-
“Tumefikia Kauli Moja”“Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
-
-
SURA YA 14
“Tumefikia Kauli Moja”
Jinsi baraza linaloongoza lilivyofikia uamuzi na jinsi uamuzi huo ulivyoyaunganisha makutaniko
1, 2. (a) Ni maswali gani mazito ambayo baraza linaloongoza la kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza linahitaji kuyashughulikia? (b) Ni nini kilichowasaidia ndugu hao kufanya uamuzi unaofaa?
KIMYA kimetanda! Mitume na wazee waliokusanyika katika chumba kimoja jijini Yerusalemu watazamana, wakijua kwamba suala lililo mbele yao ni zito. Suala la tohara limetokeza maswali kadhaa mazito. Je, Wakristo wako chini ya Sheria ya Musa? Je, kunapaswa kuwa na tofauti yoyote kati ya Wakristo Wayahudi na Wakristo wa Mataifa?
2 Wanaume hao wanaoongoza wamesikia uthibitisho mbalimbali. Wanakumbuka unabii wa Neno la Mungu na mambo yaliyoonwa yenye kusadikisha, yanayoonyesha baraka za Yehova. Kila mmoja ameeleza waziwazi maoni yake na wana habari zote wanazohitaji ili kufanya uamuzi. Roho takatifu ya Yehova iko juu yao. Je, wanaume hao watakubali mwongozo wa roho hiyo?
3. Tunaweza kufaidikaje kwa kuchunguza masimulizi ya Matendo sura ya 15?
3 Ili kukubali mwongozo wa roho takatifu, wanaume hao wanahitaji kuwa na imani ya kweli na ujasiri. Huenda uamuzi wao ukazidisha chuki ya viongozi wa dini ya Kiyahudi. Isitoshe, wangekabili upinzani kutoka kwa watu fulani ndani ya kutaniko ambao waliazimia kuwalazimisha watu wa Mungu waendelee kuishika Sheria ya Musa. Baraza linaloongoza litafanya nini? Acheni tuone. Tunapochanganua habari hii, tutaona jinsi wanaume hao waaminifu walivyoweka mfano mzuri unaoweza kuigwa na Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova leo. Ni mfano ambao sisi pia tunapaswa kuiga tunapohitaji kufanya uamuzi au tunapokabili hali fulani ngumu katika maisha yetu ya Kikristo.
“Maneno ya Manabii Yanaunga Mkono Jambo Hilo” (Mdo. 15:13-21)
4, 5. Yakobo alinukuu maneno gani ya manabii?
4 Mwanafunzi Yakobo, ndugu wa kambo wa Yesu, akaanza kuzungumza.a Inaonekana alikuwa mwenyekiti katika mkutano huo. Huenda maneno yake yalikuwa muhtasari wa mambo waliyokubaliana wakiwa baraza. Yakobo akawaambia hivi wanaume waliokusanyika: “Simioni amesimulia kikamili jinsi Mungu kwa mara ya kwanza alivyoelekeza uangalifu wake kwa mataifa ili achukue kutoka kwao watu kwa ajili ya jina lake. Na maneno ya Manabii yanaunga mkono jambo hilo.”—Mdo. 15:14, 15.
5 Huenda baada ya kusikiliza hotuba ya Simioni, au Simoni Petro, na uthibitisho uliotolewa na Barnaba na Paulo, Yakobo alikumbuka maandiko kadhaa yaliyotaja jambo hilo muhimu lililozungumziwa. (Yoh. 14:26) Baada ya kusema “maneno ya Manabii yanaunga mkono jambo hilo,” Yakobo akanukuu maneno ya Amosi 9:11, 12. Kitabu hicho kiliorodheshwa kati ya Maandiko ya Kiebrania yanayoitwa “Manabii.” (Mt. 22:40; Mdo. 15:16-18) Utaona kwamba maneno yaliyonukuliwa na Yakobo yanatofautiana kidogo na yale yaliyo katika kitabu cha Amosi leo. Huenda Yakobo alinukuu Septuajinti, tafsiri ya Kigiriki ya Maandiko ya Kiebrania.
6. Maandiko yaliwasaidiaje akina ndugu kujua mapenzi ya Mungu?
6 Kupitia nabii Amosi, Yehova alitabiri kwamba angesimamisha “kibanda cha Daudi,” yaani, ukoo wa kifalme ambao hatimaye ungetokeza Ufalme wa Kimasihi. (Eze. 21:26, 27) Je, Yehova angeshughulika tena kwa njia ya pekee na Wayahudi wa asili? Hapana. Unabii huo unasema kwamba “watu wa mataifa yote” watakusanywa pamoja wakiwa “watu wanaoitwa kwa jina [la Mungu].” Kumbuka, Petro alitoa ushahidi kwamba Mungu “hakutofautisha hata kidogo kati yetu [Wakristo Wayahudi] na wao [Watu wa Mataifa walioamini], bali aliisafisha mioyo yao kwa imani.” (Mdo. 15:9) Kwa hiyo, mapenzi ya Mungu ni kwamba Wayahudi na Watu wa Mataifa, wawe warithi wa Ufalme. (Rom. 8:17; Efe. 2:17-19) Hakuna unabii wowote ulioongozwa kwa roho unaoonyesha kwamba waamini wasio Wayahudi walipaswa kwanza kutahiriwa au kugeuzwa imani kabla ya kuwa warithi wa Ufalme.
7, 8. (a) Yakobo alipendekeza nini? (b) Yakobo alimaanisha nini aliposema “uamuzi wangu”?
7 Akichochewa na uthibitisho huo wa Maandiko na mambo yenye kusadikisha aliyosikia, Yakobo akapendekeza hivi: “Kwa hiyo uamuzi wangu ni kutowataabisha watu wa mataifa wanaomgeukia Mungu, bali kuwaandikia wajiepushe na vitu vilivyochafuliwa na sanamu, na uasherati, na vitu vilivyonyongwa, na damu. Kwa maana tangu nyakati za kale kuna watu ambao wamekuwa wakihubiri kumhusu Musa katika kila jiji, kwa sababu yeye husomwa kwa sauti kubwa katika masinagogi kila sabato.”—Mdo. 15:19-21.
8 Yakobo aliposema “kwa hiyo uamuzi wangu,” je, alikuwa akitumia mamlaka yake—labda kwa sababu alikuwa mwenyekiti wa mkutano huo—ili kuwalazimisha wale ndugu wengine wakubaliane na jambo analosema? Hapana! Katika Kigiriki, neno linalotafsiriwa “uamuzi wangu,” linaweza pia kumaanisha “nafikiria” au “maoni yangu ni.” Hivyo basi, Yakobo hakuwa akitoa uamuzi kwa niaba ya baraza zima, bali, baada ya kusikia ushahidi uliotolewa na Maandiko yaliyochunguzwa alipendekeza hatua inayoweza kuchukuliwa.
9. Pendekezo la Yakobo lilikuwa na manufaa gani?
9 Je, Yakobo alitoa pendekezo zuri? Bila shaka, kwa sababu baadaye mitume na wazee waliamua kufuata pendekezo hilo. Uamuzi huo ungetimiza nini? Kwa upande mmoja, ‘haungewataabisha’ Wakristo wasio Wayahudi kwa kuwalazimisha kufuata matakwa ya Sheria ya Musa. (Mdo. 15:19) Kwa upande mwingine, uamuzi huo ungeheshimu dhamiri za Wakristo Wayahudi, ambao kwa muda mrefu walisikia “Musa . . . [akisomwa] kwa sauti kubwa katika masinagogi kila sabato.”b (Mdo. 15:21) Kwa kweli pendekezo hilo lingeleta umoja kati ya Wakristo Wayahudi na Wakristo kutoka kwa Watu wa Mataifa. Zaidi ya yote, lingempendeza Yehova Mungu kwa kuwa linapatana na kusudi lake. Hiyo ilikuwa njia nzuri ya kutatua tatizo lililohatarisha umoja na hali njema ya kutaniko zima la watu wa Mungu! Nao ni mfano mzuri kwa kutaniko la Kikristo leo!
Albert Schroeder akitoa hotuba katika kusanyiko la kimataifa la mwaka wa 1998
10. Baraza Linaloongoza leo, linafuata jinsi gani mfano uliowekwa na baraza linaloongoza la karne ya kwanza?
10 Kama tulivyoona katika Sura ya 13, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova leo hufuata mfano uliowekwa katika karne ya kwanza, kwa kumtegemea Yehova, Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, na Yesu Kristo, Kichwa cha kutaniko, ili kupata mwongozo katika mambo yote.c (1 Kor. 11:3) Wanafanyaje hivyo? Albert D. Schroeder, aliyetumikia katika Baraza Linaloongoza tangu mwaka wa 1974 hadi alipofikia mwisho wa maisha yake hapa duniani Machi 2006, alieleza: “Baraza Linaloongoza huanza mkutano wao wa Jumatano kwa sala ili kuomba mwongozo wa roho ya Yehova. Baraza Linaloongoza huhakikisha kwamba kila jambo linalozungumziwa na uamuzi unaofanywa unapatana na Neno la Mungu Biblia.” Naye Milton G. Henschel, aliyekuwa mshiriki wa muda mrefu wa Baraza Linaloongoza ambaye alikufa Machi 2003 na kwenda mbinguni, aliwauliza swali lenye kuchochea fikira wahitimu wa darasa la 101 la Shule ya Gileadi. Aliwauliza, “Je, kuna tengenezo lingine duniani ambalo Baraza lake Linaloongoza hutumia ushauri kutoka katika Neno la Mungu, Biblia, kabla ya kufanya maamuzi muhimu?” Hakuna.
