-
‘Lo! Kina cha Hekima ya Mungu!’Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 17
‘Lo! Kina cha Hekima ya Mungu!’
1, 2. Kusudi la Yehova kwa siku ya saba lilikuwa nini, na hekima Yake ilijaribiwaje mwanzoni mwa siku hiyo?
WAMEHARIBIKA! Wanadamu, upeo wa fahari ya siku ya sita ya uumbaji, walitumbukia ghafula katika hali mbaya yenye kusikitisha. Yehova alikuwa ametangaza kwamba “kila kitu alichokifanya,” kutia ndani mwanadamu, “ni chema sana.” (Mwanzo 1:31) Lakini mwanzoni mwa siku ya saba, Adamu na Hawa waliamua kumfuata Shetani katika uasi. Wakatumbukia katika dhambi, kutokamilika, na kifo.
2 Huenda ilionekana kwamba kusudi la Yehova kwa siku ya saba lilikuwa limeenda mrama kabisa. Siku hiyo, kama siku sita zilizotangulia, ingekuwa na urefu wa maelfu ya miaka. Yehova alikuwa ameitangaza kuwa takatifu. Hatimaye katika siku hiyo, dunia yote ingekuwa paradiso iliyojaa wanadamu wakamilifu. (Mwanzo 1:28; 2:3) Lakini kusudi hilo lingetimizwaje baada ya ule uasi ulioleta msiba? Mungu angechukua hatua gani? Wakati huo, hekima ya Yehova ilijaribiwa kwa njia isiyo na kifani—labda hilo ndilo lililokuwa jaribu kuu zaidi.
3, 4. (a) Kwa nini hatua ambayo Yehova alichukua baada ya uasi katika Edeni inaonyesha hekima yake yenye kutia kicho? (b) Kwa unyenyekevu, tunapaswa kukumbuka jambo gani hakika tunapojifunza juu ya hekima ya Yehova?
3 Yehova alichukua hatua mara moja. Aliwahukumu hao waasi katika Edeni, na wakati huohuo, akatangaza tumaini zuri la wakati ujao: alikusudia kukomesha taabu ambazo walikuwa wameanzisha tu. (Mwanzo 3:15) Kusudi la Yehova la muda mrefu lilianzia Edeni na kuendelea kwa maelfu ya miaka ambayo mwanadamu amekuwapo, na litaendelea hadi wakati ujao. Ni kusudi rahisi sana lakini lenye mambo mengi muhimu hivi kwamba msomaji wa Biblia anaweza kufurahia kujifunza kusudi hilo na kulitafakari maisha yake yote. Isitoshe, hapana shaka yoyote kwamba kusudi la Yehova litafanikiwa. Litakomesha kabisa uovu, dhambi, na kifo. Mungu anakusudia kuwafanya wanadamu waaminifu wawe wakamilifu. Mambo hayo yote yatatukia kabla ya siku ya saba kwisha. Yehova atakuwa ametimiza kusudi lake kuhusu dunia na wanadamu kwa wakati barabara licha ya vipingamizi vyote!
4 Hekima ya aina hiyo inatutia kicho, sivyo? Mtume Paulo alichochewa kuandika hivi: ‘Lo! kina cha hekima ya Mungu!’ (Waroma 11:33) Tunapojifunza wonyesho mbalimbali wa sifa hii ya Mungu, na tukumbuke kwa unyenyekevu jambo moja hakika—kwamba hatuwezi kamwe kufahamu kikamili hekima ya Yehova yenye kina sana. (Ayubu 26:14) Kwanza, hebu tufafanue sifa hii yenye kutia kicho.
Hekima ya Mungu Ni Nini?
5, 6. Kuna uhusiano gani kati ya ujuzi na hekima, na ujuzi wa Yehova ni mwingi kadiri gani?
5 Hekima si sawa na ujuzi. Kompyuta zinaweza kuhifadhi ujuzi mwingi sana, lakini hakuna mtu anayeweza kusema kwamba mashine hizo ni zenye hekima. Hata hivyo, ujuzi na hekima zinahusiana. (Mithali 10:14) Kwa mfano, kama ungehitaji shauri la hekima ili kutibu ugonjwa hatari, je, ungemwomba msaada mtu asiye na ujuzi wowote au mwenye ujuzi wa kijuu-juu tu wa tiba? La hasha! Kwa hiyo, ujuzi sahihi ni muhimu ili kuwa na hekima ya kweli.
6 Yehova ana ujuzi usio na kikomo. Akiwa “Mfalme wa umilele,” yeye peke yake ndiye ambaye ameishi milele. (Ufunuo 15:3) Na amejua mambo yote yaliyotukia kwa miaka hiyo yote. Biblia inasema hivi: “Hakuna kiumbe kisichokuwa dhahiri machoni pake, bali vitu vyote viko uchi na vikiwa vimefunuliwa wazi machoni pake ambaye kwake sisi tuna kutoa hesabu.” (Waebrania 4:13; Mithali 15:3) Akiwa Muumba, Yehova anajua kabisa vitu alivyoumba, naye ameona utendaji wote wa wanadamu tangu mwanzo. Yeye huchunguza moyo wa kila mwanadamu, na anaona kila jambo. (1 Mambo ya Nyakati 28:9) Anafurahi anapoona tukifanya maamuzi ya hekima maishani kwa sababu alituumba tukiwa na hiari. Akiwa “Msikiaji wa sala,” yeye husikiliza sala nyingi sana kwa wakati mmoja! (Zaburi 65:2, NW) Na bila shaka Yehova ana kumbukumbu kamilifu.
7, 8. Yehova anaonyeshaje ufahamu, utambuzi, na hekima?
7 Mbali na ujuzi, Yehova ana uwezo mwingine. Anaona jinsi mambo mbalimbali yanavyohusiana, na anatambua matokeo kamili ya mambo yote. Anachanganua mambo na kufanya maamuzi, anatofautisha mema na mabaya, mambo muhimu na yasiyo muhimu. Zaidi ya hayo, hachunguzi mambo kijuujuu tu bali anachunguza ndani ya moyo. (1 Samweli 16:7) Kwa hiyo, Yehova ana ufahamu na utambuzi, sifa ambazo ni bora zaidi ya ujuzi. Lakini hekima ni bora zaidi ya sifa hizo zote.
8 Hekima ni kutumia ujuzi, utambuzi, na ufahamu ili kutekeleza jambo fulani. Kwa kweli, baadhi ya maneno ya awali ya Biblia yaliyotafsiriwa “hekima” yanamaanisha kihalisi “kufanya kazi kwa matokeo” au “hekima inayofanya kazi kwa matokeo.” Kwa hiyo, hekima ya Yehova si ya kuwazia tu, bali inafanya kazi na ina matokeo. Sikuzote Yehova hufanya maamuzi bora kabisa kwa kutumia hekima na ufahamu wake usio na mipaka, na anatekeleza maamuzi hayo kwa njia bora kabisa. Hiyo ni hekima ya kweli! Yehova anaonyesha ukweli wa maneno haya ya Yesu: “Hekima huthibitishwa kuwa yenye uadilifu kwa kazi yayo.” (Mathayo 11:19) Kazi za Yehova ulimwenguni pote huthibitisha pasina shaka yoyote kwamba ana hekima.
Uthibitisho wa Hekima ya Mungu
9, 10. (a) Yehova ana hekima ya aina gani, naye ameionyeshaje? (b) Chembe huthibitishaje hekima ya Yehova?
9 Je, umewahi kustaajabia ustadi wa fundi anayetengeneza vifaa maridadi vinavyofanya kazi vizuri? Hekima hiyo inavutia sana. (Kutoka 31:1-3) Yehova mwenyewe ndiye chanzo hasa cha hekima hiyo. Mfalme Daudi alisema hivi kumhusu Yehova: “Nitakushukuru kwa kuwa nimeumbwa kwa jinsi ya ajabu ya kutisha. Matendo yako ni ya ajabu, na nafsi yangu yajua sana.” (Zaburi 139:14) Kwa kweli, kadiri tunavyojifunza kuhusu mwili wa mwanadamu, ndivyo tunavyozidi kutiwa kicho na hekima ya Yehova.
10 Kwa mfano: Uhai wako ulianza kwa chembe moja—mbegu ya mama yako iliungana na mbegu ya baba yako. Baada ya muda, chembe hiyo ilianza kugawanyika. Mwishowe mwili wako ukawa na chembe ndogo sana zipatazo trilioni 100. Chembe 10,000 hivi zenye ukubwa wa wastani zinaweza kutoshea kwenye kichwa kidogo sana cha pini. Lakini, kila chembe ina umbo tata sana. Chembe moja ni tata sana kushinda kiwanda au mashine yoyote iliyotengenezwa na mwanadamu. Wanasayansi wanasema kwamba chembe moja ni kama jiji lililozingirwa na ukuta—lenye malango yanayolindwa, lenye mfumo wa usafiri, mfumo wa mawasiliano, mitambo ya nguvu, viwanda, mifumo ya kuondoa na kusafisha maji machafu, walinzi, na hata kuna aina fulani ya makao makuu ya serikali katika kiini chake. Isitoshe, chembe inaweza kutengeneza chembe nyingine pacha kwa saa chache tu!
11, 12. (a) Ni nini kinachofanya chembe za kiini-tete kinachokua zigawanyike, na hilo linapatanaje na Zaburi 139:16? (b) Ubongo wa mwanadamu unaonyeshaje kwamba ‘tumeumbwa kwa jinsi ya ajabu’?
11 Bila shaka chembe zote hazifanani. Chembe za kiini-tete zinapoendelea kugawanyika, chembe mpya zinafanya kazi mbalimbali. Baadhi yake zitakuwa chembe za neva; nyingine zitakuwa chembe za mifupa, misuli, damu, au za macho. Utaratibu huo wa kugawanyika kwa chembe umehifadhiwa kiasili katika “maktaba” yenye ramani za chembe za urithi, DNA. Inastaajabisha kwamba Daudi aliongozwa kumwambia Yehova hivi: “Wewe uliniona hata kabla sijazaliwa, uliandika kila kitu kitabuni mwako.”—Zaburi 139:16, BHN.
12 Viungo fulani vya mwili ni tata kupindukia. Kwa mfano, fikiria ubongo wa mwanadamu. Baadhi ya watu wamesema kwamba ubongo ndicho kitu tata zaidi katika ulimwengu wote. Una chembe za neva zipatazo bilioni 100—idadi hiyo inakaribia idadi ya nyota katika kundi letu la nyota. Kila moja ya chembe hizo inaungana na maelfu ya chembe nyingine. Wanasayansi wanasema kwamba ubongo wa mwanadamu unaweza kuhifadhi habari zilizo katika maktaba zote ulimwenguni na kwamba uwezo wake haupimiki. Licha ya kuchunguza kwa miaka mingi sana ubongo ‘ulioumbwa kwa jinsi ya ajabu,’ wanasayansi wanakubali kwamba huenda wasifaulu kamwe kufahamu kikamili jinsi unavyofanya kazi.
13, 14. (a) Chungu na viumbe wengine wanaonyeshaje kwamba wana “akili nyingi sana,” na hilo linatufundisha nini kumhusu Muumba? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba vitu vilivyoumbwa kama vile utando wa buibui vimefanywa “kwa hekima”?
13 Lakini wanadamu ni mojawapo tu ya mambo yanayoonyesha hekima ya Yehova ya uumbaji. Zaburi 104:24 yasema hivi: “Ee, BWANA, jinsi yalivyo mengi matendo yako! Kwa hekima umevifanya vyote pia. Dunia imejaa mali zako.” Kila kiumbe kinadhihirisha hekima ya Yehova. Kwa mfano, chungu ana “akili nyingi sana.” (Mithali 30:24) Kwa kweli, makundi ya chungu yana utaratibu wa hali ya juu sana. Makundi fulani ya chungu hutunza, hufuga, na kupata chakula kutoka kwa wadudu fulani kana kwamba ni mifugo. Chungu wengine ni kama wakulima, wanapanda “mimea” ya kuvu. Viumbe wengine wengi wanafanya mambo yenye kustaajabisha kwa kutumia hekima ya kisilika. Nzi wa kawaida huruka kwa njia za kustaajabisha sana ambazo ndege bora ya kisasa iliyobuniwa na mwanadamu haiwezi. Ndege wanaohama huongozwa na nyota, nguvu za sumaku za dunia, au aina fulani ya ramani iliyo akilini mwao. Wanabiolojia hujifunza kwa miaka mingi tabia tata za kisilika za viumbe hao. Mungu aliyeumba viumbe hao ana hekima iliyoje!
14 Wanasayansi wamejifunza mengi kutokana na hekima ya Yehova ya uumbaji. Hata kuna elimu fulani ya uhandisi inayojaribu kuiga ubuni wa maumbile inayoitwa biomimetics. Kwa mfano, labda umewahi kustaajabia umaridadi wa utando wa buibui. Lakini mhandisi anaona kwamba utando huo umebuniwa kwa njia ya pekee sana. Tando fulani nyembamba ni ngumu kuliko chuma, ni ngumu kushinda nyuzi za mavazi yasiyopenywa na risasi. Ni ngumu kadiri gani? Hebu wazia utando wa buibui uliorefushwa kufikia ukubwa wa wavu unaovutwa na mashua ya uvuvi. Utando wa aina hiyo ungeweza kusimamisha ndege ya abiria inayosafiri kwa kasi angani! Naam, Yehova amefanya vitu hivyo vyote “kwa hekima.”
Ni nani aliyeumba viumbe hawa ambao wana “akili nyingi sana”?
Hekima ya Vitu Visivyo Duniani
15, 16. (a) Nyota zinatoa uthibitisho gani kuhusu hekima ya Yehova? (b) Wadhifa wa Yehova akiwa Amiri Mkuu wa malaika wengi sana unaonyesha nini kuhusu hekima yake akiwa Msimamizi?
15 Hekima ya Yehova inaonekana wazi katika kazi zake ulimwenguni pote. Nyota ambazo tulizungumzia kwa undani katika Sura ya 5, hazijatapakaa kiholela-holela angani. Yehova amepanga nyota kwa njia maridadi sana katika magalaksi, kwa kutumia hekima yake ya “sheria za angani.” Magalaksi hayo yamepangwa katika makundi makubwa, ambayo huungana na kufanyiza makundi mengine makubwa hata zaidi. (Ayubu 38:33, The New Jerusalem Bible) Si ajabu Yehova anasema kwamba nyota zilizo mbinguni ni kama “jeshi”! (Isaya 40:26) Hata hivyo, kuna jeshi jingine ambalo linaonyesha wazi zaidi hekima ya Yehova.
16 Kama tulivyoona katika Sura ya 4, Mungu anaitwa “BWANA wa majeshi” kwa sababu ya wadhifa wake akiwa Amiri Mkuu wa jeshi la mamia ya mamilioni ya viumbe wa roho. Hilo lathibitisha nguvu za Yehova. Hata hivyo, hekima yake inahusikaje? Fikiria hili: Yehova na Yesu wanafanya kazi daima. (Yohana 5:17) Basi, ni jambo la kiakili kwamba hata malaika wanaomtumikia Mwenye Enzi Kuu wanafanya kazi daima. Na kumbuka kwamba malaika wana wadhifa wa juu kuliko mwanadamu, wana akili na nguvu nyingi sana. (Waebrania 1:7; 2:7) Lakini Yehova amewapa malaika hao wote kazi ya kutosha. Kwa furaha na uradhi, wamekuwa ‘wakitenda neno lake’ na ‘kufanya mapenzi yake,’ kwa mabilioni ya miaka. (Zaburi 103:20, 21) Msimamizi huyo ana hekima yenye kustaajabisha sana!
Yehova Ndiye “Mwenye Hekima Peke Yake”
17, 18. Kwa nini Biblia inasema kwamba Yehova ndiye “mwenye hekima peke yake,” na kwa nini hekima yake inapaswa kututia kicho?
17 Tukizingatia ushuhuda huo wote, haishangazi kwamba Biblia hutukuza hekima ya Yehova. Kwa mfano, inasema kwamba Yehova ndiye “mwenye hekima peke yake.” (Waroma 16:27) Ni Yehova peke yake aliye na hekima kamili. Ndiye chanzo cha hekima yote ya kweli. (Mithali 2:6) Ndiyo sababu Yesu, ajapokuwa na hekima nyingi kushinda viumbe wote wa Yehova, hakutegemea hekima yake mwenyewe bali alisema yale aliyoagizwa na Baba yake.—Yohana 12:48-50.
18 Angalia jinsi mtume Paulo alivyofafanua hekima ya pekee ya Yehova: “Lo! kina cha utajiri wa Mungu na hekima na ujuzi! Jinsi hukumu zake zisivyotafutikana na njia zake zapita uwezo wa kufuatilia!” (Waroma 11:33) Neno la mshangao, “Lo!” ambalo Paulo alitaja mwanzoni mwa mstari huo, lilionyesha hisia yenye nguvu—kicho cha hali ya juu sana. Neno la Kigiriki ambalo alitumia kurejezea “kina” linahusiana sana na neno “shimo lenye kina kirefu.” Kwa hiyo, maneno yake yanatokeza picha dhahiri sana akilini. Tunapotafakari hekima ya Yehova, ni kana kwamba tunatazama katika shimo kubwa sana lisilo na mwisho, shimo lenye kina kirefu sana hivi kwamba hatuwezi kamwe kufahamu ukubwa wake, sembuse kuweka mipaka au kuchora ramani yake kwa usahihi. (Zaburi 92:5) Wazo hilo linatunyenyekeza, sivyo?
19, 20. (a) Kwa nini tai ni mfano ufaao wa hekima ya Mungu? (b) Yehova ameonyeshaje kwamba ana uwezo wa kuona matukio ya wakati ujao!
19 Yehova ni “mwenye hekima peke yake” kwa njia nyingine: Ni yeye tu anayeweza kuona matukio ya wakati ujao. Kumbuka kwamba Yehova hutumia tai mwenye uwezo wa kuona mbali kuwa mfano wa hekima yake. Tai mkubwa anaweza kuwa na uzito wa kilogramu tano tu, lakini macho yake ni makubwa kuliko macho ya mtu mzima. Tai ana uwezo bora sana wa kuona. Ndege huyo anaweza kuona mnyama mdogo sana kutoka umbali wa mamia ya meta angani, au hata mamia ya kilometa! Pindi moja, Yehova alisema hivi kumhusu tai: ‘Macho yake huangalia toka mbali.’ (Ayubu 39:29) Vivyo hivyo, Yehova anaweza kuona ‘mbali’ sana. Anaweza kuona matukio ya wakati ujao!
20 Biblia ina mambo chungu nzima yanayothibitisha jambo hilo. Ina mamia ya unabii, au mambo yaliyoandikwa kabla hayajatukia. Biblia ilitabiri matokeo ya vita, kutokea na kuanguka kwa serikali kuu za ulimwengu, na hata mbinu za kivita ambazo zingetumiwa na maamiri wa jeshi. Nyakati nyingine ilitabiri matukio hayo mamia ya miaka kabla hayajatukia.—Isaya 44:25–45:4; Danieli 8:2-8, 20-22.
21, 22. (a) Kwa nini haifai kusema kwamba Yehova anajua maamuzi ambayo utafanya maishani? Toa mfano. (b) Tunajuaje kwamba Yehova hatumii hekima yake bila kujali hisia za watu?
21 Lakini je, hilo lamaanisha kwamba tayari Mungu anajua maamuzi ambayo utafanya maishani? Baadhi ya watu ambao wanafundisha kwamba maisha yetu yameamuliwa kimbele husisitiza hivyo. Hata hivyo, imani hiyo kwa kweli inadharau hekima ya Yehova, kwa kuwa inamaanisha kwamba hawezi kudhibiti uwezo wake wa kujua matukio ya wakati ujao. Kwa mfano: Kama ungekuwa mwimbaji mwenye sauti tamu sana, je, ungeimba tu kila wakati? Hilo ni wazo la kipumbavu! Vivyo hivyo, Yehova ana uwezo wa kujua matukio ya wakati ujao, lakini hatumii uwezo huo kila wakati. Akifanya hivyo huenda akaingilia uhuru wetu wa kuchagua. Uhuru huo ni zawadi yenye thamani ambayo Yehova hawezi kutunyima kamwe.—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.
22 Imani ya kwamba maisha yameamuliwa kimbele inasikitisha hata zaidi kwa sababu inadokeza kuwa hekima ya Yehova haijali hisia za watu, haiambatani na upendo, hisia-mwenzi, au huruma. Lakini hilo si kweli hata kidogo! Biblia inafundisha kwamba Yehova ni “mwenye hekima moyoni.” (Ayubu 9:4) Si kwamba ana moyo halisi, lakini mara nyingi Biblia hutumia neno hilo kumaanisha utu wa ndani kabisa, kutia ndani nia ya mtu na hisia kama vile upendo. Kwa hiyo, hekima ya Yehova, kama sifa zake nyingine, inaongozwa na upendo.—1 Yohana 4:8.
23. Hekima ya Yehova iliyo bora sana inapaswa kutuchochea kufanya nini?
23 Bila shaka, hekima ya Yehova inaweza kutumainika kabisa. Ni bora kuliko hekima yetu ndiposa Neno la Mungu linatuhimiza hivi kwa upendo: “Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.” (Mithali 3:5, 6) Na tuchunguze kwa undani hekima ya Yehova ili tuweze kumkaribia zaidi Mungu wetu mwenye hekima kamili.
-
-
Hekima ya “Neno la Mungu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 18
Hekima ya “Neno la Mungu”
1, 2. Yehova ametuandikia “barua” gani, na kwa nini?
JE, UNAKUMBUKA mara ya mwisho ulipopokea barua kutoka kwa mpendwa wako anayeishi mbali sana? Kupokea barua yenye kugusa moyo kutoka kwa mtu tunayempenda ni mojawapo ya mambo yanayotufurahisha sana. Tunafurahi sana anapotujulisha hali yake, maisha yake, na mipango yake. Tunakuwa na uhusiano wa karibu na wapendwa wetu tunapowasiliana nao, hata kama wanaishi mbali.
2 Basi, hakuna jambo jingine lolote linaloweza kutufurahisha sana kama kupokea ujumbe ulioandikwa na Mungu tunayempenda. Tunaweza kusema kwamba Yehova ametuandikia “barua,” yaani, Neno lake, Biblia. Katika Biblia, anatueleza yeye ni nani, amefanya nini, anakusudia kufanya nini, na mambo mengine mengi. Yehova ametupatia Neno lake kwa sababu anataka tumkaribie. Mungu wetu mwenye hekima kamili alichagua njia bora ya kuwasiliana nasi. Biblia imeandikwa kwa njia inayoonyesha hekima isiyo na kifani, na ujumbe wake unaonyesha hekima hiyo pia.
Kwa Nini Aliandika Neno Lake?
3. Yehova alimpa Musa Sheria kwa njia gani?
3 Huenda watu fulani wakauliza, ‘Kwa nini Yehova hakuwasiliana na wanadamu kwa njia nyingine yenye kutokeza zaidi kama vile sauti kutoka mbinguni?’ Kwa kweli, nyakati nyingine Yehova aliongea kutoka mbinguni kupitia malaika. Kwa mfano, alifanya hivyo alipowapa Waisraeli Sheria. (Wagalatia 3:19) Sauti iliyotoka mbinguni ilikuwa yenye kutia kicho sana hivi kwamba Waisraeli walioshikwa na woga walimwomba Yehova asiwasiliane nao kwa njia hiyo bali awasiliane nao kupitia Musa. (Kutoka 20:18-20) Kwa hiyo, Musa alipewa Sheria yenye amri zipatazo 600, kwa njia ya mdomo, neno kwa neno.
4. Eleza kwa nini kupitisha sheria za Mungu kwa njia ya mdomo hakungetegemeka.
4 Vipi kama Sheria haingaliandikwa? Je, Musa angaliweza kukumbuka vizuri kila neno la Sheria hiyo yenye mambo mengi, kisha aiwasilishe kwa taifa hilo bila kukosea? Vipi watu wa vizazi vijavyo? Je, wangehitaji kutegemea tu yale waliyoambiwa? Kupitisha sheria za Mungu kwa njia ya mdomo hakungetegemeka. Wazia jambo ambalo linaweza kutukia iwapo utamwambia mtu mmoja hadithi fulani kisha ipitishwe kutoka kwa mtu mmoja hadi mwingine kwenye mlolongo wa watu wengi. Yaelekea kwamba hadithi ambayo itamfikia mtu wa mwisho katika mlolongo huo itakuwa imebadilika kabisa. Sheria ya Mungu haikukabili hatari hiyo.
5, 6. Yehova alimwagiza Musa afanye nini kuhusiana na maneno Yake, na kwa nini tunafaidika kuwa na Neno la Yehova lililoandikwa?
5 Kwa hekima Yehova aliamua maneno yake yaandikwe. Alimwagiza Musa hivi: “Andika maneno haya; kwa kuwa mimi nimefanya agano nawe, na pamoja na Israeli, kwa mujibu wa maneno haya.” (Kutoka 34:27) Kwa hiyo, Biblia ikaanza kuandikwa mnamo mwaka wa 1513 K.W.K. Kwa miaka 1,610 iliyofuata, Yehova ‘alisema katika vipindi vingi na katika njia nyingi na’ wanadamu 40 hivi ambao waliandika Biblia. (Waebrania 1:1) Ili kuhifadhi Maandiko hayo, wanakili wenye bidii walifanyiza kwa uangalifu mkubwa nakala sahihi.—Ezra 7:6; Zaburi 45:1.
6 Yehova ametubariki kwelikweli kwa kuwasiliana nasi kupitia maandiko. Je, umewahi kupokea barua uliyothamini sana—labda kwa sababu ilikupa faraja uliyohitaji sana—hivi kwamba uliitunza na kuisoma tena na tena? Ndivyo ilivyo na “barua” ambayo Yehova ametuandikia. Kwa sababu Yehova aliandika maneno yake, tunaweza kuyasoma kwa ukawaida na kuyatafakari. (Zaburi 1:2) Tunaweza kupokea “faraja kutokana na Maandiko” wakati wowote tunapoihitaji.—Waroma 15:4.
Kwa Nini AlitumiaWanadamu Kuliandika?
7. Yehova alionyeshaje hekima kwa kuwatumia wanadamu kuandika Neno lake?
7 Yehova alionyesha hekima kwa kuwatumia wanadamu kuandika Neno lake. Hebu fikiria: Kama Yehova angalitumia malaika kuandika Biblia, je, ingalivutia kwa njia ileile? Kwa kweli, malaika wangeeleza jinsi Yehova alivyo kulingana na maoni yao yaliyotukuka, wangeeleza jinsi wanavyojitoa kwake, na kuandika kuhusu wanadamu waliomtumikia Mungu kwa uaminifu. Lakini je, tungeweza kweli kuelewa maoni ya viumbe wakamilifu wa roho, ambao wana ujuzi, ufahamu, na uwezo wa hali ya juu kuliko sisi?—Waebrania 2:6, 7.
“Andiko lote limepuliziwa na Mungu”
8. Waandishi wa Biblia waliruhusiwa kutumia akili zao jinsi gani? (Ona pia kielezi-chini.)
8 Kwa kuwatumia wanadamu kuandika Neno lake, Yehova alitupatia kile tunachohitaji—kitabu ambacho ‘kimepuliziwa na Mungu’ lakini kinachozingatia hali ya binadamu. (2 Timotheo 3:16) Alifanyaje hivyo? Mara nyingi, inaonekana kwamba aliwaruhusu waandishi watumie akili zao katika kuchagua “maneno yapendezayo, na yale yaliyoandikwa kwa unyofu, yaani, maneno ya kweli.” (Mhubiri 12:10, 11) Ndiyo sababu Biblia imeandikwa kwa njia mbalimbali; njia hizo hutegemea malezi na utu wa kila mwandishi.a Lakini, wanadamu hao “walisema kutoka kwa Mungu walipokuwa wakichukuliwa na roho takatifu.” (2 Petro 1:21) Kwa hiyo, Biblia ni “neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13.
9, 10. Kwa nini kutumia wanadamu kuiandika Biblia kunaifanya ipendeze na kuvutia zaidi?
9 Biblia inapendeza na kuvutia sana kwa sababu Mungu alitumia wanadamu kuiandika. Waandishi wa Biblia walikuwa wanadamu wenye hisia kama zetu. Wakiwa wanadamu wasiokamilika, walipata majaribu na mifadhaiko kama yetu. Nyakati nyingine, roho ya Yehova iliwaongoza kuandika kuhusu hisia zao na matatizo yaliyowapata. (2 Wakorintho 12:7-10) Kwa hiyo, waliandika kama wahusika, maneno ambayo hakuna malaika angeweza kuandika.
10 Kwa mfano, fikiria Mfalme Daudi wa Israeli. Baada ya kufanya dhambi nzito sana, Daudi alitunga zaburi ambayo inaeleza mambo yaliyokuwa moyoni mwake, na jinsi alivyomwomba Mungu msamaha. Aliandika hivi: ‘Unioshe kabisa na uovu wangu, unitakase dhambi zangu. Maana nimejua mimi makosa yangu na dhambi yangu i mbele yangu daima. Tazama, mimi naliumbwa katika hali ya uovu; mama yangu alinichukua mimba hatiani. Usinitenge na uso wako, wala roho yako takatifu usiniondolee. Dhabihu za Mungu ni roho iliyovunjika; moyo uliovunjika na kupondeka, Ee Mungu hutaudharau.’ (Zaburi 51:2, 3, 5, 11, 17) Je, huguswi moyo na uchungu wa mwandishi huyo? Ni mwanadamu asiyekamilika tu ndiye angeweza kuandika maneno hayo yenye kugusa moyo, sivyo?
Kwa Nini Aandike Kitabu Kinachohusu Watu?
11. Ni masimulizi gani halisi yameandikwa katika Biblia ili ‘kutufunza’?
11 Kuna jambo jingine linalofanya Biblia ivutie. Kwa kadiri kubwa, ni kitabu kinachohusu watu—watu halisi, wale waliomtumikia Mungu na wale ambao hawakumtumikia. Tunasoma kuhusu maisha yao, magumu yao, na shangwe yao. Tunaona matokeo ya maamuzi waliyofanya maishani. Masimulizi hayo yaliandikwa ili ‘kutufunza.’ (Waroma 15:4) Kupitia masimulizi hayo halisi, Yehova anatufundisha kwa njia ambazo zinatugusa mioyo. Fikiria mifano kadhaa.
12. Masimulizi ya Biblia kuhusu wanadamu wasio waaminifu yanatusaidiaje?
12 Biblia inatuambia kuhusu wanadamu wasio waaminifu, na hata waovu na mambo yaliyowapata. Masimulizi hayo yanaonyesha jinsi watu walivyoonyesha sifa zisizofaa, na hilo linatusaidia kuelewa sifa hizo. Kwa mfano, hakuna amri inayoweza kukazia kikiki ubaya wa kutokuwa mwaminifu kuliko mfano halisi wa Yudasi akipanga njama ya kumsaliti Yesu, sivyo? (Mathayo 26:14-16, 46-50; 27:3-10) Masimulizi kama hayo hugusa sana mioyo yetu, na kutusaidia kutambua na kuzitupilia mbali sifa zinazochukiza.
13. Biblia inatusaidiaje kuelewa sifa zinazofaa?
13 Biblia pia inasimulia kuhusu watumishi wengi wa Mungu waliokuwa waaminifu. Tunasoma kuhusu ujitoaji wao na uaminifu wao. Tunasoma kuhusu watu wenye sifa ambazo tunahitaji kukuza ili kumkaribia Mungu. Kwa mfano, fikiria sifa ya imani. Biblia inatuambia imani ni nini na kwa nini tunahitaji kuwa nayo ili kumpendeza Mungu. (Waebrania 11:1, 6) Lakini Biblia pia inaeleza mifano halisi ya watu waliokuwa na imani. Fikiria imani ambayo Abrahamu alionyesha alipojaribu kumtoa Isaka. (Mwanzo, sura ya 22; Waebrania 11:17-19) Masimulizi kama hayo yanatusaidia kuthamini na kuelewa vizuri zaidi maana ya neno “imani.” Ni hekima iliyoje kwamba Yehova, mbali na kutuhimiza tukuze sifa zinazofaa anatuonyesha mifano ya watu waliokuwa na sifa hizo!
14, 15. Biblia inatuambia nini kuhusu mwanamke fulani aliyekuja hekaluni, na simulizi hilo linatufundisha nini kumhusu Yehova?
14 Masimulizi halisi yaliyo katika Biblia mara nyingi yanatufundisha kuhusu utu wa Yehova. Fikiria simulizi la mwanamke fulani ambaye Yesu alimwona hekaluni. Alipokuwa ameketi karibu na masanduku ya hazina, Yesu aliangalia jinsi watu walivyokuwa wakitumbukiza michango yao humo. Matajiri wengi walikuja na kutumbukiza “kutokana na ziada yao.” Lakini Yesu alimtazama sana mjane mmoja maskini. Mjane huyo alitoa mchango wa “sarafu ndogo mbili, ambazo zina thamani ndogo sana.”b Alitoa fedha zote alizokuwa nazo. Yesu, ambaye alidhihirisha kikamili maoni ya Yehova, alisema hivi: ‘Mjane huyu maskini alitumbukiza ndani zaidi ya wote wale waliokuwa wakitumbukiza fedha ndani ya masanduku ya hazina.’ Kulingana na maneno hayo, alitumbukiza fedha nyingi kuliko jumla ya fedha zilizotolewa na watu wengine wote.—Marko 12:41-44; Luka 21:1-4; Yohana 8:28.
15 Je, haishangazi kwamba kati ya watu wote waliokuja hekaluni siku hiyo, ni mjane huyo peke yake ndiye aliyetajwa katika Biblia? Kupitia mfano huo, Yehova anatufundisha kwamba yeye ni Mungu anayethamini mambo tunayofanya. Anakubali kwa furaha michango tunayomtolea kwa nafsi yetu yote, pasipo kuilinganisha na michango inayotolewa na wengine. Bila shaka Yehova ametumia njia bora sana kutufundisha ukweli huo wenye kutia moyo!
Mambo Ambayo Biblia Haitaji
16, 17. Yehova anaonyeshaje hekima yake kwa kutoandika mambo fulani katika Neno lake?
16 Unapomwandikia mpendwa wako barua, huwezi kuandika kila jambo. Kwa hiyo, unachagua kwa busara mambo ya kuandika. Vivyo hivyo, Yehova alitaja watu fulani na matukio fulani katika Neno lake. Lakini Biblia haielezi kinagaubaga kila jambo kuhusiana na masimulizi hayo. (Yohana 21:25) Kwa mfano, Biblia inapozungumzia hukumu ya Mungu, haijibu kila swali tulilo nalo kuhusu hukumu hiyo. Yehova anaonyesha pia hekima yake kwa kutoandika mambo fulani katika Neno lake. Jinsi gani?
17 Biblia imeandikwa kwa njia inayokusudiwa kutambua mambo yaliyo moyoni mwetu. Andiko la Waebrania 4:12 lasema hivi: “Neno [au, ujumbe] la Mungu liko hai na hukazia nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili na hudunga hata kufikia kugawanya nafsi na roho . . . na ni lenye kuweza kufahamu fikira na makusudio ya moyo.” Ujumbe wa Biblia hupenya ndani kabisa, na kufunua mawazo yetu na nia yetu halisi. Wale wanaoisoma wakiwa na nia ya kuichambua mara nyingi wanakwazwa wanapopata masimulizi ambayo hayana habari ya kutosha kuwaridhisha. Watu wa aina hiyo huenda hata wakawa na shaka kwamba Yehova ni mwenye upendo, hekima na haki.
18, 19. (a) Kwa nini hatupaswi kutatanika wakati simulizi fulani la Biblia linazusha maswali ambayo hatuwezi kujibu mara moja? (b) Tunahitaji kufanya nini ili kufahamu Neno la Mungu, na jambo hilo linaonyeshaje hekima kuu ya Yehova?
18 Kwa upande mwingine, tunapojifunza Biblia kwa uangalifu na kwa unyofu, tunapata kumjua Yehova kama anavyofafanuliwa katika Biblia nzima. Kwa hiyo, hatutataniki wakati simulizi fulani linazusha maswali ambayo hatuwezi kupata jibu mara moja. Kwa mfano: Tunapounganisha vipande vya mchezo wa chemshabongo, huenda tusipate kipande fulani mwanzoni au huenda tusielewe jinsi kipande fulani kinavyoungana na vingine. Lakini, labda tumeunganisha vipande vya kutosha kutusaidia kuelewa jinsi picha kamili itakavyokuwa. Vivyo hivyo, tunapojifunza Biblia, pole kwa pole tunajifunza jinsi Yehova Mungu alivyo, na hatimaye tunapata kumjua vizuri kabisa. Hata ikiwa mwanzoni hatuelewi simulizi fulani au hatuoni jinsi linavyopatana na utu wa Mungu, tayari tumejifunza kupitia funzo letu la Biblia mambo mengi sana ya kutusadikisha kwamba bila shaka Yehova ni Mungu mwenye upendo, asiyependelea, na mwenye haki.
19 Basi, ili kufahamu Neno la Mungu, ni lazima tusome na kujifunza Neno hilo kwa moyo mnyofu bila kushikilia mno maoni yetu. Jambo hilo linaonyesha hekima kuu ya Yehova, sivyo? Wanadamu wenye akili nyingi wanaweza kuandika vitabu ambavyo ni watu “wenye hekima na wenye akili” tu wanaovielewa. Lakini ni Mungu tu anayeweza kuandika kitabu ambacho watu wenye mwelekeo unaofaa tu wanaweza kukielewa!—Mathayo 11:25.
Kitabu Chenye “Hekima Kamili”
20. Kwa nini ni Yehova peke yake anayeweza kutuambia njia bora ya maisha, na Biblia ina nini kinachoweza kutusaidia?
20 Katika Neno lake, Yehova hutuambia njia bora ya maisha. Anajua mahitaji yetu vizuri zaidi kuliko tunavyoyajua kwa sababu yeye ni Muumba wetu. Na sikuzote wanadamu wamekuwa na mahitaji yaleyale ya msingi, kama vile, tamaa ya kupendwa, kuwa na furaha, na kuwa na mahusiano mazuri. Biblia ina “hekima kamili” ambayo inaweza kutusaidia kuwa na kusudi maishani. (Mithali 2:7) Kila sehemu ya kitabu hiki ina sura ambayo inaonyesha jinsi tunavyoweza kutumia shauri la Biblia lenye hekima. Lakini hebu tuone mfano mmoja tu.
21-23. Ni mashauri gani yenye hekima yanayoweza kutusaidia kuepuka kufungia hasira na kinyongo moyoni?
21 Je, umegundua kwamba watu ambao wanafungia uchungu na kinyongo moyoni mara nyingi hujiumiza wenyewe? Kinyongo humlemea sana mtu. Tunapofungia kinyongo moyoni, tunajawa na mawazo, na tunakosa utulivu na shangwe. Uchunguzi wa kisayansi unadokeza kwamba kufungia hasira moyoni kunaweza kuongeza uwezekano wa kupata ugonjwa wa moyo na magonjwa mengine mengi ya kudumu. Miaka mingi kabla ya uchunguzi huo wa kisayansi, Biblia ilisema hivi kwa hekima: “Ukomeshe hasira, uache ghadhabu.” (Zaburi 37:8) Lakini tunaweza kufanyaje hivyo?
22 Neno la Mungu linatoa shauri hili la hekima: “Busara ya mtu huiahirisha hasira yake; nayo ni fahari yake kusamehe makosa.” (Mithali 19:11) Busara ni uwezo wa kuchanganua jambo kwa undani zaidi, kutambua sababu zisizoonekana wazi. Busara hutokeza ufahamu, kwa kuwa inaweza kutusaidia kutambua sababu iliyomfanya mtu mwingine aseme au kutenda kwa njia fulani. Kujitahidi kuelewa nia yake halisi, hisia zake, na hali zake kwaweza kutusaidia kuondoa mawazo au hisia zozote mbaya tulizo nazo kumwelekea.
23 Biblia ina shauri hivi tena: “Endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake na kusameheana kwa hiari mtu na mwenzake.” (Wakolosai 3:13) Usemi “endeleeni kuchukuliana mtu na mwenzake” unadokeza hali ya kuwastahimili wengine, kuvumilia sifa ambazo huenda zinatuudhi. Ustahimilivu wa aina hiyo unaweza kutusaidia kuepuka kufungia kinyongo moyoni kwa sababu ya mambo madogo-madogo. Neno “kusameheana” lamaanisha kuondoa kabisa kinyongo. Mungu wetu mwenye hekima anajua kwamba tunahitaji kuwasamehe wengine kunapokuwa na sababu nzuri ya kufanya hivyo. Tunapowasamehe wengine hatuwafaidi tu wale waliotukosea bali pia sisi wenyewe tunakuwa na amani ya akilini na ya moyoni. (Luka 17:3, 4) Neno la Mungu lina hekima iliyoje!
24. Inakuwaje tunapotumia hekima ya Mungu maishani?
24 Yehova alitaka kuwasiliana nasi kwa sababu ya upendo wake usio na kifani. Alichagua njia bora sana—“barua” iliyoandikwa na wanadamu walioongozwa na roho takatifu. Ndiyo sababu Biblia ina hekima ya Yehova mwenyewe. Hekima hiyo ni “amini sana.” (Zaburi 93:5) Kadiri tunavyotumia hekima hiyo maishani, na kadiri tunavyowafundisha wengine hekima hiyo, ndivyo tunavyozidi kumkaribia Mungu wetu mwenye hekima kamili. Katika sura inayofuata, tutazungumzia mfano mwingine wenye kutokeza wa hekima ya Yehova ya kuona matukio ya wakati ujao: uwezo wake wa kutabiri matukio ya wakati ujao na kutimiza kusudi lake.
a Kwa mfano, Daudi, aliyekuwa mchungaji, anatumia mifano inayohusiana na ufugaji wa wanyama. (Zaburi 23) Mathayo, ambaye alikuwa mtoza-kodi hapo awali, mara nyingi anataja tarakimu na thamani ya fedha. (Mathayo 17:27; 26:15; 27:3) Luka, ambaye alikuwa daktari, anatumia maneno yanayohusiana na kazi yake ya tiba.—Luka 4:38; 14:2; 16:20.
b Kila moja ya sarafu hizo iliitwa leptoni. Hiyo ndiyo iliyokuwa sarafu ya Kiyahudi yenye thamani ndogo zaidi wakati huo. Lepta mbili zilikuwa sawa na thamani ya 1/64 ya mshahara wa siku moja. Sarafu mbili hata hazikutosha kununua shore mmoja. Shore alikuwa ndege mwenye gharama ya chini sana aliyeliwa na watu maskini.
-
-
“Hekima ya Mungu Katika Siri Takatifu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 19
“Hekima ya Mungu Katika Siri Takatifu”
1, 2. Tunapaswa kupendezwa na ‘siri gani takatifu,’ na kwa nini?
SIRI! Mara nyingi wanadamu hushindwa kuficha siri, kwa sababu zinavutia na kustaajabisha. Hata hivyo, Biblia inasema hivi: “Ni utukufu wa Mungu kuficha jambo.” (Mithali 25:2) Naam, akiwa Muumba na Mtawala Mwenye Enzi Kuu, Yehova ana haki ya kuweka mambo fulani yakiwa siri kwa wanadamu hadi wakati wake wa kuyafunua unapowadia.
2 Lakini, kuna siri moja yenye kuvutia na kustaajabisha ambayo Yehova amefunua katika Neno lake. Inaitwa “siri takatifu ya mapenzi [ya Mungu].” (Waefeso 1:9) Kujifunza kuhusu siri hiyo si jambo la kufurahisha tu. Kujua siri hiyo kunaweza kukusaidia upate wokovu na kufahamu kidogo hekima ya Yehova isiyo na kifani.
Siri Takatifu Yafunuliwa Hatua kwa Hatua
3, 4. Unabii wa Mwanzo 3:15 ulitoaje tumaini, na ulikuwa na fumbo gani, au ‘siri gani takatifu’?
3 Adamu na Hawa walipofanya dhambi, huenda ilionekana kana kwamba kusudi la Yehova la wanadamu wakamilifu kuishi katika paradiso duniani lilikuwa limezuiwa. Lakini Mungu alishughulikia tatizo hilo mara moja. Alisema hivi: “Nitaweka uadui kati yako na huyo mwanamke, na kati ya uzao wako na uzao wake; huo utakuponda kichwa, na wewe utamponda kisigino.”—Mwanzo 3:15.
4 Maneno hayo yalikuwa ya kifumbo na yasiyoeleweka. Ni mwanamke yupi huyo? Nyoka alikuwa nani? Ni nani angekuwa “uzao” ambao ungemponda nyoka kichwa? Adamu na Hawa waliweza kukisia-kisia tu. Hata hivyo, maneno hayo ya Mungu yalimpa tumaini mzao yeyote mwaminifu wa wenzi hao walioasi. Uadilifu ungeshinda. Kusudi la Yehova lingetimizwa. Lakini jinsi gani? Ahaa, hilo lilikuwa fumbo! Biblia inasema kwamba fumbo hilo ni “hekima ya Mungu katika siri takatifu, hekima iliyofichwa.”—1 Wakorintho 2:7.
5. Toa mfano ambao unaonyesha kwa nini Yehova alifunua siri yake hatua kwa hatua.
5 Hatimaye, Yehova, “afunuaye siri,” angefunua kila jambo kuhusu utimizo wa siri hiyo. (Danieli 2:28) Lakini angeifunua siri hiyo polepole, hatua kwa hatua. Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo baba mwenye upendo anavyomjibu mvulana wake mdogo anayemwuliza, “Baba, nilitoka wapi?” Baba mwenye hekima anamwambia mvulana huyo mdogo habari chache tu ambazo anaweza kuelewa. Kadiri mvulana huyo anavyokua, ndivyo baba anavyomweleza habari zaidi. Vivyo hivyo, Yehova huamua wakati ambapo watu wake wanaweza kuelewa unabii kuhusu mapenzi yake na kusudi lake.—Mithali 4:18; Danieli 12:4.
6. (a) Agano au mapatano hutimiza kusudi gani? (b) Kwa nini inavutia kwamba Yehova hufanya maagano na wanadamu?
6 Yehova alifunuaje siri hizo? Alifunua mambo mengi kwa kufanya maagano au mapatano kadhaa. Huenda wakati fulani umewahi kufanya mapatano—labda ya kununua nyumba au ya kuomba mkopo au ya kumkopesha mtu pesa. Mapatano hayo yalithibitisha kisheria kwamba masharti mliyokubaliana yatatimizwa. Lakini kwa nini Yehova alihitaji kufanya maagano rasmi au mapatano na wanadamu? Bila shaka, neno lake ni uthibitisho wa kutosha wa kwamba ahadi zake zitatimia. Hiyo ni kweli, lakini kwa fadhili Mungu amethibitisha neno lake katika visa kadhaa kwa kufanya maagano ya kisheria. Maagano hayo yenye masharti ya kisheria hutupatia sisi wanadamu wasiokamilika msingi thabiti zaidi wa kutumaini ahadi za Yehova.—Waebrania 6:16-18.
Agano Pamoja na Abrahamu
7, 8. (a) Yehova alifanya agano gani na Abrahamu, nalo lilifunua nini kuhusu ile siri takatifu? (b) Yehova alifunuaje hatua kwa hatua ukoo wa Mzao aliyeahidiwa?
7 Zaidi ya miaka elfu mbili baada ya mwanadamu kufukuzwa kutoka Paradiso, Yehova alimwambia hivi mtumishi wake mwaminifu Abrahamu: “Katika kuzidisha, nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni . . . na katika uzao wako mataifa yote ya dunia watajibarikia; kwa sababu umetii sauti yangu.” (Mwanzo 22:17, 18) Hiyo haikuwa ahadi tu; Yehova aliitoa kama agano la kisheria na kuithibitisha kwa kiapo chake kisichoweza kuvunjwa. (Mwanzo 17:1, 2; Waebrania 6:13-15) Ni jambo la pekee kama nini kwamba Bwana Mwenye Enzi Kuu kwa kweli alifanya agano la kuwabariki wanadamu!
“Nitauzidisha uzao wako kama nyota za mbinguni”
8 Agano la Kiabrahamu lilifunua kwamba Mzao aliyeahidiwa angekuwa mwanadamu, kwa sababu angekuwa mzao wa Abrahamu. Lakini angekuwa nani? Baada ya muda, Yehova alifunua kwamba Isaka, mmoja wa wana wa Abrahamu angekuwa babu ya Mzao huyo. Yakobo ndiye aliyechaguliwa kati ya wana wawili wa Isaka. (Mwanzo 21:12; 28:13, 14) Baadaye, Yakobo alimwambia mmoja wa wanaye 12 maneno haya ya kiunabii: “Fimbo ya enzi haitaondoka katika Yuda, wala mfanya sheria kati ya miguu yake, hata atakapokuja Yeye, mwenye milki, ambaye mataifa watamtii.” (Mwanzo 49:10) Basi ikawa wazi kwamba Mzao huyo angekuwa mfalme kutoka kwa kabila la Yuda!
Agano Pamoja na Israeli
9, 10. (a) Yehova alifanya agano gani na taifa la Israeli, na agano hilo lililinda nini? (b) Sheria ilionyeshaje kwamba wanadamu wanahitaji fidia?
9 Mwaka wa 1513 K.W.K., Yehova alifanya mpango ambao ungefunua mambo mengi zaidi kuhusu ile siri takatifu. Alifanya agano na wazao wa Abrahamu, taifa la Israeli. Ingawa agano hilo la Sheria ya Musa halitumiki leo, lilikuwa sehemu muhimu sana ya kusudi la Yehova la kutoa Mzao aliyeahidiwa. Jinsi gani? Fikiria njia hizi tatu. Kwanza, Sheria hiyo ilikuwa kama ukuta wenye kulinda. (Waefeso 2:14) Sheria zake adilifu ziliwatenganisha Wayahudi na wasio Wayahudi. Kwa hiyo, Sheria ilisaidia kulinda ukoo wa Mzao aliyeahidiwa. Kwa sababu ya ulinzi huo, taifa hilo bado lilikuwapo wakati wa Mungu ulipowadia wa Mesiya kuzaliwa katika kabila la Yuda.
10 Pili, Sheria ilionyesha waziwazi kwamba wanadamu wanahitaji fidia. Sheria hiyo kamilifu ilionyesha kwamba wanadamu wenye dhambi hawawezi kuitii kikamili. Kwa hiyo, ilikusudiwa “kufanya mikiuko-sheria iwe dhahiri, mpaka mbegu iwasili ambayo kwayo ahadi ilikuwa imetolewa.” (Wagalatia 3:19) Sheria hiyo ilikuwa na mipango ya kusamehe dhambi kwa muda kupitia dhabihu za wanyama. Lakini, dhabihu hizo ziliashiria dhabihu ya fidia ya Kristo, kwa kuwa kama Paulo alivyoandika, “haiwezekani damu ya mafahali na ya mbuzi kuziondolea mbali dhambi.” (Waebrania 10:1-4) Kwa hiyo, kwa Wayahudi waaminifu, agano hilo lilikuwa ‘mfunzi aliyeongoza kwa Kristo.’—Wagalatia 3:24.
11. Agano la Sheria liliandalia Israeli tumaini gani tukufu, lakini kwa nini karibu taifa hilo lote lilipoteza tumaini hilo?
11 Tatu, agano hilo liliandalia taifa la Israeli tumaini tukufu. Yehova aliwaambia kwamba ikiwa wangetii agano hilo, wangekuwa “ufalme wa makuhani, na taifa takatifu.” (Kutoka 19:5, 6) Hatimaye, Waisraeli wa asili wakaja kuwa washiriki wa kwanza wa ufalme wa makuhani wa kimbingu. Hata hivyo, karibu taifa lote la Israeli liliasi agano la Sheria, likamkataa yule Mzao wa Kimesiya, na likapoteza tumaini hilo. Basi, ni nani wangekamilisha ufalme wa makuhani? Na taifa hilo lililobarikiwa lingekuwa na uhusiano gani na Mzao aliyeahidiwa? Mambo hayo ya siri takatifu yangefunuliwa katika wakati barabara wa Mungu.
Agano la Ufalme la Daudi
12. Yehova alifanya agano jipi na Daudi, na lilifunua mambo gani kuhusu siri takatifu ya Mungu?
12 Katika karne ya 11 K.W.K., Yehova alifunua mambo zaidi kuhusu ile siri takatifu alipofanya agano jingine. Alimwahidi hivi Mfalme Daudi aliyekuwa mwaminifu: “Nitainua mzao wako nyuma yako, . . . nami nitaufanya imara ufalme wake. . . . Nacho kiti cha enzi cha ufalme wake nitakifanya imara milele.” (2 Samweli 7:12, 13; Zaburi 89:3) Wakati huo ilijulikana kwamba ukoo wa Mzao aliyeahidiwa ungetokea katika nyumba ya Daudi. Lakini je, mwanadamu wa kawaida angeweza kutawala “milele”? (Zaburi 89:20, 29, 34-36) Na je, mfalme huyo wa kibinadamu angeweza kuwaokoa wanadamu kutoka kwa dhambi na kifo?
13, 14. (a) Kulingana na Zaburi 110, Yehova anamwahidi nini Mfalme wake aliyetiwa mafuta? (b) Manabii wa Yehova walifunua mambo gani mengine kuhusu Mzao ambaye angekuja?
13 Daudi aliongozwa kuandika hivi: “Neno la BWANA kwa Bwana wangu, Uketi mkono wangu wa kuume, hata niwafanyapo adui zako kuwa chini ya miguu yako. BWANA ameapa, wala hataghairi, Ndiwe kuhani hata milele, kwa mfano wa Melkizedeki.” (Zaburi 110:1, 4) Maneno hayo ya Daudi yalimhusu moja kwa moja, Mzao aliyeahidiwa, au Mesiya. (Matendo 2:35, 36) Mfalme huyo hangetawala kutoka Yerusalemu, bali kutoka mbinguni kwenye ‘mkono wa kuume’ wa Yehova. Basi angekuwa na mamlaka, si juu ya nchi ya Israeli tu, bali juu ya dunia yote. (Zaburi 2:6-8) Jambo jingine lilifunuliwa. Angalia kwamba Yehova aliapa kwa dhati kwamba huyo Mesiya angekuwa “kuhani . . . kwa mfano wa Melkizedeki.” Kama Melkizedeki, ambaye alitumika akiwa mfalme na kuhani katika siku za Abrahamu, Mzao ambaye angekuja angechaguliwa na Mungu moja kwa moja awe Mfalme na Kuhani!—Mwanzo 14:17-20.
14 Kwa miaka mingi, Yehova alitumia manabii wake kufunua mambo zaidi kuhusu siri yake takatifu. Kwa mfano, Isaya alitabiri kwamba Mzao huyo angekufa kifo cha kidhabihu. (Isaya 53:3-12) Mika alitabiri mahali ambapo Mesiya angezaliwa. (Mika 5:2) Danieli hata alitabiri wakati hususa ambapo Mzao huyo angetokea na wakati ambapo angekufa.—Danieli 9:24-27.
Siri Takatifu Yafunuliwa!
15, 16. (a) Mwana wa Yehova ‘alitokana na mwanamke’ kwa njia gani? (b) Yesu alirithi nini kutoka kwa wazazi wake wa kibinadamu, naye akawa Mzao aliyeahidiwa lini?
15 Utimizo wa unabii huo mbalimbali haukujulikana hadi Mzao huyo alipotokea. Andiko la Wagalatia 4:4 lasema: “Kikomo kamili cha wakati kilipowasili, Mungu alimtuma Mwana wake, aliyekuja kuwa kutokana na mwanamke.” Mnamo mwaka wa 2 K.W.K., malaika alimwambia hivi bikira Myahudi aliyeitwa Maria: “Tazama! utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana, nawe itakupasa kumwita jina lake Yesu. Huyu atakuwa mkubwa na ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi Sana; na Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake . . . Roho takatifu itakuja juu yako, na nguvu ya Aliye Juu Zaidi Sana itakufunika kivuli. Kwa sababu hiyo pia kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.”—Luka 1:31, 32, 35.
16 Baadaye, Yehova alihamisha uhai wa Mwanaye kutoka mbinguni hadi kwenye tumbo la uzazi la Maria, hivyo, akatokana na mwanamke. Maria hakuwa mwanamke mkamilifu. Lakini, Yesu hakurithi kutokamilika kutoka kwa Maria, kwa sababu alikuwa “Mwana wa Mungu.” Lakini, wazazi wa kibinadamu wa Yesu, ambao walikuwa wazao wa Daudi, walimwezesha kuwa mrithi wa Daudi kiasili na kisheria. (Matendo 13:22, 23) Yesu alipobatizwa mwaka wa 29 W.K., Yehova alimtia mafuta kwa roho takatifu na kusema: “Huyu ni Mwana wangu, mpendwa.” (Mathayo 3:16, 17) Hatimaye, Mzao aliyeahidiwa alikuwa amewasili! (Wagalatia 3:16) Wakati wa kufunua mambo mengi zaidi kuhusu ile siri takatifu ulikuwa umewadia.—2 Timotheo 1:10.
17. Andiko la Mwanzo 3:15 lilifafanuliwaje?
17 Wakati wa huduma yake, Yesu alimtambulisha yule nyoka aliyetajwa katika Mwanzo 3:15 kuwa Shetani, na uzao wa nyoka kuwa wafuasi wa Shetani. (Mathayo 23:33; Yohana 8:44) Baadaye, ilifunuliwa jinsi ambavyo hao wote watapondwa milele. (Ufunuo 20:1-3, 10, 15) Na mwanamke alitambuliwa kuwa “Yerusalemu la juu,” tengenezo la Yehova la mbinguni la viumbe wa roho, ambalo ni kama mke.a—Wagalatia 4:26; Ufunuo 12:1-6.
Agano Jipya
18. Ni nini kusudi la “agano jipya”?
18 Huenda jambo la kutokeza hata zaidi lilifunuliwa siku iliyotangulia kifo cha Yesu, alipowaambia wanafunzi wake waaminifu kuhusu “agano jipya.” (Luka 22:20) Agano hilo jipya, sawa na agano la Sheria ya Musa, lilikusudiwa kufanyiza “ufalme wa makuhani.” (Kutoka 19:6; 1 Petro 2:9) Hata hivyo, agano hilo halingefanyiza taifa la kiasili bali taifa la kiroho, yaani, “Israeli wa Mungu.” Taifa hilo lingekuwa tu na wafuasi waaminifu wa Kristo waliotiwa mafuta. (Wagalatia 6:16) Washiriki hao wa agano jipya wangeshirikiana na Yesu kubariki wanadamu!
19. (a) Kwa nini agano jipya linafanikiwa kufanyiza “ufalme wa makuhani”? (b) Kwa nini Wakristo watiwa-mafuta wanaitwa “kiumbe kipya,” na ni wangapi watakaotawala na Kristo wakiwa mbinguni?
19 Lakini kwa nini agano jipya linafanikiwa kufanyiza “ufalme wa makuhani” ambao utawabariki wanadamu? Kwa sababu badala ya kuwahukumu wanafunzi wa Kristo kuwa watenda-dhambi, linafungua njia ya dhambi zao kusamehewa kupitia dhabihu yake. (Yeremia 31:31-34) Mara tu baada ya kuhesabiwa kuwa waadilifu machoni pa Yehova, anawakubali kuwa wana wa familia yake ya mbinguni na kuwatia mafuta kwa roho takatifu. (Waroma 8:15-17; 2 Wakorintho 1:21) Kwa hiyo, wanapata ‘uzaliwa mpya kwenye tumaini lililo hai ambao umewekwa akiba katika mbingu.’ (1 Petro 1:3, 4) Wakristo watiwa-mafuta waliozaliwa kwa roho wanaitwa “kiumbe kipya,” kwa sababu cheo chao cha juu ni kipya kabisa kwa wanadamu. (2 Wakorintho 5:17) Biblia inafunua kwamba hatimaye watu 144,000 wakiwa mbinguni watashiriki kutawala wanadamu waliokombolewa.—Ufunuo 5:9, 10; 14:1-4.
20. (a) Ni jambo gani lililofunuliwa mwaka wa 36 W.K. kuhusu ile siri takatifu? (b) Ni nani watakaofurahia baraka ambazo Abrahamu aliahidiwa?
20 Yesu pamoja na hao watiwa-mafuta wanakuwa “mbegu ya Abrahamu.”b (Wagalatia 3:29) Wayahudi wa asili ndiyo waliochaguliwa kwanza. Lakini mwaka wa 36 W.K., jambo jingine la siri takatifu lilifunuliwa: Watu wa Mataifa, au wasio Wayahudi, wangekuwa pia na tumaini la kwenda mbinguni. (Waroma 9:6-8; 11:25, 26; Waefeso 3:5, 6) Je, ni Wakristo watiwa-mafuta peke yao ambao wangefurahia baraka ambazo Abrahamu aliahidiwa? La, kwa sababu dhabihu ya Yesu inafaidi ulimwengu wote. (1 Yohana 2:2) Baada ya muda, Yehova alifunua kwamba “umati mkubwa” usiohesabika ungeokoka mwisho wa mfumo wa mambo wa Shetani. (Ufunuo 7:9, 14) Halaiki kubwa zaidi ya watu wangefufuliwa wakiwa na tumaini la kuishi milele katika Paradiso!—Luka 23:43; Yohana 5:28, 29; Ufunuo 20:11-15; 21:3, 4.
Hekima ya Mungu na Siri Takatifu
21, 22. Siri takatifu ya Yehova inaonyeshaje hekima yake?
21 Siri takatifu ni wonyesho wenye kustaajabisha wa “hekima ya Mungu ya namna nyingi.” (Waefeso 3:8-10) Yehova alionyesha hekima iliyoje alipotunga siri hiyo na kuifunua hatua kwa hatua! Kwa hekima alifikiria udhaifu wa wanadamu, akawaruhusu waonyeshe hali yao halisi ya moyoni.—Zaburi 103:14.
22 Yehova pia alionyesha hekima isiyo na kifani alipomchagua Yesu kuwa Mfalme. Mwana wa Yehova ni mwenye kutumainika kuliko kiumbe mwingine yeyote ulimwenguni. Yesu alipata magumu ya kila namna alipokuwa mwanadamu. Anaelewa kabisa matatizo yanayotupata. (Waebrania 5:7-9) Vipi watawala-wenzi wa Yesu? Kwa miaka mingi, wanaume na wanawake waliochaguliwa kutoka kwa makabila, lugha, na malezi mbalimbali wametiwa mafuta. Kila mmoja wao amepata matatizo ya kila namna na kuyashinda. (Waefeso 4:22-24) Itakuwa furaha iliyoje kutawaliwa na wafalme na makuhani hao wenye huruma!
23. Wakristo wana pendeleo gani kuhusiana na siri takatifu ya Yehova?
23 Mtume Paulo aliandika hivi: “Siri takatifu iliyokuwa imefichwa tangu mifumo ya mambo iliyopita na tangu vizazi vilivyopita . . . imefanywa dhahiri kwa watakatifu wake.” (Wakolosai 1:26) Naam, watakatifu wa Yehova waliotiwa mafuta wamepata kuelewa mengi kuhusu siri hiyo takatifu, nao wamewafundisha mamilioni ya watu ujuzi huo. Basi sote tuna pendeleo lililoje! Yehova ‘ametujulisha siri takatifu ya mapenzi yake.’ (Waefeso 1:9) Na tuwaambie wengine siri hiyo ya ajabu, na kuwasaidia pia wachunguze hekima isiyo na kifani ya Yehova Mungu!
a “Siri takatifu ya ujitoaji-kimungu” ilifunuliwa pia katika maisha ya Yesu. (1 Timotheo 3:16) Kwa muda mrefu, haikujulikana kama mwanadamu yeyote angeweza kubaki mwaminifu kabisa kwa Yehova. Yesu alijibu suala hilo. Alibaki mwaminifu licha ya majaribu yote ambayo Shetani alimletea.—Mathayo 4:1-11; 27:26-50.
b Yesu pia alifanya “agano . . . kwa ajili ya ufalme” na kikundi hichohicho. (Luka 22:29, 30) Kwa kweli, Yesu alifanya mapatano na “kundi [hilo] dogo” ili watawale pamoja naye mbinguni wakiwa sehemu ya pili ya mbegu ya Abrahamu.—Luka 12:32.
-
-
“Yeye Ni Mwenye Hekima Moyoni”—Lakini MnyenyekevuMkaribie Yehova
-
-
Sura ya 20
“Yeye Ni Mwenye Hekima Moyoni”—Lakini Mnyenyekevu
1-3. Tunajuaje kwamba Yehova ni mnyenyekevu?
BABA anataka kumfundisha mtoto wake mdogo somo muhimu. Ana hamu ya kugusa moyo wa mtoto huyo. Afanyeje hivyo? Je, asimame na kumtisha mtoto huyo? Au apaswa kuchuchumaa kufikia kimo cha mtoto huyo na kuzungumza naye kwa upole, na kwa urafiki? Bila shaka, baba mnyenyekevu na mwenye hekima humfikia mtoto wake kwa njia ya upole.
2 Yehova ni Baba wa aina gani—je, yeye ni mwenye kiburi au mnyenyekevu, mkali au mpole? Yehova anajua kila jambo, ana hekima kamili. Hata hivyo, je, umeona kwamba mara nyingi watu wenye ujuzi na akili hawawi wanyenyekevu? Ni kama Biblia inavyosema, ‘ujuzi hututumua.’ (1 Wakorintho 3:19; 8:1) Lakini Yehova, ni “mwenye hekima moyoni,” na mnyenyekevu pia. (Ayubu 9:4) Yehova hana kiburi licha ya kwamba ana cheo cha juu na fahari. Kwa nini?
3 Yehova ni mtakatifu. Kwa hiyo, hana sifa ya kiburi ambayo inamtia mtu unajisi. (Marko 7:20-22) Isitoshe, angalia maneno ambayo nabii Yeremia alimwambia Yehova: “Bila shaka nafsi yako [Yehova mwenyewe] itanikumbuka na kuniinamia.”a (Maombolezo 3:20, NW) Hebu wazia! Yehova, Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu, alikuwa tayari ‘kumwinamia,’ au kujinyenyekeza kufikia kiwango cha Yeremia. Alifanya hivyo ili kumpa uangalifu unaofaa mwanadamu huyo asiyekamilika. (Zaburi 113:7) Naam, Yehova ni mnyenyekevu. Lakini Mungu anaonyeshaje unyenyekevu? Unahusianaje na hekima? Na kwa nini unyenyekevu ni muhimu kwetu?
Jinsi Yehova Alivyo Mnyenyekevu
4, 5. (a) Unyenyekevu ni nini, na unaonyeshwaje, na kwa nini unyenyekevu haupasi kuonwa kuwa udhaifu au woga? (b) Yehova alionyeshaje unyenyekevu aliposhughulika na Daudi, na unyenyekevu wa Yehova unatufaidi jinsi gani?
4 Unyenyekevu unamaanisha kujiweka katika hali ya chini, kutojivuna na kutokuwa na kiburi. Unyenyekevu ni sifa ya moyoni na huonyeshwa kwa sifa kama vile upole, subira, na kuzingatia maoni ya wengine. (Wagalatia 5:22, 23) Lakini sifa hizo za kimungu hazipasi kamwe kuonwa kuwa udhaifu au woga. Sifa hizo zinapatana na hasira ya Yehova ya uadilifu au jinsi anavyotumia nguvu zake za kuangamiza. Lakini unyenyekevu na upole wa Yehova unaonyesha kwamba ana nguvu nyingi, yaani, uwezo wa kujidhibiti kikamili. (Isaya 42:14) Unyenyekevu unahusianaje na hekima? Kichapo kimoja kinachozungumzia Biblia kinasema hivi: “Unyenyekevu unafafanuliwa kuwa . . . hali ya kutokuwa na ubinafsi na ni chanzo muhimu cha hekima yote.” Basi, hakuwezi kuwa na hekima ya kweli pasipo unyenyekevu. Unyenyekevu wa Yehova unatufaidi jinsi gani?
Baba mwenye hekima huwatendea watoto wake kwa upole na unyenyekevu
5 Mfalme Daudi alimwimbia Yehova hivi: “Umenipa ngao ya wokovu wako, mkono wako wa kuume umenitegemeza, na unyenyekevu wako umenikuza.” (Zaburi 18:35) Ni kana kwamba Yehova aliinama ili amsaidie mwanadamu huyo asiyekamilika, alimlinda na kumtunza siku kwa siku. Daudi alitambua kwamba hangeweza kamwe kuokolewa—na hata, hatimaye kuwa mfalme—endapo Yehova hangejinyenyekeza. Kwa kweli, ni nani kati yetu angeweza kuwa na tumaini lolote la kuokoka ikiwa Yehova hangekuwa mnyenyekevu, na kama hangekuwa tayari kujiweka katika hali ya chini ili kushughulika nasi akiwa Baba mpole mwenye upendo?
6, 7. (a) Kwa nini Biblia haisemi kamwe kwamba Yehova ni mwenye kiasi kama wanadamu? (b) Kuna uhusiano gani kati ya upole na hekima, na ni nani aliye mfano bora kabisa wa sifa hizo?
6 Inafaa kukumbuka kwamba kuna tofauti kati ya unyenyekevu na kiasi. Kiasi ni sifa nzuri sana ambayo wanadamu waaminifu wanapaswa kukuza. Sifa hiyo, kama vile sifa ya unyenyekevu, inahusiana na hekima. Kwa mfano, Mithali 11:2, NW, yasema: “Hekima hukaa na wenye kiasi.” Hata hivyo, Biblia haisemi kamwe kwamba Yehova ni mwenye kiasi kama wanadamu. Kwa nini? Kulingana na Maandiko, mtu mwenye kiasi ni mtu anayetambua mipaka yake mwenyewe. Mungu Mweza-Yote hana mipaka yoyote ila mipaka anayojiwekea mwenyewe kwa sababu ya kanuni zake adilifu. (Marko 10:27; Tito 1:2) Isitoshe, hajitiishi kwa yeyote kwa sababu yeye ni Mungu Mwenyezi. Kwa hiyo, Yehova si mwenye kiasi katika maana hiyo.
7 Hata hivyo, Yehova ni mnyenyekevu na mpole. Yeye huwafundisha watumishi wake kwamba hawawezi kuwa na hekima ya kweli wasipokuwa wapole. Neno lake hutaja “upole ulio wa hekima.”b (Yakobo 3:13) Fikiria jinsi Yehova anavyoonyesha sifa hizo.
Yehova Huwakabidhi Wengine Madaraka Naye Huwasikiliza kwa Unyenyekevu
8-10. (a) Kwa nini inashangaza kwamba Yehova yu tayari kuwakabidhi wengine madaraka na kuwasikiliza? (b) Mwenyezi ameonyeshaje unyenyekevu anaposhughulika na malaika wake?
8 Utayari wa Yehova wa kusikiliza na kuwakabidhi wengine madaraka unaonyesha kwamba yeye ni mnyenyekevu. Inashangaza kwamba Yehova yu tayari kufanya hivyo ingawa yeye hahitaji msaada wala shauri. (Isaya 40:13, 14; Waroma 11:34, 35) Hata hivyo, Biblia inaonyesha tena na tena kwamba Yehova hujinyenyekeza katika njia hizo.
9 Kwa mfano, fikiria kisa kimoja cha pekee kilichotukia katika maisha ya Abrahamu. Abrahamu alitembelewa na wageni watatu, alimwita mmoja wao “Bwana.” Wageni hao walikuwa malaika, lakini mmoja wao alikuja kwa jina la Yehova na alikuwa akitenda kwa jina hilo. Malaika huyo aliponena na kutenda, ni kana kwamba Yehova mwenyewe alikuwa akinena na kutenda. Kupitia malaika hao, Yehova alimwambia Abrahamu kwamba Alikuwa amesikia “kilio cha Sodoma na Gomora.” Yehova alisema hivi: “Nitashuka sasa nione kama wanayotenda ni kiasi cha kilio kilichonijia; na kama sivyo, nitajua.” (Mwanzo 18:3, 20, 21) Bila shaka, ujumbe huo wa Yehova haukumaanisha kwamba Mweza Yote ‘angeshuka’ kihalisi. Badala yake, aliwatuma malaika wamwakilishe tena. (Mwanzo 19:1) Kwa nini? Je, Yehova ambaye ana uwezo wa kuona kila jambo hangeweza ‘kujua’ hali ya eneo hilo bila msaada? Bila shaka angeweza. Lakini badala yake, kwa unyenyekevu Yehova aliwapa malaika hao kazi ya kuchunguza hali na kumtembelea Loti na familia yake Sodoma.
10 Isitoshe, Yehova husikiliza. Pindi moja aliwaomba malaika wake watoe maoni kuhusu njia mbalimbali za kumshinda Mfalme Ahabu aliyekuwa mwovu. Yehova hakuhitaji msaada huo. Lakini, alikubali maoni ya malaika mmoja, naye akamtuma atekeleze jambo hilo. (1 Wafalme 22:19-22) Tukio hilo linaonyesha kwamba yeye ni mnyenyekevu, sivyo?
11, 12. Abrahamu alipataje kuelewa unyenyekevu wa Yehova?
11 Yehova yu tayari pia kuwasikiliza wanadamu wasiokamilika ambao wanataka sana kumweleza mahangaiko yao. Kwa mfano, Yehova alipomwambia Abrahamu kwamba alikusudia kuharibu Sodoma na Gomora, mwanamume huyo mwaminifu alishtuka. Abrahamu akasema, “Hasha usifanye hivyo,” kisha akaongezea hivi: “Mhukumu ulimwengu wote asitende haki?” Alimwuliza Yehova kama angeacha miji hiyo iwapo ingekuwa na watu 50 wenye haki. Yehova alimhakikishia kwamba Hangeiangamiza. Lakini Abrahamu akamwuliza swali hilo tena na tena, na kupunguza idadi hiyo hadi 45, kisha 40, na kuendelea. Abrahamu aliendelea kuuliza maswali hadi idadi hiyo ilipofikia kumi licha ya Yehova kumhakikishia kwamba hangeangamiza miji hiyo. Huenda Abrahamu hakufahamu vyema rehema ya Yehova. Vyovyote iwavyo, kwa subira Yehova alimruhusu rafiki na mtumishi wake Abrahamu aeleze mahangaiko yake.—Mwanzo 18:23-33.
12 Ni wanadamu wangapi wenye akili, na wenye elimu ambao wangemsikiliza kwa subira mtu asiye na akili nyingi sana?c Mungu wetu alionyesha unyenyekevu mkubwa kwa kumsikiliza Abrahamu kwa makini sana. Wakati wa mazungumzo hayo, Abrahamu alitambua pia kwamba Yehova “si mwepesi wa hasira.” (Kutoka 34:6) Huenda Abrahamu alitambua kwamba hakuwa na haki ya kumwuliza Mungu mambo aliyokusudia kufanya, kwa hiyo alimsihi hivi mara mbili: “Bwana asiwe na hasira.” (Mwanzo 18:30, 32) Bila shaka Yehova hakukasirika. Kwa kweli, Yehova ana “upole ulio wa hekima.”
Yehova Hukubali Sababu
13. Usemi “kukubali sababu” hutumiwa katika Biblia kumaanisha nini, na kwa nini sifa hiyo inamfaa kabisa Yehova?
13 Unyenyekevu wa Yehova unadhihirishwa na sifa nyingine yenye kupendeza—kukubali sababu. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba wanadamu wengi wasiokamilika hawana sifa hiyo. Yehova yuko tayari kuwasikiliza viumbe wake wenye akili, na yuko tayari pia kukubali maoni yao maadamu hayakiuki kanuni zake za uadilifu. Usemi “kukubali sababu” hutumiwa katika Biblia kumaanisha kihalisi ‘kukubali maoni ya wengine.’ Hiyo pia ni sifa muhimu ya hekima ya Mungu. Andiko la Yakobo 3:17 lasema hivi: ‘Hekima ya kutoka juu ni yenye kukubali sababu.’ Yehova ambaye ni mwenye hekima kamilifu anakubali sababu kwa njia gani? Kwanza, yeye hujipatanisha na hali mbalimbali. Kumbuka kwamba jina lake linatufundisha kwamba Yeye hujisababisha kuwa chochote kinachohitajiwa ili kutimiza makusudi yake. (Kutoka 3:14) Je, hilo halionyeshi kwamba yeye hujipatanisha na hali na ni mwenye kukubali sababu?
14, 15. Ono la Ezekieli la gari la kimbingu la Yehova linatufunza nini kuhusu tengenezo Lake la kimbingu, na hilo linatofautianaje na mashirika ya wanadamu?
14 Kuna ono moja la Biblia linalotusaidia kuelewa kwa kadiri fulani jinsi Yehova anavyojipatanisha na hali mbalimbali. Nabii Ezekieli alipata ono la tengenezo la kimbingu la Yehova la viumbe wa roho. Aliona gari kubwa ajabu na Yehova mwenyewe ndiye anayelielekeza gari hilo daima. Lilienda kwa njia ya kustaajabisha sana. Magurudumu yake makubwa yenye pande nne, yalijaa macho hivi kwamba yaliweza kuona kila mahali na kusafiri kuelekea upande wowote ghafula bila kusimama wala kugeuka. Na gari hilo kubwa mno halikujikokota polepole kama gari lililotengenezwa na wanadamu. Liliweza kwenda kwa mwendo wa umeme, na hata kugeuka ghafula! (Ezekieli 1:1, 14-28) Naam, tengenezo la Yehova linaweza kujipatanisha kabisa na hali mbalimbali na kushughulikia mahitaji yanayotokea kama anavyofanya Mungu Mwenye Enzi Kuu na mweza-yote ambaye analiongoza.
15 Wanadamu hawawezi kamwe kujipatanisha kikamili na hali kwa njia hiyo. Mara nyingi wanadamu na mashirika yao hushikilia mno maoni yao bila kubadilika, na hawakubali sababu. Kwa mfano: Meli ya mafuta au garimoshi la kubeba mizigo laweza kuwa kubwa sana na lenye nguvu nyingi sana. Lakini je, garimoshi au meli inaweza kugeuka mara moja hali zikibadilika? Garimoshi la mizigo haliwezi kuepuka kitu fulani kinachoanguka kwenye reli yake. Haliwezi kusimama ghafula. Baada ya breki kufungwa, garimoshi lenye mizigo mizito laweza kwenda umbali wa kilometa mbili hivi kabla ya kusimama! Vivyo hivyo, huenda meli kubwa ya mafuta ikasafiri umbali wa kilometa nane baada ya injini kuzimwa. Hata injini zikiendeshwa kinyumenyume, bado meli hiyo inaweza kusonga mbele umbali wa kilometa tatu! Ndivyo ilivyo na mashirika ya wanadamu ambayo mara nyingi hushikilia sana sera zake na kutokubali mawazo mapya. Mara nyingi watu hukataa kubadilika kulingana na mahitaji na hali mpya kwa sababu ya kiburi. Mashirika mengi yamevunjika na hata serikali nyingi kupinduliwa kwa sababu ya kutobadilika kulingana na hali. (Mithali 16:18) Twaweza kushukuru kama nini kwamba Yehova na tengenezo lake ni tofauti sana na mashirika hayo ya wanadamu!
Jinsi Yehova Anavyokubali Sababu
16. Yehova alionyeshaje sifa ya kukubali sababu aliposhughulika na Loti kabla ya kuangamizwa kwa Sodoma na Gomora?
16 Fikiria tena kuangamizwa kwa Sodoma na Gomora. Malaika wa Yehova alimpa Loti na familia yake maagizo yaliyo wazi kabisa: “Ujiponye mlimani.” Lakini maagizo hayo hayakumpendeza Loti. “Sivyo, bwana wangu!” akasihi. Akiamini kwamba angekufa kama angekimbilia milimani, Loti aliomba kwamba yeye na familia yake waruhusiwe kukimbilia mji wa karibu ulioitwa Soari. Kumbuka kwamba Yehova alikuwa amekusudia kuuangamiza mji huo. Isitoshe, Loti hakuwa na sababu nzuri ya kuogopa. Bila shaka Yehova angeweza kumlinda Loti huko milimani! Hata hivyo, Yehova alikubali ombi la Loti, hakuuangamiza mji wa Soari. Malaika akamwambia hivi Loti, “Tazama, nimekukubali hata kwa neno hili.” (Mwanzo 19:17-22) Je, jambo hilo halionyeshi kwamba Yehova ni mwenye kukubali sababu?
17, 18. Yehova alionyeshaje sifa ya kukubali sababu kuhusiana na Waninawi?
17 Yehova hukubali pia toba ya kutoka moyoni. Sikuzote yeye huonyesha rehema na kutenda yaliyo sawa. Fikiria jambo lililotukia nabii Yona alipotumwa mji wa Ninawi wenye uovu na jeuri. Yona alitangaza ujumbe rahisi sana wa Mungu kotekote katika Ninawi: Mji huo mashuhuri ungeangamizwa baada ya siku 40. Lakini, mambo yalibadilika ghafula. Waninawi walitubu!—Yona, sura ya 3.
18 Tunajifunza jambo fulani tunapolinganisha jinsi Yehova alivyohisi na jinsi Yona alivyohisi hali ilipobadilika. Yehova alijipatanisha na hali hiyo mara moja, akawa Mwenye Kusamehe dhambi badala ya kuwa “mtu wa vita.”d (Kutoka 15:3) Lakini Yona hakuwa tayari kubadilika wala hakuonyesha rehema kama Yehova alivyofanya. Badala ya kukubali sababu kama Yehova, alikuwa kama garimoshi la mizigo au meli kubwa ya mafuta tuliyotaja awali. Alitaka mji huo uangamizwe tu kama alivyokuwa ametangaza. Hata hivyo, kwa subira Yehova alimfundisha nabii wake asiye na subira somo lisilosahaulika kuhusu kukubali sababu na kuonyesha rehema.—Yona, sura ya 4.
Yehova ni mwenye kukubali sababu na anajua udhaifu wetu
19. (a) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova ni mwenye kukubali sababu kuhusiana na mambo anayotarajia tufanye? (b) Mithali 19:17 inaonyeshaje kwamba Yehova ni Bwana ‘mwema na mwenye kukubali sababu,’ na kwamba unyenyekevu wake hauna kifani?
19 Mwishowe, Yehova ni mwenye kukubali sababu kuhusiana na mambo anayotarajia tufanye. Mfalme Daudi alisema: “Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi.” (Zaburi 103:14) Yehova anajua udhaifu wetu na kasoro zetu kuliko tunavyojijua. Hatarajii kamwe tufanye mambo yanayozidi uwezo wetu. Biblia inasema kwamba mabwana fulani ni ‘wema na wenye kukubali sababu’ na wengine ni “wagumu kupendeza.” (1 Petro 2:18) Je, Yehova ni Bwana wa aina gani? Mithali 19:17 inasema: “Amhurumiaye maskini humkopesha BWANA.” Ni wazi kwamba bwana aliye mwema na mwenye kukubali sababu ndiye tu anayezingatia kila tendo la fadhili ambalo maskini wanafanyiwa. Isitoshe, andiko hilo pia linadokeza kwamba Muumba wa ulimwengu anajiona kuwa na deni kwa wanadamu duni wanaofanya matendo hayo ya rehema! Huo ni unyenyekevu usio na kifani.
20. Tuna uhakika gani kwamba Yehova husikiliza na kujibu sala zetu?
20 Hata leo Yehova ni mpole na mwenye kukubali sababu anaposhughulika na watumishi wake. Yeye husikiliza sala zetu za imani. Hatupaswi kukata kauli kwamba hajibu sala zetu kwa sababu hawatumi malaika waongee nasi. Kumbuka kwamba mtume Paulo alipowaomba waamini wenzake ‘waendeleze sala’ ili aweze kuachiliwa kutoka gerezani, aliongeza hivi: “Ili nipate kurudishwa kwenu karibuni zaidi.” (Waebrania 13:18, 19) Kwa hiyo, sala zetu zinaweza kwa kweli kumfanya Yehova atende jambo ambalo huenda hangetenda!—Yakobo 5:16.
21. Hatupaswi kuwa na maoni gani kuhusu unyenyekevu wa Yehova, lakini tunapaswa kumthamini kwa sababu gani?
21 Bila shaka, sifa zinazoonyesha unyenyekevu wa Yehova, yaani, upole, utayari wa kutusikiliza, subira, na kukubali sababu, hazimaanishi kwamba Yehova hulegeza kanuni zake adilifu. Huenda makasisi wa Jumuiya ya Wakristo wakadhani kwamba wanakubali sababu wanapotekenya masikio ya wafuasi wao kwa kulegeza kanuni za Yehova za maadili. (2 Timotheo 4:3) Lakini mwelekeo wa wanadamu wa kuridhiana ili wapendwe haupatani kabisa na sifa ya Mungu ya kukubali sababu. Yehova ni mtakatifu; hawezi kamwe kupotosha kanuni zake adilifu. (Mambo ya Walawi 11:44) Basi, na tupende sifa ya Yehova ya kukubali sababu kwa kuwa inathibitisha unyenyekevu wake. Je, hufurahi sana kujua kwamba Yehova Mungu ni mnyenyekevu sana licha ya kwamba ana hekima isiyo na kifani katika ulimwengu wote? Inapendeza kama nini kumkaribia Mungu huyu mtukufu ambaye ni mpole, mwenye subira, na mwenye kukubali sababu!
a Waandishi wa kale, au Wasoferi, walibadili mstari huu kusema kwamba ni Yeremia anayeinama wala si Yehova. Inaonekana kwamba walidhani haifai kusema kwamba Mungu alitenda kitendo hicho cha unyenyekevu. Ndiyo sababu tafsiri nyingi zinakosa maana ya mstari huu wenye kupendeza. Hata hivyo, The New English Bible inasema kwa usahihi kwamba Yeremia alimwambia Mungu hivi: “Kumbuka, Ee kumbuka, na uniinamie.”
b Tafsiri nyingine husema “unyenyekevu unaotokana na hekima” na “upole ambao ni wonyesho muhimu wa hekima.”
c Biblia inaonyesha kwamba subira ni kinyume cha kiburi. (Mhubiri 7:8) Subira ya Yehova inathibitisha hata zaidi kwamba yeye ni mnyenyekevu.—2 Petro 3:9.
d Zaburi 86:5 inasema kwamba Yehova ni ‘mwema na yuko tayari kusamehe.’ Zaburi hiyo ilipotafsiriwa katika Kigiriki, usemi “tayari kusamehe” ulitafsiriwa e·pi·ei·kesʹ, au “mwenye kukubali sababu.”
-
-
Yesu Afunua “Hekima Kutoka kwa Mungu”Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 21
Yesu Afunua “Hekima Kutoka kwa Mungu”
1-3. Majirani wa awali wa Yesu waliitikiaje mafundisho yake, na hawakutambua nini kumhusu?
WASIKILIZAJI walistaajabu. Kijana Yesu alikuwa amesimama mbele yao katika sinagogi akiwafundisha. Walimfahamu sana kwa sababu alikulia na kufanya kazi ya useremala katika mji wao kwa miaka mingi. Huenda baadhi yao waliishi katika nyumba ambazo Yesu alisaidia kujenga, au huenda walilima mashamba yao kwa plau na nira ambazo Yesu alitengeneza.a Lakini je, wangekubali mafundisho ya mtu huyo aliyekuwa seremala hapo awali?
2 Watu wengi waliokuwa wakimsikiliza walistaajabu na kuuliza: “Mtu huyu alipata wapi hekima hii?” Walisema hivi pia: “Huyu si seremala mwana wa Maria?” (Mathayo 13:54-58; Marko 6:1-3) Kwa kusikitisha, watu hao waliokuwa majirani wa Yesu pindi fulani, walisababu hivi, ‘Huyu seremala ni mtu wa kawaida tu kama sisi.’ Walimkataa ingawa alinena maneno yenye hekima. Hawakujua kwamba alipewa hekima hiyo.
3 Yesu alipata wapi hekima hiyo? Alisema hivi: “Kile nifundishacho si changu, bali ni chake yeye aliyenituma.” (Yohana 7:16) Mtume Paulo alieleza kwamba Yesu “amekuwa kwetu hekima kutoka kwa Mungu.” (1 Wakorintho 1:30) Yehova anafunua hekima yake kupitia Mwanaye, Yesu. Ndiyo sababu Yesu alisema hivi: “Mimi na Baba ni mmoja.” (Yohana 10:30) Hebu tuchunguze sehemu tatu ambazo Yesu alionyesha “hekima kutoka kwa Mungu.”
Mafundisho Yake
4. (a) Ujumbe wa Yesu ulihusu nini hasa, na kwa nini ujumbe huo ulikuwa muhimu sana? (b) Kwa nini mashauri ya Yesu yalifaa na kuwafaidi wasikilizaji wake sikuzote?
4 Kwanza, fikiria mafundisho ya Yesu. Ujumbe wake ulihusu hasa “habari njema ya ufalme.” (Luka 4:43) Huo ulikuwa ujumbe muhimu sana kwa sababu Ufalme huo utatetea enzi kuu ya Yehova na kuwaletea wanadamu baraka za kudumu. Alipokuwa akifundisha, Yesu alitoa pia mashauri ya hekima kuhusu maisha ya kila siku. Alijithibitisha kuwa yule “Mshauri wa Ajabu” aliyetabiriwa. (Isaya 9:6) Kwa kweli, mashauri yake yalikuwa bora sana. Alijua Neno la Mungu na mapenzi yake kwa undani, alifahamu vyema utu wa wanadamu, naye aliwapenda sana. Kwa hiyo, sikuzote alitoa mashauri yaliyofaa ambayo yaliwafaidi wasikilizaji wake. Yesu alinena “semi za uhai udumuo milele.” Naam, mtu anayefuata mashauri yake atapata wokovu.—Yohana 6:68.
5. Yesu alizungumzia mambo gani katika Mahubiri ya Mlimani?
5 Mahubiri ya Mlimani yanaonyesha hekima isiyo na kifani ya mafundisho ya Yesu. Mahubiri hayo yaliyo katika Mathayo 5:3–7:27, yanaweza kutolewa kwa muda wa dakika 20 tu. Hata hivyo, yana mashauri yenye faida ya kudumu, yanayofaa sana leo sawa na yalivyofaa wakati yalipotolewa. Yesu alizungumzia mambo mengi mbalimbali, kutia ndani jinsi ya kuboresha mahusiano na wengine (5:23-26, 38-42; 7:1-5, 12), jinsi ya kuwa safi kiadili (5:27-32), na jinsi ya kuishi maisha yenye kusudi (6:19-24; 7:24-27). Lakini Yesu hakuwaambia tu wasikilizaji wake jinsi ya kuishi kwa hekima; aliwaonyesha kwa kuwaeleza, kwa kusababu nao, na kwa kuwapa uthibitisho.
6-8. (a) Yesu anataja sababu zipi nzuri za kuepuka mahangaiko? (b) Ni nini kinachoonyesha kwamba Shauri la Yesu lina hekima ya kutoka juu?
6 Kwa mfano, fikiria shauri la Yesu lenye hekima katika Mathayo sura ya 6 linaloonyesha jinsi ya kupambana na mahangaiko ya vitu vya kimwili. Yesu anatushauri hivi: “Komeni kuhangaikia nafsi zenu kuhusu ni nini mtakula au ni nini mtakunywa, au juu ya miili yenu kuhusu ni nini mtavaa.” (Mstari wa 25) Chakula na mavazi ni mahitaji ya lazima, na ni jambo la kawaida tu kuhangaikia vitu hivyo. Lakini Yesu anatuambia ‘tukome kuhangaikia’ vitu hivyo.b Kwa nini?
7 Msikilize Yesu anaposababu kwa njia yenye kusadikisha. Kwa kuwa Yehova ametupatia uhai na mwili, je, anaweza kushindwa kutuandalia chakula cha kuendeleza uhai huo na mavazi ya kujivika? (Mstari wa 25) Ikiwa Mungu anawalisha ndege na kuyapamba maua, basi, hatawatunza zaidi wanadamu wanaomwabudu! (Mstari wa 26, 28-30) Kwa kweli, haifai kuwa na mahangaiko yasiyofaa. Hatuwezi kuongeza muda wetu wa uhai hata kwa dhiraa moja kwa kuhangaika.c (Mstari wa 27) Tunawezaje kuepuka mahangaiko? Yesu anatushauri hivi: Endeleeni kuitanguliza ibada ya Mungu maishani mwenu. Wale wanaofanya hivyo wanaweza kuwa na uhakika kwamba Baba yao wa mbinguni ‘atawaongezea’ mahitaji yao ya kila siku. (Mstari wa 33) Mwishowe, Yesu atoa dokezo nzuri sana—usihangaikie mambo ya kesho. Mbona uzidishe mahangaiko ya leo kwa kuhangaikia mambo ya kesho? (Mstari wa 34) Licha ya hayo, mbona uhangaikie mambo ambayo huenda yasitukie kamwe? Tunaweza kuepuka maumivu makali ya moyoni tukifuata shauri hilo la hekima katika ulimwengu huu uliojaa mikazo.
8 Ni wazi kwamba shauri la Yesu linafaa sana leo kama lilivyofaa miaka 2,000 hivi iliyopita. Je, hilo halithibitishi kwamba hekima hiyo ni ya kutoka juu? Hata mashauri bora ya wanadamu huhitaji kurekebishwa au kubadilishwa baada ya muda kupita. Lakini, miaka nenda miaka rudi, mafundisho ya Yesu yangali yanatumika na ni yenye faida. Hilo halipaswi kutushangaza kwa sababu Mshauri huyo wa Ajabu alisema “semi za Mungu.”—Yohana 3:34.
Njia Yake ya Kufundisha
9. Askari fulani walisema nini kuhusu ufundishaji wa Yesu, na kwa nini hawakuwa wakitia chumvi?
9 Njia ya Yesu ya kufundisha ni sehemu ya pili inayoonyesha hekima ya Mungu. Pindi moja, askari fulani waliotumwa kumkamata Yesu walirudi mikono mitupu na kusema: “Hajasema kamwe mtu mwingine kama hivi.” (Yohana 7:45, 46) Hawakuwa wakitia chumvi. Yesu, ambaye ‘alitoka kwenye makao ya juu,’ alikuwa na ujuzi na uzoefu mwingi sana kuliko wanadamu wote waliopata kuishi. (Yohana 8:23) Hakuna mwanadamu yeyote aliyeweza kufundisha kama Yesu. Hebu fikiria njia mbili alizotumia Mwalimu huyo mwenye hekima.
“Umati ulistaajabishwa na njia yake ya kufundisha”
10, 11. (a) Kwa nini tunastaajabia jinsi Yesu alivyotumia vielezi? (b) Vielezi ni nini, na ni mfano upi unaoonyesha kwamba vielezi vya Yesu vina matokeo katika kufundisha?
10 Alitumia vielezi vinavyofaa. Twaambiwa kwamba ‘Yesu alisema na umati kwa vielezi. ‘Kwa kweli, bila kielezi hakuwa akisema nao.’ (Mathayo 13:34) Tunastaajabia uwezo wake usio na kifani wa kufundisha kweli muhimu kwa kutumia mambo ya kawaida. Alitumia mambo ambayo wasikilizaji wake walizoea, kama vile wakulima wanaopanda mbegu, wanawake wanaojitayarisha kuoka mikate, watoto wanaocheza sokoni, wavuvi wanaokokota nyavu, na wachungaji wanaotafuta kondoo waliopotea. Kweli muhimu zinapohusianishwa na mambo ya kawaida, zinatia mizizi mara moja katika akili na moyo.—Mathayo 11:16-19; 13:3-8, 33, 47-50; 18:12-14.
11 Mara nyingi Yesu alitumia vielezi au hadithi fupi ili kufundisha kweli za kiroho na za kiadili. Watu waliweza kukumbuka mafundisho ya Yesu kwa sababu hadithi fupi hueleweka na kukumbukwa kwa urahisi kuliko hoja za kuwaziwa tu. Katika vielezi vingi, Yesu alitumia mifano rahisi isiyosahaulika ili kuonyesha jinsi Baba yake alivyo. Kwa mfano, ni nani asiyeweza kuelewa maana ya kielezi cha mwana mpotevu—kwamba Yehova atamhurumia na kumkaribisha kwa upendo mtu aliyeasi anayetubu kikweli?—Luka 15:11-32.
12. (a) Yesu alitumiaje maswali alipofundisha? (b) Yesu aliwanyamazishaje wale waliotilia shaka mamlaka yake?
12 Alitumia maswali kwa ustadi. Yesu alitumia maswali ili kuwasaidia wasikilizaji wake wafikie mikataa yao wenyewe, wachunguze madhumuni yao, au wafanye maamuzi. (Mathayo 12:24-30; 17:24-27; 22:41-46) Viongozi wa kidini walipotilia shaka mamlaka aliyopewa na Mungu, Yesu aliwauliza: “Je, ubatizo wa Yohana ulikuwa wa kutoka mbinguni au wa kutoka kwa wanadamu?” Swali hilo liliwaduwaza, wakaanza kusababu hivi miongoni mwao: “Tukisema, ‘Kutoka mbinguni,’ atatuambia, ‘Basi, kwa nini hamkumwamini?’ Ingawa hivyo, tukisema, ‘Kutoka kwa wanadamu,’ tunao umati kuuhofu, kwa maana wao wote wamchukua Yohana kuwa nabii.” Hatimaye, wakajibu: “Hatujui.” (Marko 11:27-33; Mathayo 21:23-27) Yesu aliwauliza swali rahisi ambalo liliwanyamazisha na kufunua unafiki wao.
13-15. Hadithi ya Msamaria mwema inaonyeshaje hekima ya Yesu?
13 Nyakati nyingine Yesu alitumia mbinu mbalimbali kwa pamoja, alitoa vielezi na kuuliza maswali yenye kuchochea fikira. Mwanasheria mmoja Myahudi alipomwuliza Yesu jambo ambalo alipaswa kufanya ili apate uhai wa milele, Yesu alimkumbusha Sheria ya Musa ambayo inawaamuru watu wampende Mungu na jirani. Mtu huyo aliuliza hivi ili kujithibitisha kuwa mwadilifu: “Ni nani kwa kweli aliye jirani yangu?” Yesu alimjibu kwa kusimulia hadithi. Myahudi fulani alikuwa akisafiri peke yake aliposhambuliwa na wanyang’anyi na kuachwa akiwa mahututi. Wayahudi wawili walimpita, kwanza kuhani kisha Mlawi. Wote wakampuuza. Lakini baadaye Msamaria fulani alipitia hapo na kumwona. Kwa huruma nyingi, alifunga kwa uangalifu majeraha ya mtu huyo na akaonyesha upendo kwa kumpeleka kwenye nyumba ndogo ya wageni ili apate nafuu. Alipomaliza hadithi hiyo, Yesu alimwuliza yule mwanasheria hivi: “Ni nani kati ya watatu hawa aonekana kwako kuwa alijifanya mwenyewe jirani kwa mtu aliyeanguka miongoni mwa wapokonyaji?” Mwanasheria huyo hakuwa na budi kujibu: “Yeye aliyetenda kwa rehema kumwelekea.”—Luka 10:25-37.
14 Hadithi hiyo inaonyeshaje hekima ya Yesu? Katika siku za Yesu, Wayahudi walitumia neno “jirani” kuwarejelea tu wale waliofuata mapokeo yao, na bila shaka hawakuwaona Wasamaria kuwa “jirani.” (Yohana 4:9) Kama Yesu angesema kwamba Msamaria ndiye aliyeshambuliwa na akasaidiwa na Myahudi, je, hilo lingekomesha ubaguzi wao? Kwa hekima, Yesu alitunga hadithi hiyo kwa njia ya kwamba Msamaria ndiye anayemtunza kwa upendo Myahudi. Fikiria pia swali ambalo Yesu aliuliza baada ya kusimulia hadithi hiyo. Alionyesha maana nyingine ya neno “jirani.” Ni kana kwamba yule mwanasheria aliuliza: ‘Ni nani jirani ninayepaswa kumpenda?’ Lakini Yesu akamwuliza: “Ni nani kati ya watatu hawa aonekana kwako kuwa alijifanya mwenyewe jirani?” Yesu alikazia fikira yule Msamaria aliyeonyesha fadhili, wala si yule Myahudi aliyeonyeshwa fadhili. Jirani wa kweli huchukua hatua ya kuwapenda wengine bila kujali kabila lao. Yesu alifundisha somo hilo kwa njia bora kabisa.
15 Haishangazi kwamba watu walivutiwa na Yesu na kustaajabia “njia yake ya kufundisha.” (Mathayo 7:28, 29) Pindi moja, “umati mkubwa” ulikaa naye kwa siku tatu bila kula!—Marko 8:1, 2.
Maisha Yake
16. Yesu ‘alithibitishaje’ kwamba aliongozwa na hekima ya Mungu?
16 Maisha ya Yesu ni sehemu ya tatu inayoonyesha hekima ya Yehova. Hekima huonyeshwa kwa matendo; inazaa matunda. Mwanafunzi Yakobo aliuliza: “Ni nani mwenye hekima miongoni mwenu?” Kisha akajibu swali hilo kwa kusema: “Basi, mwenendo wake bora uthibitishe jambo hilo.” (Yakobo 3:13, The New English Bible) Mwenendo wa Yesu ‘ulithibitisha’ kwamba aliongozwa na hekima ya Mungu. Hebu tuone jinsi alivyotumia busara maishani mwake na aliposhughulika na wengine.
17. Ni nini kinachoonyesha kwamba Yesu alikuwa na usawaziko kamili maishani?
17 Je, umeona kwamba mara nyingi watu wasio na busara hupita kiasi? Naam, mtu anahitaji hekima ili kuwa na usawaziko. Yesu alionyesha hekima ya Mungu kwa kuwa na usawaziko kamili. Zaidi ya yote, alitanguliza mambo ya kiroho maishani mwake. Alijishughulisha sana na kazi ya kutangaza habari njema. “Ni kwa kusudi hilo nimetokea,” akasema. (Marko 1:38) Bila shaka, vitu vya kimwili havikuwa muhimu sana kwake; inaonekana kwamba alikuwa na vitu vichache sana. (Mathayo 8:20) Hata hivyo, hakujinyima starehe. Yesu alikuwa mwenye shangwe kama Baba yake, ambaye ni “Mungu mwenye furaha,” naye alizidisha shangwe ya wengine. (1 Timotheo 1:11; 6:15) Yesu hakuhudhuria karamu ya arusi—ambayo kwa kawaida huwa na muziki, uimbaji, na furaha—ili awaharibie wengine starehe. Divai ilipokwisha, aligeuza maji yakawa divai bora, kinywaji ambacho ‘kinaufurahisha moyo wa mtu.’ (Zaburi 104:15; Yohana 2:1-11) Yesu alikubali mialiko mingi ya chakula, na mara nyingi alitumia pindi hizo kufundisha.—Luka 10:38-42; 14:1-6.
18. Yesu alishughulikaje na wanafunzi wake kwa njia ya busara?
18 Yesu alishughulika na wengine kwa njia ya busara. Aliwajua wanafunzi wake vizuri kwa sababu alifahamu kabisa utu wa wanadamu. Alijua kwamba hawakuwa wakamilifu. Lakini, alitambua sifa zao nzuri. Alitambua kwamba wanafunzi hao waliovutwa na Yehova wangeweza kufanya mengi. (Yohana 6:44) Yesu alikuwa tayari kuwatumaini licha ya kasoro zao. Kwa mfano, alionyesha kwamba aliwatumaini wanafunzi wake kwa kuwakabidhi daraka zito. Aliwaagiza wahubiri habari njema, na alikuwa na hakika kwamba wangeweza kutimiza kazi hiyo. (Mathayo 28:19, 20) Kitabu cha Matendo kinathibitisha kwamba walitimiza kwa uaminifu kazi ambayo aliwaamuru wafanye. (Matendo 2:41, 42; 4:33; 5:27-32) Basi ni wazi kwamba Yesu alionyesha hekima kwa kuwatumaini.
19. Yesu alionyeshaje kwamba alikuwa “mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni”?
19 Kama tulivyoona kwenye Sura ya 20, Biblia inaonyesha kwamba unyenyekevu na upole zinahusiana na sifa ya hekima. Bila shaka, Yehova ndiye mfano bora kabisa wa sifa hizo. Lakini vipi Yesu? Inapendeza kuona jinsi Yesu alivyoshughulika na wanafunzi wake kwa unyenyekevu. Alikuwa bora kuliko wanafunzi wake kwa sababu alikuwa mkamilifu. Lakini, hakuwadharau wanafunzi wake. Hakujaribu kamwe kuwafanya wajione hawafai au wao ni bure tu. Kinyume chake, alijua udhaifu wao na alikuwa mwenye subira walipokosea. (Marko 14:34-38; Yohana 16:12) Je, haipendezi kwamba hata watoto walifurahi sana kuwa na Yesu? Bila shaka, walivutiwa naye kwa sababu waliona kwamba alikuwa “mwenye tabia-pole na wa hali ya chini moyoni.”—Mathayo 11:29; Marko 10:13-16.
20. Yesu alionyeshaje kwamba anasikiliza maoni ya wengine aliposhughulika na yule mwanamke asiye Myahudi ambaye alikuwa na binti aliyesumbuliwa na roho waovu?
20 Yesu aliiga unyenyekevu wa Mungu kwa njia nyingine muhimu. Alizingatia maoni ya wengine, wakati ilipofaa kuonyesha rehema. Kwa mfano, kumbuka wakati mwanamke fulani asiye Myahudi alipomsihi Yesu amponye binti yake aliyesumbuliwa sana na roho waovu. Mwanzoni, Yesu alionyesha kwa njia tatu kwamba hangemsaidia—kwanza, hakumjibu; pili, alimwambia moja kwa moja kwamba alikuwa ametumwa kwa Wayahudi wala si kwa wasio Wayahudi; na tatu, alitoa mfano ambao ulikazia kwa fadhili jambo hilo. Hata hivyo, mwanamke huyo hakuchoka, alionyesha kwamba alikuwa na imani ya pekee sana. Yesu alifanya nini kuhusiana na kisa hicho cha pekee? Alifanya jambo ambalo alikuwa amesema hangefanya. Alimponya binti ya mwanamke huyo. (Mathayo 15:21-28) Huo ni unyenyekevu wa pekee sana, sivyo? Kumbuka kwamba unyenyekevu ndio msingi wa hekima ya kweli.
21. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kuiga utu, usemi, na njia ya Yesu ya kutenda mambo?
21 Tunashukuru kama nini kwamba Vitabu vya Injili vinatujulisha maneno na matendo ya mtu mwenye hekima zaidi aliyepata kuishi! Na tukumbuke kwamba Yesu alimwiga Baba yake kikamili. Tukiiga utu, usemi, na njia ya Yesu ya kutenda mambo, tutakuwa tukikuza hekima ya kutoka juu. Katika sura ifuatayo, tutaona jinsi tunavyoweza kutumia hekima ya Mungu maishani mwetu.
a Katika nyakati za Biblia, maseremala walijenga nyumba, walitengeneza fanicha, na vifaa vya kilimo. Justin Martyr, aliyeishi katika karne ya pili W.K., aliandika hivi kumhusu Yesu: “Alikuwa seremala maarufu aliyetengeneza plau na nira alipokuwa duniani.”
b Kitenzi cha Kigiriki kinachotafsiriwa “hangaikia” kinamaanisha “kukengeushwa fikira.” Katika Mathayo 6:25, neno hilo linamaanisha woga na wasiwasi ambao unakengeusha au kupotosha fikira, na kumfanya mtu akose shangwe maishani.
c Uchunguzi wa sayansi umeonyesha kwamba kuhangaika na kufadhaika kupita kiasi kwaweza kusababisha ugonjwa wa moyo na magonjwa mengine yanayoweza kusababisha kifo.
-
-
Je, “Hekima ya Kutoka Juu” Inakuongoza Maishani?Mkaribie Yehova
-
-
Sura ya 22
Je, “Hekima ya Kutoka Juu” Inakuongoza Maishani?
1-3. (a) Solomoni alionyeshaje hekima ya pekee katika kuamua ni nani aliyekuwa mama ya mtoto? (b) Yehova anaahidi kutupatia nini, na ni maswali gani yanayozuka?
ILIKUWA kesi ngumu sana—wanawake wawili walibishania mtoto mmoja mchanga. Wanawake hao waliishi pamoja, na mmoja wao alijifungua mwana siku chache tu baada ya mwingine kujifungua. Mtoto mmoja alikuwa amekufa, na kila mwanamke alidai kwamba mtoto aliyekuwa hai alikuwa wake.a Hapakuwa na watu wengine walioshuhudia lililotukia. Yaelekea kwamba kesi hiyo ilikuwa imesikilizwa katika mahakama ya chini lakini haikusuluhishwa. Mwishowe, kesi hiyo ilipelekwa kwa Solomoni, mfalme wa Israeli. Je, angefunua ukweli wa mambo?
2 Baada ya kuwasikiliza wanawake hao wakibishana kwa muda, Solomoni aliomba upanga. Kisha, akaamuru mtoto huyo akatwe vipande viwili na kila mwanamke apewe kipande kimoja. Mara moja mama ya mtoto huyo akamsihi mfalme amkabidhi yule mwanamke mwingine mtoto wake mpendwa. Lakini mwanamke yule mwingine aliendelea kusisitiza mtoto huyo akatwe vipande viwili. Sasa Solomoni akajua ukweli wa mambo. Alijua jinsi ambavyo mama humhurumia na kumpenda sana mtoto wake, naye alitumia ujuzi huo kutatua kesi hiyo. Hebu wazia furaha ya mama huyo Solomoni alipompa mtoto wake na kusema: “Yeye ndiye mama yake.”—1 Wafalme 3:16-27.
3 Solomoni alikuwa na hekima ya pekee, sivyo? Watu walistaajabu sana waliposikia jinsi Solomoni alivyosuluhisha kesi hiyo, “maana waliona ya kuwa hekima ya Mungu ilikuwa ndani yake.” Naam, hekima ya Solomoni ilikuwa zawadi kutoka kwa Mungu. Yehova alikuwa amempa “moyo wa hekima na wa akili.” (1 Wafalme 3:12, 28) Lakini vipi sisi? Je, Mungu anaweza pia kutupatia hekima? Ndiyo. Solomoni aliongozwa kuandika hivi: “BWANA huwapa watu hekima.” (Mithali 2:6) Yehova aahidi kuwapa hekima, yaani, uwezo wa kutumia ujuzi, ufahamu, na utambuzi, wale wanaoitafuta kwa unyofu. Tunawezaje kupata hekima inayotoka juu? Na tutaitumiaje maishani mwetu?
Unawezaje ‘Kujipatia Hekima’?
4-7. Ni matakwa gani manne yanayohitajiwa ili kujipatia hekima?
4 Je, ni lazima tuwe na akili nyingi au elimu ya juu ili Mungu atupatie hekima yake? La. Yehova yu tayari kutupatia hekima bila kujali malezi au elimu yetu. (1 Wakorintho 1:26-29) Lakini ni lazima tuchukue hatua fulani, kwa sababu Biblia inatuhimiza ‘tujipatie hekima.’ (Mithali 4:7) Tutajipatiaje hekima?
5 Kwanza, ni lazima tumhofu Mungu. “Kumhofu Yehova ni mwanzo wa hekima [“hatua ya kwanza ya kupata hekima,” The New English Bible],” yasema Mithali 9:10, NW. Kumhofu Mungu ndio msingi wa hekima ya kweli. Kwa nini? Kumbuka kwamba hekima inatia ndani uwezo wa kutumia ujuzi kwa mafanikio. Kumhofu Mungu si kutetemeka kwa wasiwasi, bali ni kumsujudia kwa kicho, heshima, na kumtumaini. Hofu ya aina hiyo inafaa na humchochea sana mtu. Hutuchochea kuishi kupatana na ujuzi tulio nao kuhusu mapenzi ya Mungu na njia zake. Hilo ndilo jambo la hekima zaidi tuwezalo kufanya, kwa sababu sikuzote kanuni za Yehova huwafaidi kabisa wale wanaozifuata.
6 Pili, ni lazima tuwe wanyenyekevu na wenye kiasi. Hatuwezi kuwa na hekima ya Mungu tusipokuwa wanyenyekevu na wenye kiasi. (Mithali 11:2) Kwa nini? Tukiwa wanyenyekevu na wenye kiasi, tutakuwa tayari kukubali kwamba hatujui kila jambo. Tutakubali kwamba nyakati nyingine maoni yetu si sawa na hivyo tunahitaji kujifunza maoni ya Yehova. Yehova “huwapinga wenye kiburi,” lakini hufurahi kuwapa hekima wale walio wanyenyekevu moyoni.—Yakobo 4:6.
Ili kupata hekima ya Mungu, ni lazima tuitafute kwa bidii
7 Jambo la tatu muhimu ni kujifunza Neno la Mungu. Hekima ya Yehova imefunuliwa katika Neno lake. Ili kupata hekima hiyo, ni lazima tujitahidi kabisa kuitafuta. (Mithali 2:1-5) Takwa la nne ni sala. Tukimwomba Yehova hekima kwa unyofu, atatupatia kwa ukarimu. (Yakobo 1:5) Tukiomba msaada wa roho yake hatakosa kujibu sala zetu. Na roho yake itatuongoza kupata hazina zilizo katika Neno lake ambazo zinaweza kutusaidia kutatua matatizo, kuepuka hatari, na kufanya maamuzi ya hekima.—Luka 11:13.
8. Ni nini kitakachoonyesha kwamba tumejipatia hekima ya Mungu?
8 Kama tulivyoona katika Sura ya 17, hekima ya Yehova inazaa matunda. Kwa hiyo, mwenendo wetu utaonyesha wazi kwamba tumejipatia hekima ya Mungu. Mwanafunzi Yakobo alitaja sifa za hekima ya Mungu alipoandika hivi: “Hekima ya kutoka juu kwanza kabisa ni safi kiadili, kisha yenye kufanya amani, yenye kukubali sababu, tayari kutii, yenye kujaa rehema na matunda mema, isiyofanya tofauti zenye ubaguzi, si ya kinafiki.” (Yakobo 3:17) Tunapozungumzia kila moja ya sifa hizo za hekima ya Mungu, huenda tukajiuliza, ‘Je, hekima ya kutoka juu inaniongoza maishani?’
“Ni Safi Kiadili, Kisha Yenye Kufanya Amani”
9. Kuwa safi kiadili kwamaanisha nini, na kwa nini inafaa kwamba usafi wa kiadili ndiyo sifa inayotajwa kwanza katika orodha ya sifa za hekima?
9 “Kwanza kabisa ni safi kiadili.” Kuwa safi kiadili kwamaanisha kutakata na kuwa bila unajisi, si kwa nje tu bali pia moyoni. Biblia inahusianisha hekima na moyo, lakini hekima itokayo mbinguni haiwezi kuingia katika moyo uliotiwa unajisi na tamaa na mawazo maovu, na nia mbovu. (Mithali 2:10; Mathayo 15:19, 20) Lakini, kama moyo wetu ni safi kiadili—yaani, kwa kadiri ambavyo wanadamu wasiokamilika wanaweza kuwa safi—‘tutajiepusha na uovu na tutatenda mema.’ (Zaburi 37:27; Mithali 3:7) Kwa kufaa, usafi wa kiadili unatajwa kwanza katika orodha ya sifa za hekima. Hatuwezi kuwa na sifa nyingine za hekima ya kutoka juu tusipokuwa safi kiadili na kiroho.
10, 11. (a) Kwa nini ni muhimu tuwe watu wanaofanya amani? (b) Ukigundua kwamba umemkosea mwabudu mwenzako, utaonyeshaje kwamba wewe ni mtu anayefanya amani? (Ona pia kielezi-chini.)
10 “Kisha yenye kufanya amani.” Hekima ya kutoka mbinguni hutuchochea kufuatia amani, ambayo ni tunda la roho ya Mungu. (Wagalatia 5:22) Tunajitahidi sana kutoharibu ‘kifungo cha amani’ kinachowaunganisha watu wa Yehova. (Waefeso 4:3) Sisi pia hujitahidi kabisa kurudisha amani inapovurugwa. Kwa nini ni muhimu kufanya hivyo? Biblia inasema: “Endeleeni . . . kuishi kwa kufanya amani; na Mungu wa upendo na amani atakuwa pamoja nanyi.” (2 Wakorintho 13:11) Mungu wa amani atakuwa pamoja nasi maadamu tunaendelea kufanya amani. Uhusiano wetu na Yehova unategemea jinsi tunavyowatendea waabudu wenzetu. Tunawezaje kuwa watu wanaofanya amani? Fikiria mfano ufuatao.
11 Unapaswa kufanya nini ukigundua kwamba umemkosea mwabudu mwenzako? Yesu alisema: “Basi, ikiwa wewe unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na huko wakumbuka kwamba ndugu yako ana jambo fulani dhidi yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, toa zawadi yako.” (Mathayo 5:23, 24) Unaweza kutumia shauri hilo kwa kuchukua hatua ya kwenda kumwona ndugu yako. Ukiwa na kusudi gani? Ili ‘ufanye amani yako’ naye.b Ili kutimiza kusudi hilo, huenda ukahitaji kukubali kwamba umemwumiza kihisia. Ukimfikia kwa kusudi la kufanya amani na udumishe mtazamo huo, yaelekea kwamba tatizo litasuluhishwa, utaomba msamaha na utasamehewa. Unapochukua hatua ya kufanya amani, unaonyesha kwamba unaongozwa na hekima ya Mungu.
“Yenye Kukubali Sababu, Tayari Kutii”
12, 13. (a) Neno linalotafsiriwa “-enye kukubali sababu” katika Yakobo 3:17 linamaanisha nini? (b) Tunawezaje kuonyesha kwamba sisi ni wenye kukubali sababu?
12 “Yenye kukubali sababu.” Ni nini maana ya kukubali sababu? Wasomi wa Biblia wanasema kwamba si rahisi kutafsiri neno la awali la Kigiriki linalotafsiriwa “-enye kukubali sababu” kwenye Yakobo 3:17. Watafsiri wametumia maneno kama vile “upole,” “ustahimilivu,” na “mwenye kujali.” Neno la Kigiriki linamaanisha kihalisi “mwenye kukubali maoni ya wengine.” Tunawezaje kuonyesha kwamba tunaongozwa na sifa hiyo ya hekima ya kutoka juu?
13 Andiko la Wafilipi 4:5 lasema: “Hali yenu ya kukubali sababu na ijulikane kwa watu wote.” Tafsiri nyingine inasema: “Mjulikane kuwa watu wenye kukubali sababu.” (The New Testament in Modern English, ya J. B. Phillips) Ona kwamba jambo muhimu si jinsi tunavyojiona; bali ni jinsi wengine wanavyotuona. Mtu mwenye kukubali sababu hafuatilii mambo madogo-madogo ya sheria au hasisitizi mambo yafanywe jinsi anavyopenda. Badala yake, yuko tayari kuwasikiliza wengine na kukubali maoni yao inapowezekana. Yeye pia ni mpole, si mkali au mkatili. Hiyo ni sifa muhimu kwa Wakristo wote, lakini hasa kwa wazee wa kutaniko. Upole huvutia, kwa hiyo watu hujihisi huru kuongea na wazee wapole. (1 Wathesalonike 2:7, 8) Ni muhimu sote tujiulize hivi: ‘Je, wengine huniona kuwa mtu mwenye kuwajali wengine, mwenye kukubali sababu, na mpole?’
14. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tuko “tayari kutii”?
14 “Tayari kutii.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “tayari kutii” linapatikana mara moja tu katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo. Msomi mmoja anasema kwamba neno hilo “hutumiwa mara nyingi kuhusiana na nidhamu ya kijeshi.” Linaweza kumaanisha “mtu anayeshawishiwa kwa urahisi” na “mtiifu.” Mtu anayeongozwa na hekima ya kutoka juu huwa tayari kutii Maandiko. Hashikilii sana maoni yake na kukataa hoja zozote ambazo zinapinga maoni yake. Badala yake, yeye hubadili maoni mara moja anapothibitishiwa kwa Maandiko kwamba amefanya uamuzi mbaya au maoni yake ni yenye kosa. Je, ndivyo wengine wanavyokuona?
“Yenye Kujaa Rehema na Matunda Mema”
15. Rehema ni nini, na kwa nini inafaa kwamba andiko la Yakobo 3:17 linataja “rehema” pamoja na “matunda mema”?
15 “Yenye kujaa rehema na matunda mema.”c Rehema ni sifa muhimu ya hekima ya kutoka juu, kwa sababu inasemekana kwamba hekima hiyo ‘imejaa rehema.’ Ona kwamba “rehema” inatajwa pamoja na “matunda mema.” Jambo hilo linafaa kwa sababu katika Biblia, mara nyingi rehema humaanisha kuwajali sana wengine na kuwatendea mambo mengi ya fadhili kwa huruma. Kichapo kimoja cha marejeo chafafanua rehema kuwa “hali ya kuhuzunishwa na hali mbaya ya mtu mwingine na kujaribu kumsaidia.” Kwa hiyo, hekima ya Mungu si baridi wala haitegemei akili tu. Badala yake, ni yenye upendo na huruma, na inawajali wengine. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tumejaa rehema?
16, 17. (a) Mbali na kumpenda Mungu, ni nini kinachotuchochea tushiriki kazi ya kuhubiri, na kwa nini? (b) Ni katika njia zipi tunaweza kuonyesha kwamba tumejaa rehema?
16 Bila shaka njia bora ya kuonyesha sifa hiyo ni kuwahubiria wengine habari njema za Ufalme wa Mungu. Ni nini kinachotuchochea kufanya kazi hiyo? Hasa ni kwa sababu tunampenda Mungu. Tunachochewa pia na rehema, au huruma. (Mathayo 22:37-39) Watu wengi leo ‘wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.’ (Mathayo 9:36) Wamepuuzwa na kupofushwa kiroho na wachungaji wa uwongo wa kidini. Ndiyo sababu hawajui mwongozo wenye hekima ulio katika Neno la Mungu wala hawajui baraka zitakazoletwa duniani na Ufalme huo hivi karibuni. Kwa hiyo, tunapozingatia mahitaji ya kiroho ya jirani zetu, tunachochewa na huruma kutoka moyoni kujitahidi kadiri tuwezavyo kuwaambia kusudi la Yehova lenye upendo.
Tunapowaonyesha wengine rehema, au huruma, tunadhihirisha “hekima ya kutoka juu”
17 Ni katika njia zipi nyingine tunaweza kuonyesha kwamba tumejaa rehema? Kumbuka mfano wa Yesu wa yule Msamaria aliyemkuta msafiri fulani aliyelala kando ya barabara baada ya kupigwa na kuporwa. Msamaria huyo alimhurumia na ‘akatenda kwa rehema.’ Alimfunga majeraha na kumtunza. (Luka 10:29-37) Mfano huo waonyesha kwamba kuwa na rehema kwahusisha kuwasaidia wenye uhitaji. Biblia inatuambia “tufanye lililo jema kuelekea wote, lakini hasa kuelekea wale ambao katika imani ni jamaa zetu.” (Wagalatia 6:10) Fikiria mifano kadhaa. Huenda mwamini mwenzako aliye mzee kwa umri anahitaji kusaidiwa kusafiri kwenda kwenye mikutano ya Kikristo na kurudi. Huenda mjane fulani kutanikoni anahitaji kusaidiwa kurekebisha nyumba yake. (Yakobo 1:27) Huenda mtu fulani aliyeshuka moyo anahitaji kuambiwa “neno jema” la kumfariji. (Mithali 12:25) Tunapoonyesha rehema katika njia hizo, tunathibitisha kwamba tunaongozwa na hekima ya kutoka juu.
‘Isiyobagua, Si ya Kinafiki’
18. Ikiwa tunaongozwa na hekima ya kutoka juu, tunapaswa kujitahidi kuondoa nini mioyoni mwetu, na kwa nini?
18 “Isiyobagua.” Hekima ya Mungu hushinda kabisa ubaguzi wa kikabila na uzalendo. Ikiwa tunaongozwa na hekima hiyo, tunapaswa kujitahidi kuondoa kabisa mioyoni mwetu mwelekeo wowote wa kuonyesha upendeleo. (Yakobo 2:9) Hatuwapendelei watu fulani kwa sababu ya elimu yao, utajiri wao, au madaraka yao kutanikoni; wala hatumdharau mwabudu mwenzetu, hata ikiwa anaonekana kuwa na cheo cha chini sana katika jamii. Ikiwa Yehova anawapenda watu hao, hapana shaka kwamba sisi tunapaswa kuwapenda pia.
19, 20. (a) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mnafiki” latokana na nini? (b) Tunaonyeshaje “shauku ya kidugu isiyo na unafiki,” na kwa nini jambo hilo ni muhimu?
19 “Si ya kinafiki.” Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mnafiki” linaweza kurejelea “mwigizaji katika mchezo wa kuigiza.” Katika nyakati za kale, waigizaji Wagiriki na Waroma walivaa vinyago vikubwa usoni katika michezo ya kuigiza. Kwa hiyo, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “mnafiki” likaanza kutumiwa kumaanisha mtu anayejifanya, au mtu anayejisingizia. Hekima ya Mungu inapaswa kuongoza jinsi tunavyowatendea waabudu wenzetu na pia jinsi tunavyowaona.
20 Mtume Petro alisema kwamba ‘tukitii ile kweli’ tutakuwa na “shauku ya kidugu isiyo na unafiki.” (1 Petro 1:22) Naam, shauku yetu kwa ndugu zetu haipaswi kuwa ya kujionyesha tu. Hatujifanyi wala kujisingizia ili tuwadanganye wengine. Ni lazima shauku yetu iwe ya kweli, ya kutoka moyoni. Tukiwa na shauku ya aina hiyo, waamini wenzetu watatuamini kwa sababu watajua kwamba sisi si wanafiki. Unyofu wa aina hiyo hutokeza uhusiano mzuri kati ya Wakristo na pia huchangia hali ya kuaminiana kutanikoni.
“Shika Hekima Kamili”
21, 22. (a) Solomoni alishindwaje kushika hekima kamili? (b) Tunawezaje kushika hekima, na tutapata faida gani tukifanya hivyo?
21 Tunahitaji kushika hekima kwa sababu ni zawadi kutoka kwa Yehova. Solomoni alisema: “Mwanangu, . . . shika hekima kamili na busara.” (Mithali 3:21) Kwa kusikitisha, Solomoni mwenyewe alishindwa kufanya hivyo. Alikuwa mwenye hekima maadamu alitii kutoka moyoni. Lakini mwishowe, wake zake wengi wa kigeni waliugeuza moyo wake kutoka kwa ibada safi ya Yehova. (1 Wafalme 11:1-8) Hali iliyompata Solomoni inaonyesha kwamba tusipotumia ifaavyo ujuzi tulio nao hautatufaidi.
22 Tunawezaje kushika hekima kamili? Haitoshi tu kusoma kwa ukawaida Biblia na vichapo vya Biblia vinavyotayarishwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” Ni lazima pia tujitahidi kutumia mambo tunayojifunza. (Mathayo 24:45) Tuna kila sababu ya kutumia hekima ya Mungu. Tukifanya hivyo, tutakuwa na maisha bora sasa. Inatuwezesha “kuwa na mshiko imara juu ya uhai ulio halisi,” yaani, uhai katika ulimwengu mpya wa Mungu. (1 Timotheo 6:19) Na jambo la muhimu hata zaidi ni kwamba tunapokuza hekima ya kutoka juu tunamkaribia zaidi Yehova Mungu, chanzo cha hekima yote.
a Andiko la 1 Wafalme 3:16 linasema kwamba wanawake hao walikuwa makahaba. Kichapo Insight on the Scriptures chasema: “Huenda wanawake hao hawakuwa makahaba wa kulipwa bali walikuwa wamefanya uasherati. Labda walikuwa wanawake Wayahudi au wanawake wa kigeni.”—Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
b Usemi wa Kigiriki unaotafsiriwa “fanya amani yako” unatokana na kitenzi kinachomaanisha “‘kuleta badiliko, kubadilishana,’ na hivyo, ‘kupatanisha.’” Kwa hiyo, kusudi lako ni kubadilisha hali, na ikiwezekana, kuondoa chuki iliyo moyoni mwa yule aliyekosewa.—Waroma 12:18.
c Biblia Habari Njema inatafsiri hivi maneno hayo: “Imejaa huruma na huzaa matunda ya matendo mema.”
-