-
Kutafuta Matabiri YanayotumainikaMnara wa Mlinzi—1999 | Julai 15
-
-
Kutafuta Matabiri Yanayotumainika
PUNDE baada ya kuanza kutawala mwaka wa 336 K.W.K., Mfalme wa Makedonia aliyekuja kuitwa Aleksanda Mkuu alizuru madhabahu ya uaguzi ya Delphi huko Ugiriki ya kati. Katika mipango yake ya wakati ujao, yeye alikuwa na lengo la kushinda sehemu kubwa ya ulimwengu wa wakati huo. Lakini alitaka uhakikisho wa kimungu kwamba angefanikiwa katika shughuli hiyo kubwa. Hekaya husema kwamba siku ambapo alizuru Delphi, haikuruhusika kuwasiliana na mwaguzi wa madhabahu hiyo. Kwa kuwa hakutaka kuondoka bila jibu, Aleksanda alisisitiza, akimlazimisha kuhani huyo wa kike kutabiri. Kwa kukata tamaa, alisema hivi kwa sauti kubwa: “Ee, mtoto, hushindiki!” Mfalme huyo mchanga alichukua maneno hayo kuwa ishara ya mema—iliyotoa ahadi ya ushindi katika kampeni yake ya kijeshi.
Hata hivyo, Aleksanda angaliarifiwa vema zaidi juu ya matokeo ya kampeni yake kama angalichunguza unabii mbalimbali unaopatikana katika kitabu cha Biblia cha Danieli. Kwa usahihi wenye kutokeza, kilitabiri juu ya ushindi wake wa haraka-haraka. Mapokeo husema kwamba hatimaye Aleksanda alipata fursa ya kuona yale Danieli aliyokuwa ameandika kumhusu. Kulingana na Josephus, mwanahistoria Myahudi, mfalme huyo wa Makedonia alipoingia Yerusalemu, alionyeshwa unabii wa Danieli—huenda sura ya 8 ya kitabu hicho. (Danieli 8:5-8, 20, 21) Yasemekana kwamba kwa sababu hiyo, majeshi ya Aleksanda yenye kuharibu yaliachilia jiji hilo.
Uhitaji wa Kiasili wa Binadamu
Mfalme au mtu wa kawaida, mtu wa kale au wa kisasa—mwanadamu ameona uhitaji wa kupata matabiri yenye kutumainika kuhusu wakati ujao. Tukiwa viumbe wenye akili, sisi wanadamu huchunguza wakati uliopita, tuna habari juu ya wakati uliopo, na tunapendezwa hasa na wakati ujao. Mithali moja ya Kichina yasema hivi kwa kufaa: “Mtu ambaye angeweza kujua mambo yatakayotukia siku tatu kimbele, angekuwa tajiri kwa maelfu ya miaka.”
Katika enzi zote, mamilioni ya watu wamejaribu kuchungua wakati ujao kwa kutafuta habari kutokana na walichokiona kuwa mungu. Kwa mfano, fikiria Wagiriki wa kale. Walikuwa na madhabahu nyingi takatifu za uaguzi, kama zile za Delphi, Delos, na Dodona, ambapo walikuwa wakienda kutafuta habari kutoka kwa miungu yao kuhusiana na matukio ya kisiasa na ya kijeshi na pia mambo ya kibinafsi kama vile safari, ndoa, na watoto. Mbali na wafalme na viongozi wa kijeshi, makabila mazima-mazima pia yalitafuta mwongozo kutoka kwa makao ya roho kupitia habari hizi za waaguzi.
Kulingana na profesa mmoja, sasa kuna “ongezeko kubwa la ghafula la matengenezo ambayo yanajishughulisha na kuchunguza wakati ujao peke yake.” Hata hivyo, watu wengi hupendelea kupuuza chanzo pekee cha unabii sahihi—Biblia. Wao hupuuza waziwazi uwezekano wowote wa kwamba unabii mbalimbali wa Biblia una habari zilezile wanazotafuta. Wasomi wengine hata hulinganisha unabii wa Biblia na matabiri yaliyotolewa na waaguzi wa kale. Na kwa kawaida, watu wa kisasa wenye kutilia shaka hawapendelei unabii wa Biblia.
Twakualika uchunguze mwenyewe rekodi hiyo. Kulinganisha kwa makini matabiri ya Biblia na habari za waaguzi wa kibinadamu hufunua nini? Je, unaweza kuutumaini unabii wa Biblia kuliko habari za waaguzi wa kale? Na je, unaweza kutegemeza maisha yako juu ya unabii mbalimbali wa Biblia?
-
-
Sababu Waweza Kuutumaini Unabii wa BibliaMnara wa Mlinzi—1999 | Julai 15
-
-
Sababu Waweza Kuutumaini Unabii wa Biblia
MFALME PIRO wa Epirus, kaskazini-magharibi mwa Ugiriki, alipambana kwa muda mrefu na Milki ya Roma. Akitaka sana kupata habari yenye kutegemeka kuhusu matokeo ya pambano hilo, alienda kutafuta habari katika madhabahu ya uaguzi ya Delphi. Lakini jibu alilopata lingeweza kueleweka katika mojawapo ya njia hizi mbili: (1) “Nasema kwamba wewe mwana wa Æacus unaweza kuwashinda Waroma. Wewe utaenda, wewe utarudi, hutaangamia vitani kamwe.” (2) “Nasema kwamba Waroma wanaweza kukushinda wewe, mwana wa Æacus. Wewe utaenda, wewe hutarudi, utaangamia vitani.” Aliamua kuelewa habari zilizotolewa katika sehemu ya kwanza ya jibu hilo, hivyo akafanya vita dhidi ya Roma. Piro alishindwa kabisa.
Visa kama hivyo vilifanya habari za waaguzi wa kale ziwe na sifa mbaya kwa kuwa hazikutolewa waziwazi nazo zilikuwa na maana zaidi ya moja. Lakini namna gani unabii wa Biblia? Wachambuzi fulani husisitiza kwamba unabii mbalimbali unaopatikana katika Biblia ni sawa tu na habari za waaguzi. Wachambuzi hao hukisia kwamba matabiri ya Biblia yalikuwa tu ubashiri wa werevu wa matukio ya wakati ujao, uliotolewa na watu wenye akili nyingi na wenye kufahamu mambo vizuri, kwa kawaida watu wa jamii ya kikuhani. Tuseme kwamba watu hao, kwa kujionea mambo tu au kupitia ukoo wao mbalimbali wa pekee, walijua kimbele jinsi ambavyo hali fulani zingekuja kuwa kiasili. Kwa kulinganisha sifa tofauti-tofauti za unabii mbalimbali wa Biblia na habari za waaguzi hao, tutakuwa katika hali nzuri zaidi kuamua mambo ifaavyo.
Mambo Yanayotofautiana
Habari za waaguzi zilitambuliwa kwa kuwa na maana zaidi ya moja. Kwa mfano, mjini Delphi majibu yalitolewa kwa sauti zisizoeleweka. Hilo lilifanya iwe lazima kwa makuhani kuzifasiri na kubuni mistari ambayo ingeweza kutoa fasiri zilizo tofauti kabisa. Jibu lililopewa Croesus, mfalme wa Lidia, ni mfano halisi. Alipotafuta habari kwenye madhabahu ya uaguzi, aliambiwa hivi: “Croesus akivuka Halys, ataharibu milki yenye nguvu.” Kwa kweli, “milki yenye nguvu” iliyoharibiwa ilikuwa yake mwenyewe! Wakati Croesus alipovuka mto Halys ili kushambulia Kapadokia, alishindwa na Koreshi Mwajemi.
Kinyume kabisa na habari za waaguzi, unabii mbalimbali wa Biblia unatambuliwa kwa kuwa sahihi na wazi. Mfano mmoja ni ule unabii kuhusu kuanguka kwa Babiloni, ambao umerekodiwa katika kitabu cha Biblia cha Isaya. Miaka ipatayo 200 kabla ya tukio hilo, nabii Isaya alitabiri kinaganaga na kwa usahihi jinsi Muungano wa Umedi na Uajemi ungepindua Babiloni. Unabii huo ulifunua kwamba mshindi huyo angeitwa Koreshi, ukafunua mkakati hasa wa kukausha mto uliokuwa kama handaki ya kujikinga na kufunua pia kule kuingia ndani ya jiji lenye kuta kupitia malango yaliyokuwa wazi. Hayo yote yalitimizwa kwa usahihi. (Isaya 44:27–45:2) Pia ilitabiriwa kwa usahihi kwamba baadaye Babiloni lingekuwa ukiwa kabisa.—Isaya 13:17-22.
Fikiria pia, udhahiri wa onyo hili lililotolewa na nabii Yona: “Baada ya siku arobaini Ninawi utaangamizwa.” (Yona 3:4) Hakuna maana zaidi ya moja hapa! Ujumbe huo ulikuwa wenye kutokeza sana na wa moja kwa moja hivi kwamba papo hapo watu wa Ninawi “wakamsadiki Mungu; wakatangaza kufunga, wakajivika nguo za magunia.” Kwa sababu ya toba yao, Yehova hakuleta maafa dhidi ya Waninawi wakati huo.—Yona 3:5-10.
Habari za waaguzi zilitumiwa kama njia ya kuwa na uvutano wa kisiasa. Mara nyingi watawala na viongozi wa kijeshi walitaja fasiri waliyopendelea ili waendeleze masilahi na shughuli zao za kibinafsi, hivyo wakitoa “wonyesho wa upendeleo wa kimungu.” Hata hivyo, jumbe za Mungu za unabii zilitolewa bila kufikiria hadhi ya watu binafsi.
Kwa mfano: Nathani, nabii wa Yehova, hakusita kumkaripia Mfalme Daudi mwenye kukosa. (2 Samweli 12:1-12) Wakati Yeroboamu wa Pili alitawala ufalme wa Israeli wa makabila kumi, manabii Hosea na Amosi walimchambua vikali mfalme huyo mwenye kuasi pamoja na wale waliomwunga mkono kwa sababu ya uasi wao na mwenendo wao wenye kumshushia Mungu heshima. (Hosea 5:1-7; Amosi 2:6-8) Onyo hili ambalo Yehova alimtolea mfalme huyo kupitia kinywa cha nabii Amosi ndilo lililokuwa kali zaidi: “Nami nitaondoka nishindane na nyumba ya Yeroboamu kwa upanga.” (Amosi 7:9) Nyumba ya Yeroboamu iliangamizwa kabisa.—1 Wafalme 15:25-30; 2 Mambo ya Nyakati 13:20.
Mara nyingi, habari za waaguzi zilitolewa kwa ada fulani. Yule aliyetoa ada kubwa zaidi ndiye angepokea habari alizotaka. Wale waliotafuta habari kwenye madhabahu ya uaguzi ya Delphi walilipa ada kubwa sana kwa habari zisizofaa kitu na kwa njia hiyo wakajaza hekalu la Apolo, na majumba yaliyoongezwa kwenye hekalu hilo, vitu vyenye thamani kubwa. Kinyume cha hilo, unabii na maonyo mbalimbali ya Biblia yalitolewa bila malipo na bila upendeleo wowote. Hivyo ndivyo ilivyokuwa bila kujali cheo au utajiri wa mtu ambaye kwa ajili yake yalitolewa, kwa kuwa nabii wa kweli hangeweza kupokea rushwa. Nabii Samweli, aliyekuwa pia mwamuzi, angeweza kuuliza hivi kwa moyo mweupe: “Kwa mkono wa nani nimepokea rushwa inipofushe macho?”—1 Samweli 12:3.
Kwa kuwa habari za waaguzi zilipatikana tu katika sehemu hususa, mtu alilazimika kujitahidi sana kusafiri kwenda huko ili kuzipokea. Kwa mtu wa kawaida, ilikuwa vigumu sana kufika kwenye nyingi za sehemu hizo kwa sababu zilikuwa katika maeneo kama Dodona lililokuwa kwenye Mlima Tomarus huko Epirus na Delphi lililokuwa katika sehemu ya milima-milima ya Ugiriki ya kati. Kwa kawaida, ni matajiri tu na watu wenye uwezo ambao wangeweza kutafuta habari kutoka kwa miungu katika madhabahu hizo za uaguzi. Isitoshe, “mapenzi ya miungu” yalifunuliwa siku chache tu kwa mwaka. Kinyume kabisa cha hilo, Yehova Mungu aliwatuma wajumbe wake manabii waende moja kwa moja kwa watu ili kuwatangazia unabii mbalimbali waliohitaji kusikia. Kwa mfano, wakati wa uhamisho wa Wayahudi huko Babiloni, Mungu alikuwa na angalau manabii watatu waliokuwa wakitumikia miongoni mwa watu wake—Yeremia jijini Yerusalemu, Ezekieli miongoni mwa wahamishwa, na Danieli katika jiji kuu la Milki ya Babiloni.—Yeremia 1:1, 2; Ezekieli 1:1; Danieli 2:48.
Kwa kawaida, habari za waaguzi zilitolewa faraghani ili yule aliyezipokea aweze kutumia fasiri ya habari hizo kwa faida yake mwenyewe. Kinyume cha hilo, unabii mbalimbali wa Biblia ulitolewa hadharani ili wote waweze kusikia ujumbe na kuelewa maana yake. Mara nyingi nabii Yeremia alisema hadharani huko Yerusalemu, ingawa alijua kwamba ujumbe wake haukupendwa na viongozi na wakazi wa jiji hilo.—Yeremia 7:1, 2.
Leo, habari za waaguzi huonwa kuwa sehemu ya historia ya kale. Hazina thamani yoyote yenye kutumika kwa watu wanaoishi katika nyakati zetu zenye hatari. Hakuna habari kama hizo zinazohusiana na wakati wetu au wakati ujao. Kinyume cha hilo, unabii mbalimbali wa Biblia ni sehemu ya “neno la Mungu [lililo] hai na hukazia nguvu.” (Waebrania 4:12) Unabii mbalimbali wa Biblia ambao tayari umetimizwa huandaa kiolezo cha namna Yehova alivyoshughulika na watu na pia hufunua sehemu kuu za makusudi yake na utu wake. Kwa kuongezea, unabii mbalimbali wa Biblia, ulio muhimu, utatimizwa hivi karibuni. Akifafanua mambo yajayo, mtume Petro aliandika hivi: “Lakini ziko mbingu mpya [Ufalme wa Kimesiya wa kimbingu] na dunia mpya [jamii ya kibinadamu yenye uadilifu] ambazo tunangojea kulingana na ahadi yake [Mungu], na katika hizo uadilifu utakaa.”—2 Petro 3:13.
Huenda ulinganisho huo mfupi wa unabii wa Biblia na habari za waaguzi wa dini zisizo za kweli ukafanya ufikie mkataa sawa na ule ambao umeonyeshwa katika kitabu chenye kichwa The Great Ideas: “Kwa habari ya ujuzi wa kimbele wa wanadamu wawezao kufa, manabii Waebrania waonekana kuwa wa kipekee. Tofauti na waaguzi au watabiri wapagani, . . . hawahitaji kutumia ufundi au mbinu ili kufahamu siri za Mungu. . . . Kwa sehemu kubwa, yaonekana walitoa unabii wenye kueleweka, tofauti na ule wa waaguzi. Angalau nia yaonekana ni kufunua wala si kuficha mpango wa Mungu kuhusu mambo hayo, kwa kuwa Yeye Mwenyewe hutaka wanadamu wajue kimbele jinsi ya kuenenda kwa busara.”
-