Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kutokeza Fasihi za Biblia Ili Zitumiwe Katika Huduma
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Kwa hiyo, katika 1879 wakati Russell alipoanza kuchapa Zion’s Watch Tower and Herald of Christ’s Presence, alilazimika kutegemea wachapaji wa kibiashara.

      Mwaka uliofuata, trakti za kwanza kati ya mfululizo mwingi wa trakti zilizobuniwa ili kuwavutia watu na kweli za Biblia zilitayarishwa ili zichapwe. Upesi kazi hiyo ikawa ya kadiri kubwa. Ili kuishughulikia, Zion’s Watch Tower Tract Society ilifanyizwa mnamo Februari 16, 1881, W. H. Conley akiwa msimamizi na C. T. Russell akiwa katibu na mweka-hazina. Mipango ilifanywa ili mashirika ya kibiashara yaweze kuchapa katika majiji mbalimbali ya Pennsylvania, New York, na Ohio, kutia na Uingereza. Katika 1884, Zion’s Watch Tower Tract Societya ilianzishwa kihalali, C. T. Russell akiwa msimamizi, na mkataba wayo ulionyesha kwamba ilikuwa sosaiti ambayo ingefanya zaidi ya kuelekeza uchapaji. Kusudi layo halisi lilikuwa la kidini; lilianzishwa “ili kueneza Kweli za Biblia katika lugha mbalimbali.”

      Kusudi hilo lilifuatiliwa kwa bidii iliyoje, Katika 1881, katika muda wa miezi minne, trakti 1,200,000 zenye jumla ya kurasa 200,000,000 zilichapwa. (“Trakti” nyingi zilikuwa hasa kwa namna ya vitabu vidogo.) Baadaye, kutokezwa kwa trakti za Biblia kwa ajili ya kugawanywa bure kuliongezeka kufikia makumi ya mamilioni mwaka baada ya mwaka. Trakti hizo zilichapwa katika lugha 30 na kugawanywa si katika Amerika tu, bali pia katika Ulaya, Afrika Kusini, Australia, na nchi nyinginezo.

      Jambo jingine la kazi hiyo lilianza katika 1886, wakati Ndugu Russell alipomaliza kuandika kitabu The Divine Plan of the Ages, buku la kwanza kati ya mfululizo wa mabuku sita ambayo yeye binafsi aliandika. Kuhusiana na kutangazwa kwa mabuku ya kwanza manne katika mfululizo huo (1886-1897), pamoja na trakti na Watch Tower kuanzia 1887 hadi 1898, alitumia Tower Publishing Company.b Baadaye, kupanga chapa na kutunga kulifanywa na akina ndugu kwenye Bible House katika Pittsburgh. Ili kupunguza gharama, walinunua karatasi ya kuchapa pia. Mara nyingi Ndugu Russell alipeleka maagizo kwa mashirika zaidi ya moja ili hasa yachape na kujalidi. Alipanga kwa uangalifu, akiagiza kimbele vitabu vingi vya kutosha ili avipate kwa bei ya chini. Kuanzia wakati wa kuchapwa kwa kitabu cha kwanza kilichoandikwa na C. T. Russell kufikia 1916, mabuku sita yaliyojumlika kuwa 9,384,000 yalitokezwa na kugawanywa.

      Kuchapa fasihi za Biblia hakukukoma baada ya kifo cha Ndugu Russell. Mwaka uliofuata, buku la saba la Studies in the Scriptures lilichapwa. Lilitolewa kwa familia ya Betheli mnamo Julai 17, 1917. Uhitaji wacho ulikuwa mwingi sana hivi kwamba kufikia mwisho wa mwaka huo, Sosaiti ilikuwa imetoa maagizo ya nakala 850,000 katika Kiingereza na wachapaji na wajalidi wa kibiashara. Chapa katika lugha nyinginezo zilikuwa zikitolewa katika Ulaya. Kwa kuongezea, mwaka huo trakti karibu milioni 38 zilichapwa.

      Lakini, wakati wa kipindi cha mnyanyaso mwingi katika 1918, huku maofisa wa Sosaiti wakiwa wamefungwa isivyo haki, makao yao makuu (yaliyoko Brooklyn, New York) yalibomolewa. Mabamba ya kuchapia yaliharibiwa. Wafanyakazi waliopungua sana walihamisha ofisi kurudi Pittsburgh kwenye orofa ya tatu ya jengo moja katika 119 Federal Street. Je, hilo lingewazuia kutokeza fasihi za Biblia?

      Je, Wapaswa Wafanye Uchapaji Wao Wenyewe?

      Baada ya kuachiliwa kwa msimamizi wa Sosaiti, J. F. Rutherford, na washiriki wake kutoka gerezani, Wanafunzi wa Biblia walikusanyika katika Cedar Point, Ohio, katika 1919. Walifikiria yale ambayo Mungu alikuwa ameruhusu yatukie wakati wa mwaka uliotangulia na yale ambayo Neno lake lilionyesha kwamba wanapaswa kuwa wakifanya wakati wa siku zilizokuwa mbele. Tangazo lilitolewa kwamba gazeti jipya, The Golden Age, lingechapwa likiwa chombo cha kutumia katika kuelekeza watu kwa Ufalme wa Mungu ukiwa tumaini pekee la wanadamu.

      Kama ilivyokuwa imefanya zamani, Sosaiti ilipanga ili mashirika ya kibiashara yachape. Lakini nyakati zilikuwa zimebadilika. Kulikuwa na matatizo ya wafanyakazi katika shughuli ya uchapaji na matatizo katika soko la karatasi. Mpango wenye kutegemeka zaidi ulihitajiwa. Ndugu walisali juu ya jambo hilo na wakawa macho kuona maelekezo ya Bwana.

      Kwanza, wangepaswa waweke wapi ofisi za Sosaiti? Je, wangepaswa kuhamisha makao makuu kurudi Brooklyn? Baraza la waelekezi la Sosaiti ilifikiria juu ya jambo hilo, na halmashauri iliteuliwa ili ichunguze hali hiyo.

      Ndugu Rutherford aliagiza C. A. Wise, makamu wa msimamizi wa Sosaiti, aende Brooklyn aone kama Betheli ingefunguliwa tena na kukodisha mahali ambapo Sosaiti ingeanza shughuli za uchapaji. Akiwa na tamaa ya kujua ni mwendo upi Mungu angebariki, Ndugu Rutherford alisema: “Nenda ukaone ikiwa ni mapenzi ya Bwana turudi Brooklyn.”

      “Nitajuaje ikiwa ni mapenzi ya Bwana tuweze kurudi au la?” akauliza Ndugu Wise.

      “Kushindwa kupata makaa-mawe katika 1918 ndiko kulikotulazimisha tuhame kutoka Brooklyn turudi Pittsburgh,”c Ndugu Rutherford akajibu. “Acha tufanye makaa-mawe yawe ndiyo jaribio. Wewe nenda ukaagize makaa-mawe.”

      “Unafikiri ninapaswa kuagiza tani ngapi ili kufanya jaribio hilo?”

      “Lifanye liwe jaribio linalofaa,” Ndugu Rutherford akapendekeza. “Agiza tani 500.”

      Hivyo ndivyo Ndugu Wise alivyofanya barabara. Na tokeo lilikuwa nini? Alipopeleka maombi kwa wenye mamlaka, alipewa hati ya kupata makaa-mawe tani 500—ya kutosha kutimiza mahitaji yao kwa miaka kadhaa! Lakini wangeiweka wapi? Sehemu kubwa za orofa ya chini ya Kao la Betheli ziligeuzwa kuwa maghala ya makaa-mawe.

      Matokeo ya jaribio hilo yalichukuliwa kuwa ishara ya mapenzi ya Mungu. Kufikia mwanzo wa Oktoba 1919, kwa mara nyingine tena walikuwa wakianza kuendeleza utendaji wao wakiwa Brooklyn.

      Sasa, je, wanapaswa wafanye uchapaji wao wenyewe? Walijitahidi kununua matbaa-mabamba-mviringo ya kuchapa magazeti lakini waliambiwa kwamba kulikuwa na chache tu katika Marekani na kwamba kulikuwa hakuna uwezekano wa kupata moja kwa miezi mingi. Hata hivyo, walikuwa na uhakika kwamba ikiwa yalikuwa mapenzi ya Bwana, angeweza kufungua njia. Na alifanya hivyo!

      Miezi michache tu baada ya wao kurudi Brooklyn, waliweza kununua matbaa-mabamba-mviringo. Walikodisha orofa tatu katika jengo moja lililokuwa umbali wa majengo manane kutoka Kao la Betheli, kwenye 35 Myrtle Avenue. Kufikia mapema 1920 Sosaiti ilikuwa na kiwanda chayo cha kuchapisha—kidogo, lakini chenye vifaa vingi. Ndugu waliokuwa na ujuzi wa kutosha kuendesha vifaa hivyo walijitoa wenyewe ili kusaidia katika kazi hiyo.

      Toleo la Februari 1 la The Watch Tower mwaka huo lilichapwa kwa matbaa ya Sosaiti. Kufikia Aprili, The Golden Age pia lilikuwa likitolewa kwa matbaa yao wenyewe. Kufikia mwisho wa mwaka huo, ilikuwa furaha kwa The Watch Tower kuripoti: “Wakati wa sehemu kubwa ya mwaka kazi yote ya THE WATCH TOWER, THE GOLDEN AGE, na vijitabu vingi, ilikuwa imefanywa na mikono iliyojitakasa, lakini kusudi moja ndilo lililoelekeza vitendo vyao, na kusudi hilo ni kumpenda Bwana na kusudi lake la uadilifu. . . . Majarida mengine na vichapo yalipotakiwa kukoma kwa sababu ya upungufu wa karatasi au matatizo ya wafanyakazi, vichapo vyetu viliendelea kutokezwa bila tatizo.”

      Nafasi kwenye kiwanda ilikuwa ndogo sana, lakini kiasi cha kazi kilichofanywa kilistaajabisha. Kiasi cha The Watch Tower kilichochapwa kilikuwa nakala 60,000 kwa kila toleo. Lakini The Golden Age lilichapwa huko pia, na katika mwaka wa kwanza, toleo la Septemba 29 lilikuwa la pekee. Lilikuwa na habari nyingi juu ya kufunuliwa kwa wachochezi wa mnyanyaso dhidi ya Wanafunzi wa Biblia kuanzia 1917 hadi 1920. Nakala milioni nne zilichapwa! Mmojawapo wafanyakazi wa matbaa ya kiwanda alisema hivi baadaye: ‘Kila mtu isipokuwa mpishi alitumikia ili kutokeza toleo hilo.’

      Katika mwaka wao wa kwanza wa kutumia matbaa-mabamba-mviringo ya kuchapa magazeti, Ndugu Rutherford aliomba akina ndugu ikiwa wangeweza pia kuchapa vijitabu kwa matbaa hiyo. Mwanzoni, haikuonekana kuwa yawezekana. Wafanyakazi wa matbaa hiyo walisema kwamba haingewezekana. Lakini akina ndugu walijaribu na wakapata matokeo mazuri. Pia walifanyiza mashine yao wenyewe ya kukunja na hivyo wakapunguza uhitaji wa wafanyakazi katika sehemu hiyo ya kazi kutoka 12 hadi 2. Ni nini kilichowafanikisha? “Ujuzi na baraka ya Bwana” ndivyo msimamizi wa kiwanda alivyokata kauli.

      Hata hivyo, haikuwa katika Brooklyn pekee kwamba Sosaiti ilikuwa ikianzisha shughuli za uchapaji. Baadhi za shughuli za uchapaji katika lugha za kigeni zilisimamiwa na ofisi katika Michigan. Ili kushughulikia mahitaji yaliyohusiana na kazi hiyo, Sosaiti ilipeleka mashine ya Linotaipu, matbaa za kuchapa, na vifaa vingine vilivyohitajika katika Detroit, Michigan katika 1921. Huko fasihi zilichapwa katika Kipoland, Kirusi, Kiukrainia, na lugha nyinginezo.

      Katika mwaka uo huo, Sosaiti ilitoa kitabu The Harp of God, kilichoandikwa kwa njia inayofaa wale wanaoanza kujifunza Biblia. Kufikia 1921 Sosaiti haikuwa imejaribu kuchapa na kujalidi vitabu vyayo yenyewe. Je, wangepaswa kujitahidi kuanza kazi hiyo pia? Kwa mara nyingine, walitafuta mwelekezo wa Bwana.

      Ndugu Waliojitoa Wachapa na Kujalidi Vitabu

      Katika 1920, The Watch Tower lilikuwa limeripoti kwamba makolpota wengi walikuwa wamelazimika kuacha utumishi huo kwa sababu wachapaji na wajalidi wa vitabu walishindwa kufanyiza vitabu vilivyoagizwa na Sosaiti. Akina ndugu kwenye makao makuu walitoa sababu kwamba ikiwa hawangewategemea watengenezaji wa kibiashara wenye matatizo mengi ya kazi, wangetimiza ushahidi mwingi zaidi kuhusu makusudi ya Mungu kwa wanadamu. Ikiwa wangechapa na kujalidi vitabu vyao wenyewe, ingekuwa pia vigumu zaidi kwa wapinzani kuingilia kazi hiyo. Na baadaye walitumaini wangeweza kupunguza gharama ya kuchapa mabuku na hivyo waweze kuyafanya yapatikane kwa urahisi zaidi kwa umma.

      Lakini hilo lingetaka nafasi na vifaa vingi zaidi, na wangelazimika kujifunza stadi mpya. Je, wangeweza kufanya hivyo? Robert J. Martin, mwangalizi wa kiwanda, alikumbuka kwamba katika siku za Musa, Yehova alikuwa ‘amewajaza Bezaleli na Oholiabu hekima ya moyoni ili waifanye kazi yote’ iliyohitajiwa katika kujenga tabenakulo takatifu. (Kut. 35:30-35) Akiwa na simulizi hilo la Biblia akilini, Ndugu Martin alikuwa na uhakika kwamba Yehova angeweza pia kufanya chochote kilichohitajiwa ili kwamba watumishi wake waweze kuchapa fasihi ili wautangaze Ufalme.

      Baada ya kutafakari kwingi na sala nyingi, mipango hususa ilianza kutokea. Akitazama nyuma kwa yale yaliyotokea, Ndugu Martin alimwandikia Ndugu Rutherford baadaye hivi: “Siku iliyo kuu kupita zote ilikuwa ile siku ulipotaka kujua ikiwa kulikuwa na sababu yoyote nzuri kwa nini sisi hatupaswi kuchapa na kujalidi vitabu vyetu vyote. Lilikuwa wazo la kusisimua, kwa sababu lilimaanisha kufunguliwa kwa kiwanda kamili cha kupanga chapa, kupakaza kwa umeme, kuchapa na kujalidi, ikihitaji kuendesha mashine nyingi tusizofahamu, sanasana mashine ambazo hatukujua zilikuwako, na uhitaji wa kujifunza stadi nyingi. Lakini hiyo ilionekana kuwa ndiyo njia bora zaidi ya kupunguza gharama ya vitabu baada ya ile vita.

      “Ulikodisha jengo la orofa sita kwenye barabara ya 18 Concord Street (kukiwa na wakazi katika orofa mbili); na mnamo Machi 1, 1922, tukahamia humo. Ulitununulia mashine kamili za kupanga chapa, kupakaza kwa umeme, kuchapa na kujalidi, nyingi zazo zikiwa mpya, baadhi yazo zikiwa zimetumiwa; na tukaanza kazi.

      “Mojawapo kiwanda kikubwa cha uchapaji kilichokuwa kimekuwa kikifanya sehemu kubwa ya kazi yetu kilisikia yale tuliyokuwa tukifanya na msimamizi wa kiwanda hicho akaja, ili kutuzuru. Aliona vifaa vipya na akasema hivi kwa uzito, ‘Hapa mna kiwanda cha uchapaji kilicho bora zaidi, na hakuna yeyote katika kiwanda anayejua jinsi ya kukiendesha. Katika miezi sita kiwanda chote cha uchapaji kitakuwa takataka; na mtagundua kwamba watu wanaostahili kuwachapia ni wale ambao sikuzote wamekuwa wakiwachapia, wakiifanya iwe shughuli yao.’

      “Hilo lilisikika kuwa jambo la akili vya kutosha, lakini lilisahau Bwana; na sikuzote amekuwa pamoja nasi. Ujalidi ulipoanza alimtuma ndugu ambaye ametumia maisha yake yote katika shughuli ya ujalidi. Alikuwa msaada mkubwa wakati alipohitajiwa zaidi. Kwa msaada wake, na roho ya Bwana ikitenda kazi miongoni mwa ndugu waliokuwa wakijaribu kujifunza, upesi tulianza kufanyiza vitabu.”

      Kwa kuwa kiwanda kwenye barabara ya Concord Street kilikuwa na nafasi kubwa, shughuli za uchapaji kutoka Detroit ziliunganishwa na zile za Brooklyn. Kufikia mwaka wa pili katika sehemu hiyo, ndugu walikuwa wakifanyiza asilimia 70 ya vitabu na vijitabu vilivyohitajiwa, kutia na magazeti, trakti, na vikaratasi vya ukaribishaji. Mwaka uliofuata, walilazimika kutumia orofa mbili zilizobaki za kiwanda kwa sababu ya ukuzi wa kazi.

      Je, wangeweza kuongeza mwendo wa kutokeza vitabu? Matbaa ya kuchapia ilitengenezwa katika Ujerumani, ikasafirishwa kwa meli hadi Amerika, na kuanza kufanya kazi katika 1926 hasa kwa kusudi hilo. Kwa kadiri walivyojua, matbaa hiyo ya kuchapa ndiyo iliyokuwa ya aina yake ya kwanza kutumiwa katika Amerika ili kuchapa vitabu.

      Hata hivyo, shughuli zote za uchapaji za Wanafunzi wa Biblia hazikuwa katika Amerika pekee.

      Shughuli za Uchapaji za Ramaniema Katika Nchi Nyinginezo

      Akitumia mashirika ya kibiashara, Ndugu Russell alikuwa amefanya uchapaji katika Uingereza mapema kama 1881. Hilo lilikuwa likifanywa katika Ujerumani kufikia 1903, Ugiriki kufikia 1906, Finland kufikia 1910, na hata Japani kufikia 1913. Wakati wa miaka iliyofuata vita ya ulimwengu ya kwanza, kiasi kikubwa cha uchapaji huo—wa vitabu, vijitabu, magazeti, na trakti—kilifanywa katika Uingereza, nchi za Skandinavia, Ujerumani, na Poland, na mwingine ulifanywa katika Brazili na India.

      Kisha, katika 1920, mwaka uleule ambao Sosaiti ilianza kufanya uchapaji wayo yenyewe wa magazeti katika Brooklyn, mipango ilifanywa ili ndugu zetu pia katika Ulaya wafanye kiasi cha kazi hiyo. Kikundi kimoja katika Uswisi kilianzisha kiwanda cha uchapaji katika Bern. Hilo lilikuwa shirika lao wenyewe la biashara. Lakini wote walikuwa Wanafunzi wa Biblia, na walitokeza fasihi za Sosaiti katika lugha za Ulaya kwa gharama ya chini sana. Baadaye, Sosaiti ilipata umiliki wa kiwanda hicho cha uchapaji na ikakipanua. Ili kujazia uhitaji wa haraka katika nchi za Ulaya zilizodhoofika kiuchumi wakati huo, kiasi kikubwa sana cha fasihi za bure kilitokezwa huko. Wakati wa miaka ya mwisho ya 1920, vichapo katika lugha nyingi vilisafirishwa kutoka kwa kiwanda hicho.

      Wakati uleule, kupendezwa kwingi katika ujumbe wa Ufalme kulikuwa kukionyeshwa katika Rumania. Kujapokuwa na upinzani mwingi kwa kazi yetu huko, Sosaiti ilianzisha kiwanda cha kuchapa katika Cluj, ili kupunguza gharama za fasihi na kuifanya ipatikane kwa urahisi zaidi kwa watu wenye njaa ya kweli katika Rumania na nchi zilizo karibu. Katika 1924 kiwanda hicho kiliweza kutokeza vitabu vilivyojalidiwa karibu robo milioni, kwa kuongezea magazeti na vijitabu, katika Kirumania na Kihungaria. Lakini yule aliyesimamia kazi huko alithibitika kuwa asiye mwaminifu kwa amana yake na akafanya vitendo vilivyotokeza kupotea kwa mali na vifaa vya Sosaiti. Kujapokuwa hayo, ndugu waaminifu katika Rumania waliendelea kufanya yote waliyoweza ili kushiriki kweli za Biblia na wengine.

      Katika Ujerumani kufuatia Vita ya Ulimwengu 1, idadi kubwa ya watu walikuwa wakimiminika kwenye mikutano ya Wanafunzi wa Biblia. Lakini Wajerumani walikuwa wakipata taabu kubwa ya kiuchumi. Ili kupunguza gharama ya fasihi za Biblia kwa manufaa yao, Sosaiti ilisitawisha kazi ya uchapaji yayo yenyewe huko pia. Katika Barmen, mwaka 1922, uchapaji ulifanywa kwa kutumia matbaa-tambarare kwenye sehemu ya ngazi katika Kao la Betheli na kwenye nyingine katika kibanda cha mbao. Mwaka uliofuata akina ndugu walihamia Magdeburg kwenye vifaa bora zaidi. Walikuwa na majengo mazuri huko, mengine yaliongezwa, na vifaa vya kuchapa na kujalidi vitabu vikawekwa. Kufikia mwisho wa 1925, iliripotiwa kwamba uwezo wa kutokeza vitabu wa kiwanda hicho ungekuwa mkubwa angalau kama ule uliotumiwa kwenye makao makuu katika Brooklyn.

      Uchapaji mwingi uliofanywa hasa na akina ndugu ulianza kwa kiwango kidogo. Ilikuwa hivyo katika Korea, ambako katika 1922 Sosaiti ilianzisha kiwanda kidogo cha kuchapa chenye vifaa vya kutokeza fasihi katika Kikorea na pia Kijapani na Kichina. Baada ya miaka michache, vifaa hivyo vilihamishiwa Japani.

      Kufikia 1924 kuchapwa kwa vitu vidogo kulifanywa pia katika Kanada na katika Afrika Kusini. Katika 1925 matbaa ndogo ilianzishwa katika Australia na nyingine katika Brazili. Upesi ndugu katika Brazili walikuwa wakitumia vifaa vyao kuchapa The Watch Tower kwa Kireno. Tawi la Sosaiti katika Uingereza lilipata kifaa chayo cha kwanza cha kuchapia katika 1926. Katika 1929 njaa ya kiroho ya watu wanyenyekevu katika Hispania ilikuwa ikitoshelezwa kwa kuchapwa kwa The Watch Tower katika matbaa ndogo huko. Miaka miwili baadaye matbaa ilianza kuendeshwa katika orofa ya chini ya ofisi ya tawi katika Finland.

      Wakati uo huo, upanuzi ulikuwa ukiendelea kwenye makao makuu ya ulimwenguni.

      Kiwanda Chao Wenyewe Kwenye Makao Makuu ya Ulimwengu

      Tangu 1920 Sosaiti ilikuwa ikikodiwa nafasi ya kiwanda katika Brooklyn. Hata jengo lililotumiwa kuanzia 1922 na kuendelea halikuwa katika hali nzuri; jengo zima lingetikisika sana wakati matbaa-mabamba-mviringo ilipokuwa ikiendeshwa katika orofa ya chini. Isitoshe, nafasi zaidi ilihitajiwa ili kushughulikia kazi iliyokuwa ikikua. Ndugu walitoa sababu kwamba fedha zilizopatikana zingeweza kutumiwa vyema zaidi ikiwa wangekuwa na kiwanda chao wenyewe.

      Eneo fulani lililokuwa karibu na Kao la Betheli lilionekana kuwa sehemu inayofaa sana, kwa hiyo wakashindania bei yalo. Matokeo yakawa, Shirika la Madawa la Squibb liliwashinda kwa kutoa fedha nyingi zaidi; lakini walipojenga kwenye eneo hilo, walilazimika kushindilia mabamba 1,167 ya saruji ili kuwa na msingi imara. (Miaka mingi baadaye, Watch Tower Society ilinunua majengo hayo kutoka kwa Squibb, yakiwa tayari na ule msingi mzuri!) Hata hivyo, sehemu ambayo Sosaiti ilinunua katika 1926 ilikuwa na udongo unaoweza kustahimili uzito uliofaa kujengea.

      Katika Februari 1927 walihamia kwenye jengo lao jipya kabisa kwenye barabara ya 117 Adams Street katika Brooklyn. Liliwaandalia karibu nafasi mara mbili zaidi ya ile waliyokuwa wakitumia kufikia wakati huo. Lilijengwa vizuri, kazi ikianzia kutoka orofa za juu kuelekea chini kwenye idara mbalimbali hadi ilipofika Idara ya Usafirishaji kwenye orofa ya chini.

      Hata hivyo, ukuzi haukuwa umekamilika. Katika muda wa miaka kumi ilibidi kiwanda hicho kipanuliwe; na upanuzi zaidi ungefuata baadaye. Zaidi ya kuchapa mamilioni ya nakala za magazeti na vijitabu kila mwaka, kiwanda kilikuwa kikitokeza vitabu vilivyojalidiwa vipatavyo 10,000 kila siku. Biblia zilizokamilishwa zilipotiwa miongoni mwa vitabu hivyo katika 1942, Watch Tower Society ilikuwa mbele katika uwanja mpya wa shughuli ya uchapaji. Ndugu walijaribujaribu hadi walipoweza kuchapa karatasi nyepesi ya Biblia kwenye matbaa-mabamba-mviringo—jambo ambalo wachapaji wengine hawakujaribu hadi miaka mingi baadaye.

      Wakati ambapo kutokeza vitabu vingi kulikuwa kukiendelea, vikundi vyenye mahitaji ya pekee havikukosa kushughulikiwa. Mapema kama 1910, Mwanafunzi wa Biblia katika Boston, Massachusetts, na mwingine katika Kanada walikuwa wakishirikiana ili kutokeza tena fasihi za Sosaiti katika Braille (chapa kwa ajili ya vipofu). Kufikia 1924, kutoka kwa ofisi katika Logansport, Indiana, Sosaiti ilikuwa ikitokeza vichapo ili kunufaisha vipofu. Hata hivyo, kwa sababu ya itikio dogo sana wakati huo, kazi ya Braille ilikomeshwa katika 1936, na mkazo ukatiwa kwenye kuwasaidia vipofu kwa njia ya rekodi za vinanda pamoja na uangalifu wa kibinafsi. Baadaye, katika 1960, fasihi za Braille zilianza tena kutokezwa—wakati huu katika unamnanamna mwingi zaidi, na kwa itikio bora zaidi hatua kwa hatua.

      Kukabiliana na Tatizo la Mnyanyaso Mkali

      Katika nchi kadhaa, uchapaji ulifanywa kujapokuwa na hali ngumu sana. Lakini ndugu zetu walivumilia, wakijua kwamba kupiga mbiu ya habari njema za Ufalme kulikuwa kazi ambayo Yehova Mungu, kupitia Mwanae, alikuwa ameamuru ifanywe. (Isa. 61:1, 2; Mk. 13:10) Katika Ugiriki kwa kielelezo, ndugu walikuwa wamepata vifaa vya kuchapia katika 1936 na kuviendesha kwa miezi michache tu ambapo kulitukia badiliko katika serikali na wenye mamlaka wakafunga kiwanda chao. Vivyo hivyo katika India, katika 1940, Claude Goodman alifanya kazi kwa miezi mingi ili kupata matbaa na kujifunza jinsi ya kuiendesha, lakini punde baadaye, polisi waliotumwa na maharaja (mkuu) wakaja na kunyakua matbaa, na kuweka kwenye mikebe mikubwa chapa zote zilizowekwa kwa uangalifu.

      Katika sehemu nyingine nyingi, sheria zilizohusu fasihi zilizoingizwa nchini ziliwalazimisha akina ndugu kuwapa kazi hiyo wachapaji wa kibiashara, hata ingawa Sosaiti ilikuwa na kiwanda cha uchapaji katika nchi ya karibu iliyokuwa na vifaa vya kufanya kazi hiyo. Ilikuwa hivyo katika miaka ya katikati ya 1930 katika sehemu kama Denmark, Latvia, na Hungaria.

      Katika 1933 serikali ya Ujerumani, ikichochewa na makasisi, ilikomesha utendaji wa kuchapa wa Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani. Polisi walitwaa kiwanda cha Watch Tower Society katika Magdeburg na kukifunga katika Aprili wa mwaka huo, lakini hawangeweza kupata ushahidi wowote wenye kuwashtaki, kwa hiyo wakaondoka. Hata hivyo, waliingilia tena katika Juni. Ili kuendelea kueneza ujumbe wa Ufalme, Sosaiti ilianzisha kiwanda cha kuchapia katika Prague, Chekoslovakia, na vifaa vingi vilihamishwa huko kutoka Magdeburg. Kwa mipango hiyo, magazeti katika lugha mbili na vijitabu katika lugha sita vilitokezwa wakati wa miaka michache iliyofuata.

      Kisha katika 1939, majeshi ya Hitler yalivamia Prague, kwa hiyo upesi ndugu wakabomoa vifaa vyao na kuvisafirisha nje ya nchi. Baadhi yavyo vilienda Uholanzi. Hatua hiyo ilifaa sana. Uwasiliano na Uswisi ulikuwa umekuwa mgumu sana kwa ndugu Waholanzi. Kwa hiyo sasa walikodisha mahali na wakiwa na matbaa zao mpya walizopata, walijichapia vichapo wao wenyewe. Hata hivyo, hilo liliendelea kwa muda mfupi tu, kabla ya kiwanda hicho kunyakuliwa na wavamizi Wanazi. Lakini ndugu walikuwa wametumia vifaa hivyo kwa muda mrefu kadiri walivyoweza.

      Wakati hatua rasmi isiyofaa katika Finland ilipokomesha uchapaji wa Mnara wa Mlinzi wakati wa vita, akina ndugu huko walirudufisha makala kuu na kuzipeleka kwa kutumia mjumbe. Baada ya Austria kutwaliwa na Wanazi katika 1938, Mnara wa Mlinzi lilichapwa kwenye mashine ya urudufishaji ambayo ilihamishwahamishwa ili isipatikane na polisi wa Gestapo. Vivyo hivyo, katika Kanada wakati Mashahidi walipokuwa chini ya marufuku ya wakati wa vita, walilazimika kuhamishahamisha vifaa vyao ili kuendelea kuandaa chakula cha kiroho kwa ndugu zao.

      Katika Australia wakati ambapo kazi ya Mashahidi wa Yehova ilipokuwa chini ya marufuku, akina ndugu walichapa magazeti yao wenyewe na hata wakachapa na kujalidi vitabu—jambo ambalo hawakuwa wamepata kufanya huko hata chini ya hali zilizofaa. Ilibidi wahamishe kifaa chao cha ujalidi mara 16 ili kuzuia kisinyakuliwe, lakini waliweza kutokeza vitabu 20,000 vyenye jalada gumu kwa wakati barabara ili vitolewe kwenye mkusanyiko uliofanywa katika 1941 kujapokuwa na vizuizi vyenye kulemea!

      Upanuzi Baada ya Vita ya Ulimwengu 2

      Baada ya vita kwisha, Mashahidi wa Yehova walikutana katika kusanyiko la kimataifa katika Cleveland, Ohio, katika 1946. Huko Nathan H. Knorr, wakati huo akiwa msimamizi wa Watch Tower Society, alizungumza juu ya kujenga upya na upanuzi. Tangu mwanzo wa Vita ya Ulimwengu 2, idadi ya Mashahidi ilikuwa imeongezeka kwa asilimia 157, na wamishonari walikuwa wakifungua kazi upesi katika mashamba mapya. Ili kujazia uhitaji wa duniani pote wa fasihi za Biblia, Ndugu Knorr alitoa mipango ya kupanua vifaa vya makao makuu ya ulimwenguni. Kama tokeo la upanuzi uliodokezwa, kiwanda kingekuwa na nafasi iliyo mara mbili ile iliyokuwa katika jengo la kwanza la 1927, na Kao la Betheli yaliyopanuliwa sana yangeandaliwa kwa ajili ya wafanyakazi wa kujitolea. Nyongeza hizo zilikamilishwa na kuanza kutumiwa mapema katika 1950.

      Kiwanda na ofisi kwenye makao makuu ya ulimwenguni katika Brooklyn vimepanuliwa tena na tena tangu 1950. Kufikia 1992 vilienea sehemu kama ya majengo manane ya jijini na kutia ndani meta za mraba 230,071 za nafasi ya sakafu. Hayo si majengo ya kufanyiza vitabu tu. Yamewekwa wakfu kwa Yehova, ili yatumiwe katika kutokeza fasihi zilizobuniwa ili kuwaelimisha watu katika matakwa yake kwa ajili ya uhai.

      Katika sehemu nyingine ilikuwa vigumu kuanzisha tena shughuli za uchapaji za Sosaiti baada ya vita ya ulimwengu ya pili. Jengo la kiwanda na la ofisi lililo mali ya Sosaiti katika Magdeburg, Ujerumani, lilikuwa katika eneo lililotawalwa na Wakomunisti. Mashahidi Wajerumani walihamia humo tena, lakini waliweza kufanya kazi kwa muda mfupi tu kabla halijanyakuliwa tena. Ili kujazia uhitaji katika Ujerumani Magharibi, kiwanda cha uchapaji kilitakiwa kianzishwe huko. Majiji yalikuwa yameharibiwa kabisa kwa sababu ya kupigwa mabomu. Hata hivyo, upesi Mashahidi waliweza kutumia kiwanda kidogo cha uchapaji kilichokuwa kimetumiwa na Wanazi, katika Karlsruhe. Kufikia 1948 walikuwa na matbaa-tambarare mbili za kuchapia zikiendeshwa mchana na usiku katika jengo walilopewa katika Wiesbaden. Mwaka uliofuata walipanua jengo la Wiesbaden na wakaongeza hesabu ya matbaa mara nne ili kutimiza mahitaji ya idadi iliyokuwa ikikua haraka sana ya wapiga-mbiu wa Ufalme katika sehemu hiyo ya shamba.

      Sosaiti ilipoanza kuchapa tena peupe katika Ugiriki katika 1946, nguvu za umeme hazikuwa zikitegemeka. Nyakati nyingine umeme ungekosekana kwa muda wa saa nyingi. Nchini Nigeria katika 1977, ndugu walikabili tatizo lilo hilo. Hadi ofisi ya tawi ya Nigeria ilipopata jenereta yayo yenyewe, wafanyakazi wa kiwanda wangerudi kazini wakati wowote, mchana au usiku, umeme uliporudi. Wakiwa na roho hiyo, hawakukosa kupata toleo la Mnara wa Mlinzi.

      Kufuatia ziara ya Ndugu Knorr katika Afrika Kusini katika 1948, sehemu ilinunuliwa katika Elandsfontein; na mapema katika 1952, ofisi ya tawi ilihamia kwenye kiwanda kipya huko—cha kwanza kilichojengwa hasa na Sosaiti katika Afrika Kusini. Wakitumia matbaa-tambarare mpya, walichapa magazeti katika lugha nane zinazotumiwa barani Afrika. Katika 1954 ofisi ya tawi katika Sweden ilipata vifaa ili kuchapa magazeti yalo katika matbaa-tambarare, na vilevile tawi la Denmark lilipata vifaa katika 1957.

      Uhitaji wa fasihi ulipozidi kukua, matbaa-mabamba-mviringo yenye mwendo wa kasi yaliandaliwa, kwanza katika tawi moja kisha katika nyingine. Kanada ilipokea yayo ya kwanza katika 1958; Uingereza, katika 1959. Kufikia 1975 Watch Tower Society ilikuwa na matbaa-mabamba-mviringo 70 kubwa zikifanya kazi katika viwanda vyayo vya uchapaji ulimwenguni pote.

      Vituo vya Duniani Pote ili Kutangaza Kweli ya Biblia

      Katika miaka ya mwisho ya 1960 na baada ya hapo, jitihada nyingi zilifanywa ili kutawanya zaidi shughuli za uchapaji za Watch Tower Society badala ya kuwa mahali pamoja. Ukuzi wa idadi ya Mashahidi wa Yehova ulikuwa wa haraka sana. Nafasi zaidi ya kiwanda ilihitajiwa ili kuandaa fasihi za Biblia kwa utumizi wao na kwa kugawanyia umma. Lakini upanuzi katika Brooklyn ulikuwa wa mwendo wa polepole kwa sababu ya nafasi ndogo iliyopatikana pamoja na kulazimika kufuata utaratibu mwingi wa kiofisi serikalini. Mipango ilifanywa ili kufanya uchapaji mwingi kwingineko.

      Hivyo, katika 1969 kazi ilianza ya kuchora ramani ya kiwanda kipya cha kuchapia ambacho kingejengwa karibu na Wallkill, New York, karibu kilometa 150 kaskazini-magharibi mwa Brooklyn. Hiyo ingeongezea na kueneza majengo ya makao makuu, na hatimaye karibu magazeti yote ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! ya Marekani yangetoka Wallkill. Miaka mitatu baadaye kiwanda cha pili cha Wallkill kilichorwa, hicho kikiwa kikubwa zaidi ya kile cha kwanza. Kufikia 1977 matbaa-mabamba-mviringo zilizoko huko zilikuwa zikitokeza magazeti zaidi ya milioni 18 kila mwezi. Kufikia 1992, matbaa kubwa za MAN-Roland na Hantscho (4 tu badala ya zile za kwanza 15) zilitumiwa, na uwezo wa kutokezwa kwa magazeti ulikuwa zaidi ya milioni moja kwa siku.

      Mipango kwa ajili ya shughuli za kuchapa katika Wallkill ilipofanywa mwanzoni, Mnara wa Mlinzi lilikuwa likichapwa katika Brooklyn katika lugha 32 kati ya 72 zayo; Amkeni! lilikuwa likichapwa katika lugha 14 kati ya 26 zayo. Asilimia 60 hivi ya jumla ya hesabu ya nakala zilizokuwa zikichapwa ulimwenguni pote zilikuwa zikitokezwa huko kwenye makao makuu. Ingenufaisha kufanya kazi hiyo katika nchi zilizo nje ya Marekani na kufanywa na ndugu zetu wenyewe huko badala ya mashirika ya kibiashara. Hivyo, iwapo tatizo la ulimwenguni la wakati ujao au kuingiliwa kwa kazi ya Mashahidi wa Yehova na serikali kungezuia shughuli katika sehemu yoyote ya dunia, chakula cha kiroho cha maana bado kingeandaliwa.

      Hivyo katika 1971, karibu miaka miwili kabla ya kiwanda cha kwanza cha Watch Tower katika Wallkill kuanza kufanya kazi, kazi ilianzishwa ili kuandaa kiwanda kipya kifaacho cha kuchapa katika Numazu, Japani. Ongezeko la zaidi ya mara tano la wapiga-mbiu wa Ufalme katika Japani wakati wa mwongo uliotangulia lilionyesha kwamba fasihi nyingi za Biblia zingehitajiwa huko. Wakati uo huo, majengo ya tawi katika Brazili yalikuwa yakipanuliwa. Ilikuwa hivyo pia katika Afrika Kusini, ambako fasihi za Biblia zilikuwa zikitokezwa katika lugha nyingi za Kiafrika. Mwaka uliofuata, 1972, vifaa vya kuchapa vya Sosaiti katika Australia viliongezwa mara nne zaidi kwa ukubwa, wakiwa na kusudi la kuandaa kila toleo la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! katika sehemu hiyo ya ulimwengu bila kuchelewesha usafirishaji. Viwanda vya ziada vilijengwa pia katika Ufaransa na Filipino.

      Mapema katika 1972, N. H. Knorr na mwangalizi wa kiwanda cha Brooklyn, M. H. Larson, walifanya ziara ya kimataifa ili kuchunguza kazi iliyokuwa ikifanywa, ili kupanga mambo kwa utumizi bora zaidi wa vifaa hivyo na kuweka msingi kwa ajili ya upanuzi zaidi ambao ungefuata. Ziara zao zilitia ndani nchi 16 katika Amerika Kusini, Afrika, na Mashariki ya Mbali.

      Punde baadaye, ofisi ya tawi katika Japani ilikuwa ikitokeza yenyewe magazeti katika lugha ya Kijapani yaliyohitajika katika sehemu hiyo ya shamba, badala ya kutegemea wachapaji wa kibiashara. Mwaka uo huo, 1972, ofisi ya tawi katika Ghana ilianza kuchapa Mnara wa Mlinzi katika lugha tatu kati ya lugha za wenyeji, badala ya kungoja safirisho kutoka Marekani na Nigeria. Halafu, ofisi ya tawi ya Filipino ilianza kushughulikia utungaji na uchapaji wa Mnara wa Mlinzi na Amkeni! katika lugha nane za wenyeji (kutia na kuchapa magazeti yaliyohitajika katika lugha ya Kiingereza). Hiyo ilikuwa hatua kubwa sana katika kutawanya shughuli za uchapaji za Watch Tower.

      Kufikia mwisho wa 1975, Watch Tower Society ilikuwa ikichapa fasihi za Biblia katika vifaa vyayo yenyewe katika nchi 23 duniani pote—vitabu katika nchi tatu; vijitabu au magazeti au yote mawili katika sehemu zote 23. Sosaiti ilikuwa ikitokeza tena vitu vidogovidogo zaidi katika vifaa vyayo yenyewe, katika nchi 25.

      Uwezo wa Sosaiti wa kutokeza vitabu vilivyojalidiwa ulikuwa unaongezwa pia. Ujalidi fulani ulikuwa umefanywa katika Uswisi na katika Ujerumani mapema kama katikati ya miaka ya 1920. Kufuatia Vita vya Ulimwengu 2, katika 1948 ndugu katika Finland walianza kujalidi vitabu (mwanzoni, kwa mkono sanasana) ili kushughulikia hasa mahitaji ya nchi hiyo. Miaka miwili baadaye ofisi ya tawi katika Ujerumani ilikuwa ikiendesha kifaa cha kujalidi, na baadaye kikafanya kazi ya ujalidi wa vitabu iliyokuwa ikifanywa katika Uswisi.

      Kisha, katika 1967, kukiwa na Mashahidi zaidi ya milioni moja ulimwenguni pote na kwa kutokezwa kwa vitabu vya ukubwa wa mfukoni kwa utumizi katika huduma yao, uhitaji wa aina hiyo ya fasihi za Biblia uliongezeka sana. Katika muda wa miaka tisa, kulikuwa na ongezeko la zaidi ya mara sita la vifaa vya kujalidi katika Brooklyn. Kufikia 1992 Watch Tower Society ilikuwa na jumla ya vifaa vya kujalidi 28 vikiendeshwa katika nchi nane tofauti.

      Katika mwaka uo huo, 1992, si kwamba tu Watch Tower Society ilikuwa ikichapa fasihi za Biblia katika lugha 180 katika Marekani bali pia viwanda vyayo vikubwa vinne vya kuchapia katika Amerika ya Latin vilikuwa vikiandaa fasihi nyingi zilizohitajiwa nchini humo na pia katika nchi nyinginezo katika sehemu hiyo ya ulimwengu. Viwanda vingine 11 vilikuwa vikitokeza fasihi katika Ulaya, na zote hizo zilikuwa zinasaidia kujazia uhitaji wa fasihi wa nchi nyinginezo. Kati ya hizo, Ufaransa ilikuwa ikitoa fasihi kwa nchi 14, na Ujerumani, ambayo ilichapa katika lugha zaidi ya 40, ilikuwa ikisafirisha ugavi mkubwa kwa nchi 20 na ugavi mdogo zaidi kwenye nchi nyinginezo nyingi. Barani Afrika, viwanda sita vya kuchapia vya Watch Tower vilikuwa vikitokeza fasihi za Biblia katika jumla ya lugha 46. Viwanda vingine 11 vya kuchapia—vingine vikubwa, vingine vidogo—vilikuwa vikiandalia Mashariki ya Kati na Mashariki ya Mbali, visiwa vya Pasifiki, Kanada, na maeneo mengineyo fasihi za kutumia katika kueneza ujumbe wenye uharaka kuhusu Ufalme wa Mungu. Katika nchi 27 nyingine, Sosaiti ilikuwa ikichapa vitu vidogovidogo vilivyohitajiwa na makutaniko ili yatende kazi vema.

      Njia Mpya, Vifaa Vipya

      Wakati wa miaka ya 1960 na 1970, kulikuwa na mvuvumko (ukuzi wa haraka) katika viwanda vya uchapaji. Kwa kadiri ya kustaajabisha, matbaa ya kuchapa maandishi yaliyoinuliwa ilikuwa ikiachwa na kupendelea uchapaji wa ofseti.d Watch Tower Society haikuanza mara hiyo kutumia njia mpya za kuchapa. Mabamba ya matbaa ya ofseti hayakufaa sana kuchapa kiasi kikubwa cha fasihi ambazo Sosaiti ilihitaji. Zaidi ya hiyo, badiliko la aina hiyo lingehitaji aina mpya kabisa za kupanga chapa na kutunga. Matbaa mpya za kuchapa zingehitajiwa. Ingebidi kujifunza tekinolojia mpya. Karibu vifaa vyote vya kuchapa vya viwanda vya Sosaiti vingehitaji kubadilishwa. Gharama ingekuwa kubwa ajabu.

      Hata hivyo, baadaye ikawa dhahiri kwamba ugavi wa kutegemeza kupiga chapa kwa maandishi yaliyoinuliwa haungepatikana tena. Uwezo wa kudumu wa mabamba ya ofseti ulifanya maendeleo haraka. Ilibidi badiliko lifanywe.

      Mapema kama 1972, kwa sababu ya kupendezwa kwao sana na maendeleo ya upigaji chapa wa ofseti, washiriki watatu wa familia ya Betheli katika Afrika Kusini walinunua matbaa ndogo iliyotumiwa ya ofseti yenye kutiwa karatasi. Ujuzi fulani ulipatikana wa kufanya kazi ndogondogo za kuchapa kwa kuitumia. Kisha, katika 1974, matbaa hiyo ilitumiwa kuchapa Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, kitabu chenye ukubwa wa mfukoni, katika lugha ya Kironga. Kwa kuweza kufanya hilo, upesi waliweza kupeleka maagizo ya Biblia yenye thamani kwa maelfu ya watu wenye njaa ya kiroho kabla ya kazi ya Mashahidi wa Yehova kupigwa marufuku tena katika eneo ambalo watu hao waliishi. Matbaa nyingine ya ofseti yenye kutiwa karatasi, iliyopewa kwa ofisi ya tawi ya Sosaiti ya Afrika Kusini punde baada ya ndugu zetu kununua ile ya kwanza, ilisafirishwa hadi Zambia na kutumiwa huko.

      Kiwanda cha Sosaiti katika Ujerumani pia kilikuwa na mwanzo wa mapema katika upigaji chapa wa ofseti. Katika Aprili 1975 ndugu huko walianza kutumia matbaa yenye kutiwa karatasi ili kuchapa magazeti kwenye karatasi ya kuchapa Biblia kwa ajili ya Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani Mashariki, ambako Mashahidi walikuwa chini ya marufuku wakati huo. Hilo lilifuatwa mwaka uliofuata, na kutokezwa kwa vitabu kwenye matbaa ya ofseti kwa ajili ya hao ndugu waliokuwa wakinyanyaswa.

      Karibu na wakati huo, katika 1975, Watch Tower Society ilianza kuendesha matbaa yayo ya kwanza ya ofseti ya web (kuchapa karatasi mfululizo) ya kuchapa magazeti katika Argentina. Hata hivyo, iliendeshwa kwa muda unaozidi kidogo tu mwaka mmoja, kabla ya serikali ya Argentina kupiga marufuku kazi ya Mashahidi na kufunga kiwanda. Lakini shughuli za uchapaji katika nchi nyinginezo ziliendelea kupanuka. Mapema katika 1978, kwenye kiwanda cha makao makuu ya Watch Tower Society katika Brooklyn, New York, matbaa ya ofseti ya web ilianza kutokeza uchapaji wa rangi tatu wa vitabu.e Matbaa ya pili ilinunuliwa katika mwaka uo huo. Na bado, vifaa vingi zaidi vilihitajiwa ili kukamilisha ule mbadiliko.

      Baraza Linaloongoza lilikuwa na uhakika kwamba Yehova angeandaa chochote kilichohitajiwa ili kukamilisha kazi aliyotaka ifanywe. Katika Aprili 1979 na Januari 1980, barua zilipelekwa kwa makutaniko katika Marekani zikieleza jinsi hali ilivyo. Upaji ulipokewa—kidogo mwanzoni, lakini baadaye kulikuwa na upaji wa kutosha kununua vifaa vya uchapaji wa ofseti kwa ajili ya viwanda vya vituo vyote vya Watch Tower duniani pote.

      Wakati uo huo, ili kutumia vifaa vilivyopo kwa njia bora zaidi na kuharakisha ule mbadiliko, Watch Tower Society ilifanya mpango ili aina ya matbaa ya karibuni zaidi ya MAN iweze kubadilishwa iwe ya kuchapa kwa ofseti. Nchi 12 ziliandaliwa matbaa hizo, kutia na 6 ambazo hazikuwa zimechapa magazeti yazo kwao.

      Kuchapa Katika Rangi Nne

      Ofisi ya tawi katika Finland ndiyo iliyokuwa ya kwanza kufanya uchapaji wa ofseti wa kila toleo la magazeti yayo katika rangi nne, ikianza kwa njia rahisi na matoleo ya Januari 1981 na kisha wakiendelea kutumia stadi zenye maendeleo. Halafu, Japani ilitumia uchapaji wa rangi nne kwa kitabu kilichojalidiwa. Matbaa nyinginezo za Watch Tower zilifanya vivyo hivyo kadiri vifaa vilivyopatikana. Baadhi ya matbaa zimenunuliwa na kusafirishwa na makao makuu ya ulimwengu. Mengine yamenunuliwa na Mashahidi wa Yehova katika nchi zile ambazo kiwanda hicho kiko. Katika visa vingine tena, Mashahidi katika nchi moja wametoa zawadi ya vifaa vilivyohitajiwa kwa ndugu zao katika nchi nyingine.

      Wakati wa kipindi kilichofuata Vita ya Ulimwengu 2, ulimwengu ulipendezwa zaidi na chapa zenye picha, na utumizi wa rangi halisi ulisaidia sana kufanya vichapo vivutie zaidi kwa macho. Utumizi huo wa rangi umefanya vichapo vivutie zaidi na hivyo kutia moyo usomaji. Katika sehemu nyingi ilionwa kwamba kugawanywa kwa Mnara wa Mlinzi na Amkeni! kuliongezeka sana baada ya sura zayo kufanywa zivutie.

      Kufanyiza Mifumo ya Kompyuta Inayofaa

      Ili kutegemeza uchapaji wa rangi nne, mfumo wa kompyuta wa kutayarisha habari ya kuchapwa ungepaswa ufanyizwe; na uamuzi wa kutekeleza hilo ulifanywa katika 1977. Mashahidi waliokuwa stadi katika uwanja huo walijitolea kufanya kazi kwenye makao makuu ya ulimwengu ili kusaidia Sosaiti kutimiza mahitaji hayo upesi. (Punde baada ya hilo, katika 1979, kikundi cha Mashahidi 50 hivi katika Japani hatimaye kilianza kazi katika programu hizo zilizohitajiwa kwa ajili ya lugha ya Kijapani.) Kompyuta za kibiashara zilipatikana na kutumiwa, na programu zilitayarishwa na Mashahidi ili zisaidie kujazia mahitaji ya usimamizi ya Sosaiti na ya uchapaji katika lugha nyingi. Ili kudumisha viwango vya juu na kuwa na ubadilikano uliohitajiwa, ilihitajiwa kufanyiza programu za pekee za kupanga chapa na kuyatunga kwa picha. Hakukuwa na programu za kibiashara zilizopatikana ili kuingiza na kupanga chapa kwa picha lugha nyingi kati ya 167 ambazo Watch Tower Society ilikuwa ikichapa wakati huo, kwa hiyo ilibidi Mashahidi wafanyize programu yao wenyewe.

      Wakati huo ulimwengu wa biashara haukuona faida ya pesa katika lugha zilizotumiwa na idadi ndogo ya watu au watu wenye mapato madogo, lakini Mashahidi wa Yehova hupendezwa na uhai. Katika kipindi ambacho ni kifupi, programu za kupanga chapa walizokuwa wamefanyiza zilikuwa zikitumiwa ili kutokeza fasihi katika lugha zaidi ya 90. Kuhusu kazi yao kichapo kinachoheshimiwa Seybold Report on Publishing Systems kilisema: “Sisi tunasifu sana mradi, ujianzishaji na ufahamu wa ndani wa watu wa Mnara wa Mlinzi. Leo ni watu wachache walio na tamaa ya kutimiza mambo makubwa au wajasiri vya kutosha hata waanze mradi kama huo, hasa kwa kujifanyia karibu kila jambo.”—Buku 12, Na. 1, Septemba 13, 1982.

      Shughuli za uchapaji na udumishaji zingewezekana sana ikiwa vifaa vilivyotumiwa ulimwenguni pote vingekuwa vilevile. Kwa hiyo katika 1979, uamuzi ulifanywa na Watch Tower Society ili kufanyiza mfumo wayo yenyewe ya kupanga chapa kwa picha. Kikundi kilichofanya shughuli hiyo kingefanyiza kompyuta, badala ya kutegemea sana zile za kibiashara.

      Hivyo, katika 1979 kikundi cha Mashahidi wa Yehova wakiwa na kituo cha shughuli zao katika Watchtower Farms, Wallkill, New York, walianza kubuni na kuunda Mfumo wa Elektroni wa Kupanga Chapa kwa Picha Katika Lugha Nyingi (MEPS). Kufikia Mei 1986 kikundi kilichokuwa kikishughulika na mradi huo hakikuwa kimebuni na kuunda tu kompyuta za MEPS, mashine za kupanga chapa kwa picha na vifaa vya chapa, bali, ya maana hata zaidi, walikuwa pia wamefanyiza vifaa vya kuendesha kompyuta vilivyohitajiwa ili kutayarisha habari ya kuchapwa katika lugha 186.

      Mfumo mkubwa wa nambari zinazowakilisha aina ya herufi ulipatanishwa na kule kufanyizwa kwa programu za kompyuta. Hilo lilitaka kujifunza mengi juu ya mambo yanayopambanua kila lugha. Ilibidi kuchora kila alama katika lugha fulani (kwa kielelezo, kila alama ya herufi kubwa na herufi ndogo, pamoja na alama za kuonyesha jinsi neno linavyotamkwa na zile za kutenga maneno—zote zikiwa na ukubwa mbalimbali), kukiwa na mchoro tofauti kwa kila aina ya herufi (kama vile, rangi hafifu, italiki, rangi nzito, na rangi nzito sana), labda katika hesabu fulani za aina za herufi tofauti au mtindo wa chapa. Kila herufi ya kirumi ilihitaji alama 202. Kwa hiyo, herufi za kirumi 369 zimehitaji jumla ya alama 74,538. Kutayarishwa kwa aina ya herufi za Kichina kulihitaji kuchorwa kwa alama 8,364 kwa kila moja, alama zaidi zikiongezwa baadaye.

      Baada ya kazi ya kuchora kwisha, programu za kuendesha kompyuta ambazo zingewezesha kuchapa alama hizo kwa njia nadhifu, yenye kutokeza, zilibuniwa. Programu hizo zingeweza kushughulikia si alfabeti ya Kirumi tu bali pia ya Kibengali, Kikambodia, Kisirili, Kigiriki, Kihindi, na Kikorea kutia na Kiarabu na Kiebrania (ambazo zote mbili husomwa kutokea kulia kwenda kushoto) na Kijapani na Kichina (ambazo hazitumii alfabeti). Kuanzia 1992 vifaa vya kuendesha kompyuta vilipatikana ili kutayarisha habari katika lugha zaidi ya 200, na programu za lugha nyinginezo zinazotumiwa na mamilioni ya watu zilikuwa bado zikifanyizwa.

      Ilibidi kutumia utaratibu mpya na kujifunza stadi mpya baada ya ule mbadiliko katika matawi. Wafanyakazi walitumwa kwenye makao makuu ya ulimwenguni ili kujifunza jinsi ya kuanzisha, kuendesha, na kudumisha matbaa kubwa za ofseti za web. Wengine walifunzwa jinsi ya kufanya kazi ya kutenganisha rangi kwa kutumia kifaa chenye kutoa nuru. Wafanyakazi zaidi walizoezwa katika utumizi na udumishaji wa vifaa vya kompyuta. Hivyo, matatizo ya kutokeza vitabu yanayozuka mahali popote duniani, yangeweza kutatuliwa upesi ili kazi iendelee kusonga mbele.

      Baraza Linaloongoza liling’amua kwamba ikiwa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wangejifunza habari ileile katika mikutano yao juma baada ya juma na kugawanya fasihi zilezile katika huduma ya shambani, hilo lingeweza kuwa na tokeo lenye nguvu la kuunganisha. Wakati uliopita, mara nyingi fasihi zilizochapwa katika Kiingereza hazikupatikana katika lugha nyinginezo hadi angalau miezi minne baadaye; katika lugha nyingi ilikuwa mwaka mmoja, au mara nyingi, miaka mingi baadaye. Lakini sasa badiliko liliwezekana. Ili kuweza kuchapa fasihi sawia (wakati uleule) katika lugha mbalimbali, jambo la maana lilikuwa ni kuwa na vifaa vinavyofanya kazi kwa upatani kamili katika matawi yenye kuchapa. Kufikia 1984, uchapaji sawia wa Mnara wa Mlinzi ulifanywa katika lugha 20. Katika 1989, wakati ujumbe wenye nguvu uliomo katika kitabu Ufunuo—Upeo Wao Mtukufu U Karibu! ulipogawanywa kwa umma miezi michache tu baada ya kutolewa kwacho, kitabu hicho kilipatikana katika lugha 25. Kufikia 1992, uchapaji sawia wa Mnara wa Mlinzi ulikuwa umepanuka kutia ndani lugha 66, zile zinazotumiwa na idadi kubwa ya watu ulimwenguni.

      Tangu mradi wa MEPS uanzishwe katika 1979, biashara ya kompyuta imefanya maendeleo ya kutokeza sana. Kompyuta ndogo zenye uwezo mkubwa na matumizi mbalimbali sasa zinapatikana kwa gharama ndogo kuliko vifaa vya mapema zaidi. Ili kwenda sambamba na mahitaji ya kazi yayo ya kuchapa, Watch Tower Society iliamua kutumia kompyuta hizo ndogo, pamoja na progamu zayo yenyewe. Hilo liliongeza sana mwendo wa utokezaji vitabu. Pia liliwezesha kuandaa manufaa za programu za kompyuta za kuchapa kwa matawi mengi ya Sosaiti, na hesabu ya matawi yaliyotumia hizo ilipanda upesi kufikia 83. Kufikia 1992 Watch Tower Society ilikuwa na kompyuta 3,800 ambazo ilikuwa ikitumia programu zayo yenyewe za kompyuta. Si matawi yote yenye vifaa hivyo huweza kuchapa, lakini tawi lolote ambalo lina kompyuta ndogo na programu ya Sosaiti, pamoja na mashine ndogo ya kuchapa kwa kutumia nuru, lina uwezo wa kufanya kazi inayotangulia uchapaji wa trakti, magazeti, vitabu, na uchapaji mwingine wowote unaohitajiwa.

      Utegemezo wa Kompyuta Ulioongezwa kwa Ajili ya Watafsiri

      Je, kompyuta zingeweza kutumiwa ili kuwapa watafsiri utegemezo mkubwa zaidi kwa kazi yao? Watafsiri wa vichapo vya Watch Tower sasa hufanya kazi yao, katika visa vingi, kwenye kompyuta. Wengi wao, wako katika ofisi za tawi za Sosaiti. Wengine, ambao wanaweza kutafsiri wakiwa nyumbani na ambao wamefanya kazi yao kwa miaka mingi kwa kutumia taipureta au hata kwa mkono, wamesaidiwa kujifunza jinsi ya kuingiza tafsiri yao katika kompyuta au kwa kompyuta za laputopu (zilizo ndogo ifaavyo) zilizonunuliwa na Sosaiti. Marekebisho katika tafsiri yaweza kufanywa kwa urahisi papo hapo kwenye kiwambo cha kompyuta. Ikiwa tafsiri inafanywa mahali pengine isipokuwa kwenye ofisi ya tawi fulani ambamo uchapaji wenyewe utafanywa, yote yanayotakiwa ni kuhamisha maandishi kwenye diski nyembamba inayoyumbika na kuipeleka kwenye ofisi ya tawi yenye kuchapa ili ishughulikiwe.

      Wakati wa 1989-1990, mabadiliko makubwa yalipotukia katika serikali za nchi nyingi, uwasiliano wa kimataifa ukawa rahisi zaidi. Upesi, Mashahidi wa Yehova walikusanyika kwenye semina ya watafsiri kutoka Ulaya Mashariki. Hilo lilikusudiwa kuwasaidia wafanye kazi yao iwe bora, kuwawezesha wanufaike kutokana na vifaa vya kompyuta vilivyopatikana, na kuwezesha uchapaji sawia wa Mnara wa Mlinzi katika lugha zao. Kwa kuongezea, watafsiri katika Kusini-Mashariki mwa Asia walipewa msaada uo huo.

      Lakini je, kompyuta ingeweza kutumiwa kuongeza mwendo wa kazi ya kutafsiri au kufanyia maendeleo ubora wayo? Ndiyo. Kufikia 1989, mifumo ya kompyuta yenye nguvu ilikuwa ikitumiwa na Mashahidi wa Yehova ili kusaidia katika kutafsiri Biblia. Baada ya kazi nyingi ya mwanzoni, faili za elektroni ziliandaliwa ambazo zingemwezesha mtafsiri aone kwenye kiwambo cha kompyuta neno lolote la lugha ya awali ya Biblia pamoja na rekodi ya njia zote ambazo lilitumiwa katika Kiingereza, kulingana na muktadha, katika Biblia New World Translation. Pia angeweza kuteua neno kuu la Kiingereza na kuona kwenye kompyuta maneno yote ya lugha ya awali ambayo hilo (na labda maneno yenye maana ileile) lilitokana nayo. Mara nyingi hiyo ingefunua kwamba kikundi cha maneno kilikuwa kikitumiwa katika Kiingereza ili kuonyesha wazo lililo katika neno moja la lugha ya awali. Hilo lingemwandalia mtafsiri upesi mwono wenye kina kirefu wa yale aliyokuwa akitafsiri. Lingemsaidia kunasa maana halisi ya maneno ya msingi ya lugha ya awali pamoja na maana hususa inayotakiwa na muktadha na hivyo kuitafsiri kwa usahihi katika lugha yake mwenyewe.

      Kwa kutumia faili hizo za kompyuta, watafsiri wenye ujuzi wangechunguza sehemu zote litokeapo neno lolote la Biblia na kuipa visawe vya lugha ya wenyeji kila moja ya hizi sehemu kulingana na yale yaliyohitajiwa na muktadha. Hilo lingehakikisha kwamba kungekuwa na upatani wa hali ya juu. Kazi ya kila mtafsiri ingepitiwa na wengine wanaofanya kazi katika kikundi hicho hivi kwamba tafsiri hiyo ingenufaika kutokana na utafiti na ujuzi wa wote. Baada ya hilo kufanywa, kompyuta ingetumiwa kuonyesha kifungu fulani cha Andiko, ikionyesha kila neno katika maandishi ya Kiingereza, ufunguo wa yale yaliyotumiwa katika lugha ya asili, na yale yanayolingana katika lugha ya wenyeji ambayo yalikuwa yameteuliwa. Hilo halingekamilisha kazi. Bado mtafsiri alihitaji kunyorosha muundo wa sentensi na kuifanya isomeke vizuri katika lugha yake mwenyewe. Lakini akiwa anafanya hivyo, lingekuwa jambo la maana kuelewa waziwazi maana ya andiko. Ili kumsaidia, alipewa uwezo wa kupata kwenye kompyuta mara ileile mafafanuzi ya Watch Tower yaliyochapwa ya mstari wa Biblia au neno lolote ndani yalo.

      Hivyo, wakati wa kufanya utafiti ungepunguzwa, na kiwango kikubwa cha upatani kingeweza kufikiwa. Kwa kufanya maendeleo zaidi katika uwezekano huo, inatumainiwa kwamba vichapo vingine vyenye thamani vinaweza kupatikana upesi hata katika lugha zenye wafanyakazi wachache wa kutafsiri. Utumizi wa kompyuta ili kuandaa fasihi katika kutegemeza kupiga mbiu ya ujumbe wa Ufalme umefungua uwanja mkubwa wa uchapaji.

      Hivyo, kama vile Wakristo wenzao wa mapema, Mashahidi wa Yehova katika nyakati za kisasa hutumia njia za karibuni zaidi ili kueneza Neno la Mungu. Ili kuwafikia watu wengi na habari njema kwa kadiri iwezekanavyo, hawajaogopa kukabili magumu katika uwanja wa kuchapa.

      [Maelezo ya Chini]

      a Katika 1896 jina la shirika hilo lilibadilishwa rasmi kuwa Watch Tower Bible and Tract Society.

      b Hiyo ilikuwa kampuni ya Charles Taze Russell. Katika 1898 alihamisha mali za Tower Publishing Company hadi kwenye Watch Tower Bible and Tract Society zikiwa mchango.

      c Kushindwa kupata makaa-mawe hakukusababishwa tu na upungufu wa wakati wa vita. Hugo Riemer, aliyekuwa mshiriki wa wafanyakazi wa makao makuu wakati huo, aliandika baadaye kwamba kwa msingi ni kwa sababu ya chuki dhidi ya Wanafunzi wa Biblia iliyokuwa nyingi sana katika New York wakati huo.

      d Kupiga chapa kwa matbaa za maandishi yaliyoinuliwa hufanywa katika sehemu iliyoinuliwa ambayo huwa na taswira ya yale yatakayochapwa katika ukurasa. Sehemu hiyo iliyoinuka hupakwa rangi na kushindiliwa kwenye karatasi. Kupiga chapa kwa ofseti hufanywa kwa kutia alama kwa bamba lenye rangi juu ya silinda iliyofunikwa kwa mpira na kisha kuhamisha alama hiyo kwenye karatasi.

      e Kuanzia 1959 hadi 1971, Sosaiti ilikuwa imetumia matbaa ya ofseti yenye kutiwa karatasi kwenye kiwanda chayo katika Brooklyn ili kutokeza kalenda katika rangi nne zenye vichwa vinavyohusu kuhubiri habari njema.

      [Blabu katika ukurasa wa 578]

      “Acha tufanye makaa-mawe yawe ndiyo jaribio”

      [Blabu katika ukurasa wa 595]

      Kununua vifaa vya uchapaji wa ofseti kwa ajili ya viwanda vya vituo vyote vya Watch Tower duniani pote

      [Blabu katika ukurasa wa 596]

      “Sisi tunasifu sana . . . watu wa Mnara wa Mlinzi”

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 581]

      Kupanga Chapa

      Mwanzoni yote yalifanywa kwa mkono, herufi mojamoja

      Afrika Kusini

      Kuanzia 1920 hadi miaka ya 1980, mashine za Linotaipu zilitumiwa

      Marekani

      Katika sehemu nyingine kupanga chapa kulifanywa na vifaa vya Monotaipu

      Japani

      Sasa njia inayotumiwa ni kupanga chapa kwa picha katika kompyuta

      Ujerumani

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 582]

      Kutengeneza Mabamba

      Kuanzia miaka ya 1920 hadi ya 1980, mabamba ya chuma cha risasi yalitengenezwa kwa ajili ya kuchapa kwa matbaa ya maandishi yaliyoinuliwa

      [Picha]

      1. Mistari ya maandishi ya kurasa za habari iliyochapwa ilitiwa katika fremu za chuma ziitwazo viunzi

      2. Chini ya kani-eneo, alama ya maandishi ilifanywa kwenye chombo ambacho kingeweza kutumiwa kuwa mfinyango

      3. Chuma moto cha risasi kilimwagwa kwenye mfinyango ili kufanyiza mabamba ya chuma ya kuchapa

      4. Chuma kisichotakiwa kiliondolewa kwenye bamba

      5. Mabamba yalitiwa nikeli ili yaweze kudumu

      Baadaye, negativu za kurasa zilizopigwa chapa kwa picha ziliwekwa mahali pafaapo, na picha zikaongezwa. Mafungu ya kurasa yalihamishwa kwa kupigwa picha hadi kwenye mabamba yenye kunyumbulika ya uchapaji wa ofseti

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 585]

      ‘Uthibitisho wa Roho ya Yehova’

      “Kuchapwa kwa vitabu na Biblia kwa mafanikio kwenye matbaa-mabamba-mviringo na watu wasio na ujuzi [na katika wakati ambao wengine hawakuwa ­wakichapa bado] ni uthibitisho wa usimamizi wa Yehova na uelekezo wa roho yake,” akasema Charles Fekel. Ndugu Fekel alijua vema yale yaliyohusika, kwa kuwa alikuwa ameshiriki katika usitawishaji wa shughuli za kuchapa kwenye makao makuu ya Sosaiti kwa zaidi ya nusu karne. Katika miaka yake ya baadaye, alitumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza.

      [Picha]

      Charles Fekel

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 586]

      Kutegemea Mungu Mweza Yote

      Ono lililosimuliwa na Hugo Riemer, aliyekuwa wakala (ajenti) wa ununuzi wa Watch Tower Society, laonyesha njia ambayo Watch Tower Society huendesha shughuli zayo.

      Wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, karatasi za kuchapia zilipatikana kwa kiasi katika Marekani. Maombi ya ugavi yalipaswa yatolewe kwa halmashauri iliyoteuliwa na serikali. Katika pindi moja mojawapo sosaiti mashuhuri za Biblia lilikuwa na mawakili, watu wenye biashara kubwakubwa, wahubiri, na wengineo huko ili kuwawakilisha mbele ya halmashauri hiyo. Walipewa idhini ya kupata kiasi kidogo kuliko kile walichotaka. Baada ya maombi yao kusikizwa, halmashauri hiyo iliita Watchtower Bible and Tract Society. Hugo Riemer na Max Larson walipokuja mbele, mwenyekiti aliuliza: “Ni nyinyi wawili tu?” Jibu: “Ndiyo. Tunatumaini kwamba Mungu Mweza Yote yuko pamoja nasi pia.” Walipewa ugavi wote waliohitaji.

      [Picha]

      Hugo Riemer

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 587]

      Matbaa za Kuchapa

      Matbaa za aina mbalimbali zimetumiwa na Watch Tower Society katika shughuli zayo za kuchapa

      [Picha]

      Kwa miaka mingi matbaa-tambarare za aina mbalimbali zilitumiwa (Ujerumani)

      Matbaa za kazi zimetumiwa kuchapa si fomu na vikaratasi vya ukaribishaji tu bali pia magazeti (Marekani)

      Katika viwanda vyayo mbalimbali vya kuchapa, matbaa 58 za kuchapa kwa maandishi yaliyoinuliwa yenye mabamba-mviringo ya MAN ­kutoka Ujerumani ­zilitumiwa (Kanada)

      Sasa, matbaa za mwendo wa kasi za ofseti ya “web” za kuchapa kwa rangi kamili zinazofanyizwa katika nchi mbalimbali hutumiwa katika viwanda vikuu vya kuchapia vya Sosaiti

      Italia

      Ujerumani

      [Picha katika ukurasa wa 588, 589]

      Kujalidi Vitabu

      Baadhi ya kazi za kujalidi vitabu siku za mapema katika viwanda vya Watch Tower ilifanywa kwa mkono (Uswisi)

      Kutokeza vitabu vingi katika Marekani kulitaka kazi nyingi mbalimbali

      1. Kukusanya mafungu ya kurasa za vitabu

      2. Kuyashona pamoja

      3. Kupaka gundi karatasi za ndani ya jalada

      4. Kukata ili kuvisawazisha

      5. Kutia maneno malidadi kwenye jalada

      6. Kutia jalada kwenye vitabu

      7. Kushindilia vitabu hadi gundi inaposhika imara

      Sasa, badala ya kushona, mara nyingi njia ya kujalidi vitabu imara kwa gundi hutumiwa, na mashine za mwendo wa kasi zaweza kutokeza vitabu 20,000 au zaidi kila siku

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 594]

      Kuendeleza Ujuzi wa Ufalme wa Mungu

      Katika nyakati mbalimbali Watch Tower Society imetokeza fasihi katika lugha mbalimbali zaidi ya 290. Kufikia 1992 walikuwa wakichapa fasihi katika lugha 210. Yote hayo yalifanywa ili kuwasaidia watu kujua kuhusu Ufalme wa Mungu na yale unaomaanisha kwao. Miongoni mwa misaada yao ya kujifunza Biblia ambayo imepata kugawanywa zaidi kufikia sasa ni hii ifuatayo:

      “Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele” (1968): nakala 107,553,888, katika lugha 117

      “Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani” (1982): nakala 62,428,231, katika lugha 115

      “Furahia Milele Maisha Duniani!” (1982): nakala 76,203,646, katika lugha 200

      Tarakimu zilizo juu ni za kufikia 1992.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 598]

      Rekodi za Kaseti

      Zaidi ya kutumia vichapo katika kazi yayo ya kueneza evanjeli, tangu 1978 Watch Tower Society imetokeza kaseti—zaidi ya milioni 65 kwa kutumia vifaa vyayo yenyewe katika Marekani na Ujerumani.

      Biblia nzima ya “New World Translation” imo katika kaseti katika Kiingereza, Kifaransa, Kijerumani, Kiitalia, Kijapani, na Kihispania. Kufikia 1992 kiasi mbalimbali cha tafsiri hiyo ya Biblia kilipatikana pia katika kaseti katika lugha nyinginezo nane.

      Ikiwa msaada wa kufundishia watoto wachanga, rekodi za kaseti zimefanywa kwa ajili ya vichapo “Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia” na “Kumsikiliza Mwalimu Mkuu,” ambavyo vilibuniwa kwa ajili ya watoto.

      Kwa kuongezea, katika nchi fulani kaseti hutolewa ili zitumiwe kwa ajili ya matangazo ya redio.

      Rekodi hutokezwa na okestra iliyofanyizwa na Mashahidi pekee. Kaseti hizo hutumiwa kuwa mifuatano kwa ajili ya kuimba katika mikusanyiko ya Mashahidi wa Yehova. Miziki zilizopangwa vizuri za okestra hupatikana pia ili zifurahiwe nyumbani.

      Drama zilizorekodiwa (masimulizi ya kisasa na ya Biblia pia) hutumiwa kwenye mikusanyiko, ambako waigizaji Mashahidi husaidia wasikilizaji wawazie matukio. Baadhi yazo hutumiwa baadaye kuwa vitumbuizo vyenye kufundisha na kufurahisha vya familia.

      Magazeti ya “Mnara wa Mlinzi” na “Amkeni!” hupatikana katika kaseti katika Kiingereza na Kifinland. Pia, “Mnara wa Mlinzi” hupatikana katika Kifaransa, Kijerumani, Kidenmark, Kinorway, na Kisweden. Zikiwa zimekusudiwa hapo awali kwa watu wenye uwezo hafifu wa kuona, kaseti hizo huthaminiwa na maelfu mengi ya watu wengineo.

      [Picha]

      J. E. Barr katika chumba cha kurekodia

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 600, 601]

      Utumizi wa Kaseti za Vidio Katika Kupiga Mbiu ya Ufalme

      Katika 1990 Watch Tower Society iliingia katika uwanja mpya kwa kutoa kaseti ya vidio yayo ya kwanza iliyobuniwa ili igawanywe kwa umma.

      Ilikadiriwa mwaka huo kwamba familia zaidi ya 200,000,000 duniani pote zilikuwa na VCR (mashine za vidio) za aina mbalimbali. Hata katika nchi ambazo hazikuwa na stesheni za televisheni, VCR zilitumiwa. Hivyo, utumizi wa kaseti za vidio zikiwa njia ya kufundishia ulitoa njia mpya ya kufikia wasikilizaji wengi.

      Mapema kama 1985, kazi ilikuwa imeanza ya kutayarisha maonyesho ya vidio yaliyobuniwa ili wale wanaozuru makao makuu ya ulimwengu ya Sosaiti waweze kuonyeshwa baadhi ya utendaji kwenye makao hayo. Baadaye, maonyesho ya vidio pia yalithibitika kuwa yenye kuokoa wakati katika kuwazoeza washiriki wapya wa Betheli. Je, njia hiyo ya kufundisha ingeweza kutumiwa katika njia nyinginezo ili kusaidia katika kazi ya duniani pote ya kufanya wanafunzi? Baadhi ya ndugu waliamini kwamba ingewezekana.

      Kama tokeo, katika Oktoba 1990, kaseti ya vidio “Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name” ilitolewa. Itikio lilikuwa la kutokeza. Maombi mengi ajabu kwa ajili ya programu zaidi kama hizo yalipokewa. Ili kujazia uhitaji huo, idara mpya iitwayo Huduma za Vidio ilianzishwa.

      Mashahidi waliokuwa wataalamu katika uwanja huo wa vidio walitoa msaada wao kwa furaha. Vifaa vilipatikana. Vyumba vya kurekodia vikatayarishwa. Kikundi cha wapiga-picha kilianza kusafiri kwenda nchi mbalimbali ili kupiga picha watu na vitu ambavyo vingeweza kutumiwa katika maonyesho ya vidio yaliyobuniwa ili kujenga imani. Okestra ya kimataifa ya Mashahidi pekee iliyokuwa imesaidia tena na tena katika miradi ya pekee iliandaa muziki ambao ungefanya maonyesho ya vidio yawe bora.

      Mipango ilifanywa ili kufikia vikundi zaidi vya lugha. Kufikia katikati ya 1992, vidio “Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name” ilikuwa ikipelekwa katika lugha nyingi. Ilikuwa imerekodiwa katika lugha 25, kutia ndani nyinginezo za Ulaya Mashariki. Kwa kuongezea, mipango ilikuwa inafanywa ili kuirekodi katika Kimandarini na pia Kikantoni kwa ajili ya Wachina. Sosaiti pia ilikuwa imepata idhini ya kutokeza na kugawanya “Purple Triangles,” vidio kuhusu uaminifu-maadili wa familia moja ya Mashahidi katika Ujerumani wakati wa utawala wa Wanazi. Katika kipindi cha miaka miwili, kaseti za vidio zaidi ya milioni moja zilikuwa zimetokezwa ili zitumiwe na Mashahidi wa Yehova katika huduma yao.

      Uangalifu wa pekee ulitolewa kwa mahitaji ya viziwi. Chapa ya “Jehovah’s Witnesses—The Organization Behind the Name” ilitokezwa katika Lugha ya Ishara ya Amerika. Na utafiti ulifanywa kwa kusudi la kuandaa vidio ambazo zingewafaa viziwi katika nchi nyinginezo.

      Hilo lilipokuwa likifanywa, kazi ilianza ya kutokeza mfululizo ambao ungesaidia kujenga imani katika kitabu ambacho ndicho msingi wenyewe wa imani ya Kikristo, Biblia. Kufikia Septemba 1992, sehemu ya kwanza ya programu hiyo, “The Bible—Accurate His­tory, Reliable Prophecy,” ilikamilishwa katika Kiingereza, na chapa katika lugha nyinginezo zilikuwa zikitayarishwa.

      Kaseti za vidio hazichukui hata kidogo mahali pa vichapo au kutoa ushahidi kibinafsi. Vichapo vya Sosaiti vinaendelea kujazia sehemu ya maana katika kueneza habari njema. Kazi ya nyumba hadi nyumba ya Mashahidi wa Yehova inabaki ikiwa sehemu ya msingi imara wa Kimaandiko ya huduma yao. Hata hivyo, sasa kaseti za vidio zinategemeza hizo, zikiwa vifaa vyenye thamani vya kusitawishia imani katika ahadi zenye thamani za Yehova na kuchochea uthamini kwa yale ambayo anaendesha sasa duniani katika siku yetu.

      [Picha]

      1. Baada ya mambo ya msingi yaliyotiwa ndani kujulikana, picha za vidio huanza kupigwa huku hati ikiendelea kukuzwa

      2. Picha huteuliwa na jinsi zinavyofuatana huamuliwa wakati wa kutayarisha vidio mapema

      3. Muziki wa okestra ambao umetungwa kipekee hurekodiwa ili kufanya wonyesho uwe bora

      4. Muziki wa kubonyezwa kwa vidole na sauti zinazofaa huwekwa pamoja na masimulizi na picha

      5. Sauti na picha hutayarishwa kwa mara ya mwisho

      [Picha katika ukurasa wa 576]

      Uchapaji halisi wa vichapo hivi vya mapema ulifanywa na mashirika ya kibiashara

      [Picha katika ukurasa wa 577]

      C. A. Wise alifanya jaribu la kuona ikiwa Wanafunzi wa Biblia wapaswa kufungua tena makao makuu katika Brooklyn

      [Picha katika ukurasa wa 579]

      Matbaa ya kwanza yenye mabamba- mviringo ya Sosaiti ilitumiwa kuchapa nakala 4,000,000 za “Golden Age” Na. 27 yenye maneno ya kuchoma

      [Picha katika ukurasa wa 580]

      R. J. Martin, (kulia), mwangalizi wa kwanza wa kiwanda cha Sosaiti cha Brooklyn, akizungumza na Ndugu Rutherford

      [Picha katika ukurasa wa 583]

      Kimojawapo viwanda vya kuchapa vya kwanza vya Sosaiti katika Ulaya (Bern, Uswisi)

      [Picha katika ukurasa wa 584]

      Katika Magdeburg, Ujerumani, Sosaiti ilianzisha kiwanda cha kuchapa wakati wa miaka ya 1920

      [Picha katika ukurasa wa 590, 591]

      Elandsfontein, Afrika Kusini (1972)

      [Picha katika ukurasa wa 590]

      Numazu, Japani (1972)

      [Picha katika ukurasa wa 590]

      Strathfield, Australia (1972)

      [Picha katika ukurasa wa 590]

      São Paulo, Brazili (1973)

      [Picha katika ukurasa wa 591]

      Lagos, Nigeria (1974)

      [Picha katika ukurasa wa 591]

      Wiesbaden, Ujerumani (1975)

      [Picha katika ukurasa wa 591]

      Toronto, Kanada (1975)

      [Picha katika ukurasa wa 597]

      Nambari nyingi zinazowakilisha herufi zimefanyizwa na Mashahidi ili kutimiza mahitaji ya fasihi za Biblia katika lugha nyingi (Brooklyn, N.Y.)

      [Picha katika ukurasa wa 599]

      Vituo vya kompyuta za rangi huwezesha wasanii wa picha kuweka picha mahali pafaapo, kuondoa sehemu zisizotakwa, na kuzifanya ziwe bora kielektroni

      [Picha katika ukurasa wa 602]

      Mashahidi wa Yehova hutumia mifumo ya kompyuta ili kuongeza mwendo na kufanya kazi ya kutafsiri Biblia iwe bora (Korea)

  • Kuchapa na Kugawanya Neno Takatifu la Mungu Mwenyewe
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Sura ya 27

      Kuchapa na Kugawanya Neno Takatifu la Mungu Mwenyewe

      UPANDE wa nje wa jengo kuu la kiwanda kwenye makao yao makuu, Mashahidi wa Yehova kwa miongo ya miaka wameonyesha ishara inayohimiza kila mtu hivi: “Soma Neno la Mungu Biblia Takatifu Kila Siku.”

      Wao wenyewe ni wanafunzi wenye bidii wa Neno la Mungu. Kwa muda wa miaka wametumia aina mbalimbali za tafsiri ya Biblia katika jitihada ya kufahamu maana halisi ya Maandiko ya awali yaliyopuliziwa roho. Kila Shahidi hutiwa moyo kuwa na programu ya kibinafsi ya kusoma Biblia kila siku. Kwa kuongezea funzo lao la habari kuu ya Neno la Mungu, wao huendelea kusoma na kuzungumza juu ya Biblia yenyewe katika mikutano yao ya kutaniko. Kusudi lao si kutafuta maandiko ili wategemeze mawazo yao. Wao huitambua Biblia kuwa Neno lililopuliziwa la Mungu mwenyewe. Wanajua kwamba hiyo hutoa karipio na nidhamu, nao hujitahidi sana kupatanisha kufikiri kwao na mwenendo wao na yale inayosema.—2 Tim. 3:16, 17; linganisha 1 Wathesalonike 2:13.

      Kwa sababu ya kusadikishwa kwao kwamba Biblia ni Neno takatifu la Mungu mwenyewe na kwa sababu wanajua habari njema za utukufu ambazo inazo, Mashahidi wa Yehova ni wahubiri na wagawanyaji wa Biblia wenye bidii.

      Sosaiti Yenye Kuchapa Biblia

      Ilikuwa katika 1896 kwamba rejezeo la moja kwa moja kwenye Biblia lilitiwa rasmi katika jina la shirika halali lililokuwa likitumiwa wakati huo na Wanafunzi wa Biblia katika kazi yao ya kuchapa. Wakati huo Zion’s Watch Tower Tract Society ilikuja kuitwa kihalali Watch Tower Bible and Tract Society.a Sosaiti haikuwa mchapaji na mjalidi wa Biblia mara hiyo, lakini ilikuwa mtangazaji wazo mwenye bidii, ikipanga mambo mengi hususa, ikiandaa mambo ya ziada yenye thamani, na kisha kupanga na mashirika ya kibiashara ili yazichape na kuzijalidi.

      Hata kabla ya 1896, Sosaiti ilikuwa ikifanya mengi ikiwa mgawanyaji wa Biblia. Ilivuta fikira kwenye tafsiri mbalimbali za Biblia zilizopatikana, ikazinunua kwa wingi ili iweze kuzipata kwa bei nafuu, na kisha ikaziuza kwa bei ambayo nyakati nyingine ilikuwa asilimia 35 tu ya ile bei ya kawaida, si ili ipate faida ya kibiashara bali ili itoe utumishi kwa wasomaji wayo. Miongoni mwa Biblia hizo kulikuwa na chapa nyingi za King James Version zilizokuwa rahisi kubeba na kutumia, pia ‘Biblia za Walimu’ (King James Version ikiwa na misaada kama konkodansi, ramani, na marejezo ya pambizoni) zilizokuwa kubwa zaidi, The Emphatic Diaglott ikiwa na fasili ya mstari kati ya mstari wa Kigiriki na Kiingereza, tafsiri ya Leeser iliyotia maandiko ya Kiingereza kando ya yale ya Kiebrania, tafsiri ya Murdock kutoka Siria ya kale, The Newberry Bible yenye marejezo ya pambizoni yaliyoelekeza fikira kwenye sehemu ambazo jina la kimungu lilitokea katika lugha ya awali pamoja na mambo mengi yenye thamani yaliyoonyeshwa katika maandiko ya Kiebrania na Kigiriki, New Testament ya Tischendorf yenye marejezo ya vielezi-chini yaliyoonyesha maelezo tofauti-tofauti katika hati tatu kati ya zile za Biblia ya Kigiriki ya kale zilizo kamili zaidi (Sinaitic, Vatican, na Alexandrine), Biblia ya Variorum yenye vielezi-chini vilivyoonyesha si maandishi tofauti ya hati za kale tu bali pia tafsiri mbalimbali za sehemu za maandiko za wanachuo mashuhuri, na tafsiri halisi ya Young. Sosaiti pia ilitoa misaada kama vile Cruden’s Concordance na Analytical Concordance ya Young yenye maelezo juu ya maneno ya awali ya Kiebrania na Kigiriki. Katika miaka iliyofuata, mara nyingi Mashahidi wa Yehova duniani pote walipata maelfu mengi ya Biblia kutoka kwa sosaiti za Biblia katika lugha zozote zilizopatikana na wakazigawanya.

      Mapema kama 1890, kulingana na ithibati inayopatikana, Sosaiti ilipanga kuwa na uchapaji wa pekee, wenye jina layo, wa Chapa ya Pili ya The New Testament Newly Translated and Critically Emphasised, kama ilivyotayarishwa na mtafsiri wa Biblia Mwingereza Joseph B. Rotherham. Kwa nini tafsiri hiyo? Kwa sababu ya uhalisi wayo na jitihada yayo ya kunufaika kikamili na utafiti uliokuwa umefanywa ili kuwa na maandiko ya Kigiriki yaliyo sahihi zaidi na kwa sababu msomaji alisaidiwa na alama zilizotumiwa na mtafsiri ili kutambulisha ni maneno au semi gani zilizokaziwa kipekee katika maandiko ya Kigiriki.

      Katika 1902 uchapaji wa pekee wa Chapa ya Mistari Sambamba ya Biblia ya Holman ulifanywa kwa mpango wa Watch Tower Society. Ilikuwa na pambizo zilizo pana ambazo ndani yazo kulichapwa marejezo ya mahali katika vichapo vya Watch Tower ambapo mistari mbalimbali ilielezwa, na pia ilikuwa na faharisi ikiorodhesha vichwa vingi vya habari pamoja na mitajo ya Maandiko na marejezo yenye msaada kwenye vichapo vya Sosaiti. Biblia hiyo ilikuwa na maneno ya tafsiri mbili—tafsiri ya King James ikiwa juu ya ile ya Revised Version mahali palipokuwa na tofauti yoyote. Pia ilitia ndani konkodansi yenye kutia mambo mengi iliyofahamisha mtumizi maana mbalimbali za maneno ya lugha ya awali.

      Mwaka uo huo, Watch Tower Society ilimiliki mabamba ya kuchapia ya The Emphatic Diaglott, yanayotia ndani maandiko ya Kigiriki ya J. J. Griesbach ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo (chapa ya 1796-1806) pamoja na tafsiri ya Kiingereza ya mistari kati ya mistari. Pamoja na hiyo kulikuwa na fasili ya maandiko ya Benjamin Wilson mzaliwa wa Uingereza, aliyekuwa akiishi Geneva, Illinois, Marekani. Mabamba hayo na haki ya kuwa wachapaji pekee yalikuwa yamenunuliwa na kisha Sosaiti ikapewa kuwa zawadi. Baada ya nakala ambazo tayari zilikuwa katika akiba kuweza kupelekewa watu, mipango ilifanywa na Sosaiti ili nakala zaidi zitokezwe, na hizo zilipatikana katika 1903.

      Miaka minne baadaye, katika 1907, Chapa ya Wanafunzi wa Biblia ya King James Version ilichapwa. “Kitabu cha Walimu wa Biblia Waberoya” kilijalidiwa pamoja nayo ikiwa nyongeza. Hiyo ilitia ndani maelezo hususa ya mistari kutoka sehemu zote za Biblia, pamoja na marejezo kwenye vichapo vya Watch Tower kwa ajili ya maelezo kamili zaidi. Chapa yenye nyongeza iliyopanuliwa zaidi ilichapwa mwaka mmoja hivi baadaye.

      Biblia hizo ziliagizwa kutoka kwa wachapaji na wajalidi katika vifungu vya kati ya 5,000 na 10,000 wakati mmoja, ili gharama isiwe kubwa. Sosaiti ilitamani kufanya tafsiri mbalimbali za Biblia na vifaa vya utafiti vinavyohusiana vipatikane kwa urahisi kwa watu wengi kadiri iwezekanavyo.

      Kisha katika 1926 Watch Tower Society ilichukua hatua kubwa kwenda mbele katika kuhusika kwayo katika kuchapa Biblia.

      Kuchapa Biblia Kwenye Matbaa Yetu Wenyewe

      Ilikuwa miaka 36 baada ya Watch Tower Bible and Tract Society kuanza kutangaza Biblia kwa mara ya kwanza, kwamba iliweza kuchapa na kujalidi Biblia katika kiwanda chayo yenyewe. Biblia ya kwanza kutokezwa hivyo ilikuwa The Emphatic Diaglott, ambayo mabamba yayo yalikuwa mali ya Sosaiti kwa miaka 24. Katika Desemba 1926 Biblia hiyo ilichapwa kwenye matbaa-tambarare katika kiwanda cha Sosaiti cha Concord Street katika Brooklyn. Kufikia sasa, 427,924 yazo zimetokezwa.

      Miaka 16 baadaye, katikati ya Vita ya Ulimwengu 2, Sosaiti ilianza kuchapa Biblia yote. Kwa kusudi hilo, mabamba ya King James Version yenye marejezo ya pambizoni yalinunuliwa katika 1942 kutoka kwa Kampuni ya A. J. Holman, ya Philadelphia, Pennsylvania. Tafsiri hiyo ya Biblia yote katika Kiingereza ilitokezwa, si kutoka kwa Vulgate ya Latini, bali kutoka kwa wanachuo walioweza kulinganisha tafsiri za mapema na Kiebrania Kiaramu, na Kigiriki cha awali. Konkodansi iliyotayarishwa na watumishi wa Yehova 150 wenye kushirikiana iliongezwa. Hiyo ilibuniwa kipekee ili kusaidia Mashahidi wa Yehova wapate upesi maandiko yanayofaa wanapokuwa katika huduma ya shambani na hivyo watumie Biblia kwa matokeo ikiwa “upanga wa roho,” ili kuondolea mbali na kufunua uwongo wa kidini. (Efe. 6:17, NW) Ili kufanya Biblia ipatikane kwa watu kila mahali kwa gharama ya chini, ilichapwa kwenye matbaa-mabamba-mviringo ya web—jambo ambalo halikuwa limepata kujaribiwa na wachapaji wengine wa Biblia. Kufikia 1992, jumla ya 1,858,368 ya Biblia hizo zilikuwa zimetokezwa.

      Tamaa ya Mashahidi wa Yehova ilikuwa zaidi tu ya kutia nakala za Biblia, kitabu chenyewe, mikononi mwa watu. Mashahidi walitaka kusaidia watu wajue jina la kibinafsi, pamoja na kusudi, la mtungaji wacho wa kimungu, Yehova Mungu. Kulikuwa na tafsiri katika Kiingereza—American Standard Version ya 1901—iliyotumia jina la kimungu katika sehemu zaidi ya 6,870 ambazo ilitokea katika vyanzo ambavyo kutoka kwavyo watafsiri walifanya kazi. Katika 1944, baada ya miezi kadhaa ya maafikiano, Watch Tower Society ilinunua haki ya kufanyiza seti za mabamba zenye mambo mengi ya Biblia hiyo kutoka kwa mabamba na maandishi yaliyotolewa na kampuni ya Thomas Nelson and Sons, ya New York. Wakati wa miaka 48 iliyofuata, nakala 1,039,482 zilitokezwa.

      Steven Byington, wa Ballard Vale, Massachusetts, Marekani, alikuwa pia amefanyiza tafsiri ya Biblia ya Kiingereza cha kisasa ambayo ilitia jina la kimungu mahali palo pafaapo. Watch Tower Society ilimiliki hati ambayo haikuwa imechapwa bado katika 1951 na ikapata haki pekee ya kuchapa katika 1961. Tafsiri hiyo kamili ilichapwa katika 1972. Hadi kufikia 1992, kulikuwa na 262,573 zilizotokezwa.

      Hata hivyo, wakati uo huo, jambo jingine lilikuwa likitokea.

      Kutokeza Biblia New World Translation

      Ilikuwa mapema katika Oktoba 1946 kwamba Nathan H. Knorr, aliyekuwa msimamizi wa Watch Tower Society wakati huo, alipendekeza kwanza kwamba Sosaiti itokeze tafsiri mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Kazi yenyewe ya tafsiri hiyo ilianza Desemba 2, 1947. Tafsiri yote ilipitiwa tena kwa uangalifu na halmashauri yote ya tafsiri, wote wakiwa Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho. Kisha, mnamo Septemba 3, 1949, Ndugu Knorr alifanya mkutano wa pamoja na baraza la wakurugenzi wa mashirika ya Sosaiti ya New York na Pennsylvania. Aliwatangazia kwamba New World Bible Translation Committee ilikuwa imekamilisha kazi ya tafsiri ya lugha ya kisasa ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na ilikuwa imeikabidhi Sosaiti ili ichapwe.b Hiyo ilikuwa tafsiri mpya kutoka kwa Kigiriki cha awali.

      Je, kwa kweli kulikuwa na uhitaji wa tafsiri nyingine? Tayari wakati huo, Biblia yote ilikuwa imechapwa katika lugha 190 na angalau sehemu yayo ilikuwa imetafsiriwa katika lugha na lahaja 928 zaidi. Nyakati fulani-fulani, Mashahidi wa Yehova wametumia nyingi za tafsiri hizo. Lakini jambo hakika ni kwamba nyingi zazo zilifanyizwa na makasisi na wamishonari wa mafarakano ya kidini ya Jumuiya ya Wakristo, na kwa kadiri inayotofautiana tafsiri zao ziliongozwa na falsafa za kipagani na mapokeo yasiyo ya kimaandiko ambayo mifumo yao ya kidini ilirithi kutoka zamani kutia na kupendelea uhakiki wa Biblia. Zaidi ya hayo, hati za Biblia za kale zaidi na zenye kutegemeka zaidi zilikuwa zikipatikana. Lugha ya Kigiriki ya karne ya kwanza ilikuwa ikieleweka kwa uwazi zaidi kama tokeo la uvumbuzi wa kiakiolojia. Pia, lugha ambazo katika hizo tafsiri hufanyizwa hupata mabadiliko katika muda wa miaka.

      Mashahidi wa Yehova walitaka tafsiri ambayo ilitia ndani manufaa za usomi wa karibuni zaidi, tafsiri ambayo haikuwa imeongozwa na mafundisho na mapokeo ya Jumuiya ya Wakristo, tafsiri halisi ambayo ilitoa kwa uaminifu yale yaliyokuwa katika maandishi ya awali na hivyo ingeweza kuandaa msingi wa ukuzi wenye kuendelea katika ujuzi wa kweli ya kimungu, tafsiri ambayo ingekuwa wazi na yenye kueleweka kwa wasomaji wa kisasa. Biblia New World Translation of the Christian Greek Scriptures, iliyotolewa katika 1950, ilijazia uhitaji huo—angalau kwa sehemu hiyo ya Biblia. Mashahidi wa Yehova walipoanza kuitumia, wengi walisisimuliwa si kwa sababu tu lugha yayo ya kisasa ilikuwa rahisi kusoma bali kwa sababu walijua kwamba walikuwa wakipata uelewevu wa wazi zaidi katika maana ya Neno la Mungu lililopuliziwa.

      Mojawapo mambo yenye kutokeza katika tafsiri hiyo ni kurudishwa kwa jina la kimungu, jina la kibinafsi la Mungu, Yehova, mara 237 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Hiyo haikuwa tafsiri ya kwanza kurudisha jina hilo.c Lakini huenda ilikuwa ya kwanza kulirudisha kwa upatani katika maandiko yenyewe kutoka Mathayo hadi Ufunuo. Mazungumzo marefu juu ya jambo hilo katika dibaji yalionyesha msingi ufaao wa yale yaliyofanywa.

      Baadaye, kuanzia mwaka 1953, Maandiko ya Kiebrania yalitafsiriwa katika Kiingereza na yakatolewa kwa kuendelea, katika mabuku matano tofauti. Kama vile ilivyokuwa imefanywa na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, uangalifu ulitumiwa ili kutafsiri yale yaliyokuwa katika maandiko ya lugha ya awali kwa uhalisi kwa kadiri iwezekanavyo. Uangalifu wa pekee ulitolewa ili kufanya matumizi ya maneno yapatane, yakionyesha kwa usahihi kitendo au hali iliyoonyeshwa katika vitenzi, na kutumia lugha rahisi ambayo ingeeleweka kwa urahisi na wasomaji wa kisasa. Mahali popote ambapo Tetragramatoni ilitokea katika maandiko ya Kiebrania, ilifasiliwa kwa kufaa kuwa jina la kibinafsi la Mungu, badala ya kutumia neno jingine tofauti, kama vile ilivyokuwa kawaida katika tafsiri nyingine nyingi. Makala za nyongeza na vielezi-chini katika mabuku hayo yaliwawezesha wanafunzi waangalifu wachunguze msingi wa fasili iliyotumiwa.

      Katika Machi 13, 1960, New World Bible Translation Committee ilikamilisha usomaji wayo wa mwisho wa maandiko ya sehemu ya Biblia iliyokusudiwa iwe ya buku la tano. Hiyo ilikuwa miaka 12, miezi 3, na siku 11 baada ya kutafsiri kwenyewe kwa Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kuanza. Miezi michache baadaye, buku hilo la mwisho la Maandiko ya Kiebrania, likiwa limechapwa, lilitolewa ili ligawanywe.

      Badala ya kuacha baada ya mradi huo kwisha, halmashauri ya tafsiri iliendelea kufanya kazi. Pitio lenye kutia mambo mengi la tafsiri yote lilifanywa. Kisha, Biblia ya New World Translation of the Holy Scriptures, chapa iliyosahihishwa katika buku moja, ilitangazwa na Watch Tower Society katika 1961. Ilifanywa ipatikane ili igawanywe kwa dola moja tu ili kwamba kila mtu, bila kujali hali yake ya kiuchumi, aweze kupata nakala ya Neno la Mungu.

      Miaka miwili baadaye chapa ya pekee ya wanafunzi ilitangazwa. Hiyo iliweka pamoja mabuku yote ya awali katika jalada moja, yakiwa hayajasahihishwa, yakiwa na maelfu ya vielezi-chini vya thamani vya maandiko, kutia na mazungumzo ya dibaji na nyongeza. Pia ilidumisha marejezo-vitomeo yenye thamani yaliyoelekeza wasomaji kwenye maneno yaliyofanana, fikira au matukio yanayofanana, habari-maisha ya watu, mambo mengi ya kijiografia, kutimizwa kwa unabii mwingi, na manukuu ya moja kwa moja katika au kutoka kwa sehemu nyingine za Biblia.

      Tangu chapa ya buku moja ya 1961 ilipotangazwa, nyingine nne zilizosahihishwa na kutiwa habari za kisasa zimetolewa. Chapa ya karibuni zaidi kati ya hizo ilikuwa katika 1984, wakati ambapo chapa yenye maandishi makubwa yenye nyongeza yenye mambo mengi, marejezo ya pambizoni kama 125,000, vielezi-chini vyenye kuelimisha vipatavyo 11,400, na konkodansi ilitangazwa. Sehemu mbalimbali za chapa hiyo husaidia wanafunzi waelewe kwa nini maandiko mbalimbali yahitaji kufasiliwa katika njia fulani ili kuwa sahihi, kutia na wakati ambapo maandiko yanaweza kufasiliwa kwa usahihi katika zaidi ya njia moja. Marejezo-vitomeo pia huwasaidia kuthamini upatano unaokamatana kati ya vitabu mbalimbali vya Biblia.

      Ikiwa sehemu ya jitihada nyingi za New World Bible Translation Committee ili kusaidia wapendao Neno la Mungu kujua sana yaliyomo katika maandiko ya Koine ya awali (Kigiriki cha kawaida) ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, halmashauri hiyo ilitokeza The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures. Hiyo ilitangazwa kwanza na Watch Tower Society katika 1969 na kisha ikatiwa habari za kisasa katika 1985. Ina The New Testament in the Original Greek, kama ilivyotungwa na B. F. Westcott na F. J. A. Hort. Upande wa kulia wa ukurasa huo kuna maandiko ya New World Translation (chapa ya 1984 iliyosahihishwa na kutiwa habari za sasa). Lakini, kati ya mistari ya maandiko ya Kigiriki, kuna tafsiri nyingine, fasili iliyo halisi sana, ya neno kwa neno ya yale ambayo Kigiriki husema hasa kulingana na maana ya msingi na aina ya sarufi ya kila neno. Hilo huwawezesha hata wanafunzi ambao hawawezi kusoma Kigiriki wapate kujua yale hasa yaliyoko katika maandiko ya awali ya Kigiriki.

      Je, kazi hiyo ya New World Translation ingenufaisha tu wale ambao wangeweza kusoma Kiingereza? Katika mahali pengi wamishonari wa Watch Tower walikuwa wakiona vigumu kupata Biblia za lugha za wenyeji za kutosha ili kuzigawanya kwa watu waliotamani kupata nakala za kibinafsi za Neno la Mungu. Katika sehemu fulani za ulimwengu, ilikuwa kawaida kwa wamishonari hao kuwa wagawanyaji wakuu wa Biblia zilizochapwa na sosaiti nyinginezo za Biblia. Lakini hilo halikuwapendeza wafanyakazi wa kidini waliowakilisha sosaiti hizo za Biblia. Isitoshe, baadhi ya Biblia hizo hazikuwa tafsiri zilizo bora zaidi.

      Kutafsiri Katika Lugha Nyinginezo

      Ule mwaka ambao New World Translation iliyo kamili ilipotokea kwa mara ya kwanza ikiwa katika buku moja, yaani, mwaka 1961, kikundi cha watafsiri wenye ujuzi kilikutana ili kutafsiri maandiko ya Kiingereza katika lugha nyinginezo sita zilizotumiwa sana—Kiholanzi, Kifaransa, Kijerumani, Kiitalia, Kireno, na Kihispania. Kutafsiri tena kutoka Kiingereza, pamoja na kulinganisha na Kiebrania na Kigiriki, kuliwezekana kwa sababu ya uhalisi wa tafsiri ya Kiingereza yenyewe. Watafsiri hao walifanya kazi wakiwa halmashauri ya kimataifa katika kushirikiana na New World Bible Translation Committee, kwenye makao makuu ya Sosaiti katika Brooklyn, New York. Katika 1963 Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yalichapwa na kutolewa katika lugha zote sita.

      Kufikia 1992 New World Translation of the Holy Scriptures iliyo kamili ilipatikana katika lugha 12—Kicheki, Kidenmark, Kiholanzi, Kiingereza, Kifaransa, Kijerumani, Kiitalia, Kijapani, Kireno, Kislovaki, Kihispania, na Kisweden. Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yalipatikana katika lugha nyingine mbili. Hilo lilimaanisha kwamba tafsiri hiyo ilipatikana katika lugha za kienyeji za watu 1,400,000,000 hivi, au zaidi ya robo ya idadi ya watu wote duniani, na wengi zaidi walikuwa wakinufaika nayo kupitia kutafsiriwa kwa madondoo yayo katika lugha nyinginezo 97 katika Mnara wa Mlinzi. Hata hivyo wale waliosoma lugha hizo 97, walikuwa na hamu ya kupata New World Translation iliyo kamili katika lugha yao wenyewe. Kufikia 1992, tayari mipango ilikuwa ikiendelea ili kutokeza tafsiri hiyo katika lugha 16 kati ya hizo na kukamilisha Maandiko ya Kiebrania katika lugha 2 zilizokuwa na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo pekee.

      Kwa kuwa uchapaji wa Biblia hizo ulifanywa katika viwanda vya Sosaiti na wafanyakazi wa kujitolea, iliwezekana kuzitoa kwa gharama ya chini. Katika 1972 wakati Shahidi kutoka Austria alipomwonyesha mjalidi vitabu mmoja New World Translation katika Kijerumani na kumwuliza anafikiri hiyo ingegharimuje, mtu huyo alishangaa kujua kwamba mchango uliodokezwa ulikuwa sehemu moja kwa kumi ya bei aliyotaja.

      Mifano fulani inaonyesha matokeo ya tafsiri hii. Katika Ufaransa, kwa karne nyingi Kanisa Katoliki lilikuwa limewakataza watu wa kawaida wasiwe na Biblia. Tafsiri za Wakatoliki zilizopatikana zilikuwa zenye gharama kubwa, na ni nyumba chache zilizokuwa nazo. Biblia New World Translation of the Christian Greek Scriptures ilitolewa katika Kifaransa mwaka 1963, ikifuatwa na Biblia yote katika 1974. Kufikia 1992 jumla ya pamoja ya nakala 2,437,711 za New World Translation zilikuwa zimesafirishwa ili zigawanywe katika Ufaransa; na idadi ya Mashahidi wa Yehova katika Ufaransa ikaongezeka kwa asilimia 488 wakati wa kipindi hichohicho, kufikia jumla ya 119,674.

      Hali ilikuwa iyo hiyo katika Italia. Kwa muda mrefu watu walikuwa wamekatazwa kuwa na nakala ya Biblia. Baada ya kutolewa kwa chapa ya Kiitalia ya New World Translation hadi kufikia 1992, kulikuwa na nakala 3,597,220 zilizogawanywa; nyingi zazo zikiwa Biblia kamili. Watu walitaka kujichunguzia wenyewe yale yaliyomo katika Neno la Mungu. Kwa kupendeza, wakati wa kipindi hichohicho, idadi ya Mashahidi wa Yehova katika Italia ilipanda sana—kutoka 7,801 hadi 194,013.

      Wakati New World Translation of the Christian Greek Scriptures ilipotolewa katika Kireno, kulikuwa na Mashahidi 30,118 tu katika Brazili na 1,798 katika Ureno. Wakati wa miaka iliyofuata, hadi kufikia 1992, jumla ya nakala 213,438 za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo na nakala 4,153,738 za Biblia kamili katika Kireno zilipelekwa kwa watu mmoja-mmoja na makutaniko katika nchi hizo. Matokeo yalikuwa nini? Katika Brazili, wasifaji wa Yehova waliongezeka wakawa mara 11 zaidi; na katika Ureno, wakawa mara 22 zaidi. Makumi ya maelfu ya watu ambao hawakuwa wamepata kuwa na Biblia walishukuru kupata moja, na wengine walithamini kuwa na Biblia iliyotumia maneno ambayo wangeweza kuelewa. Wakati New World Translation of the Holy Scriptures—With References ilipotolewa katika Brazili, vyombo vya habari vilisema kwamba hiyo ilikuwa tafsiri iliyo kamili zaidi (yaani, yenye marejezo-vitomeo na vielezi-chini vingi) iliyopatikana nchini. Pia ilisema kwamba uchapaji wa kwanza ulikuwa mkubwa mara kumi zaidi ya chapa nyingi za kitaifa.

      Chapa ya Kihispania ya New World Translation of the Christian Greek Scriptures ilitolewa pia katika 1963, ikifuatwa na Biblia kamili katika 1967. Kulikuwa na nakala 527,451 za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zilizochapwa, na baadaye, hadi kufikia 1992, jumla ya nakala 17,445,782 za Biblia kamili katika Kihispania. Hiyo ilitokeza ongezeko lenye kutazamisha la idadi ya wasifaji wa Yehova katika nchi zinazosema Kihispania. Hivyo, kuanzia 1963 hadi 1992, katika nchi ambazo watu wengi husema Kihispania ambapo Mashahidi wa Yehova huendelea na huduma yao, idadi zao zilikua kutoka 82,106 hadi 942,551. Na katika Marekani, mwaka 1992, kulikuwa na Mashahidi wa Yehova wengineo kama 130,224 wenye kusema Kihispania.

      Haikuwa katika milki za Jumuiya ya Wakristo tu ambako New World Translation ilipokewa kwa idili. Katika mwaka wa kwanza wa kuchapwa kwa chapa ya Kijapani, ofisi ya tawi ya Japani ilipokea maagizo ya nakala nusu milioni.

      Kufikia 1992 kuchapwa kwa New World Translation of the Holy Scriptures iliyo kamili, katika lugha 12 zilizopatikana wakati huo, kulifikia nakala 70,105,258. Zaidi ya hiyo, nakala 8,819,080 za sehemu za tafsiri hiyo zilikuwa zimechapwa.

      Kutoa Biblia Katika Namna Nyingi

      Kutumiwa kwa kompyuta katika shughuli za Watch Tower Society, kuanzia 1977, kumesaidia katika kutokezwa kwa Biblia, kama vile ambavyo kumesaidia katika njia nyinginezo za shughuli za uchapaji. Imesaidia watafsiri waweze kuwa na upatani zaidi katika kazi yao; pia imefanya iwe rahisi zaidi kuchapa Biblia katika namna mbalimbali.

      Baada ya maandiko yote ya Biblia kutiwa ndani ya kompyuta, haikuwa vigumu kutumia mashine ya kupanga chapa kwa kupiga picha kielektroni ili kuchapa maandiko yakiwa katika unamnanamna wa ukubwa na sura. Kwanza, katika 1981, kulitokezwa chapa ya ukubwa wa kawaida katika Kiingereza yenye konkodansi na mambo mengine ya nyongeza yenye kusaidia. Hiyo ndiyo iliyokuwa chapa ya kwanza kuchapwa na Watch Tower Society kwenye matbaa ya ofseti ya web. Baada ya masahihisho kuingizwa katika maandishi yaliyohifadhiwa ndani ya kompyuta, chapa yenye maandishi makubwa ya Kiingereza ilitolewa katika 1984; hiyo ilitia ndani sehemu nyingi muhimu kwa ajili ya utafiti. Chapa ya ukubwa wa kawaida ya Biblia ya Kiingereza iyo hiyo iliyosahihishwa ilitolewa pia mwaka huo; marejezo-vitomeo na konkodansi ilitiwa ndani, lakini si vielezi-chini; na nyongeza yayo ilibuniwa ifae huduma ya shambani badala ya funzo la kina kirefu zaidi. Kisha, kwa manufaa ya wale waliotaka chapa ndogo sana ya mfukoni, hiyo ilitangazwa katika Kiingereza katika 1987. Chapa hizo zote zilitangazwa upesi katika lugha nyinginezo pia.

      Kwa kuongezea, uangalifu ulitolewa ili kusaidia wale wenye mahitaji ya pekee. Ili kusaidia wale ambao wangeweza kuona lakini ambao walihitaji maandishi makubwa sana, New World Translation iliyo kamili ya lugha ya Kiingereza katika mabuku manne makubwa ilitangazwa katika 1985. Upesi chapa iyo hiyo ilichapwa katika Kijerumani, Kifaransa, Kihispania, na Kijapani. Kabla ya hapo, katika 1983, New World Translation of the Christian Greek Scriptures, katika mabuku manne, ilikuwa imetolewa katika Braille (chapa ya vipofu) ya Kiingereza cha gredi ya pili. Katika muda wa miaka mingine mitano, New World Translation iliyo kamili ilikuwa imetokezwa katika Braille ya Kiingereza katika mabuku 18.

      Je, watu fulani wangesaidiwa ikiwa wangeweza kusikiliza rekodi ya Biblia? Bila shaka. Kwa hiyo Watch Tower Society ilianza kutokeza hiyo pia. Kaseti ya kwanza iliyorekodiwa ilikuwa The Good News According to John, katika Kiingereza, iliyotolewa katika 1978. Baadaye New World Translation yote katika Kiingereza ilifanywa ipatikane katika kaseti 75. Ile iliyoanza ikiwa kazi ndogo upesi ilikua ikawa mradi mkubwa. Upesi, ilipatikana katika lugha nyinginezo. Kufikia 1992 New World Translation, ikiwa yote au kwa sehemu, ilipatikana katika kaseti katika lugha 14. Mwanzoni, kazi ya baadhi ya matawi ilifanywa na kampuni za kibiashara. Hadi kufikia 1992, Watch Tower Society ilikuwa imetokeza kaseti kama hizo zaidi ya 31,000,000 kwa kutumia vifaa vyayo yenyewe.

      Manufaa za kaseti za Biblia na njia ambazo kwazo zilitumiwa yalizidi sana matarajio ya awali. Katika sehemu zote za dunia, watu walikuwa wakitumia vinanda vya kaseti. Wengi ambao hawangeweza kusoma walisaidiwa katika njia hiyo kunufaika kibinafsi kutokana na Neno takatifu la Mungu. Wanawake waliweza kusikiliza kaseti walipokuwa wakifanya kazi za nyumbani. Wanaume walizisikiliza kwenye vinanda vya magari yao walipokuwa wakisafiri kwenda kazini. Uwezo wa kufundisha wa Shahidi mmoja-mmoja ulifanywa kuwa bora waliposikiliza Neno la Mungu kwa ukawaida na kutoa uangalifu kwa matamshi ya majina ya Biblia na njia ambayo vifungu vya Maandiko vilisomwa.

      Kufikia 1992, chapa mbalimbali za New World Translation zilikuwa zikichapwa kwenye matbaa za Sosaiti katika Amerika Kaskazini na Kusini, Ulaya, na nchi za Mashariki. Jumla ya mabuku 78,924,338 yalikuwa yametokezwa na kufanywa yapatikane ili yagawanywe. Katika Brooklyn pekee, kulikuwa na matbaa kubwa tatu za ofseti ya web zenye mwendo wa kasi zilizotumiwa hasa kwa utokezaji wa Biblia. Kwa ujumla, matbaa hizo zaweza kutokeza Biblia 7,900 kwa saa, na nyakati nyingine zimehitajiwa zifanye kazi kwa wakati wa ziada.

      Hata hivyo, Mashahidi wa Yehova hutolea watu zaidi ya Biblia tu inayoweza kuwekwa tu juu ya rafu. Wao pia hutolea yeyote anayependezwa na Biblia—iwe anapata nakala kutoka kwa Mashahidi wa Yehova au la—funzo la Biblia nyumbani bila malipo. Mafunzo hayo hayaendelei daima. Baadhi ya wanafunzi huthamini kwa moyo yale wanayojifunza, wanakuwa Mashahidi waliobatizwa, na kisha kushiriki katika kufundisha wengine. Baada ya miezi kadhaa, ikiwa mtu hafanyi maendeleo yanayofaa katika kutumia yale ambayo anajifunza, mara nyingi mafunzo hukomeshwa ili kuendelea na watu wengine wanaopendezwa kikweli. Kufikia 1992, Mashahidi wa Yehova walikuwa wakiandalia watu mmoja-mmoja na wenye nyumba kama 4,278,127 utumishi wa funzo la Biblia nyumbani bila malipo, mara nyingi kila juma.

      Hivyo, Mashahidi wa Yehova ni watangazaji na wagawanyaji wa Biblia na ni walimu wa Neno takatifu la Mungu kwa njia isiyopata kufanywa na tengenezo jingine lolote.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kama ilivyoonyeshwa na Watch Tower la Julai 15, 1892 (uku. 210), jina Watch Tower Bible and Tract Society lilikuwa limetumiwa kwa miaka mingi kabla ya jina hilo kusajiliwa kihalali. Trakti iliyochapwa katika 1890 katika ule mfululizo wa trakti za Old Theology ilitambulisha watangazaji kuwa Tower Bible and Tract Society.

      b Tafsiri hiyo ilitolewa kwa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania ili ichapwe, pamoja na ombi kwamba majina ya watafsiri yasitangazwe kamwe. Walitaka heshima yote imwendee Yehova Mungu, Mtungaji wa Kimungu wa Neno lake lililopuliziwa.

      c Baadhi ya tafsiri za mapema zaidi katika Kiebrania, Kijerumani, na Kiingereza zilirudisha jina la kimungu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, pamoja na tafsiri nyingi za wamishonari.

      [Sanduku katika ukurasa wa 609]

      Tafsiri Mpya

      Wakati buku la kwanza la “New World Translation of the Hebrew Scriptures” lilipotangazwa, Alexander Thomson, mhakiki wa Biblia Mwingereza, aliandika: “Tafsiri za awali za Maandiko ya Kiebrania hadi lugha ya Kiingereza ni chache sana. Kwa hiyo inatupatia furaha kubwa kukaribisha kutangazwa kwa sehemu ya kwanza ya New World Translation [ya Maandiko ya Kiebrania], Mwanzo hadi Ruthu. . . . Tafsiri hiyo kwa wazi imefanya jitihada ya pekee ili isomeke kwa urahisi. Hakuna yeyote ambaye angeweza kusema imepungukiwa katika upya na uasili. Matumizi ya maneno hayategemei tafsiri za awali hata kidogo.”—“The Differentiator,” Juni 1954, uku. 131.

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 610]

      “Maandiko Yenye Msamiati wa Hapohapo”

      Katika “The Classical Journal,” Thomas N. Winter wa Chuo Kikuu cha Nebraska aliandika pitio la “The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures” ambayo alisema: “Hiyo ni tafsiri ya mistari kati ya mistari isiyo ya kawaida: uaminifu-maadili wa maandiko unadumishwa, na Kiingereza kinachotokea chini yayo ni maana ya neno la Kigiriki kimsingi. Hivyo sehemu ya mistari kati ya mistari ya kitabu hicho si tafsiri hata kidogo. Maandiko yenye msamiati wa hapohapo waieleza tafsiri hiyo kwa usahihi zaidi. Tafsiri katika Kiingereza safi hutokea katika safu nyembamba kwenye pambizo la upande wa kulia wa kurasa. . . .

      “Maandiko hayo yanategemea yale ya Brooke F. Westcott na Fenton J. A. Hort (1881, iliyotokezwa tena), lakini tafsiri iliyofanywa na halmashauri isiyojitambulisha ni ya kisasa kabisa na sahihi kwa upatani.”—Toleo la Aprili-Mei la 1974, kur. 375-376.

      [Picha]

      Chapa za 1969 na 1985

      [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 611]

      Maoni ya Mwanachuo Mwebrania

      Kuhusu “New World Translation,” Profesa Dakt. Benjamin Kedar, mwanachuo Mwebrania katika Israeli, alisema hivi katika 1989: “Katika utafiti wangu wa lugha kuhusu Biblia ya Kiebrania na tafsiri mbalimbali, mara nyingi mimi hurejezea chapa ya Kiingereza ya ile inayoitwa ‘New World Translation.’ Katika kufanya hivyo, mimi huona hisia yangu ikithibitishwa tena na tena kwamba kitabu hicho chaonyesha jitihada ya unyoofu ili kupata uelewevu wa maandiko kwa usahihi kwa kadiri iwezekanavyo. Ikitoa uthibitisho wa utaalamu mkubwa wa lugha ya awali, inatafsiri maneno ya awali katika lugha ya pili kwa njia yenye kueleweka bila kukengeuka isivyo lazima kwenye muundo ule wa Kiebrania. . . . Kila taarifa ya lugha huruhusu nafasi fulani ya kufasiri au kutafsiri. Kwa hiyo utatuzi wa kilugha katika chochote kile waweza kubishaniwa. Lakini sijapata kamwe kugundua katika ‘New World Translation’ nia yoyote yenye upendeleo ya kutia jambo lisilo la kimaandiko.”

      [Grafu katika ukurasa wa 613]

      (Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

      Ukuzi wa Mashahidi Tangu Kutangazwa kwa “New World Translation”

      Ufaransa

      150,000

      100,000

      50,000

      1963 1970 1980 1992

      Italia

      150,000

      100,000

      50,000

      1963 1970 1980 1992

      Ureno na Brazili

      300,000

      200,000

      100,000

      1963 1970 1980 1992

      Nchi Zenye Kusema Kihispania

      900,000

      600,000

      300,000

      1963 1970 1980 1992

      [Picha katika ukurasa wa 604]

      Tafsiri Chache Kati ya Zile Zilizotumiwa na Wanafunzi wa Biblia wa Ramaniema

      Tafsiri halisi ya Young

      Tafsiri ya Leeser (Kiebrania kando ya Kiingereza)

      “New Testament” ya Tischendorf (yenye fasili tofauti-tofauti kutoka hati za Kigiriki MSS)

      Tafsiri ya Murdock (kutoka Kisiria)

      “The Emphatic Diaglott” (Kigiriki hadi Kiingereza)

      Variorum Bible (yenye fasili mbalimbali za Kiingereza)

      “The Newberry Bible” (yenye maandishi ya thamani pambizoni)

      [Picha katika ukurasa wa 605]

      Utangulizi wa chapa ya Rotherham “New Testament” iliyochapwa kwa ajili ya Watch Tower Society karibu 1890

      [Picha katika ukurasa wa 606]

      Chapa ya Mistari Sambamba ya Biblia ya Holman, kama ilivyochapwa kwa mpango wa Watch Tower Society katika 1902

      [Picha katika ukurasa wa 606]

      Chapa ya Watchtower ya “King James Version,” yenye konkodansi iliyobuniwa kipekee (1942)

      [Picha katika ukurasa wa 607]

      “American Standard Version,” tafsiri inayotumia jina la kimungu, Yehova, mara zaidi ya 6,870; chapa ya Watchtower (1944)

      [Picha katika ukurasa wa 607]

      Tafsiri ya Byington (1972)

      [Picha katika ukurasa wa 608]

      “New World Translation,” iliyotolewa kwanza katika Kiingereza katika mabuku sita, kuanzia 1950 hadi 1960; baadaye iliunganishwa katika chapa ya pekee ya wanafunzi

      Ilitangazwa ikiwa buku moja lenye kutia mambo yote katika 1961

      Chapa ya maandishi makubwa, yenye marejezo kwa ajili ya funzo, ilitangazwa katika 1984

      [Picha katika ukurasa wa 612]

      “New World Translation” imetolewa katika lugha zaidi kwa kuendelea

      [Picha katika ukurasa wa 614]

      “New World Translation” katika chapa kubwa sana

      . . . katika Braille

      . . . katika kaseti

      . . . katika disketi za kompyuta

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki