-
Kwa Nini Watu Wanashindwa Kumpenda Mungu?Mnara wa Mlinzi—2013 | Novemba 1
-
-
HABARI KUU | UWONGO UNAOFANYA WATU WASIMPENDE MUNGU
Kwa Nini Watu Wanashindwa Kumpenda Mungu?
“‘Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.’ Hii ndiyo amri iliyo kuu na ya kwanza.”—Yesu Kristo, 33 W.K.a
Baadhi ya watu huhisi ni vigumu kumpenda Mungu. Wao hufikiri Mungu haeleweki, hajali, au hata ni mkatili. Fikiria maneno yafuatayo:
“Nilisali kwa Mungu ili anisaidie lakini wakati huo huo nilihisi yuko mbali sana na haiwezekani kumkaribia. Nilifikiri kwamba Mungu hana utu wala hisia.”—Marco, Italia.
“Ingawa nilitamani sana kumtumikia Mungu, nilihisi yuko mbali sana. Nilifikiri kwamba yeye ni Mungu mkatili ambaye hupenda kutuadhibu tu. Sikuamini kwamba ana hisia nyororo.”—Rosa, Guatemala.
“Nilipokuwa mtoto, niliamini kwamba Mungu hutafuta makosa yetu na yuko tayari kutuadhibu tunapomkosea. Baadaye, nilihisi Mungu hajali. Nilimwona Mungu kama waziri mkuu anayeongoza mambo ya watu lakini hapendezwi nao.”—Raymonde, Kanada.
Wewe una maoni gani? Je, inawezekana kumpenda Mungu? Wakristo wamejiuliza swali hilo kwa karne nyingi. Isitoshe, katika Enzi za Kati, Wakristo wengi hawakusali kwa Mungu Mweza-Yote. Kwa nini? Watu wengi walimwogopa Mungu kupita kiasi. Mwanahistoria Will Durant anafafanua hivi hali hiyo: “Mtenda dhambi anawezaje kusali kwa Mungu mkatili na asiyejali?”
Ni nini kilichofanya watu waanze kumwona Mungu kuwa “mkatili na asiyejali”? Biblia inafundisha nini hasa? Je, kujifunza ukweli kumhusu Mungu kunaweza kukufanya umpende?
-
-
Uwongo Unaomfanya Mungu Asiwe na JinaMnara wa Mlinzi—2013 | Novemba 1
-
-
HABARI KUU | UWONGO UNAOFANYA WATU WASIMPENDE MUNGU
Uwongo Unaomfanya Mungu Asiwe na Jina
MAONI YA WATU WENGI
“Hatujafikia muafaka ikiwa Mungu ana jina, na ikiwa analo, hatulijui.”—Profesa David Cunningham, Theological Studies.
UKWELI WA BIBLIA
Mungu alisema: “Mimi ni Yehova. Hilo ni jina langu.” (Isaya 42:8) Yehova ni jina la Kiebrania linalomaanisha “Yeye Husababisha Kuwa.”—Mwanzo 2:4.
Yehova anataka tutumie jina lake. “Liitieni jina lake,” Biblia inasema. “Tangazeni matendo yake kati ya vikundi vya watu. Semeni kwamba jina lake limeinuliwa juu.”—Isaya 12:4.
Yesu alilitumia jina la Mungu. Yesu alisali hivi kwa Yehova: “Nimewajulisha [wanafunzi wa Yesu] jina lako nami nitalijulisha.” Kwa nini Yesu aliwajulisha wanafunzi wake jina la Mungu? Aliendelea kusema hivi: “Ili upendo ulionipenda nao upate kuwa ndani yao nami katika muungano pamoja nao.”—Yohana 17:26.
KWA NINI NI MUHIMU?
Mwanatheolojia Walter Lowrie aliandika hivi: “Mtu asiyelijua jina la Mungu hawezi kumwona Mungu kuwa mtu halisi na pia hawezi kumpenda ikiwa anafikiri Mungu ni nguvu isiyo na utu.”
Mwanamume mmoja anayeitwa Victor alienda kanisani kila juma, lakini hakuhisi kwamba anamjua Mungu vizuri. Anasema: “Kisha nilijifunza kwamba Mungu anaitwa Yehova, na hivyo nikamjua rasmi. Nilihisi kama hatimaye nimekutana na Mtu niliyemsikia kwa muda mrefu. Nilianza kumuona kama Mtu halisi na kuanzisha urafiki pamoja naye.”
Yehova huwakaribia wale wanaotumia jina lake. Mungu anawaahidi “wale wanaolifikiria jina lake” hivi: “Nitawaonyesha huruma, kama vile mwanamume anavyomwonyesha huruma mwana wake ambaye anamtumikia.” (Malaki 3:16, 17) Pia, Mungu huwathawabisha wale wanaoliitia jina lake. Biblia inasema hivi: “Kila mtu anayeliitia jina la Yehova ataokolewa.”—Waroma 10:13.
-
-
Uwongo Unaomfanya Mungu AsielewekeMnara wa Mlinzi—2013 | Novemba 1
-
-
HABARI KUU | UWONGO UNAOFANYA WATU WASIMPENDE MUNGU
Uwongo Unaomfanya Mungu Asieleweke
MAONI YA WATU WENGI
“Wakatoliki, Kanisa Othodoksi la Mashariki, na Waprotestanti huamini Utatu, yaani Mungu mmoja katika nafsi tatu: Mungu Baba, Mungu Mwana, na Mungu Roho Mtakatifu. Kulingana na fundisho la Ukristo, si kwamba hao ni miungu watatu badala yake ni nafsi tatu katika mungu mmoja.”—The New Encyclopædia Britannica.
UKWELI WA BIBLIA
Yesu, Mwana wa Mungu, hakuwahi kamwe kusema kwamba yeye na Baba yake wako sawa au kwamba ni mtu yuleyule. Badala yake, alisema hivi: “Ninaenda kwa Baba, kwa sababu Baba ni mkuu kuliko mimi.” (Yohana 14:28) Hata alimwambia hivi mmoja wa wanafunzi wake: “Mimi ninapanda kwenda kwa Baba yangu na Baba yenu na kwa Mungu wangu na Mungu wenu.”—Yohana 20:17.
Roho takatifu si mtu. Wakristo wa karne ya kwanza ‘walijazwa roho takatifu,’ na Yehova alisema hivi: “Nitaimimina sehemu ya roho yangu juu ya kila namna ya mwili.” (Matendo 2:1-4, 17) Roho takatifu si sehemu ya Utatu. Ni nguvu ya utendaji ya Mungu.
KWA NINI NI MUHIMU?
Kulingana na wasomi wa Kikatoliki Karl Rahner na Herbert Vorgrimler, fundisho la Utatu “haliwezi kueleweka hadi mtu apate ufunuo, na hata akiupata hawezi kuuelewa Utatu kikamili.” Je, unaweza kumpenda mtu ambaye huwezi kumjua au kumwelewa? Hiyo ndiyo sababu fundisho la Utatu huzuia mtu kumjua Mungu na kumpenda.
Marco, aliyetajwa katika makala ya kwanza hakuelewa fundisho la Utatu. Alisema,“Nilifikiri kwamba Mungu hakutaka nimjue na hilo lilinifanya nimwone Mungu kuwa asiyejali na asiyeeleweka.” Hata hivyo, “Mungu si Mungu wa machafuko.” (1 Wakorintho 14:33) Mungu anataka tumjue. Yesu alisema hivi: “Sisi tunaabudu tunachokijua.”—Yohana 4:22.
Marco anasema hivi: “Nilipojifunza kwamba Mungu si sehemu ya Utatu, ndipo nilipoweza kuanzisha urafiki na Mungu.” Tukimwona Mungu kuwa halisi badala ya kufikiri Yeye ni fumbo lisiloeleweka, ni rahisi kumpenda. Biblia inasema hivi: “Yeye ambaye hapendi hajamjua Mungu, kwa sababu Mungu ni upendo.”—1 Yohana 4:8.
-
-
Uwongo Unaomfanya Mungu Aonekane Kuwa MkatiliMnara wa Mlinzi—2013 | Novemba 1
-
-
HABARI KUU | UWONGO UNAOFANYA WATU WASIMPENDE MUNGU
Uwongo Unaomfanya Mungu Aonekane Kuwa Mkatili
MAONI YA WATU WENGI
“Punde tu baada ya kifo nafsi za watu wanaokufa wakiwa watenda dhambi zinaenda motoni, ambako zinateseka milele.” (Catechism of the Catholic Church) Baadhi ya viongozi wa kidini wanasema kwamba mtu akifa anatengwa kabisa na Mungu.
UKWELI WA BIBLIA
“Nafsi inayotenda dhambi—hiyo yenyewe itakufa.” (Ezekieli 18:4) Wafu “hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5) Ikiwa nafsi inayokufa haijui lolote inawezaje kuteseka kwenye “moto wa mateso”?
Katika Biblia neno ambalo hutafsiriwa “kuzimu” kihalisi linarejelea kaburi la watu wote. Kwa mfano, Ayubu alipopatwa na ugonjwa mbaya sana, alisali hivi: “Laiti ungenificha kuzimuni.” (Ayubu 14:13, Biblia Habari Njema) Ayubu alitaka kupumzika kaburini na si mahali penye mateso.
KWA NINI NI MUHIMU?
Ikiwa Mungu ni mkatili hatuwezi kumpenda, tutamchukia. “Tangu nikiwa mtoto nilifundishwa kuhusu moto wa mateso,” anasema Rocío, anayeishi Mexico. “Niliogopa sana na kudhani Mungu ni mkatili. Nilifikiri kwamba alikuwa mwenye hasira na asiye na upendo.”
Rocío alibadili maoni yake kumwelekea Mungu aliposoma katika Biblia kuhusu hukumu za Mungu na hali ya wafu. Anasema, “Nilijihisi huru—ni kama nilikuwa nimeondolewa mzigo mkubwa wa kihisia. Nilianza kuamini kwamba Mungu anataka tufanikiwe, anatupenda, na ninaweza kumpenda. Yeye ni kama baba anayewapenda na kuwajali watoto wake.”—Isaya 41:13.
Watu wengi wamejitahidi kumcha Mungu kwa sababu wanaogopa kuteswa motoni, hata hivyo, Mungu hataki umtumikie kwa sababu unamwogopa. Badala yake, Yesu alisema hivi: “Lazima umpende Yehova Mungu wako.” (Marko 12:29, 30) Zaidi ya hayo, tukiwa na uhakika kwamba Mungu anatenda kwa haki sasa, tunaweza kutazamia kwamba atahukumu kwa haki wakati ujao. Kama Elihu, rafiki ya Ayubu, tunaweza kusema: “Hasha, Mungu wa kweli asitende kwa uovu, na Mweza-Yote kutenda isivyo haki!”—Ayubu 34:10.
-
-
Ukweli Unaweza Kukuweka HuruMnara wa Mlinzi—2013 | Novemba 1
-
-
HABARI KUU | UWONGO UNAOFANYA WATU WASIMPENDE MUNGU
Ukweli Unaweza Kukuweka Huru
Siku moja, huko Yerusalemu, Yesu alikuwa akizungumza kuhusu Baba yake, Yehova, na alifichua mafundisho ya uwongo ya viongozi wa kidini wa wakati huo. (Yohana 8:12-30) Maneno ya Yesu yanatufundisha jinsi ya kuchunguza mafundisho yanayofanya watu wasimpende Mungu. Yesu alisema hivi: “Mkikaa katika neno langu, ninyi kwa kweli ni wanafunzi wangu, nanyi mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.”—Yohana 8:31, 32.
Yesu aliposema, “mkikaa katika neno langu,” aliweka kiwango cha kupima mafundisho ya viongozi wa kidini. Unaposikia mafundisho kumhusu Mungu, kwanza jiulize, ‘Je, yanapatana na maneno ya Yesu na Biblia kwa ujumla?’ Fuata mfano wa wale waliomsikia mtume Paulo akizungumza na ambao walikuwa “wakiyachunguza Maandiko kwa uangalifu kila siku ili kuona kama mambo hayo [waliyokuwa wakijifunza] ndivyo yalivyo.”—Matendo 17:11.
Marco, Rosa, na Raymonde, waliotajwa katika makala ya kwanza, walichunguza kwa makini imani yao kwa kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova. Waligundua nini?
Marco: “Mwalimu wetu wa Biblia alitumia Maandiko kujibu maswali yote ambayo mimi na mke wangu tulimwuliza. Upendo wetu kwa Yehova ulianza kukua, na pia uhusiano wangu na mke wangu ukaimarika!”
Rosa: “Mwanzoni nilifikiri kwamba Biblia ilikuwa kitabu chenye mawazo ya wanadamu. Hatua kwa hatua, nilipata majibu ya maswali yangu katika Biblia. Sasa, Yehova ni halisi kwangu na ninaweza kumtumaini.”
Raymonde: “Nilisali kwa Mungu ili anisaidie kumjua. Punde si punde, mimi na mume wangu tulianza kujifunza Biblia. Hatimaye, tulijifunza ukweli kumhusu Yehova! Tulifurahi sana kumjua Mungu.”
Biblia haifunui tu mafundisho ya uwongo kumhusu Mungu, badala yake inaeleza pia kuhusu sifa zake zenye kupendeza. Biblia iliandikwa kwa mwongozo wa roho ya Mungu, na inatusaidia ‘kuyajua mambo ambayo Mungu ametupa sisi kwa fadhili.’ (1 Wakorintho 2:12) Tafadhali chunguza jinsi Biblia inavyojibu maswali muhimu kuhusu Mungu, kusudi lake, na wakati wetu ujao. Soma majibu ya baadhi ya maswali hayo chini ya kichwa “Mafundisho ya Biblia > Majibu ya Maswali ya Biblia” kwenye www.jw.org/sw. Pia, kwenye Tovuti hiyo unaweza kuomba ufundishwe Biblia na Shahidi wa Yehova. Bila shaka, ukifanya hivyo utaona kwamba inawezekana kuwa na uhusiano mzuri na Mungu kuliko ulivyodhani.
-