Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kutoa Ushahidi kwa Watu wa Lugha na Dini Zote
    Huduma ya Ufalme—1998 | Februari
    • Kutoa Ushahidi kwa Watu wa Dini Zisizo za Kikristo

      11 Kuwa na ujuzi fulani wa habari za dini ya mtu huyo hutusaidia tutoe ushahidi wenye matokeo kuhusu Ufalme wa Mungu. Kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu hutupa ufahamu wenye kina juu ya dini kubwa za ulimwengu ili tuweze kuelewa itikadi za watu vizuri kabisa ili tuwasaidie wapate ujuzi kuhusu ile kweli.

      12 Sanduku kwenye ukurasa wa mwisho wa nyongeza hii latoa orodha ya sasa ya vichapo ambavyo tengenezo la Yehova limeandaa kwa matumizi ya kutoa ushahidi kwa watu wasio Wakristo. Kwa kusoma vichapo hivi, twaelewa jinsi ya kufikia watu tukiwa na habari njema. Chombo chenye msaada kisichopaswa kusahauliwa ni kitabu Kutoa Sababu. Ukurasa wa 21-24 katika kitabu hicho huandaa madokezo yenye kutumika ya jinsi ya kujibu Wabuddha, Wahindu, Wayahudi, na Waislamu.

      13 Kuwa Mwangalifu Kuhusu Usemayo: Twapaswa kuwa waangalifu kutohukumu kimbele watu wa dini fulani kwa kuamua kwamba itikadi zao za kibinafsi zafanana tu na zile za wengine wa imani hiyo. Badala yake, jitahidi kuelewa jinsi mtu unayeongea naye afikirivyo. (Mdo. 10:24-35) Alipokuwa Mwislamu, Salimoon alilelewa akiamini kwamba Kurani ni neno la Mungu. Lakini hakuweza kukubali kabisa fundisho la Uislamu kwamba Mungu mwenye rehema yote angetesa watu katika helo yenye kuwaka moto. Siku moja, Mashahidi wa Yehova walimwalika kwenye mkutano. Akitambua kweli mara moja, sasa yeye atumikia kwa furaha akiwa mzee katika kutaniko la Kikristo.

      14 Tunapotoa ushahidi kwa wasio na itikadi za Kikristo, twahitaji kuwa waangalifu kwamba mfikio wetu hauondoi fursa yetu ya kuzungumza pamoja nao juu ya habari njema. (Mdo. 24:16) Wafuasi wa dini fulani ni wanyetivu sana kuhusu majaribio yoyote ya kuwageuza kutoka imani yao. Kwa hiyo uwe chonjo kutafuta mambo ya kujengea msingi wenye masikilizano ili uwavutie kwenye kweli yote ya Neno la Mungu. Watu wenye mfano wa kondoo wataitikia mfikio wenye fadhili na utoaji ulio wazi wa ile kweli.

      15 Ni jambo la maana kufikiria pia uchaguzi wa maneno yetu, tusije tukaondoa watu isivyo lazima kwenye ujumbe wetu. Kwa mfano, ukijitambulisha kwa mwenye nyumba mara moja kuwa Mkristo, msikilizaji wako aweza kukushirikisha mara hiyo na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo, ambalo laweza kuweka kizuizi. Pia ingefaa kurejezea Biblia kuwa “Maandiko” au “maandishi matakatifu.”—Mt. 21:42; 2 Tim. 3:15.

      16 Ukikutana na mtu wa dini isiyo ya Kikristo na wahisi hauko tayari kutoa ushahidi hapohapo, tumia fursa hiyo kufahamiana tu, mwachie trakti, na mjuane majina. Kisha urudi baada ya siku moja au mbili baada ya kujitayarisha ifaavyo kutoa ushahidi.—1 Tim. 4:16; 2 Tim. 3:17.

      17 Kuwatolea Wabuddha Ushahidi: (Ona sura ya 6 katika kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu.) Itikadi za Kibuddha za mwamini mmoja zatofautiana sana na zile za mwamini mwingine. Badala ya kutetea kuwapo kwa Muumba mwenye utu, Ubuddha humwona mwanamume Mhindi Buddha Gautama, wa karne ya sita K.W.K., kuwa mfano bora wa kidini. Mara ya kwanza Gautama alipoona mwanamume mgonjwa, mwanamume mzee, na mwanamume aliyekufa, alipatwa na maumivu makali kuhusu maana ya uhai. ‘Je, wanadamu walizaliwa wateseke, wazeeke, na kufa tu?’ alijiuliza. Bila shaka, twaweza kujibu maswali hayo kwa ajili ya Wabuddha wenye moyo mweupe ambao wanataka kujua majibu.

      18 Unaposema na Wabuddha, tumia tu ujumbe ulio chanya na kweli zilizo wazi zipatikanazo katika kitabu kitakatifu kilicho kikubwa zaidi ya vyote, Biblia. Kama vile watu wengine walio wengi, Wabuddha wanapendezwa sana na amani, adili, na maisha ya familia, na mara nyingi wao hukaribisha mazungumzo juu ya mambo hayo. Hilo laweza kuongoza katika kukazia kwako Ufalme kuwa utatuzi halisi wa matatizo ya wanadamu.

      19 Katika sehemu fulani za mji mkuu za Afrika Mashariki, kumekuwa na Wachina kadhaa ambao huamini Ubuddha na falsafa nyinginezo za Kimashariki. Wengi wanafanya kazi katika miradi tofauti-tofauti. Kwa mfano, dada mmoja katika Montana, Marekani, alipomwona mwanamume Mchina katika duka la kuuzia mboga, alimpa trakti katika lugha yake na kumtolea funzo la Biblia. Yeye alisema: “Wamaanisha Biblia Takatifu? Nimekuwa nikiitafuta maishani mwangu mwote!” Alianza kujifunza juma hilo na kuanza kuhudhuria mikutano yote. Vivyo hivyo, wahubiri fulani katika eneo letu wameweza kuanzisha mafunzo ya Biblia na Wachina fulani.

      20 Kwa muda wa zaidi ya mwongo moja, dada painia katika Nevada amekuwa akifundisha wanafunzi Wachina kweli. Alipokuwa akihubiri jengo moja lililokuwa na vyumba vinane vilivyokaliwa na wanafunzi hawa, alisali kwa Yehova amsaidie kuanzisha funzo katika kila chumba. Katika majuma mawili alikuwa akijifunza na angalau mwanafunzi mmoja katika kila chumba. Mfikio ufanyao kazi vizuri kwake ni kusema kwamba amepata miongoni mwa wanafunzi hao hangaiko moja linalofanana—wote wanataka amani na furaha. Kisha yeye huuliza kama hilo ni hangaiko lao pia. Sikuzote wao hukubali. Yeye huelekeza uangalifu wao kwenye broshua Lasting Peace and Happiness—How to Find Them, ambayo imekusudiwa Wachina. Baada ya kujifunza masomo matano tu, mwanafunzi mmoja alimwambia amekuwa akitafuta kweli kwa muda mrefu na sasa ameipata.

      21 Kutoa Ushahidi kwa Wahindu: (Ona sura ya 5 katika kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu.) Uhindu hauna kanuni za imani hususa. Falsafa yake ni tata sana. Wahindu wana dhana ya utatu ya mungu wao mkubwa Brahman (Brahma aliye Muumba, Vishnu aliye Mhifadhi, na Siva aliye Mwangamizi). Itikadi ya nafsi isiyoweza kufa ni muhimu kwa fundisho lao la kuzaliwa upya katika umbo jingine, ambalo huelekea kuwapa Wahindu maoni ya maisha kuwa ni majaliwa tu. (Ona kitabu Kutoa Sababu, ukurasa wa 154-158, na Mnara wa Mlinzi, Mei 15, 1997, ukurasa wa 3-8.) Uhindu hufunza uvumilivu, kwamba dini zote zaongoza kwenye kweli ileile.

      22 Mfikio upaswao kuchukuliwa ili kutolea Mhindu ushahidi ni kueleza tumaini letu linalotegemea Biblia la kuishi milele tukiwa binadamu wakamilifu duniani na vilevile majibu yenye kuridhisha ambayo Biblia hutoa kwa maswali ya maana wanayokabili wanadamu wote.

      23 Kutoa Ushahidi kwa Wayahudi: (Ona sura ya 9 katika kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu.) Tofauti na dini zile nyingine zisizo za Kikristo, Dini ya Kiyahudi imetia mizizi katika historia, si mithiolojia. Kupitia Maandiko ya Kiebrania yaliyopulizwa, kiungo muhimu chatolewa katika jitihada ya wanadamu ya kumtafuta Mungu wa kweli. Lakini, tofauti na Neno la Mungu, fundisho la msingi la Dini ya Kiyahudi ya kisasa ni itikadi katika nafsi ya kibinadamu isiyoweza kufa. Msingi wa masikilizano waweza kuanzishwa kwa kuthibitisha kwamba twaabudu Mungu wa Abrahamu na kwa kukubali kwamba sisi hukabili magumu yaleyale katika ulimwengu wa leo.

      24 Ukikutana na Myahudi asiye na imani katika Mungu, kumwuliza kama sikuzote amehisi hivyo huenda kukakusaidia ufahamu ni nini kitakachomvutia zaidi. Kwa mfano, huenda ikawa hajapata kusikia kamwe maelezo yenye kuridhisha juu ya sababu imfanyayo Mungu aruhusu kuteseka. Wayahudi wenye moyo mweupe wanaweza kutiwa moyo kuchunguza upya utambulisho wa Yesu akiwa Mesiya, si kupitia kuwakilishwa kwake vibaya na Jumuiya ya Wakristo, bali katika njia ambayo waandikaji Wayahudi wa Maandiko ya Kigiriki wanavyomweleza.

      25 Kutoa Ushahidi kwa Waislamu: (Ona Sura ya 12 katika kitabu Jitihada ya Ainabinadamu ya Kutafuta Mungu.) Waislamu, ni wafuasi wa Uislamu (au, Umuhammad), ambao hutia ndani itikadi katika Allah kuwa mungu wao wa pekee na katika Muhammad (570-632 W.K.) kuwa nabii wake wa mwisho na wa maana zaidi. Kwa sababu hawaamini kwamba Mungu alikuwa na mwana, Waislamu humtambua Yesu Kristo kuwa nabii mdogo zaidi wa Mungu, lakini si zaidi ya hilo. Kurani, ambacho ni kitabu chenye miaka isiyozidi 1,400, hutaja Maandiko ya Kiebrania na pia ya Kigiriki. Ufanani mkubwa upo kati ya Uislamu na Ukatoliki. Dini zote mbili hufundisha hali ya kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu, hali ya mateso ya muda tu, na kuwako kwa helo yenye kuwaka moto.

      26 Masikilizano yaliyo wazi katika itikadi yetu ni kwamba kuna Mungu mmoja tu wa kweli na kwamba Biblia ilipuliziwa naye. Msomaji mwangalifu wa Kurani ameona marejezeo kwenye Torah, Zaburi, na Gospeli kuwa Neno la Mungu na amesoma kwamba vitabu hivyo vyapasa kutambuliwa kuwa hivyo na kutiiwa. Kwa sababu hiyo, waweza kujitoa kujifunza vitabu hivyo na mtu huyo.

      27 Utoaji huu waweza kufanya kazi kwa mtu anayejitambulisha kuwa Mwislamu: “Sijaongea na Waislamu wengi, lakini nimesoma jambo fulani juu ya mafundisho machache ya dini yenu katika kitabu hiki chenye kubebeka kwa urahisi. [Fungua ukurasa wa 24 katika kitabu Kutoa Sababu.] Kinasema nyinyi huamini kwamba Yesu alikuwa nabii lakini kwamba Muhammad alikuwa nabii wa mwisho na wa maana zaidi. Je, waamini pia kwamba Musa alikuwa nabii wa kweli? [Ruhusu itikio.] Je, naweza kukuonyesha jambo ambalo Musa alijifunza kutoka kwa Mungu kuhusu jina Lake la kibinafsi?” Kisha usome Kutoka 6:2, 3. Katika ziara ya kurudia, unaweza kuzungumzia kichwa kidogo “Mungu Mmoja, Dini Moja,” kwenye ukurasa wa 13 katika kijitabu Sasa Ndio Wakati wa Kumtii Mungu Kweli Kweli.

      28 Leo, watu wengi wanatenda kupatana na maneno ya Isaya 55:6, yasemayo: “Mtafuteni BWANA, maadamu anapatikana, Mwiteni, maadamu yu karibu.” Hayo yatia wote wenye moyo wa kufuatia haki, bila kujali lugha wanayosema au malezi yao ya kidini. Twaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atabariki jitihada zetu tujitahidipo kwenda na “[kufanya] wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.”—Mt. 28:19.

  • Kutoa Ushahidi kwa Watu wa Lugha na Dini Zote
    Huduma ya Ufalme—1998 | Februari
    • Fasihi Zikusudiwazo Watu Wasio Wakristo

      Wabuddha

      “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya” (Broshua)

      In Search of a Father (Kijitabu)

      Wachina

      Lasting Peace and Happiness—How to Find Them (Broshua)

      Wahindu

      From Kurukshetra to Armageddon—And Your Survival (Kijitabu)

      Our Problems—Who Will Help Us Solve Them? (Broshua)

      The Path of Divine Truth Leading to Liberation (Kijitabu)

      Victory Over Death—Is It Possible for You? (Kijitabu)

      Why Should We Worship God in Love and Truth? (Broshua)

      Wayahudi

      Je! Ulimwengu Usio na Vita Utakuwako Wakati Wowote? (Broshua)

      Mashahidi wa Yehova—Huamini Nini? (Trakti Na. 18)

      A Peaceful New World—Will It Come? (Trakti Na. 17)

      Waislamu

      Jinsi ya Kuipata Barabara ya Kwenda Kwenye Paradiso (Trakti)

      Sasa Ndio Wakati wa Kumtii Mungu Kweli Kweli (Kijitabu)

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki