Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • “Mwenyezi-Mungu . . . Amejaa Nguvu”
    Mkaribie Yehova
    • Eliya anatazama wonyesho wa nguvu nyingi za Mungu Mweza-Yote

      Sura ya 4

      “Mwenyezi-Mungu Amejaa Nguvu”

      1, 2. Eliya alikuwa ameona mambo gani ya ajabu maishani mwake, lakini aliona matukio gani ya kustaajabisha alipokuwa katika pango kwenye Mlima Horebu?

      ELIYA alikuwa ameona mambo ya ajabu hapo awali. Alikuwa ameona kunguru wakimletea chakula mara mbili kwa siku alipokuwa mafichoni. Alikuwa ameona unga na mafuta yaliyokuwa katika vyombo viwili yakitumiwa kwa muda mrefu sana wakati wa njaa kali. Hata alikuwa ameona moto ukishuka kutoka mbinguni baada ya kutoa sala. (1 Wafalme, sura ya 17, 18) Na bado, Eliya hakupata kuona tukio lolote la kustaajabisha kama matukio yafuatayo.

      2 Eliya aliyejikunyata kwenye mwingilio wa pango kwenye Mlima Horebu aliona mfululizo wa matukio yenye kustaajabisha. Kwanza upepo ulivuma. Haikosi ulivuma kwa nguvu sana, na kwa sauti kubwa sana kwa kuwa uliipasua milima na kuvunja-vunja miamba. Kisha kukawa na tetemeko la nchi, nishati kubwa sana iliibuka na kutikisa dunia kwa nguvu sana. Halafu kukawa na moto. Yaelekea Eliya alipigwa na joto kali sana moto huo uliposambaa kwenye eneo hilo.—1 Wafalme 19:8-12.

      “Na tazama, BWANA akapita”

      3. Eliya aliona uthibitisho wa sifa ipi ya Mungu, nasi tuna uthibitisho gani wa sifa hiyo?

      3 Matukio hayo mbalimbali ambayo Eliya aliona yalikazia jambo moja tu—yalidhihirisha nguvu nyingi za Yehova Mungu. Bila shaka, si lazima tuone muujiza ili tufahamu kwamba Mungu ana sifa hii. Sifa hii yaonekana waziwazi. Biblia yatuambia kwamba uumbaji unathibitisha ‘nguvu za Yehova za milele na Uungu’ wake. (Waroma 1:20) Hebu fikiria nuru yenye kupofusha na ngurumo za dhoruba ya radi, poromoko kubwa maridadi la maji, na anga pana kupindukia lililotapakaa nyota! Je, unaona nguvu za Mungu katika vitu hivyo? Lakini ni watu wachache tu ulimwenguni wanaotambua kikweli nguvu za Mungu. Na ni watu wachache hata zaidi walio na maoni yanayofaa kuhusu nguvu hizo. Hata hivyo, kufahamu sifa hii ya Mungu kunatupa sababu nyingi za kumkaribia Yehova zaidi. Katika sehemu hii, tutajifunza kwa undani kuhusu nguvu za Yehova zisizo na kifani.

      Sifa Muhimu ya Yehova

      4, 5. (a) Kuna uhusiano gani kati ya jina la Yehova na uwezo wake, au nguvu zake? (b) Kwa nini inafaa kwamba Yehova alitumia fahali kuwakilisha nguvu zake?

      4 Nguvu za Yehova hazina kifani. Andiko la Yeremia 10:6 lasema hivi: “Hapana hata mmoja aliye kama wewe, Ee BWANA; wewe ndiwe uliye mkuu, na jina lako ni kuu katika uweza.” Ona kwamba uweza, au nguvu, zinahusianishwa na jina la Yehova. Ni wazi kwamba jina hilo linamaanisha “Yeye Husababisha Kuwe.” Ni nini kinachomwezesha Yehova aumbe kitu chochote anachotaka na awe chochote anachotaka? Sababu moja ni nguvu zake. Naam, uwezo wa Yehova wa kutenda, na wa kutimiza mapenzi yake hauna mipaka. Nguvu hizo ni mojawapo ya sifa zake muhimu.

      5 Hatuwezi kamwe kufahamu nguvu kamili za Yehova, kwa hivyo yeye hutumia mifano ili kutusaidia. Kama tulivyoona, yeye hutumia fahali kuwakilisha nguvu zake. (Ezekieli 1:4-10) Mfano huo unafaa, kwa sababu hata fahali wa kufugwa ni kiumbe mkubwa na mwenye nguvu. Katika nyakati za Biblia, ilikuwa vigumu sana kwa wakazi wa Palestina kukutana na mnyama yeyote mwenye nguvu kuliko fahali. Lakini walimjua fahali mwingine mwenye kutisha zaidi—fahali-mwitu, au auroch, ambaye ametoweka kabisa sasa. (Ayubu 39:9-12) Maliki Mroma Yulio Kaisari alisema wakati mmoja kwamba fahali hao walikuwa na ukubwa unaokaribia wa ndovu. “Wana nguvu nyingi sana, na wanakimbia kasi sana,” akaandika. Hebu wazia jinsi ungehisi dhaifu na mdogo mno kama ungesimama karibu na kiumbe huyo!

      6. Kwa nini ni Yehova peke yake anayeitwa “Mweza-Yote”?

      6 Vivyo hivyo, mwanadamu ni duni na dhaifu sana anapolinganishwa na Mungu mwenye nguvu, Yehova. Yehova huona mataifa yenye nguvu kama mavumbi membamba katika mizani. (Isaya 40:15) Yehova ana nguvu zisizo na mipaka, yeye si kama viumbe, kwa kuwa yeye peke yake ndiye anayeitwa “Mweza-Yote.”a (Ufunuo 15:3) Yehova ni “hodari kwa nguvu zake.” (Isaya 40:26) Yeye ni chanzo cha kudumu cha nguvu maridhawa. Hategemei nishati kutoka kwa chanzo kingine chochote, kwa kuwa “nguvu ni mali ya Mungu.” (Zaburi 62:11, NW) Lakini Yehova hutumiaje nguvu zake?

      Jinsi Yehova Anavyotumia Nguvu Zake

      7. Roho takatifu ya Yehova ni nini, na maneno ya lugha ya awali yanayotumiwa katika Biblia yanadokeza nini?

      7 Roho takatifu humiminika kutoka kwa Yehova kwa wingi sana, ni nguvu yake inayotenda kazi. Kwa kweli, kwenye Mwanzo 1:2, (NW) Biblia hurejezea roho hiyo kuwa “nguvu ya Mungu ya utendaji.” Maneno ya awali ya Kiebrania na Kigiriki yanayotafsiriwa “roho” huenda nyakati nyingine, yakatafsiriwa “upepo,” “pumzi,” na “mkumbo wa hewa.” Watungaji wa kamusi wanasema kwamba maneno ya lugha ya awali yanadokeza nguvu isiyoonekana inayotenda kazi. Hatuwezi kuona roho ya Mungu kama tusivyoweza kuona upepo, lakini tunaweza kuona na kutambua matokeo yake.

      8. Biblia hufananisha roho ya Mungu na nini, na kwa nini ufananisho huo mbalimbali unafaa?

      8 Roho takatifu ya Mungu inaweza kutimiza mambo mengi sana. Yehova anaweza kuitumia kutimiza kusudi lolote alilo nalo. Ndiyo sababu Biblia hufananisha roho ya Mungu na viungo kama vile “kidole,” ‘mkono wenye nguvu,’ au ‘mkono ulionyoshwa.’ (Luka 11:20; Kumbukumbu la Torati 5:15; Zaburi 8:3) Kama vile tu mwanadamu anavyoweza kutumia mikono yake kufanya kazi mbalimbali zinazohitaji nguvu au uwezo mbalimbali, ndivyo Mungu anavyoweza kutumia roho yake kutimiza kusudi lolote lile—kama vile kuumba atomu ndogo sana au kugawanya Bahari Nyekundu au kuwawezesha Wakristo wa karne ya kwanza kuongea kwa lugha za kigeni.

      9. Nguvu za Yehova za kutawala ni nyingi kadiri gani?

      9 Yehova pia hudhihirisha nguvu zake kupitia mamlaka yake akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Je, waweza kuwazia ukiwa na mamilioni ya mamilioni ya viumbe wenye akili na uwezo, walio tayari kutekeleza amri yako? Yehova ana nguvu hizo za utawala. Ana wanadamu wanaomtumikia, ambao mara nyingi Maandiko huwafananisha na jeshi. (Zaburi 68:11; 110:3) Hata hivyo, mwanadamu ni kiumbe dhaifu sana anapolinganishwa na malaika. Kwani, wakati jeshi la Ashuri liliposhambulia watu wa Mungu, malaika mmoja tu aliua wanajeshi 185,000 wa Ashuri katika usiku mmoja! (2 Wafalme 19:35) Malaika wa Mungu wana “uwezo kwa nguvu.”—Zaburi 103:19, 20, ZSB.

      10. (a) Kwa nini Mweza-Yote anaitwa Yehova wa majeshi? (b) Ni kiumbe yupi aliye na uwezo zaidi ya viumbe wote wa Yehova?

      10 Kuna malaika wangapi? Nabii Danieli alipata ono la mbinguni ambapo aliona viumbe wa roho zaidi ya milioni 100 wakiwa mbele ya kiti cha enzi cha Yehova, lakini hakuna uthibitisho wa kwamba aliona malaika wote ambao Yehova alikuwa ameumba. (Danieli 7:10) Kwa hivyo, huenda kukawa na mamia ya mamilioni ya malaika. Ndiyo sababu Mungu anaitwa Yehova wa majeshi. Cheo hicho kinaonyesha wadhifa wake mkubwa akiwa Amiri wa kikosi kikubwa kilichopangwa cha malaika wenye nguvu. Amemweka Mwanaye mpendwa, “mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote,” kusimamia viumbe hao wote wa roho. (Wakolosai 1:15) Akiwa malaika-mkuu—mkuu wa malaika, maserafi, na makerubi wote—Yesu ndiye kiumbe mwenye uwezo zaidi ya viumbe wote wa Yehova.

      11, 12. (a) Neno la Mungu hukaziaje nguvu? (b) Yesu alisema nini kuhusu nguvu za Yehova?

      11 Yehova hudhihirisha nguvu zake kwa njia nyingine pia. Andiko la Waebrania 4:12 lasema: “Neno la Mungu liko hai na hukazia nguvu.” Je, umeona nguvu za ajabu za neno la Mungu, au za ujumbe uliopuliziwa na roho, ambao sasa umehifadhiwa katika Biblia? Unaweza kutuimarisha, kujenga imani yetu, na kutusaidia kufanya mabadiliko makubwa maishani mwetu. Mtume Paulo aliwaonya waamini wenzake wajiepushe na watu walioishi maisha mapotovu. Halafu akasema: “Hata hivyo baadhi yenu ndivyo mlivyokuwa.” (1 Wakorintho 6:9-11) Naam, “neno la Mungu” lilikuwa na nguvu maishani mwao na liliwasaidia kubadilika.

      12 Yehova ana nguvu nyingi sana naye huzitumia kwa matokeo hivi kwamba hakuna kitu kinachoweza kumzuia. Yesu alisema hivi: “Kwa Mungu mambo yote yawezekana.” (Mathayo 19:26) Yehova hutumia nguvu zake kutimiza makusudi yapi?

      Anatumia Nguvu Zake Kupatana na Makusudi Yake

      13, 14. (a) Kwa nini tunaweza kusema kwamba Yehova si chanzo cha nguvu kisicho na utu? (b) Yehova anatumia nguvu zake kwa njia zipi?

      13 Roho ya Yehova ni bora kuliko kani yoyote ile; na Yehova si kani tu isiyo na utu, chanzo tu cha nguvu. Yeye ni Mungu mwenye utu ambaye anadhibiti nguvu zake kikamili. Lakini ni nini kinachomchochea azitumie?

      14 Kama tutakavyoona, Mungu hutumia nguvu zake kuumba, kuharibu, kulinda, au kuhuisha—kwa ufupi, yeye huzitumia kufanya jambo lolote linalofaa makusudi yake makamilifu. (Isaya 46:10) Pindi fulani-fulani, Yehova hutumia nguvu zake kufunua sifa na sheria zake muhimu. Na zaidi ya yote, anatumia nguvu zake kutimiza mapenzi yake—kutetea enzi yake kuu na kutakasa jina lake takatifu kupitia Ufalme wa Kimesiya. Hakuna kitu chochote kinachoweza kuzuia kusudi hilo.

      15. Yehova hutumia nguvu zake kwa kusudi gani kuhusiana na watumishi wake, na hali iliyompata Eliya inathibitishaje jambo hilo?

      15 Yehova hutumia pia nguvu zake kutusaidia tukiwa mtu mmoja-mmoja. Hebu angalia andiko la 2 Mambo ya Nyakati 16:9 linavyosema: “Kwa maana macho ya BWANA hukimbia-kimbia duniani mwote, ili ajionyeshe mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.” Kisa cha Eliya kilichotajwa mwanzoni ni mfano unaofaa. Kwa nini Yehova alimwonyesha tukio hilo la kustaajabisha la nguvu Zake? Malkia mwovu Yezebeli alikuwa ameapa kumwua Eliya. Nabii huyo alitoroka ili asiuawe. Alihisi upweke, aliogopa, na alikuwa amevunjika moyo—kana kwamba kazi yake yote ilikuwa ya bure. Yehova alimfariji Eliya aliyekuwa taabani kwa kumkumbusha waziwazi kuhusu nguvu Zake. Upepo, tetemeko la nchi, na moto vilionyesha kwamba Mungu mwenye nguvu zaidi katika ulimwengu wote alikuwa pamoja na Eliya. Kwa nini amhofu Yezebeli huku Yehova akiwa upande wake?—1 Wafalme 19:1-12.b

      16. Kwa nini tunaweza kupata faraja kwa kutafakari juu ya nguvu nyingi za Yehova?

      16 Ijapokuwa huu si wakati wa Yehova wa kufanya miujiza, yeye hajabadilika tangu siku za Eliya. (1 Wakorintho 13:8) Yeye angali na hamu ileile ya kutumia nguvu zake kwa niaba ya wale wanaompenda. Ni kweli kwamba anaishi katika makao matukufu ya roho, lakini hayuko mbali nasi. Nguvu zake hazina mipaka, kwa hiyo umbali si kizuizi. Badala yake, “BWANA yu karibu na wote wamwitao.” (Zaburi 145:18) Pindi moja wakati nabii Danieli alipomwomba Yehova msaada, malaika alifika alipokuwa angali anasali! (Danieli 9:20-23) Hakuna kitu kinachoweza kumzuia Yehova kuwasaidia na kuwaimarisha wale anaowapenda.—Zaburi 118:6.

      Je, Nguvu za Mungu Hutuzuia Tusimkaribie?

      17. Nguvu za Yehova hututiaje woga, lakini huo si woga wa aina gani?

      17 Je, tunapaswa kumwogopa Mungu kwa sababu ya nguvu zake? Ni lazima tujibu ndiyo na la. Ndiyo, kwa sababu sifa hii hutupatia sababu nzuri ya kumwogopa Mungu, kuwa na kicho na staha ya hali ya juu ambayo tulizungumzia kwa ufupi katika sura iliyotangulia. Biblia inatuambia kwamba woga huo ni “mwanzo wa hekima.” (Zaburi 111:10) Hata hivyo, twajibu la kwa sababu nguvu za Mungu hazifanyi tuwe na woga usiofaa au tuhofu kumkaribia.

      18. (a) Kwa nini watu wengi hukosa kuwatumaini wenye mamlaka? (b) Twajuaje kwamba Yehova hawezi kufisidiwa na mamlaka yake?

      18 “Mamlaka hufisidi; na mamlaka kamili hufisidi kikamili.” Ndivyo alivyoandika mwanahistoria Mwingereza Bwana Acton mnamo mwaka wa 1887. Maneno yake yamerudiwa mara nyingi, na huenda ni kwa sababu watu wengi huyaona kuwa ya kweli kabisa. Mara nyingi, wanadamu wasiokamilika hutumia vibaya mamlaka waliyo nayo, jambo hilo limethibitishwa na historia tena na tena. (Mhubiri 4:1; 8:9) Ndiyo sababu watu wengi hukosa kuwatumaini na huwaepuka wenye mamlaka. Yehova ana mamlaka kamili. Je, mamlaka hayo yamemfisidi kwa njia yoyote? Bila shaka la! Kama tulivyoona, yeye ni mtakatifu, hawezi kamwe kufisidiwa. Yehova si kama wanaume na wanawake wasiokamilika wenye mamlaka katika ulimwengu huu wenye ufisadi. Hajawahi kutumia vibaya mamlaka yake na hatafanya hivyo kamwe.

      19, 20. (a) Sikuzote Yehova hutumia nguvu zake kwa kupatana na sifa gani nyingine, na kwa nini hilo linafariji? (b) Simulia mfano ambao unaonyesha jinsi Yehova anavyojidhibiti, na kwa nini hilo linakuvutia?

      19 Kumbuka kwamba Yehova ana sifa nyingine mbali na nguvu. Baadaye tutajifunza kuhusu haki yake, hekima yake, na upendo wake. Lakini hatupaswi kudhani kwamba Yehova hudhihirisha sifa zake bila hisia wala ufikirio, kana kwamba anadhihirisha sifa moja tu kwa wakati mmoja. Kinyume chake, tutaona katika sura zijazo kwamba sikuzote Yehova hutumia nguvu zake kwa kupatana na haki yake, hekima yake, na upendo wake. Fikiria sifa nyingine ya Mungu, sifa ambayo watawala wengi leo ulimwenguni hawana—kujidhibiti.

      20 Wazia kama ungekutana na mtu mkubwa mno mwenye nguvu nyingi, anayetisha. Lakini baada ya muda, unagundua kwamba yeye ni mpole. Yuko tayari kila wakati kutumia nguvu zake kuwasaidia na kuwalinda watu, hasa wale walio dhaifu na wanyonge. Hatumii vibaya kamwe nguvu zake. Waona akichongewa bila sababu, lakini yeye ni thabiti na mtulivu, ana staha na hata ni mwenye fadhili. Washangaa iwapo ungebaki mpole na kujidhibiti endapo ungekuwa na nguvu kama mwanamume huyo! Kadiri unavyomjua mwanamume huyo, je, hungetaka kuwa karibu naye? Tuna sababu nzuri sana za kumkaribia Yehova aliye mweza-yote. Hebu angalia mstari ambao ni msingi wa kichwa kikuu cha sura hii: “Mwenyezi-Mungu hakasiriki upesi, lakini amejaa nguvu.” (Nahumu 1:3, BHN) Yehova hatumii nguvu zake haraka-haraka kuwaadhibu watu, hata watu waovu. Yeye ni mpole na mwenye fadhili. Amethibitika kuwa ‘asiyekasirika upesi’ ajapochukizwa mara nyingi.—Zaburi 78:37-41.

      21. Kwa nini Yehova hawalazimishi watu kufanya mapenzi yake, na hilo latufundisha nini kumhusu?

      21 Fikiria kujidhibiti kwa Yehova kwa njia nyingine. Kama ungekuwa na nguvu zisizo na mipaka, je, wafikiri kwamba nyakati nyingine, ungekuwa na mwelekeo wa kuwalazimisha watu wafanye mambo jinsi unavyotaka? Licha ya nguvu nyingi alizo nazo, Yehova hawalazimishi kamwe watu wamtumikie. Hata ingawa kumtumikia Mungu ndiyo njia pekee ya kupata uhai udumuo milele, Yehova hatulazimishi kumtumikia. Badala yake, kwa fadhili yeye humstahi kila mtu kwa kumpa uhuru wa kuchagua. Anaonya kuhusu matokeo ya kufanya uchaguzi usiofaa na kutuambia faida za kufanya uchaguzi mzuri. Lakini anaturuhusu kufanya uchaguzi wetu binafsi. (Kumbukumbu la Torati 30:19, 20) Yehova hataki kamwe watu wamtumikie kwa kulazimishwa au kwa sababu wanahofu isivyofaa nguvu zake za kutisha. Anatafuta watu watakaomtumikia kwa hiari, kwa sababu wanampenda.—2 Wakorintho 9:7.

      22, 23. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova hufurahia kuwapa wengine mamlaka? (b) Tutazungumzia nini katika sura inayofuata?

      22 Na tuchunguze sababu ya mwisho inayotufanya tusiwe na woga usiofaa kumwelekea Mungu Mweza-Yote. Wanadamu wenye uwezo huogopa kuwapa wengine mamlaka. Lakini Yehova hufurahia kuwapa waabudu wake waaminifu mamlaka. Yeye huwapa wengine mamlaka kubwa, kama vile Mwanaye. (Mathayo 28:18) Yehova pia huwapa watumishi wake uwezo kwa njia nyingine. Biblia yaeleza: “Ee BWANA, ukuu ni wako, na uweza, na utukufu, na kushinda, na enzi; maana vitu vyote vilivyo mbinguni na duniani ni vyako. . . . Mkononi mwako mna uweza na nguvu; tena mkononi mwako mna kuwatukuza na kuwawezesha wote.”—1 Mambo ya Nyakati 29:11, 12.

      23 Ndiyo, Yehova atafurahi kukuimarisha. Yeye hata huwapa “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” wale wanaotaka kumtumikia. (2 Wakorintho 4:7) Je, huvutiwi kumkaribia Mungu huyo mwenye nguvu sana, ambaye anatumia nguvu zake kwa fadhili na kupatana na kanuni za juu za maadili? Katika sura inayofuata, tutazungumzia jinsi Yehova anavyotumia nguvu zake za kuumba.

      a Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “Mweza-Yote” humaanisha kihalisi “Mtawala Juu ya Wote; Yule Aliye na Nguvu Zote.”

      b Biblia inasema kwamba “BWANA hakuwamo katika upepo ule . . . , tetemeko la nchi . . . , moto ule.” Tofauti na wale wanaoabudu miungu ya kihekaya ya nguvu za asili, watumishi wa Yehova hawamtafuti katika nguvu za maumbile. Yeye ni mkuu sana hivi kwamba hawezi kuishi katika kitu chochote alichoumba.—1 Wafalme 8:27.

      Maswali ya Kutafakari

      • 2 Mambo ya Nyakati 16:7-13 Kielelezo cha Mfalme Asa kinaonyesha jinsi gani hatari ya kutotumaini nguvu za Yehova?

      • Zaburi 89:6-18 Nguvu za Yehova zina matokeo gani kwa waabudu wake?

      • Isaya 40:10-31 Nguvu za Yehova zinaelezwaje katika andiko hilo, nazo ni nyingi kadiri gani, na zinaweza kumfaidi kila mmoja wetu jinsi gani?

      • Ufunuo 11:16-18 Yehova anaahidi atatumia jinsi gani nguvu zake wakati ujao, na kwa nini jambo hilo linawafariji Wakristo wa kweli?

  • Nguvu za Kuumba—“Aliyezifanya Mbingu na Nchi”
    Mkaribie Yehova
    • Jua lenye nguvu

      Sura ya 5

      Nguvu za Kuumba—“Aliyezifanya Mbingu na Nchi”

      1, 2. Jua linaonyeshaje nguvu za Yehova za kuumba?

      JE, UMEWAHI kusimama karibu na moto usiku wenye baridi? Labda ulinyoosha mikono yako umbali ufaao kutoka kwenye miali ya moto ili ufurahie joto lake. Uliposonga karibu zaidi, ulishindwa kustahimili joto hilo kali. Uliporudi nyuma zaidi, hewa baridi ya usiku ilikulemea, nawe ukaanza kutetemeka.

      2 Kuna “moto” unaopasha joto miili yetu wakati wa mchana. “Moto” huo uko umbali wa kilometa milioni 150!a Ni wazi kwamba jua lina nguvu nyingi kiasi cha kwamba unaweza kuhisi joto lake kutoka umbali huo! Lakini, dunia inazunguka tanuru hiyo kubwa yenye joto kali la nyuklia kwa umbali barabara. Ikiwa dunia ingekaribia jua, maji yote duniani yangekuwa mvuke; na ikiwa dunia ingesonga mbali zaidi, maji yote yangekuwa barafu. Joto au baridi kali ingeangamiza kila kiumbe duniani. Nuru ya jua ni muhimu sana kwa uhai duniani, ni safi na ina manufaa tele, na inapendeza.—Mhubiri 11:7.

      Yehova ‘aliufanya mwanga na jua’

      3. Jua huthibitisha ukweli upi muhimu?

      3 Hata hivyo, watu wengi wanaona jua kuwa kitu cha kawaida tu, ingawa uhai wao unalitegemea. Hivyo basi, hawajifunzi somo lolote kutokana na jua. Biblia inasema hivi kumhusu Yehova: “Ndiwe uliyeufanya mwanga na jua.” (Zaburi 74:16) Naam, jua humletea sifa Yehova, “Aliyezifanya mbingu na nchi.” (Zaburi 19:1; 146:6) Jua ni mojawapo ya sayari chungu nzima zilizo angani ambazo zinatufundisha kuhusu nguvu nyingi za Yehova za kuumba. Hebu tuchunguze baadhi ya sayari hizo kwa undani zaidi halafu tuchunguze dunia na viumbe mbalimbali waliomo.

      “Inueni Macho Yenu Juu, Mkaone”

      4, 5. Jua lina nguvu nyingi kadiri gani, na ni kubwa kadiri gani, lakini likoje linapolinganishwa na nyota nyinginezo?

      4 Huenda unajua kwamba jua letu ni nyota. Jua huonekana kubwa kuliko nyota tunazoona usiku kwa sababu liko karibu sana kuliko nyota hizo. Lina nguvu nyingi kadiri gani? Kipimo cha joto kwenye kiini cha jua ni nyuzi Selsiasi 15,000,000 hivi. Kama ungeweza kuchukua kipande cha kiini cha jua kinachotoshana na kichwa cha pini ndogo na kukiweka duniani, ungeteketea hata ukiwa umbali wa kilometa 140 kutoka kwenye chanzo hicho kidogo sana cha joto! Kila sekunde, jua hutoa nishati inayolingana na mlipuko wa mamia ya mamilioni ya mabomu ya nyuklia.

      5 Jua ni kubwa sana hivi kwamba zaidi ya dunia 1,300,000 zinaweza kutoshea ndani yake. Je, jua ni nyota kubwa kupindukia? La, wataalamu wa nyota husema kwamba jua ni nyota ndogo sana yenye mwangaza hafifu. Mtume Paulo aliandika kwamba “nyota hutofautiana na nyota kwa utukufu.” (1 Wakorintho 15:41) Paulo hakuweza kuelewa kabisa maneno hayo ya Mungu. Kuna nyota moja kubwa hivi kwamba ikiwa ingewekwa mahali lilipo jua, basi ingefika ilipo dunia yetu. Endapo nyota nyingine ambayo ni kubwa sana ingewekwa lilipo jua, ingefikia sayari ya Zohali—japo sayari hiyo iko mbali sana na dunia hivi kwamba roketi ya angani ilisafiri kwa muda wa miaka minne ili kufika huko. Mwendo wake ulizidi mara 40 mwendo wa risasi inayofyatuliwa na bunduki yenye nguvu!

      6. Biblia inaonyeshaje kwamba idadi ya nyota ni kubwa sana wanadamu wasiweze kuhesabu?

      6 Lakini idadi ya nyota inastaajabisha zaidi ya ukubwa wake. Kwa kweli, Biblia inasema kwamba nyota haziwezi kuhesabiwa, kama vile “mchanga wa bahari” usivyoweza kuhesabiwa. (Yeremia 33:22) Maneno hayo yanadokeza kwamba kuna nyota nyingi sana ambazo hatuwezi kuona pasipo vifaa maalumu. Endapo mwandikaji wa Biblia, kama Yeremia, angetazama angani wakati wa usiku na kujaribu kuhesabu nyota zionekanazo, angefaulu kuhesabu nyota zipatazo 3,000 hivi. Wanadamu huweza kuona idadi hiyo tu ya nyota katika anga jangavu la usiku bila kutumia vifaa maalumu. Idadi hiyo yaweza kulinganishwa na idadi ya chembe za mchanga zinazoweza kujaza kiganja kimoja tu cha mkono. Hata hivyo, idadi halisi ya nyota haijulikani, ni nyingi kama mchanga wa bahari. Ni nani awezaye kuhesabu idadi kubwa hivyo?b

      Nyota nyingi sana za mbinguni na makundi ya nyota

      “Aziita zote kwa majina”

      7. (a) Kundi letu la Kilimia lina nyota ngapi, na hiyo ni idadi kubwa kadiri gani? (b) Kushindwa kwa wataalamu wa nyota kuhesabu makundi ya nyota kwaonyesha nini, na hilo latufundisha nini kuhusu nguvu za Yehova za kuumba?

      7 Andiko la Isaya 40:26 linajibu hivi: “Inueni macho yenu juu, mkaone; ni nani aliyeziumba hizi; aletaye nje jeshi lao kwa hesabu; aziita zote kwa majina.” Zaburi 147:4 yasema: “Huihesabu idadi ya nyota.” “Idadi ya nyota” ni ngapi? Hilo si swali rahisi. Wataalamu wa nyota wanakadiria kwamba kuna zaidi ya nyota bilioni 100 katika kundi letu la nyota la Kilimia peke yake. Lakini kuna makundi mengine mengi mbali na kundi letu, ambayo yana nyota nyingi zaidi. Kuna makundi mangapi? Baadhi ya wataalamu wa nyota wamekadiria kwamba kuna makundi bilioni 50. Wengine wamekadiria kwamba kuna makundi yapatayo bilioni 125. Kwa hiyo, mwanadamu hawezi hata kujua idadi ya makundi ya nyota, sembuse kujua idadi kamili ya mabilioni ya nyota zilizomo. Lakini, Yehova anajua idadi yake. Isitoshe, yeye huipa kila nyota jina lake!

      8. (a) Kundi la Kilimia ni kubwa kadiri gani? (b) Yehova anapangaje mizunguko ya sayari na nyota mbinguni?

      8 Tunakuwa na kicho zaidi kwa Mungu tunapotafakari juu ya ukubwa wa kundi moja la nyota. Kundi la Kilimia limekadiriwa kuwa na upana wa kipimo cha miaka 100,000 cha mwendo wa mwanga. Hebu wazia mwali wa mwanga unaosafiri kwa mwendo wa kasi sana wa kilometa 300,000 kwa sekunde. Ingechukua mwali huo miaka 100,000 kuvuka kundi letu la nyota!c Na makundi fulani ni makubwa zaidi ya Kilimia. Biblia inasema kwamba Yehova ‘amezitandika mbingu’ hizi pana kana kwamba ni pazia tu. (Zaburi 104:2) Pia anapanga mizunguko ya sayari na nyota alizoumba. Kila kitu kinazunguka kupatana na sheria za asili ambazo Mungu ametunga na kutekeleza, kuanzia chembe ndogo sana ya vumbi lililo angani hadi kundi kubwa zaidi la nyota. (Ayubu 38:31-33) Ndiyo sababu, wanasayansi wamelinganisha mizunguko barabara ya sayari na nyota na miendo hususa ya wachezaji-dansi wenye utaratibu wa hali ya juu! Basi fikiria Muumba wa vitu hivyo vyote. Je, hustaajabishwi na Mungu huyo mwenye nguvu nyingi hivyo za kuumba?

      “Ameiumba Dunia kwa Uweza Wake”

      9, 10. Nguvu za Yehova zinadhihirishwaje na mahali ambapo mfumo wetu wa jua, Jupita, dunia, na mwezi ulipo?

      9 Nguvu za Yehova za kuumba zinadhihirishwa katika makao yetu, dunia. Ameiweka dunia mahali pafaapo katika ulimwengu huu mkubwa. Wanasayansi fulani wanaamini kwamba mazingira ya makundi mengi ya nyota huenda yasifae sayari yenye uhai kama sayari yetu. Ni dhahiri kwamba sehemu kubwa ya kundi letu la nyota la Kilimia haikubuniwa ili iwe makao ya viumbe. Sehemu ya katikati ya kundi hilo imejaa nyota. Mnururisho ni mkali mno, na mara nyingi nyota huponea chupuchupu kugongana. Kingo za kundi hilo la nyota hazina vitu vingi ambavyo ni muhimu kwa uhai. Mfumo wetu wa jua uko mahali pafaapo kabisa.

      10 Dunia hulindwa na sayari moja kubwa iliyo mbali sana—sayari ya Jupita. Sayari hiyo ya Jupita yenye ukubwa ambao ni mara 1,000 zaidi ya ukubwa wa Dunia, ina nguvu nyingi za uvutano. Matokeo ni nini? Inafyonza au kugeuza mwelekeo wa vitu vinavyosonga kasi angani. Wanasayansi wanasema kwamba kama Jupita haingekuwapo, vitu vikubwa vinavyosonga kasi angani vingegonga dunia na kuiathiri mara 10,000 zaidi ya ilivyo sasa. Dunia yetu hunufaishwa pia na sayari nyingine ya pekee iliyo karibu zaidi—mwezi. Licha ya kuwa sayari maridadi sana na “taa ya usiku,” mwezi hudumisha mwinamo uleule wa dunia. Mwinamo huo huwezesha dunia kuwa na majira thabiti na yasiyobadilika—jambo jingine muhimu kwa uhai duniani.

      11. Angahewa ya dunia imebuniwaje ili kulinda dunia?

      11 Nguvu za Yehova za kuumba zinadhihirishwa na kila kitu duniani. Fikiria angahewa ambayo inalinda dunia. Jua hutoa miale inayonufaisha mwili na miale hatari. Miale hatari inapofika kwenye angahewa ya juu ya dunia, inabadili oksijeni katika hewa kuwa hewa ya ozoni. Tabaka la hewa ya ozoni linalofanyizwa, linafyonza sehemu kubwa ya miale hiyo. Kwa kweli, sayari yetu imebuniwa ikiwa na kifuniko kinachoilinda!

      12. Mzunguko wa maji wa angahewa unathibitishaje nguvu za Yehova za kuumba?

      12 Angahewa yetu, ambayo ni mchanganyiko tata wa gesi zifaazo zinazotegemeza viumbe wanaoishi karibu au juu ya uso wa dunia inahusisha mambo mengine mengi. Mzunguko wa maji ni mojawapo ya maajabu ya angahewa. Kila mwaka jua huvukiza zaidi ya kilometa 400,000 za kipimo cha ujazo wa maji kutoka kwa bahari zote duniani. Maji hayo hufanyiza mawingu, ambayo husambazwa kotekote na pepo za angahewa. Maji hayo ambayo yamechujwa na kusafishwa, hunyesha yakiwa mvua, theluji, na barafu, na hivyo kuongeza hifadhi za maji duniani. Ni kama vile Mhubiri 1:7 inavyosema: “Mito yote huingia baharini, walakini bahari haijai; huko iendako mito, ndiko irudiko tena.” Yehova tu ndiye aliye na uwezo wa kuanzisha mzunguko huo.

      13. Mimea na udongo wa dunia vinadhihirishaje nguvu za Muumba?

      13 Kila kitu kilicho hai kinatudhihirishia nguvu za Muumba. Miti mikubwa mno aina ya sequoia ambayo ni mirefu kushinda jengo lenye orofa 30, na mimea mingi midogo mno ya baharini inayotokeza kiasi kikubwa cha hewa tunayopumua, inadhihirisha nguvu za Yehova za kuumba. Hata udongo una mimea na wanyama wengi walio hai—minyoo, kuvu, na vijiumbe vidogo sana, ambavyo hushirikiana kwa njia za pekee sana ili kuchangia ukuzi wa mimea. Ndiyo sababu Biblia inasema kwamba udongo una nguvu.—Mwanzo 4:12, ZSB.

      14. Atomu ndogo sana ina nguvu zipi zilizofichika?

      14 Hapana shaka kwamba Yehova ndiye ‘Aliyeiumba dunia kwa uweza wake.’ (Yeremia 10:12) Nguvu za Yehova zinadhihirishwa pia na vitu vidogo sana alivyoumba. Kwa mfano, atomu milioni moja zikipangwa karibu-karibu haziwezi kufikia unene wa unywele wa mwanadamu. Na hata kama atomu ingerefushwa kufikia kimo cha jengo lenye orofa 14, kiini chake kingelingana na chembe moja tu ya chumvi iliyo kwenye orofa ya 7 ya jengo hilo. Lakini kiini hicho kidogo sana ndicho chanzo cha nguvu za kutisha za mlipuko wa kombora la nyuklia!

      “Kila Mwenye Pumzi”

      15. Yehova alimfunza Ayubu somo gani alipozungumzia wanyama mbalimbali wa mwitu?

      15 Wanyama chungu nzima walio duniani wanathibitisha pia waziwazi nguvu za Yehova za kuumba. Zaburi 148 inaorodhesha baadhi ya viumbe wanaomsifu Yehova, na mstari wa 10 unataja “hayawani, na wanyama wafugwao.” Ili kuonyesha kwa nini mwanadamu anapaswa kuwa na kicho kumwelekea Muumba, pindi moja Yehova alizungumza na Ayubu kuhusu wanyama kama vile simba, punda-milia, nyati, kiboko, na mamba. Yehova alitaka kufunza somo gani? Ikiwa mwanadamu hupigwa na butwaa kwa sababu ya viumbe hao wakubwa, wenye kutisha, na wasioweza kufugwa, je, hapaswi kumhofu hata zaidi Muumba wa viumbe hao?—Ayubu, sura ya 38-41.

      16. Ni nini kinachokuvutia kuhusu baadhi ya ndege ambao Yehova ameumba?

      16 Andiko la Zaburi 148:10 linataja pia “ndege wenye mbawa.” Hebu fikiria jamii nyingi zilizopo! Yehova alimwambia Ayubu kuhusu mbuni ambaye “humdharau farasi na mwenye kumpanda.” Ijapokuwa ndege huyu mwenye kimo cha meta 2.5 hawezi kuruka, anaweza kukimbia kwa mwendo wa kilometa 65 kwa saa, na anafikia umbali wa meta 4.5 anapopiga hatua moja tu! (Ayubu 39:13, 18) Kwa upande mwingine, ndege aitwaye alibatrosi huruka juu ya bahari muda mwingi wa maisha yake. Kwa kawaida ndege huyo hunyiririka tu hewani, na kipimo cha mabawa yake ni meta 3 kutoka ncha hadi ncha. Anaweza kupaa angani kwa saa nyingi sana bila kupigapiga mabawa yake. Kwa upande mwingine, ndege aina ya bee hummingbird mwenye urefu wa sentimeta 5 tu ndiye ndege mdogo zaidi ulimwenguni. Anaweza kupigapiga mabawa yake mara 80 kwa sekunde! Ndege hao wanaomeremeta kama vito vidogo vyenye mabawa, wanaweza kuelea hewani kama helikopta na hata kupaa kinyumenyume.

      17. Nyangumi wa rangi ya buluu-kijivu ni mkubwa kadiri gani, na tunapaswa kufikia mkataa gani baada ya kuchunguza wanyama walioumbwa na Yehova?

      17 Andiko la Zaburi 148:7 linasema kwamba hata “nyangumi” wanamsifu Yehova. Mfikirie kiumbe anayedhaniwa na wengi kuwa kiumbe mkubwa zaidi aliyewahi kuishi duniani, nyangumi mwenye rangi ya buluu-kijivu. Mnyama huyo mkubwa sana anayeishi baharini anaweza kuwa na urefu wa meta 30 au zaidi. Anaweza kuwa na uzito wa ndovu 30 wakomavu. Ulimi wake peke yake una uzito wa ndovu mmoja. Moyo wake unalingana na gari ndogo. Moyo huo mkubwa hupigapiga mara 9 tu kwa dakika—tofauti na moyo wa ndege aina ya hummingbird, ambao unaweza kupigapiga mara 1,200 hivi kwa dakika. Angalau mshipa mmoja wa nyangumi huyo ni mkubwa sana hivi kwamba mtoto mdogo anaweza kutambaa ndani yake. Bila shaka mioyo yetu hutuchochea kutangaza himizo la mstari wa mwisho wa kitabu cha Zaburi: “Kila mwenye pumzi na amsifu BWANA.”—Zaburi 150:6.

      Kujifunza Kutokana na Nguvu za Yehova za Kuumba

      18, 19. Vitu ambavyo Yehova ameumba duniani ni vingi kadiri gani, na uumbaji hutufundisha nini kuhusu enzi yake kuu?

      18 Twajifunza nini kutokana na jinsi Yehova anavyotumia nguvu zake za kuumba? Tunatiwa kicho tunapotambua kwamba vitu vilivyoumbwa ni vingi sana. Mtunga-zaburi mmoja alisema hivi kwa mshangao: “Ee BWANA, jinsi yalivyo mengi matendo yako! . . . Dunia imejaa mali zako.” (Zaburi 104:24) Ni kweli kama nini! Wanabiolojia wamegundua jamii zaidi ya milioni moja za vitu hai duniani; lakini hawajui kama kuna jamii milioni 10, milioni 30, au zaidi. Wakati mwingine msanii anaweza kushindwa kubuni jambo jipya. Lakini ubuni wa Yehova—uwezo wake wa kubuni na kuumba vitu mbalimbali vipya—bila shaka hauna kikomo.

      19 Tunajifunza kuhusu enzi kuu ya Yehova kutokana na jinsi anavyotumia nguvu zake za kuumba. Neno “Muumba” linamtofautisha Yehova na vitu vyote ulimwenguni, kwani vitu vyote “viliumbwa.” Hata Mwana mzaliwa-pekee wa Yehova, ambaye alikuwa “stadi wa kazi” wakati wa uumbaji, haitwi kamwe Muumba au Muumba-msaidizi katika Biblia. (Mithali 8:30; Mathayo 19:4) Badala yake, yeye ni “mzaliwa wa kwanza wa uumbaji wote.” (Wakolosai 1:15) Cheo cha Yehova akiwa Muumba humpa haki kamili ya kuwa mwenye enzi kuu pekee wa ulimwengu wote.—Waroma 1:20; Ufunuo 4:11.

      20. Yehova amepumzikaje tangu alipomaliza kuumba vitu duniani?

      20 Je, Yehova ameacha kutumia nguvu zake za kuumba? Ni kweli kwamba Biblia inasema kuwa Yehova alipomaliza kazi yake ya kuumba siku ya sita ya uumbaji, ‘siku ya saba Mungu alipumzika baada ya kazi yake yote aliyoifanya.’ (Mwanzo 2:2, BHN) Mtume Paulo alionyesha kwamba hiyo “siku” ya saba ina urefu wa maelfu ya miaka, kwa kuwa ilikuwa ikiendelea katika siku zake. (Waebrania 4:3-6) Lakini je, neno ‘alipumzika’ lamaanisha kwamba Yehova ameacha kufanya kazi kabisa? La, Yehova hufanya kazi daima. (Zaburi 92:4; Yohana 5:17) Basi, bila shaka pumziko lake linarejezea tu kuacha kwake kufanya kazi ya kuumba vitu duniani. Hata hivyo, kazi yake ya kutimiza makusudi yake imeendelea bila kukatishwa. Kazi hiyo imetia ndani kupulizia Maandiko Matakatifu. Kazi yake imetia ndani pia kutokeza “kiumbe kipya.” Habari hiyo itazungumziwa katika Sura ya 19.—2 Wakorintho 5:17.

      21. Nguvu za Yehova za kuumba zitakuwa na matokeo gani kwa wanadamu waaminifu kwa umilele wote?

      21 Siku ya Yehova ya pumziko itakapofikia mwisho hatimaye, ndipo atakapoweza kutangaza kazi yake yote duniani kuwa ‘njema sana,’ kama alivyofanya mwishoni mwa siku sita za uumbaji. (Mwanzo 1:31) Bado tunangoja kuona jinsi atakavyoamua kutumia nguvu zake za kuumba zisizo na mipaka baadaye. Kwa vyovyote vile, tunaweza kuwa na hakika kwamba tutaendelea kustaajabishwa na jinsi Yehova anavyotumia nguvu zake za kuumba. Kwa umilele wote, tutajifunza mengi zaidi kumhusu Yehova kupitia uumbaji wake. (Mhubiri 3:11) Kadiri tunavyojifunza mengi kumhusu, ndivyo tutakavyokuwa na kicho zaidi—na ndivyo tutakavyomkaribia zaidi Muumba wetu Mtukufu.

      a Ili kufahamu vyema umbali huo mkubwa, fikiria hili: Ukisafiri umbali huo kwa gari—linaloenda kwa mwendo wa kilometa 160 kwa saa, saa 24 kwa siku—ungehitaji kusafiri kwa muda wa zaidi ya miaka 100!

      b Watu fulani hufikiri kwamba watu walioishi katika nyakati za Biblia walitumia darubini fulani ya kienyeji. Wanatoa sababu kwamba watu walioishi nyakati hizo hawangeweza kujua kwamba idadi ya nyota ni kubwa sana wanadamu wasiweze kuhesabu. Makisio hayo yasiyo na msingi hayamheshimu wala kumtambua Yehova, Mtungaji wa Biblia.—2 Timotheo 3:16.

      c Fikiria muda ambao ungehitaji kutumia kuhesabu nyota bilioni 100 tu. Kama ungeweza kuhesabu nyota moja kila sekunde—kwa muda wa saa 24 kwa siku—ingekuchukua miaka 3,171!

      Maswali ya Kutafakari

      • Zaburi 8:3-9 Uumbaji wa Yehova unatufundishaje kuwa wanyenyekevu?

      • Zaburi 19:1-6 Nguvu za Yehova za kuumba zinaweza kutuchochea kufanya nini, na kwa nini?

      • Mathayo 6:25-34 Kutafakari nguvu za Yehova za kuumba kunaweza kutusaidiaje kushinda mahangaiko na kutanguliza mambo yanayofaa maishani?

      • Matendo 17:22-31 Jinsi Yehova alivyotumia nguvu zake za kuumba kunatufundishaje kwamba ibada ya sanamu ni kosa na hayuko mbali nasi?

  • Nguvu za Kuangamiza—Yehova, “Ni Mtu wa Vita”
    Mkaribie Yehova
    • Yehova Mungu anamwangamiza Farao mwenye kiburi na jeshi la Wamisri katika Bahari Nyekundu

      Sura ya 6

      Nguvu za Kuangamiza—Yehova, “Ni Mtu wa Vita”

      1-3. (a) Waisraeli walikabili tisho gani kutoka kwa Wamisri? (b) Yehova aliwapigania watu wake jinsi gani?

      WAISRAELI walinaswa kati ya majabali makubwa yaliyochongoka ya mlima na bahari isiyopitika. Jeshi la Misri, ambalo liliua watu kikatili, lilikuwa likiwafukuza Waisraeli hima-hima. Lilikuwa limeazimia kuwaangamiza kabisa.a Hata hivyo, Musa aliwasihi watu wa Mungu wasikate tamaa. “BWANA atawapigania ninyi,” akawahakikishia.—Kutoka 14:14.

      2 Hata hivyo, Musa alimlilia Yehova, Naye akamjibu hivi: “Mbona unanililia mimi? . . . Inua fimbo yako, ukanyoshe mkono wako juu ya bahari, na kuigawanya.” (Kutoka 14:15, 16) Hebu wazia mambo yanayotukia. Yehova anamwamuru malaika wake mara moja, na ile nguzo ya wingu inarudi nyuma ya Waisraeli, yaelekea inakuwa kama ukuta na kuwazuia Wamisri kushambulia. (Kutoka 14:19, 20; Zaburi 105:39) Musa aunyosha mkono wake. Bahari yapigwa na upepo wenye nguvu na maji yagawanyika. Kwa njia fulani maji yagandamana na kusimama wima kama kuta, na kutokeza njia pana inayotoshea taifa zima!—Kutoka 14:21; 15:8.

      3 Farao anapaswa kuwaamuru wanajeshi wake warudi nyumbani baada ya kuona wonyesho huo wa kustaajabisha wa nguvu. Badala yake, Farao mwenye kiburi anawaamuru washambulie. (Kutoka 14:23) Wamisri watimua mbio na kuwafuata Waisraeli hima-hima katika bonde la bahari, lakini punde si punde mashambulizi yao yanaambulia patupu wakati magurudumu ya magari yao yanapoanza kutoka. Mara tu Waisraeli wafikapo ng’ambo ya bahari wakiwa salama, Yehova anamwamuru hivi Musa: “Nyosha mkono wako juu ya bahari, ili maji yarudi tena juu ya Wamisri, juu ya magari yao, na juu ya farasi zao.” Kuta za maji zaporomoka, na kumfunika Farao na majeshi yake!—Kutoka 14:24-28; Zaburi 136:15.

      Kwenye Bahari Nyekundu Yehova alijithibitisha kuwa “mtu wa vita”

      4. (a) Yehova alijithibitisha kuwa nani kwenye Bahari Nyekundu? (b) Huenda tendo hilo la Yehova likaathirije watu fulani?

      4 Ukombozi wa taifa la Israeli katika Bahari Nyekundu ulikuwa tukio muhimu sana katika simulizi la matendo ya Mungu kuelekea wanadamu. Pindi hiyo, Yehova alijithibitisha kuwa “mtu wa vita.” (Kutoka 15:3) Lakini wewe unaonaje tendo hilo la Yehova? Kwa kweli, vita vimewaletea wanadamu majonzi na taabu nyingi sana. Je, yaweza kuwa kwamba unashindwa kumkaribia Mungu kwa sababu anatumia nguvu zake za kuangamiza?

      Vita vya Mungu na Mapambano ya Wanadamu

      5, 6. (a) Kwa nini Mungu anaitwa ifaavyo “BWANA wa majeshi”? (b) Vita vya Mungu vinatofautiana na vita vya wanadamu jinsi gani?

      5 Mungu anaitwa kwa jina la cheo “BWANA wa majeshi” mara 300 hivi katika Maandiko ya Kiebrania, na mara 2 katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. (1 Samweli 1:11) Akiwa Mtawala Mwenye Enzi Kuu, Yehova anasimamia jeshi kubwa sana la malaika. (Yoshua 5:13-15; 1 Wafalme 22:19) Jeshi hilo lina uwezo mkubwa ajabu wa kuangamiza. (Isaya 37:36) Kuwaangamiza wanadamu si jambo lenye kufurahisha. Hata hivyo, ni sharti tukumbuke kwamba vita vya Mungu si kama mapambano ya wanadamu yasiyo na maana. Huenda viongozi wa kijeshi na wa kisiasa wakadai kwamba wanapigana kwa makusudi mazuri. Lakini vita vyote vya wanadamu huchochewa na pupa na ubinafsi.

      6 Kinyume chake, Yehova hatendi bila kufikiri. Andiko la Kumbukumbu la Torati 32:4 latangaza hivi: “Yeye Mwamba, kazi yake ni kamilifu; maana, njia zake zote ni haki. Mungu wa uaminifu, asiye na uovu, Yeye ndiye mwenye haki na adili.” Neno la Mungu linashutumu hasira isiyodhibitiwa, ukatili, na jeuri. (Mwanzo 49:7; Zaburi 11:5) Kwa hiyo, Yehova hatendi kamwe bila sababu. Yeye hutumia nguvu zake za kuangamiza mara chache sana wakati jitihada nyingine zote zinaposhindwa. Ni kama alivyosema kupitia nabii wake Ezekieli: “Je, mimi ninafurahia kufa kwake mtu mwovu? asema Bwana MUNGU, si afadhali kwamba aghairi, na kuiacha njia yake akaishi?”—Ezekieli 18:23.

      7, 8. (a) Ayubu alifikiri nini kimakosa kuhusu mateso yake? (b) Elihu alisahihishaje maoni ya Ayubu kuhusu jambo hilo? (c) Tunajifunza somo gani kutokana na mambo yaliyompata Ayubu?

      7 Basi kwa nini Yehova hutumia nguvu zake za kuangamiza? Kabla ya kujibu swali hilo, tumfikirie Ayubu yule mwanamume mwadilifu. Shetani alitilia shaka iwapo Ayubu, au mwanadamu yeyote angebaki mwaminifu chini ya jaribu. Yehova alijibu shtaka hilo kwa kumruhusu Shetani ajaribu uaminifu wa Ayubu. Tokeo ni kwamba Ayubu alitaabishwa na ugonjwa, akapoteza mali yake na watoto wake. (Ayubu 1:1–2:8) Bila kujua masuala yaliyohusika, Ayubu alifikiri kimakosa kwamba Mungu alikuwa akimwadhibu isivyo haki kupitia mateso hayo. Alimwuliza Mungu kwa nini Alimweka awe “shabaha” yake, na “adui” yake?—Ayubu 7:20; 13:24.

      8 Mwanamume kijana aliyeitwa Elihu alionyesha kasoro ya maoni ya Ayubu, alipomwambia hivi: “Wasema, Haki yangu ni zaidi kuliko ya Mungu.” (Ayubu 35:2) Naam, si jambo la hekima kufikiri kwamba tunajua mengi kumliko Mungu au kudhani kwamba ametenda isivyo haki. “Mungu asidhaniwe kutenda udhalimu, wala Mwenyezi kufanya uovu,” akasema Elihu. Baadaye, alisema hivi: “Yeye Mwenyezi hamwezi kumwona; Yeye ni mkuu mwenye uweza; tena mwenye hukumu, na mwingi wa haki, hataonea.” (Ayubu 34:10; 36:22, 23; 37:23) Tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu anapopigana, anakuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo. Tukiwa na jambo hilo akilini, hebu tuchunguze baadhi ya sababu zinazomfanya Mungu wa amani aamue kuwa shujaa wa vita.—1 Wakorintho 14:33.

      Mambo Yanayomfanya Mungu wa Amani Apigane

      9. Kwa nini Mungu wa amani hupigana?

      9 Baada ya kumsifu Mungu kuwa “mtu wa vita,” Musa aliuliza hivi: “Ee BWANA, katika miungu ni nani aliye kama wewe? Ni nani aliye kama wewe, mtukufu katika utakatifu?” (Kutoka 15:11) Vivyo hivyo, nabii Habakuki aliandika hivi: “Wewe uliye na macho safi hata usiweze kuangalia uovu, wewe usiyeweza kutazama ukaidi.” (Habakuki 1:13) Ijapokuwa Yehova ni Mungu wa upendo, yeye pia ni Mungu wa utakatifu, uadilifu, na haki. Nyakati nyingine, yeye hutumia nguvu zake za kuangamiza kwa sababu ya sifa hizo. (Isaya 59:15-19; Luka 18:7) Kwa hiyo, Mungu hachafui utakatifu wake anapopigana. Badala yake, yeye hupigana kwa sababu yeye ni mtakatifu.—Kutoka 39:30.

      10. (a) Mungu alihitaji kupigana vita kwa mara ya kwanza lini na jinsi gani? (b) Uadui uliotabiriwa kwenye Mwanzo 3:15 unaweza kukomeshwa tu kwa njia gani, na wanadamu waadilifu watapata baraka gani?

      10 Hebu fikiria hali iliyotokea baada ya wenzi wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, kumwasi Mungu. (Mwanzo 3:1-6) Kama Yehova angalivumilia uasi wao, angalidunisha cheo chake mwenyewe akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote. Akiwa Mungu mwadilifu, alikuwa na wajibu wa kuwahukumia kifo. (Waroma 6:23) Katika unabii wa kwanza wa Biblia, alitabiri kwamba kungekuwa na uadui kati ya watumishi wake na wafuasi wa “nyoka,” yaani, Shetani. (Ufunuo 12:9; Mwanzo 3:15) Mwishowe, uadui huo ungekomeshwa tu kwa kumponda-ponda Shetani. (Waroma 16:20) Lakini tendo hilo la hukumu litawaletea wanadamu waadilifu baraka nyingi, litakomesha uvutano wa Shetani duniani halafu paradiso itaenea ulimwenguni pote. (Mathayo 19:28) Kabla ya wakati huo, wale waliomwunga mkono Shetani wangeendelea kuhatarisha hali ya kimwili na ya kiroho ya watu wa Mungu. Pindi kwa pindi, Yehova angelazimika kuchukua hatua.

      Matendo ya Mungu ya Kuondoa Uovu

      11. Kwa nini Mungu alikuwa na wajibu wa kuleta gharika duniani pote?

      11 Gharika ya siku ya Noa ilikuwa mojawapo ya matendo hayo ya Mungu. Andiko la Mwanzo 6:11, 12 lasema hivi: “Dunia ikaharibika mbele za Mungu, dunia ikajaa dhuluma. Mungu akaiona dunia, na tazama, imeharibika; maana kila mwenye mwili amejiharibia njia yake duniani.” Je, Mungu angeruhusu waovu waharibu kabisa maadili yote duniani? La. Yehova alikuwa na wajibu wa kuleta gharika duniani pote ili kuwaangamiza wale walioazimia kuendeleza jeuri na ukosefu wa adili.

      12. (a) Yehova alitabiri nini kuhusu “uzao” wa Abrahamu? (b) Waamori wangeangamizwa kwa sababu gani?

      12 Ndivyo ilivyokuwa kuhusu hukumu ya Mungu dhidi ya Wakanaani. Yehova alifunua kwamba jamaa zote duniani zingejibariki kupitia “uzao” wa Abrahamu. Kwa kupatana na kusudi hilo, Mungu aliagiza kwamba uzao wa Abrahamu upewe nchi ya Kanaani, iliyokaliwa na Waamori. Je, Mungu alikuwa na sababu halali ya kuwafukuza watu hao kutoka nchi yao? Yehova alitabiri kwamba hangewafukuza kwa muda wa miaka 400—hadi ‘uovu wa Waamori utimie.’b (Mwanzo 12:1-3; 13:14, 15; 15:13, 16; 22:18) Katika kipindi hicho, Waamori walitumbukia katika ukosefu mbaya sana wa adili. Kanaani ikawa nchi iliyojaa ibada ya sanamu, umwagaji-damu, na mazoea machafu sana ya ngono. (Kutoka 23:24; 34:12, 13; Hesabu 33:52) Wenyeji wa nchi hiyo hata waliwaua watoto kwa kuwadhabihu katika moto. Je, Mungu mtakatifu angeweza kuwaacha watu wake waishi katika uovu huo? La hasha! Alisema hivi: “Hiyo nchi imekuwa najisi; kwa ajili ya hayo naipatiliza uovu wake juu yake, na hiyo nchi yatapika wenyeji wake na kuwatoa.” (Mambo ya Walawi 18:21-25) Hata hivyo, Yehova hakuwaua watu wote bila kujali. Wakanaani wenye mwelekeo unaofaa, kama vile Rahabu na Wagibeoni, hawakuuawa.—Yoshua 6:25; 9:3-27.

      Anapigania Jina Lake

      13, 14. (a) Kwa nini Yehova alikuwa na wajibu wa kutakasa jina lake? (b) Yehova aliondoleaje jina lake lawama?

      13 Jina la Yehova ni takatifu kwa sababu yeye ni Mtakatifu. (Mambo ya Walawi 22:32) Yesu aliwafundisha wanafunzi wake wasali hivi: “Jina lako na litakaswe.” (Mathayo 6:9) Uasi katika Edeni ulichafua jina la Mungu na kutilia shaka sifa yake na utawala wake. Yehova hangeweza kamwe kuachilia tu uchongezi na uasi wa aina hiyo. Alikuwa na wajibu wa kutakasa jina lake.—Isaya 48:11.

      14 Fikiria tena Waisraeli. Maadamu walikuwa watumwa nchini Misri, ahadi ya Mungu kwa Abrahamu kwamba kupitia uzao wake jamaa zote duniani zingejibarikia ilionekana kuwa ya bure. Lakini Yehova aliondolea jina lake lawama alipowakomboa na kuwafanya kuwa taifa. Kwa hiyo, nabii Danieli alisema hivi aliposali: ‘Ee Bwana Mungu wetu, uliwatoa watu wako hawa katika nchi ya Misri kwa mkono hodari, ukajipatia sifa.’—Danieli 9:15.

      15. Kwa nini Yehova aliwaokoa Wayahudi kutoka utekwani Babiloni?

      15 Inapendeza kwamba Danieli alisali hivyo Wayahudi walipohitaji Yehova achukue hatua mara nyingine ili kutetea jina Lake. Wayahudi hao wasiotii walikuwa utekwani huko Babiloni. Mji wao mkuu, Yerusalemu, ulikuwa magofu. Danieli alijua kwamba kurudishwa kwa Wayahudi nchini mwao kungelitukuza jina la Yehova. Hivyo Danieli alisali hivi: “Ee Bwana, usamehe; Ee Bwana, usikilize, ukatende, usikawie; kwa ajili yako wewe, Ee Mungu wangu; kwa sababu mji wako na watu wako wanaitwa kwa jina lako.”—Danieli 9:18, 19.

      Anawapigania Watu Wake

      16. Eleza kwa nini nia ya Yehova ya kutetea jina lake haimaanishi kwamba yeye hana hisia na ni mwenye ubinafsi.

      16 Je, nia ya Yehova ya kutetea jina lake yamaanisha kwamba yeye hana hisia na ni mwenye ubinafsi? La, yeye huwalinda watu wake ili kutetea haki na utakatifu wake. Fikiria Mwanzo sura ya 14. Twasoma kuhusu wafalme wanne wavamizi waliomteka nyara mpwa wa kiume wa Abrahamu, Loti, na familia yake. Kwa msaada wa Yehova, Abrahamu alishinda kabisa majeshi makubwa sana! Yaelekea ushindi huo ulikuwa kisa cha kwanza kurekodiwa katika “kitabu cha vita vya Mwenyezi Mungu.” Na yaonekana kwamba mapambano kadhaa ya kijeshi ambayo hayakuandikwa katika Biblia yalirekodiwa pia katika kitabu hicho. (Hesabu 21:14, BHN) Ushindi mwingine mwingi ungefuata.

      17. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yehova aliwapigania Waisraeli baada ya wao kuingia katika nchi ya Kanaani? Toa mifano.

      17 Muda mfupi kabla ya Waisraeli kuingia katika nchi ya Kanaani, Musa aliwahakikishia hivi: “BWANA, Mungu wenu, anayetangulia mbele yenu, ndiye atakayewapigania, kwa mfano wa yote aliyowafanyia huko Misri.” (Kumbukumbu la Torati 1:30; 20:1) Kwa kweli Yehova aliwapigania watu wake kuanzia wakati wa Yoshua yule mrithi wa Musa, hadi muhula wote wa Waamuzi na utawala wa Wafalme waaminifu wa Yuda. Mara nyingi, aliwasaidia kushinda kabisa maadui wao.—Yoshua 10:1-14; Waamuzi 4:12-17; 2 Samweli 5:17-21.

      18. (a) Kwa nini tushukuru kwamba Yehova hajabadilika? (b) Ni nini kitakachotukia wakati uadui unaoelezwa kwenye Mwanzo 3:15 unapofikia kilele?

      18 Yehova hajabadilika; wala kusudi lake la kuifanya dunia hii iwe paradiso yenye amani halijabadilika. (Mwanzo 1:27, 28) Bado Mungu anachukia uovu. Na vilevile, anawapenda mno watu wake, naye atawapigania hivi karibuni. (Zaburi 11:7) Kwa kweli, uadui unaoelezwa kwenye Mwanzo 3:15 unatarajiwa kufikia hatua muhimu sana ya ghafula na yenye msukosuko hivi karibuni. Kwa mara nyingine, Yehova atakuwa “mtu wa vita” ili kutakasa jina lake na kuwalinda watu wake!—Zekaria 14:3; Ufunuo 16:14, 16.

      19. (a) Toa mfano unaoonyesha kwamba nguvu za Mungu za kuangamiza zinaweza kutuvuta karibu naye. (b) Tunapaswa kuhisije kuhusu utayari wa Mungu wa kupigana?

      19 Fikiria mfano huu: Tuseme kwamba familia ya mwanamume mmoja ilikuwa ikishambuliwa na mnyama hatari kisha mwanamume huyo akaingilia pambano hilo na kumwua mnyama huyo mkali. Je, ungetarajia mke na watoto wake wakasirishwe na tendo lake? Kinyume chake, ungetarajia waguswe na upendo wake usio na ubinafsi. Vivyo hivyo, hatupaswi kukasirika Mungu anapotumia nguvu zake za kuangamiza. Tunapaswa kumpenda hata zaidi kwa sababu yu tayari kupigana ili kutulinda. Vilevile tunapaswa kumstahi hata zaidi kwa sababu ya nguvu zake zisizo na mipaka. Kwa hiyo, tunaweza “kumtolea Mungu . . . utumishi mtakatifu kwa hofu ya kimungu na kicho.”—Waebrania 12:28.

      Mkaribie Yule “Mtu wa Vita”

      20. Tunapaswa kufanya nini tunaposoma masimulizi ya Biblia kuhusu vita vya Mungu ambavyo huenda tusielewe kikamili, na kwa nini tufanye hivyo?

      20 Bila shaka, Biblia haielezi kila jambo linalohusika katika maamuzi ya Yehova kuhusu vita vyake. Lakini sikuzote tunaweza kuwa na hakika kuhusu jambo hili: Yehova hatumii kamwe nguvu zake za kuangamiza kwa njia isiyo ya haki, bila sababu nzuri, au kwa ukatili. Mara nyingi, kuchunguza muktadha wa simulizi la Biblia au habari fulani za ziada kunaweza kutusaidia kuelewa visa hivyo. (Mithali 18:13) Hata tusipokuwa na habari zote, kujifunza mengi juu ya Yehova na kutafakari juu ya sifa zake tukufu kunaweza kutusaidia kuondoa shaka yoyote tunayoweza kuwa nayo. Kwa kufanya hivyo tunagundua kwamba tuna sababu nyingi sana za kumtumaini Mungu wetu Yehova.—Ayubu 34:12.

      21. Ajapokuwa “mtu wa vita” nyakati nyingine, Yehova ana sifa zipi?

      21 Ijapokuwa Yehova huwa “mtu wa vita” nyakati nyingine, hilo halimaanishi kwamba yeye ni mpenda-vita. Katika ono la Ezekieli kuhusu gari la kimbingu, Yehova anaonyeshwa akiwa tayari kupigana na maadui wake. Hata hivyo, Ezekieli alimwona Mungu akiwa amezungukwa na upinde wa mvua—ishara ya amani. (Mwanzo 9:13; Ezekieli 1:28; Ufunuo 4:3) Ni wazi kwamba Yehova ni mtulivu na mwenye kutafuta amani. “Mungu ni upendo,” akaandika mtume Yohana. (1 Yohana 4:8) Sifa zote za Yehova zimesawazika kikamili. Basi, tuna pendeleo lililoje la kuweza kumkaribia Mungu huyo mwenye nguvu na upendo!

      a Mwanahistoria Myahudi Josephus anasema kwamba Waebrania, “walifukuzwa na magari 600 yanayokokotwa na farasi na wapanda-farasi 50,000 na askari 200,000 wa miguu.”—Jewish Antiquities, II, 324 [xv, 3].

      b Kwa wazi, neno hili “Waamori” latia ndani wenyeji wote wa Kanaani.—Kumbukumbu la Torati 1:6-8, 19-21, 27; Yoshua 24:15, 18.

      Maswali ya Kutafakari

      • 2 Wafalme 6:8-17 Akiwa “Bwana wa majeshi,” Yehova anaweza kututiaje moyo tunapopata matatizo?

      • Ezekieli 33:10-20 Kabla ya kutumia nguvu zake za kuangamiza, kwa rehema Yehova huwapa wale wanaovunja sheria yake nafasi ya kufanya nini?

      • 2 Wathesalonike 1:6-10 Uharibifu unaokuja wa watu waovu utawaleteaje watumishi waaminifu wa Mungu kitulizo?

      • 2 Petro 2:4-13 Ni nini kinachomfanya Yehova atumie nguvu zake za kuangamiza, na hilo lawafunza wanadamu wote masomo gani?

  • Nguvu za Kulinda—“Mungu Ni Kimbilio Letu”
    Mkaribie Yehova
    • Mwana-kondoo akiwa salama kifuani mwa mchungaji

      Sura ya 7

      Nguvu za Kulinda—“Mungu Ni Kimbilio Letu”

      1, 2. Waisraeli walikabili hatari gani walipofika eneo la Sinai mwaka wa 1513 K.W.K., na Yehova aliwatiaje moyo?

      WAISRAELI walikuwa hatarini walipofika eneo la Sinai mapema mwaka wa 1513 K.W.K. Wangefunga safari ndefu yenye kuogofya sana, wangesafiri katika “lile jangwa kubwa na la kutisha, lenye nyoka wenye sumu na ng’e.” (Kumbukumbu la Torati 8:15, BHN) Walikabili pia tisho la kushambuliwa na mataifa yenye uadui. Yehova aliwaleta watu wake katika hali hiyo. Je, angeweza kuwalinda akiwa Mungu wao?

      2 Maneno ya Yehova yalikuwa yenye kutia moyo sana: “Mmeona jinsi nilivyowatendea Wamisri, na jinsi nilivyowachukua ninyi juu ya mbawa za tai, nikawaleta ninyi kwangu mimi.” (Kutoka 19:4) Yehova aliwakumbusha watu wake kwamba aliwakomboa kutoka kwa Wamisri, ni kama aliwachukua juu ya mbawa za tai na kuwapeleka mahali salama. Lakini kuna sababu nyingine zinazofanya “mbawa za tai” ziwe mfano ufaao wa ulinzi wa Mungu.

      3. Kwa nini “mbawa za tai” ni mfano ufaao wa ulinzi wa Mungu?

      3 Tai hutumia mbawa zake pana na zenye nguvu sana kwa sababu nyingine mbali na kupaa hewani. Kunapokuwa na joto kali wakati wa mchana, tai mama hukunja mbawa zake—ambazo zinaweza kuwa na upana wa zaidi ya meta mbili—ili kufunika na kulinda makinda yake dhaifu kutokana na joto kali sana la jua. Nyakati nyingine, yeye huyafunika makinda yake kwa mbawa zake na kuyalinda na upepo wenye baridi. Yehova alilinda na kukinga taifa changa la Israeli kama tai anavyolinda makinda yake. Sasa wakiwa jangwani, watu wake wangeendelea kukimbilia uvuli wa mbawa zake za mfano zenye nguvu maadamu walibaki waaminifu. (Kumbukumbu la Torati 32:9-11; Zaburi 36:7) Lakini je, leo tunaweza kutarajia kwa kufaa kupata ulinzi wa Mungu?

      Ahadi ya Kupata Ulinzi wa Mungu

      4, 5. Kwa nini tunaweza kutumaini kabisa ahadi ya Mungu ya kutulinda?

      4 Bila shaka Yehova anaweza kuwalinda watumishi wake. Yeye ni “Mungu Mwenyezi”—cheo hicho kinamaanisha kwamba ana nguvu zisizoweza kushindwa. (Mwanzo 17:1) Kama wimbi lenye nguvu sana, nguvu za Yehova haziwezi kuzuiwa. Kwa kuwa anaweza kufanya jambo lolote kulingana na mapenzi yake, huenda tukauliza hivi, ‘Je, ni mapenzi ya Yehova kutumia nguvu zake ili kuwalinda watu wake?

      5 Kwa neno moja, jibu ni ndiyo! Yehova anatuhakikishia kwamba atawalinda watu wake. “Mungu ni kimbilio letu na nguvu yetu, yeye ni msaada wetu daima wakati wa taabu,” yasema Zaburi 46:1, BHN. Kwa kuwa Mungu ‘hawezi kusema uwongo,’ tunaweza kutumaini kabisa ahadi yake ya kutulinda. (Tito 1:2) Hebu tuchunguze baadhi ya mifano dhahiri ambayo Yehova anatumia ili kuonyesha ulinzi wake.

      6, 7. (a) Mchungaji katika nyakati za Biblia aliwalinda kondoo wake kutokana na nini? (b) Biblia inatoa mfano gani unaoonyesha jinsi Yehova anavyotaka kwa dhati kulinda na kutunza kondoo wake?

      6 Yehova ni Mchungaji, nasi tu “watu wake, na kondoo wa malisho yake.” (Zaburi 23:1; 100:3) Wanyama wengi si hoi kama kondoo anayefugwa. Mchungaji katika nyakati za Biblia alihitaji kuwa jasiri ili kuwalinda kondoo wake kutoka kwa simba, mbwa-mwitu, na dubu, na vilevile wezi. (1 Samweli 17:34, 35; Yohana 10:12, 13) Lakini nyakati nyingine kuwalinda kondoo kulihitaji wororo. Kondoo alipozalia mbali na zizi, mchungaji mwenye kujali angemlinda mama huyo pindi hiyo alipohitaji sana ulinzi, kisha angembeba mwana-kondoo wake dhaifu na kumpeleka zizini.

      mchungaji akiwa amembeba mwana-kondoo kwa wororo akiwa salama kifuani mwake

      ’Atawachukua kifuani mwake’

      7 Kwa kujilinganisha na mchungaji, Yehova anatuhakikishia kwamba anataka kwa dhati kutulinda. (Ezekieli 34:11-16) Hebu kumbuka jinsi Yehova anavyoelezwa kwenye Isaya 40:11, kama Sura ya 2 ya kitabu hiki ilivyoonyesha: “Atalilisha kundi lake kama mchungaji, atawakusanya wana-kondoo mikononi mwake; na kuwachukua kifuani mwake.” Mwana-kondoo mchanga anafikaje “kifuani” mwa mchungaji—katika mapindo ya vazi lake la juu? Huenda mwana-kondoo huyo akamkaribia mchungaji, na hata kugusa mguu wake kwa upole. Hata hivyo, ni lazima mchungaji ainame, amchukue mwana-kondoo huyo, na kumweka taratibu kifuani penye usalama. Huo ni mfano wenye kugusa moyo kama nini unaoonyesha jinsi Mchungaji wetu Mkuu alivyo tayari kutukinga na kutulinda!

      8. (a) Ni nani wanaoahidiwa kupata ulinzi wa Mungu, na hilo linaonyeshwaje na Mithali 18:10? (b) Kukimbilia jina la Mungu kunahusisha nini?

      8 Ahadi ya Mungu ya kuandaa ulinzi ina masharti—wale tu wanaomkaribia ndiyo wanaopata ulinzi huo. Andiko la Mithali 18:10 lasema: “Jina la BWANA ni ngome imara. Mwenye haki huikimbilia, akawa salama.” Katika nyakati za Biblia, mara kwa mara ngome zilijengwa jangwani kama mahali salama pa kukimbilia. Lakini yule aliyekuwa hatarini ndiye aliyekuwa na daraka la kukimbilia kwenye ngome hizo ili kupata usalama. Ndivyo ilivyo na kukimbilia jina la Mungu. Hilo halimaanishi kurudia-rudia tu jina la Mungu; jina la Mungu si hirizi ya kimizungu. Badala yake, tunahitaji kumjua na kumtumaini Yule anayeitwa kwa jina hilo na kuishi kwa kupatana na viwango vyake vya uadilifu. Yehova ni mwenye fadhili kama nini kwa kutuhakikishia kwamba endapo tutamfikia kwa imani, atakuwa ngome ya kutulinda!

      “Mungu Wetu . . . Aweza Kutuokoa”

      9. Yehova amefanyaje mengi mbali na kuahidi ulinzi?

      9 Yehova amefanya mengi mbali na kuahidi tu ulinzi. Katika nyakati za Biblia, alionyesha kupitia miujiza kwamba anaweza kuwalinda watu wake. Katika historia yote ya Waisraeli, mara nyingi “mkono” wa Yehova wenye uwezo uliwakomesha maadui wenye nguvu. (Kutoka 7:4) Lakini Yehova alitumia pia nguvu zake za kulinda kwa niaba ya watu fulani.

      10, 11. Ni mifano gani ya Kibiblia inayoonyesha jinsi Yehova alivyotumia nguvu zake za kulinda kwa niaba ya watu fulani?

      10 Vijana watatu Waebrania—Shadraka, Meshaki, na Abednego—walipokataa kuisujudia sanamu ya dhahabu ya Mfalme Nebukadneza, mfalme huyo mwenye hasira alitisha kuwatupa katika tanuru yenye moto mkali sana. “Ni nani Mungu yule atakayewaokoa ninyi na mikono yangu?” akadhihaki Nebukadneza, mtawala mwenye nguvu zaidi duniani. (Danieli 3:15) Vijana hao watatu walijua kwa hakika kwamba Mungu wao alikuwa na nguvu za kuwalinda, lakini hawakutarajia kwamba angewalinda. Kwa hiyo, walijibu hivi: “Kama ni hivyo, Mungu wetu tunayemtumikia aweza kutuokoa.” (Danieli 3:17) Kwa kweli, tanuru hiyo ijapotiwa moto mara saba kuliko ilivyo kawaida, haikuwa kitu kwa Mungu wao mwenye nguvu zote. Aliwalinda, na mfalme huyo alilazimika kukiri hivi: “Hakuna Mungu mwingine awezaye kuokoa namna hii.”—Danieli 3:29.

      11 Yehova alionyesha pia nguvu zake kuu za kulinda alipohamisha uhai wa Mwanaye mzaliwa-pekee hadi kwenye tumbo la uzazi la bikira Myahudi Maria. Malaika alimwambia Maria kwamba ‘angechukua mimba katika tumbo [lake] la uzazi na kuzaa mwana.’ Malaika huyo alieleza hivi: “Roho takatifu itakuja juu yako, na nguvu ya Aliye Juu Zaidi Sana itakufunika kivuli.” (Luka 1:31, 35) Yaonekana kwamba Mwana wa Mungu angeweza kushambuliwa kwa urahisi sana pindi hiyo. Je, dhambi na kutokamilika kwa mama yake wa kibinadamu kungechafua kiini-tete hicho? Je, Shetani angeweza kumjeruhi au kumwua Mwana huyo kabla hajazaliwa? Haiwezekani! Kwa kweli Yehova alimlinda Maria tangu mimba ilipotungwa na kuendelea ili kitu chochote—iwe ni kutokamilika, hatari yoyote, mwanadamu yeyote mwenye nia ya kuua, wala roho yeyote mwovu asiweze kuharibu kiini-tete hicho. Yehova aliendelea kumlinda Yesu alipokuwa kijana. (Mathayo 2:1-15) Mwana mpendwa wa Mungu hangeweza kushambuliwa hadi wakati uliowekwa na Mungu.

      12. Kwa nini Yehova aliwalinda kimuujiza watu fulani katika nyakati za Biblia?

      12 Kwa nini Yehova aliwalinda watu fulani kimuujiza? Katika visa vingi, Yehova aliwalinda watu fulani akiwa na kusudi la kulinda jambo muhimu zaidi: kutimia kwa kusudi lake. Kwa kielelezo, kuokoka kwa mtoto mchanga Yesu kulikuwa muhimu katika utimizo wa kusudi la Mungu, ambalo litafaidi wanadamu wote hatimaye. Masimulizi ya maonyesho hayo ya nguvu za kulinda ni sehemu ya Maandiko yaliyopuliziwa, ambayo “yaliandikwa kwa kufunzwa kwetu, ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutokana na Maandiko tupate kuwa na tumaini.” (Waroma 15:4) Naam, mifano hiyo inaimarisha imani yetu katika Mungu wetu mwenye nguvu zote. Lakini tunaweza kutarajia kupata ulinzi gani kutoka kwa Mungu leo?

      Ahadi ya Kupata Ulinzi wa Mungu Haimaanishi Nini?

      13. Je, Yehova ana wajibu wa kutuokoa kimuujiza? Eleza.

      13 Ahadi ya kupata ulinzi wa Mungu haimaanishi kwamba Yehova ana wajibu wa kutuokoa kimuujiza. La, Mungu wetu hajaahidi kwamba tutaishi bila matatizo katika mfumo huu wa kale. Watumishi wengi waaminifu wa Yehova wanakumbwa na taabu nyingi sana, kutia ndani umaskini, vita, magonjwa, na kifo. Yesu aliwaambia wanafunzi wake waziwazi kwamba huenda baadhi yao wakauawa kwa sababu ya imani yao. Ndiyo sababu Yesu alikazia uhitaji wa kuvumilia hadi mwisho. (Mathayo 24:9, 13) Ikiwa Yehova angetumia nguvu zake kuokoa watu kimuujiza kila wakati, yamkini Shetani angekuwa na sababu ya kumdhihaki Yehova na kutilia shaka unyofu wetu wa kumtumikia Mungu.—Ayubu 1:9, 10.

      14. Ni mifano gani inayoonyesha kwamba sikuzote Yehova hawalindi watumishi wake wote kwa njia ileile?

      14 Hata katika nyakati za Biblia, Yehova hakutumia nguvu zake za kulinda ili kuwakinga watumishi wake wote na kifo cha mapema. Kwa mfano, Herode alimwua mtume Yakobo kwa upanga yapata mwaka wa 44 W.K.; lakini, muda mfupi baadaye, Petro alikombolewa “kutoka kwenye mkono wa Herode.” (Matendo 12:1-11) Na Yohana, ndugu ya Yakobo, aliishi kwa muda mrefu kuliko Petro na Yakobo. Ni wazi kwamba hatuwezi kumtarajia Mungu wetu awalinde watumishi wake wote kwa njia ileile. Isitoshe, “wakati na tukio lisilotazamiwa” hutupata sote. (Mhubiri 9:11, NW) Basi, Yehova anatulindaje leo?

      Yehova Anatulinda Kimwili

      15, 16. (a) Kuna uthibitisho gani kwamba Yehova amewalinda kimwili waabudu wake wakiwa kikundi? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atawalinda watumishi wake sasa na wakati wa ile “dhiki kubwa”?

      15 Kwanza, fikiria kuhusu ulinzi wa kimwili. Tukiwa waabudu wa Yehova, tunaweza kutarajia kulindwa kimwili tukiwa kikundi. La sivyo, tungeshambuliwa kwa urahisi na Shetani. Hebu fikiria jambo hili: Shetani, “mtawala wa ulimwengu huu,” angependa sana kukomesha ibada ya kweli. (Yohana 12:31; Ufunuo 12:17) Baadhi ya serikali zenye nguvu sana duniani zimepiga marufuku kazi yetu ya kuhubiri na kujaribu kutuangamiza kabisa. Hata hivyo, watu wa Yehova wamedumu wakiwa imara na wameendelea kuhubiri bila kuacha! Kwa nini mataifa yenye nguvu yameshindwa kukomesha utendaji wa kikundi hiki kidogo cha Wakristo kinachoonekana kuwa bila ulinzi? Kwa sababu Yehova ametufunika kwa mbawa zake za mfano zenye nguvu!—Zaburi 17:7, 8.

      16 Je, atatulinda kimwili wakati wa ile “dhiki kubwa” inayokuja? Hatuhitaji kuogopa hukumu ya Mungu. Kwa sababu “Yehova ajua jinsi ya kukomboa watu wenye ujitoaji-kimungu kutoka katika jaribu, bali kuweka akiba watu wasio waadilifu kwa ajili ya siku ya hukumu ili kukatiliwa mbali.” (Ufunuo 7:14; 2 Petro 2:9) Kwa sasa, tunaweza kuwa na hakika kabisa kuhusu mambo mawili. Kwanza, Yehova hataruhusu kamwe watumishi wake waaminifu waangamizwe kabisa duniani. Pili, atawapa wale wanaobaki waaminifu zawadi ya kuishi milele katika ulimwengu wake mpya wa uadilifu—hata kama itambidi awafufue. Kwa wale wanaokufa, hakuna mahali pengine salama pa kuwa isipokuwa katika kumbukumbu ya Mungu.—Yohana 5:28, 29.

      17. Yehova anatulindaje kupitia Neno lake?

      17 Hata sasa, Yehova anatulinda kupitia “neno” lake lililo hai, ambalo lina nguvu ya kuponya watu mioyo na kubadili maisha yao. (Waebrania 4:12) Tunapoishi kwa kupatana na kanuni zake, tunaweza kulindwa kutokana na madhara fulani ya kimwili. “Mimi ni BWANA, . . . nikufundishaye ili upate faida,” yasema Isaya 48:17. Bila shaka, kuishi kwa kupatana na Neno la Mungu kunaweza kuboresha afya yetu na kurefusha maisha yetu. Kwa mfano, tunapotii shauri la Biblia la kujiepusha na uasherati na kujisafisha na kila unajisi, tunaepuka mazoea machafu na yenye kuumiza ambayo yanaharibu kabisa maisha ya watu wengi wasiomtii Mungu. (Matendo 15:29; 2 Wakorintho 7:1) Tunashukuru kama nini kwamba tunalindwa na Neno la Mungu!

      Yehova Anatulinda Kiroho

      18. Yehova anatulindaje kiroho?

      18 Jambo muhimu zaidi ni kwamba Yehova anatulinda kiroho. Mungu wetu mwenye upendo anatulinda kutokana na madhara ya kiroho kwa kutupatia chochote tunachohitaji ili kuvumilia majaribu na kulinda uhusiano wetu naye. Kwa hiyo, Yehova huhifadhi uhai wetu, si kwa miaka michache tu bali kwa umilele. Fikiria baadhi ya maandalizi ya Mungu yanayoweza kutulinda kiroho.

      19. Roho ya Yehova inaweza kutusaidiaje kukabiliana na jaribu lolote ambalo huenda likatukumba?

      19 Yehova ni “msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2, NW) Tunaweza kupata kitulizo wakati mikazo ya maisha inapotulemea, kwa kumwambia mambo yaliyo mioyoni mwetu. (Wafilipi 4:6, 7) Huenda asiondoe majaribu yetu kimuujiza, lakini anaweza kujibu sala zetu za kutoka moyoni kwa kutupa hekima ya kukabiliana nayo. (Yakobo 1:5, 6) Na zaidi ya hayo, Yehova huwapa roho takatifu wale wanaomwomba. (Luka 11:13) Roho hiyo yenye nguvu inaweza kutusaidia kukabiliana na jaribu au tatizo lolote ambalo huenda likatukumba. Inaweza kututia “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili tuvumilie hadi Yehova atakapoondoa matatizo yote yenye kuumiza katika ulimwengu mpya ulio karibu sana.—2 Wakorintho 4:7.

      20. Nguvu za Yehova za kulinda zinaweza kuonekanaje kupitia waamini wenzetu?

      20 Nyakati nyingine, nguvu za Yehova za kulinda zinaweza kuonekana kupitia waabudu wenzetu. Yehova amewakusanya watu wake katika ‘ushirika [wa ulimwenguni pote] wa ndugu.’ (1 Petro 2:17; Yohana 6:44) Kupitia ushirika huo wenye upendo, tunaona kihalisi jinsi roho takatifu ya Mungu ilivyo na nguvu za kuboresha maisha ya watu. Roho hiyo hukuza matunda ndani yetu, yaani, sifa muhimu zenye kuvutia sana kama vile upendo, fadhili, na wema. (Wagalatia 5:22, 23) Kwa hiyo, tunapokuwa taabani na mwamini mwenzetu anachochewa kutupa shauri lenye kusaidia au kututia moyo inapohitajika, tunaweza kumshukuru Yehova kwa sababu ya ulinzi na utunzaji anaotoa kwa njia hiyo.

      21. (a) Yehova anaandaa chakula kipi cha kiroho kwa wakati ufaao kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara”? (b) Je, wewe binafsi umefaidika na maandalizi ya Yehova ya kutulinda kiroho?

      21 Yehova hutayarisha mambo mengine ya kutulinda: chakula cha kiroho kwa wakati ufaao. Ili kutusaidia kuimarishwa na Neno lake, Yehova amemwagiza “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” aandae chakula cha kiroho. Mtumwa huyo mwaminifu hutumia vichapo, kama magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, vilevile mikutano, na makusanyiko ili kutupatia ‘chakula kwa wakati ufaao’—chochote tunachohitaji, wakati tunapokihitaji. (Mathayo 24:45) Je, umewahi kusikia jambo fulani kwenye mikutano ya Kikristo—katika maelezo, hotuba, au hata katika sala—ambalo lilikupa nguvu na kitia-moyo ulichohitaji sana? Je, maisha yako yamewahi kuathiriwa na makala fulani hususa iliyochapishwa katika mojawapo ya magazeti yetu? Kumbuka kwamba Yehova hutayarisha maandalizi hayo yote ili kutulinda kiroho.

      22. Sikuzote Yehova hutumia nguvu zake kwa njia gani, na kwa nini jambo hilo linatufaidi?

      22 Hapana shaka kwamba Yehova ni ngao ‘ya wote wanaomkimbilia.’ (Zaburi 18:30) Tunafahamu kwamba yeye hatumii nguvu zake kutulinda tusipatwe na misiba sasa. Hata hivyo, sikuzote yeye hutumia nguvu zake za kulinda kuhakikisha kwamba kusudi lake linatimizwa. Yeye hufanya hivyo ili kuwafaidi watu wake hatimaye. Tukimkaribia na kudumu katika upendo wake, Yehova atatupatia uhai mkamilifu utakaodumu milele. Tukikumbuka tumaini hilo, kwa kweli tunaweza kuona mateso yoyote yanayotupata katika mfumo huu kuwa ‘ya dakika na mepesi.’—2 Wakorintho 4:17.

      Maswali ya Kutafakari

      • Zaburi 23:1-6 Akiwa Mchungaji Mkuu, Yehova anawalindaje na kuwatunza watu wake wa mfano wa kondoo?

      • Zaburi 91:1-16 Yehova anatulindaje tusipatwe na msiba wa kiroho, na ni lazima tufanye nini ili atulinde?

      • Danieli 6:16-22, 25-27 Yehova alimfundishaje mfalme wa kale kuhusu nguvu Zake za kulinda, nasi twajifunza somo gani kutokana na mfano huo?

      • Mathayo 10:16-22, 28-31 Tunaweza kutarajia kupata upinzani upi, lakini kwa nini hatupaswi kuwaogopa wapinzani?

  • Uwezo wa Kurudisha Hali Nzuri—Yehova ‘Anafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya’
    Mkaribie Yehova
    • Kwa furaha mjane anamkumbatia mvulana wake aliyefufuliwa.

      Sura ya 8

      Uwezo wa Kurudisha Hali Nzuri—Yehova ‘Anafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya’

      1, 2. Wanadamu hukumbwa na matatizo gani leo, nayo yanatuathirije?

      MTOTO hulia kwa uchungu sana kitu cha kuchezea anachopenda kinapoharibika. Kilio chake huhuzunisha sana! Lakini je, umewahi kuona jinsi mtoto anavyosisimuka mzazi anapokirekebisha kitu hicho na kukirudisha katika hali nzuri? Huenda mzazi akarekebisha kitu hicho kwa urahisi sana. Lakini mtoto anafurahi sana na kupigwa na bumbuazi. Kitu cha kuchezea alichofikiri kimeharibika kabisa kimerudishwa katika hali nzuri!

      2 Yehova ambaye ni Baba bora zaidi, ana uwezo wa kurudisha katika hali nzuri vitu na hali mbalimbali ambazo watoto wake wa kidunia huenda wakadhani haziwezi kuboreshwa. Bila shaka, hatumaanishi vitu vya kuchezea. Hatuna budi kupatwa na matatizo makubwa zaidi katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.’ (2 Timotheo 3:1-5) Vitu ambavyo watu wanathamini sana, kama vile makao, mali, kazi, hata afya viko hatarini daima. Huenda pia tukafadhaika kuona mazingira yakiharibiwa na kuona hasara kubwa inayosababishwa na uharibifu huo, au kuona jamii nyingi za viumbe zikitoweka kabisa. Hata hivyo, hakuna jambo linalotuhuzunisha zaidi kuliko kifo cha mpendwa wetu. Uchungu wa kumpoteza mpendwa na kuhisi tukiwa hoi unaweza kutulemea sana.—2 Samweli 18:33.

      3. Ni taraja gani lenye kufariji linalotajwa kwenye Matendo 3:21, na Yehova atalitimizaje?

      3 Basi inafariji kama nini kujua kwamba Yehova ana uwezo wa kurudisha mambo yote katika hali nzuri! Kama tutakavyoona, Mungu ana uwezo wa kurudisha katika hali nzuri mambo mengi sana yaliyoharibika duniani. Kwa kweli, Biblia inaonyesha kwamba Yehova anakusudia ‘kurudisha mambo yote.’ (Matendo 3:21) Yehova atatumia Ufalme wa Kimesiya, unaotawaliwa na Mwanaye, Yesu Kristo ili kutimiza hayo. Kuna uthibitisho kwamba Ufalme huo ulianza kutawala mbinguni mwaka wa 1914.a (Mathayo 24:3-14) Ni mambo gani yatakayorudishwa katika hali nzuri? Tuchunguze baadhi ya mambo matukufu ambayo Yehova amenuia kurudisha katika hali nzuri. Tunaweza kuona na kufurahia mojawapo ya mambo hayo hivi sasa. Mambo mengineyo yatarudishwa kikamili wakati ujao.

      Kurudishwa kwa Ibada Safi

      4, 5. Ni nini kilichowapata watu wa Mungu mwaka wa 607 K.W.K., na Yehova aliwaahidi nini?

      4 Jambo moja ambalo Yehova tayari amerudisha sasa ni ibada safi. Ili kufahamu jambo hilo, tuchunguze kifupi historia ya ufalme wa Yuda. Uchunguzi huo wenye kusisimua utatusaidia kuelewa jinsi ambavyo Yehova amekuwa akitumia uwezo wake wa kurudisha mambo katika hali nzuri.—Waroma 15:4.

      5 Hebu wazia jinsi Wayahudi waaminifu walivyohisi mwaka wa 607 K.W.K. wakati jiji la Yerusalemu lilipoharibiwa. Jiji lao walilopenda liliharibiwa, na kuta zake zikabomolewa. Jambo la kusikitisha hata zaidi ni kwamba hekalu tukufu lililojengwa na Solomoni, kitovu pekee cha ibada safi ya Yehova duniani kote, liliharibiwa kabisa. (Zaburi 79:1) Wale walionusurika walipelekwa uhamishoni Babiloni. Waliacha nchi yao ikiwa makao ya wanyama wa mwitu tu. (Yeremia 9:11) Kwa wanadamu, ilionekana ni kana kwamba hakukuwa na tumaini tena. (Zaburi 137:1) Lakini Yehova, aliyekuwa ametabiri hapo kale kuhusu uharibifu huo, aliwaahidi kwamba angewarudisha nchini mwao na kurudisha ibada safi.

      6-8. (a) Manabii Waebrania waliandika tena na tena kuhusu nini, na unabii huo mbalimbali ulitimizwaje kwa mara ya kwanza? (b) Katika nyakati za kisasa, unabii mbalimbali wa kurudishwa umetimizwaje kuhusiana na watu wa Mungu?

      6 Kwa kweli, manabii Waebrania waliandika tena na tena kuhusu kurudishwa huko.b Kupitia manabii hao, Yehova aliahidi kwamba angewarudisha katika nchi yenye rutuba, na kuwalinda dhidi ya maadui na wanyama wakali. Alieleza kuwa nchi yao iliyofanywa upya ingekuwa kama paradiso! (Isaya 65:25; Ezekieli 34:25; 36:35) Zaidi ya yote, ibada safi ingeanzishwa tena, na hekalu lingejengwa upya. (Mika 4:1-5) Unabii huo mbalimbali uliwapa Wayahudi hao waliohamishwa tumaini, na uliwasaidia kuvumilia kwa miaka 70 walipokuwa uhamishoni huko Babiloni.

      7 Hatimaye, wakati wa kurudishwa ulifika. Wayahudi walipoachiliwa huru kutoka Babiloni, walirudi Yerusalemu na kujenga upya hekalu la Yehova. (Ezra 1:1, 2) Maadamu walishikamana na ibada safi, Yehova aliwabariki na kufanya nchi yao kuwa na rutuba na ufanisi. Aliwalinda dhidi ya maadui na wanyama wakali ambao walikuwa wamevamia nchi yao kwa miaka mingi. Walishangilia kama nini kuona Yehova akitumia uwezo wake wa kurudisha mambo katika hali nzuri! Lakini mambo hayo yalikuwa utimizo mdogo wa kwanza wa unabii mbalimbali wa kurudishwa. Utimizo mkubwa ungetukia “katika siku za mwisho,” katika siku zetu, wakati ambapo Mrithi aliyeahidiwa tangu kale wa Mfalme Daudi angetawazwa.—Isaya 2:2-4; 9:6, 7.

      8 Punde tu baada ya Yesu kutawazwa katika Ufalme wa mbinguni mwaka wa 1914, alianza kushughulikia mahitaji ya kiroho ya watu waaminifu wa Mungu duniani. Kama vile mshindi Mwajemi aitwaye Koreshi alivyowaachilia huru mabaki ya Wayahudi kutoka Babiloni mwaka wa 537 K.W.K., Yesu aliweka huru mabaki ya Wayahudi wa kiroho, yaani, wafuasi wake, kutoka kwa uvutano wa Babiloni la kisasa, milki ya ulimwenguni pote ya dini za uwongo. (Waroma 2:29; Ufunuo 18:1-5) Tangu mwaka wa 1919 na kuendelea, ibada safi imerudishwa mahali pafaapo katika maisha ya Wakristo wa kweli. (Malaki 3:1-5) Tangu hapo, watu wa Yehova wamekuwa wakimwabudu katika hekalu la kiroho lililosafishwa, yaani, mpango wa Mungu wa ibada safi. Kwa nini jambo hilo ni muhimu kwetu leo?

      Kurudishwa kwa Ibada Safi Ni Muhimu Sana

      9. Baada ya mitume kufa, makanisa ya Jumuiya ya Wakristo yaliathirije ibada ya Mungu, lakini Yehova amechukua hatua gani wakati wetu?

      9 Fikiria matukio ya kihistoria. Wakristo walioishi katika karne ya kwanza walibarikiwa sana kiroho. Lakini Yesu na mitume walitabiri kwamba ibada ya kweli ingechafuliwa na kutokomea. (Mathayo 13:24-30; Matendo 20:29, 30) Jumuiya ya Wakristo ilitokea baada ya mitume kufa. Makasisi wake walifuata mafundisho na mazoea ya kipagani. Waliwazuia watu wasiwe na uhusiano na Mungu kwa sababu walifundisha fundisho la Utatu lisiloeleweka, na waliwafundisha watu kuungama mbele ya makasisi na kusali kwa Maria na “watakatifu” mbalimbali badala ya kusali kwa Yehova. Sasa, Yehova amechukua hatua gani baada ya watu kuacha ibada safi kwa miaka mingi? Katika ulimwengu wa leo uliojaa mafundisho ya uwongo ya dini na mazoea yake maovu, Yehova amechukua hatua ya kurudisha ibada safi! Si kutilia chumvi kusema kwamba kurudishwa kwa ibada safi ni mojawapo ya matukio muhimu katika nyakati za kisasa.

      10, 11. (a) Paradiso ya kiroho inahusisha mambo gani mawili muhimu, na yanakuhusuje? (b) Yehova amekusanya watu wa aina gani katika paradiso ya kiroho, nao watakuwa na pendeleo la kuona nini?

      10 Basi Wakristo wa kweli leo wanafurahia paradiso ya kiroho. Paradiso hiyo inahusisha nini? Inahusisha hasa mambo mawili muhimu. Jambo la kwanza ni ibada safi ya Mungu wa kweli, Yehova. Ametubariki kwa kutupatia ibada isiyo na upotovu wala uwongo. Ametuandalia chakula cha kiroho. Hilo hutusaidia tujifunze kuhusu Baba yetu wa mbinguni, tumpendeze, na tumkaribie. (Yohana 4:24) Jambo la pili katika paradiso ya kiroho linahusu watu. Kama Isaya alivyotabiri, “katika siku za mwisho,” Yehova amewafundisha waabudu wake njia za amani. Amekomesha vita miongoni mwetu. Licha ya hali yetu ya kutokamilika, yeye hutusaidia kuvaa “utu mpya.” Anabariki jitihada zetu kwa kutupatia roho yake takatifu, ambayo inatokeza matunda bora sana maishani mwetu. (Waefeso 4:22-24; Wagalatia 5:22, 23) Unapotenda kupatana na roho ya Mungu, unakuwa kwelikweli sehemu ya paradiso ya kiroho.

      11 Yehova amekusanya watu anaowapenda katika paradiso hiyo ya kiroho, yaani, watu wanaompenda, wanaopenda amani, na ‘wanaona uhitaji wao wa kiroho.’ (Mathayo 5:3) Watu hao watakuwa na pendeleo la pekee la kuona wanadamu na dunia nzima ikirudishwa katika hali nzuri ajabu.

      “Tazama! Mimi Ninafanya Vitu Vyote Kuwa Vipya”

      12, 13. (a) Kwa nini kutakuwa na utimizo mwingine wa unabii wa kurudisha hali nzuri? (b) Katika Edeni, Yehova alisema kusudi lake ni nini kwa dunia, na kwa nini hilo linatupatia tumaini la wakati ujao?

      12 Yaonekana kwamba unabii mbalimbali wa kurudisha haurejezei tu kurudishwa kwa ibada safi. Kwa mfano, Isaya alitabiri kuhusu wakati ambapo wagonjwa, walemavu, vipofu, na viziwi wataponywa na hata kifo kitamezwa milele. (Isaya 25:8; 35:1-7) Ahadi hizo hazikutimizwa kihalisi katika Israeli la kale. Na ijapokuwa tumeona ahadi hizo zikitimizwa kwa njia ya kiroho nyakati zetu, kuna msingi thabiti wa kuamini kwamba ahadi hizo zitatimizwa kihalisi na kikamili wakati ujao.

      13 Katika Edeni, Yehova alitaja waziwazi kusudi lake kwa dunia: Ilipasa kukaliwa na familia ya wanadamu wenye furaha, afya na umoja. Mwanamume na mwanamke walipaswa kutunza dunia na viumbe wake wote, na kufanya dunia yote iwe paradiso. (Mwanzo 1:28) Leo, hali ni tofauti kabisa. Hata hivyo, tunaweza kuwa na hakika kwamba makusudi ya Yehova hayawezi kuzuiwa kamwe. (Isaya 55:10, 11) Yesu, ambaye ni Mfalme wa Kimesiya aliyeteuliwa na Yehova, atafanya dunia yote kuwa Paradiso.—Luka 23:43.

      14, 15. (a) Yehova ‘atafanyaje vitu vyote viwe vipya’? (b) Maisha yatakuwaje katika Paradiso, na ni jambo gani linalokuvutia zaidi?

      14 Hebu wazia dunia yote ikiwa Paradiso! Yehova anasema hivi kuhusu wakati huo: “Tazama! Mimi ninafanya vitu vyote kuwa vipya.” (Ufunuo 21:5) Fikiria hali itakavyokuwa. Baada ya Yehova kuharibu mfumo huu mwovu wa kale kwa kutumia nguvu zake za kuangamiza, “mbingu mpya na dunia mpya” zitabaki. Hilo lamaanisha kwamba serikali mpya ikiwa mbinguni, itatawala jamii mpya ya kidunia ya wanadamu wanaompenda Yehova na kufanya mapenzi yake. (2 Petro 3:13) Shetani pamoja na mashetani wake, watafungwa ili wasiweze kutenda. (Ufunuo 20:3) Baada ya maelfu ya miaka kupita, kwa mara ya kwanza kabisa wanadamu hawataathiriwa tena na uvutano wake wenye kupotosha, wa chuki, na wenye kuumiza. Hapana shaka kwamba wanadamu watapata faraja isiyo na kifani.

      15 Hatimaye, tutaweza kutunza dunia hii maridadi kama ilivyokusudiwa mwanzoni. Dunia ina uwezo wa kujisafisha yenyewe. Maziwa na mito michafu inaweza kujisafisha yenyewe isipoendelea kuchafuliwa; sehemu zilizoharibiwa na vita zinaweza kuwa nzuri endapo vita vitakoma. Itafurahisha kama nini kufanya kazi kwa kupatana na maumbile ya dunia, na kuifanya iwe bustani maridadi, yaani, Edeni ya duniani pote yenye viumbe na mimea ya kila namna! Badala ya kuangamiza wanyama na mimea mbalimbali, mwanadamu ataishi kwa amani na uumbaji wote. Hata watoto hawataogopa wanyama wa mwitu.—Isaya 9:6, 7; 11:1-9.

      16. Katika Paradiso, watu wote waaminifu watarudishwa katika hali gani?

      16 Tutafurahi pia kurudishiwa afya njema. Baada ya Har–Magedoni, waokokaji wataona maponyo ya kimuujiza ulimwenguni pote. Yesu atatumia nguvu alizopewa na Mungu kuwaponya vipofu, viziwi, walemavu na walio wagonjwa kama alivyofanya alipokuwa duniani. (Mathayo 15:30) Watu wazee watafurahi kuwa tena na nguvu, afya, na juhudi za ujanani. (Ayubu 33:25) Makunyanzi yatatoweka, viungo vitanyooka, na misuli itakuwa na nguvu tena. Wanadamu wote waaminifu wataona madhara ya dhambi na kutokamilika yakididimia hatua kwa hatua, na hatimaye kutokomea. Tutamshukuru Yehova Mungu kama nini kwa sababu ya nguvu zake za kustaajabisha za kufanya mambo yote kuwa mapya! Sasa tukazie fikira jambo moja lenye kuchangamsha litakalotukia wakati huo wenye kusisimua wa kufanya mambo kuwa mapya.

      Kuwafufua Wafu

      17, 18. (a) Kwa nini Yesu aliwashutumu Masadukayo? (b) Ni tukio gani lililomfanya Eliya amwombe Yehova amfufue mfu?

      17 Katika karne ya kwanza W.K., viongozi fulani wa kidini, wanaoitwa Masadukayo, hawakuamini ufufuo. Yesu aliwashutumu hivi: “Mwakosea, kwa sababu hamjui wala Maandiko wala nguvu ya Mungu.” (Mathayo 22:29) Naam, Maandiko yanafunua kwamba Yehova ana nguvu za kufufua. Jinsi gani?

      18 Hebu wazia jambo lililotukia siku za Eliya. Mjane mmoja alikuwa amebeba mwili wa mwanaye pekee. Mvulana huyo alikuwa mfu. Haikosi jambo hilo lilimshtua nabii Eliya, aliyekuwa ameishi katika nyumba ya mjane huyo kwa muda fulani. Mapema, alimwokoa mtoto huyo asife njaa. Yaelekea Eliya alimpenda sana mvulana huyo. Mamaye alihuzunika sana. Mvulana huyo pekee ndiye aliyemfanya amkumbuke mume wake aliyekuwa amekufa. Huenda alitumaini kwamba mwanaye angemtunza akizeeka. Mjane huyo aliyefadhaika alidhani kwamba labda alikuwa akiadhibiwa kwa sababu ya dhambi fulani aliyotenda zamani. Eliya hakuweza kuvumilia msiba huo wenye kusikitisha sana. Alitwaa huyo mfu kwa upole kutoka katika kifua cha mamaye, akampeleka katika chumba chake orofani, kisha akamwomba Yehova Mungu arudishe nafsi au uhai, wa mtoto huyo.—1 Wafalme 17:8-21.

      19, 20. (a) Abrahamu alionyeshaje imani kwamba Yehova anaweza kufufua, na imani hiyo ilitegemea nini? (b) Yehova alimthawabishaje Eliya kwa sababu ya imani yake?

      19 Eliya hakuwa mtu wa kwanza kuamini ufufuo. Miaka mingi mapema, Abrahamu aliamini kwamba Yehova ana uwezo wa kufufua. Na alikuwa na sababu nzuri ya kuamini hivyo. Abrahamu alipokuwa na umri wa miaka 100 na Sara miaka 90, Yehova alirudisha uwezo wao wa kuzaa, na Sara akamzaa mwana kimuujiza. (Mwanzo 17:17; 21:2, 3) Baadaye, kijana huyo alipokuwa mtu mzima, Yehova alimwamuru Abrahamu amtoe kuwa dhabihu. Abrahamu alikuwa na imani, alitambua kwamba Yehova angeweza kumfufua Isaka mwanaye mpendwa. (Waebrania 11:17-19) Yaonekana imani hiyo thabiti ndiyo iliyomfanya Abrahamu, kabla ya kukwea mlimani kumtoa mwanaye, awahakikishie watumishi wake kwamba yeye na Isaka wangerudi pamoja.—Mwanzo 22:5.

      Mjane akimpokea kwa furaha mwana wake aliyefufuliwa na nabii Eliya

      “Tazama, mwanao yu hai”!

      20 Yehova aliingilia na Isaka hakuuawa, hivyo ufufuo haukuhitajiwa wakati huo. Hata hivyo, katika kisa cha Eliya, mwana wa mjane tayari alikuwa amekufa—lakini si kwa muda mrefu. Yehova alimthawabisha nabii huyo mwenye imani kwa kumfufua mwana huyo! Kisha Eliya akamrudisha mvulana huyo kwa mamaye, akanena maneno haya yasiyoweza kusahaulika: “Tazama, mwanao yu hai”!—1 Wafalme 17:22-24.

      21, 22. (a) Ufufuo mbalimbali unaosimuliwa katika Maandiko ulikuwa na kusudi gani? (b) Ni watu wangapi watakaofufuliwa katika Paradiso, na ni nani atakayewafufua?

      21 Hivyo basi, kwa mara ya kwanza kabisa katika Biblia, twaona Yehova akitumia uwezo wake wa kuwafufua wanadamu. Baadaye, Yehova pia aliwapa Elisha, Yesu, Paulo, na Petro uwezo wa kufufua wafu. Bila shaka, wale waliofufuliwa walikufa hatimaye. Hata hivyo, matukio hayo ya Biblia yanatuonyesha mambo mazuri yatakayotukia wakati ujao.

      22 Katika Paradiso, Yesu atakuwa “ufufuo na uhai.” (Yohana 11:25) Atafufua mamilioni ya wafu, na kuwapa fursa ya kuishi milele katika Paradiso duniani. (Yohana 5:28, 29) Hebu wazia jinsi marafiki wapendwa na watu wa jamaa waliotenganishwa na kifo watakavyokumbatiana kwa shangwe kubwa ajabu! Wanadamu wote watamsifu Yehova kwa ajili ya uwezo wake wa kufufua.

      23. Ni tukio gani lililokuwa uthibitisho mkuu zaidi wa uwezo wa Yehova, na hilo linatuhakikishia jinsi gani tumaini letu la wakati ujao?

      23 Yehova ametuhakikishia kabisa kwamba tumaini hilo ni hakika. Yehova alithibitisha uwezo wake kwa njia kuu kupita zote alipomfufua Mwanaye, Yesu, akiwa kiumbe wa roho mwenye uwezo, na kumpa cheo cha pili katika ulimwengu mzima. Mamia ya watu walimwona Yesu aliyefufuliwa. (1 Wakorintho 15:5, 6) Ushahidi huo unatosha kuwasadikisha wale wanaotilia shaka jambo hilo. Yehova ana uwezo wa kufufua.

      24. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atafufua wafu, na sote tunaweza kuthamini tumaini gani?

      24 Si kwamba tu Yehova ana uwezo wa kufufua wafu bali pia ana tamaa ya kufanya hivyo. Mwanamume mwaminifu Yobu alipuliziwa kusema kwamba kwa kweli Yehova ana tamaa ya kuwafufua wafu. (Ayubu 14:15) Je, wewe huvutiwa na Mungu wetu, ambaye anatamani kutumia kwa upendo uwezo wake wa kufufua? Kumbuka kwamba ufufuo ni sehemu moja tu ya kazi kubwa ambayo Yehova atafanya wakati ujao ya kufanya mambo kuwa mapya. Kadiri unavyomkaribia zaidi, endelea kuthamini tumaini la pekee sana la kwamba huenda ukawapo Yehova ‘atakapofanya vitu vyote kuwa vipya.’—Ufunuo 21:5.

      a “Nyakati za kurudishwa kwa mambo yote” zilianza wakati Ufalme wa Kimesiya uliposimamishwa, mrithi wa Mfalme Daudi aliyekuwa mwaminifu alipowekwa kuwa mtawala wa Ufalme huo. Yehova alikuwa amemwahidi Daudi kwamba mrithi wake angetawala milele. (Zaburi 89:35-37) Lakini baada ya Babiloni kuharibu Yerusalemu mnamo mwaka wa 607 K.W.K., kiti cha enzi cha Mungu hakikukaliwa na mwanadamu mwingine yeyote aliye mzao wa Daudi. Yesu, aliyezaliwa duniani akiwa mrithi wa Daudi, akawa Mfalme aliyeahidiwa tangu kale alipotawazwa mbinguni.

      b Kwa mfano, Musa, Isaya, Yeremia, Ezekieli, Hosea, Yoeli, Amosi, Obadia, Mika, na Sefania walikazia jambo hilo.

      Maswali ya Kutafakari

      • 2 Wafalme 5:1-15 Mtu mmoja aliyeonyesha unyenyekevu katika nyakati za Biblia alinufaishwaje na nguvu za Yehova za kuponya?

      • Ayubu 14:12-15 Ayubu alikuwa na uhakika gani, na mistari hiyo inaonyesha nini kuhusu wakati wetu ujao?

      • Zaburi 126:1-6 Wakristo wanaweza kuhisije leo kuhusu kurudishwa kwa ibada safi na fungu lao katika ibada hiyo?

      • Waroma 4:16-25 Kwa nini ni muhimu kuwa na imani katika uwezo wa Yehova wa kurudisha hali nzuri?

  • “Kristo Ni Nguvu ya Mungu”
    Mkaribie Yehova
    • Yesu akitembea juu ya bahari ya Galilaya katika usiku wenye dhoruba kali

      Sura ya 9

      “Kristo Ni Nguvu ya Mungu”

      1-3. (a) Wanafunzi walipatwa na tukio gani lenye kutisha katika Bahari ya Galilaya, na Yesu alifanya nini? (b) Kwa nini inafaa kusema kwamba “Kristo ni nguvu ya Mungu”?

      WANAFUNZI waliogopa sana. Dhoruba ilizuka ghafula walipokuwa wakivuka Bahari ya Galilaya kwa mashua. Hapana shaka kwamba walizoea kuona dhoruba katika bahari hiyo, kwa sababu baadhi yao walikuwa wavuvi hodari sana.a (Mathayo 4:18, 19) Lakini hiyo ilikuwa “dhoruba kubwa ya upepo wenye nguvu nyingi.” Bahari ilichafuka kwa sababu ya dhoruba hiyo. Wanaume hao walijikakamua sana kuongoza mashua, lakini dhoruba ilikuwa kali sana. Mawimbi makubwa yalikuwa ‘yanapiga kwa nguvu ndani ya mashua,’ hata ikaanza kujaa maji. Kujapokuwa na vurugu hiyo, Yesu alikuwa amelala usingizi katika tezi, akiwa amechoka baada ya kuwafundisha watu siku nzima. Huku wakiogopa kufa, wanafunzi walimwamsha na kumsihi hivi: “Bwana, tuokoe, tuko karibu kuangamia!”—Marko 4:35-38; Mathayo 8:23-25.

      2 Yesu hakuogopa. Kwa ujasiri, aliukemea upepo na bahari: “Usu! Nyamaa!” Mara moja, upepo na bahari vikatii—dhoruba ikakoma, mawimbi yakatulia tuli, “kukawa shwari kubwa.” Wanafunzi wakahisi hofu isiyo ya kawaida. Wakanong’onezana: “Ni binadamu wa namna gani huyu?” Kwa kweli, ni mwanadamu gani angeweza kuukemea upepo na bahari kana kwamba anamkemea mtoto mtukutu?—Marko 4:39-41; Mathayo 8:26, 27.

      3 Lakini Yesu hakuwa mwanadamu wa kawaida. Yehova alidhihirisha nguvu zake kupitia Yesu, naye Yesu alizitumia kwa njia za pekee sana. Mtume Paulo aliyepuliziwa alisema kwa kufaa kwamba “Kristo ni nguvu ya Mungu.” (1 Wakorintho 1:24) Mungu anaonyeshaje nguvu zake kupitia Yesu? Na jinsi Yesu anavyotumia nguvu hizo kunaweza kuwa na matokeo gani maishani mwetu?

      Nguvu za Mwana Mzaliwa-Pekee wa Mungu

      4, 5. (a) Yehova alimpa Mwana wake mzaliwa-pekee nguvu na mamlaka ya kufanya nini? (b) Mwana huyo angetumia nini kutimiza makusudi ya uumbaji ya Baba yake?

      4 Fikiria nguvu alizokuwa nazo Yesu kabla hajawa mwanadamu. Yehova alitumia “nguvu zake za milele” alipomwumba Mwana wake mzaliwa-pekee, ambaye alikuja kuitwa Yesu Kristo. (Waroma 1:20; Wakolosai 1:15) Baadaye, Yehova alimpa Mwana huyo mamlaka na nguvu nyingi sana. Alimpa kazi ya kutimiza makusudi Yake ya uumbaji. Biblia yasema hivi kumhusu Mwana huyo: “Vitu vyote vilikuja kuwako kupitia yeye, na bila yeye hata kitu kimoja hakikuja kuwako.”—Yohana 1:3.

      5 Hatuwezi kufahamu kikamili uzito wa kazi hiyo. Hebu wazia nguvu zinazohitajiwa kuumba mamilioni ya malaika wenye uwezo, mabilioni ya makundi ya nyota, dunia na viumbe wote waliomo. Mwana mzaliwa-pekee alifanya kazi hizo kwa kutumia roho takatifu ya Mungu ambayo ni nguvu isiyo na kifani katika ulimwengu mzima. Mwana huyo alifurahia kuwa Stadi wa Kazi, na alitumiwa na Yehova kuumba vitu vingine vyote.—Mithali 8:22-31.

      6. Baada ya kufa na kufufuliwa, Yesu alipewa nguvu na mamlaka gani?

      6 Je, Mwana huyo mzaliwa-pekee angeweza kupewa nguvu na mamlaka zaidi? Yesu alisema hivi baada ya kufa na kufufuliwa: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na juu ya dunia.” (Mathayo 28:18) Naam, Yesu alikuwa amepewa uwezo na haki ya kutawala ulimwengu mzima. Akiwa “Mfalme wa wafalme na Bwana wa mabwana,” amepewa mamlaka ya kufanya “serikali yote na mamlaka yote na nguvu”—zinazoonekana na zile zisizoonekana—ambazo zinampinga Baba yake “kuwa si kitu.” (Ufunuo 19:16; 1 Wakorintho 15:24-26) ‘Vitu vyote vilitiishwa chini ya’ Yesu, ila Yehova Mungu mwenyewe.—Waebrania 2:8; 1 Wakorintho 15:27.

      7. Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu hatatumia vibaya kamwe nguvu ambazo Yehova amempa?

      7 Je, tuwe na wasiwasi kwamba huenda Yesu akatumia nguvu zake vibaya? La hasha! Yesu anampenda sana Baba yake na hawezi kamwe kutenda jambo lolote lisilompendeza. (Yohana 8:29; 14:31) Yesu anajua vizuri kwamba Yehova hatumii vibaya nguvu na uweza wake. Yesu ameona kwamba Yehova hutafuta fursa za ‘kujionyesha mwenye nguvu kwa ajili ya hao, waliokamilika moyo kuelekea kwake.’ (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Bila shaka, Yesu anawapenda wanadamu kama Baba yake, kwa hiyo tunaweza kuwa na hakika kwamba sikuzote Yesu atatumia nguvu zake kwa faida yetu. (Yohana 13:1) Yesu hajapata kamwe kutumia nguvu zake vibaya. Hebu tuone nguvu alizokuwa nazo alipokuwa duniani na jinsi alivyozitumia.

      “Mwenye Nguvu Katika . . . Neno”

      8. Baada ya kutiwa mafuta, Yesu alipewa nguvu za kufanya nini, naye alitumiaje nguvu zake?

      8 Yesu hakufanya miujiza huko Nazareti alipokuwa mvulana. Lakini hali ilibadilika alipobatizwa mwaka wa 29 W.K., akiwa na umri wa miaka 30 hivi. (Luka 3:21-23) Biblia yatuambia hivi: ‘Mungu alimtia mafuta kwa roho takatifu na nguvu, naye akaenda akipita katika nchi akitenda mema na kuwaponya wote wale walioonewa na Ibilisi.’ (Matendo 10:38) Bila shaka, maneno “akitenda mema” yanaonyesha kwamba alitumia nguvu zake ifaavyo. Baada ya kutiwa mafuta, ‘akawa nabii mwenye nguvu katika kazi na neno.’—Luka 24:19.

      9-11. (a) Mara nyingi Yesu alifundisha wapi, na alikabili tatizo gani? (b) Kwa nini umati wa watu ulistaajabia njia ya Yesu ya kufundisha?

      9 Yesu alikuwa mwenye nguvu katika neno jinsi gani? Mara nyingi alifundisha nje—kando ya ziwa, milimani, mitaani, na pia masokoni. (Marko 6:53-56; Luka 5:1-3; 13:26) Wale waliomsikiliza walikuwa huru kuondoka iwapo maneno yake hayakuwapendeza. Wasikilizaji waliothamini mafundisho ya Yesu waliweza tu kuyahifadhi mafundisho hayo katika akili na mioyo yao kwa sababu hawakuwa na vitabu. Basi ilimbidi Yesu afundishe kwa njia yenye kugusa moyo sana, iliyo wazi na yenye kueleweka kwa urahisi. Lakini hilo halikuwa tatizo kwa Yesu. Hebu fikiria Mahubiri yake ya Mlimani.

      10 Asubuhi moja mapema mwaka wa 31 W.K., umati wa watu ulikusanyika mlimani karibu na Bahari ya Galilaya. Baadhi yao walikuwa wametoka Yudea na Yerusalemu, umbali wa kilometa 100 hadi 110. Wengine walikuwa wametoka upande wa kaskazini katika mwambao wa pwani wa Tiro na Sidoni. Wagonjwa wengi walimkaribia Yesu na kumgusa, naye aliwaponya wote. Baada ya kuwaponya wagonjwa wote, alianza kufundisha. (Luka 6:17-19) Alipomaliza kuwafundisha, walistaajabia mambo waliyosikia. Kwa nini?

      11 Miaka mingi baadaye, mmojawapo wa wale waliosikia mahubiri hayo aliandika hivi: “Umati ulishangaa juu ya njia yake ya kufundisha; kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye mamlaka.” (Mathayo 7:28, 29) Waliweza kuhisi kwamba Yesu alizungumza kwa mamlaka. Alimwakilisha Mungu, na mafundisho yake yalitegemea Neno la Mungu. (Yohana 7:16) Yesu aliwafundisha kwa maneno yaliyoeleweka, aliwasadikisha, na kutoa sababu zisizoweza kupingwa. Alikazia mambo muhimu na kufikia mioyo ya wasikilizaji wake. Aliwafundisha jinsi ya kupata furaha, jinsi ya kusali, jinsi ya kutafuta Ufalme wa Mungu, na jinsi ya kuwa na wakati ujao salama. (Mathayo 5:3–7:27) Maneno yake yalichochea mioyo ya wale waliokuwa na njaa ya kweli na uadilifu. Watu hao walikuwa tayari ‘kujikana’ wenyewe na kuacha kila kitu ili wamfuate. (Mathayo 16:24; Luka 5:10, 11) Huo ni uthibitisho ulioje wa nguvu za maneno ya Yesu!

      “Mwenye Nguvu Katika Kazi”

      12, 13. Yesu alikuwa “mwenye nguvu katika kazi” jinsi gani, naye alifanya miujiza gani mbalimbali?

      12 Yesu alikuwa pia “mwenye nguvu katika kazi.” (Luka 24:19) Vitabu vya Injili vinataja zaidi ya miujiza 30 hususa aliyofanya—kwa “nguvu ya Yehova.”b (Luka 5:17) Miujiza ya Yesu ilifaidi maelfu ya watu. Katika miujiza miwili peke yake—alipolisha wanaume 5,000 na baadaye wanaume 4,000, “bila kuhesabu wanawake na watoto wachanga”—yaelekea alilisha jumla ya watu wapatao 20,000!—Mathayo 14:13-21; 15:32-38.

      “Wakamwona Yesu akitembea juu ya bahari”

      13 Yesu alifanya miujiza mbalimbali. Alikuwa na mamlaka ya kudhibiti roho waovu—aliwafukuza kwa urahisi sana. (Luka 9:37-43) Alikuwa na mamlaka juu ya vitu vya asili—aligeuza maji yakawa divai. (Yohana 2:1-11) Wanafunzi wake walishangaa walipomwona akitembea juu ya Bahari ya Galilaya yenye upepo mkali. (Yohana 6:18, 19) Alikuwa na uwezo wa kuponya ulemavu, magonjwa ya kudumu, na magonjwa ya kufisha. (Marko 3:1-5; Yohana 4:46-54) Aliponya kwa njia mbalimbali. Watu kadhaa waliponywa wakiwa mbali, ilhali aliwaponya wengine kwa kwa kuwagusa. (Mathayo 8:2, 3, 5-13) Baadhi ya watu waliponywa mara moja, wengine waliponywa hatua kwa hatua.—Marko 8:22-25; Luka 8:43, 44.

      14. Yesu alionyesha kwamba alikuwa na nguvu za kufufua katika hali gani mbalimbali?

      14 Yesu alikuwa na nguvu za pekee sana za kufufua wafu. Biblia inaonyesha kwamba alifufua wafu watatu. Alimfufua binti mwenye umri wa miaka 12 na kumrudisha kwa wazazi wake, alimfufua mwana-pekee wa mjane, na akamfufua ndugu mpendwa wa dada fulani. (Luka 7:11-15; 8:49-56; Yohana 11:38-44) Yesu aliweza kumfufua mtu katika hali zozote. Alimfufua yule msichana mwenye umri wa miaka 12 muda mfupi baada ya kufa. Alimfufua mwana wa mjane kutoka kwenye machela, siku ileile aliyokufa. Naye Lazaro alifufuliwa na Yesu baada ya kukaa siku nne kaburini.

      Alitumia Nguvu kwa Busara, kwa Huruma na Bila Ubinafsi

      15, 16. Kuna ushuhuda gani kwamba Yesu hakutumia nguvu zake kwa ubinafsi?

      15 Hebu wazia jinsi ambavyo mtawala asiyekamilika angeweza kuwakandamiza watu kama angepewa nguvu za Yesu. Lakini Yesu hakuwa na dhambi. (1 Petro 2:22) Hakujiruhusu kuathiriwa na ubinafsi, tamaa ya makuu, na pupa ambayo huwafanya wanadamu wasiokamilika wenye mamlaka wawakandamize wengine.

      16 Yesu hakutumia nguvu zake kwa ubinafsi ili kujifaidi. Alipohisi njaa, alikataa kugeuza mawe yawe mkate. (Mathayo 4:1-4) Yesu hakuwa na mali nyingi. Hiyo inaonyesha kwamba hakutumia nguvu zake ili kujitajirisha. (Mathayo 8:20) Kuna mambo mengine yanayothibitisha kwamba hakufanya miujiza kwa sababu ya ubinafsi. Alipofanya miujiza, alijidhabihu kwa kadiri fulani. Nguvu zilimtoka alipowaponya wagonjwa. Alihisi nguvu zikimtoka hata alipomponya mtu mmoja tu. (Marko 5:25-34) Na bado aliruhusu umati wa watu umguse, naye akawaponya. (Luka 6:19) Alionyesha roho isiyo ya ubinafsi kama nini!

      17. Yesu alitumiaje nguvu zake kwa busara?

      17 Yesu alitumia nguvu zake kwa busara. Hakufanya miujiza ili kujionyesha tu au kuwastaajabisha watu bila kusudi lolote. (Mathayo 4:5-7) Alikataa kufanya ishara ili kumfurahisha Herode mwenye nia mbaya. (Luka 23:8, 9) Badala ya kutangaza nguvu zake, mara nyingi Yesu aliwaagiza wale aliowaponya wasimwambie mtu yeyote. (Marko 5:43; 7:36) Hakutaka watu wamjue kupitia uvumi wenye kusisimua.—Mathayo 12:15-19.

      18-20. (a) Yesu alionyesha sifa zipi alipotumia nguvu zake? (b) Wahisije kuhusu jinsi ambavyo Yesu alimponya mtu fulani aliyekuwa kiziwi?

      18 Huyo Yesu mwenye nguvu sana, alikuwa tofauti kabisa na watawala ambao wamekuwa wakitumia nguvu zao bila kujali mahitaji na kuteseka kwa wengine. Yesu aliwajali watu. Alisikitika sana alipowaona watu wakiteseka hivi kwamba alichochewa kukomesha mateso yao. (Mathayo 14:14) Alijali hisia zao na mahitaji yao, kwa hiyo, alitumia nguvu zake kwa upendo. Kisa kimoja chenye kugusa moyo kinasimuliwa kwenye Marko 7:31-37.

      19 Pindi hiyo, umati mkubwa ulimfikia Yesu na kumletea wagonjwa wengi, naye akawaponya wote. (Mathayo 15:29, 30) Lakini Yesu alimshughulikia mtu mmoja kwa njia ya pekee sana. Mtu huyo alikuwa kiziwi asiyeweza kuongea. Yaelekea Yesu alitambua wasiwasi au aibu ya mtu huyo. Hivyo kwa kuonyesha kwamba anamjali, Yesu alimpeleka faraghani, mbali na umati. Kisha Yesu akamwonyesha ishara fulani ili kumjulisha jambo ambalo alitaka kufanya. Alitia “vidole vyake ndani ya masikio ya yule mtu na, baada ya kutema mate, akamgusa ulimi wake.”c (Marko 7:33) Halafu, Yesu akatazama juu mbinguni na kutweta kwa sala. Ni kana kwamba alikuwa akimwambia mtu huyo, ‘Muujiza ninaotaka kukufanyia unategemea nguvu za Mungu.’ Hatimaye, Yesu akasema: “Funguka.” (Marko 7:34) Basi, akayaponya masikio yake, kisha mtu huyo akaanza kuongea kama kawaida.

      20 Inagusa moyo kama nini kujua kwamba Yesu alijali hisia za wagonjwa hata ingawa aliwaponya kwa nguvu za Mungu! Je, si jambo lenye kutia moyo kujua kwamba Yehova amemchagua Mtawala mwenye kujali na mwenye huruma jinsi hiyo ili awe mtawala wa Ufalme wake wa Kimesiya?

      Miujiza Ilionyesha Baraka Zitakazokuja

      21, 22. (a) Miujiza ya Yesu ilionyesha nini? (b) Kwa kuwa Yesu anaweza kudhibiti nguvu za asili, tunaweza kutarajia nini wakati wa utawala wa Ufalme wake?

      21 Miujiza ambayo Yesu alifanya duniani ilionyesha kwamba baraka nyingi ajabu zitaletwa na Ufalme wake. Katika ulimwengu mpya wa Mungu, Yesu atafanya tena miujiza—lakini ulimwenguni pote! Hebu chunguza baadhi ya mataraja yenye kufurahisha ya wakati ujao.

      22 Yesu atarudisha uhusiano mzuri kati ya viumbe na mazingira. Kumbuka kwamba alionyesha uwezo wake wa kudhibiti nguvu za asili kwa kutuliza dhoruba kali. Basi, hapana shaka kwamba wakati wa utawala wa Ufalme wa Kristo, wanadamu hawatahitaji kuogopa vimbunga, matetemeko ya ardhi, volkeno, au misiba mingine ya asili. Kwa kuwa Yesu ni Stadi wa Kazi aliyetumiwa na Yehova kuumba dunia na viumbe wote, anaelewa kabisa maumbile ya dunia. Anajua jinsi ya kutumia ifaavyo rasilimali za dunia. Wakati wa utawala wake, dunia nzima itakuwa Paradiso.—Luka 23:43.

      23. Akiwa Mfalme, Yesu atatoshelezaje mahitaji ya wanadamu?

      23 Vipi mahitaji ya wanadamu? Uwezo wa Yesu wa kulisha maelfu ya watu kwa vyakula vichache tu unatuhakikishia kwamba utawala wake utakomesha kabisa njaa. Kwa kweli, njaa itakoma milele kwa sababu kila mtu atakuwa na chakula cha kutosha. (Zaburi 72:16) Uwezo wa Yesu wa kuponya waonyesha kwamba wagonjwa, vipofu, viziwi, na walemavu hawatakuwa wagonjwa tena kamwe. (Isaya 33:24; 35:5, 6) Uwezo wake wa kufufua wafu unatuhakikishia kwamba akiwa Mfalme wa mbinguni ana nguvu za kufufua mamilioni ya watu ambao Baba yake anawakumbuka.—Yohana 5:28, 29.

      24. Tunapotafakari juu ya nguvu za Yesu, tukumbuke nini, na kwa nini?

      24 Tunapotafakari juu ya nguvu za Yesu, tukumbuke kwamba Mwana huyo humwiga kikamili Baba yake. (Yohana 14:9) Kwa hivyo, jinsi Yesu anavyotumia nguvu zake kunatuonyesha waziwazi jinsi Yehova anavyotumia nguvu zake. Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo Yesu alimponya kwa fadhili mtu fulani mwenye ukoma. Yesu alimsikitikia mtu huyo, akamgusa na kusema: “Mimi nataka.” (Marko 1:40-42) Kupitia masimulizi kama hayo, ni kana kwamba Yehova anasema, ‘Hivyo ndivyo ninavyotumia nguvu zangu!’ Je, wewe huchochewi kumsifu Mungu wetu mweza yote na kushukuru kwa sababu anatumia nguvu zake kwa upendo?

      a Bahari ya Galilaya hupata dhoruba za ghafula mara nyingi. Kwa sababu bahari hiyo iko chini sana (meta 200 chini ya usawa wa bahari), eneo hilo lina joto kuliko maeneo ya karibu, kwa hiyo, hali ya hewa hubadilika ghafula. Pepo kali sana huvuma kwenye Bonde la Yordani kutoka kwenye Mlima Hermoni ulio upande wa kaskazini. Dhoruba kali inaweza kutokea ghafula na kuvuruga bahari.

      b Isitoshe, nyakati nyingine Vitabu vya Injili hutaja miujiza mingi kwa ujumla. Kwa mfano, pindi moja “jiji lote” lilikuja kumwona, naye akaponya wagonjwa “wengi.”—Marko 1:32-34.

      c Kutema mate kulikuwa njia au ishara ya kuponya iliyokubaliwa na Wayahudi na Wasio Wayahudi. Na maandishi ya marabi yanataja tiba ya kutumia mate. Huenda Yesu alitema mate ili kumjulisha mtu huyo kwamba alitaka kumponya. Vyovyote iwavyo, Yesu hakuwa akitumia mate yake kama dawa ya asili.

      Maswali ya Kutafakari

      • Isaya 11:1-5 Yesu anatumiaje “roho ya . . . uweza,” na hivyo tunaweza kuwa na uhakika gani kuhusu utawala wake?

      • Marko 2:1-12 Maponyo ya Yesu ya kimuujiza yanaonyesha kwamba amepewa mamlaka ya kufanya nini?

      • Yohana 6:25-27 Ijapokuwa Yesu alitosheleza kimuujiza mahitaji ya kimwili ya watu, kusudi kuu la huduma yake lilikuwa nini?

      • Yohana 12:37-43 Kwa nini baadhi ya watu ambao waliiona miujiza ya Yesu hawakumwamini, na hilo latufunza nini?

  • “Iweni Waigaji wa Mungu” Mnapotumia Uwezo
    Mkaribie Yehova
    • Wahubiri wawili wakimhubiria mwanamke mmoja habari njema nyumbani kwake

      Sura ya 10

      “Iweni Waigaji wa Mungu” Mnapotumia Uwezo

      1. Wanadamu wasiokamilika hutumbukia kwa urahisi katika mtego gani?

      “PALIPO na uwezo hapakosi mtego.” Maneno hayo yaliyosemwa na mtungaji-mashairi wa karne ya 19 yanaonyesha hatari ya kutumia uwezo vibaya. Inasikitisha kwamba wanadamu wasiokamilika hutumbukia kwa urahisi katika mtego huo. Kwa kweli, katika muda wote wa historia ya mwanadamu, ‘mtu mmoja amekuwa na mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.’ (Mhubiri 8:9) Wanadamu wameteseka sana kwa sababu ya kutawaliwa na watawala wasio na upendo.

      2, 3. (a) Ni nini kinachostaajabisha kuhusu jinsi Yehova anavyotumia nguvu zake? (b) Twaweza kuwa na uwezo gani, nasi twapaswa kutumiaje uwezo huo wote?

      2 Hata hivyo, je, haistaajabishi kwamba Yehova Mungu hatumii kamwe vibaya nguvu zake zisizo na mipaka? Kama tulivyoona kwenye sura zilizotangulia, sikuzote yeye hutumia nguvu zake kupatana na makusudi yake ya upendo, iwe ni nguvu za uumbaji, za kuharibu, kulinda, au za kufanya hali upya. Tunapotafakari jinsi anavyotumia nguvu zake, tunachochewa kumkaribia. Na hilo linatutia moyo ‘tumwige Mungu’ tunapotumia uwezo tulio nao. (Waefeso 5:1) Lakini sisi wanadamu duni tuna uwezo gani?

      3 Kumbuka kwamba mwanadamu aliumbwa kwa sura na “mfano wa Mungu.” (Mwanzo 1:26, 27) Hivyo basi, hata sisi tuna uwezo, angalau kwa kadiri fulani. Twaweza kutimiza mambo kwa kufanya kazi; kuwa na mamlaka juu ya wengine; kuwa na uvutano juu ya wengine, hasa wale wanaotupenda; pia tunaweza kuwa na nguvu ya kimwili; au uwezo wa kifedha. Mtunga-zaburi alisema hivi kumhusu Yehova: “Wewe ndiwe asili ya uhai.” (Zaburi 36:9, BHN) Kwa hiyo, kwa njia ya moja kwa moja au isiyo ya moja kwa moja, Mungu ndiye chanzo cha uwezo wowote ufaao ambao huenda tukawa nao. Kwa hiyo, tunataka kutumia uwezo wetu katika njia zinazompendeza. Tutafanyaje hivyo?

      Upendo Ni Muhimu

      4, 5. (a) Tunahitaji sifa gani muhimu ili kutumia uwezo kwa njia ifaayo, na kielelezo cha Mungu kinaonyeshaje hivyo? (b) Upendo utatusaidiaje kutumia uwezo wetu kwa njia ifaayo?

      4 Upendo ni muhimu ili kutumia uwezo kwa njia ifaayo. Je, kielelezo cha Mungu hakionyeshi hivyo? Kumbuka Sura ya 1 iliyozungumzia sifa nne kuu za Mungu, yaani, nguvu, haki, hekima na upendo. Kati ya sifa hizo nne ni ipi iliyo kuu zaidi? Upendo. Andiko la 1 Yohana 4:8 lasema kwamba “Mungu ni upendo.” Naam, upendo ni utu wa Yehova; unamwongoza katika kila jambo analotenda. Kwa hiyo, kila jambo analotenda kwa nguvu zake linachochewa na upendo na mwishowe huwafaidi wale wanaompenda.

      5 Upendo utatusaidia pia kutumia uwezo wetu kwa njia ifaayo. Kwani, Biblia hutuambia kwamba upendo ni “wenye fadhili” na “hautafuti masilahi yao wenyewe.” (1 Wakorintho 13:4, 5) Kwa hiyo, tukiwa na upendo hatutakuwa wakali au wakatili kwa wale walio chini ya mamlaka yetu. Badala yake, tutawatendea wengine kwa staha na kutanguliza mahitaji na hisia zao wala si zetu.—Wafilipi 2:3, 4.

      6, 7. (a) Kumhofu Mungu kwamaanisha nini, na sifa hiyo itatusaidiaje kuepuka kutumia uwezo vibaya? (b) Simulia mfano ambao unaonyesha uhusiano uliopo kati ya kumpenda Mungu na hofu ya kutompendeza.

      6 Upendo unahusiana na sifa nyingine ambayo inaweza kutusaidia kuepuka kutumia uwezo wetu vibaya: kumhofu Mungu. Sifa hii ni muhimu jinsi gani? Andiko la Mithali 16:6 lasema: “Kwa kumcha [“kumhofu,” NW] BWANA watu hujiepusha na maovu.” Bila shaka kutumia uwezo vibaya ni miongoni mwa mambo maovu ambayo tunapaswa kuepuka. Kumhofu Mungu kutatuzuia kuwakandamiza wale walio chini ya mamlaka yetu. Kwa nini? Kwanza, tunajua kwamba tunawajibika kwa Mungu kwa sababu ya jinsi tunavyowatendea wengine. (Nehemia 5:1-7, 15) Lakini kumhofu Mungu kwatia ndani mambo mengi zaidi. Maneno ya lugha ya awali yaliyotafsiriwa “hofu” mara nyingi humaanisha staha nyingi sana na kicho kwa Mungu. Basi, Biblia inaonyesha kwamba hofu inahusiana na kumpenda Mungu. (Kumbukumbu la Torati 10:12, 13) Staha hiyo yenye kicho inatia ndani hofu inayofaa ya kutompendeza Mungu—si kwa sababu tu tunahofu kuadhibiwa bali kwa sababu tunampenda kikweli.

      7 Kwa mfano: Fikiria uhusiano mzuri uliopo kati ya mvulana mdogo na baba yake. Mvulana huyo anajua kwamba baba yake anampenda sana naye humtendea kwa fadhili. Lakini anajua pia mambo ambayo baba yake anamtarajia afanye, na anajua kwamba atatiwa nidhamu akikosa adabu. Mvulana huyo hana hofu isiyofaa kumwelekea baba yake. Badala yake, anampenda sana baba yake. Anapenda kufanya mambo ambayo yatamfurahisha baba yake. Ndivyo ilivyo na kumhofu Mungu. Kwa sababu tunampenda Yehova, Baba yetu wa mbinguni, tunaogopa kutenda jambo lolote ambalo ‘litamhuzunisha moyo.’ (Mwanzo 6:6) Badala yake, tunataka sana kuufurahisha moyo wake. (Mithali 27:11) Ndiyo sababu tunataka kutumia uwezo wetu kwa njia ifaayo. Na tuchunguze jinsi tunavyoweza kufanya hivyo.

      Katika Familia

      8. (a) Waume wana mamlaka gani katika familia, na wanapaswa kuitumiaje? (b) Mume anawezaje kuonyesha kwamba anamheshimu mkewe?

      8 Fikiria kwanza familia. Andiko la Waefeso 5:23 lasema kwamba “mume ni kichwa cha mke wake.” Mume anapaswa kutumiaje mamlaka aliyopewa na Mungu? Biblia inawaambia waume wakae na wake zao ‘kulingana na ujuzi, wakiwapa heshima kama chombo dhaifu zaidi.’ (1 Petro 3:7) Nomino ya Kigiriki inayotafsiriwa “heshima” yamaanisha “thamani, ubora, . . . staha.” Neno hilo hutafsiriwa pia “zawadi” na “-enye bei.” (Matendo 28:10; 1 Petro 2:7) Mume anayemheshimu mkewe hawezi kamwe kumpiga; wala hawezi kumwaibisha au kumtukana, na kumfanya ajihisi hafai. Badala yake, anatambua kwamba yeye ni mwenye thamani sana na anamtendea kwa heshima. Anaonyesha kwa maneno na matendo kwamba anamthamini sana mkewe iwe faraghani au mbele ya watu. (Mithali 31:28) Mume kama huyo hupendwa na kuheshimiwa na mkewe, na la muhimu hata zaidi ni kwamba anapata kibali cha Mungu.

      Mume na Mke wenye furaha wakitembea pamoja

      Waume na wake wanatumia uwezo wao kwa njia inayofaa kwa kuonyeshana upendo na heshima

      9. (a) Wake wana uwezo gani katika familia? (b) Ni nini kinachoweza kumsaidia mke atumie vipawa vyake kumwunga mkono mumewe, na matokeo yatakuwa nini?

      9 Wake pia wana uwezo fulani katika familia. Biblia hutaja wanawake fulani waliomhofu Mungu ambao walichukua hatua ya kuwasaidia waume zao kufanya maamuzi yanayofaa, au kuwasaidia kuepuka kufanya maamuzi yasiyofaa bila kudharau ukichwa wao. (Mwanzo 21:9-12; 27:46–28:2) Mke anaweza kuwa na akili nyingi kumshinda mumewe, au anaweza kuwa na vipawa vingine ambavyo mumewe hana. Hata hivyo, anahitaji “kuwa na staha yenye kina kirefu” kwa mume wake na ‘kujitiisha’ kwake “kama kwa Bwana.” (Waefeso 5:22, 33) Mke aliye na lengo la kumpendeza Mungu atatumia vipawa vyake kumwunga mkono mumewe, badala ya kumdharau au kujaribu kumtawala. “Mwanamke mwenye hekima ” kama huyo hushirikiana kabisa na mumewe kujenga familia. Kwa kufanya hivyo anakuwa na amani pamoja na Mungu.—Mithali 14:1, BHN.

      10. (a) Mungu amewapa wazazi mamlaka gani? (b) Neno “nidhamu” linamaanisha nini, na inapasa kutolewaje? (Ona pia kielezi-chini.)

      10 Wazazi pia wamepewa mamlaka na Mungu. Biblia inashauri hivi: “Akina baba, msiwe mkiwasumbua watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Katika Biblia, neno “nidhamu” linaweza kumaanisha “malezi, mazoezi, mafundisho.” Watoto wanahitaji nidhamu; wanafurahi na kufanikiwa wanapopewa maagizo yaliyo wazi, na wanapowekewa mipaka na vizuizi. Kulingana na Biblia, nidhamu au mafundisho huhusisha upendo. (Mithali 13:24) Kwa hiyo, “fimbo ya adhabu” haipaswi kamwe kuwaumiza watoto kihisia-moyo au kimwili.a (Mithali 22:15; 29:15) Mzazi anayetoa nidhamu kwa ukali bila upendo anatumia vibaya mamlaka yake. Kufanya hivyo kunaweza kumvunja moyo mtoto. (Wakolosai 3:21) Kwa upande mwingine, kutoa nidhamu kwa usawaziko na kwa njia ifaayo kunawathibitishia watoto kwamba wazazi wanawapenda na wanapendezwa na utu wanaositawisha.

      11. Watoto wanawezaje kutumia nguvu zao ifaavyo?

      11 Vipi watoto? Wanawezaje kutumia ifaavyo nguvu zao? Mithali 20:29 yasema kwamba “fahari ya vijana ni nguvu zao.” Kwa kweli, hakuna njia nyingine bora zaidi ya vijana kutumia nguvu na nishati yao isipokuwa kumtumikia ‘Muumba wetu Mtukufu.’ (Mhubiri 12:1, NW) Vijana wanapaswa kukumbuka kwamba matendo yao yanaweza kuathiri hisia za wazazi wao. (Mithali 23:24, 25) Watoto wanapotii na kufuata mwenendo unaofaa, wanafurahisha mioyo ya wazazi wao wanaomhofu Mungu. (Waefeso 6:1) Mwenendo huo ‘unapendeza vema katika Bwana.’—Wakolosai 3:20.

      Kutanikoni

      12, 13. (a) Wazee wanapaswa kuwa na maoni gani kuhusu mamlaka yao kutanikoni? (b) Toa mfano ambao unaonyesha umuhimu wa wazee kuwatendea kondoo kwa fadhili.

      12 Yehova ameweka waangalizi wa kuongoza kutaniko la Kikristo. (Waebrania 13:17) Wanaume hao wenye sifa za kustahili wanapaswa kutumia mamlaka waliyopewa na Mungu kutoa msaada unaohitajiwa na kulisaidia kutaniko likue kiroho. Je, wazee wana haki ya kupiga ubwana juu ya waamini wenzao kwa sababu ya wadhifa wao? La hasha! Wazee wanahitaji kuwa na usawaziko na unyenyekevu wanapotimiza daraka lao kutanikoni. (1 Petro 5:2, 3) Biblia inawaambia hivi waangalizi: ‘Lichungeni kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.’ (Matendo 20:28) Kwa sababu hiyo, wazee wanapaswa kumtendea kila mshiriki wa kutaniko kwa fadhili.

      13 Mfano ufuatao unaonyesha jambo hilo: Rafiki yako mpendwa anakuomba umtunzie mali fulani yenye thamani kubwa. Wajua kwamba mali hiyo ilimgharimu pesa nyingi sana. Je, hutaitunza kwa tahadhari na uangalifu mkubwa mno ili isiharibike? Vivyo hivyo, Mungu amewakabidhi wazee wajibu wa kutunza mali yenye thamani kubwa sana: kutaniko, ambalo washiriki wake wanalinganishwa na kondoo. (Yohana 21:16, 17) Yehova anapenda sana kondoo wake—anawapenda kiasi cha kwamba aliwanunua kwa damu yenye thamani ya Mwana wake mzaliwa-pekee, Yesu Kristo. Yehova aliwanunua kondoo wake kwa bei ya juu sana. Wazee wanyenyekevu hukumbuka jambo hilo na kuwatendea kondoo wa Yehova kwa njia inayofaa.

      “Uwezo wa Ulimi”

      14. Ulimi una uwezo gani?

      14 Biblia inasema kwamba “mauti na uzima huwa katika uwezo wa ulimi.” (Mithali 18:21) Kwa kweli, ulimi unaweza kusababisha madhara makubwa sana. Ni nani kati yetu hajapata kuumizwa moyoni na maneno ya madharau au yaliyonenwa bila kufikiri? Lakini ulimi unaweza pia kujenga. Mithali 12:18 yasema kwamba “ulimi wa mwenye haki ni afya.” Naam, maneno yenye kutia moyo na yenye kujenga yanaweza kufariji na kutuliza moyo kama dawa. Angalia mifano kadhaa.

      15, 16. Tunawezaje kutumia ulimi wetu kuwatia moyo wengine?

      15 Andiko la 1 Wathesalonike 5:14 linasihi hivi: “Semeni kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo.” Naam, hata watumishi waaminifu wa Yehova wanaweza kushuka moyo nyakati nyingine. Tunawezaje kuwasaidia watu hao? Toa pongezi hususa na ya kutoka moyoni ili watambue kwamba wanathaminiwa sana na Yehova. Wasomee maandiko ya Biblia yenye kuimarisha sana yanayoonyesha kwamba Yehova anawapenda na anawajali kikweli wale “waliovunjika moyo” na “waliopondeka roho.” (Zaburi 34:18) Tunapotumia uwezo wa ulimi kuwafariji wengine, tunaonyesha kwamba tunamwiga Mungu wetu mwenye rehema, “ambaye hufariji walioshuka moyo.”—2 Wakorintho 7:6, New American Standard Bible.

      16 Tunaweza pia kutumia uwezo wetu wa ulimi kuwatia moyo wengine wanaohitaji sana kitia-moyo. Je, mwamini mwenzetu amefiwa na mpendwa wake? Tunaweza kumfariji aliyefiwa kwa kuzungumza naye kwa huruma na kumwonyesha kwamba tunamjali na tunamhangaikia. Je, kuna ndugu au dada mzee kwa umri ambaye anahisi kwamba hafai? Tunaweza kuwahakikishia wale walio wazee kwa umri kwamba wanathaminiwa sana kwa kuwaambia maneno yenye kujenga. Je, kuna mtu anayepambana na ugonjwa wa kudumu? Tunaweza kumtia moyo mgonjwa huyo kwa kuzungumza naye kwa fadhili tunapomtembelea au kumpigia simu. Muumba wetu hufurahi kama nini kuona tukitumia uwezo wa ulimi kusema mambo ‘yaliyo mema kwa ajili ya kujenga’!—Waefeso 4:29.

      Kuhubiri habari njema​—ni njia bora ya kutumia uwezo wetu

      17. Tunaweza kutumia ulimi wetu kuwafaidi wengine kwa njia gani bora zaidi, na kwa nini tufanye hivyo?

      17 Njia bora zaidi ya kutumia uwezo wa ulimi ni kuwahubiria wengine habari njema za Ufalme wa Mungu. Mithali 3:27 yasema hivi: “Usiwanyime watu mema yaliyo haki yao, ikiwa katika uwezo wa mkono wako kuyatenda.” Tuna wajibu wa kuwaeleza wengine habari njema zinazookoa uhai. Ni kosa kuwanyima wengine ujumbe huo muhimu sana ambao Yehova ametupatia kwa ukarimu. (1 Wakorintho 9:16, 22) Lakini Yehova anataka tushiriki kwa kadiri gani katika kazi hiyo?

      Kumtumikia Yehova kwa ‘Nguvu Zetu Zote’

      18. Yehova anataka tufanye nini?

      18 Upendo wetu kwa Yehova hutuchochea kushiriki kikamili zaidi katika huduma ya Kikristo. Yehova anataka tushiriki kwa kadiri gani katika huduma hiyo? Anataka tufanye yote tuwezayo haidhuru hali yetu maishani: “Lolote mnalofanya, lifanyeni kwa nafsi yote kama kwa Yehova, na si kwa wanadamu.” (Wakolosai 3:23) Yesu alisema kwamba amri kuu kupita zote ni hii: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Ndiyo, Yehova anataka kila mmoja wetu ampende na kumtumikia kwa nafsi yote.

      19, 20. (a) Kwa kuwa nafsi inatia ndani moyo, akili, na nguvu, kwa nini sehemu hizo zinatajwa kwenye Marko 12:30? (b) Yamaanisha nini kumtumikia Yehova kwa nafsi yote?

      19 Yamaanisha nini kumtumikia Mungu kwa nafsi yote? Nafsi ni mtu mwenyewe, akiwa na uwezo wake wote wa kimwili na kiakili. Kwa kuwa nafsi inatia ndani moyo, akili, na nguvu, kwa nini sehemu hizo zinatajwa kwenye Marko 12:30? Fikiria mfano mmoja. Katika nyakati za Biblia, mtu angeweza kujiuza (nafsi yake) na kuwa mtumwa. Lakini, huenda mtumwa asimtumikie bwana wake kwa moyo wake wote; huenda asitumie nguvu zake zote au uwezo wake wote wa akili kutunza masilahi ya bwana wake. (Wakolosai 3:22) Kwa hiyo, ni wazi kwamba Yesu alitaja moyo, akili, na nguvu ili kukazia kwamba tunapaswa kumtumikia Mungu kwa uwezo wetu wote. Kumtumikia Mungu kwa nafsi yote kwamaanisha kujitoa wenyewe, kutumia nguvu na nishati yetu yote katika utumishi wake.

      20 Je, kutumikia kwa nafsi yote kwamaanisha kwamba ni lazima sote tutumie kiasi kilekile cha wakati na nishati katika huduma? Hilo haliwezekani, kwa kuwa sote tuna hali na uwezo mbalimbali. Kwa mfano, kijana mwenye nguvu na afya njema anaweza kuhubiri kwa saa nyingi zaidi kuliko mzee aliye dhaifu. Mseja asiye na wajibu wa familia anaweza kutimiza mengi zaidi kuliko mtu mwenye familia. Tunapaswa kushukuru sana ikiwa hali na nguvu zetu zinaturuhusu kufanya mengi katika huduma. Bila shaka, hatutaki kamwe kuwachambua-chambua wengine, wala kulinganisha utumishi wetu na wao. (Waroma 14:10-12) Badala yake, tunataka kutumia uwezo wetu kuwatia moyo wengine.

      21. Ni njia ipi iliyo bora kabisa na muhimu zaidi ya kutumia uwezo wetu?

      21 Yehova ametuwekea kielelezo bora kabisa cha kutumia uwezo kwa njia ifaayo. Tunataka kumwiga yeye kadiri tuwezavyo tukiwa wanadamu wasiokamilika. Tunaweza kutumia uwezo wetu kwa njia ifaayo kwa kuwatendea kwa heshima wale walio chini ya mamlaka yetu. Zaidi ya hayo, tunataka kutimiza kwa nafsi yote kazi ya kuhubiri inayookoa uhai ambayo Yehova ametukabidhi. (Waroma 10:13, 14) Kumbuka kwamba Yehova anafurahi unapomtolea yaliyo bora kabisa kulingana na uwezo wako. Je, huchochewi na moyo kutaka kumtumikia Mungu huyo mwenye kujali na mwenye upendo kulingana na uwezo wako? Hiyo ndiyo njia bora kabisa au muhimu zaidi ya kutumia uwezo wetu.

      a Katika nyakati za Biblia, neno la Kiebrania linalotafsiriwa “fimbo” lilimaanisha kijiti au gongo kama lile lililotumiwa na mchungaji kuwaongoza kondoo. (Zaburi 23:4) Vivyo hivyo, “fimbo” ya mamlaka ya wazazi inaonyesha mwongozo wa upendo, wala si adhabu kali au ya kikatili.

      Maswali ya Kutafakari

      • Mithali 3:9, 10 Tuna “mali” gani, na tunawezaje kuzitumia kumheshimu Yehova?

      • Mhubiri 9:5-10 Kwa nini unapaswa kutumia uwezo wako sasa kwa njia ambayo itampendeza Mungu?

      • Matendo 8:9-24 Uwezo ulitumiwaje vibaya katika simulizi hilo, na tunawezaje kuepuka kufanya kosa kama hilo?

      • Matendo 20:29-38 Wale walio na madaraka kutanikoni wanajifunza nini kutokana na kielelezo cha Paulo?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki