Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya Kweli
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Katika miaka ya mapema ya 1870, Charles Taze Russell na washirika wake walianzisha funzo la Biblia la moyo wa bidii. Ikawa wazi kwao kwamba Jumuiya ya Wakristo ilikuwa imeondoka sana katika mafundisho na mazoea ya Ukristo wa mapema. Ndugu Russell hakudai kuwa wa kwanza kutambua jambo hilo, naye alikiri waziwazi jinsi alivyokuwa na deni kwa wengine kwa usaidizi waliotoa wakati wa miaka yake ya mapema ya funzo la Maandiko. Alisema kwa uthamini juu ya kazi njema ambayo harakati tofauti-tofauti za yale Marekebisho Makubwa ya Kidini zilikuwa zimefanya ili kuacha nuru ya kweli iangaze kwa uangavu zaidi. Yeye alitaja kwa jina wanaume waliomzidi umri kama vile Jonas Wendell, George Stetson, George Storrs, na Nelson Barbour, ambao walichangia kibinafsi uelewevu wake wa Neno la Mungu katika njia mbalimbali.a

      Pia yeye alitaarifu hivi: “Mafundisho mbalimbali tuaminiyo na ambayo huonekana kuwa mapya na ya asili na tofauti sana yaliaminiwa kwa namna fulani muda mrefu uliopita: mathalani—Kuchaguliwa, Neema ya Bure, Rudisho, Kuhesabiwa Haki, Utakaso, Utukuzo, Ufufuo.” Hata hivyo, mara nyingi ilikuwa kwamba kikundi kimoja cha kidini kilitofautishwa kwa uelewevu wa wazi zaidi wa kweli moja ya Biblia; kikundi kingine, na kweli tofauti. Kuendelea kwao zaidi kulizuiwa mara nyingi kwa sababu walifungwa na mafundisho na imani za kidini zilizokuwa na itikadi ambazo zilikuwa zimesitawi katika Babiloni na Misri ya kale au ambazo ziliazimwa kutoka wanafalsafa Wagiriki.

      Lakini ni kikundi kipi, ambacho kikisaidiwa na roho ya Mungu, kingejipatia tena hatua kwa hatua “kiolezo cha maneno yenye afya” ambayo Wakristo wa karne ya kwanza walithamini sana? (2 Tim. 1:13, NW) Ni nani ambao ingefaa kusemwa kuwa kweli kwamba kijia chao kingekuwa “kama nuru nyangavu ambayo inaendelea kunurika na kunurika mpaka mchana upate kuthibitishwa imara”? (Mit. 4:18, NW) Ni nani ambao kwa kweli wangefanya ile kazi ambayo Yesu aliamuru aliposema: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia”? Ni nani ambao hawangefanya wanafunzi tu bali pia ‘wangewafundisha kushika mambo yote’ ambayo Yesu aliamuru? (Mdo. 1:8; Mt. 28:19, 20, NW) Kwelikweli, je, wakati ulikuwa umekaribia ambapo Bwana angeonyesha utofautisho wa wazi kati ya wale walio Wakristo wa kweli aliowafananisha na ngano na wale wa mwigo ambao alitaja kuwa kama magugu (hasa, magugu ya aina ambayo hufanana sana na ngano mpaka yafikiapo ukomavu)?b (Mt. 13:24-30, 36-43) Ni nani ambao wangethibitika kuwa ndio yule “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ambaye kwake, Bwana-Mkubwa, Yesu Kristo, wakati wa kuwapo kwake katika mamlaka ya Ufalme, angeaminisha daraka zaidi kuhusiana na kazi iliyotabiriwa kwa ajili ya umalizio wa huu mfumo wa mambo?—Mt. 24:3, 45-47, NW.

      Kuacha Nuru Iangaze

      Yesu aliwaagiza wanafunzi wake washiriki pamoja na wengine nuru ya kweli ya kimungu waliyokuwa wamepokea kutoka kwake. “Ninyi ni nuru ya ulimwengu,” akasema. “Nuru yenu iangaze mbele ya watu.” (Mt. 5:14-16; Mdo. 13:47) Charles Taze Russell na washirika wake walitambua kwamba walikuwa na wajibu wa kufanya hivyo.

      Je, wao waliamini kwamba walikuwa na majibu yote, ile nuru kamili ya kweli? Ndugu Russell alijibu swali hilo waziwazi hivi: “Hakika sivyo; wala hatutakuwa nayo mpaka ule ‘mchana mkamilifu.’” (Mit. 4:18) Mara nyingi walirejezea imani za Kimaandiko walizokuwa nazo kuwa “kweli ya sasa”—si wakiwa na wazo la kwamba kweli yenyewe hubadilika bali kwa wazo la kwamba uelewevu wao juu yayo ulikuwa wenye kuendelea.

      Hawa wanafunzi wa Biblia wenye moyo wa bidii hawakuepuka wazo la kwamba kuna jambo kama kweli katika mambo ya dini. Walitambua Yehova kuwa “Mungu wa kweli” na Biblia kuwa Neno lake la kweli. (Zab. 31:5; Yos. 21:45; Yn. 17:17) Walijua kwamba kulikuwa na mengi ambayo hawakujua, lakini hawakujizuia kusema kwa usadikisho yale waliyokuwa wamejifunza katika Biblia. Na wakati mafundisho na mazoea ya kidini ya kimapokeo yalipopingana na yale waliyopata yamesemwa waziwazi katika Neno la Mungu lililopuliziwa, basi, kwa kumwiga Yesu Kristo walifunua uwongo, hata ingawa kufanya hivyo kulileta dhihaka na chuki juu yao kutoka kwa makasisi.—Mt. 15:3-9.

      Ili kufikia na kulisha wengine kiroho, C. T. Russell alianza utangazaji, katika Julai 1879, wa gazeti Zions’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence.

      Biblia—Neno la Mungu Kwelikweli

      Usadikisho wa Charles Taze Russell katika Biblia haukuwa jambo la kukubali tu maoni ya kimapokeo yaliyopendwa na wengi wakati ule. Tofauti na hilo, jambo lililopendwa miongoni mwa wengi wakati ule lilikuwa uhakiki wa Biblia. Wale walioutetea walitilia shaka kutegemeka kwa maandishi ya Biblia.

      Akiwa kijana, Russell alikuwa amejiunga na Congregational Church naye alikuwa mtendaji katika kazi yalo, lakini kutopatana na akili kwa mafundisho ya kimapokeo kulimwongoza katika hali ya kutilia shaka mafundisho. Alipata kwamba yale aliyokuwa amefundishwa hayangeweza kutetewa kwa kutumia Biblia kwa njia yenye kuridhisha. Kwa hiyo akatupilia mbali mafundisho hayo ya kanisa, na pia Biblia. Halafu, alichunguza dini kuu za Mashariki, lakini hizo pia zilithibitika kuwa zisizoridhisha. Kisha akaanza kujiuliza kama labda imani za Jumuiya ya Wakristo zilikuwa zikiiwakilisha vibaya Biblia. Kwa kutiwa moyo na jambo alilosikia jioni moja kwenye mkutano wa Waadventisti, alianza kujifunza Maandiko kwa utaratibu. Yale aliyoona yakifunuka mbele yake yalikuwa kwelikweli Neno la Mungu lililopuliziwa.

      Alikuja kuvutiwa sana na upatani wa Biblia yenyewe pamoja na utu wa Yeye ambaye hutambuliwa kuwa Mtungaji wa Kimungu wayo. Ili kusaidia wengine wanufaike na jambo hilo, baadaye aliandika kitabu The Divine Plan of the Ages, ambacho alitangaza katika 1886. Katika kitabu hicho alitia ndani mazungumzo makuu juu ya “Biblia Ikiwa Ufunuo wa Kimungu Ikionwa kwa Kutumia Akili.” Kuelekea mwisho wa sura hiyo, yeye alitaarifu waziwazi hivi: “Kina na nguvu na hekima na mweneo wa ushuhuda wa Biblia hutusadikisha kwamba si binadamu, bali Mungu Mweza Yote, ndiye mtungaji wa mipango na mafunuo yayo.”

      Usadikisho katika Biblia nzima kuwa Neno la Mungu huendelea kuwa msingi wa imani za Mashahidi wa kisasa wa Yehova. Ulimwenguni pote, wana misaada ya kujifunza ambayo huwasaidia kuchunguza binafsi uthibitisho wa kupuliziwa kwayo. Pande za habari hiyo huzungumzwa mara nyingi katika magazeti yao. Katika 1969 walitangaza kitabu Is the Bible Really the Word of God? Miaka 20 baadaye kitabu Biblia—Neno la Mungu au la Binadamu? kilizungumzia tena habari ya uasilia wa Biblia, kilivuta fikira kwenye uthibitisho zaidi, na kikafikia mkataa uleule: Kwelikweli, Biblia ni Neno la Mungu lililopuliziwa. Kingine cha vitabu vyao, kilichochapwa kwanza katika 1963 na kupatanishwa na habari za karibuni zaidi katika 1990 (katika Kiingereza), ni “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa.” Habari nyingi zaidi zapatikana katika ensaiklopidia yao ya Biblia, Insight on the Scriptures, kilichotangazwa katika 1988.

      Kutokana na funzo lao la kibinafsi na la kutaniko la habari kama hizo, wao wanasadikishwa kwamba ijapokuwa wanadamu kama 40 walitumiwa kuandika yale yaliyo katika vitabu 66 vya Biblia kwa pindi ya karne 16, kwa roho yake Mungu mwenyewe alielekeza kwa bidii uandikaji huo. Mtume Paulo aliandika: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu.” (2 Tim. 3:16, NW; 2 Pet. 1:20, 21) Usadikisho huo ni jambo lenye nguvu katika maisha ya Mashahidi wa Yehova. Likitoa maelezo juu ya jambo hilo, gazeti la habari la Uingereza lilitaja hivi: “Kwa kila jambo analofanya Shahidi kuna sababu ya Kimaandiko. Kwa kweli, imani yao ya msingi ni kuitambua Biblia kuwa . . . ya kweli.”

      Kupata Kumjua Mungu wa Kweli

      Kadiri Ndugu Russell na washirika wake walivyojifunza Maandiko, haikuwachukua muda mrefu kuona kwamba Mungu aliyeonyeshwa katika Biblia siye mungu wa Jumuiya ya Wakristo. Hilo lilikuwa jambo la maana kwa sababu, kama vile Yesu Kristo alivyosema, mataraja ya watu ya uhai wa milele yalitegemea kujua kwao Mungu wa pekee wa kweli na yule aliyemtuma, Wakili Mkuu wake wa wokovu. (Yn. 17:3; Ebr. 2:10) C. T. Russell na kikundi kilichoshiriki pamoja naye katika funzo la Biblia walitambua kwamba haki ya Mungu ina usawaziko mkamilifu na hekima ya kimungu, upendo, na nguvu, na kwamba sifa hizo zinaonyeshwa katika kazi zake zote. Kwa msingi wa ujuzi waliokuwa nao wakati huo wa kusudi la Mungu, walitayarisha mazungumzo kuhusu sababu inayofanya uovu uruhusiwe na kuyatia katika kimojapo vichapo vyao vya mapema zaidi na ambacho kiligawanywa kwa wingi sana, kile kitabu cha kurasa 162 Food for Thinking Christians (Chakula kwa Wakristo Wenye Kufikiri), kilichotolewa kwanza kikiwa chapa ya pekee ya Zion’s Watch Tower katika Septemba 1881.

      Funzo lao la Neno la Mungu liliwasaidia kujua kwamba Muumba ana jina la kibinafsi na kwamba yeye hufanya iwezekane kwa wanadamu kumjua na kufurahia uhusiano wa karibu naye. (1 Nya. 28:9; Isa. 55:6; Yak. 4:8) Watch Tower la Oktoba-Novemba 1881 lilitaja wazi hivi: “YEHOVA ndilo jina litumiwalo si kwa mwingine ila kwa Mtu Mkuu Kupita Wote—Baba yetu, na yeye ambaye Yesu alimwita Baba na Mungu.”—Zab. 83:18; Yn. 20:17.

      Mwaka uliofuata, katika kujibu swali, “Je, nyinyi mwadai kwamba Biblia haifundishi kwamba kuna watu watatu katika Mungu mmoja?” jibu lililotolewa ni: “Ndiyo: Tofauti na hilo, [Biblia] hutuambia kwamba kuna Mungu mmoja na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo ambaye vitu vyote vyatoka kwake (au aliyeumba vitu vyote). Basi sisi twaamini katika Mungu na Baba Mmoja, na pia katika Bwana mmoja Yesu Kristo . . . Lakini hao ni wawili wala si mtu mmoja. Wao ni mmoja tu katika maana ya kuwa katika upatani. Sisi twaamini pia katika roho ya Mungu . . . Lakini hiyo si mtu kama vile roho ya maibilisi na roho ya Ulimwengu na roho ya Mpinga-Kristo isivyokuwa mtu.”—Zion’s Watch Tower, Juni 1882; Yn. 17:20-22.

  • Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya Kweli
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Kufichua Utatu

      Wakiwa mashahidi wa Yehova, C. T. Russell na washirika wake walihisi sana daraka la kufichua mafundisho yaliyomwakilisha Mungu vibaya, ili kusaidia wapendao kweli wajue kwamba hayo hayakuwa na msingi wa Biblia. Wao sio waliokuwa wa kwanza kutambua kwamba Utatu si wa kimaandiko,c lakini walifahamu kwamba ikiwa wangekuwa watumishi waaminifu wa Mungu, walikuwa na daraka la kujulisha kweli juu ya utatu. Kwa ujasiri, walifunua mashina ya fundisho hilo kuu la Jumuiya ya Wakristo, kwa manufaa ya wote wapendao kweli.

      Watch Tower la Juni 1882 lilitaarifu hivi: “Wanafalsafa wengi wapagani wakipata kwamba ingekuwa hekima kujiunga na orodha ya waliojiandikisha katika dini yenye kuzuka [namna fulani ya Ukristo ulioasi imani uliokubaliwa na maliki Waroma katika karne ya nne W.K.], walianza kutayarisha njia rahisi ya kuuendea kwa kujaribu kuvumbua milingano kati ya Ukristo na Upagani, na hivyo kuziunganisha zote mbili pamoja. Walifanikiwa vizuri sana. . . . Kwa kuwa ile theolojia ya kale ilikuwa na hesabu fulani ya miungu mikuu, pamoja na nusu-miungu mingi ya jinsia zote mbili, hao Wakristo-wapagani (tukiunda neno) wakaanza kutengeneza upya orodha ya theolojia hiyo mpya. Kwa hiyo, wakati huo, fundisho la Miungu watatu likabuniwa—Mungu Baba, Mungu Mwana, na Mungu Roho Mtakatifu.”

      Baadhi ya makasisi walijaribu kulipa fundisho lao ladha ya Kibiblia kwa kunukuu maandiko kama vile 1 Yohana 5:7, lakini Ndugu Russell alitoa uthibitisho wa kuonyesha kwamba ilijulikana sana na wasomi kwamba sehemu ya andiko hilo ilikuwa maneno yaliyoongezwa, maneno bandia yaliyopachikwa na mwandishi kuunga mkono fundisho lisilopatikana katika Maandiko. Wateteaji wengine wa Utatu walitumia Yohana 1:1, lakini Watch Tower lilichanganua andiko hilo kwa msingi wa yaliyomo na habari inayolizunguka kuonyesha kwamba hilo haliungi mkono kwa vyovyote imani katika Utatu. Kupatana na hilo, katika toleo lalo la Julai 1883, Watch Tower lilisema hivi: “Funzo zaidi la Biblia badala ya funzo la maandishi ya kanisa lingalifanya habari hiyo kuwa wazi zaidi kwa wote. Fundisho la utatu linapingana kabisa na Maandiko.”

      Ndugu Russell alifichua waziwazi upumbavu wa kudai kuamini Biblia na wakati uleule kufundisha fundisho kama vile Utatu, ambalo hupingana na yale ambayo Biblia husema. Hivyo aliandika hivi: “Wanajikuta wakiwa katika mapingano yenye mvurugo kama nini wale wasemao kwamba Yesu na Baba ni Mungu mmoja! Hilo lingehusisha ndani wazo la kwamba Bwana yetu Yesu alikuwa mnafiki alipokuwa duniani na alijisingizia tu kusema na Mungu katika sala, hali Yeye Mwenyewe alikuwa Mungu yuleyule. . . . Tena, sikuzote Baba amekuwa asiyeweza kufa, kwa hiyo hangeweza kufa. Basi, Yesu angaliwezaje kufa? Mitume ni mashahidi bandia wote kwa kujulisha kifo na ufufuo wa Yesu ikiwa Yeye hakufa. Hata hivyo, Maandiko hujulisha kwamba Yeye alikufa hakika.”d

      Hivyo, mapema katika historia yao ya kisasa, Mashahidi wa Yehova walikataa katakata fundisho la Utatu la Jumuiya ya Wakristo kwa kupendelea fundisho lenye kupatana na akili, lenye kuchangamsha moyo la Biblia yenyewe.e Kazi ambayo wamefanya katika kutangaza kweli hizi na kuwapa watu kila mahali fursa ya kuzisikia imekuwa ya kadiri isiyopata kufikiwa kamwe na mtu mwingine au kikundi kingine chochote, wakati uliopita au wa sasa.

      Hali ya Wafu Ni Nini?

      Tangu alipokuwa kijana, C. T. Russell alihangaikia sana hali ya wakati ujao ya wale wasiokubali uandalizi wa Mungu wa wokovu. Alipokuwa kivulana tu, yeye aliamini yale yaliyofundishwa na makasisi juu ya helo; yeye alifikiri kwamba walikuwa wakihubiri Neno la Mungu. Alikuwa akitoka nje usiku na kuandika kwa chokaa maandiko ya Biblia katika mahali yanapoweza kuonekana waziwazi ili wafanyakazi wapitao hapo waweze kuonywa na kupata kuokolewa na hukumu mbaya sana ya mateso ya milele.

      Baadaye, baada ya yeye mwenyewe kuwa amejionea yale ambayo kwa kweli Biblia hufundisha, alinukuliwa na mmoja wa washirika wake kuwa alitaarifu hivi: “Ikiwa Biblia inafundisha kwamba mateso ya milele ndiyo hukumu ya wote isipokuwa watakatifu, yapasa kuhubiriwa—naam, kwa sauti kuu ili wote wasikie, kila juma, kila siku, kila saa; ikiwa haifundishi hivyo, uhakika huo wapasa kujulishwa, na doa baya lenye kuvunjia heshima jina takatifu la Mungu liondolewe.”

      Kwenye hatua ya mapema ya funzo lake la Biblia, C. T. Russell aliona waziwazi kwamba helo (kuzimu) si mahali pa mateso ya nafsi baada ya kifo. Yaelekea sana alisaidiwa katika jambo hilo na George Storrs, mhariri wa Bible Examiner, ambaye Ndugu Russell alimtaja kwa uthamini mchangamfu katika maandishi yake na ambaye yeye mwenyewe aliandika mengi juu ya yale aliyotambua katika Biblia kuwa ndiyo hali ya wafu.

      Lakini namna gani juu ya nafsi? Je, Wanafunzi wa Biblia waliunga mkono imani ya kwamba hiyo ni sehemu ya mtu ya roho, kitu ambacho huendelea kuishi baada ya kifo cha mwili? Tofauti na hilo, katika 1903 Watch Tower lilitaarifu hivi: “Ni lazima sisi tuone kwa uangalifu kwamba somo si kwamba mtu ana nafsi, bali kwamba mtu ni nafsi, au aliyeko. Acha tutwae kielezi kutokana na asili—hewa tupumuayo: inafanyizwa kwa oksijeni na nitrojeni, hapana yoyote yazo ambayo ndiyo angahewa, au hewa; lakini zote mbili ziunganapo, kama zifanyavyo katika kiasi kifaacho cha kemikali, kitu kitokeacho ni angahewa. Ndivyo na nafsi. Mungu husema nasi kutokana na msimamo huu, wa kuwa sisi sote ni nafsi. Yeye hasemi na miili yetu wala pumzi ya uhai wetu, bali yeye husema na sisi tukiwa watu wenye akili, au nafsi. Akitangaza adhabu ya kuhalifu sheria yake, yeye hakusema na mwili wa Adamu hasa, bali na mtu, nafsi, aliyeko mwenye akili: ‘Wewe!’ ‘Katika siku ambayo wewe utakula kutokana nao wewe utakufa hakika.’ ‘Ile nafsi ambayo hufanya dhambi hiyo itakufa.’—Mwa 2:17; Eze. 18:20.” Hiyo ilipatana na yale ambayo Watch Tower lilikuwa limetaarifu mapema sana kama Aprili 1881.f

      Basi, imani katika kutokufa kulikorithiwa kwa nafsi ya kibinadamu ilisitawije? Ni nani aliyekuwa mwanzilishi wayo? Baada ya kuchunguza kwa uangalifu Biblia na pia historia ya kidini, Ndugu Russell aliandika katika Watch Tower la Aprili 15, 1894 hivi: “Kwa wazi haikutoka katika Biblia . . . Biblia hujulisha waziwazi kwamba mtu ni mwenye kufa, kwamba yeye aweza kufa. . . . Tukichunguza historia, twapata kwamba, ingawa fundisho la kutokufa kwa kibinadamu halifundishwi na mashahidi wa Mungu waliopuliziwa, ndilo msingi hasa wa dini zote za kipagani. . . . Kwa hiyo, si kweli kwamba Socrates na Plato walikuwa ndio wa kwanza kulifunza: lilikuwa na mwenye kulifunza mapema zaidi ya yeyote wao, na hata hivyo mwenye uwezo zaidi. . . . Maandishi ya kwanza ya fundisho hilo bandia yapatikana katika historia ya kale zaidi ijulikanayo kwa mwanadamu—Biblia. Mfunzi huyo bandia alikuwa Shetani.”g

      Kulielekeza “Bomba la Maji” Kwenye Helo

      Kwa kupatana na tamaa yenye nguvu ya Ndugu Russell ya kuondolea jina la Mungu doa baya lililotokana na fundisho la moto wa helo wenye mateso ya milele, yeye aliandika trakti iliyozungumzia habari, “Je, Maandiko Hufundisha Kwamba Mateso ya Milele Ndiyo Mshahara wa Dhambi?” (The Old Theology, 1889) Humo alisema hivi:

      “Nadharia ya mateso ya milele ilikuwa na chanzo cha kipagani ingawa kama ilivyoaminiwa na wapagani haikuwa fundisho lisilo la huruma kama vile ilivyopata kuwa baadaye, ilipoanza kujishikamanisha hatua kwa hatua na Ukristo wa jina tu wakati huo ulipochanganyana na falsafa za kipagani katika karne ya pili. Ilibaki juu ya uasi-imani mkubwa kubandika kwenye falsafa ya kipagani yale mambo mengi yenye kuogofya yanayoaminiwa sana sasa kwa ujumla, kuyachora kwenye kuta za makanisa, kama ilivyofanywa katika Ulaya, kuyaandika katika taarifa za imani zao na katika nyimbo zao za kidini, na kulipotoa sana Neno la Mungu ili kulipa kufuru hilo lenye kumvunjia Mungu heshima lile linaloonekana kuwa uungaji mkono wa kimungu. Kwa hiyo, ile imani ya kisasa isiyo na uthibitisho, huipokea ikiwa urithi, si kutoka kwa Bwana, wala mitume, wala manabii, bali kutoka kwa ile roho ya kuridhiana iliyodhabihu kweli na kusababu kuzuri, ikapotoa kwa njia ya aibu mafundisho ya Ukristo kwa kuwa na tamaa ya makuu isiyo takatifu na ugomvi juu ya mamlaka na mali na idadi za watu. Mateso ya milele yakiwa adhabu ya dhambi, mjeledi ambao wale wenye kuamini bila uthibitisho, wale wasiojua kitu na wenye ushirikina wa ulimwengu wamepigwa kwao ili watii ukatili kitumwa—hayakujulikana kwa wazee wa ukoo wa enzi zilizopita; hayakujulikana kwa manabii wa enzi ya Kiyahudi na hayakujulikana kwa Bwana na mitume; bali yamekuwa ndiyo fundisho kuu la Ukristo wa Jina tangu ule uasi-imani mkubwa. Mateso ya milele yalitangazwa kwa wote waliokinza au waliopuuza mamlaka ya Kanisa la Roma, na kupasishwa kwayo katika maisha haya kulianza kwa kadiri Kanisa la Roma lilivyokuwa na nguvu.”

      Ndugu Russell alifahamu sana kwamba wengi zaidi kati ya watu wenye akili hawakuamini kikweli fundisho la moto wa helo. Lakini, kama vile alivyotaja, katika 1896, katika kijitabu What Say the Scriptures About Hell?, “kwa kuwa wao hufikiri kwamba Biblia hulifundisha, kila hatua ya maendeleo wafanyayo katika akili ya kweli na fadhili ya kidugu . . . katika visa vingi zaidi ni hatua ya kwenda mbali na Neno la Mungu, ambalo wao hushtakia fundisho hilo kwa uwongo.”

      Ili kuwavuta watu kama hao wenye kufikiri warudie Neno la Mungu, yeye alitoa katika kijitabu hicho kila andiko katika King James Version ambamo neno helo lilipatikana, ili wasomaji waweze kujionea wenyewe yale ambayo hayo yalisema, na kisha akataarifu hivi: “Twashukuru Mungu, hatupati mahali kama hapo pa mateso ya milele kama inavyofundishwa kimakosa na taarifa za imani za kidini, na vitabu vya nyimbo za kidini, na mimbari. Hata hivyo tumepata ‘helo,’ sheoli, hadesi, ambamo jamii yetu yote ilihukumiwa kwenda kwa sababu ya dhambi ya Adamu, na ambamo wote watoka kwa kukombolewa na kifo cha Bwana yetu; na ‘helo’ hiyo ni ziara—hali ya kifo. Na sisi twapata ‘helo’ nyingine (gehena—kile kifo cha pili—uharibifu kabisa) iliyoletwa kwenye uangalifu wetu ikiwa adhabu ya mwisho juu ya wote ambao, baada ya kukombolewa na kuletwa kwenye ujuzi kamili wa kweli, na kwenye uwezo kamili wa kuutii, bado watachagua kifo kwa kuchagua mwendo wa kupinga Mungu na uadilifu. Na mioyo yetu yasema, Amina. Ni za haki, na za kweli, njia zako, Ee Mfalme wa mataifa. Ni nani asiyekucha, Ee Bwana na kulitukuza jina lako? Kwa kuwa wewe peke yako u mtakatifu kabisa. Na mataifa yote yatakuja na kuabudu mbele zako, kwa kuwa matendo yako ya haki yamedhihirishwa.”—Ufu. 15:3, 4.

      Aliyokuwa akifundisha yalikuwa chanzo cha udhia na aibu kwa makasisi wa Jumuiya ya Wakristo. Katika 1903 alitolewa mwito wa kushindana kwenye mjadala wa hadhara. Hali ya wafu lilikuwa mojapo masuala katika mfululizo uliotokea wa mijadala kati ya C. T. Russell na Dakt. E. L. Eaton aliyetumikia akiwa msemaji wa muungano usio rasmi wa wahudumu Waprotestanti katika sehemu ya magharibi ya Pennsylvania.

      Wakati wa mijadala hiyo Ndugu Russell alitegemeza imara hoja ya kwamba “kifo ni kifo, na kwamba wapendwa wetu, wafapo, kwa kweli wamekufa, kwamba hawako hai wala pamoja na malaika wala pamoja na roho waovu katika mahali pasipo na tumaini.” Ili kuunga mkono hilo, yeye alirejezea maandiko kama vile Mhubiri 9:5, 10; Warumi 5:12; 6:23; na Mwanzo 2:17. Yeye alisema hivi pia: “Maandiko yanapatana kabisa na yale ambayo wewe na mimi na mtu mwingine yeyote mwenye akili timamu, mwenye kusababu ifaavyo katika ulimwengu atakubali kuwa ndio utu wenye kupatana na akili na wenye kufaa wa Mungu wetu. Ni nini lijulishwalo kuhusu Baba yetu wa mbinguni? Kwamba yeye ni mwenye haki, kwamba yeye ni mwenye hekima, kwamba yeye ni mwenye upendo, kwamba yeye ni mwenye nguvu. Watu wote Wakristo watakiri sifa hizo za utu wa kimungu. Ikiwa ni hivyo, je, sisi twaweza kupata maana yoyote ya neno ambamo tungeweza kumfikiria Mungu kuwa mwenye haki na bado aadhibu kiumbe [aliyeumbwa kwa] mkono Wake kwa umilele wote, haidhuru dhambi yake ilikuwa nini? Mimi si mteteaji wa dhambi; wala siishi katika dhambi mimi mwenyewe, na mimi sihubiri dhambi kamwe. . . . Lakini nakuambia kwamba watu hawa wote waliopo hapa ambao ndugu yetu [Dakt. Eaton] asema wanasema bila staha kwa makufuru yao kwa Mungu na jina takatifu la Yesu Kristo wote ni watu ambao wamefundishwa fundisho hilo la mateso ya milele. Na wauaji-kimakusudi, wevi na watenda maovu wote waliomo gerezani, wote walifundishwa fundisho hilo. . . . Hayo ni mafundisho mabaya; yamekuwa yakidhuru ulimwengu kwa muda wote huu; hayo si sehemu ya fundisho la Bwana hata kidogo, na uwezo wa kuona wa kiroho wa ndugu yetu mpendwa ungali una giza.”

      Inaripotiwa kwamba baada ya mjadala huo, kasisi mmoja aliyehudhuria alimwendea Russell na kusema: “Naterema kuona ukielekeza bomba la maji kwenye helo na kuuzima moto huo.”

      Ili kueneza hata zaidi kweli juu ya hali ya wafu, Ndugu Russell alitumikia mfululizo wenye kuenea sana wa mikusanyiko ya siku moja, tokea 1905 kufika 1907, ambako alitoa hotuba ya watu wote, “Kwenda Helo na Kurudi! Nani Walio Humo? Tumaini la Kurudi kwa Wengi.” Kichwa hicho kiliamsha hamu, nacho kilivuta fikira sana. Wasikilizaji walijaa kabisa majumba ya kusanyiko katika majiji makubwa na madogo katika Marekani na Kanada kusikiliza hotuba hiyo.

      Miongoni mwa wale waliovutwa sana na yale ambayo Biblia husema juu ya hali ya wafu alikuwa mwanafunzi wa chuo kikuu katika Cincinnati, Ohio, aliyekuwa akijitayarisha kuwa mhudumu Mpresbiteri. Katika 1913 alipokea kutoka kwa ndugu yake kijitabu Where Are the Dead? (Wafu Wako Wapi?), kilichoandikwa na John Edgar, Mwanafunzi wa Biblia ambaye pia alikuwa daktari katika Scotland. Mwanafunzi aliyepokea kijitabu hicho alikuwa Frederick Franz. Baada ya kukisoma kwa uangalifu, alijulisha kwa uthabiti hivi: “Hii ndiyo kweli.” Bila kusita, alibadili miradi yake maishani akaingia katika huduma ya wakati wote akiwa kolpota mweneza-evanjeli. Katika 1920 akawa mshiriki wa wafanyakazi wa makao makuu ya Watch Tower Society. Miaka mingi baadaye akawa mshiriki wa Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova na, baadaye, msimamizi wa Watch Tower Society.

      Dhabihu ya Fidia ya Yesu Kristo

      Katika 1872, kuhusiana na uchunguzi wake wa Maandiko, Ndugu Russell na washirika wake walifikiria upya habari ya kurudishwa, kwa kufikiria fidia iliyotolewa na Yesu Kristo. (Mdo. 3:21, KJ) Alisisimuka alipoona kwenye Waebrania 2:9 kwamba ‘Yesu alionja mauti kwa neema ya Mungu kwa ajili ya kila mtu.’ Hilo halikumwongoza aamini katika wokovu wa kila mtu, kwa kuwa yeye alijua kwamba Maandiko husema pia kwamba lazima mtu adhihirishe imani katika Yesu Kristo ili aokolewe. (Mdo. 4:12; 16:31) Lakini alianza kufahamu—ijapokuwa si mambo yote kwa wakati uleule—fidia ya Yesu Kristo ilifanya wanadamu wapate fursa nzuri kama nini. Iliwafungulia njia wapate kile ambacho Adamu alikuwa amepoteza, taraja la uhai wa milele katika ukamilifu wa kibinadamu. Ndugu Russell hakukaa kimya juu ya jambo hilo; yeye alitambua umaana mkubwa wa fidia naye akaitegemeza kwa juhudi, hata wakati washirika wake wa karibu waliporuhusu kufikiri kwao kupotoshwe na maoni ya kifalsafa.

      Kufikia katikati ya 1878, Ndugu Russell alikuwa amekuwa, kwa mwaka mmoja na nusu hivi, mhariri-msaidizi wa gazeti Herald of the Morning, ambalo N. H. Barbour alikuwa mhariri mkuu. Lakini wakati Barbour, katika toleo la Agosti 1878 la gazeti lao, alipodharau fundisho la Kimaandiko la fidia, Russell alijibu kwa kutetea kwa juhudi kweli hiyo muhimu ya Biblia.

      Chini ya kichwa “Ule Ufuniko,” Barbour alikuwa ametoa kielezi cha jinsi alivyohisi juu ya fundisho hilo, akisema hivi: “Mimi namwambia boi wangu, au mmoja wa watumishi, James aumapo dada yake, wewe kamata inzi, uchome mwili wake kwa sindano umtundike ukutani, nami nitamsamehe James. Hiyo yatolea kielezi fundisho la kutoa kilicho badala.” Ingawa alidai kuamini katika fidia, Barbour alilirejezea kuwa “si la kimaandiko, na lenye kuchukiza sana kwa mawazo yetu yote ya haki”h lile wazo la kwamba kwa kifo chake Kristo alilipa adhabu ya dhambi kwa ajili ya uzao wa Adamu.

      Katika toleo lile hasa lililofuata la Herald of the Morning (Septemba 1878), Ndugu Russell alipinga kwa nguvu sana yale ambayo Barbour alikuwa ameandika. Russell alichanganua yale ambayo Maandiko husema kwelikweli na upatani wayo na “ukamilifu wa haki [ya Mungu], na hatimaye rehema na upendo wake mkuu” kama ulivyoonyeshwa kwa njia ya upaji wa fidia. (1 Kor. 15:3; 2 Kor. 5:18, 19; 1 Pet. 2:24; 3:18; 1 Yoh. 2:2) Kufikia masika yaliyofuata, baada ya jitihada nyingi za kusaidia Barbour aone mambo Kimaandiko, Russell aliacha kutegemeza Herald kifedha; na kuanzia toleo la Juni 1879, jina lake halikuonekana tena akiwa mhariri-msaidizi wa kichapo hicho. Msimamo wake wa ujasiri, usio wa kuridhiana kuhusiana na fundisho hilo kuu la Biblia ulikuwa na matokeo makubwa sana.

      Muda wote wa historia yao ya kisasa, Mashahidi wa Yehova wametetea daima fundisho la Kimaandiko la fidia. Toleo lilelile la kwanza la Zion’s Watch Tower (Julai 1879) lilikazia kwamba “ustahili kuelekea Mungu umo . . . katika dhabihu kamilifu ya Kristo.” Katika 1919, kwenye mkusanyiko uliodhaminiwa na International Bible Students Association huko Cedar Point, Ohio, programu iliyochapwa ilionyesha kwa njia yenye kutokeza maneno “Karibuni! Nyinyi Nyote Mwaminio Katika Ile Dhabihu Kuu ya Fidia.” Upande wa ndani wa jalada la mbele la Mnara wa Mlinzi huendelea kuvuta fikira kwenye fidia, ukisema hivi kuhusu kusudi la gazeti hilo: “Hutia moyo kuwa na imani katika Mfalme wa Mungu anayetawala sasa, Yesu Kristo, ambaye damu yake iliyomwagwa yafungulia wanadamu njia ya kupata uhai wa milele.”

      Wenye Kuendelea, Si Wenye Kufungwa na Itikadi za Kidini

      Uelewevu wa wazi wa Neno la Mungu haukuja mara hiyo. Katika visa vingi Wanafunzi wa Biblia walifahamu jambo moja katika kile kigezo cha kweli lakini hawakuelewa kila jambo. Hata hivyo, wao walikuwa tayari kujifunza. Hawakufungwa na itikadi za kidini; walikuwa wenye kuendelea. Yale waliyojifunza walishiriki na wengine. Wao hawakujisifu kwa mambo waliyofundisha; walitafuta ‘kufundishwa na Yehova.’ (Yn. 6:45, NW) Nao walikuja kuthamini kwamba Yehova huwezesha kuwa na uelewevu wa mambo madogomadogo ya kusudi lake katika wakati wake mwenyewe na katika njia yake mwenyewe.—Dan. 12:9; linganisha Yohana 16:12, 13.

      Kujifunza mambo mapya hutaka marekebisho katika maoni. Ikiwa makosa yatakubaliwa na mabadiliko yenye manufaa kufanywa, unyenyekevu wahitajiwa. Sifa hiyo na matunda yayo yatamanika kwa Yehova, na mwendo kama huo huvuta sana wapendao kweli. (Sef. 3:12) Lakini unadhihakiwa na wale ambao hujisifia itikadi za kidini ambazo zimeendelea bila kubadilika kwa karne nyingi, ingawa hizo zilifanyizwa na wanadamu wasiokamilika.

      Jinsi ya Kurudi kwa Bwana

      Ilikuwa katika miaka ya katikati ya 1870 kwamba Ndugu Russell na wale waliokuwa wakichunguza Maandiko pamoja naye walitambua kwamba Bwana arudipo angekuwa asiyeonekana kwa macho ya kibinadamu.—Yn. 14:3, 19.

      Ndugu Russell alisema hivi baadaye: “Tulihisi tumehuzunishwa sana na kosa la Waadventisti wa Pili, ambao walikuwa wakimtarajia Kristo katika mwili, na kufundisha kwamba ulimwengu na vyote vilivyomo isipokuwa Waadventisti wa Pili ungeteketezwa katika 1873 au 1874, ambao nyakati zao zilizowekwa kimbele na kukata tamaa na mawazo hafifu kwa ujumla kwa habari ya lengo na jinsi ya kuja kwake yalileta kwa kadiri fulani suto juu yetu na juu ya wale wote waliotamani sana na kupiga mbiu ya kuja kwa Ufalme wake. Maoni hayo yenye makosa yaliyoshikiliwa kwa ujumla hivyo juu ya lengo na pia jinsi ya kuja kwa Bwana yaliniongoza kuandika kijitabu—‘The Object and Manner of Our Lord’s Return.’” Kijitabu hicho kilitangazwa katika 1877. Ndugu Russell alichapisha na kugawanya nakala 50,000 zacho.

      Katika kijitabu hicho, yeye aliandika hivi: “Sisi twaamini maandiko hufundisha, kwamba, wakati wa kuja Kwake na kwa wakati fulani baada ya Yeye kuwa amekuja, Yeye ataendelea kuwa asiyeonekana; baadaye akijidhihirisha au kujionyesha Mwenyewe katika hukumu mbalimbali na namna mbalimbali, hivi kwamba ‘kila jicho litamwona Yeye.’” Katika kuunga mkono hilo, yeye alizungumzia maandiko kama vile Matendo 1:11 (‘yeye atakuja jinsi iyo hiyo mlivyomwona akienda’—yaani, bila kuonekana na ulimwengu) na Yohana 14:19, (“bado muda kidogo zaidi na ulimwengu hautaniona tena,” NW). Ndugu Russell pia alirejezea uhakika wa kwamba The Emphatic Diaglott, ambayo ilikuwa imetangazwa kwanza kwa namna kamili katika 1864 ikiwa na tafsiri ya Kiingereza ya neno kwa neno katikati ya mistari, ilitoa uthitibisho wa kwamba neno la Kigiriki pa·rou·siʹa lilimaanisha “kuwapo.” Katika kuchanganua utumizi wa Biblia wa usemi huo, Russell alieleza katika kijitabu hicho hivi: “Neno la Kigiriki litumiwalo kwa ujumla kurejezea kuja kwa pili—Parousia, litafsiriwalo mara nyingi kuja—sikuzote huonyesha kuwapo kwake mwenyewe, kuwa amekuja, amewasili na halionyeshi kamwe kuwa njiani [akija], kama vile tutumiavyo neno kuja.”

      Alipokuwa akizungumzia kusudi la kuwapo kwa Kristo, Russell alieleza wazi kwamba hilo halingekuwa jambo ambalo lingetimizwa katika kitambo kimoja cha kutikisa ulimwengu. “Kuja kwa pili, kama kule kwa kwanza,” yeye akaandika, “ni kwa kipindi cha wakati, na si tukio la kitambo.” Wakati wa pindi hiyo, akaandika, “kundi dogo” lingepewa thawabu yao pamoja na Bwana wakiwa warithi-washirika wa Ufalme wake; wengine, labda mabilioni, wangepewa fursa ya uhai mkamilifu juu ya dunia iliyorudishwa kwenye uzuri wa Edeni.—Luka 12:32.

      Katika muda wa miaka michache tu, kwa msingi wa funzo zaidi la Maandiko, Russell alitambua kwamba Kristo hangerudi bila kuonekana tu bali pia angeendelea kuwa asiyeonekana, hata wakati adhihirishapo kuwapo kwake kwa hukumu juu ya waovu.

      Katika 1876, Russell alipokuwa amesoma kwa mara ya kwanza nakala ya Herald of the Morning, alikuwa amejifunza kwamba kulikuwa kikundi kingine ambacho wakati huo kiliamini kwamba kurudi kwa Kristo kungekuwa kusikoonekana na ambacho kilishirikisha kurudi huko na baraka kwa ajili ya familia zote za dunia. Kutokana na Bw. Barbour, mhariri wa kichapo hicho, Russell akaja pia kushawishwa kwamba kuwapo kusikoonekana kwa Kristo kulikuwa kumeanza katika 1874.i Fikira zilivutwa baadaye kwenye jambo hilo kwa kichwa kidogo “Mpiga-Mbiu wa Kuwapo kwa Kristo,” kilichoonekana juu ya jalada la Zion’s Watch Tower.

      Utambuzi wa kwamba kuwapo kwa Kristo ni kwa kutoonekana ukawa msingi wa maana ambao juu yao uelewevu wa unabii mwingi wa Biblia ungejengwa. Hao Wanafunzi wa Biblia wa mapema walitambua kwamba kuwapo kwa Bwana kwapaswa kuwa hangaikio la kwanza la Wakristo wote wa kweli. (Mk. 13:33-37) Walipendezwa sana na kurudi kwa Bwana-Mkubwa na walikuwa chonjo kuona uhakika wa kwamba walikuwa na daraka la kukutangaza, lakini walikuwa hawajatambua mambo yote madogomadogo. Hata hivyo, yale ambayo roho ya Mungu iliwawezesha kuelewa tangu wakati wa mapema sana yalikuwa yenye kutokeza kwelikweli. Mojapo kweli hizo ilihusu ile tarehe ya maana sana iliyoonyeshwa na unabii wa Biblia.

      Mwisho wa Nyakati za Mataifa

      Kwa muda mrefu habari ya kronolojia ya Biblia ilikuwa imewavutia sana wanafunzi wa Biblia. Waelezaji walikuwa wameonyesha maoni mbalimbali juu ya unabii wa Yesu kuhusu “nyakati za Mataifa” na maandishi ya Danieli juu ya ndoto ya Nebukadreza kuhusu kile kisiki cha mti kilichofungwa kwa pingu muda wa “nyakati saba.”—Luka 21:24, KJ; Dan. 4:10-17.

      Mapema kama 1823, John A. Brown, ambaye kitabu chake kilitangazwa katika London, Uingereza, alihesabu zile “nyakati saba” za Danieli sura ya 4 kuwa zenye urefu wa miaka 2,520. Lakini yeye hakutambua waziwazi tarehe ambayo kipindi hicho cha wakati wa kiunabii kilianza au wakati kingekoma. Hata hivyo, yeye alihusianisha hizo “nyakati saba” na Nyakati za Mataifa za Luka 21:24. Katika 1844, E. B. Elliott, kasisi Mwingereza, alivuta uangalifu kwenye 1914 kuwa tarehe iwezekanayo kuwa ukomo wa “nyakati saba” za Danieli, lakini yeye alionyesha pia maoni tofauti yaliyoelekeza kwenye wakati wa Mapinduzi ya Ufaransa. Robert Seeley, wa Uingereza, katika 1849, alishughulikia habari hiyo kwa njia iyo hiyo. Angalau kufikia 1870, kichapo kilichohaririwa na Joseph Seiss na washiriki wake na kuchapwa katika Philadelphia, Pennsylvania, kilikuwa kikionyesha hesabu ambazo zilielekeza kwenye 1914 kuwa tarehe ya maana, hata ingawa sababu kiliyotoa ilitegemea kronolojia ambayo C. T. Russell alikataa baadaye.

      Halafu, katika matoleo ya Agosti, Septemba, na Oktoba 1875 ya Herald of the Morning, N. H. Barbour alisaidia kupatanisha mambo madogomadogo ambayo yalikuwa yameonyeshwa na wengine. Akitumia kronolojia iliyotungwa na Christopher Bowen, ambaye ni kasisi katika Uingereza, na kutangazwa na E. B. Elliott, Barbour alihusianisha mwanzo wa Nyakati za Mataifa na kuondolewa kwa Mfalme Sedekia kutoka kwenye ufalme wake kama ilivyotabiriwa kwenye Ezekieli 21:25, 26, akaelekeza kwenye 1914 kuwa waonyesha mwisho wa Nyakati za Mataifa.

      Mapema katika 1876, C. T. Russell alipokea nakala moja ya Herald of the Morning. Mara hiyo yeye aliandikia Barbour kisha akatumia wakati pamoja naye katika Philadelphia wakati wa kiangazi, wakizungumzia, miongoni mwa mambo mengine, vipindi vya wakati wa kiunabii. Muda mfupi baada ya hapo, katika makala moja yenye kichwa “Nyakati za Mataifa: Zakoma Wakati Gani?,” Russell pia alitoa sababu juu ya habari hiyo kwa kutumia Maandiko akataarifu kwamba uthibitisho ulionyesha kwamba “nyakati saba zitakoma katika A.D. 1914.” Makala hiyo ilichapwa katika toleo la Oktoba 1876 la Bible Examiner.j Kile kitabu Three Worlds, and the Harvest of This World, kilichotokezwa katika 1877 na N. H. Barbour kwa kushirikiana na C. T. Russell, kilielekeza kwenye mkataa huohuo. Baada ya hapo, matoleo ya mapema ya Watch Tower, kama yale ya tarehe ya Desemba 1879 na Julai 1880, yalivuta fikira kwenye 1914 W.K. kuwa mwaka wa maana sana kwa maoni ya unabii wa Biblia. Katika 1889 sura nzima ya nne ya Buku 2 la Millennial Dawn (baadaye liliitwa Studies in the Scriptures) ilitumiwa kuzungumzia “Nyakati za Mataifa.” Lakini ukomo wa Nyakati za Mataifa ungemaanisha nini?

      Hawa Wanafunzi wa Biblia hawakuwa na uhakika kabisa ni jambo gani lingetukia. Walisadikishwa kwamba tokeo halingekuwa kuteketezwa kwa dunia na kufutiliwa mbali kwa uhai wa kibinadamu. Badala ya hivyo, walijua kwamba ingeonyesha hatua yenye maana katika utawala wa kimungu. Mwanzoni, walifikiri kwamba kufikia tarehe hiyo Ufalme wa Mungu ungekuwa umepata udhibiti kamili, wa ulimwengu wote mzima. Wakati jambo hilo halikutukia, uhakika wao katika unabii mbalimbali wa Biblia ulioonyesha tarehe hiyo haukuyumbayumba. Walifikia mkataa kwamba, badala ya hivyo, tarehe hiyo ilionyesha tu mwanzo kwa habari ya utawala wa Ufalme.

      Hali kadhalika, mwanzoni walifikiri pia kwamba taabu za duniani pote zikifikia upeo katika machafuko ya utawala (ambayo walielewa kwamba yangeshirikishwa na vita ya “siku kubwa ya Mungu Mweza-Yote”) yangetangulia tarehe hiyo. (Ufu. 16:14, NW) Lakini, miaka kumi kabla ya 1914, Watch Tower lilidokeza kwamba msukosuko wa ulimwenguni pote ambao ungetokeza kuangamizwa kwa mipango yote ya kibinadamu ungekuja mara tu baada ya mwisho wa Nyakati za Mataifa. Walitarajia mwaka 1914 ulete badiliko kubwa kwa Yerusalemu, kwa kuwa unabii ulikuwa umesema kwamba ‘Yerusalemu ungekanyagwa’ mpaka Nyakati za Mataifa zitimie. Walipoona 1914 ukikaribia na bado hawakuwa wamekufa wakiwa wanadamu na ‘kunyakuliwa katika mawingu’ wamlaki Bwana—kupatana na matarajio ya mapema—walitumaini sana kwamba badiliko lao lingetukia mwishoni mwa Nyakati za Mataifa.—1 The. 4:17.

      Kadiri miaka ilivyopita nao wakachunguza na kuchunguza tena Maandiko, imani yao katika unabii mbalimbali iliendelea kuwa yenye nguvu, nao hawakusita kutaarifu yale waliyotarajia yangetukia. Kwa mafanikio ya kiwango mbalimbali, walijaribu kuepuka kushikilia bila uthibitisho mambo madogomadogo ambayo hayakutajwa moja kwa moja katika Maandiko.

      Je, “Kengele ya Saa” Ililia Mapema Mno?

      Bila shaka msukosuko mkubwa ulikumba ulimwengu katika 1914 kwa kufyatuka kwa Vita ya Ulimwengu 1, ambayo kwa miaka mingi iliitwa tu ile Vita Kuu, lakini haikuongoza mara hiyo kwenye kupinduliwa kwa tawala zote za kibinadamu zilizokuwako. Kadiri matukio kuhusiana na Palestina yalivyositawi kufuatia 1914, Wanafunzi wa Biblia walifikiri kwamba waliona uthibitisho wa mabadiliko ya maana kwa ajili ya Israeli. Lakini kadiri miezi na kisha miaka ilivyopita, Wanafunzi wa Biblia hawakupokea thawabu yao ya kimbingu, kama walivyokuwa wametarajia. Waliitikiaje jambo hilo?

      The Watch Tower la Februari 1, 1916, lilivuta fikira hususa kwenye Oktoba 1, 1914, kisha likasema: “Hiyo ilikuwa ndiyo hatua ya mwisho ya wakati ambayo kronolojia ya Biblia ilielekeza kwetu kuwa ilihusiana na mambo ambayo yangelipata Kanisa la Katoliki ya Roma. Je, Bwana alituambia kwamba tungechukuliwa huko [mbinguni]? Hapana. Yeye alisema nini? Neno lake na matimizo ya unabii yalionekana yakielekeza bila kukosea kwamba tarehe hiyo ilionyesha mwisho wa Nyakati za Mataifa. Sisi tuliamua kutokana na hilo kwamba ‘badiliko’ la Kanisa lingetukia katika au kabla ya tarehe hiyo. Lakini Mungu hakutuambia kwamba ingekuwa hivyo. Yeye alituruhusu tufikie uamuzi huo; nasi tunaamini kwamba umethibitika kuwa mtihani uliohitajiwa juu ya watakatifu wapendwa wa Mungu kila mahali.” Lakini je, matukio hayo yalithibitisha kwamba tumaini lao tukufu lilikuwa limekuwa la bure? Hapana. Ilimaanisha tu kwamba si kila kitu kilikuwa kikitukia upesi kama walivyokuwa wametarajia.

      Miaka kadhaa kabla ya 1914, Russell alikuwa ameandika hivi: “Kwa wazi kronolojia (unabii wa wakati kwa ujumla) haikukusudiwa kuwapa watu wa Mungu habari sahihi ya kronolojia muda wa karne zote. Kwa wazi ilikusudiwa zaidi itumike kama kengele ya saa iwaamshe na kuwatia nishati watu wa Bwana katika wakati ufaao. . . . Lakini tuseme, mathalani, kwamba Oktoba, 1914, ungepita na kusitukie anguko kubwa la serikali za Mataifa. Hilo lingethibitisha au lisingethibitisha nini? Lisingeondoa uthibitisho wa sehemu yoyote ya Mpango wa Kimungu wa Zile Enzi. Bei ya fidia iliyokamilishwa huko Kalvari bado ingekuwa uthibitisho wa utimizo wa mwisho wa Programu ya Kimungu iliyo kubwa kwa ajili ya rudisho la wanadamu. Ule ‘mwito wa juu’ wa Kanisa lipate kuteseka pamoja na Mkombozi na kutukuzwa pamoja naye likiwa washiriki wake au likiwa Bibi-Arusi wake bado ungekuwa vile vile. . . . Jambo pekee lililoathiriwa na kronolojia lingekuwa wakati wa kutimizwa kwa matumaini hayo matukufu kwa ajili ya Kanisa na kwa ajili ya ulimwengu. . . . Na tarehe hiyo ikipita ingethibitisha tu kwamba kronolojia yetu, ‘kengele ya saa’ yetu, ililia mapema kidogo kabla ya wakati. Je, sisi tungefikiri kwamba ni msiba mkuu ikiwa kengele ya saa yetu ingetuamsha nukta chache mapema zaidi asubuhi ya siku fulani kuu yenye kujawa na shangwe na furaha? Hakika sivyo!”

      Lakini hiyo “kengele ya saa” haikuwa imelia mapema mno. Kwa kweli, mambo waliyoona ambayo “saa” ilikuwa imewaamsha ndiyo hayakuwa mambo barabara waliyokuwa wametarajia.

      Miaka fulani baadaye, wakati nuru ilipokuwa imekuwa nyangavu zaidi, wao walikiri hivi: “Walio wengi kati ya watakatifu hao wapendwa walifikiri kwamba kazi yote ilikuwa imefanywa. . . . Walishangilia kwa sababu ya uthibitisho ulio wazi kwamba ulimwengu ulikuwa umekwisha, kwamba ufalme wa mbingu ulikuwa umekaribia, na kwamba siku ya ukombozi wao ilikaribia. Lakini walikuwa wamekosa kuona jambo jingine ambalo lazima lifanywe. Habari njema ambazo walikuwa wamepokea lazima wangeambia wengine; kwa sababu Yesu alikuwa ameamuru: ‘Habari njema ya ufalme itahubiriwa katika ulimwengu wote, kuwa ushuhuda kwa mataifa yote; hapo ndipo ule mwisho utakapokuja.’ (Mathayo 24:14)”—The Watch Tower, Mei 1, 1925.

      Kadiri matukio yaliyofuata 1914 yalivyoanza kufunuka, nao Wanafunzi wa Biblia wakayalinganisha na yale ambayo Bwana-Mkubwa alikuwa ametabiri, walikuja kuthamini hatua kwa hatua kwamba walikuwa wakiishi katika siku za mwisho za mfumo wa kale na kwamba zilianza 1914. Pia walikuja kuelewa kwamba katika mwaka 1914 ndipo kuwapo kusikoonekana kwa Kristo kulipokuwa kumeanza na kwamba, huko hakukuwa katika maana ya kurudi kwake binafsi (hata kwa kutoonekana) kwenye ujirani wa dunia, bali kwa kuelekeza uangalifu wake kwenye dunia akiwa Mfalme anayetawala. Waliona nao wakakubali daraka muhimu lililokuwa lao la kupiga mbiu ya hii “habari njema ya ufalme” kwa ajili ya ushahidi kwa mataifa yote katika huu wakati wa hatari wa historia ya kibinadamu.—Mt. 24:3-14.

      Ujumbe ambao wangehubiri juu ya Ufalme ungekuwa nini hasa? Je, ulikuwa tofauti na ujumbe wa Wakristo wa karne ya kwanza?

      Ufalme wa Mungu, Tumaini Pekee la Wanadamu

      Kama tokeo la funzo la uangalifu la Neno la Mungu, Wanafunzi wa Biblia walioshirikiana na Ndugu Russell walielewa kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali ambayo Yehova aliahidi kusimamisha kwa njia ya Mwanae ili kubariki wanadamu. Yesu Kristo, akiwa mbinguni, angekuwa na washirika pamoja naye wakiwa watawala, “kundi dogo” lililoteuliwa na Mungu kutoka miongoni mwa wanadamu. Walielewa kwamba serikali hiyo ingewakilishwa na wanaume waaminifu wa kale ambao wangetumikia wakiwa wakuu katika dunia yote. Hao walirejezewa kuwa “wakuu wa kale.”—Luka 12:32; Dan. 7:27; Ufu. 20:6; Zab. 45:16.

      Kwa muda mrefu Jumuiya ya Wakristo ilikuwa imefundisha nadharia ya kwamba ‘wenye kumiliki hupokea haki ya kuwa wafalme kutoka kwa Mungu,’ kuwa njia ya kufanya watu watii. Lakini hao Wanafunzi wa Biblia waliona kutoka Maandiko kwamba wakati ujao wa serikali za kibinadamu haukufanywa salama na uhakikisho wowote wa kimungu. Kupatana na yale waliyokuwa wakijifunza, Watch Tower la Desemba 1881 lilitaarifu: “Bila shaka kusimamishwa kwa ufalme huu, kutahusisha kupinduliwa kwa falme zote za dunia, kwa kuwa zote—hata zile bora kati yazo—zimetegemezwa juu ya utovu wa haki na haki zisizo sawa na uonevu wa wengi na kupendelea wachache—kama tusomavyo: ‘Utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.’”—Dan. 2:44.

      Kwa habari ya njia ambayo falme hizo zenye uonevu zingevunjwavunjwa, hao Wanafunzi wa Biblia bado walikuwa na mengi ya kujifunza. Bado wao hawakuelewa waziwazi jinsi manufaa za Ufalme wa Mungu zingeenea kwa wanadamu wote. Lakini wao hawakuchanganyikiwa juu ya Ufalme wa Mungu wakifikiri kwamba ulikuwa hisi isiyoeleweka iliyo ndani ya moyo wa mtu au kuwa ndio ule utawala wa viongozi wa kidini uliotumia Serikali ya kilimwengu kuwa mkono wayo.

      Kufikia 1914, watumishi waaminifu wa Mungu wa nyakati za kabla ya Ukristo hawakuwa wamefufuliwa duniani wakiwa wakuu wenye kuwakilisha Mfalme wa Kimesiya, kama ilivyokuwa imetarajiwa, wala wabakio wa “kundi dogo” hawakuwa wamejiunga na Kristo katika Ufalme wa kimbingu katika mwaka huo. Hata hivyo The Watch Tower la Februari 15, 1915, lilitaarifu kwa uhakika kwamba 1914 ulikuwa ndio wakati uliowekwa “wa Bwana wetu kutwaa uweza Wake mkuu na kuanza kutawala,” hivyo kumaliza zile mileani nyingi za utawala usiokatizwa wa Mataifa.

  • Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya Kweli
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Vita ya Ile Siku Kubwa ya Mungu Mweza Yote

      Ile vita ya ulimwengu iliyoanza katika 1914 ilitikisa mfumo wa mambo ulioko hadi kwenye misingi yao. Kwa wakati fulani ilionekana kana kwamba matukio yangesonga mbele kama vile Wanafunzi wa Biblia walivyokuwa wametarajia.

      Huko nyuma katika Agosti 1880, Ndugu Russell alikuwa ameandika hivi: “Sisi twaelewa kwamba kabla familia ya kibinadamu haijarudishwa au hata kuanza kubarikiwa, serikali za dunia ambazo sasa hufunga na kuonea wanadamu zitapinduliwa zote na kwamba ufalme wa Mungu utatwaa udhibiti na kwamba baraka na rudisho zitakuja kupitia huo ufalme mpya.” ‘Kupinduliwa kwa falme’ kungetukiaje? Akitegemea hali ambazo angeweza kuona wakati ule zikitukia katika ulimwengu, Russell aliamini kwamba wakati wa vita ya Har–Magedoni, Mungu angetumia vikundi vyenye kuzozana vya wanadamu kupindua mipango iliyoko. Alisema hivi: “Kazi ya kubomoa milki ya kibinadamu inaanza. Mamlaka itakayozipindua inatenda kazi sasa. Tayari watu wanapanga majeshi yao chini ya jina la Wakomunisti, Wasosholisti, na Wanamapinduzi, n.k.”

      Kitabu The Day of Vengeance (baadaye kiliitwa The Battle of Armageddon), kilichotangazwa katika 1897, kiliongeza habari zaidi juu ya njia ambayo Wanafunzi wa Biblia wakati ule walielewa jambo hilo, kikisema hivi: “Bwana, kwa maongozi yake ya kimungu yenye kushinda, atatwaa uongozi wa ujumla wa jeshi hili kubwa la wasioridhika—wazalendo, warekebishaji, wasosholisti, wateteaji-maadili, wanamachafuko, wajinga na wasio na tumaini—na kutumia matumaini yao, hofu, upumbavu na ubinafsi, kulingana na hekima yake ya kimungu, kutimiza makusudi yake mwenyewe makuu katika kupindua mipango ya sasa, na katika kutayarisha binadamu kwa ajili ya Ufalme wa Uadilifu.” Hivyo wao walielewa kwamba vita ya Har–Magedoni ingeshirikishwa na mapinduzi ya kijamii yenye jeuri.

  • Kukua Katika Ujuzi Sahihi Juu ya Kweli
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Sanduku katika ukurasa wa 126]

      ‘Je, Sisi Tutampinganisha Kristo Mwenyewe?’

      Baada ya kufichua kutopatana na maandiko na kutopatana na kufikiri kiakili kwa fundisho la Utatu, C. T. Russell alionyesha ghadhabu yenye uadilifu alipouliza hivi: “Je, hivyo sisi tutapinganisha Mitume na Manabii na Yesu Mwenyewe, na kupuuza kufikiri kiakili na busara, ili tushike fundisho lililopokezwa kwetu na Kanisa fisadi lililoasi imani kutoka ule wakati wa giza, wa ushirikina uliopita? Hasha! ‘Kwa Sheria na ushuhuda! Wasiposema kulingana na Neno hili, ni kwa sababu hamna nuru ndani yao.’”—“The Watch Tower,” Agosti 15, 1915.

      [Sanduku katika ukurasa wa 133]

      Kweli Yenye Kuendelea

      Katika 1882, C. T. Russell aliandika hivi: “Biblia ndiyo kiwango chetu pekee, na mafundisho yayo ni itikadi yetu pekee ya kidini, na kwa kutambua hali yenye kuendelea ya kufunguka kwa kweli za Kimaandiko, sisi tuko tayari na tumejitayarisha kuongeza au kurekebisha itikadi yetu ya kidini (imani) kadiri tupatavyo ongezeko la nuru kutoka katika Kiwango chetu.” —“Watch Tower,” Aprili 1882, uku. 7.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki