-
Muumba Ajifunua—Kwa Manufaa Yetu!Je, Kuna Muumba Anayekujali?
-
-
Sura Ya Nane
Muumba Ajifunua—Kwa Manufaa Yetu!
KATI ya ngurumo na radi, watu wapatao milioni tatu walisimama mbele ya mlima mrefu katika Peninsula ya Sinai. Mawingu yalifunika Mlima Sinai, ardhi ikatetemeka. Katika hali hizo zenye kukumbukwa, Musa aliongoza Israeli la kale kufanya agano pamoja na Muumba wa mbingu na dunia.—Kutoka, sura ya 19; Isaya 45:18.
Lakini, kwa nini Muumba wa ulimwengu angejifunua kwa njia ya kipekee kwa taifa moja tu, na isitoshe taifa dogo tu? Musa alitufahamisha hivi: ‘Kwa sababu BWANA anawapenda, na kwa sababu alitaka kuutimiza uapo wake aliowaapia baba zenu.’—Kumbukumbu la Torati 7:6-8.
Taarifa kama hiyo yafunua kwamba Biblia inatupa habari nyingi zaidi kuliko tu mambo ya chanzo cha ulimwengu na maisha duniani. Inasema mengi kuhusu shughuli za Muumba pamoja na wanadamu—katika wakati uliopita, wakati wa sasa, na wakati ujao. Biblia ndicho kitabu ambacho kimesomwa zaidi na kuenezwa zaidi ulimwenguni, na basi kila mtu anayethamini elimu apaswa kufahamu yaliyomo ndani yake. Ebu tuone muhtasari wa yale tuwezayo kupata ndani ya Biblia, kwanza tukikazia akili sehemu ambayo huitwa Agano la Kale. Kwa kufanya hivyo, tutapata pia ufahamu wa ndani wa utu wa Muumba wa ulimwengu aliye pia Mtungaji wa Biblia.
Katika Sura ya 6, “Rekodi ya Kale ya Uumbaji—Je, Unaweza Kuitumaini?,” tuliona kwamba ni masimulizi ya Biblia juu ya uumbaji ndiyo pekee yaliyo na mambo yahusuyo wazazi wetu wa kale zaidi—ndiyo asili yetu. Kitabu hiki cha kwanza cha Biblia kina mambo mengi sana. Kama yapi?
Hekaya za Kigiriki na nyinginezo hueleza juu ya wakati ambapo miungu na nusu-miungu ilipokuwa na uhusiano na wanadamu. Pia, wataalamu wa asili ya wanadamu waripoti kwamba duniani kote kuna hekaya kuhusu furiko moja la kale lililowafagia wengi wa wanadamu. Kwa haki huenda ukapuuza hekaya kama hizo. Lakini, je, ulijua kwamba ni kitabu cha Mwanzo peke yake hutufunulia historia ambayo baadaye ilitajwa katika hekaya na ngano kama hizo?—Mwanzo, sura ya 6, 7.a
Katika kitabu cha Mwanzo, utasoma pia juu ya wanaume na wanawake—watu wenye kustahiwa walio kama sisi—ambao walijua kwamba Muumba yuko na ambao walifanya mapenzi yake maishani mwao. Utanufaika kujua mambo juu ya wanaume kama Abrahamu, Isaka, na Yakobo, ambao walikuwa miongoni mwa “baba” ambao Musa alitaja. Muumba alimjua Abrahamu akamwita “rafiki yangu.” (Isaya 41:8; Mwanzo 18:18, 19) Kwa nini? Yehova alikuwa amemtazama Abrahamu akawa na uhakika wa kwamba alikuwa na imani. (Waebrania 11:8-10, 17-19; Yakobo 2:23) Mambo aliyojionea Abrahamu yaonyesha kwamba Mungu aweza kufikika. Yeye ana uwezo mkubwa sana, lakini yeye si kani au kisababishi fulani tu kisicho na utu. Yeye ni mtu halisi ambaye wanadamu kama sisi wanaweza kusitawisha uhusiano wenye staha naye—kwa manufaa yetu ya milele.
Yehova alimwahidi Abrahamu hivi: “Na katika uzao wako [“mbegu yako,” NW] mataifa yote ya dunia watajibarikia.” (Mwanzo 22:18) Hilo laongezea ahadi iliyotolewa wakati wa Adamu kuhusu “mbegu” ijayo. (Mwanzo 3:15) Ndiyo, yale ambayo Yehova alimwambia Abrahamu yalithibitisha tumaini la kwamba mtu fulani—Mbegu—angekuja baadaye na kuwaletea watu wote baraka. Utapata kwamba hicho ndicho kichwa kikuu kinachopatikana kotekote katika Biblia, kikikazia kwamba kitabu hiki si mkusanyo tu wa maandishi tofauti-tofauti ya wanadamu. Na kujua kichwa kikuu cha Biblia kutakusaidia kutambua kwamba Mungu alitumia taifa moja la kale—kwa lengo la kubariki mataifa yote.—Zaburi 147:19, 20.
Jambo la kwamba Yehova alikuwa na lengo hilo katika kushughulika na Israeli laonyesha kwamba ‘yeye si mwenye ubaguzi.’ (Matendo 10:34; Wagalatia 3:14) Isitoshe, hata Mungu alipokuwa akishughulika hasa na wazao wa Abrahamu, watu wa mataifa mengine walikubaliwa kuja na kumtumikia Yehova pia. (1 Wafalme 8:41-43) Na, kama tutakavyoona baadaye, kutobagua kwa Mungu ni kwa namna ya kwamba sisi sote leo—hata tuwe wa kabila gani au taifa gani—tunaweza kumjua na kumpendeza.
Tunaweza kujifunza mengi kutokana na historia ya taifa ambalo Muumba alishughulika nalo kwa karne nyingi. Ebu tugawanye historia hiyo katika sehemu tatu. Tunapozungumzia sehemu hizo, ona jinsi Yehova alivyotenda kwa kupatana na maana ya jina lake, “Yeye Husababisha Iwe,” na jinsi utu wake ulivyodhihirika katika shughuli zake na watu halisi.
Sehemu ya Kwanza—Taifa Lililotawalwa na Muumba
Wazao wa Abrahamu walikuwa watumwa Misri. Hatimaye Mungu alimteua Musa, ambaye aliwaongoza wakapata uhuru mnamo 1513 K.W.K. Israeli lilipopata kuwa taifa, Mungu alikuwa mtawala wake. Lakini mnamo 1117 K.W.K., watu walitaka wawe na mfalme wa kibinadamu.
Ni mambo gani yaliyofanya Musa awe pamoja na Israeli kwenye Mlima Sinai? Kitabu cha Biblia cha Mwanzo chatupa historia hiyo. Mapema, Yakobo (aliyeitwa pia Israeli) alipokuwa anaishi kaskazini-mashariki ya Misri, njaa kuu ilitokea kotekote katika ulimwengu uliojulikana wakati huo. Kwa kuihangaikia familia yake, Yakobo alitafuta chakula huko Misri, ambapo chakula kingi kilihifadhiwa. Akagundua kwamba kumbe yule msimamizi wa chakula alikuwa mwana wake Yosefu, ambaye Yakobo alidhani alikuwa amekufa miaka mingi iliyopita. Yakobo na familia yake wakahamia Misri nao waliombwa wabaki huko. (Mwanzo 45:25–46:5; 47:5-12) Lakini, baada ya kifo cha Yosefu, Farao mpya akawalazimisha wazao wa Yakobo wawe watumwa na ‘kufanya maisha yao kuwa uchungu kwa kazi ngumu; kazi ya chokaa na matofali.’ (Kutoka 1:8-14) Unaweza kusoma masimulizi hayo dhahiri na mengi zaidi katika kitabu cha pili cha Biblia, Kutoka.
Waisraeli walitendwa vibaya kwa miongo mingi, na “kilio chao kikafika juu kwa Mungu.” Lilikuwa jambo la hekima kumgeukia Yehova. Yeye alipendezwa na wazao wa Abrahamu naye aliazimia kutimiza kusudi Lake la kuandaa baraka ya wakati ujao kwa watu wote. Yehova ‘akasikia kuugua kwa Israeli na kuwaangalia,’ jambo linaloonyesha kwamba Muumba anawahurumia watu wanaoonewa na kuteseka. (Kutoka 2:23-25) Alimchagua Musa aongoze Waisraeli kutoka utumwani. Lakini Musa na ndugu yake, Aroni, walipokuja kumwomba Farao wa Misri awaachilie watu hao waliotumikishwa, yeye alijibu hivi kwa ukaidi: “BWANA ni nani, hata niisikilize sauti yake, na kuwapa Israeli ruhusa waende zao?”—Kutoka 5:2.
Je, ungeweza kuwazia Muumba wa ulimwengu akitishwa na wito kama huo, hata kama ulitolewa na mtawala wa mamlaka yenye nguvu zaidi kijeshi iliyokuwapo wakati huo? Mungu akawapiga Farao na Wamisri kwa mfululizo wa mapigo. Hatimaye, baada ya pigo la kumi, Farao akakubali kuwaachilia Waisraeli. (Kutoka 12:29-32) Basi, wazao wa Abrahamu wakamjua Yehova kuwa mtu halisi—mtu anayeandaa uhuru kwa wakati wake. Ndiyo, kama jina lake lidokezavyo, Yehova akawa mtimizaji wa ahadi zake katika njia zenye kutazamisha sana. (Kutoka 6:3) Lakini, Farao na Waisraeli bado walikuwa wajifunze hata mengi zaidi kuhusu jina hilo.
Hilo lilitukia kwa sababu Farao alibadili maoni yake upesi. Aliongoza jeshi lake kuwakimbiza kwa bidii wale watumwa waliokuwa wakienda, akiwafikia karibu na Bahari Nyekundu. Waisraeli walinaswa kati ya bahari na jeshi la Misri. Kisha Yehova akaingilia kwa kufungua njia kupitia Bahari Nyekundu. Farao angalipaswa kutambua kwamba huo ulikuwa wonyesho wa uwezo wa Mungu usioweza kushindwa. Badala yake, yeye aliongoza jeshi lake himahima kufuata Waisraeli—akazama na jeshi lake Mungu aliporudisha bahari katika hali yake ya kawaida. Masimulizi yaliyo katika Kutoka hayasemi kihususa jinsi Mungu alivyotimiza matendo hayo. Twaweza kuyaita kwa haki kuwa miujiza kwa sababu matendo hayo na wakati yalipotukia hayangeweza kuongozwa na wanadamu. Kwa hakika, matendo kama hayo hayangemshinda Yule aliyeuumba ulimwengu pamoja na sheria zake zote.—Kutoka 14:1-31.
Tukio hili likawadhihirishia Waisraeli—na hata sisi pia—kwamba Yehova ndiye Mwokoaji atendaye kulingana na jina lake. Lakini, kutokana na masimulizi haya twapaswa kufahamu hata mengi zaidi kuhusu njia za Mungu. Kwa mfano, yeye alitekeleza haki dhidi ya taifa lenye kuonea, na kuonyesha upendo wenye fadhili kwa watu wake ambao kupitia hao Mbegu ingekuja. Kwa habari ya mbegu hiyo, yale tusomayo katika Kutoka ni zaidi ya historia tu ya kale; inahusiana na kusudi la Mungu la kufanya baraka ipatikane kwa wote.
Kuendelea Hadi Bara Lililoahidiwa
Baada ya kuondoka Misri, Musa na watu walivuka jangwa hadi Mlima Sinai. Kile kilichotukia huko kiliongoza shughuli za Mungu na taifa hilo kwa karne nyingi zilizofuata. Yeye aliandaa sheria. Bila shaka, muda mrefu sana kabla ya tukio hilo tayari Muumba alikuwa amefanyiza sheria zenye kuongoza ulimwengu wetu, na sheria hizo zingali zinatumika. Lakini, kwenye Mlima Sinai alimtumia Musa kuandaa sheria za taifa. Twaweza kusoma yale ambayo Mungu alifanya na juu ya mfumo wa Sheria alioandaa katika kitabu cha Kutoka na vile vitabu vitatu vinavyofuata—Mambo ya Walawi, Hesabu, na Kumbukumbu la Torati. Wasomi wanaamini kwamba Musa aliandika pia kitabu cha Ayubu. Tutazungumzia baadhi ya mambo yake makuu katika Sura ya 10.
Hata leo hii, mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanajua au wanajaribu kufuata zile Amri Kumi, ambazo ndizo mwongozo mkuu wa maadili wa huu mfumo kamili wa Sheria. Lakini, sheria hizo zina mielekezo mingine mingi ambayo huvutia watu kwa ubora wake. Inaeleweka kwamba sheria nyingi zilihusu maisha ya Waisraeli wakati huo, kama vile sheria za usafi wa kimwili, usafi wa kiafya, na zenye kuhusu maradhi. Ingawa awali zilikusudiwa zitumiwe na watu wa kale, sheria hizo huonyesha mambo ya kisayansi ambayo wataalamu wa kibinadamu wamegundua tu katika karne moja hivi iliyopita. (Mambo ya Nyakati 13:46, 52; 15:4-13; Hesabu 19:11-20; Kumbukumbu la Torati 23:12, 13) Kwa kufaa huenda mtu akauliza, Inawezekanaje kwamba sheria za Israeli la kale zilionyesha ujuzi na hekima zilizoshinda kwa mbali zile zilizojulikana na mataifa ya wakati huo? Jibu lenye kupatana na akili ni kwamba sheria hizo zilitoka kwa Muumba.
Sheria pia zilisaidia kuhifadhi vizazi vya familia na kuweka wajibu wa kidini ambao ungefuatwa na Waisraeli mpaka wakati ambapo ile Mbegu ingetokea. Kwa kukubali kufanya yale yote ambayo Mungu alikuwa amesema, waliwajibika kuishi kwa kupatana na Sheria hiyo. (Kumbukumbu la Torati 27:26; 30:17-20) Ni kweli kwamba wao hawangeweza kushika Sheria kikamilifu. Na hata hiyo ilikuwa na kusudi zuri. Mtaalamu mmoja wa sheria alieleza baadaye kwamba Sheria ilifanya “mikiuko-sheria iwe dhahiri, mpaka mbegu iwasili ambayo kwayo ahadi ilikuwa imetolewa.” (Wagalatia 3:19, 24) Basi mfumo wa Sheria uliwafanya wawe watu walio tofauti, uliwakumbusha kwamba walihitaji ile Mbegu, au Mesiya, na kuwatayarisha wamkaribishe.
Waisraeli, waliokuwa wamekusanyika kwenye Mlima Sinai, walikubali kushika mfumo wa Sheria wa Mungu. Basi wao wakafanya kile Biblia inachokiita agano, au mapatano. Agano hilo lilifanywa kati ya taifa hilo na Mungu. Japo walifanya agano hilo kwa hiari, wao wakawa wenye shingo ngumu. Kwa mfano, wao walifanyiza ndama ya dhahabu ili iwakilishe Mungu. Hiyo ilikuwa dhambi kwa sababu ibada ya sanamu ilivunja moja kwa moja zile Amri Kumi. (Kutoka 20:4-6) Isitoshe, walilalamika juu ya maandalizi waliyopewa, walimwasi kiongozi wao (Musa) aliyewekwa rasmi na Mungu, na kujiingiza katika ukosefu wa adili pamoja na wanawake wa kigeni walioabudu sanamu. Lakini kwa nini mambo haya yatupendeze, sisi tunaoishi mbali sana na wakati wa Musa?
Tena, hii si historia tu ya kale. Masimulizi ya Biblia kuhusu matendo ya Israeli yasiyo na shukrani na jinsi Mungu alivyotenda yaonyesha kwamba kwa kweli yeye anajali. Biblia yasema kwamba Waisraeli walimjaribu Yehova “tena na tena,” wakimfanya “ahuzunike” na kumtia “uchungu.” (Zaburi 78:40, 41, NW) Kwa hiyo, twaweza kuwa na uhakika wa kwamba Muumba ana hisia na kwamba yeye anajali kile ambacho wanadamu wanafanya.
Kwa maoni yetu sisi wanadamu, huenda mtu akafikiri kwamba kosa la Israeli lingefanya Mungu afutilie mbali agano lake na labda achague taifa jingine ili atimize ahadi yake. Lakini hakufanya hivyo. Badala yake, yeye aliwaadhibu wakosaji hao waliokuwa waovu lakini akawaonyesha rehema taifa zima lililopotoka. Ndiyo, Mungu aliendelea kuwa mwaminifu-mshikamanifu kwa ahadi aliyompa rafiki yake mwaminifu Abrahamu.
Baada ya muda mfupi, Israeli lilikaribia Kanaani, ambayo Biblia huita Bara Lililoahidiwa. Lilikuwa limekaliwa na watu wenye matendo mapotovu sana kiadili. Muumba alikuwa ameruhusu miaka 400 ipite bila kuwaingilia, lakini sasa aliamua kwa haki kulipatia Israeli la kale bara hilo. (Mwanzo 15:16; ona pia “Mungu Mwenye Wivu—Katika Maana Gani?,” ukurasa wa 132-133.) Kwa matayarisho Musa aliwatuma wapelelezi 12 kwenye bara hilo. Kumi kati yao hawakuonyesha imani katika nguvu ya Yehova ya kuokoa. Ripoti yao iliwasukuma watu wanung’unike dhidi ya Mungu na kufanya hila ya kutaka kurudi Misri. Tokeo likawa kwamba Mungu akawahukumu watu watange-tange jangwani kwa miaka 40.—Hesabu 14:1-4, 26-34.
Hukumu hiyo ilitimiza nini? Kabla ya kifo chake, Musa aliwahimiza wana wa Israeli wakumbuke ile miaka ambayo Yehova aliwanyenyekeza. Musa aliwaambia: “Nawe fikiri moyoni mwako, ya kuwa kama vile baba amrudivyo mwanawe, ndivyo BWANA, Mungu wako, akurudivyo.” (Kumbukumbu la Torati 8:1-5) Japo walitenda kwa njia ya kumtukana, Yehova aliwatunza, akionyesha kwamba wao hawangeweza kujitegemea. Kwa mfano, wao waliokoka kwa sababu aliandalia taifa hilo mana, vitu vyenye kulika vyenye ladha kama ya keki zenye asali. Kwa wazi, wao wangalijifunza mengi kutokana na mambo waliyojionea jangwani. Hayo yangalithibitisha umuhimu wa kumtii Mungu wao mwenye rehema na kumtegemea.—Kutoka 16:13-16, 31; 34:6, 7.
Baada ya kifo cha Musa, Mungu alimpa Yoshua utume wa kuongoza Israeli. Mwanamume huyo shujaa aliye mwaminifu-mshikamanifu aliingiza taifa hilo Kanaani na kwa moyo mkuu akaanza kuliteka. Kwa kipindi kifupi sana, Yoshua alishinda wafalme 31 na kukalia sehemu kubwa ya Bara Lililoahidiwa. Unaweza kupata masimulizi haya yenye kuvutia katika kitabu cha Yoshua.
Utawala Bila Mfalme wa Kibinadamu
Kotekote katika safari yao jangwani na katika miaka ya mapema wakiwa katika Bara Lililoahidiwa, taifa hilo liliongozwa na Musa kisha Yoshua. Waisraeli hawakuhitaji mfalme wa kibinadamu, kwa kuwa Yehova alikuwa ndiye Mwenye Enzi Kuu wao. Yeye alifanya maandalizi ya wanaume wazee waliowekwa rasmi wasikize kesi za kisheria kwenye malango ya jiji. Wao walidumisha utaratibu na kuwasaidia watu kiroho. (Kumbukumbu la Torati 16:18; 21:18-20) Kitabu cha Ruthu chatuonyesha kifupi jinsi wanaume hao wazee walivyoshughulikia kesi moja ya kisheria kwa kutegemea sheria iliyopatikana katika Kumbukumbu la Torati 25:7-9.
Katika miaka iliyopita, mara nyingi taifa hilo halikumpendeza Mungu kwa sababu mara kwa mara hawakumtii nao waligeukia miungu ya Wakanaani. Lakini, hali ilipokuwa mbaya sana na wakamwitia Yehova awape msaada, yeye aliwakumbuka. Aliwateua waamuzi wenye kuchukua uongozi katika kukomboa Israeli, wakiwaokoa kutokana na majirani wao wenye kuwadhulumu. Kitabu kiitwacho Waamuzi chaonyesha dhahiri matendo ya waamuzi 12 miongoni mwa waamuzi hao wenye moyo mkuu.—Waamuzi 2:11-19; Nehemia 9:27.
Rekodi hiyo inasema hivi: “Siku hizo hapakuwa na mfalme katika Israeli; kila mtu alifanya yaliyokuwa ni mema machoni pake mwenyewe.” (Waamuzi 21:25) Taifa lilikuwa na viwango vya maadili vilivyokuwa katika Sheria, basi kwa msaada wa wanaume wazee na maagizo kutoka kwa makuhani, watu walikuwa na msingi wa ‘kufanya yaliyokuwa ni mema machoni pao’ na wawe salama. Na zaidi, mfumo wa Sheria uliandaa tabenakulo, au hema lenye kubebeka, ambamo dhabihu zilitolewa. Ibada ya kweli ilikuwa ikifanywa huko nayo ilisaidia kuunganisha taifa wakati huo.
Sehemu ya Pili—Ufanisi Chini ya Wafalme
Samweli alipokuwa mwamuzi katika Israeli, watu walidai kwamba wanataka mfalme wa kibinadamu. Wafalme wa kwanza watatu—Sauli, Daudi, na Solomoni—walitawala kwa miaka 40 kila mmoja, tokea mwaka wa 1117 hadi 997 K.W.K. Israeli likafikia kilele cha utajiri na utukufu, na Muumba alichukua hatua muhimu za kutayarisha utawala kwa ajili ya Mbegu ijayo.
Akiwa mwamuzi na nabii, Samweli alitunza vema hali ya kiroho ya Israeli, lakini wana wake walikuwa tofauti. Hatimaye watu wakamsisitizia Samweli hivi: “Basi, tufanyie mfalme atuamue, mfano wa mataifa yote.” Yehova akamweleza Samweli umaana wa madai yao: “Isikilize sauti ya watu hawa . . . kwa maana hawakukukataa wewe, bali wamenikataa mimi, ili nisiwe mfalme juu yao.” Yehova aliona kimbele matokeo yenye kuhuzunisha ya jambo hilo. (1 Samweli 8:1-9) Lakini, kwa kupatana na dai lao, yeye alimteua mtu mmoja mwenye kiasi aliyeitwa Sauli kuwa mfalme wa Israeli. Japo alianza vizuri, baada ya kuwa mfalme, Sauli alionyesha mitazamo iliyopotoka, akakiuka amri za Mungu. Nabii wa Mungu akatangaza kwamba ufalme huo ungepewa mtu anayekubalika machoni pa Yehova. Jambo hilo lapasa kutukazia jinsi Muumba anavyothamini utii kutoka moyoni.—1 Samweli 15:22, 23.
