabu wenyewe. Ebu fikiria jitihada za wanadamu za kuondoa vita. Je! zimefanikiwa?

Hata kidogo! Tangu mwaka 1945 zaidi ya watu milioni 25 wameuawa katika vita vipatavyo 150 vilivyopiganwa kuzunguka dunia. Katika siku yo yote ile, kumekuwako, kwa wastani, vita 12 vikiendelea mahali fulani ulimwenguni. Serikali za kibinadamu hutumia zaidi ya shilingi 7,500,000,000 (2,500,000,000Z) kwa siku moja kwa ajili ya kujitayarisha kijeshi, zikitumia fedha ambazo kama si hivyo zingetumiwa kwa ajili ya ujenzi, kuifanya ardhi iwe bustani, elimu, uchunguzi, na mengineyo. Lo! namna zilivyoshindwa kutimiza mahitaji ya watu!

Jambo la akili lingekuwa kwamba serikali zikusanyike na kukubaliana kuacha kuunda silaha. Lakini zinafanya hivyo? Haziwezi kufikia mapatano. Kwa hiyo zinaendelea kushindana kuunda silaha ili kuhifadhi ‘usawa wa kuogopana.’ Kiangazi kilichopita katibu wa serikali ya United States (Amerika), Cyrus Vance, alitoa wazo fulani juu ya uwezo wa kuharibu ambao nchi yake inao, kwa kusema hivi:

“Mingine ya mizinga ya leo ina—katika silaha moja—zaidi ya mara tano ya mlipuko wa baruti ulioangushwa na ndege zetu zote za kubeba makombora, katika sehemu zote, katika Vita ya Ulimwengu ya Pili yote. Nyingi za silaha zetu ni ndogo zaidi kuliko hizo. Walakini kwa ujumla tuna silaha za nuklea na makombora zaidi ya 9,000 zenye kuchukuliwa na mizinga na ndege zenye kuruka mwendo mrefu za kubeba makombora. Urusi ina yapata 5,000 inayoelekezwa kwetu—na uwezo wa kuongeza hesabu hiyo kwa kadiri kubwa sana. Mojawapo au mbili ya hizo yaweza kufagilia mbali mji mkubwa kama Milwaukee [wenye idadi ya watu kubwa kidogo kuliko Nairobi].”

Uwezo mkubwa kama nini wa kuharibu kabisa dunia na kila kitu kilicho hai juu yake! Je! uwezo huo wa uharibifu wa nuklea unakufanya ujione kuwa salama? Je! unatokeza ‘uzima, uhuru na furaha’ kwako na kwa wapendwa wako? Yaelekea sivyo.

Lakini huenda ukawa unahangaishwa zaidi na kushindwa kwa serikali za kibinadamu kuzuia uvunjaji wa sheria. Kama vile alivyoandika mtunga mashairi mwenye kupewa tuzo la Nobel Albert Szent-Gyorgyi, M.D., wa United States: “Hatuwezi kuondoka nje katika mji wetu giza likiisha ingia kwa ajili ya kuogopa kunyang’anywa au kuuawa nasi hatujioni salama hata nyumbani.” Kwa kusikitisha, uvunjaji wa sheria umefanya maelfu ya watu watumwa nyumbani mwao! Nazo serikali zi hoi zisiweze kurekebisha hali hiyo.

Pamoja na hayo, mamilioni ya watu wanakufa njaa ulimwenguni pote, hali chakula katika sehemu fulani kimejazana katika ghala. Walakini hata katika nchi ambako kuna chakula cha ziada, bei zinapanda juu sana kwa haraka hata kwamba wengi wanashindwa kununua chakula cha kuhifadhi afya yao. Kushindwa kwa serikali za kibinadamu kutatua tatizo hilo kunahuzunisha moyo kweli kweli.

Kisha kuna tatizo la kupata nguvu za kuendesha vitu. Kuna nguvu nyingi sana ambazo zinarudishwa upya, zisizochafua kutoka kwa jua, upepo, mito, maziwa na bahari. Walakini serikali za kibinadamu zimefanya nini? Kwa kukosa ufahamu wa kimbele inasikitisha kwamba zimetumia vibaya akiba za mafuta na gas (mvuke) zisizoweza kufanywa upya, na kwa kufanya hivyo vilevile zimeitia sumu hewa tunayopumua kwa kadiri fulani.

Uchunguzi wa jitihada za kibinadamu za kusimamia mambo ya dunia unaongoza kwenye kukata shauri gani?

MAMBO WASIYOWEZA WANADAMU KUFANYA

Shauri hili: Wanadamu wameshindwa kusimamisha serikali yenye kufaulu ambayo inatosheleza mahitaji ya watu. “Kila ustaarabu uliopata kuwapo ulianguka mwishowe,” Katibu wa zamani wa Nchi ya U.S. (Amerika) Henry Kissinger akasema. “Historia ni hadithi ya jitihada zilizoshindwa, ya tamaa ambazo hazikutimizwa . . . Kwa hiyo, kama mwanahistoria, mtu analazimika kuishi akifahamu kwamba kuna msiba usioepukika.”

Kwa kweli, unapolifikiria jambo hilo, kuna sababu yo yote ya kutazamia viongozi wa nchi leo waweze kutatua matatizo ya ulimwengu ambayo ni magumu zaidi sana kuliko yale ambayo viongozi wa wakati uliopita walishindwa kutatua? James M. Fallows, aliyetumikia kama mwandishi mkuu wa hotuba za Rais Carter kwa muda wa miaka mwili u nusu, aliandika karibuni hivi: “Nafahamu namna lilivyo jambo lisilowezekana kabisa kubadili mambo mengi katika serikali. . . . Sasa naelekea sana kuwa na shaka kama Rais Carter au mtu mwingine ye yote anaweza kuibadili serikali hii.”

Hata hivyo, je! twapaswa kushangaa kuona wanadamu wakishindwa mara nyingi kujitawala? Sivyo, ikiwa sisi ni wanafunzi wa Biblia. Uchunguzi wa jitihada za wanadamu za kujitawala unakazia ukweli wa tangazo hili la kimungu: “Mwanadamu hawezi kuongoza mwendo wake, wala mwanadamu hana uwezo wa kuongoza hatua zake anapoenenda.”​—Yer. 10:23, The Jerusalem Bible

Hata hivyo, tangu wanadamu wawili wa kwanza walipoasi mamlaka Yake, Mungu Mwenye Nguvu Zote ameruhusu wanadamu wajaribu serikali za kujitawala. Sababu gani? Ili kutoa somo la kitendo kwa wanadamu na malaika. Nalo ni jambo gani wangepaswa kujifunza? Ni jambo lile lile tu ambalo tumeona: Kwamba wanadamu hawana uwezo wa kujiongoza wenyewe kwa njia yenye kufanikiwa. Hivyo tungepaswa kujifunza jambo hili vilevile: Kwamba, ijapokuwa serikali za kibinadamu zimetenda kwa ruhusa ya Mungu, wanadamu wanahitaji ufalme wa Mungu kusudi wafurahie namna ya ulimwengu ambao sote tungependa kuishi ndani yake.

NAMNA AMBAYO UFALME WA MUNGU UTAKUJA

Walakini, huenda mtu akapinga hivi: “Je! si ni lazima wanadamu wajaribu kutimiza mahitaji ambayo watu wanatazamia serikali itimize? Je! Mungu hatazamii jambo hilo? Ni kwa njia gani nyingine ulimwengu utafanywa kuwa mahali pazuri zaidi tusipojitahidi kutokeza serikali nzuri?”

Kwa sababu ya fundisho la makanisa kwamba Mungu atatumia wanadamu ili kusimamisha ufalme wake, dai hilo linafahamika. Walakini Biblia haifundishi kwamba Ufalme huo utakuja kupitia kwa jitihada za wanadamu. Yesu Kristo alikataa kuchukuliwa awe mfalme wa kibinadamu. Yeye alisema hivi: “Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu.” (Yohana 6:15; 18:36) Kitabu The Zondervan Pictorial Encyclopedia of the Bible chasema hivi kwa usahihi:

“Ufalme wa Mungu haumaanishi wakati wo wote tendo linalochukuliwa na wanadamu au tengenezo ambalo wamelisimamisha. Hata wazo la kujitahidi kusimamisha ufalme wa Mungu liwe bora namna gani maneno yanayotumiwa na Biblia hayapatani hata kidogo na lugha ya wataalamu wa elimu ya kidini wa kisasa wenye kujitegemea. Ufalme ni tendo la kimungu, si jambo linalotokezwa na wanadamu wala si jambo hata linalotokezwa na Wakristo waliojiweka wakf.”

Kwa hiyo, basi, ufalme wa Mungu utakujaje katika kujibu sala za Wakristo? Angalia vizuri jibu la Biblia. Baada ya kusimulia juu ya serikali za kibinadamu na ubatili wazo, inasema hivi: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaangamizwa milele. . . . Utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”​—Dan. 2:44.

Je! jambo hilo linaonekana kuwa kali au lisilo la haki kwa upande wa Mungu—kuharibu serikali za kibinadamu na kuitengezea njia serikali yake? Linaweza kuonekana kuwa hivyo kwa wanadamu wanaotaka kuendeleza milele namna za kisasa za serikali zisizotosheleza. Walakini kwa umati ule unaotazamia serikali kamilifu ya Mungu, na ambao wataokoka, litakuwa jambo la kuwa na furaha tele. Akitaja juu ya utawala wa hizo “mbingu mpya” umiminapo baraka juu ya jamii ya wanadamu duniani, Yehova anasema hivi: “Furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo.”​—Isa. 65:17-19.

Kwa hakika, basi, kwa sababu ya kushindwa kwa wanadamu kutokeza serikali inayotimiza mahitaji ya watu, je! sote hatukubali kwamba ni wakati unaofaa kwa Mungu kuzimamisha serikali yake mwenyewe? Twapaswa kutaka kujifunza yote tuwezayo juu ya ufalme wa Mungu, na namna tunavyoweza kuunga mkono, kwa ajili ya faida yetu ya milele. Kwa sababu hiyo twakualika ufikirie makala zinazofuata.

[Maelezo ya Chini]

a Kitabu The Dictionary of the Apostolic Church, kama kilivyoandikwa na James Hastings, Kit. cha I, Uku. 658, mwaka 1916.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki