Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kunyanyaswa kwa Ajili ya Uadilifu
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Oktoba 1
    • Kunyanyaswa kwa Ajili ya Uadilifu

      “Wenye furaha ni wale ambao wamenyanyaswa kwa ajili ya uadilifu.”—MATHAYO 5:10.

      1. Kwa nini Yesu alikuwa mbele ya Pontio Pilato, naye alisema nini?

      “KWA ajili ya hili mimi nimezaliwa, na kwa ajili ya hili nimekuja kuingia ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” (Yohana 18:37) Yesu alisema maneno hayo akiwa mbele ya Pontio Pilato, Gavana Mroma wa Yudea. Yeye hakuwa hapo kwa mwaliko wa Pilato au kwa sababu alikuwa ameamua kwenda hapo. Lakini, Yesu alijikuta hapo kwa sababu viongozi wa dini ya Kiyahudi walikuwa wamemshtaki kwa uwongo kuwa mkosaji aliyestahili kifo.—Yohana 18:29-31.

      2. Yesu alichukua hatua gani, na matokeo yakawaje?

      2 Yesu alijua vizuri sana kwamba Pilato alikuwa na mamlaka ya kumwachilia au kumuua. (Yohana 19:10) Lakini jambo hilo halikumzuia asizungumze na Pilato kwa ujasiri kuhusu Ufalme. Ingawa maisha ya Yesu yalikuwa hatarini, alitumia nafasi hiyo kumtolea ushahidi mtu aliyekuwa na mamlaka kubwa zaidi ya kiserikali katika eneo hilo. Ijapokuwa alitoa ushahidi huo, Yesu alihukumiwa na kuuawa. Aliuawa kifo chenye maumivu makali kwenye mti wa mateso kwa ajili ya imani yake.—Mathayo 27:24-26; Marko 15:15; Luka 23:24, 25; Yohana 19:13-16.

      Shahidi au Mfia-Imani?

      3. Neno “mfia-imani” lilimaanisha nini nyakati za Biblia, lakini linamaanisha nini leo?

      3 Leo watu wengi humwona mfia-imani kuwa mtu aliye na imani kali au msimamo mkali kuhusu dini. Mara nyingi watu walio tayari kufa kwa ajili ya imani yao, hasa imani ya kidini, hutuhumiwa kuwa magaidi au watu hatari katika jamii. Hata hivyo, nyakati za Biblia neno la Kigiriki (marʹtys) ambalo linatafsiriwa mfia-imani lilimaanisha “shahidi,” yaani, mtu ambaye hutoa ushuhuda, labda katika kesi ya mahakama, kuhusu yale anayoamini kuwa kweli. Hata hivyo, baadaye neno hilo lilitumiwa kumaanisha “mtu ambaye hutoa uhai wake kwa sababu ya kutoa ushahidi,” au hata kufa ili atoe ushahidi.

      4. Neno la Kigiriki marʹtys lilitumiwa hasa katika maana gani kumhusu Yesu?

      4 Kumhusu Yesu, neno la Kigiriki marʹtys lilitumiwa hasa kumaanisha mtu anayetoa ushahidi. Yesu alimwambia Pilato kwamba alikuja ‘kutoa ushahidi juu ya ile kweli.’ Watu waliitikia ushahidi wake kwa njia mbalimbali. Baadhi ya watu wa kawaida waliguswa moyo sana na mambo waliyosikia na kuona, na hivyo wakamwamini Yesu. (Yohana 2:23; 8:30) Watu kwa ujumla na hasa viongozi wa kidini waliitikia ujumbe kwa njia isiyofaa kwa kuupinga vikali. Yesu aliwaambia hivi jamaa zake wasioamini: “Ulimwengu hauna sababu ya kuwachukia nyinyi, lakini huo wanichukia mimi, kwa sababu natoa ushahidi kuhusu huo kwamba kazi zao ni mbovu.” (Yohana 7:7) Yesu alichukiwa na kuuawa na viongozi wa taifa kwa sababu ya kutoa ushahidi kuhusu kweli. Naam, alikuwa “shahidi mwaminifu na wa kweli (marʹtys).”—Ufunuo 3:14.

      “Mtakuwa Vitu vya Kuchukiwa”

      5. Mapema katika huduma yake, Yesu alisema nini kuhusu mnyanyaso?

      5 Yesu mwenyewe alinyanyaswa vikali naye aliwaonya wafuasi wake kwamba wangenyanyaswa pia. Mapema katika huduma yake, Yesu aliwaambia hivi wasikilizaji wake katika Mahubiri yake ya Mlimani: “Wenye furaha ni wale ambao wamenyanyaswa kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa ufalme wa mbingu ni wao. Wenye furaha ni nyinyi watu wawashutumupo na kuwanyanyasa nyinyi na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo ovu dhidi yenu kwa ajili yangu. Shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa katika mbingu.”—Mathayo 5:10-12.