“Kuwatuma Wanaume Waliochaguliwa” (Mdo. 15:22-29)
11. Uamuzi wa baraza linaloongoza ulifikaje makutanikoni?
11 Baraza linaloongoza huko Yerusalemu, lilifanya uamuzi wa pamoja kuhusu suala la tohara. Hata hivyo, ili akina ndugu makutanikoni watende kwa umoja, walihitaji kujulishwa uamuzi huo kwa njia iliyo wazi na yenye kutia moyo. Ni njia gani iliyotumiwa? Masimulizi hayo yanaeleza: “Ndipo mitume na wazee, pamoja na kutaniko lote wakaamua kuwatuma wanaume waliochaguliwa kutoka miongoni mwao waende Antiokia pamoja na Paulo na Barnaba; waliwatuma Yuda aliyeitwa Barsaba, na Sila, wanaume waliokuwa wakiongoza kati ya akina ndugu.” Pia, wanaume waliotumwa walipewa barua ambayo ingesomwa katika makutaniko yote ya Antiokia, Siria, na Kilikia.—Mdo. 15:22-26.
12, 13. Ni mambo gani mazuri yaliyotimizwa baada ya (a) Yuda na Sila kutumwa? (b) baraza linaloongoza kutuma barua?
12 Wakiwa “wanaume waliokuwa wakiongoza kati ya akina ndugu,” Yuda na Sila, walistahili kuliwakilisha baraza linaloongoza. Wanaume wanne wangethibitisha kwamba habari waliyokuwa nayo haikuwa tu jibu la swali lililoulizwa bali ni maagizo ya baraza linaloongoza. Kuwepo kwa ‘wanaume hao waliochaguliwa’ kungesaidia kuleta umoja kati ya Wakristo Wayahudi waliokuwa Yerusalemu na Wakristo kutoka kwa Watu wa Mataifa waliokuwa katika maeneo mengine. Huo ulikuwa mpango mzuri na wenye upendo. Bila shaka, ulichangia umoja na amani kati ya watu wa Mungu.
13 Barua hizo zilikuwa na maagizo yaliyokuwa wazi kwa ajili ya Wakristo kutoka kwa Watu wa Mataifa kuhusu suala la tohara na mambo waliyopaswa kufanya ili kupata baraka na kibali cha Yehova. Sehemu muhimu ya barua hiyo ilisema: “Roho takatifu na sisi wenyewe tumeona ni vizuri tusiwaongezee ninyi mzigo zaidi ila mambo haya ya lazima: kuendelea kujiepusha na vitu vilivyotolewa dhabihu kwa sanamu, na damu, na vitu vilivyonyongwa, na uasherati. Mkijiepusha kwa uangalifu na mambo haya, mtafanikiwa. Afya njema kwenu!”—Mdo. 15:28, 29.
14. Inawezekanaje kwa watu wa Yehova kufanya kazi kwa umoja katika ulimwengu huu uliogawanyika?
14 Leo, Mashahidi wa Yehova zaidi ya 8,000,000, katika makutaniko zaidi ya 100,000 ulimwenguni pote, wanaamini na kutenda kwa umoja. Kwa kuwa ulimwengu wa leo umejaa misukosuko na migawanyiko, inawezekanaje kuwa na umoja huo? Kwanza kabisa, umoja huo unatokana na mwongozo ulio wazi ambao Yesu Kristo, Kichwa cha kutaniko, anatoa kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” yaani, Baraza Linaloongoza. (Mt. 24:45-47) Umoja huo pia unawezekana kwa sababu ndugu ulimwenguni pote hufuata kwa hiari mwongozo wa Baraza Linaloongoza.
“Wakashangilia kwa Sababu ya Kutiwa Moyo” (Mdo. 15:30-35)
15, 16. Suala la tohara lilitatuliwaje, na kwa nini uamuzi uliofikiwa ulikuwa na matokeo mazuri?
15 Kitabu cha Matendo kinaendelea kusema kwamba ndugu hao waliotumwa kutoka Yerusalemu walipofika Antiokia, “wakakusanya kundi lote pamoja na kuwapa barua hiyo.” Akina ndugu waliitikiaje mwongozo huo wa baraza linaloongoza? “Baada ya kuisoma[barua hiyo], wakashangilia kwa sababu ya kutiwa moyo.” (Mdo. 15:30, 31) Isitoshe, Yuda na Sila “wakawatia moyo akina ndugu kwa hotuba nyingi na kuwaimarisha.” Wanaume hao wawili walikuwa “manabii,” kama vile Barnaba, Paulo na wengine walioitwa manabii—walipewa jina hilo kwa sababu walikuwa wakitangaza au kujulisha mapenzi ya Mungu.—Mdo. 13:1; 15:32; Kut. 7:1, 2.
16 Ilionekana wazi kwamba Yehova alibariki uamuzi wa baraza linaloongoza na hivyo suala hilo likatatuliwa vizuri. Kwa nini matokeo yalikuwa mazuri? Kwa sababu ya mwongozo ulio wazi na unaotegemea Neno la Mungu na roho takatifu uliotolewa na baraza linaloongoza kwa wakati unaofaa. Sababu nyingine ni kwamba makutaniko yalijulishwa moja kwa moja na kwa upendo kuhusu uamuzi huo.
17. Waangalizi wa mzunguko leo hufuata mfano gani?
17 Leo, Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova hufuata mfano huo kwa kuwapa ndugu ulimwenguni pote mwongozo kwa wakati unaofaa. Uamuzi fulani unapofanywa, makutaniko hujulishwa moja kwa moja na kwa njia inayoeleweka wazi. Njia moja ni kupitia ziara za waangalizi wa mzunguko. Ndugu hao wanaojitolea kwa moyo wote, hutembelea makutaniko wakiyatia moyo na kutoa mwelekezo. Kama walivyofanya Paulo na Barnaba, wao pia hutumia wakati mwingi “wakifundisha na kutangaza habari njema ya neno la Yehova, wakiwa pamoja na wengine wengi.” (Mdo. 15:35) Kama Yuda na Sila, wanawaimarisha akina ndugu na kuwatia ‘moyo kwa hotuba nyingi.’
18. Watu wa Yehova wanawezaje kuendelea kupokea baraka zake?
18 Kwa upande mwingine, ni nini kitakachoyawezesha makutaniko ulimwenguni pote kuendelea kuwa na amani na umoja katika ulimwengu uliogawanyika leo? Mwanafunzi Yakobo aliandika hivi baadaye: “Hekima inayotoka juu kwanza kabisa ni safi, kisha yenye kufanya amani, yenye usawaziko, tayari kutii . . . Zaidi ya hayo, tunda la uadilifu hupandwa katika hali zenye amani kwa wale wanaofanya amani.” (Yak. 3:17, 18) Hatujui ikiwa kilichomchochea kuandika hivyo ni ule mkutano wa Yerusalemu au la. Hata hivyo, matukio yanayozungumziwa katika Matendo sura ya 15 yanaonyesha wazi kwamba Yehova hubariki roho ya umoja na ushirikiano.
19, 20. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba kulikuwa na amani na umoja katika kutaniko la Antiokia? (b) Paulo na Barnaba wangeweza kufanya nini sasa?
19 Ni wazi kwamba kulikuwa na amani na umoja katika kutaniko la Antiokia. Badala ya kubishana na ndugu waliotumwa kutoka Yerusalemu, akina ndugu wa Antiokia walithamini sana kutembelewa na Yuda na Sila. Ndugu wa Antiokia hawakuwaruhusu waondoke. Hata hivyo, “baada ya kukaa huko kwa muda fulani, ndugu hao wakawaacha warudi kwa amani kwa wale waliokuwa wamewatuma,” yaani, warudi Yerusalemu.d (Mdo. 15:33) Bila shaka, ndugu waliokuwa Yerusalemu walifurahi pia walipowasikia Yuda na Sila wakisimulia matokeo ya safari yao. Fadhili zisizostahiliwa za Yehova ziliwawezesha kuutimiza mgawo wao!
20 Paulo na Barnaba, ambao walibaki Antiokia, wangeweza sasa kukazia fikira kazi ya kuhubiri kama vile waangalizi wa mzunguko wanavyofanya wanapotembelea makutaniko. (Mdo. 13:2, 3) Ndugu hao ni baraka kubwa sana! Hata hivyo, Yehova aliwatumia waeneza-injili hao wawili wenye bidii kutimiza mambo gani zaidi? Tutaona katika sura inayofuata.
Leo, Wakristo hufaidika kutokana na maagizo kutoka kwa Baraza Linaloongoza na wawakilishi wake
a Ona sanduku lenye kichwa “Yakobo—‘Ndugu ya Bwana.’”
b Yakobo alirejelea kwa busara maandishi ya Musa ambayo zaidi ya kuwa na Sheria, yalitia ndani masimulizi ya jinsi Mungu alivyoshughulika na watu wake na maoni yake kabla ya Sheria kutolewa. Kwa mfano, maoni ya Mungu kuhusu damu, uzinzi, na ibada ya sanamu yanaonekana wazi katika kitabu cha Mwanzo. (Mwa. 9:3, 4; 20:2-9; 35:2, 4) Hivyo, Yehova alionyesha kanuni zinazowahusu wanadamu wote iwe ni Wayahudi au Watu wa Mataifa.
c Ona sanduku lenye kichwa “Jinsi Baraza Linaloongoza Lilivyopangwa Leo.”
d Katika mstari wa 34, tafsiri fulani za Biblia husema kwamba Sila aliamua kubaki Antiokia. (Union Version) Hata hivyo, inaonekana kwamba maneno hayo yaliongezwa baadaye.
-
-
“Baada ya . . . Kutoelewana”“Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
-
-
SURA YA 13
“Baada ya . . . Kutoelewana”
Suala la tohara lapelekwa kwenye baraza linaloongoza
1-3. (a) Ni suala gani lililotishia kuvunja kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza? (b) Tunaweza kunufaikaje na masimulizi ya kitabu cha Matendo?
PAULO na Barnaba wamerudi Antiokia ya Siria wakiwa na shangwe baada ya safari yao ya kwanza ya umishonari. Wana furaha nyingi kwa sababu Yehova “amewafungulia mataifa mlango wa kuingia kwenye imani.” (Mdo. 14:26, 27) Kwa kweli, habari njema zinahubiriwa kotekote jijini Antiokia na “idadi kubwa” ya Watu wa Mataifa wanajiunga na kutaniko.—Mdo. 11:20-26.
2 Baada ya muda mfupi, habari hizo zenye kusisimua kuhusu ongezeko zinafika Yudea. Lakini si watu wote waliofurahishwa na habari hizo; ongezeko hili linasababisha mabishano kuhusu suala la tohara. Waamini Wayahudi wanapaswa kuwaonaje waamini wasio Wayahudi, na wale ambao si Wayahudi wanapaswa kuionaje Sheria ya Musa? Suala hilo linatokeza mgawanyiko mkubwa unaotishia kulivunja kutaniko la Kikristo. Suala hilo lingetatuliwaje?
3 Tunapoendelea kuchunguza kitabu cha Matendo, tutajifunza mambo mengi muhimu. Mambo hayo yatatusaidia kutenda kwa busara suala linaloleta mgawanyiko litakapotokea.
“Msipotahiriwa” (Mdo. 15:1)
4. Watu fulani walieneza maoni gani yasiyofaa, na ni swali gani linalotokea?
4 Luka anaandika: “Watu fulani wakashuka [Antiokia] kutoka Yudea na kuanza kuwafundisha akina ndugu: ‘Msipotahiriwa kulingana na desturi ya Musa, hamwezi kuokolewa.’” (Mdo. 15:1) Huenda hao “watu fulani” wanaotajwa walikuwa Mafarisayo kabla ya kuwa Wakristo. Na inaonekana kwamba waliathiriwa na mtazamo wa Mafarisayo wa kushikilia sheria kupita kiasi. Pia, huenda walidai wametumwa na mitume na wanaume wazee wa Yerusalemu. (Mdo. 15:23, 24) Hivyo, kwa nini Wakristo Wayahudi bado walifikiri kwamba tohara ilikuwa muhimu, hata baada ya Mungu kuweka wazi kupitia mtume Petro kwamba amekubali watu wasio Wayahudi waingie katika kutaniko la Kikristo?a—Mdo. 10:24-29, 44-48.
5, 6. (a) Kwa nini baadhi ya Wakristo Wayahudi waliamini kwamba tohara ni muhimu? (b) Eleza ni kwa nini agano la tohara halikuwa sehemu ya agano la Kiabrahamu. (Ona maelezo ya chini.)
5 Huenda kulikuwa na sababu kadhaa. Kwanza, Yehova ndiye aliyeagiza wanaume watahiriwe, na tohara ilikuwa ishara ya uhusiano wa pekee pamoja naye. Tohara ilianza kabla ya agano la Sheria na baadaye ikaja kuwa sehemu ya agano hilo. Abrahamu na nyumba yake walikuwa watu wa kwanza kutahiriwa.b (Law. 12:2, 3) Kulingana na Sheria ya Musa, hata wageni walipaswa kutahiriwa kabla ya kupata mapendeleo fulani, kama vile kula mlo wa Pasaka. (Kut. 12:43, 44, 48, 49) Hivyo, Wayahudi walimwona mtu ambaye hajatahiriwa kuwa si safi na mwenye kuchukiza.—Isa. 52:1.
6 Waabudu Wayahudi walihitaji imani na unyenyekevu ili kukubali fundisho hilo jipya. Agano jipya lilichukua nafasi ya agano la Sheria. Hivyo, mtu hakuwa sehemu ya watu wa Mungu kwa kuwa tu alizaliwa akiwa Myahudi. Na Wakristo Wayahudi walioishi na Wayahudi wengine—kama wale walioishi Yudea—walihitaji ujasiri ili kumkiri Kristo na kuwakubali Watu wa Mataifa ambao hawakutahiriwa wawe waabudu wenzao.—Yer. 31:31-33; Luka 22:20.
7. “Watu . . . kutoka Yudea” hawakuelewa kweli gani?
7 Bila shaka, viwango vya Mungu havikubadilika. Agano jipya lina kanuni fulani za msingi zilizokuwa katika Sheria ya Musa. (Mt. 22:36-40) Kwa mfano, Paulo aliandika hivi baadaye kuhusu tohara: “Yeye ni Myahudi aliye hivyo kwa ndani, na kutahiriwa kwake ni kule kwa moyo kupitia roho, wala si kupitia sheria zilizoandikwa.” (Rom. 2:29; Kum. 10:16) “Watu . . . kutoka Yudea” waliotajwa mwanzoni, hawakuelewa kweli hizo bali walifikiri kwamba Mungu hakuondoa kamwe sheria ya tohara. Je, wangebadili maoni yao?
“Kutoelewana na Kubishana” (Mdo. 15:2)
8. Kwa nini suala la tohara lilipelekwa kwenye baraza linaloongoza lililokuwa jijini Yerusalemu?
8 Luka anasema hivi: “Baada ya Paulo na Barnaba kutoelewana na kubishana sana na watu hao [“kutoka Yudea”], wakapanga Paulo na Barnaba na wengine wapande kwenda kwa mitume na wazee huko Yerusalemu kuuliza kuhusu jambo hilo.”c (Mdo. 15:2) Maneno “kutoelewana na kubishana” yanaonyesha kwamba kila upande ulishikilia maoni yake, na kutaniko la Antiokia halingeweza kushughulikia jambo hilo. Ili kudumisha amani na umoja, kutaniko lilitenda kwa hekima lilipoamua kuwauliza “mitume na wazee huko Yerusalemu,” waliokuwa baraza linaloongoza. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa wazee hao wa Antiokia?
Wengine wakasisitiza: “Ni lazima . . . kuwaamuru [Watu wa Mataifa] washike Sheria ya Musa”
9, 10. Ndugu wa Antiokia na pia Paulo na Barnaba walituwekea mfano gani?
9 Jambo moja muhimu tunalojifunza ni kwamba tunapaswa kuliamini tengenezo la Mungu. Fikiria hili: Ndugu wa Antiokia walijua kwamba washiriki wote wa baraza linaloongoza ni Wakristo wenye asili ya Kiyahudi. Hata hivyo, waliamini kwamba baraza hilo lingetatua suala la kutahiriwa kupatana na Maandiko. Kwa nini? Kutaniko lilikuwa na uhakika kwamba Yehova ataongoza mambo kupitia roho yake takatifu na Kichwa cha kutaniko la Kikristo, Yesu Kristo. (Mt. 28:18, 20; Efe. 1:22, 23) Masuala mazito yanapotokea, na tuige mfano mzuri wa Wakristo wa Antiokia kwa kuliamini tengenezo la Mungu na Baraza Linaloongoza.
10 Pia, kisa hicho kinatukumbusha faida ya unyenyekevu na uvumilivu. Paulo na Barnaba waliwekwa rasmi na roho takatifu ili wawahubirie watu wa mataifa, lakini, waliamua kutotumia mamlaka hiyo kutatua suala la tohara lilipotokea Antiokia. (Mdo. 13:2, 3) Isitoshe, Paulo aliandika hivi baadaye: “Nilienda [Yerusalemu] kutokana na ufunuo”—akionyesha alipata mwongozo kutoka kwa Mungu. (Gal. 2:2) Leo, wazee hujitahidi kuwa wanyenyekevu na wavumilivu hasa mambo yanayoweza kusababisha mgawanyiko yanapotokea. Badala ya kubishana, wao humtegemea Yehova kwa kuchunguza Maandiko na pia maagizo na miongozo inayotolewa na mtumwa mwaminifu.—Flp. 2:2, 3.
11, 12. Kwa nini tunahitaji kumsubiri Yehova?
11 Nyakati nyingine, huenda tukahitaji kumsubiri Yehova atusaidie kuelewa vizuri jambo fulani. Kumbuka kwamba katika siku za Paulo, akina ndugu walihitaji kungoja kwa miaka 13 hivi, tangu mwaka wa 36 W.K. Kornelio alipotiwa mafuta mpaka mwaka wa 49 W.K., Yehova alipotatua suala la tohara. Kwa nini muda mrefu ulipita? Huenda Mungu alitaka muda wa kutosha upite ili kuwasaidia Wayahudi wanyoofu wabadili maoni yao kuhusu badiliko hilo kubwa. Kwa kweli, kukomeshwa kwa agano la tohara lililodumu kwa miaka 1,900, ambalo Yehova alifanya na babu yao mpendwa Abrahamu, kulikuwa badiliko kubwa!—Yoh. 16:12.
12 Ni pendeleo kubwa sana kufundishwa na kufinyangwa na Baba yetu wa mbinguni mwenye subira na fadhili! Sikuzote mambo anayotufundisha yanatunufaisha. (Isa. 48:17, 18; 64:8) Kwa hiyo, tusishikilie kamwe maoni yetu kwa kiburi au kupinga mabadiliko yanayofanywa na tengenezo au mabadiliko ya uelewaji wetu wa maandiko fulani. (Mhu. 7:8) Ukigundua kwamba una mtazamo kama huo, hata kwa kiasi kidogo, sali na utafakari kanuni zinazopatikana katika Matendo sura ya 15.d
13. Tunawezaje kuiga subira ya Yehova katika huduma yetu?
13 Subira inahitajika hasa tunapojifunza Biblia na watu ambao huona ni vigumu kuacha desturi au mafundisho yasiyopatana na maandiko. Katika hali kama hizo, tunahitaji kusubiri ili roho takatifu ya Mungu ichochee moyo wa mwanafunzi kufanya mabadiliko. (1 Kor. 3:6, 7) Pia, ni vizuri kusali kwa ajili yao. Mwishowe, Yehova atatusaidia tupate njia bora ya kuwasaidia.—1 Yoh. 5:14.
“Wakisimulia Kirefu” Mambo Yaliyoonwa Yenye Kutia Moyo (Mdo. 15:3-5)
14, 15. Kutaniko la Antiokia liliwaonyeshaje heshima Paulo, Barnaba, na wale ndugu wengine waliosafiri pamoja nao, na ndugu hao waliwatia moyo waabudu wenzao jinsi gani?
14 Masimulizi ya Luka yanaendelea: “Baada ya kusindikizwa umbali fulani na kutaniko, watu hao wakaenda wakapitia Foinike na Samaria, wakisimulia kirefu kuhusu kugeuka kwa watu wa mataifa, nao wakafanya akina ndugu washangilie sana.” (Mdo. 15:3) Kutaniko liliwasindikiza Paulo, Barnaba na ndugu wengine waliosafiri pamoja nao. Kwa kufanya hivyo, walionyesha ndugu hao heshima na upendo wa Kikristo na waliwatakia baraka za Mungu. Ndugu wa Antiokia wanatuwekea mfano mzuri sana! Je, unawaonyesha heshima ndugu na dada zako Wakristo, “hasa wale [wazee] wanaofanya kazi kwa bidii katika kusema na kufundisha”?—1 Tim. 5:17.
15 Wakiwa njiani, wasafiri hao waliwatia moyo Wakristo wenzao waliokuwa Foinike na Samaria, “wakisimulia kirefu” mambo yaliyoonwa kuhusu matokeo mazuri waliyopata kwa kuwahubiria Watu wa Mataifa. Huenda baadhi ya watu waliowasikiliza walikuwa Wakristo Wayahudi waliokimbilia maeneo hayo baada ya Stefano kuuawa. Ndivyo ilivyo leo. Ripoti kuhusu jinsi ambavyo Yehova amebariki kazi ya kufanya wanafunzi huwatia moyo sana ndugu zetu, hasa wale walio katika hali ngumu. Je, wewe hufaidika kikamili kutokana na ripoti hizo kwa kuhudhuria mikutano ya Kikristo, makusanyiko, na kwa kusoma mambo yaliyoonwa au masimulizi ya maisha yaliyo kwenye machapisho yetu yaliyochapishwa au kwenye tovuti yetu ya jw.org?
16. Ni nini kinachoonyesha kwamba suala la tohara lilikuwa tatizo kubwa?
16 Baada ya kusafiri kuelekea kusini, kilomita 550 hivi, Paulo na wenzake walifika mwisho wa safari yao. Luka anaandika: “Walipofika Yerusalemu, walikaribishwa kwa fadhili na kutaniko na mitume na wazee, nao wakawasimulia mambo mengi ambayo Mungu alifanya kupitia kwao.” (Mdo. 15:4) Hata hivyo, “baadhi ya wale wa madhehebu ya Mafarisayo ambao sasa walikuwa waamini wakasimama kutoka kwenye viti vyao na kusema: ‘Ni lazima watahiriwe na kuwaamuru washike Sheria ya Musa.’” (Mdo. 15:5) Ni wazi kwamba suala la kutahiriwa kwa Wakristo wasio Wayahudi lilikuwa tatizo kubwa, na lilipaswa kutatuliwa.
“Mitume na Wazee Wakakusanyika Pamoja” (Mdo. 15:6-12)
17. Ni nani waliofanyiza baraza linaloongoza la Yerusalemu, na huenda ni kwa nini baraza hilo lilitia ndani “wazee”?
17 Methali 13:10 inasema: “Hekima ni ya wale wanaotafuta ushauri.” Wakitenda kulingana na kanuni hiyo, “mitume na wazee wakakusanyika pamoja ili kulichunguza [suala la tohara].” (Mdo. 15:6) “Mitume na wazee” waliwakilisha kutaniko lote la Kikristo, kama Baraza Linaloongoza linavyofanya leo. Kwa nini “wazee” walitumikia pamoja na mitume? Kumbuka kwamba mtume Yakobo alikuwa ameuawa, na kwa kipindi fulani mtume Petro alikuwa gerezani. Je, mitume wengine pia wangepatwa na mambo kama hayo? Wazee hao wenye sifa za kustahili ambao walitiwa mafuta wangesaidia kusimamia kazi vizuri hata ikiwa hali zingebadilika.
18, 19. Ni maneno gani yenye kusadikisha ambayo Petro alisema, na waliomsikiliza walifikia mkataa gani?
18 Luka anaendelea: “Baada ya kujadiliana sana, Petro akasimama na kuwaambia: ‘Wanaume, akina ndugu, mnajua vema kwamba tangu siku za zamani Mungu alinichagua kati yenu ili kupitia kinywa changu watu wa mataifa wasikie neno la habari njema na kuamini. Pia, Mungu anayeujua moyo, alitoa ushahidi kwa kuwapa roho takatifu, kama vile alivyotupatia sisi. Naye hakutofautisha hata kidogo kati yetu na wao, bali aliisafisha mioyo yao kwa imani.’” (Mdo. 15:7-9) Kulingana na kitabu kimoja cha marejeo, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kujadiliana” katika mstari wa 7 linaweza kumaanisha pia “kutafuta,” au “mahojiano.” Inaonekana kwamba maoni ya ndugu hao yalitofautiana, na waliyazungumzia waziwazi.
19 Maneno yenye kusadikisha ya Petro yaliwakumbusha wote kwamba yeye mwenyewe alikuwepo wakati watu wa kwanza wa Mataifa wasiotahiriwa—Kornelio na nyumba yake—walipotiwa mafuta kwa roho takatifu mwaka wa 36 W.K. Kwa hiyo, ikiwa Yehova aliacha kutofautisha Myahudi na asiye Myahudi, wanadamu wana mamlaka gani ya kutenda kinyume? Isitoshe, mtu hutangazwa kuwa mwadilifu kwa sababu ya imani yake kwa Kristo bali si kupitia Sheria ya Musa.—Gal. 2:16.
20. Watu waliopendekeza tohara walikuwa ‘wakimjaribu Mungu’ jinsi gani?
20 Akitoa uthibitisho usioweza kupingwa wa neno la Mungu na roho takatifu, Petro akamalizia kwa kusema: “Basi kwa nini sasa mnamjaribu Mungu kwa kuweka kwenye shingo za wanafunzi nira ambayo mababu zetu na sisi wenyewe tulishindwa kuibeba? Badala yake, sisi tunaamini kwamba tunaokolewa kupitia fadhili zisizostahiliwa za Bwana Yesu katika njia ileile wanayookolewa.” (Mdo. 15:10, 11) Kwa kweli wale waliopendekeza tohara, walikuwa ‘wakimjaribu Mungu.’ Walitaka kuwabebesha Watu wa Mataifa mfumo wa sheria ambao Wayahudi wenyewe hawakuwa wakifuata kikamili, na kwa sababu hiyo walistahili kufa. (Gal. 3:10) Badala yake, Wayahudi waliomsikiliza Petro walipaswa kuthamini fadhili zisizostahiliwa za Mungu kupitia Yesu.
21. Barnaba na Paulo walisimulia mambo gani yaliyowasaidia akina ndugu kufanya uamuzi mzuri?
21 Bila shaka, maneno ya Petro yalikuwa yenye kusadikisha sana, hivi kwamba “kikundi chote kikanyamaza.” Kisha, Barnaba na Paulo wakasimulia “ishara nyingi na mambo ya ajabu ambayo Mungu alifanya kupitia kwao miongoni mwa mataifa.” (Mdo. 15:12) Sasa, mitume na wanaume wazee wangeweza kuchanganua uthibitisho wote uliotolewa na kufanya uamuzi ambao ungeonyesha waziwazi mapenzi ya Mungu kuhusu suala hilo la tohara.
22-24. (a) Baraza Linaloongoza leo, linafuata jinsi gani mfano uliowekwa na baraza linaloongoza la karne ya kwanza? (b) Wazee wote wanaweza kuonyeshaje kwamba wanashughulikia mambo kwa njia ya Yehova?
22 Leo, washiriki wa Baraza Linaloongoza wanapokutana, wanachunguza Neno la Mungu ili kupata mwongozo, na kusali kwa bidii ili wapate roho takatifu. (Zab. 119:105; Mt. 7:7-11) Ndiyo sababu kila mshiriki wa Baraza Linaloongoza hupokea ajenda mapema ili aweze kutafakari na kusali kuhusu mambo yatakayozungumziwa. (Met. 15:28) Wanapokutana, ndugu hao watiwa-mafuta huzungumza kwa uhuru na kwa heshima. Biblia hutumiwa mara nyingi katika mazungumzo yao.
23 Wazee wa kutaniko wanapaswa kuiga mfano huo. Ikiwa kuna jambo zito ambalo wameshindwa kulitatua katika mkutano wa wazee, baraza la wazee linaweza kuwasiliana na ofisi ya tawi au mwakilishi aliyewekwa rasmi na ofisi ya tawi, kama vile, mwangalizi wa mzunguko. Ikihitajika, ofisi ya tawi italiandikia Baraza Linaloongoza.
24 Yehova huwabariki wanyenyekevu, washikamanifu na wenye subira na wale wanaofuata kwa hiari miongozo inayotolewa kwenye tengenezo na kutanikoni. Kama tutakavyoona katika sura inayofuata, Mungu huwapa wote wanaofanya hivyo amani ya kweli, ufanisi wa kiroho, na umoja wa Kikristo.
a Ona sanduku “Mafundisho ya Wayudaiza.”
b Agano la tohara halikuwa sehemu ya agano la Kiabrahamu linalotumika mpaka leo. Agano la Kiabrahamu lilianzishwa mwaka wa 1943 K.W.K., wakati ambapo Abrahamu (aliyekuwa akiitwa Abramu), alivuka Mto Efrati akielekea Kanaani. Alikuwa na umri wa miaka 75. Agano la tohara lilianzishwa baadaye, mwaka wa 1919 K.W.K., Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 99.—Mwa. 12:1-8; 17:1, 9-14; Gal. 3:17.
c Inaonekana kwamba Tito, Mkristo Mgiriki ambaye baadaye alifanya kazi bega kwa bega na Paulo, alikuwa miongoni mwa wale waliotumwa Yerusalemu. (Gal. 2:1; Tito 1:4) Alikuwa Mtu wa Mataifa asiyetahiriwa, lakini alitiwa mafuta kwa roho takatifu na alikuwa ndugu mwenye mfano mzuri.—Gal. 2:3.
d Ona sanduku lenye kichwa ‘Imani ya Mashahidi wa Yehova Inategemea Biblia.’
-