Daudi, ambaye angekuwa mfalme afuataye wa Israeli, alikuwa mwana mchanga zaidi katika familia moja ya kabila la Yuda. Kuhusu chaguo hilo lenye kushangaza, Mungu alimwambia Samweli: “Wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA huutazama moyo.” (1 Samweli 16:7) Je, haitii moyo kwamba Muumba hutazama jinsi tulivyo ndani, bali si sura ya nje? Lakini, Sauli alikuwa na mawazo yake mwenyewe. Tokea wakati ambapo Yehova alimchagua Daudi awe mfalme wa wakati ujao, Sauli alishikwa na kichaa—akiwa na mori ya kumwua Daudi. Yehova hakuruhusu jambo hilo litendeke, na hatimaye Sauli na wana wake wakafa vitani dhidi ya watu waitwao Wafilisti.
Daudi alitawala akiwa mfalme katika jiji la Hebroni. Kisha akateka Yerusalemu na kuhamisha makao yake makuu huko. Pia alipanua mipaka ya Israeli kufikia kiwango kamili ambacho Mungu alikuwa ameahidi kuwapa wazao wa Abrahamu. Unaweza kusoma juu ya kipindi hiki (na historia ya wafalme wa baadaye) katika vitabu sita vya historia vya Biblia.b Vitabu hivyo vinafunua kwamba maisha ya Daudi yalikuwa pia na matatizo. Kwa mfano, akishindwa na tamaa ya kibinadamu, alifanya uzinzi na yule Bath-sheba mrembo kisha akafanya makosa mengine ya kufunika dhambi yake. Akiwa Mungu wa haki, Yehova hangepuuza tu kosa la Daudi. Lakini kwa sababu ya toba ya moyoni ya Daudi, Mungu hakutaka adhabu ya Sheria itumiwe kikamili; lakini, bado Daudi angepata matatizo mengi ya familia kwa sababu ya dhambi zake.
Kupitia matatizo hayo yote, Daudi akamjua Mungu kuwa mtu halisi—mtu mwenye hisia. Yeye aliandika hivi: ‘BWANA yu karibu na wote wamwitao naye atakisikia kilio chao na kuwaokoa.’ (Zaburi 145:18-20) Weupe wa moyo wa Daudi na ujitoaji wake waonyeshwa wazi katika nyimbo tamu alizotunga, ambazo zimefanyiza karibu nusu ya kitabu cha Zaburi. Mamilioni ya watu wamefarijika na kutiwa moyo na mashairi hayo. Ebu fikiria jinsi Daudi alivyokuwa karibu na Mungu, kama ionyeshwavyo katika Zaburi 139:1-4: “Ee BWANA, umenichunguza na kunijua. Wewe wajua kuketi kwangu na kuondoka kwangu; umelifahamu wazo langu tokea mbali. . . . Maana hamna neno ulimini mwangu usilolijua kabisa, BWANA.”
Daudi hasa alifahamu nguvu ya Mungu ya kuokoa. (Zaburi 20:6; 28:9; 34:7, 9; 37:39) Kila wakati alipojionea nguvu hiyo, tumaini lake kwa Yehova lilikua. Unaweza kuona uthibitisho wa jambo hilo katika Zaburi 30:5; 62:8; na 103:9. Au soma Zaburi 51, ambayo Daudi alitunga baada ya kukaripiwa kwa kutenda dhambi na Bath-sheba. Inafariji kama nini kujua kwamba tunaweza kujieleza kwa utayari kwa Muumba, tukiwa na uhakika wa kwamba yeye hana kiburi bali yuko tayari kusikiliza kwa unyenyekevu! (Zaburi 18:35; 69:33; 86:1-8) Daudi hakupata uthamini huo kupitia mambo aliyojionea tu. Aliandika hivi: “Nimeyatafakari matendo yako yote, naziwaza kazi za mikono yako.”—Zaburi 63:6; 143:5.
Yehova alifanya agano la kipekee na Daudi kwa ajili ya ufalme wa milele. Labda Daudi hakuelewa umaana hasa wa agano hilo, lakini kutokana na mambo madogo-madogo yaliyorekodiwa baadaye katika Biblia, twaweza kuona kwamba Mungu alikuwa akionyesha kwamba Mbegu iliyoahidiwa ingekuja katika nasaba ya Daudi.—2 Samweli 7:16.
Mfalme Solomoni Mwenye Hekima na Umaana wa Maisha
Solomoni, mwana wa Daudi alijulikana sana kwa hekima yake, nasi twaweza kunufaika nayo kwa kusoma vitabu vyenye kutumika sana maishani vya Mithali na Mhubiri.c (1 Wafalme 10:23-25) Hasa kitabu cha Mhubiri ni chenye msaada sana kwa watu ambao wanatafuta umaana wa maisha, kama tu alivyofanya Mfalme Solomoni mwenye hekima. Akiwa mfalme wa kwanza Mwisraeli aliyezaliwa katika familia ya kifalme, Solomoni alikuwa na mambo mengi sana ambayo angeweza kufanya. Pia alianzisha miradi mitukufu ya ujenzi, alikuwa na vyakula vya aina nyingi mezani pake, na kufurahia muziki na ushirika wa waandamani wenye kutokeza sana. Lakini, akaandika hivi: “Nikaziangalia kazi zote zilizofanywa kwa mikono yangu, na taabu yote niliyotaabika katika kuzitenda; na tazama, yote ni ubatili.” (Mhubiri 2:3-9, 11) Alimaanisha nini?
Solomoni aliandika: “Hii ndiyo jumla ya maneno; yote yamekwisha sikiwa; Mche Mungu, nawe uzishike amri zake, maana kwa jumla ndiyo impasayo mtu. Kwa maana Mungu ataleta hukumuni kila kazi, pamoja na kila neno la siri, likiwa jema au likiwa baya.” (Mhubiri 12:13, 14) Kwa kupatana na hayo, Solomoni alijishughulisha na mradi wa miaka saba, wa kujenga hekalu tukufu, ambamo watu wangemwabudu Mungu.—1 Wafalme, sura ya 6.
Kwa miaka mingi utawala wa Solomoni ulikuwa wenye amani na wingi wa vitu. (1 Wafalme 4:20-25) Lakini, bado moyo wake haukuwa mkamilifu kwa Yehova kama moyo wa Daudi. Solomoni alioa wake wengi wa kigeni akawaruhusu wafanye moyo wake uelekee miungu yao. Hatimaye Yehova akasema: “Hakika nitaurarua ufalme usiwe wako . . . Nitampa mwana wako kabila moja, kwa ajili ya Daudi mtumishi wangu, na kwa ajili ya Yerusalemu.”—1 Wafalme 11:4, 11-13.
Sehemu ya Tatu—Ufalme Wagawanywa
Baada ya kifo cha Solomoni, mnamo 997 K.W.K., makabila kumi ya kaskazini yalijitenga. Hayo yalifanyiza ufalme wa Israeli, ambao Waashuru waliuteka mnamo 740 K.W.K. Wafalme wa Yerusalemu walitawala makabila mawili. Ufalme huu, Yuda, ulidumu mpaka Wababiloni walipolishinda Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K. na kuwateka wakazi. Yuda ukawa ukiwa kwa miaka 70.
Solomoni alipokufa, mwana wake Rehoboamu akatwaa mamlaka na kufanya maisha yawe magumu kwa watu. Hilo lilitokeza maasi, na makabila kumi yalijitenga na kuwa ufalme wa Israeli. (1 Wafalme 12:1-4, 16-20) Katika miaka iliyopita, ufalme huu wa kaskazini haukushikamana na Mungu wa kweli. Watu walizoea kuinamia sanamu za ndama ya dhahabu au waliingia katika namna nyinginezo za ibada isiyo ya kweli. Baadhi ya wafalme waliuawa na utawala wa familia zao kupinduliwa na wanyakuaji. Yehova alivumilia kwa subira sana, akiwatuma tena na tena manabii wa kuonya taifa hilo kwamba lingepatwa na msiba iwapo lingeendelea na uasi wao. Vitabu vya Hosea na Amosi viliandikwa na manabii ambao ujumbe wao hasa ulikazia ufalme huu wa kaskazini. Hatimaye, mnamo 740 K.W.K., Waashuru walileta msiba ambao manabii wa Mungu walikuwa wametabiri.
Kule kusini, mfuatano wa wafalme 19 wa nyumba ya Daudi walitawala Yuda hadi mwaka wa 607 K.W.K. Mfalme Asa, Yehoshafati, Hezekia, na Yosia walitawala kama vile baba yao wa kale Daudi alivyotawala, nao walimpendeza Yehova. (1 Wafalme 15:9-11; 2 Wafalme 18:1-7; 22:1, 2; 2 Mambo ya Nyakati 17:1-6) Wafalme hao walipotawala, Yehova alibariki taifa hilo. Kitabu The Englishman’s Critical and Expository Bible Cyclopædia chaonelea hivi: “Desturi kuu tukufu ya Y[uda] ilikuwa ni hekalu, ukuhani, sheria iliyoandikwa, ambazo zote ziliwekwa na Mungu, na kutambua kwamba Mungu mmoja tu wa kweli Yehova ndiye mfalme wao halisi wa kitheokrasi. . . . Kushika sheria . . . kulitokeza mfululizo wa wafalme wazuri wenye hekima . . . Kwa hiyo Y[uda] ulidumu kwa muda mrefu kuliko ufalme wa kaskazini.” Wafalme hao wazuri walikuwa wachache sana kwa kulinganisha na wale ambao hawakutembea katika njia ya Daudi. Lakini, Yehova aliongoza mambo ili ‘Daudi, mtumishi wake apate kuwa na taa sikuzote mbele zake katika Yerusalemu, mji ule aliouchagua Mungu aweke jina lake huko.’—1 Wafalme 11:36.
Kuelekea Uharibifu
Manase alikuwa mmojawapo wa wafalme wa Yuda ambao waliacha ibada ya kweli. “Akampitisha mwanawe motoni, akatazama bao, akafanya uganga, akajishughulisha na hao wenye pepo wa utambuzi, na wachawi; akafanya mabaya mengi machoni pa BWANA, hata kumkasirisha.” (2 Wafalme 21:6, 16) Mfalme Manase aliwashawishi watu wake “wakazidi kufanya mabaya kuliko mataifa, aliowaharibu BWANA.” Baada ya kumwonya Manase na watu wake kwa kurudia-rudia, Muumba akatangaza: “Nitaifuta Yerusalemu, kama mtu afutavyo sahani.”—2 Mambo ya Nyakati 33:9, 10; 2 Wafalme 21:10-13.
Ukiwa kama utangulizi, Yehova aliwaruhusu Waashuru wamkamate Manase na kumchukua mateka akiwa amefungwa pingu za shaba. (2 Mambo ya Nyakati 33:11) Akiwa uhamishoni Manase akatambua makosa yake na ‘kujinyenyekeza sana mbele za Mungu wa baba zake.’ Yehova alitendaje? “[Mungu] akayasikia maombi yake; akamrudisha tena Yerusalemu katika ufalme wake. Ndipo Manase akajua ya kwamba BWANA [“Yehova,” NW] ndiye Mungu.” Mfalme Manase na mjukuu wake, Mfalme Yosia, wote walifanya marekebisho yaliyotakikana. Lakini, bado taifa hilo halikuacha kabisa upotovu mwingi wa kiadili na wa kidini.—2 Mambo ya Nyakati 33:1-20; 34:1–35:25; 2 Wafalme, sura ya 22.
Jambo la muhimu ni kwamba Yehova aliwatuma manabii wenye bidii wakatangaze maoni yake juu ya mambo yaliyokuwa yakitendeka.d Yeremia alisimulia maneno ya Yehova: “Tokea siku ile baba zenu walipotoka katika nchi ya Misri hata leo, nimewatuma watumishi wangu wote manabii kwenu ninyi, nikiamka mapema kila siku, na kuwatuma.” Lakini watu hawakumsikiliza Mungu. Wao walitenda vibaya hata zaidi ya baba zao! (Yeremia 7:25, 26) Yeye aliwaonya kwa kurudia-rudia “kwa sababu aliwahurumia watu wake.” (Italiki ni zetu.) Bado walikataa kutii. Basi akaruhusu Wababiloni waharibu Yerusalemu na kulifanya ukiwa mnamo 607 K.W.K. Kwa miaka 70 lilibaki ukiwa.—2 Mambo ya Nyakati 36:15, 16; Yeremia 25:4-11.
Pitio hili fupi la matendo ya Mungu lapasa kutusaidia kutambua hangaiko la Yehova na shughuli zake zenye haki pamoja na taifa lake. Yeye hakuachilia tu mambo na kungoja kuona kile ambacho watu wangefanya, kana kwamba hakujali. Yeye alijaribu kuwasaidia. Unaweza kuthamini ni kwa nini Isaya alisema hivi: “Ee BWANA, wewe u baba yetu . . . sisi sote tu kazi ya mikono yako.” (Isaya 64:8) Kwa kupatana na hayo, wengi leo hurejezea Muumba kuwa “Baba,” kwa kuwa yeye hutenda kama vile baba wa kibinadamu mwenye upendo na mwenye kupendezwa na mambo atendavyo. Hata hivyo, yeye hutambua pia kwamba ni lazima tuchukue daraka la mwendo wetu na matokeo yake.
Baada ya taifa hilo kuwa utekwani kwa kipindi cha miaka 70 Babiloni, Yehova Mungu alitimiza unabii wake wa kurudisha Yerusalemu. Watu waliachiliwa huru na kuruhusiwa kurudi nyumbani ili ‘kuijenga nyumba ya BWANA Yerusalemu.’ (Ezra 1:1-4; Isaya 44:24–45:7) Vitabu kadhaa vya Bibliae vyazungumzia urudisho huo, kujengwa upya kwa hekalu, na matukio yaliyofuata. Mojawapo ya vitabu hivyo, Danieli, hasa ni chenye kupendeza kwa sababu kilitoa unabii juu ya wakati hasa ambapo ile Mbegu, au Mesiya, ingetokea, nacho kilitabiri matukio ya ulimwengu ya wakati wetu.
Hatimaye hekalu lilijengwa upya, lakini Yerusalemu lilikuwa katika hali yenye kusikitisha. Kuta zake na malango yake yalikuwa yamekuwa magofu. Basi Mungu akawateua wanaume kama vile Nehemia ili awatie moyo Wayahudi na kuwapanga. Sala ambayo twaweza kusoma katika Nehemia sura ya 9 inajumlisha ifaavyo shughuli za Yehova pamoja na Waisraeli. Inaonyesha kwamba Yehova ni ‘Mungu aliye tayari kusamehe, mwenye neema, mwenye huruma nyingi, si mwepesi wa hasira, mwingi wa rehema.’ Sala hiyo inaonyesha pia kwamba Yehova hutenda kwa kupatana na viwango vyake vikamilifu vya haki. Hata wakati ambapo ana sababu nzuri ya kudhihirisha uwezo wake wa kutekeleza hukumu, yeye yu tayari kutenda kwa haki na kwa upendo. Kuweza kwake kufanya hivyo kwa usawaziko na kwa njia yenye kuvutia kwahitaji hekima. Kwa wazi, shughuli za Muumba pamoja na taifa la Israeli, zapasa kutuvuta kwake na kutuchochea kutaka kufanya mapenzi yake.
Sehemu hii ya Biblia (Agano la Kale) imalizikapo, Yuda, pamoja na hekalu lake Yerusalemu, lilirudishwa lakini likiwa chini ya utawala wa kipagani. Basi, lile agano la Mungu pamoja na Daudi kuhusu “mbegu” ambayo ingetawala “milele” lingetimizwaje? (Zaburi 89:3, 4; 132:11, 12, linganisha NW.) Wayahudi bado walikuwa wakitazamia kutokea kwa “Masihi aliye mkuu” ambaye angewaweka huru watu wa Mungu na kuweka ufalme wa kitheokrasi (wenye kutawalwa na Mungu) duniani. (Danieli 9:24, 25) Lakini, je, hilo lilikuwa kusudi la Yehova? Kama sivyo, Mesiya aliyeahidiwa angeletaje wokovu? Na jambo hilo latuhusuje leo? Sura ifuatayo itazungumzia masuala haya muhimu.
[Maelezo ya Chini]
a Majina ya vitabu vya Biblia yana maandishi mazito ili kusaidia kutambua yaliyomo.
b Vitabu hivyo ni 1 Samweli, 2 Samweli, 1 Wafalme, 2 Wafalme, 1 Mambo ya Nyakati, na 2 Mambo ya Nyakati.
c Pia aliandika Wimbo Ulio Bora, shairi la mapenzi linalokazia uaminifu-mshikamanifu wa mwanamke kijana kwa mchungaji mnyenyekevu.
d Vitabu kadhaa vya Biblia vina ujumbe kama huo uliopuliziwa. Vitabu hivyo vinatia ndani Isaya, Yeremia, Maombolezo, Ezekieli, Yoeli, Mika, Habakuki, Sefania. Vitabu vya Obadia, Yona, na Nahumu vilikazia mataifa jirani ambayo shughuli zao ziliathiri watu wa Mungu.
e Hivi vitabu vya historia na unabii vyatia ndani Ezra, Nehemia, Esta, Hagai, Zekaria, na Malaki.
[Sanduku katika ukurasa wa 126, 127]
Miujiza—Je, Unaweza Kuiamini?
“Haiwezekani kukubali tekinolojia ya kisasa kama vile taa za umeme, redio na maendeleo ya kitiba, na wakati huohuo kuamini roho na miujiza ya Agano Jipya.” Maneno hayo ya mwanatheolojia Mjerumani Rudolf Bultmann yaonyesha maoni ya watu wengi leo juu ya miujiza. Je, una maoni kama hayo kuhusu miujiza iliyorekodiwa katika Biblia, kama ule ambao Mungu aligawanya Bahari Nyekundu?
Kamusi The Concise Oxford Dictionary yafafanua “muujiza” kuwa “tukio lisilo la kawaida ambalo limesababishwa na nguvu zipitazo za wanadamu.” Tukio kama hilo lisilo la kawaida lahusisha kuvurugwa kwa utaratibu wa asili, jambo linalofanya wengi wasiamini miujiza. Lakini, kile kionekanacho kuwa kuvunja sheria ya asili chaweza kuelezwa kwa kufikiria sheria nyinginezo za asili zinazohusika.
Kwa mfano, gazeti New Scientist liliripoti kwamba wataalamu wawili wa fizikia katika Chuo Kikuu cha Tokyo walitumia sumaku yenye nguvu sana kwenye mrija uliolazwa ambao ulitiwa maji kwa kiasi. Maji yalikimbilia miisho ya huo mrija, sehemu ya katikati ikakauka. Tukio hilo, lililogunduliwa mnamo 1994, linatokea kwa sababu maji husukumwa kihafifu na sumaku. Tukio hilo lililothibitishwa la maji kutoka penye nguvu nyingi za sumaku hadi mahali ambapo hapana nguvu nyingi za sumaku limeitwa Athari ya Moses. Gazeti New Scientist lilisema kwamba: “Ni rahisi kusukuma-sukuma maji—ikiwa una sumaku kubwa ya kutosha. Na ikiwa hivyo, karibu kitu chochote kinawezekana.”
Bila shaka, mtu hawezi kusema kwa uhakika kabisa njia ambayo Mungu alitumia kugawanya Bahari Nyekundu kwa ajili ya Waisraeli. Lakini, Muumba ajua kabisa sheria zote za asili. Yeye angeweza kudhibiti kwa urahisi sehemu fulani ya sheria moja kwa kutumia sheria nyinginezo ambazo alifanyiza. Kwa wanadamu, matokeo yaweza kuonekana kuwa ya kimuujiza, hasa kama hawakujua vizuri sheria zilizohusika.
Kuhusu miujiza iliyo katika Biblia, Akira Yamada, profesa mstaafu wa Chuo Kikuu cha Kyoto nchini Japani, asema: “Ingawa ni sahihi kusema kwamba [muujiza] hauwezi kueleweka kwa sasa kutokana na maoni ya kisayansi ambayo mtu amejihusisha nayo (au maoni ya sasa ya sayansi), ni makosa kukata kauli kwamba haukufanyika, kwa kutegemea tu fizikia bora ya kisasa au elimu bora ya kisasa ya Biblia. Miaka kumi tokea sasa, sayansi ya kisasa ya leo itakuwa sayansi iliyopita. Kadiri sayansi ifanyavyo maendeleo haraka ndivyo uongezekavyo uwezekano wa kwamba wanasayansi wa leo watakuwa wakidhihakiwa hivi, ‘Wanasayansi wa miaka kumi iliyopita walishikilia hili na hili.’”—Gods in the Age of Science.
Akiwa Muumba, akiweza kuratibu sheria zote za asili, Yehova aweza kutumia uwezo wake ili kufanyiza miujiza.
[Sanduku katika ukurasa wa 132, 133]
Mungu Mwenye Wivu—Katika Maana Gani?
“Yehova, ambaye jina lake ni Wivu, yeye ni Mungu mwenye wivu.” Twaweza kusoma maneno hayo katika Kutoka 34:14 (NW), lakini yanamaanisha nini?
Neno la Kiebrania lililotafsiriwa “wivu” laweza kumaanisha “kudai ujitoaji usiohusisha wengine, kutovumilia ushindani.” Katika maana nzuri inayonufaisha viumbe wake, Yehova ni mwenye wivu kuhusu jina lake na ibada yake. (Ezekieli 39:25) Bidii yake ya kutimiza kile ambacho jina lake lawakilisha yamaanisha kwamba yeye atatekeleza kusudi lake kwa ajili ya wanadamu.
Kwa mfano, ebu fikiria hukumu yake dhidi ya watu walioishi katika bara la Kanaani. Msomi mmoja aeleza mambo haya yenye kushtua: “Ibada ya Baali, Ashtorethi, na miungu mingine ya Kanaani ilikuwa na desturi zenye kushangaza sana; mahekalu yao yalikuwa vitovu vya upotovu wa maadili. . . . Wakanaani waliabudu kwa kujiingiza sana katika ibada ya ukosefu wa adili, . . . kisha, waliwaua watoto wao wa kwanza kuwa dhabihu kwa miungu iyo hiyo.” Wataalamu wa mambo ya kale wamegundua magudulia yenye mabaki ya watoto waliotolewa dhabihu. Ingawa Mungu aliona kosa la Wakanaani katika siku za Abrahamu, yeye aliwaonyesha subira kwa miaka 400, akiwaruhusu muda wa kutosha wa kubadilika.—Mwanzo 15:16.
Je, Wakanaani walijua uzito wa kosa lao? Wao walikuwa na dhamiri ya kibinadamu, ambao wanasheria hutambua kuwa msingi wa ulimwenguni pote wa maadili na haki. (Waroma 2:12-15) Japo hayo, Wakanaani waliendelea kutoa dhabihu zenye kuchukiza za watoto na matendo yaliyopotoka ya kingono.
Kwa haki yake yenye usawaziko, Yehova aliazimia kwamba bara hilo lilihitaji kutakaswa. Hilo halikuwa uchinjaji wa jamii nzima-nzima. Wakanaani, wakiwa watu mmoja-mmoja kama vile Rahabu na vikundi-vikundi kama vile Wagibeoni, ambao walikubali kwa hiari viwango vya juu vya maadili vya Mungu hawakuuawa. (Yoshua 6:25; 9:3-15) Rahabu akaja kuwa katika nasaba ya kifalme iliyoelekeza kwa Mesiya, na wazao wa Wagibeoni walikuwa na pendeleo la kuhudumu katika hekalu la Yehova.—Yoshua 9:27; Ezra 8:20; Mathayo 1:1, 5-16.
Basi, mtu atafutapo habari kamili inayotegemea mambo ya hakika, ni rahisi kumwona Yehova kuwa Mungu avutiaye na mwenye haki, mwenye wivu katika njia nzuri inayonufaisha viumbe wake waaminifu.
-
-
Mwalimu Mkuu Atudhihirishia Muumba ZaidiJe, Kuna Muumba Anayekujali?
-
-
Sura Ya Tisa
Mwalimu Mkuu Atudhihirishia Muumba Zaidi
WATU wa Palestina ya karne ya kwanza ‘walikuwa na tarajio.’ Walikuwa wakitarajia nini? “Kristo,” au “Mesiya,” aliyetabiriwa na manabii wa Mungu karne nyingi zilizopita. Watu walikuwa na uhakika wa kwamba Biblia iliandikwa chini ya uelekezo wa Mungu na kwamba ilikuwa inasema mambo ya wakati ujao. Unabii mmoja kama huo, ulio katika kitabu cha Danieli, ulielekezea kufika kwa Mesiya mapema katika karne yao.—Luka 3:15; Danieli 9:24-26.
Lakini, wao walihitaji kutahadhari kwa sababu watu wenye kujifanya mesiya wangetokea. (Mathayo 24:5) Mwanahistoria Myahudi Yosefo ataja baadhi yao: Theudasi, aliyewaongoza wafuasi wake hadi Mto Yordani na kudai eti maji yake yangegawanyika; mtu fulani kutoka Misri ambaye aliongoza watu hadi Mlima wa Mizeituni, akisisitiza kwamba ukuta wa Yerusalemu ungeanguka kwa amri yake; na mlaghai mmoja wa wakati wa Gavana Festo aliyeahidi kwamba angewaondolea watu matatizo.—Linganisha Matendo 5:36; 21:38.
Tofauti na wafuasi hao waliodanganyika, kikundi kilichokuja kuitwa “Wakristo” kilimtambua Yesu wa Nazareti kuwa mwalimu mkuu aliye pia Mesiya wa kweli. (Matendo 11:26; Marko 10:47) Yesu hakuwa mesiya bandia; alikuwa na sifa za kumstahilisha kabisa, kama inavyothibitishwa vizuri katika vitabu vinne vya kihistoria viitwavyo Gospeli.a Kwa mfano, Wayahudi walijua kwamba Mesiya angezaliwa Bethlehemu, angekuwa wa uzao wa Daudi, naye angefanya matendo ya ajabu. Yesu alitimiza hayo yote, kama inavyoonyeshwa hata na ushuhuda wa wapinzani. Ndiyo, Yesu alitimiza sifa za Mesiya wa Biblia.—Mathayo 2:3-6; 22:41-45; Yohana 7:31, 42.
Umati wa watu waliokutana na Yesu walitazama matendo yake yenye kutokeza, walisikia maneno yake ya kipekee yenye hekima, na kutambua busara yake, walisadiki kwamba alikuwa ndiye Mesiya. Katika huduma yake (29-33 W.K.), uthibitisho wenye kutegemeza Umesiya wake uliongezeka. Hata akathibitika kuwa zaidi ya Mesiya. Mwanafunzi mmoja aliyefahamu mambo yake alikata kauli ya kwamba “Yesu ndiye Kristo Mwana wa Mungu.”b—Yohana 20:31.
Kwa sababu Yesu alikuwa na uhusiano wa karibu sana na Mungu, angeweza kueleza na kufunua vile Muumba alivyo. (Luka 10:22; Yohana 1:18) Yesu alitoa ushuhuda wa kwamba ukaribu wake na Baba yake ulianza akiwa mbinguni, ambako alifanya kazi pamoja na Mungu katika kutokeza vitu vingine vyote, vyenye uhai na visivyo na uhai.—Yohana 3:13; 6:38; 8:23, 42; 13:3; Wakolosai 1:15, 16.
Biblia yaripoti kwamba huyo Mwana alihamishwa kutoka makao ya roho “akaja kwa namna ya wanadamu.” (Wafilipi 2:5-8) Tukio kama hilo si la kawaida, lakini je, lawezekana? Wanasayansi wanathibitisha kwamba elementi ya asili, kama vile urani, yaweza kubadilishwa kuwa elementi nyingine; wao hata hupiga hesabu ya matokeo wakati masi inapobadilishwa kuwa nishati (E=mc2). Basi kwa nini tutilie shaka wakati Biblia isemapo kwamba kiumbe wa roho alibadilishwa ili aishi kama binadamu?
Tukitoa mfano mwingine, ebu fikiria kile ambacho baadhi ya matabibu hufanya katika utungaji wa mimba nje ya mwili. Uhai unaoanza katika “tesitubu” unaingizwa katika mwanamke na baadaye unazaliwa ukiwa mtoto mchanga. Katika kisa cha Yesu, Biblia yatuhakikishia ya kwamba kwa “nguvu ya Aliye Juu Zaidi Sana,” uhai wake uliingizwa ndani ya bikira aliyeitwa Maria. Yeye alikuwa wa nasaba ya Daudi, basi Yesu angekuwa mrithi wa daima wa Ufalme wa Mesiya ulioahidiwa Daudi.—Luka 1:26-38; 3:23-38; Mathayo 1:23.
Kwa msingi wa uhusiano wake wa karibu pamoja na Muumba na kufanana kwao, Yesu alisema: “Yeye ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yohana 14:9) Pia alisema hivi: “Ya kwamba Baba ni nani, hakuna ajuaye ila Mwana, na yeye ambaye Mwana anapenda kumfunulia.” (Luka 10:22) Kwa hiyo, tujifunzapo kile ambacho Yesu alifundisha na kufanya duniani, twaweza kuona utu wa Muumba vizuri zaidi. Ebu tufikirie hili, tukitumia mambo waliyojionea wanaume na wanawake ambao walishughulika na Yesu.
Mwanamke Msamaria
“Huyu labda ndiye Kristo, sivyo?” akauliza mwanamke Msamaria baada ya kuzungumza na Yesu kwa muda fulani. (Yohana 4:29) Hata akawahimiza wengine katika mji ulio karibu wa Sikari waje kumwona Yesu. Ni nini kilichomfanya amkubali Yesu kuwa Mesiya?
Mwanamke huyo alikutana na Yesu wakati Yesu alipokuwa akipumzika baada ya kutembea asubuhi yote kwenye barabara zenye vumbi katika vilima vya Samaria. Ingawa Yesu alikuwa amechoka, alizungumza na mwanamke huyo. Akiona upendezi wake wa kiroho wenye makini, Yesu alimweleza kweli zenye kustaajabisha kuhusu uhitaji wa ‘kumwabudu Baba kwa roho na kweli.’ Baadaye akamfunulia kwamba kwa kweli yeye ndiye Kristo, jambo ambalo bado hakuwa amekiri peupe.—Yohana 4:3-26.
Huyo mwanamke Msamaria alipata mazungumzo yake na Yesu kuwa yenye umaana sana. Ibada yake ya awali ilitegemea kuabudu kwenye Mlima Gerizimu na kutegemea vile vitabu vitano tu vya kwanza vya Biblia. Wayahudi waliwaepuka Wasamaria, wengi wao wakiwa wa uzao mchanganyiko wa kati ya makabila kumi ya Israeli na watu wengine. Yesu alikuwa tofauti kama nini! Kwa hiari, alimfundisha Msamaria huyo, hata ingawa alitumwa kuwaendea “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli.” (Mathayo 15:24) Hapo Yesu alionyesha utayari wa Yehova wa kukubali watu wanyoofu wa mataifa yote. (1 Wafalme 8:41-43) Ndiyo, Yesu na Yehova hawana uhasama wa kidini ambao umejaa ulimwenguni leo. Kujua jambo hilo kwapasa kutuvutia kwa Muumba na Mwana wake.
Kuna somo jingine tuwezalo kupata katika utayari wa Yesu wa kumfundisha mwanamke huyu. Wakati huo huyo mwanamke alikuwa akiishi na mwanamume ambaye hakuwa mume wake. (Yohana 4:16-19) Lakini, Yesu hakuacha jambo hilo limzuie asiseme naye. Unafahamu kwamba ni lazima mwanamke huyo alithamini kutendewa kwa staha. Na si yeye pekee aliyetendewa hivyo. Viongozi fulani wa Kiyahudi (Mafarisayo) walipomchambua Yesu kwa kula pamoja na watenda-dhambi wenye kutubu, yeye alisema: “Watu wenye afya hawahitaji tabibu, bali wenye kuugua wahitaji. Nendeni, basi, na mjifunze kile ambacho hili lamaanisha, ‘Mimi nataka rehema, wala si dhabihu.’ Kwa maana nilikuja kuita, si watu waadilifu, bali watenda-dhambi.” (Mathayo 9:10-13) Yesu aliwapa msaada watu waliokuwa wakiugua kwa mzigo wa dhambi zao—za kukiuka sheria au viwango vya Mungu. Ni jambo lenye kuchangamsha moyo kama nini kujifunza kwamba Mungu na Mwana wake watasaidia wale ambao wana matatizo yatokanayo na mwenendo wao wa zamani!—Mathayo 11:28-30.c
Tusipuuze jambo la kwamba pindi hii katika Samaria, Yesu alizungumza na mwanamke kwa fadhili na kwa njia yenye msaada. Kwa nini hilo ni jambo muhimu? Wakati huo wanaume Wayahudi walifundishwa kwamba wanapaswa kuepuka kuzungumza na wanawake peupe, hata wake zao wenyewe. Marabi wa Kiyahudi waliwaona wanawake kuwa hawangeweza kufahamu mambo ya ndani ya kiroho na kuwaona kuwa “wenye akili ndogo.” Wengine walisema: “Ni afadhali maneno ya sheria yachomwe kuliko kuwaambia wanawake juu yake.” Wanafunzi wa Yesu walilelewa katika mazingira kama hayo; basi waliporudi, “wakaanza kustaajabu kwa sababu alikuwa akisema na mwanamke.” (Yohana 4:27) Masimulizi hayo—ambayo ni mojawapo ya mengi—yaonyesha kwamba Yesu alifanana na Baba yake, ambaye aliwaumba na kuwapa heshima wanaume na wanawake.—Mwanzo 2:18.
Baadaye yule mwanamke Msamaria aliwasadikisha wakazi wenzake wa mji kumsikiliza Yesu. Wengi waliyachunguza mambo wakawa waamini, wakisema: “Twajua kwamba mtu huyu kwa hakika ndiye mwokozi wa ulimwengu.” (Yohana 4:39-42) Kwa kuwa sisi ni sehemu ya “ulimwengu” wa wanadamu, Yesu ni muhimu katika wakati wetu ujao pia.
Maoni ya Mvuvi
Sasa ebu tumchunguze Yesu kupitia maoni ya washiriki wake wawili wa karibu—Petro kisha Yohana. Wavuvi hao wa kawaida walikuwa miongoni mwa wafuasi wake wa kwanza. (Mathayo 4:13-22; Yohana 1:35-42) Mafarisayo waliwaona kuwa “watu wasio na elimu na wa kawaida tu,” wakiwa baadhi ya watu wa hali ya chini (ʽam-ha·ʼaʹrets), ambao walidharauliwa kwa sababu hawakusoma kama marabi. (Matendo 4:13; Yohana 7:49) Watu wengi kama hao, waliokuwa ‘wakimenyeka na kulemezwa mzigo’ na nira ya washika-mapokeo wa kidini, walitamani kupata nuru ya kiroho. Profesa Charles Guignebert wa Sorbonne alisema kwamba “mioyo yao ilikuwa ya Yahweh [Yehova] kabisa.” Yesu hakuwapuuza watu hao wanyenyekevu kwa kupendelea wenye mali au walio mashuhuri. Badala yake, aliwafunulia Baba kupitia mafundisho na matendo yake.—Mathayo 11:25-28.
Petro alijionea mtazamo wa Yesu wa kujali. Punde tu baada ya kujiunga na Yesu katika huduma, mama-mkwe wa Petro akawa mgonjwa kwa homa. Akija nyumbani kwa Petro, Yesu akamshika mama huyo kwa mkono, na homa ikaisha! Huenda tusijue hasa njia hiyo ya tiba, kama vile tu leo wanatiba hawawezi kueleza vizuri jinsi ambavyo baadhi ya tiba hutokea, lakini homa ilimwondoka mwanamke huyo. Jambo kubwa zaidi kuliko kujua njia yake ya tiba ni kuthamini kwamba kwa kuponya wagonjwa na wenye mapigo, Yesu alionyesha jinsi alivyowasikitikia. Kwa kweli alitaka kuwasaidia watu, na ndivyo ilivyo na Baba yake. (Marko 1:29-31, 40-43; 6:34) Kutokana na mambo aliyojionea akiwa na Yesu, Petro angeweza kuona kwamba Muumba amwona kila mtu kuwa astahili kutunzwa.—1 Petro 5:7.
Baadaye, Yesu alikuwa katika Ua wa Wanawake katika hekalu la Yerusalemu. Aliwatazama watu wakiweka michango katika masanduku ya hazina. Matajiri waliweka sarafu nyingi. Akiwa makini, Yesu aliona mjane maskini akitumbukiza sarafu mbili zenye thamani kidogo sana. Yesu akawaambia Petro, Yohana, na wengine: “Kwa kweli nawaambia nyinyi kwamba mjane maskini huyu alitumbukiza ndani zaidi ya wote wale waliokuwa wakitumbukiza fedha ndani ya masanduku ya hazina; kwa maana wote walitumbukiza ndani kutokana na ziada yao, lakini yeye, kutokana na uhitaji wake, alitumbukiza ndani vyote alivyokuwa navyo.”—Marko 12:41-44.
Unaweza kuona kwamba Yesu aliangalia sifa nzuri za watu naye alithamini jitihada za kila mtu. Unafikiri hilo liliwavutiaje Petro na mitume wengine? Kwa kutazama kutokana na kielelezo cha Yesu jinsi Yehova alivyo, Petro alinukuu zaburi moja: “Macho ya Yehova yako juu ya waadilifu, na masikio yake yaelekea dua zao.” (1 Petro 3:12; Zaburi 34:15, 16) Je, wewe huvutiwi na Muumba na Mwana wake ambao hutaka kuona wema wako na ambao watasikiliza dua zako?
Baada ya miaka miwili hivi ya kushirikiana na Yesu, Petro alikuwa na uhakika wa kwamba Yesu alikuwa ndiye Mesiya. Pindi moja Yesu aliwauliza wanafunzi wake hivi: “Watu wanasema kwamba mimi ni nani?” Akapata majibu tofauti-tofauti. Akawauliza: “Ingawa hivyo, nyinyi mwasema mimi ni nani?” Petro akajibu akiwa na uhakika: “Wewe ndiwe Kristo.” Unaweza kushangazwa na hatua ambayo Yesu alichukua. “Akawaagiza kwa mkazo wasimwambie yeyote” jambo hilo. (Marko 8:27-30; 9:30; Mathayo 12:16) Kwa nini alisema hivyo? Yesu mwenyewe alikuwapo kati yao, basi hakutaka watu wafikie maamuzi yaliyotegemea tu mambo yaliyosikiwa. Hilo lapatana na akili, sivyo? (Yohana 10:24-26) Jambo kuu ni kwamba, Muumba wetu vilevile anataka tujue mambo juu yake kupitia kujichunguzia wenyewe ushuhuda halisi. Anatutarajia tuwe na usadikisho unaotegemea mambo ya hakika.—Matendo 17:27.
Kama unavyojua, baadhi ya watu wa nchi ya Yesu hawakumkubali, japo uthibitisho wa kutosha wa kwamba alikuwa ameungwa mkono na Muumba. Wengi, wakishughulikia tu vyeo vyao au miradi yao ya kisiasa, hawakumpenda huyo Mesiya mnyenyekevu na mwenye kufuatia haki. Huduma yake ilipokaribia mwisho, Yesu alisema: “Yerusalemu, muuaji wa manabii na mpigaji kwa mawe wale waliotumwa kwake,—ni mara nyingi kadiri gani nilitaka kuwakusanya watoto wako pamoja . . . Lakini nyinyi watu hamkutaka hilo. Tazameni! Nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mathayo 23:37, 38) Badiliko hilo kwa taifa hilo likawa hatua muhimu katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu la kubariki mataifa yote.
Punde tu baadaye Petro na mitume wengine watatu walisikia Yesu akitoa unabii wenye mambo mengi kuhusu “umalizio wa mfumo wa mambo.”d Mambo ambayo Yesu alitabiri yalitimizwa kwanza wakati wa shambulio la Waroma dhidi ya Yerusalemu na kuharibiwa kwake mnamo 66-70 W.K. Historia yathibitisha kwamba yale aliyoyatabiri Yesu kwa kweli yalitukia. Petro alishuhudia mambo yaleyale ambayo Yesu alitabiri, na hilo laonyeshwa katika Petro wa 1 na wa 2, vile vitabu viwili ambavyo Petro aliviandika.—1 Petro 1:13; 4:7; 5:7, 8; 2 Petro 3:1-3, 11, 12.
Katika huduma yake, kwa subira Yesu alikuwa amewaonyesha fadhili Wayahudi waliokuwa naye. Lakini hakusita kushutumu uovu wao. Jambo hilo lilimsaidia Petro, nalo laweza kutusaidia kumwelewa Muumba wetu vizuri zaidi. Petro alipoona mambo mengine yakitimiza unabii wa Yesu, aliandika kwamba Wakristo wadumishe “kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova.” Petro pia alisema: “Yehova si wa polepole kwa habari ya ahadi yake, kama watu fulani waonavyo kuwa ni upolepole, bali yeye ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” Kisha Petro akatoa maneno yenye kutia moyo kuhusu ‘mbingu mpya na dunia mpya ambazo katika hizo uadilifu utakaa.’ (2 Petro 3:3-13) Je, sisi kama Petro, tunathamini sifa za Mungu zinazoonyeshwa katika Yesu, na je tunadhihirisha kwamba tunatumaini ahadi zake za wakati ujao?
Kwa Nini Yesu Alikufa?
Usiku wake wa mwisho akiwa na mitume, Yesu alishiriki mlo wa kipekee pamoja nao. Kwenye mlo kama huo, mkaribishaji Myahudi angeonyesha ukaribishaji wake kwa kuwaosha miguu wageni wake, ambao huenda walikuwa wametembea kwenye barabara zenye vumbi kwa makubazi. Lakini, hakuna mtu aliyejitolea kumwosha Yesu miguu. Basi, kwa unyenyekevu aliinuka, akachukua taulo na beseni, na kuanza kuosha miguu ya mitume wake. Zamu ya Petro ilipofika, aliona aibu kukubali kutumikiwa na Yesu. Petro akasema: “Hakika wewe hutaosha kamwe miguu yangu.” Yesu akajibu, “Isipokuwa nikuoshe, wewe huna sehemu pamoja na mimi.” Yesu alijua ya kwamba karibuni atakufa, kwa hiyo akaongezea: “Ikiwa mimi, nijapokuwa Bwana na Mwalimu, niliosha miguu yenu, nyinyi pia mwapaswa kuoshana miguu. Kwa maana mimi niliweka kiolezo kwa ajili yenu, ili, kama vile nilivyowafanyia nyinyi, nyinyi mpaswe kufanya pia.”—Yohana 13:5-17.
Miongo kadhaa baadaye Petro aliwahimiza Wakristo wamwige Yesu, si kwa kufuata desturi ya kuosha miguu, bali kwa kuwatumikia wengine kwa unyenyekevu badala ya ‘kupiga ubwana.’ Petro pia alitambua kwamba kielelezo cha Yesu kilithibitisha kwamba “Mungu hupinga wenye kiburi, lakini huwapa wanyenyekevu fadhili isiyostahiliwa.” Hilo ni somo lililoje kuhusu Muumba! (1 Petro 5:1-5; Zaburi 18:35) Lakini, Petro alijifunza hata mengi zaidi.
Baada ya mlo huo wa mwisho, Yudasi Iskariote, ambaye alikuwa mtume lakini akawa mwizi, aliongoza kikosi cha watu waliojihami wamkamate Yesu. Walipokuwa wakimkamata, Petro alichukua hatua. Alichomoa upanga wake na kumjeruhi mtu mmoja aliyekuwa katika umati huo. Yesu akamrekebisha Petro: “Rudisha upanga wako mahali pao, kwa maana wale wote wauchukuao upanga wataangamia kwa upanga.” Kisha, Petro akitazama, Yesu alimgusa mtu yule, akamponya. (Mathayo 26:47-52; Luka 22:49-51) Kwa wazi, Yesu alitenda kwa kupatana na fundisho lake la “endeleeni kupenda maadui wenu” kwa kuiga Baba yake, ambaye “hufanya jua lake lichomoze juu ya watu waovu na wema na kufanya mvua inyeshe juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.”—Mathayo 5:44, 45.
Katika usiku huo wenye mikazo sana, Yesu alisikilizwa kijuu-juu tu na mahakama kuu ya Kiyahudi. Alishtakiwa kwa uwongo kwa kukufuru, akapelekwa kwa Gavana Mroma, kisha akapelekwa kuuawa isivyo haki. Wayahudi na Waroma walimdhihaki. Alitendwa kikatili sana na hatimaye kutundikwa mtini. Kutendwa vibaya huko kwingi kulitimiza unabii mbalimbali ulioandikwa karne nyingi awali. Hata askari waliokuwa wakimtazama Yesu akiwa kwenye mti wa mateso walikiri hivi: “Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu.”—Mathayo 26:57–27:54; Yohana 18:12–19:37.
Ni lazima matukio hayo yalifanya Petro na wengine waulize, ‘Kwa nini Kristo alilazimika kufa?’ Ni baadaye tu ndipo walipoelewa. Kwanza, matukio hayo yalitimiza unabii ulio katika Isaya sura ya 53, ambao ulionyesha kwamba Kristo angefanya wokovu upatikane si kwa Wayahudi tu bali pia kwa wanadamu wote. Petro aliandika hivi: “Yeye mwenyewe alichukua dhambi zetu katika mwili wake mwenyewe juu ya mti, ili tupate kuachana kabisa na dhambi na kuishi kuelekea uadilifu. Na ‘kwa mapigo yake mliponywa.’” (1 Petro 2:21-25) Petro alipata umaana wa kweli ambayo Yesu alikuwa ametaja: ‘Mwana wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake kuwa fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi.’ (Mathayo 20:28) Ndiyo, ilikuwa lazima Yesu aache haki yake ya kuishi akiwa mwanadamu mkamilifu ili awakomboe wanadamu kutokana na dhambi ambayo walirithi kutoka kwa Adamu. Hilo ni fundisho la msingi la Biblia—fidia.
Fidia inahusisha nini? Unaweza kufikiria jambo hilo kwa njia hii: Tuseme una kompyuta lakini mojawapo ya faili zake imevurugwa na kasoro fulani ambayo mtu mwingine alitia katika programu hiyo iliyokuwa kamilifu. Hilo latoa mfano wa athari ya kitendo cha Adamu alipokosa kumtii Mungu kimakusudi, au kutenda dhambi. Ebu tuendelee na ule mfano. Nakala zozote utakazofanyiza na ile faili yenye kasoro ya kompyuta zitaathiriwa. Lakini, hiyo haimaanishi kwamba hakuna namna ya kurekebisha hali. Kwa programu ya kipekee, unaweza kugundua na kuondoa ile kasoro yenye kuvuruga kwenye faili zako na kompyuta yako. Kwa kulinganisha, wanadamu walipokea kasoro, dhambi, kutoka kwa Adamu na Hawa, nasi twahitaji msaada wa nje ili kuiondoa. (Waroma 5:12) Kulingana na Biblia, Mungu aliandaa utakaso huo kupitia kifo cha Yesu. Ni uandalizi wenye upendo ambao tunaweza kunufaika nao.—1 Wakorintho 15:22.
Kuthamini kile alichofanya Yesu kulimsukuma Petro “kuishi wakati wake uliobaki katika mwili, si tena kwa ajili ya tamaa za wanadamu, bali kwa ajili ya mapenzi ya Mungu.” Kwa Petro na kwetu sisi, hiyo yamaanisha kuepuka tabia zenye kufisidi na mitindo-maisha isiyo ya adili. Wengine wanaweza kujaribu kutaabisha mtu anayejaribu kufanya “mapenzi ya Mungu.” Hata hivyo, yeye atapata kwamba maisha yake ni yenye kuthawabisha zaidi, na yenye umaana zaidi. (1 Petro 4:1-3, 7-10, 15, 16) Ndivyo ilivyokuwa na Petro, na inaweza kuwa hivyo kwetu ‘tukabidhipo nafsi zetu, au uhai wetu, kwa Muumba mwaminifu tunapotenda mema.’—1 Petro 4:19.
Mwanafunzi Aliyetambua Upendo
Mtume Yohana alikuwa mwanafunzi mwingine ambaye alishirikiana kwa ukaribu na Yesu na ambaye basi, aweza kutusaidia kumwelewa Muumba vizuri zaidi. Yohana aliandika Gospeli moja na pia barua tatu (Yohana ya 1, ya 2 na ya 3). Katika mojawapo ya barua hizo, yeye alitufahamisha hivi: “Twajua kwamba Mwana wa Mungu amekuja, na yeye ametupa sisi uwezo wa akili ili tupate ujuzi juu ya aliye wa kweli [Muumba]. Na sisi tumo katika muungano na aliye wa kweli, kwa njia ya Mwana wake Yesu Kristo. Huyu ndiye Mungu wa kweli na uhai udumuo milele.”—1 Yohana 5:20.
Yohana alipata ujuzi wa yule “aliye wa kweli” kwa kutumia “uwezo wa akili.” Yohana alitambua nini kuhusu sifa za Muumba? “Mungu ni upendo,” Yohana akaandika, “na yeye ambaye hukaa katika upendo hukaa katika muungano na Mungu.” Kwa nini Yohana alikuwa na uhakika juu ya jambo hilo? “Upendo uko hivi, si kwamba sisi tumempenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda akamtuma Mwana wake” atoe dhabihu ya fidia kwa ajili yetu. (1 Yohana 4:10, 16) Kama Petro, Yohana pia aliguswa na upendo ambao Mungu alionyesha kwa kumtuma Mwana wake afe kwa niaba yetu.
Kwa kuwa Yohana alikuwa karibu sana naye, angeweza kufahamu hisia za Yesu. Tukio moja katika Bethania, karibu na Yerusalemu, lilivutia sana Yohana. Baada ya Yesu kupokea ripoti ya kwamba rafikiye Lazaro alikuwa mgonjwa mahututi, alisafiri kwenda Bethania. Yeye na mitume walipofika, Lazaro alikuwa amekufa kwa angalau siku nne. Yohana alijua kwamba Muumba, aliye Chanzo cha uhai wa kibinadamu, alikuwa akimpa Yesu nguvu. Basi, je, Yesu angeweza kumfufua Lazaro? (Luka 7:11-17; 8:41, 42, 49-56) Yesu alimwambia dada ya Lazaro aitwaye Martha: “Ndugu yako atainuka.”—Yohana 11:1-23.
Kisha Yohana akamwona dada mwingine wa Lazaro, Maria, akija kumlaki Yesu. Yesu aliitikiaje? Yeye “akapiga kite katika roho na kuwa mwenye kutaabika.” Ili kufafanua itikio la Yesu, Yohana alitumia neno la Kigiriki (lililotafsiriwa ‘kupiga kite’ katika Kiswahili) ambalo lilimaanisha hisia za ndani zitokazo moyoni bila kukusudia. Yohana aliona kwamba Yesu ‘alikuwa akitaabika,’ au alikuwa na hisia nyingi za ndani, huzuni nyingi. Yesu alijali na hakujitenga. “Akatokwa na machozi.” (Yohana 11:30-37) Kwa wazi, Yesu alikuwa na hisia nyororo za ndani, jambo ambalo lilimsaidia Yohana afahamu hisia za Muumba, nalo lapasa kutusaidia sisi vilevile.
Yohana alijua kwamba hisia za Yesu zilifuatana na matendo mazuri kwa sababu alimsikia Yesu akipaaza sauti akisema: “Lazaro, njoo huku nje!” Na ikafanyika hivyo. Lazaro akapata uhai akatoka kaburini. Ni lazima dada zake na watazamaji wengine walipata shangwe iliyoje! Kisha wengi wakawa na imani kwa Yesu. Maadui wake hawangeweza kukana kwamba alikuwa amefanya ufufuo, lakini habari hiyo ilipoenea, wao “wakafanya shauri kumuua Lazaro” na Yesu pia.—Yohana 11:43; 12:9-11.
Biblia inafafanua Yesu kuwa ‘mwakilisho sawasawa wa utu wa Muumba mwenyewe.’ (Waebrania 1:3) Basi, huduma ya Yesu iliandaa uthibitisho wa kutosha wa tamaa yake kubwa na ya Baba yake ya kuondoa madhara ya ugonjwa na kifo. Na hiyo inahusu mengi kuliko idadi ndogo tu ya ufufuo mbalimbali uliorekodiwa katika Biblia. Kwa hakika, Yohana alikuwapo na kusikia Yesu akisema: “Saa inakuja ambayo katika hiyo wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho watasikia sauti [ya Mwana] na kutoka.” (Yohana 5:28, 29) Ona kwamba badala ya neno la kawaida la kaburi, hapo Yohana alitumia neno lililotafsiriwa “makaburi ya ukumbusho.” Kwa nini?
Kumbukumbu ya Mungu yahusika. Kwa hakika Muumba wa ulimwengu huu mkubwa aweza kukumbuka kila kijambo kidogo cha kila mmoja wa wapendwa wetu waliokufa, kutia ndani tabia zilizorithiwa na alizositawisha. (Linganisha Isaya 40:26.) Na si kwamba aweza tu kukumbuka. Wote wawili yeye na Mwana wake wanataka kukumbuka. Kuhusu tarajio tukufu la ufufuo, Ayubu mwaminifu aliuliza Mungu hivi: “Mtu akifa, je! atakuwa hai tena? . . . Wewe [Yehova] ungeita, nami ningekujibu; ungekuwa na tamaa ya kazi ya mikono yako.” (Ayubu 14:14, 15, italiki ni zetu; Marko 1:40-42) Tuna Muumba mzuri ajabu kama nini, astahiliye ibada yetu!
Yesu Aliyefufuliwa—Ufunguo wa Maisha Yenye Umaana
Mwanafunzi mpendwa Yohana alimtazama Yesu kwa makini hadi kifo Chake. Isitoshe, Yohana alirekodi ufufuo mkubwa zaidi uliowahi kutokea, tukio ambalo linaweka msingi thabiti wa kuwa na uhai wa milele na wenye umaana.
Maadui wa Yesu walimfanya auawe, akiwa amepigiliwa misumari kwenye mti kama mhalifu tu. Watazamaji—kutia ndani viongozi wa kidini—walimdhihaki alipokuwa akiteseka kwa saa kadhaa. Ajapokuwa na maumivu makali kwenye mti, Yesu alimwona mama yake mwenyewe na kumwambia mamake hivi kumhusu Yohana: “Mwanamke, ona! Mwana wako!” Kufikia wakati huo ni lazima Maria alikuwa mjane, na wale watoto wake wengine bado hawakuwa wanafunzi.e Kwa hiyo, Yesu alikabidhi utunzi wa mamake aliyekuwa akizeeka kwa mwanafunzi Yohana. Jambo hilo pia lilionyesha kufikiri kwa Muumba, ambaye alitia moyo kuwatunza wajane na mayatima.—Yohana 7:5; 19:12-30; Marko 15:16-39; Yakobo 1:27.
Lakini alipokufa, Yesu angetekelezaje fungu lake, akiwa “mbegu” ambaye kupitia kwake ‘mataifa yote yangejibarikia’? (Mwanzo 22:18) Kwa kifo chake, katika alasiri hiyo ya Aprili mnamo 33 W.K., Yesu alitoa uhai wake kuwa msingi wa fidia. Baba yake mwenye kufahamu aliyokuwa akipitia ni lazima alihisi uchungu kwa maumivu makali ya Mwana wake asiye na hatia. Lakini kwa njia hiyo, uandalizi ulifanywa wa kulipa thamani ya fidia iliyohitajiwa ili kuwaondolea wanadamu dhambi na kifo. (Yohana 3:16; 1 Yohana 1:7) Basi msingi ulikuwa umewekwa kwa ajili ya tukio tukufu.
Kwa sababu Yesu Kristo anatimiza fungu kuu katika kutimizwa kwa makusudi ya Mungu, ilikuwa lazima arudie uhai. Ikatokea hivyo, Yohana akashuhudia. Mapema katika siku ya tatu baada ya kifo na kuzikwa kwa Yesu, baadhi ya wanafunzi walienda kwenye kaburi. Lilikuwa tupu. Walishangaa hadi Yesu alipowatokea kadhaa kati yao. Maria Magdalena akaripoti, “Nimemwona Bwana!” Wanafunzi hawakukubali ushahidi wake. Baadaye wanafunzi walikusanyika katika chumba kilichokuwa kimefungwa na Yesu akawatokea tena, hata akazungumza nao. Kwa siku chache, zaidi ya wanaume na wanawake 500 wakajionea ya kwamba kwa kweli Yesu alikuwa hai. Watu wa wakati huo ambao huenda walikuwa wenye kutilia shaka wangeweza kuwahoji mashahidi hao wenye kuaminika na kuthibitisha ushuhuda wao. Wakristo waliweza kuwa na uhakika wa kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa na alikuwa hai akiwa kiumbe wa roho kama Muumba. Uthibitisho wa jambo hilo ulikuwa mwingi na wenye kutegemeka hivi kwamba wengi walikabili kifo badala ya kukana kufufuliwa kwa Yesu.—Yohana 20:1-29; Luka 24:46-48; 1 Wakorintho 15:3-8.f
Mtume Yohana pia alinyanyaswa kwa kutoa ushuhuda kuhusu ufufuo wa Yesu. (Ufunuo 1:9) Lakini alipokuwa uhamishoni kwa sababu ya adhabu, alipokea zawadi isiyo ya kawaida. Yesu alimpa mfululizo wa njozi ambazo zinatuonyesha Muumba kwa udhahiri zaidi na kufunua mambo ambayo yatakuja wakati ujao. Utapata hayo katika kitabu cha Ufunuo, ambacho kinatumia ishara nyingi. Katika kitabu hicho, Yesu Kristo anaonyeshwa akiwa Mfalme mshindi ambaye karibuni atamaliza ushindi wake dhidi ya maadui wake. Maadui hao wanatia ndani kifo (adui wetu sote) na kiumbe wa roho aliyefisidika aitwaye Shetani.—Ufunuo 6:1, 2; 12:7-9; 19:19–20:3, 13, 14.
Karibu na mwisho wa ujumbe wa ufunuo, Yohana alikuwa na njozi ya wakati ambapo dunia itakuwa paradiso. Sauti moja ikataja hali ambazo zitaenea wakati huo: “Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao [wanadamu]. Naye atafuta kabisa kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala ombolezo wala kupaaza kilio wala umivu halitakuwapo tena kamwe. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:3, 4) Katika utimizo wa kusudi la Mungu, ahadi ambayo Mungu alimpa Abrahamu itatimizwa.—Mwanzo 12:3; 18:18.
Wakati huo uhai utakuwa “uhai ulio halisi,” unaolingana na yale yaliyokuwa mbele ya Adamu alipoumbwa. (1 Timotheo 6:19) Mwanadamu hatatafuta-tafuta tena Muumba wao na kuelewa uhusiano wao naye. Lakini, huenda ukauliza, ‘Hayo yatatokea lini? Na kwa nini Muumba mwenye kujali anaruhusu uovu na kuteseka kuwepo hadi wakati wetu?’ Ebu tufuatie kuzungumzia maswali hayo.
[Maelezo ya Chini]
a Mathayo, Marko, na Yohana walikuwa mashahidi waliojionea. Luka alichunguza kitaaluma hati na ushuhuda wa watu waliojionea mambo hayo. Hizo Gospeli zadhihirisha ishara ya kwamba rekodi hizo ni sahihi, zenye kufuatia haki, na zenye kutumainika.—Ona kichapo Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, ukurasa wa 16-17, kilichochapishwa na Watchtower Bible and Tract Society of New York, Inc.
b Qurani yasema: “Jina lake ni Masih, Isa [Kristo Yesu], mwana wa Maryamu, mwenye hishima katika dunia na Akhera.” (Sura 3:45) Akiwa binadamu, Yesu alikuwa mwana wa Maria. Lakini ni baba yupi aliyemzaa? Qurani yasema: “Hali ya Isa [Yesu] kwa Mwenyezi Mungu ni kama hali ya Adam.” (Sura 3:59) Maandiko Matakatifu yasema juu ya Adamu kuwa “mwana wa Mungu.” (Luka 3:23, 38) Wala Adamu wala Yesu hakuwa na baba wa kibinadamu; hakuna mmoja wao aliyezaliwa kutokana na ngono iliyofanywa na mwanamke fulani. Kwa hiyo, Adamu alikuwa mwana wa Mungu, na ndivyo ilivyo na Yesu.
c Mtazamo wa Yesu unalingana na wa Yehova, kama unavyoonyesha katika Zaburi ya 103 na Isaya 1:18-20.
d Twaweza kusoma unabii huo katika Mathayo sura ya 24, Marko sura ya 13, na Luka sura ya 21.
e Angalau wawili kati yao baadaye wakawa wanafunzi na wakaandika barua za kitia-moyo zinazopatikana katika Biblia, Yakobo na Yuda.
f Ofisa mmoja Mroma mwenye cheo alisikia ushuhuda wa Petro wa mambo aliyojionea: “Nyinyi mwaijua habari iliyoongewa kotekote katika Yudea . . . Mungu alimfufua Huyu katika siku ya tatu na kumruhusu awe dhahiri . . . Alituagiza sisi tuwahubiri watu na kutoa ushahidi kamili kwamba Huyu ndiye aliyeagizwa na Mungu kuwa hakimu wa walio hai na wafu.”—Matendo 2:32; 3:15; 10:34-42.
[Sanduku katika ukurasa wa 150]
Huenda ukafurahia kulinganisha masimulizi yanayolingana ya jinsi Yesu alivyomponya mama-mkwe wa Petro. (Mathayo 8:14-17; Marko 1:29-31; Luka 4:38, 39) Tabibu Luka alitia ndani jambo la kitiba la kwamba huyo mama-mkwe alikuwa na “homa kali.” Ni nini kilichomwezesha Yesu amponye na kuponya wengine? Luka alikiri kwamba “nguvu ya Yehova ilikuwa hapo ili [Yesu] afanye uponyaji.”—Luka 5:17; 6:19; 9:43.
[Sanduku katika ukurasa wa 152]
Mahubiri Makuu Zaidi
Kiongozi wa Kihindu Mohandas Gandhi alinukuliwa akisema kwamba kwa kufuata mafundisho hayo, “tutakuwa tumetatua matatizo . . . ya ulimwengu wote.” Mtaalamu mashuhuri wa asili ya binadamu Ashley Montagu aliandika kwamba ugunduzi wa kisasa kuhusu umuhimu wa upendo kisaikolojia ni “uthibitisho” tu wa mahubiri hayo.
Watu hao walikuwa wakirejezea Mahubiri ya Mlimani ya Yesu. Gandhi alisema pia kwamba “mafundisho ya Mahubiri hayo yalikusudiwa kila mmoja wetu.” Hivi majuzi Profesa Hans Dieter Betz alisema hivi: “Mavutano ya yale Mahubiri ya Mlimani kwa ujumla yapita mipaka ya Dini ya Kiyahudi na Ukristo, au hata utamaduni wa Magharibi.” Aliongezea kusema ya kwamba mahubiri hayo “yana uvutio wa kipekee ulimwenguni pote.”
Mbona usisome hotuba hii fupi lakini yenye kuvutia? Utaipata katika Mathayo sura ya 5 hadi 7 na katika Luka 6:20-49. Hapa pana mambo makuu ambayo tunapata katika mahubiri hayo makuu zaidi:
Jinsi ya kuwa mwenye furaha—Mathayo 5:3-12; Luka 6:20-23.
Jinsi ya kudumisha kujistahi—Mathayo 5:14-16, 37; 6:2-4, 16-18; Luka 6:43-45.
Jinsi ya kuboresha uhusiano na wengine—Mathayo 5:22-26, 38-48; 7:1-5, 12; Luka 6:27-38, 41, 42.
Jinsi ya kupunguza matatizo ya familia—Mathayo 5:27-32.
Jinsi ya kukabiliana na mahangaiko—Mathayo 6:25-34.
Jinsi ya kutambua ubandia wa dini—Mathayo 6:5-8, 16-18; 7:15-23.
Jinsi ya kupata umaana wa maisha—Mathayo 6:9-13, 19-24, 33; 7:7-11, 13, 14, 24-27; Luka 6:46-49.
[Sanduku katika ukurasa wa 159]
Mtu wa Matendo
Yesu Kristo hakuwa mtu ajitengaye asiyetenda. Yeye alikuwa mtu mwenye kauli moja na mwenye matendo. Alisafiri “vijijini katika mzunguko, akifundisha,” akiwasaidia watu ambao walikuwa ‘wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.’ (Marko 6:6; Mathayo 9:36; Luka 8:1) Tofauti na viongozi wengi wa kidini wa sasa walio matajiri, Yesu hakujirundikia mali, hakuwa na “mahali popote pa kulaza kichwa chake.”—Mathayo 8:20.
Ingawa Yesu alikazia jitihada zake kwenye uponyaji na ulishaji wa kiroho, hakupuuza mahitaji ya kimwili ya watu. Aliwaponya wagonjwa, walemavu, na waliopagawa na roho waovu. (Marko 1:32-34) Mara mbili alilisha maelfu ya wasikilizaji wenye hamu kwa sababu aliwahurumia. (Marko 6:35-44; 8:1-8) Alifanya miujiza kwa sababu aliwahangaikia watu.—Marko 1:40-42.
Yesu alitenda kwa kauli moja alipowaondosha wafanya-biashara wenye pupa kutoka hekaluni. Wale waliomtazama walikumbuka maneno ya mtunga-zaburi: “Bidii kwa ajili ya nyumba yako itanila mimi kabisa.” (Yohana 2:14-17) Aliwashutumu waziwazi viongozi wa kidini wenye unafiki. (Mathayo 23:1-39) Wala hakushindwa na mkazo wa watu maarufu kisiasa.—Mathayo 26:59-64; Yohana 18:33-37.
Utasisimuka sana kusoma huduma yenye nguvu ya Yesu. Wengi ambao huisoma kwa mara ya kwanza huanza na masimulizi mafupi lakini yenye kusisimua ya Marko juu ya mtu huyo wa matendo.
[Sanduku katika ukurasa wa 164]
Yesu Aliwachochea Watende
Katika kitabu cha Matendo, tunaweza kupata rekodi ya kihistoria ya jinsi Petro, Yohana, na wengine walivyotoa ushahidi kuhusu ufufuo wa Yesu. Sehemu kubwa ya kitabu hicho inasimulia matukio yanayohusu mwanafunzi mmoja wa sheria mwerevu aliyeitwa Sauli, au Paulo, ambaye aliupinga Ukristo kijeuri sana. Yesu aliyefufuliwa alimtokea. (Matendo 9:1-16) Akiwa na uthibitisho usioweza kukanushwa kwamba Yesu alikuwa hai mbinguni, baadaye Paulo alitoa ushahidi kwa bidii kuhusu jambo hilo kwa Wayahudi na kwa wasio-Wayahudi, kutia ndani wanafalsafa na watawala. Inavutia kusoma kile alichowaambia watu mashuhuri na wenye elimu kama hao.—Matendo 17:1-3, 16-34; 26:1-29.
Katika kipindi cha miongo kadhaa, Paulo aliandika vitabu vingi vya lile liitwalo Agano Jipya, au Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Biblia nyingi zina orodha ya yaliyomo, au orodha ya vitabu. Paulo aliandika vitabu 14 kati ya hivyo, tokea Waroma hadi Waebrania. Vitabu hivyo viliandaa kweli za ndani na mwongozo wenye hekima kwa Wakristo wa wakati huo. Na vitabu hivyo ni muhimu hata zaidi kwetu, sisi ambao hatukupata kuwaona moja kwa moja mitume na mashahidi wengine wa mafundisho, matendo, na ufufuo wa Yesu. Utapata kwamba maandiko ya Paulo yanaweza kukusaidia katika maisha yako ya familia, katika shughuli zako na wafanyakazi wenzako na majirani, na katika kuongoza maisha yako ili yawe na maana halisi na yenye kukuletea uradhi.
-