      6. Yesu alitoa onyo gani alipowatuma wale mitume 12?

      6 Baadaye, alipowatuma mitume 12, Yesu aliwaambia hivi: “Jilindeni dhidi ya watu; kwa maana watawakabidhi nyinyi kwenye mahakama za mtaa, nao watawapiga nyinyi mijeledi katika masinagogi yao. Naam, mtaburutwa mbele ya magavana na wafalme kwa ajili yangu, kuwa ushahidi kwao na kwa mataifa.” Lakini wanafunzi wa Yesu hawangenyanyaswa tu na viongozi wa kidini. Yesu pia alisema: “Ndugu atakabidhi ndugu kwenye kifo, na baba mtoto wake, na watoto watainuka dhidi ya wazazi na kufanya wauawe. Nanyi mtakuwa vitu vya kuchukiwa na watu wote kwa sababu ya jina langu; lakini yeye ambaye amevumilia hadi mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mathayo 10:17, 18, 21, 22) Mambo yaliyowapata Wakristo wa karne ya kwanza yanathibitisha kwamba maneno hayo ni kweli.

      Habari Kuhusu Watu Waliovumilia kwa Uaminifu

      7. Ni nini kilichofanya Stefano afe kwa ajili ya imani?

      7 Muda mfupi baada ya Yesu kufa, Stefano ndiye aliyekuwa Mkristo wa kwanza kufa kwa sababu ya kutoa ushahidi kuhusu kweli. Alikuwa “mwenye kujaa wema na nguvu, [na] alikuwa akifanya mambo makubwa ya ajabu na ishara miongoni mwa watu.” Maadui wake wa kidini “hawakuweza kufaulu katika pambano dhidi ya hekima na roho aliyokuwa akisema kwayo.” (Matendo 6:8, 10) Kwa kujawa na wivu, walimburuta Stefano mbele ya Sanhedrini, mahakama kuu ya Kiyahudi ambapo alikabili watu waliomshtaki kwa uwongo na kuwatolea ushahidi wenye nguvu. Hata hivyo, mwishowe maadui wa Stefano walimuua shahidi huyo mwaminifu.—Matendo 7:59, 60.

      8. Wanafunzi waliokuwa Yerusalemu walitendaje waliponyanyaswa baada ya Stefano kuuawa?

      8 Baada ya Stefano kuuawa, “mnyanyaso mkubwa ulitokea dhidi ya kutaniko lililokuwa katika Yerusalemu; wote isipokuwa mitume walitawanywa kotekote katika mikoa ya Yudea na Samaria.” (Matendo 8:1) Je, mnyanyaso ulikomesha kazi ya Kikristo ya kutoa ushahidi? La, kwa kuwa tunaelezwa kwamba “wale waliokuwa wametawanywa walipita katika nchi wakitangaza habari njema ya lile neno.” (Matendo 8:4) Bila shaka, walihisi kama mtume Petro alivyohisi aliposema hivi awali: “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” (Matendo 5:29) Ijapokuwa walinyanyaswa, wanafunzi hao waaminifu na wenye ujasiri waliendelea na kazi ya kutoa ushahidi kuhusu kweli, hata ingawa walijua kwamba wangepatwa na magumu zaidi kwa kufanya hivyo.—Matendo 11:19-21.

      9. Wafuasi wa Yesu waliendelea kupatwa na mnyanyaso gani?

      9 Bila shaka, wanafunzi hao waliendelea kupatwa na magumu. Kwanza, tunaona kwamba Sauli, aliyeshuhudia na kuunga mkono wakati Stefano alipokuwa akipigwa mawe, alikuwa ‘bado anapumua tisho na uuaji-kimakusudi dhidi ya wanafunzi wa Bwana, alipomwendea kuhani wa cheo cha juu na kumwomba barua za kwenda kwenye masinagogi katika Damasko, ili apate kuwaleta hadi Yerusalemu wakiwa wamefungwa wowote ambao angewapata walio wa Ile Njia, wanaume na pia wanawake.’ (Matendo 9:1, 2) Kisha, yapata mwaka wa 44 W.K., “Herode mfalme alitumia mikono yake kutenda vibaya baadhi ya wale wa kutaniko. Alimmaliza Yakobo ndugu ya Yohana kwa upanga.”—Matendo 12:1, 2.

      10. Tunapata habari gani kuhusu mnyanyaso katika kitabu cha Matendo na Ufunuo?

      10 Sura zilizosalia za kitabu cha Matendo zina habari zisizoweza kusahaulika kuhusu majaribu, vifungo vya gerezani, na mnyanyaso uliowapata watu waaminifu kama vile Paulo, ambaye hapo awali alikuwa mnyanyasaji kabla ya kuwa mtume. Yaelekea mwaka wa 65 W.K. hivi, Maliki Mroma Nero, aliamuru mtume huyo auawe kwa ajili ya imani yake. (2 Wakorintho 11:23-27; 2 Timotheo 4:6-8) Mwishowe, katika kitabu cha Ufunuo kilichoandikwa karne ya kwanza ikikaribia kwisha, tunaona kwamba mtume Yohana aliyekuwa mzee alifungwa kwenye kisiwa cha kuadhibia wafungwa cha Patmosi “kwa ajili ya kusema juu ya Mungu na kutoa ushahidi kuhusu Yesu.” Kitabu cha Ufunuo pia kinamtaja “Antipasi, shahidi wangu, aliye mwaminifu, aliyeuawa” huko Pergamamu.—Ufunuo 1:9; 2:13.

      11. Maisha ya Wakristo wa mapema yalithibitishaje ukweli wa maneno ya Yesu kuhusu mnyanyaso?

      11 Minyanyaso hiyo yote ilithibitisha ukweli wa maneno haya ambayo Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Ikiwa wameninyanyasa mimi, watawanyanyasa nyinyi pia.” (Yohana 15:20) Wakristo waaminifu wa mapema walikuwa tayari kukabiliana na jaribu kuu zaidi ambalo ni kuuawa—kwa kuteswa, kutupiwa wanyama, au kwa njia nyinginezo—ili kufanya kazi hii ambayo Bwana Yesu Kristo aliwapa: “Mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu na pia katika Yudea yote na Samaria na hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.”—Matendo 1:8.

      12. Kwa nini kunyanyaswa kwa Wakristo si jambo lililotokea wakati wa zamani tu?

      12 Mtu yeyote akifikiri kwamba wafuasi wa Yesu walinyanyaswa kikatili wakati wa zamani tu, atakuwa amekosea sana. Paulo, ambaye kama tulivyoona alivumilia magumu, aliandika hivi: “Wote wale wanaotamani kuishi kwa ujitoaji-kimungu katika ushirika na Kristo Yesu watanyanyaswa pia.” (2 Timotheo 3:12) Petro alisema hivi kuhusu mnyanyaso: “Kwa kweli, kwenye mwendo huu mliitwa, kwa sababu hata Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia kigezo ili nyinyi mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Tangu wakati huo hadi ‘siku hizi za mwisho’ za mfumo huu wa mambo, watu wa Yehova wanaendelea kuwa vitu vya kuchukiwa na kuonyeshwa uadui. (2 Timotheo 3:1) Katika sehemu zote za dunia, Mashahidi wa Yehova wamenyanyaswa wakati fulani chini ya utawala wa kimabavu na katika nchi za kidemokrasia wakiwa mtu mmoja-mmoja au kikundi.

      Kwa Nini Wanachukiwa na Kunyanyaswa?

      13. Watumishi wa Yehova wa sasa wanapaswa kukumbuka nini kuhusu mnyanyaso?

      13 Hata ingawa wengi wetu leo tunafurahia uhuru wa kadiri wa kuhubiri na kukutana pamoja kwa amani, lazima tusikilize kikumbusho cha Biblia kwamba “mandhari ya ulimwengu huu inabadilika.” (1 Wakorintho 7:31) Mambo yanaweza kubadilika kwa ghafula hivi kwamba tusipojitayarisha kiakili, kihisia, na kiroho, tunaweza kukwazwa kwa urahisi. Kwa hiyo, tunapaswa kufanya nini ili kujilinda? Njia nzuri zaidi ya kujilinda ni kukumbuka sababu inayofanya Wakristo wanaopenda amani na kutii sheria wachukiwe na kunyanyaswa.

      14. Petro alisema Wakristo walinyanyaswa kwa sababu gani?

      14 Mtume Petro alizungumzia jambo hilo katika barua yake ya kwanza aliyoandika yapata mwaka wa 62-64 W.K., wakati Wakristo katika Milki yote ya Roma walipokuwa wakikabili majaribu na mnyanyaso. Alisema: “Wapendwa, msitatanishwe juu ya kuwaka miongoni mwenu, ambako kunatukia kwenu kuwa jaribu, kama kwamba jambo geni linawapata.” Ili kufafanua jambo alilokuwa akizungumzia, Petro aliendelea kusema: “Acheni mmoja wenu asiteseke akiwa muuaji-kimakusudi au mwizi au mtenda-maovu au akiwa mjishughulishaji katika mambo ya watu wengine. Lakini ikiwa ateseka akiwa Mkristo, acheni asione aibu, bali acheni afulize kumtukuza Mungu katika jina hili.” Petro alisema kwamba waliteseka kwa sababu walikuwa Wakristo wala si kwa sababu walitenda makosa yoyote. Kama wangalikuwa wamejitia katika “dimbwi lilelile la chini la ufasiki” kama watu waliowazunguka, basi wangekubalika kwa watu hao. Lakini ukweli ni kwamba waliteseka kwa sababu walijitahidi kutimiza daraka lao wakiwa wafuasi wa Kristo. Hali ya Wakristo wa kweli leo inafanana na hiyo.—1 Petro 4:4, 12, 15, 16.

      15. Kwa nini leo Mashahidi wa Yehova hupigwa marufuku na kudhulumiwa ingawa wana mwenendo mzuri?

      15 Katika sehemu nyingi duniani, Mashahidi wa Yehova husifiwa hadharani kwa umoja na muungano wanaoonyesha kwenye makusanyiko yao na kwenye miradi ya ujenzi, kwa unyoofu na bidii yao, kwa maadili yao na maisha mazuri ya familia, na hata kwa mavazi na mwenendo wao mzuri.a Kwa upande mwingine, wakati makala hii ilipoandikwa, bado kulikuwa na marufuku au vizuizi katika nchi 28, na Mashahidi wengi wanadhulumiwa na kupoteza mali yao kwa ajili ya imani yao. Kwa nini Mashahidi wa Yehova hupigwa marufuku na kudhulumiwa ingawa wana mwenendo mzuri? Na kwa nini Mungu huruhusu jambo hilo?

      16. Sababu kuu ambayo humfanya Mungu aruhusu watu wake wanyanyaswe ni gani?

      16 Tunapaswa kukumbuka hasa maneno ya Mithali 27:11: “Mwanangu, uwe na hekima na kunifurahisha moyo wangu; ili nipate kumjibu anilaumuye.” Naam, tunanyanyaswa kwa sababu ya suala lililozushwa zamani linalohusu enzi kuu ya ulimwengu wote. Ingawa ushuhuda mwingi sana umetolewa na wote walioshika uaminifu-maadili kwa Yehova katika karne zilizopita, bado Shetani anaendelea kumdhihaki Yehova kama alivyofanya siku za Ayubu mwadilifu. (Ayubu 1:9-11; 2:4, 5) Bila shaka, Shetani amekuwa na pirikapirika nyingi zaidi katika jitihada yake ya mwisho ya kuthibitisha dai lake, kwa kuwa sasa Ufalme wa Mungu umesimamishwa imara, nao una raia waaminifu na wawakilishi duniani pote. Je, raia hao wataendelea kuwa waaminifu kwa Mungu hata wakipatwa na matatizo na magumu? Kila mtumishi wa Yehova anapaswa kujibu kibinafsi swali hilo.—Ufunuo 12:12, 17.

      17. Yesu alimaanisha nini aliposema kwamba “itageuka kwenu kuwa ushahidi”?

      17 Alipowaambia wanafunzi wake mambo ambayo yangetukia wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo,” Yesu alionyesha sababu nyingine inayomfanya Yehova aruhusu watumishi wake wanyanyaswe. Aliwaambia hivi: ‘Mtaburutwa mbele ya wafalme na magavana kwa ajili ya jina langu. Itageuka kwenu kuwa ushahidi.’ (Mathayo 24:3, 9; Luka 21:12, 13) Yesu mwenyewe alitoa ushahidi mbele ya Herode na Pontio Pilato. Mtume Paulo pia ‘aliburutwa mbele ya wafalme na magavana.’ Kwa mwongozo wa Bwana Yesu Kristo, Paulo alitafuta njia ya kumtolea ushahidi mtawala aliyekuwa na mamlaka kuu zaidi wakati huo aliposema: “Mimi nakata rufani kwa Kaisari!” (Matendo 23:11; 25:8-12) Vivyo hivyo leo, mara nyingi hali ngumu zimefanya iwezekane kuwatolea ushahidi maofisa na watu kwa ujumla kwa njia nzuri.b

      18, 19. (a) Kuvumilia majaribu kunaweza kutunufaishaje? (b) Ni maswali gani yatakayozungumziwa katika makala inayofuata?

      18 Kwa kumalizia, tunaweza kunufaika kwa kuvumilia majaribu na dhiki. Jinsi gani? Mwanafunzi Yakobo aliwakumbusha Wakristo wenzake hivi: “Fikirieni yote kuwa shangwe, ndugu zangu, mkutanapo na majaribu ya namna mbalimbali, kama mjuavyo kwamba ubora huu uliojaribiwa wa imani yenu hutokeza uvumilivu.” Ndiyo, mnyanyaso unaweza kuboresha imani yetu na kufanya tuwe na uvumilivu zaidi. Hivyo, hatuogopi mnyanyaso, wala hatutafuti njia zisizo za Kimaandiko ili kuuepuka au kuukomesha. Badala yake, tunatii shauri la Yakobo: “Acheni uvumilivu uwe na kazi yao ikiwa kamili, ili nyinyi mpate kuwa kamili na timamu katika mambo yote, bila ukosefu katika kitu chochote.”—Yakobo 1:2-4.

      19 Hata ingawa Neno la Mungu hutusaidia kuelewa kwa nini watumishi waaminifu wa Mungu hunyanyaswa na kwa nini Yehova huruhusu mnyanyaso, jambo hilo halifanyi iwe rahisi kuvumilia. Ni nini kinachoweza kutuimarisha ili kuuvumilia? Tunaweza kufanya nini tunaponyanyaswa? Tutazungumzia mambo hayo muhimu katika makala inayofuata.

      [Maelezo ya Chini]

      a Ona gazeti Mnara wa Mlinzi la Desemba 15, 1995, ukurasa wa 27-29; Aprili 15, 1994, ukurasa wa 16-17; na Amkeni! la Desemba 22, 1993, ukurasa wa 6-13.

      b Ona gazeti Amkeni! la Januari 8, 2003, ukurasa wa 3-11.

  • Kuvumilia Chini ya Majaribu Humletea Yehova Sifa
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Oktoba 1
    • Kuvumilia Chini ya Majaribu Humletea Yehova Sifa

      “Ikiwa, mnapotenda mema na kuteseka, mwalivumilia, hili ni jambo lenye kukubalika kwa Mungu.”—1 PETRO 2:20.

      1. Kwa kuwa Wakristo wa kweli wanahangaikia kuishi kupatana na wakfu wao, ni swali gani linalopaswa kufikiriwa?

      WAKRISTO wamejiweka wakfu kwa Yehova nao wanataka kufanya mapenzi yake. Ili kuishi kupatana na wakfu wao, wao hujitahidi kadiri wawezavyo kufuata hatua za Yesu Kristo aliye Kielelezo chao, na hutoa ushahidi kuhusu kweli. (Mathayo 16:24; Yohana 18:37; 1 Petro 2:21) Hata hivyo, Yesu na watu wengine waaminifu walikufa kwa ajili ya imani yao. Je, hilo linamaanisha kwamba Wakristo wote watarajie kufa kwa ajili ya imani yao?

      2. Wakristo huyaonaje majaribu na mateso?

      2 Tukiwa Wakristo tunahimizwa tuwe waaminifu mpaka kifo, lakini si lazima tufe kwa ajili ya imani. (2 Timotheo 4:7; Ufunuo 2:10) Hilo linamaanisha kwamba hatungependa kufa hata ingawa tuko tayari kuteseka—na ikiwa lazima, kufa—kwa ajili ya imani yetu. Hatufurahii kuteseka wala hatufurahii kupatwa na maumivu na kufedheheshwa. Hata hivyo, kwa kuwa tunatarajia majaribu na mnyanyaso, tunahitaji kufikiria kwa makini jinsi tunavyoweza kutenda tunapopatwa na mambo hayo.

      Waaminifu Chini ya Jaribu

      3. Unaweza kusimulia mifano ya watu gani katika Biblia ambao walikabiliana na mnyanyaso? (Ona sanduku “Jinsi Walivyokabiliana na Mnyanyaso,” kwenye ukurasa unaofuata.)

      3 Katika Biblia, tunapata masimulizi mengi yanayoonyesha jinsi watumishi wa Mungu wa zamani walivyotenda walipokabili hali zilizohatarisha maisha yao. Watumishi hao walitenda kwa njia mbalimbali ambazo zinaweza kuwasaidia Wakristo leo wakipatwa na hali kama hizo. Soma masimulizi mbalimbali kwenye sanduku lenye kichwa “Jinsi Walivyokabiliana na Mnyanyaso,” na uone ni mambo gani unayoweza kujifunza kutokana nayo.

      4. Tunaweza kusema nini kuhusu jinsi Yesu na watumishi wengine waaminifu walivyotenda walipopatwa na majaribu?

      4 Waliponyanyaswa, Yesu na watumishi wengine waaminifu wa Mungu walitenda kwa njia mbalimbali ikitegemea hali. Lakini ni wazi kwamba hawakuhatarisha maisha yao isivyo lazima. Walipojikuta katika hali hatari, walikuwa jasiri lakini wenye kujihadhari. (Mathayo 10:16, 23) Walikuwa na lengo la kuendelea kuhubiri na kudumisha uaminifu-maadili wao kwa Yehova. Matendo yao katika hali mbalimbali ni mfano mzuri kwa Wakristo ambao leo wanakabiliana na majaribu na minyanyaso.

      5. Ni mnyanyaso gani uliotokea Malawi miaka ya 1960, nao Mashahidi wa nchi hiyo walitendaje?

      5 Leo, mara nyingi watu wa Yehova hujikuta katika hali ngumu sana na umaskini kwa sababu ya vita, marufuku, au kunyanyaswa. Kwa mfano katika miaka ya 1960 Mashahidi wa Yehova walinyanyaswa kikatili nchini Malawi. Majumba yao ya Ufalme, nyumba, vyakula, na biashara zao, yaani, vitu vyote walivyokuwa navyo viliharibiwa. Walipigwa na kutendewa mambo mengine yenye kusikitisha. Ndugu hao walitendaje? Maelfu walikimbia vijiji vyao. Wengi walikimbilia msituni, huku wengine wakihamia nchi jirani ya Msumbiji kwa muda. Ingawa ndugu wengi waaminifu walikufa, wengine waliamua kukimbia eneo lenye hatari, hatua ambayo yaonekana ilifaa kuchukuliwa katika hali hizo. Kwa kufanya hivyo, ndugu hao waliiga kielelezo cha Yesu na Paulo.

      6. Ni nini ambacho Mashahidi wa Malawi hawakuacha kufanya kujapokuwa mnyanyaso mkali?

      6 Hata ingawa ndugu wa Malawi walilazimika kuhama au kujificha, walitafuta na kufuata mwongozo wa kiroho nao waliendelea kufanya kazi ya Kikristo kisiri kadiri walivyoweza. Ikawaje? Kulikuwa na kilele cha watangazaji wa Ufalme 18,519 kabla tu ya marufuku iliyotokea mwaka wa 1967. Kufikia mwaka wa 1972 kulikuwa na kilele kipya cha watangazaji 23,398 ingawa marufuku ilikuwa bado haijaondolewa na wengi walikuwa wamekimbilia Msumbiji. Walihubiri kwa wastani wa saa zaidi ya 16 kila mwezi. Bila shaka, walimletea Yehova sifa kwa jinsi walivyotenda, naye aliwabariki ndugu hao waaminifu wakati huo mgumu sana.a

      7, 8. Ni kwa sababu gani wengine huamua kutokimbia, hata ingawa upinzani unaleta matatizo?

      7 Kwa upande mwingine, katika nchi ambako upinzani unaleta matatizo, huenda baadhi ya akina ndugu wakaamua wasikimbie, hata ingawa wanaweza kufanya hivyo. Huenda kukimbia kukatatua matatizo fulani, lakini kunaweza kusababisha magumu mengine. Kwa mfano, je, wataweza kudumisha mawasiliano na ndugu zao Wakristo na wasitengwe nao kiroho? Je, wataweza kuendelea na programu yao ya kawaida ya mambo ya kiroho huku wakijitahidi kuanza maisha mapya, labda katika nchi tajiri au nchi ambako wanaweza kujipatia vitu vingi vya kimwili?—1 Timotheo 6:9.

      8 Wengine huamua kutokimbia kwa sababu wanajali hali ya kiroho ya ndugu zao. Wao huamua kubaki na kukabiliana na hali ili waendelee kuhubiri katika maeneo ya kwao na kuwatia moyo waabudu wenzao. (Wafilipi 1:14) Kwa kuamua kufanya hivyo, mwishowe wengine wameweza kuchangia kushinda kesi kadhaa katika nchi zao.b

      9. Mtu anapaswa kufikiria mambo gani anapoamua kama atabaki au atakimbia kwa sababu ya mnyanyaso?

      9 Kwa kweli uamuzi wa kukimbia au kubaki ni wa mtu binafsi. Bila shaka, maamuzi hayo yanapaswa kufanywa baada ya kutafuta mwongozo wa Yehova kupitia sala. Lakini, hata tuamue kufanya nini, tunapaswa kukumbuka maneno haya ya mtume Paulo: “Kila mmoja wetu atatoa hesabu kwa Mungu kwa ajili yake mwenyewe.” (Waroma 14:12) Kama tulivyoona awali, Yehova anataka kila mmoja wa watumishi wake aendelee kuwa mwaminifu katika hali zote. Leo, baadhi ya watumishi wake wanapatwa na majaribu na mnyanyaso na huenda wengine wakapatwa na mambo hayo baadaye. Wote watajaribiwa kwa njia moja au nyingine, na hakuna yeyote anayepaswa kufikiri kwamba hawezi kupatwa na majaribu. (Yohana 15:19, 20) Tukiwa watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu hatuwezi kuepuka lile suala la ulimwenguni pote linalohusu kutakaswa kwa jina la Yehova na kutetewa kwa enzi yake kuu.—Ezekieli 38:23; Mathayo 6:9, 10.

      “Msirudishe Ovu kwa Ovu kwa Yeyote”

      10. Yesu na mitume wake walituwekea kielelezo gani muhimu katika kukabiliana na mikazo na upinzani?

      10 Kanuni nyingine muhimu tunayoweza kujifunza kutokana na jinsi Yesu na mitume walivyotenda chini ya mkazo ni kwamba hatupaswi kulipiza kisasi dhidi ya watu wanaotunyanyasa. Biblia haisemi popote kwamba Yesu na wafuasi wake waliunda kikundi fulani cha upinzani au kutumia jeuri ili kupambana na watu waliowanyanyasa. Kinyume cha hilo, mtume Paulo aliwashauri Wakristo hivi: “Msirudishe ovu kwa ovu kwa yeyote. . . . Wapendwa, msijilipizie kisasi wenyewe bali iachieni nafasi hasira ya kisasi; kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; hakika mimi nitalipa, asema Yehova.’” Isitoshe, “usijiache mwenyewe ushindwe na lililo ovu, bali fuliza kushinda lililo ovu kwa lililo jema.”—Waroma 12:17-21; Zaburi 37:1-4; Mithali 20:22.

      11. Mwanahistoria mmoja anasema nini kuhusu mtazamo wa Wakristo wa mapema kuelekea Serikali?

      11 Wakristo wa mapema walitii shauri hilo. Katika kitabu chake The Early Church and the World, mwanahistoria Cecil J. Cadoux anaeleza mtazamo wa Wakristo kuelekea Serikali katika miaka ya 30-70 W.K. Anaandika hivi: “Hatuna uthibitisho wowote kwamba wakati huo Wakristo walitumia jeuri ili kupinga mnyanyaso. Jambo ambalo Wakristo walifanya ni kuwashutumu tu watawala au kuwatatanisha kwa kukimbia. Kwa kawaida Wakristo walikataa kwa upole lakini kwa uthabiti kutii maagizo ya serikali ambayo waliamini yalipingana na utii wao kwa Kristo.”

      12. Kwa nini inafaa kuvumilia mateso kuliko kulipiza kisasi?

      12 Je, ni jambo la hekima kwa Wakristo kuvumilia tu mateso bila kujitetea? Je, kutojitetea hakungefanya iwe rahisi kwa wale walio na nia ya kuwaangamiza Wakristo wafanye hivyo? Je, halingekuwa jambo la hekima kujitetea? Huenda jambo hilo likaonekana kuwa la hekima kulingana na maoni ya mwanadamu. Hata hivyo, tukiwa watumishi wa Yehova tuna hakika kwamba njia iliyo bora zaidi ni kufuata mwongozo wa Yehova katika mambo yote. Sisi hukumbuka maneno haya ya Petro: “Ikiwa, mnapotenda mema na kuteseka, mwalivumilia, hili ni jambo lenye kukubalika kwa Mungu.” (1 Petro 2:20) Tuna hakika kwamba Yehova anajua vizuri hali ilivyo naye hatairuhusu iendelee milele. Tunawezaje kuwa na hakika kuhusu jambo hilo? Yehova aliwaambia hivi watu wake waliokuwa utumwani Babiloni: ‘Yeye awagusaye ninyi aigusa mboni ya jicho langu.’ (Zekaria 2:8) Hakuna mtu awezaye kuruhusu mboni ya jicho lake iguswe kwa muda mrefu. Yehova ataleta kitulizo wakati unaofaa. Hatuna shaka lolote kwamba atafanya hivyo.—2 Wathesalonike 1:5-8.

      13. Kwa nini Yesu aliwaruhusu maadui wake wamkamate bila kuchukua hatua yoyote?

      13 Kuhusu hilo, tunaweza kumwiga Yesu ambaye ni kielelezo chetu. Ingawa Yesu angeweza kujitetea, aliruhusu maadui wake wamkamate katika bustani ya Gethsemane. Hata aliwaambia hivi wanafunzi wake: ‘Mnafikiri kwamba siwezi kuomba Baba yangu anipe mimi katika dakika hii malejioni zaidi ya kumi na mawili ya malaika? Katika kisa hicho, Maandiko yangetimizwaje kwamba lazima itendeke kwa njia hii?’ (Mathayo 26:53, 54) Yesu aliona kutimizwa kwa mapenzi ya Yehova kuwa jambo muhimu zaidi, hata ingawa angeteseka kwa kufanya hivyo. Aliyaamini kabisa maneno ya unabii wa zaburi hii ya Daudi: “Hutakuachia kuzimu nafsi yangu, wala hutamtoa mtakatifu wako aone uharibifu.” (Zaburi 16:10) Miaka kadhaa baadaye, mtume Paulo alisema hivi kumhusu Yesu: “Kwa ajili ya shangwe iliyowekwa mbele yake alivumilia mti wa mateso, akidharau aibu, na ameketi kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu.”—Waebrania 12:2.

      Shangwe ya Kulitakasa Jina la Yehova

      14. Ni shangwe gani iliyomtegemeza Yesu wakati wa majaribu yake yote?

      14 Ni shangwe gani iliyomtegemeza Yesu wakati alipopatwa na jaribu kali sana? Kati ya watumishi wote wa Yehova, Yesu, Mwana mpendwa wa Mungu, ndiye kwa kweli aliyekuwa shabaha kuu zaidi ya Shetani. Kwa hiyo, kwa kudumisha uaminifu-maadili chini ya jaribu, Yesu angetoa jibu bora kabisa kwa dhihaka za Shetani dhidi ya Yehova. (Mithali 27:11) Je, unaweza kuwazia shangwe na uradhi ambao Yesu alipata alipofufuliwa? Ni lazima awe alifurahi sana kutambua kwamba alikuwa ametimiza jukumu alilopewa akiwa mwanadamu mkamilifu la kutetea enzi kuu ya Yehova na kulitakasa jina Lake. Isitoshe, hapana shaka kwamba kuketi “kwenye mkono wa kuume wa kiti cha ufalme cha Mungu” ni pendeleo zuri ambalo humletea Yesu shangwe kuu sana.—Zaburi 110:1, 2; 1 Timotheo 6:15, 16.

      15, 16. Ni mnyanyaso gani wa kikatili uliowapata Mashahidi huko Sachsenhausen, na walipata wapi nguvu za kuvumilia?

      15 Vivyo hivyo, Wakristo hupata shangwe kushiriki katika kulitakasa jina la Yehova kwa kuvumilia majaribu na mnyanyaso, wakiiga kielelezo cha Yesu. Mfano mzuri unahusu Mashahidi walioteseka kwenye kambi yenye sifa mbaya ya Sachsenhausen na kunusurika ule msafara wa kifo wenye kuchosha mwishoni mwa Vita vya Pili vya Ulimwengu. Wakati wa msafara huo, maelfu ya wafungwa walikufa kwa sababu ya baridi kali, ugonjwa, au njaa au waliuawa kikatili barabarani na kikosi maalumu cha walinzi wa Hitler. Mashahidi wote 230 walinusurika kwa kukaa karibu-karibu na kusaidiana ingawa kufanya hivyo kulihatarisha maisha yao.

      16 Mashahidi hao walipata wapi nguvu za kuvumilia mnyanyaso huo wa kikatili? Mara tu walipofika mahali salama, walionyesha shangwe na shukrani zao kwa Yehova katika hati yenye kichwa, “Azimio la Mashahidi wa Yehova 230 kutoka mataifa sita waliokusanyika msituni karibu na Schwerin huko Mecklenburg.” Katika hati hiyo walisema: “Kipindi kirefu cha majaribu kimeisha, na wale walionusurika, ambao waliponea chupuchupu, hawakuathiriwa na majaribu yaliyowapata. (Ona Danieli 3:27.) Badala yake, wanajawa na nguvu na uwezo kutoka kwa Yehova na wanangojea kwa hamu maagizo mapya kutoka kwa Mfalme ili kuendeleza mambo yanayohusu Ufalme.”c

      17. Leo watu wa Mungu wanakabili majaribu ya aina gani?

      17 Kama Mashahidi hao waaminifu 230, imani yetu pia inaweza kujaribiwa, hata ingawa bado ‘hatujakinza kamwe hadi damu.’ (Waebrania 12:4) Lakini majaribu yanaweza kuwa ya namna mbalimbali. Huenda yakawa dhihaka kutoka kwa wanadarasa, au kushawishiwa kufanya uasherati na mambo mengine mabaya. Isitoshe, mara kwa mara uamuzi wa kujiepusha na damu, kufunga ndoa katika Bwana tu, au kulea watoto wanaomwamini Mungu katika familia iliyogawanyika kidini kunaweza kusababisha mikazo na majaribu makali.—Matendo 15:29; 1 Wakorintho 7:39; Waefeso 6:4; 1 Petro 3:1, 2.

      18. Tuna uhakikisho gani kwamba tunaweza kuvumilia hata jaribu kali sana?

      18 Lakini, hata tupatwe na majaribu gani, tunajua kwamba tunateseka kwa sababu ya kumtanguliza Yehova na Ufalme wake, nasi huona kufanya hivyo kuwa pendeleo kubwa na pia jambo linaloleta shangwe. Tunapata ujasiri kutokana na maneno haya ya Petro yanayotoa uhakikisho: “Ikiwa mnashutumiwa kwa ajili ya jina la Kristo, nyinyi ni wenye furaha, kwa sababu roho ya utukufu, naam, roho ya Mungu, inatulia juu yenu.” (1 Petro 4:14) Roho ya Yehova hutupa nguvu ya kuvumilia hata majaribu makali sana, na hivyo kumletea utukufu na sifa.—2 Wakorintho 4:7; Waefeso 3:16; Wafilipi 4:13.

      [Maelezo ya Chini]

      a Matukio ya miaka ya 1960 yalikuwa mwanzo tu wa mfululizo wa mnyanyaso wa kikatili ambao ungewapata Mashahidi nchini Malawi kwa miaka karibu thelathini. Kwa habari kamili, ona kitabu 1999 Yearbook of Jehovah’s Witnesses, ukurasa wa 171-212.

      b Ona makala “Mahakama Kuu Yatetea Ibada ya Kweli Katika ‘Nchi ya Ararati’” katika toleo la Mnara wa Mlinzi la Aprili 1, 2003, ukurasa wa 11-14.

      c Kwa habari kamili kuhusu azimio hilo, ona kitabu 1974 Yearbook of Jehovah’s Witnesses, ukurasa wa 208-209. Mtu mmoja aliyenusurika msafara huo anaeleza yaliyompata kwenye toleo la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1998, ukurasa wa 25-29.

  • Kuvumilia Chini ya Majaribu Humletea Yehova Sifa
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Oktoba 1
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 15]

      Jinsi Walivyokabiliana na Mnyanyaso

      • Kwa mwongozo wa malaika, Yosefu na Maria walimchukua mtoto Yesu na kukimbilia Misri kabla askari wa Herode kufika Bethlehemu ili kuwaua watoto wote wa kiume waliokuwa na umri wa miaka miwili na chini.—Mathayo 2:13-16.

      • Wakati wa huduma yake, maadui wa Yesu walijaribu mara nyingi kumuua kwa sababu ya ushahidi wake wenye nguvu. Yesu aliwakwepa kila mara walipojaribu kufanya hivyo.—Mathayo 21:45, 46; Luka 4:28-30; Yohana 8:57-59.

      • Wakati askari na maofisa walipokuja katika bustani ya Gethsemane kumkamata Yesu, alijitambulisha kwao waziwazi na kuwaambia hivi mara mbili: “Mimi ndiye.” Hata aliwazuia wafuasi wake wasipigane nao naye akawaruhusu watu hao wenye ghasia wamkamate na kwenda naye.—Yohana 18:3-12.

      • Huko Yerusalemu, Petro na wengine walikamatwa, wakapigwa viboko, na kuamriwa waache kuzungumza juu ya Yesu. Lakini walipoachiliwa ‘walishika njia yao na kila siku katika hekalu na kutoka nyumba hadi nyumba wakaendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.’—Matendo 5:40-42.

      • Wakati Sauli, aliyekuja kuwa mtume Paulo, alipojua kwamba Wayahudi huko Damasko walikuwa wamepanga njama ya kumuua, akina ndugu walimtia ndani ya kikapu na kumteremsha usiku kupitia mwanya fulani kwenye ukuta wa jiji, naye akatoroka.—Matendo 9:22-25.

      • Miaka kadhaa baadaye, Paulo aliamua kukata rufani kwa Kaisari, hata ingawa Gavana Festo na Mfalme Agripa hawakuona “lolote linalostahili kifo au vifungo” kumhusu.—Matendo 25:10-12, 24-27; 26:30-32.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki