-
“Wamtafute Mungu, . . . na kwa Kweli Wampate”“Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
-
-
SURA YA 18
“Wamtafute Mungu, . . . na kwa Kweli Wampate”
Paulo aweka msingi mzuri wa mazungumzo na kubadilika kulingana na hali ya wasikilizaji wake
1-3. (a) Ni nini kilichomkasirisha mtume Paulo akiwa Athene? (b) Tunaweza kujifunza nini kwa kuchunguza mfano wa Paulo?
PAULO amekasirika sana. Yuko jijini Athene, kitovu cha elimu nchini Ugiriki, ambako wakati fulani wanafalsafa kama vile Sokratesi, Plato, na Aristoto walifundisha. Athene ni jiji la kidini. Pande zote—mahekaluni, katika viwanja vya watu wote, na barabarani—Paulo anaona sanamu nyingi, kwa sababu Waathene huabudu miungu mingi sana. Paulo anajua maoni ya Mungu wa kweli, Yehova, kuhusiana na ibada ya sanamu. (Kut. 20:4, 5) Mtume huyo mwaminifu ana maoni kama ya Yehova—anachukia sanamu!
2 Paulo anashangazwa sana na mambo anayoona anapoingia sokoni. Kuna sanamu nyingi za mungu Herme zenye umbo la kiungo cha uzazi cha kiume zilizowekwa upande wa kaskazini-magharibi, karibu na lango kuu. Soko hilo lina madhabahu nyingi. Mtume huyo mwenye bidii atahubiri jinsi gani katika jiji hilo ambalo ibada ya sanamu imekita mizizi? Je, ataonyesha sifa ya kujizuia na kuweka msingi mzuri wa mazungumzo kwa wasikilizaji wake? Je, atafaulu kumsaidia yeyote amtafute Mungu wa kweli na kumwabudu?
3 Hotuba ya Paulo, iliyo katika Matendo 17:22-31, ambayo aliitoa mbele za watu hao wenye elimu inaonyesha kwamba alitumia ushawishi, busara, na utambuzi. Mfano wa Paulo unaweza kutusaidia sana kujua jinsi ya kuweka msingi mzuri wa mazungumzo na kuwasaidia wasikilizaji wetu kufikiri.
Kufundisha “Sokoni” (Mdo. 17:16-21)
4, 5. Paulo alihubiri wapi akiwa Athene, naye alikutana na watu wa aina gani?
4 Katika safari yake ya pili ya umishonari, mwaka wa 50 hivi W.K., Paulo alitembelea jiji la Athene.a Alipokuwa akiwasubiri Sila na Timotheo wafike kutoka Beroya, Paulo “akaanza kujadiliana katika sinagogi pamoja na Wayahudi,” kama ilivyokuwa desturi yake. Pia alienda “sokoni,” mahali ambapo angeweza kuwapata watu wa Athene wasio Wayahudi. (Mdo. 17:17) Soko hilo lililokuwa na ukubwa wa ekari 12 hivi, lilikuwa upande wa kaskazini-magharibi mwa Ngome ya Athene. Halikuwa mahali pa kuuza na kununua tu, bali pia uwanja wa watu wote. Kitabu fulani cha marejeo kinasema kwamba mahali hapo palikuwa “kituo cha kibiashara, kisiasa na kitamaduni jijini humo.” Waathene walipenda kukusanyika hapo na kuzungumzia mambo mbalimbali ya kitaalamu.
5 Akiwa sokoni, Paulo alikutana na watu ambao hawakuwa tayari kumsikiliza. Baadhi ya wasikilizaji wake walikuwa Waepikurea na Wastoa, ambao waliamini falsafa mbili tofauti.b Waepikurea waliamini kwamba uhai ulijitokeza wenyewe tu. Kwa ufupi, waliamini hivi: “Mungu hawezi kutufanya lolote; Hakuna maumivu yoyote katika kifo; Mambo mema yanaweza kufanywa; Mambo mabaya yanaweza kuvumiliwa.” Wastoa walikazia falsafa za kibinadamu nao hawakuamini kwamba kuna Mungu. Waepikurea na Wastoa hawakuamini ufufuo ambao wanafunzi wa Kristo walifundisha. Ni wazi kwamba maoni ya kifalsafa ya vikundi hivyo viwili hayakupatana hata kidogo na Ukristo wa kweli, ambao Paulo alikuwa akitangaza.
6, 7. Wasomi Wagiriki waliyaonaje mafundisho ya Paulo, na hali ikoje leo?
6 Wasomi Wagiriki walionaje mafundisho ya Paulo? Baadhi yao walimwita “mpigadomo.” (Mdo. 17:18) Kuhusu neno la Kigiriki linalotumika katika mstari huo, msomi mmoja anasema hivi: “Mwanzoni neno hilo lilitumiwa kurejelea ndege mdogo anayerukaruka akiokota punje, pia lilitumiwa kurejelea watu waliokuwa wakiokota masalio ya vyakula na vitu vingine vilivyoanguka sokoni. Baadaye, neno hilo lilianza kutumiwa kwa njia ya mfano kurejelea mtu anayekusanya habari hapa na pale, na hasa yule ambaye haelewi habari zenyewe.” Kwa kumwita “mpiga-domo,” ni kana kwamba wasomi hao walisema kwamba Paulo ni mtu anayerudia-rudia mambo asiyoelewa, ambayo amesikia kutoka kwa wengine. Kama tutakavyoona, Paulo hakuvunjika moyo kwa kuitwa jina hilo.
7 Ndivyo ilivyo leo. Tukiwa Mashahidi wa Yehova, mara nyingi tunasemwa vibaya kwa sababu ya imani yetu inayotegemea Biblia. Kwa mfano, walimu fulani hudai kwamba fundisho la mageuzi ni la kweli na kwamba ikiwa una akili, utaliamini. Ni kana kwamba wanadai wote wanaopinga fundisho hilo ni wajinga. Wasomi hao wanataka watu wengine watuone sisi kuwa wajinga kwa sababu tunafundisha mambo ambayo Biblia inasema na kuthibitisha kwamba vitu vyote viliumbwa. Hata hivyo, hilo halituvunji moyo. Badala yake, tunasema tukiwa na uhakika kwamba uhai uliopo duniani ulitokana na Muumba mwenye akili, Yehova Mungu.—Ufu. 4:11.
8. (a) Baadhi ya watu waliomsikia Paulo akihubiri walikuwa na maoni gani? (b) Kwa nini Paulo alipelekwa Areopago? (Ona maelezo ya chini katika ukurasa wa 142.)
8 Wengine waliomsikiliza Paulo akihubiri sokoni walikuwa na maoni tofauti. Walisema: “Inaonekana anatangaza miungu ya kigeni.” (Mdo. 17:18) Je, ni kweli Paulo alikuwa akiwatangazia Waathene miungu ya kigeni? Hilo lilikuwa jambo zito. Karne kadhaa mapema, Sokratesi alihukumiwa kifo kwa mashtaka kama hayo. Hivyo, haishangazi kwamba Paulo alipelekwa Areopago na kuambiwa afafanue mafundisho hayo yaliyokuwa mageni kwa Waathene.c Paulo angeuteteaje ujumbe wake mbele ya watu hao wasiojua Maandiko?
“Wanaume wa Athene, Ninaona” (Mdo. 17:22, 23)
9-11. (a) Paulo aliwekaje msingi mzuri wa mazungumzo? (b) Tunawezaje kufuata mfano wa Paulo katika huduma?
9 Kumbuka kwamba Paulo alikasirika kwa sababu ya ibada ya sanamu aliyojionea, ambayo ilienea sana. Badala ya kuanza kuishambulia ibada ya sanamu, alikuwa mtulivu. Alitumia busara, na kujitahidi kuwavutia wasikilizaji wake kwa kuweka msingi mzuri wa mazungumzo. Alianza kwa kusema hivi: “Wanaume wa Athene, ninaona kwamba katika mambo yote mnaonekana kuwa mnaogopa sana miungu kuliko watu wengine.” (Mdo. 17:22) Ni kana kwamba Paulo alikuwa akisema ‘Naona mnapenda sana mambo ya dini.’ Paulo alitenda kwa hekima alipowapongeza kwa sababu walipendezwa na mambo ya dini. Alitambua kwamba baadhi ya watu waliopofushwa na imani za uwongo wanaweza kusikiliza. Isitoshe, alijua kwamba wakati fulani hata yeye mwenyewe ‘alitenda bila ujuzi na hakuwa na imani.’—1 Tim. 1:13.
10 Baada ya kuweka msingi mzuri, Paulo alieleza kwamba ameona jambo linalothibitisha kuwa watu wa Athene wanapenda mambo ya dini. Aliona madhabahu iliyotengwa kwa ajili ya “Mungu Asiyejulikana.” Kulingana na kitabu kimoja, “Wagiriki walikuwa na mazoea ya kutenga madhabahu kwa ajili ya ‘miungu isiyojulikana,’ ili wasimsahau mungu fulani katika ibada yao, na hivyo kumkasirisha.” Kwa kutenga madhabahu hiyo, Waathene walikiri kwamba kuna Mungu ambaye hawamjui. Paulo alitumia madhabahu hiyo kuwa msingi wa kuwahubiria habari njema. Alieleza: “Kile mnachoabudu bila kujua, hicho ndicho ninachowatangazia.” (Mdo. 17:23) Paulo alitoa hoja zenye nguvu kwa busara. Hakuwa akiwahubiria mungu mpya au wa kigeni, kama watu fulani walivyodai. Alikuwa akiwaeleza kuhusu Mungu ambaye hawakumjua—Mungu wa kweli.
11 Tunawezaje kumwiga Paulo katika huduma yetu? Tukiwa wenye utambuzi, tunaweza kugundua ikiwa mtu anapendezwa na mambo ya dini, labda kwa kuona vitu fulani vya kidini ambavyo amevaa au vilivyo katika nyumba yake au kwenye uwanja wake. Tunaweza kusema: ‘Naona unapendezwa na mambo ya dini. Nilitaka kuzungumza na mtu kama wewe.’ Kwa kumpongeza, tunaweza kuweka msingi mzuri wa mazungumzo. Kumbuka kwamba lengo letu si kuwahukumu watu kwa sababu ya imani yao. Wakati fulani, baadhi ya waabudu wenzetu waliamini mafundisho ya uwongo kwa kutojua.
Jitahidi kuweka msingi mzuri wa mazungumzo
Mungu “Hayuko Mbali na Kila Mmoja Wetu” (Mdo. 17:24-28)
12. Paulo alibadili mazungumzo yake jinsi gani ili yawafae wasikilizaji wake?
12 Tayari Paulo aliweka msingi mzuri wa mazungumzo, lakini je, alijenga vizuri juu ya msingi huo? Akijua kwamba wasikilizaji wake wamefunzwa falsafa za Kigiriki na hawayajui Maandiko, alitumia mbinu mbalimbali. Kwanza alitaja mafundisho ya Biblia bila kunukuu Maandiko moja kwa moja. Pili, alijihusisha kwenye mazungumzo, nyakati nyingine alitumia maneno kama vile “sisi,” na “tuna-.” Tatu, alinukuu vitabu vya Kigiriki ili kuonyesha kwamba mambo fulani aliyokuwa akifundisha yalikuwa katika vitabu vyao wenyewe. Acheni sasa tuchanganue hotuba ya Paulo iliyokuwa na matokeo mazuri. Aliwajulisha Waathene kweli gani muhimu kuhusu Mungu ambaye hawakumjua?
13. Paulo alieleza nini kuhusu ulimwengu, na maneno yake yalikuwa na ujumbe gani?
13 Mungu aliumba ulimwengu. Paulo alisema hivi: “Mungu aliyeumba ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, akiwa, kama alivyo, Bwana wa mbingu na dunia, hakai katika mahekalu yaliyotengenezwa kwa mikono.”d (Mdo. 17:24) Ulimwengu haukujitokeza wenyewe. Mungu wa kweli ndiye Muumba wa vitu vyote. (Zab. 146:6) Tofauti na Athena au miungu mingine ambayo utukufu wao ulitegemea mahekalu na madhabahu, mahekalu yaliyojengwa na mikono ya wanadamu hayawezi kumtosha Bwana Mwenye Enzi Kuu wa mbingu na dunia. (1 Fal. 8:27) Ujumbe wa Paulo ulikuwa wazi: Mungu wa kweli ni mkuu kuliko sanamu yoyote iliyotengenezwa na mwanadamu iliyo katika mahekalu yaliyojengwa na wanadamu.—Isa. 40:18-26.
14. Paulo alionyeshaje kwamba Mungu hawategemei wanadamu?
14 Mungu hawategemei wanadamu. Waabudu-sanamu walipamba sanamu zao kwa nguo maridadi, walizipatia zawadi za bei ghali, au kuzipelekea vyakula na vinywaji—kana kwamba sanamu zilihitaji vitu hivyo! Hata hivyo, huenda baadhi ya wanafalsafa Wagiriki waliomsikiliza Paulo hawakuamini kwamba mungu anahitaji chochote kutoka kwa wanadamu. Ikiwa ndivyo, basi walikubaliana na maneno ya Paulo kwamba Mungu “hatumikiwi kwa mikono ya binadamu kana kwamba anahitaji kitu chochote.” Hakuna kitu chochote cha kimwili ambacho wanadamu wanaweza kumpa Muumba! Badala yake, Mungu huwapa wanadamu wanachohitaji—“uhai na pumzi na vitu vyote,” kutia ndani jua, mvua, na udongo wenye rutuba. (Mdo. 17:25; Mwa. 2:7) Kwa hiyo, Mungu aliye Mpaji, hawezi kuwategemea wanadamu ambao ni wapokeaji.
15. Paulo alishughulikiaje maoni ya Waathene kwamba wao ni bora kuliko watu wasio Wagiriki, nasi tunajifunza nini kutokana na mfano wake?
15 Mungu alimuumba mwanadamu. Waathene waliamini kwamba wao ni bora kuliko watu wasio Wagiriki. Lakini ubaguzi haupatani na kweli ya Biblia. (Kum. 10:17) Paulo alizungumzia kwa busara na ustadi jambo hilo ambalo lingeweza kutokeza ubishi. Huenda waliomsikiliza walitulia na kufikiri aliposema, “[Mungu] alifanyiza kila taifa la watu kutoka kwa mtu mmoja.” (Mdo. 17:26) Alikuwa akirejelea masimulizi ya Mwanzo kuhusu Adamu, baba ya wanadamu wote. (Mwa. 1:26-28) Kwa kuwa wanadamu wote wana baba mmoja, hakuna jamii au taifa bora kuliko lingine. Wasikilizaji wa Paulo walielewa vizuri hoja yake. Mfano huu unatufundisha jambo muhimu. Ingawa tunapaswa kutumia busara na kuwa wenye usawaziko katika kazi yetu ya kuhubiri, hatupaswi kamwe kupunguza uzito wa kweli ya Biblia ili kufanya watu wakubali ujumbe wetu.
16. Muumba ana kusudi gani kwa wanadamu?
16 Mungu alikusudia wanadamu wawe na uhusiano wa karibu pamoja naye. Hata ikiwa wanafalsafa waliomsikiliza Paulo walikuwa wamejadiliana kwa muda mrefu kuhusu kusudi la uhai wa binadamu, hawangeweza kamwe kutoa jibu sahihi na linaloeleweka. Hata hivyo, Paulo alieleza waziwazi kusudi la Muumba kwa wanadamu, kwamba “wamtafute Mungu, ikiwa watapapasa-papasa wakimtafuta na kwa kweli wampate, ingawa, kwa hakika, hayuko mbali na kila mmoja wetu.” (Mdo. 17:27) Mungu ambaye Waathene hawakumjua anaweza kujulikana. Hayuko mbali na wale ambao kwa kweli wanataka kumtafuta na kumjua. (Zab. 145:18) Ona kwamba Paulo anatumia maneno “kila mmoja wetu,” akijitia ndani kati ya wale wanaohitaji ‘kumtafuta’ na ‘kupapasa-papasa wakimtafuta’ Mungu.
17, 18. Kwa nini wanadamu wanapaswa kumkaribia Mungu, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Paulo alivyozungumza na wasikilizaji wake?
17 Wanadamu wanapaswa kumkaribia Mungu. Paulo alisema kwamba, kwa sababu ya Mungu “tuko hai, tunatembea, na tunaishi.” Wasomi fulani husema kwamba Paulo alikuwa akirejelea maneno ya Epimenide, mshairi Mgiriki wa karne ya sita K.W.K. “aliyeheshimiwa sana katika utamaduni wa dini ya Waathene.” Paulo alitaja sababu nyingine inayopaswa kuwafanya wanadamu wahisi wako karibu na Mungu, aliposema: “Baadhi ya washairi wenu wamesema, ‘Kwa maana sisi pia ni watoto wake.’” (Mdo. 17:28) Wanadamu wanapaswa kujiona kuwa na uhusiano wa karibu sana na Mungu, kwa kuwa Yeye ndiye Baba ya mwanadamu wa kwanza ambaye wanadamu wote walitoka kwake. Ili kuwavutia wasikilizaji wake, Paulo alitumia busara kwa kunukuu moja kwa moja vitabu vya Kigiriki ambavyo bila shaka watu waliomsikiliza waliviheshimu sana.e Kama Paulo, nyakati nyingine tunaweza kunukuu vitabu vya historia, ensaiklopedia, au vitabu vingine vya marejeo vinavyoheshimika. Kwa mfano, nukuu inayofaa kutoka katika chanzo kinachotegemeka, inaweza kumsaidia mtu ambaye si Shahidi kujua chanzo cha mazoea au maadhimisho fulani ya dini za uwongo.
18 Kufikia hapa, Paulo ameeleza kweli za msingi kumhusu Mungu, akitumia maneno yake kwa ustadi ili yawafae wasikilizaji wake. Mtume huyo alitaka Waathene hao watumie jinsi gani habari hizo muhimu? Bila kukawia, aliendelea kutoa hotuba yake na kuwaambia wanalopaswa kufanya.
“Wanadamu Wote Kila Mahali . . . Wanapaswa Kutubu” (Mdo. 17:29-31)
19, 20. (a) Paulo alitumia busara jinsi gani kuonyesha ubatili wa kuabudu sanamu zilizotengenezwa na wanadamu? (b) Waliomsikiliza Paulo walihitaji kuchukua hatua gani?
19 Paulo alikuwa tayari kuwahimiza wasikilizaji wake wachukue hatua. Akirejelea tena nukuu kutoka kwa waandishi Wagiriki, alisema: “Kwa hiyo, kwa kuwa sisi ni watoto wa Mungu, hatupaswi kufikiri kwamba Mungu ni kama dhahabu au fedha au jiwe, kama kitu kilichochongwa kwa ufundi na ubunifu wa wanadamu.” (Mdo. 17:29) Kwa kweli, ikiwa wanadamu wametoka kwa Mungu, inawezekanaje Mungu awe sanamu zinazotengenezwa na wanadamu? Njia ya Paulo ya kujadiliana nao ilionyesha ubatili wa kuabudu sanamu zilizotengenezwa na wanadamu. (Zab. 115:4-8; Isa. 44:9-20) Huenda Paulo alifanya iwe rahisi kwa wasikilizaji wake kukubali ushauri wake kwa kujihusisha katika mazungumzo na kusema, “hatupaswi.”
20 Paulo alionyesha wazi kabisa kwamba wanahitaji kuchukua hatua. Alisema: “Mungu ameachilia nyakati hizo za kutojua [za kufikiri kwamba Mungu angependezwa na watu wanaoabudu sanamu]; lakini sasa anawatangazia wanadamu wote kila mahali kwamba wanapaswa kutubu.” (Mdo. 17:30) Huenda baadhi wa wasikilizaji wa Paulo walishangaa kusikia kwamba wanapaswa kutubu. Hata hivyo, hotuba yake yenye nguvu ilionyesha wazi kwamba Mungu ndiye chanzo cha uhai wao na kwa sababu hiyo wanawajibika mbele Zake. Wanahitaji kumtafuta Mungu, kujifunza ukweli kumhusu, na kupatanisha maisha yao na ukweli huo. Kwa Waathene, hilo lilimaanisha kutambua na kuacha kabisa dhambi ya kuabudu sanamu.
21, 22. Paulo alimaliza hotuba yake kwa maneno gani yenye kuchochea, nayo yanatuhusu jinsi gani?
21 Paulo alimaliza hotuba yake kwa maneno yenye kuchochea sana: “[Mungu] ameweka siku ambayo anakusudia kuihukumu kwa uadilifu dunia inayokaliwa kupitia mwanamume ambaye amemweka rasmi, naye ametoa uhakikisho kamili kwa watu wote kwa kuwa amemfufua kutoka kwa wafu.” (Mdo. 17:31) Siku ya Hukumu inayokuja—hiyo ni sababu nzuri ya kumtafuta na kumpata Mungu wa kweli! Paulo hakutaja jina la Hakimu huyo aliyewekwa rasmi. Badala yake, alisema jambo la kustaajabisha kumhusu Hakimu huyo: Aliishi akiwa mwanadamu, akafa, na kufufuliwa na Mungu!
22 Umalizio huo wenye kuchochea una umuhimu mkubwa kwetu. Tunajua kwamba Yesu Kristo aliyefufuliwa ndiye Hakimu aliyewekwa rasmi na Mungu. (Yoh. 5:22) Pia tunajua kwamba Siku ya Hukumu ina urefu wa miaka elfu moja, nayo inakaribia sana. (Ufu. 20:4, 6) Hatuogopi Siku ya Hukumu, kwa kuwa tunajua itawaletea baraka nyingi wale watakaohukumiwa kuwa waaminifu. Kufufuliwa kwa Yesu Kristo kunatuhakikishia kwamba tumaini letu la kuwa na maisha bora ya wakati ujao litatimia hakika!
“Wanaume . . . [Wakawa] Waamini” (Mdo. 17:32-34)
23. Watu waliitikia hotuba ya Paulo katika njia gani mbalimbali?
23 Watu waliitikia hotuba ya Paulo kwa njia mbalimbali. Waliposikia kuhusu ufufuo, “baadhi yao wakaanza kumdhihaki.” Wengine walikuwa watulivu lakini hawakutaka kuchukua hatua yoyote, nao wakamwambia: “Tutakusikiliza kuhusu jambo hili wakati mwingine.” (Mdo. 17:32) Hata hivyo, wachache kati yao waliitikia vizuri: “Wanaume fulani wakajiunga naye na kuwa waamini. Miongoni mwao kulikuwa na Dionisio, aliyekuwa mwamuzi wa mahakama ya Areopago, na mwanamke aliyeitwa Damari, na wengineo.” (Mdo. 17:34) Ndivyo inavyokuwa pia katika huduma yetu. Huenda watu fulani wakatudhihaki, na wengine ingawa wanatuheshimu, lakini hawataki kuchukua hatua yoyote. Hata hivyo, sisi hufurahi sana baadhi yao wanapokubali ujumbe wa Ufalme na kuwa waamini.
24. Tunaweza kujifunza nini kutokana na hotuba aliyotoa Paulo alipokuwa amesimama Areopago?
24 Tunapochanganua hotuba ya Paulo, tunaweza kujifunza mengi kuhusu mpangilio mzuri wa habari, hoja zenye kusadikisha, na jinsi ya kubadilika kulingana na hali za wasikilizaji wetu. Pia, tunaweza kujifunza faida ya kuwa na subira na busara tunapozungumza na watu ambao wamepofushwa na imani za uwongo za kidini. Pia, tunaweza kujifunza somo hili muhimu: Hatupaswi kamwe kupunguza uzito wa kweli za Biblia ili tu kuwafurahisha wasikilizaji wetu. Hata hivyo, tukifuata mfano wa Paulo, tunaweza kuwa walimu wenye matokeo mazuri katika utumishi wa shambani. Isitoshe, waangalizi wanaweza kuwa walimu stadi kutanikoni. Hivyo, tutakuwa tayari kuwasaidia wengine “wamtafute Mungu . . . na kwa kweli wampate.”—Mdo. 17:27.
a Ona sanduku lenye kichwa “Athene—Kituo cha Utamaduni Katika Ulimwengu wa Kale.”
b Ona sanduku lenye kichwa “Waepikurea na Wastoa.”
c Kilima cha Areopago kilikuwa upande wa kaskazini-magharibi mwa Ngome ya Athene, mahali ambapo baraza kuu la Athene lilikutana. Huenda jina “Areopago” lilirejelea baraza hilo au kilima chenyewe. Hivyo, wasomi hawajui kihususa ikiwa Paulo alipelekwa kwenye kilima hicho au karibu na eneo, au mahali pengine ambapo baraza hilo lilikutana, labda sokoni.
d Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ulimwengu” ni koʹsmos. Ijapokuwa Wagiriki walilitumia neno hilo kurejelea ulimwengu halisi, neno koʹsmos kwa kawaida hutumika katika Biblia kurejelea watu. Inawezekana kwamba Paulo, aliyekuwa akijaribu kuweka msingi mzuri wa mazungumzo kati yake na Wagiriki waliomsikiliza, alitumia neno hilo katika maana hiyo.
e Paulo alinukuu shairi linaloitwa Phaenomena, la Arato, mshairi Mstoa. Maneno kama hayo yanapatikana katika vitabu vingine vya Kigiriki kutia ndani wimbo unaoitwa Hymn to Zeus, uliotungwa na Kleanthe, mwandikaji Mstoa.
-
-
“Endelea Kusema na Usinyamaze”“Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
-
-
SURA YA 19
“Endelea Kusema na Usinyamaze”
Paulo ajitegemeza kimwili na kutanguliza huduma
1-3. Mtume Paulo ameenda Korintho kufanya nini, na anakabili changamoto gani?
NI MWISHONI mwa mwaka wa 50 W.K. Mtume Paulo yuko Korintho, jiji tajiri lenye wakaaji wengi Wagiriki, Waroma, na Wayahudi.a Paulo hakwenda kununua wala kuuza bidhaa au kutafuta kazi ya kimwili. Ameenda hapo ili kufanya kazi muhimu zaidi—kutoa ushahidi kuhusu Ufalme wa Mungu. Hata hivyo, Paulo anahitaji mahali pa kuishi, na hataki kuwa mzigo kwa wengine. Hataki mtu yeyote afikiri kwamba anajiruzuku kutokana na neno la Mungu. Atafanya nini?
2 Paulo ana ujuzi wa kutengeneza mahema. Kazi ya kutengeneza mahema si rahisi, hata hivyo, yuko tayari kufanya kazi kwa mikono yake ili ajitegemeze. Je, atapata kazi katika jiji hili lenye shughuli nyingi? Je, atapata mahali pazuri pa kuishi? Ingawa ana mahitaji mengi, Paulo hasahau kamwe kazi yake kuu, kazi ya kuhubiri.
3 Paulo alikaa Korintho kwa muda fulani, naye alipata matokeo mazuri katika huduma yake. Ni mambo gani tunayoweza kujifunza kutokana na utendaji mbalimbali wa Paulo alipokuwa Korintho ambayo yanaweza kutusaidia kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu katika eneo letu?
“Kazi Yao Ilikuwa ya Kutengeneza Mahema” (Mdo. 18:1-4)
4, 5. (a) Paulo aliishi wapi alipokuwa Korintho, naye alifanya kazi gani ya kimwili? (b) Huenda Paulo alijifunzaje kazi ya kutengeneza mahema?
4 Baada ya kufika Korintho, Paulo alikutana na wenzi wa ndoa wakarimu—Akila mwenye asili ya Kiyahudi, na mke wake, Prisila, au Priska. Akila na Prisila walihamia Korintho kwa sababu Maliki Klaudio aliagiza “Wayahudi wote waondoke Roma.” (Mdo. 18:1, 2) Akila na Prisila walimkaribisha Paulo nyumbani kwao na pia katika kazi yao ya kimwili. Tunasoma: “Kwa sababu [Paulo alifanya] kazi ileile, akakaa nyumbani kwao na kufanya kazi pamoja nao, kwa maana kazi yao ilikuwa ya kutengeneza mahema.” (Mdo. 18:3) Kipindi chote cha huduma yake jijini Korintho, Paulo alikaa nyumbani kwa wenzi hao wenye fadhili na wakarimu. Inawezekana Paulo aliandika baadhi ya barua ambazo baadaye zilikuwa sehemu ya Biblia alipokuwa akiishi nyumbani kwa Akila na Prisila.b
5 Paulo, mtu aliyeelimishwa “miguuni pa Gamalieli,” angewezaje kuwa na ujuzi wa kutengeneza mahema? (Mdo. 22:3) Inaonekana kwamba Wayahudi wa karne ya kwanza hawakuona aibu kuwafundisha watoto wao kazi fulani ya mikono, ingawa watoto hao walipata elimu ya ziada pia. Kwa kuwa alikuwa mwenyeji wa Tarso ya Kilikia, eneo lililojulikana sana kwa sababu ya kitambaa kinachoitwa cilicium kilichotumiwa kutengeneza mahema, inaelekea Paulo alijifunza kazi hiyo alipokuwa kijana. Kazi hiyo ya kutengeneza mahema ilifanywaje? Huenda ilitia ndani kufuma kitambaa cha hema au kukata na kushona kitambaa hicho kigumu ili kutengeneza mahema. Bila shaka, kazi hiyo ilikuwa ngumu sana.
6, 7. (a) Paulo aliionaje kazi ya kutengeneza mahema, na ni nini kinachoonyesha kwamba Akila na Prisila walikuwa na maoni hayohayo? (b) Wakristo leo wanafuataje mfano wa Paulo, Akila, na Prisila?
6 Paulo hakuiona kazi ya kutengeneza mahema kuwa kazi muhimu sana maishani mwake. Alifanya kazi hiyo ili kujitegemeza na lengo lake lilikuwa kuhubiri habari njema “bila gharama.” (2 Kor. 11:7) Akila na Prisila waliionaje kazi yao ya kimwili? Kwa kuwa walikuwa Wakristo, bila shaka walikuwa na maoni kama ya Paulo. Isitoshe, Paulo alipoondoka Korintho mwaka wa 52 W.K., Akila na Prisila waliacha biashara yao na kusafiri pamoja na Paulo hadi Efeso, ambapo nyumba yao ilitumiwa kwa ajili ya mikutano ya kutaniko. (1 Kor. 16:19) Baadaye, walirudi Roma, halafu wakaenda tena Efeso. Wenzi hao wenye bidii walitanguliza Ufalme na walijitoa kwa hiari ili kuwatumikia wengine. Kwa sababu hiyo “makutaniko yote ya mataifa” yaliwashukuru.—Rom. 16:3-5; 2 Tim. 4:19.
7 Leo, Wakristo hufuata mfano wa Paulo, Akila, na Prisila. Wahubiri wenye bidii leo hufanya yote wawezayo ili ‘wasimpe yeyote kati yetu mzigo wenye gharama.’ (1 The. 2:9) Mapainia wengi wanatuwekea mfano mzuri kwa kufanya kazi kwa siku kadhaa katika juma au miezi fulani katika mwaka ili waweze kulipia gharama zao za maisha. Hata hivyo, wanatanguliza kazi ya upainia. Kama Akila na Prisila, watumishi wengi wa Yehova huonyesha ukarimu kwa kuwakaribisha nyumbani kwao waangalizi wa mzunguko. ‘Wakaribishaji wageni’ wanajua kwamba kuwa wakarimu hutia moyo na kujenga.—Rom. 12:13.
“Wakorintho Wengi . . . Wakaanza Kuamini” (Mdo. 18:5-8)
8, 9. Paulo alifanya nini alipopingwa na Wayahudi aliowahubiria, naye alienda kuhubiri wapi?
8 Paulo aliiona kazi ya kimwili kuwa njia ya kumtegemeza katika huduma yake. Hilo lilionekana wazi Sila na Timotheo walipowasili kutoka Makedonia wakiwa na zawadi nyingi. (2 Kor. 11:9) Mara moja, Paulo “akaanza kushughulika sana na lile neno [“alianza kutumia wakati wake wote kwa ajili ya kuhubiri,” Biblia Habari Njema].” (Mdo. 18:5) Hata hivyo, Wayahudi aliowahubiria walimpinga. Alijiondolea lawama kwa sababu walikataa ujumbe unaookoa uhai kumhusu Kristo. Paulo alikung’uta mavazi yake na kuwaambia Wayahudi hao waliompinga: “Damu yenu na iwe juu ya vichwa vyenu wenyewe. Mimi ni safi. Kuanzia sasa nitaenda kwa watu wa mataifa.”—Mdo. 18:6; Eze. 3:18, 19.
9 Paulo angehubiri wapi? Mtu anayeitwa Titio Yusto, huenda alikuwa Myahudi mgeuzwa imani na ambaye nyumba yake ilikuwa karibu na sinagogi, alimkaribisha Paulo. Hivyo, Paulo akaacha kuhubiri kwenye Sinagogi na kuendelea kuhubiri akiwa kwenye nyumba ya Yusto. (Mdo. 18:7) Paulo aliendelea kuishi katika nyumba ya Akila na Prisila alipokuwa Korintho, lakini aliitumia nyumba ya Yusto kwa ajili ya huduma yake.
10. Ni nini kinachoonyesha kwamba Paulo hakuazimia kuwahubiria tu watu wa mataifa?
10 Paulo aliposema angeenda kwa watu wa mataifa, je alimaanisha hangewahubiria kabisa Wayahudi na Wayahudi wageuzwa imani, kutia ndani wale waliokubali ujumbe wake? Hapana. Kwa mfano, “Krispo, ofisa msimamizi wa sinagogi akamwamini Bwana, yeye pamoja na watu wote wa nyumba yake.” Inaonekana kwamba wengi kati ya wale waliokuwa wakienda katika sinagogi walijiunga na Krispo, kwa sababu Biblia inasema: “Wakorintho wengi waliosikia wakaanza kuamini na kubatizwa.” (Mdo. 18:8) Basi, kutaniko jipya la Kikristo lililoanzishwa jijini Korintho likaanza kukutanika katika nyumba ya Titio Yusto. Ikiwa masimulizi ya kitabu cha Matendo yanafuata mtindo wa Luka—yaani, yanafuatana kulingana na wakati yalipotukia—basi hilo linamaanisha kwamba Wayahudi hao au Wayahudi wageuzwa imani walikuwa Wakristo baada ya Paulo kukung’uta mavazi yake. Ikiwa ndivyo, basi ni wazi kwamba Paulo alikuwa tayari kubadilika kulingana na hali.
11. Mashahidi wa Yehova leo wanafuata mfano wa Paulo jinsi gani wanapowahubiria watu walio katika dini zinazodai kuwa za Kikristo?
11 Leo watu katika nchi nyingi wanadai kwamba wao ni washiriki wa kanisa fulani linalomfuata Kristo. Na makanisa hayo yana uvutano mkubwa katika maisha yao. Wamishonari wa dini hizo wamepata wafuasi wengi. Watu wanaodai kuwa Wakristo mara nyingi huwa watumwa wa desturi, kama walivyokuwa Wayahudi wa karne ya kwanza jijini Korintho. Hata hivyo, kama Paulo, sisi hujitahidi kuwasaidia watu hao waelewe mambo wanayosoma katika Biblia zao. Hata wanapotupinga, au viongozi wao wa kidini wanapotunyanyasa, hatukati tamaa. Huenda kuna wapole kadhaa miongoni mwa watu wenye “bidii kwa ajili ya Mungu, lakini si kulingana na ujuzi sahihi.” Tunahitaji kuwatafuta wapole hao.—Rom. 10:2.
“Nina Watu Wengi Katika Jiji Hili” (Mdo. 18:9-17)
12. Paulo alihakikishiwa nini katika maono?
12 Ikiwa Paulo alikuwa na mashaka yoyote kuhusu kuendelea na huduma yake jijini Korintho, mashaka hayo yaliisha Bwana Yesu alipomtokea katika maono ya usiku na kumwambia: “Usiogope, bali endelea kusema na usinyamaze, kwa sababu niko pamoja nawe na hakuna mtu atakayekushambulia ili kukudhuru; kwa maana nina watu wengi katika jiji hili.” (Mdo. 18:9, 10) Hayo yalikuwa maono yenye kutia moyo sana! Bwana mwenyewe alimhakikishia Paulo kwamba angelindwa ili asipatwe na madhara na kuna wengi wanaostahili katika jiji hilo. Paulo alitendaje baada ya kuona maono hayo? Tunasoma hivi: “Akakaa huko kwa mwaka mmoja na miezi sita, akifundisha neno la Mungu kati yao.”—Mdo. 18:11.
13. Huenda Paulo alikumbuka tukio gani alipokaribia kiti cha hukumu, lakini kwa nini hali yake ingekuwa tofauti?
13 Baada ya kukaa Korintho mwaka mmoja hivi, Paulo alipata uthibitisho zaidi kwamba Bwana angemsaidia. “Wayahudi wakaungana, wakamshambulia Paulo na kumpeleka kwenye kiti cha hukumu,” kinachoitwa beʹma. (Mdo. 18:12) Baadhi ya watu husema kwamba kiti hicho cha hukumu kilikuwa juu ya jukwaa lililokuwa karibu na eneo la katikati ya soko la Korintho. Kiti hicho kilitengenezwa kwa marumaru za rangi ya bluu na nyeupe zilizochongwa vizuri. Eneo la mbele la beʹma lilikuwa kubwa na umati mkubwa wa watu ungeweza kukusanyika hapo. Uvumbuzi wa vitu vya kale unaonyesha kwamba huenda kiti hicho cha hukumu kilikuwa karibu sana na sinagogi, na ikiwa ndivyo, basi hakikuwa mbali na nyumba ya Yusto. Paulo alipokaribia beʹma, huenda alikumbuka jinsi Stefano, ambaye huitwa mfia-imani wa kwanza, alivyopigwa mawe. Paulo, ambaye wakati huo aliitwa Sauli, aliunga mkono “kuuawa kwa Stefano.” (Mdo. 8:1) Je, sasa jambo hilohilo lingempata Paulo? Hapana, kwa kuwa Yesu alimwahidi hivi: “Hakuna mtu atakayekushambulia ili kukudhuru.”—Mdo. 18:10.
“Ndipo akawafukuza kutoka mbele ya kiti cha hukumu.”—Matendo 18:16
14, 15. (a) Wayahudi walimshtaki Paulo kwa kosa gani, na kwa nini Galio aliitupilia mbali kesi hiyo? (b) Ni nini kilichompata Sosthene, na huenda baadaye alifanya nini?
14 Ni nini kilichotokea Paulo alipofika kwenye kiti cha hukumu? Hakimu aliyekuwa ameketi juu ya kiti hicho alikuwa liwali Akaya, anayeitwa Galio—kaka ya mwanafalsafa Mroma Seneka. Wayahudi wakamshtaki Paulo: “Mtu huyu anawashawishi watu wamwabudu Mungu kwa njia iliyo kinyume cha sheria.” (Mdo. 18:13) Walidai kwamba Paulo anageuza imani ya watu kinyume cha sheria. Hata hivyo, Galio akaona kwamba Paulo hajafanya “kosa” lolote na hana hatia ya “uhalifu mkubwa.” (Mdo. 18:14) Galio hakuwa na nia yoyote ya kujiingiza katika mizozo ya Wayahudi. Hata kabla ya Paulo kusema neno lolote ili kujitetea, Galio akaitupilia mbali kesi hiyo! Washtaki hao wakakasirika sana. Walimalizia hasira yao kwa Sosthene, ofisa msimamizi wa sinagogi, ambaye huenda alichukua nafasi ya Krispo. Walimkamata Sosthene “na kuanza kumpiga mbele ya kiti cha hukumu.”—Mdo. 18:17.
15 Kwa nini Galio hakuuzuia umati usimpige Sosthene? Huenda Galio alifikiri kwamba Sosthene ndiye aliyeuchochea umati huo dhidi ya Paulo na kwa hiyo anapata haki yake. Iwe ndivyo ilivyokuwa au la, kulikuwa na matokeo mazuri. Katika barua yake ya kwanza kwa kutaniko la Korintho, iliyoandikwa miaka kadhaa baadaye, Paulo alimtaja mtu fulani anayeitwa Sosthene akimwita ndugu. (1 Kor. 1:1, 2) Je, huyo ni Sosthene yuleyule aliyepigwa jijini Korintho? Ikiwa ndiye, kisa hicho kilimsaidia Sosthene kuukubali Ukristo.
16. Maneno ya Bwana, “endelea kusema na usinyamaze, kwa sababu niko pamoja nawe,” yanatutiaje moyo katika huduma yetu?
16 Kumbuka kwamba baada ya Wayahudi kumpinga Paulo, Bwana Yesu alimwimarisha na kumwambia, “Usiogope, bali endelea kusema na usinyamaze, kwa sababu niko pamoja nawe.” (Mdo. 18:9, 10) Tusisahau kamwe maneno hayo, hasa watu wanapokataa ujumbe wetu. Usisahau kamwe kwamba Yehova anasoma mioyo na huwavuta watu wanyofu kwake. (1 Sam. 16:7; Yoh. 6:44) Jambo hilo linatutia moyo tuendelee kuwa na bidii katika huduma! Kila mwaka, mamia ya maelfu ya watu hubatizwa, hilo linamaanisha kila siku mamia ya watu hubatizwa. Wale wanaotii amri ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ Yesu anawahakikishia hivi: “Mimi nipo pamoja nanyi sikuzote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mt. 28:19, 20.
“Yehova Akipenda” (Mdo. 18:18-22)
17, 18. Huenda Paulo alitafakari nini alipokuwa njiani kuelekea Efeso?
17 Hatujui ikiwa maoni ya Galio kuelekea watu waliomshtaki Paulo yaliliwezesha kutaniko hilo changa la Kikristo jijini Korintho kukaa kwa amani kwa muda. Hata hivyo, Paulo alikaa “siku kadhaa” kabla ya kuwaaga ndugu zake wa Korintho. Mwaka wa 52 W.K., alipanga kusafiri hadi Siria kutoka bandari ya Kenkrea, kilomita 11 hivi upande wa mashariki wa Korintho. Hata hivyo, kabla ya kuondoka Kenkrea, Paulo “alikuwa amekata nywele zake . . . , kwa sababu alikuwa ameweka nadhiri.”c (Mdo. 18:18) Baadaye, aliwachukua Akila na Prisila na kusafiri katika bahari ya Aegea hadi Efeso katika Asia Ndogo.
18 Paulo aliposafiri kutoka Kenkrea, inawezekana alikuwa akitafakari maisha yake jijini Korintho. Alikuwa na kumbukumbu kadhaa nzuri na sababu nyingi za kuridhika. Huduma yake ya miezi 18 jijini humo ilikuwa na matokeo mazuri. Kutaniko la kwanza jijini Korintho lilianzishwa, na lilikutana katika nyumba ya Yusto. Yusto, Krispo na familia yake, na wengine wengi walikuwa waamini. Paulo aliwapenda sana waamini hao wapya, kwa sababu aliwasaidia kuwa Wakristo. Baadaye aliwaandikia barua na kuwaita barua za pendekezo zilizoandikwa moyoni mwake. Sisi pia huwa na uhusiano wa karibu na watu tunaowasaidia kukubali ibada ya kweli. Ni jambo lenye kuridhisha sana kuona ‘barua hizo za pendekezo!’—2 Kor. 3:1-3.
19, 20. Paulo alifanya nini alipofika Efeso, na tunaweza kujifunza nini kutoka kwake kuhusu kufuatia malengo ya kiroho?
19 Alipofika Efeso, Paulo alianza kazi yake mara moja. “Akaingia ndani ya sinagogi na kujadiliana na Wayahudi.” (Mdo. 18:19) Pindi hiyo, Paulo alikaa Efeso kwa muda mfupi tu. Ingawa aliombwa akae muda mrefu, “hakukubali.” Alipokuwa akiwaaga, aliwaambia Waefeso: “Nitarudi kwenu tena, Yehova akipenda.” (Mdo. 18:20, 21) Paulo alijua kwamba bado kulikuwa na kazi kubwa ya kuhubiri jijini Efeso. Alipanga kurudi, hata hivyo aliamua kuacha mambo mikononi mwa Yehova. Je, huo si mfano mzuri tunaoweza kuiga? Tunapofuatia malengo ya kiroho, lazima tuchukue hatua zinazohitajika. Hata hivyo, lazima sikuzote tutegemee mwongozo wa Yehova na kujitahidi kutenda kupatana na mapenzi yake.—Yak. 4:15.
20 Akiwaacha Akila na Prisila, Paulo alisafiri baharini hadi Kaisaria. Huenda ‘alipanda’ kwenda Yerusalemu na kulisalimu kutaniko lililokuwa huko. (Mdo. 18:22) Kisha Paulo akarudi nyumbani kwake—Antiokia ya Siria. Alikuwa ameimaliza kwa mafanikio safari yake ya pili ya umishonari. Ni nini kinachomsubiri katika safari yake ya mwisho ya umishonari?
a Ona Sanduku lenye kichwa “Korintho—Jiji Lenye Bahari Mbili.”
b Ona Sanduku lenye kichwa “Barua Zenye Kutia Moyo Zilizoongozwa na Roho ya Mungu.”
c Ona sanduku lenye kichwa “Nadhiri ya Paulo.”
-
-
Neno la Yehova ‘Lilikua na Kusitawi’ Licha ya Upinzani“Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
-
-
SURA YA 20
Neno la Yehova ‘Lilikua na Kusitawi’ Licha ya Upinzani
Jinsi Apolo na Paulo walivyochangia ukuzi wa habari njema
1, 2. (a) Paulo na wenzake wanakabili hatari gani Efeso? (b) Tutazungumzia nini katika sura hii?
WATU jijini Efeso wanapiga kelele na kukimbia mitaani. Umati wa watu unakusanyika, ghasia inatokea! Baadhi ya watu wanawakamata wanaume wawili waliosafiri pamoja na Paulo na kuwaburuta. Watu wamejaa kwenye barabara pana yenye maduka kandokando. Wanajiunga na umati huo wenye hasira, na wote wanaelekea kwenye uwanja wa michezo wa jiji hilo. Uwanja huo ulikuwa mkubwa sana na mashabiki 25,000 wangeweza kukusanyika hapo. Wengi kati ya watu wanaokusanyika hapo hawajui kwa nini ghasia hiyo imetokea, lakini wanahisi kwamba hekalu lao na mungu wao wa kike Artemi yumo hatarini. Hivyo, wote wanaanza kupaaza sauti kwa pamoja kwa kurudia-rudia wakisema: “Artemi wa Waefeso ni mkuu!”—Mdo. 19:34.
2 Kwa mara nyingine tena, Shetani anajaribu kutumia umati wenye hasira kuzuia habari njema ya Ufalme wa Mungu. Bila shaka, jeuri ni mojawapo tu ya njia anazotumia Shetani. Katika sura hii, tutazungumzia mbinu mbalimbali ambazo Shetani alitumia ili kudhoofisha kazi na umoja wa Wakristo hao wa karne ya kwanza. Lakini, tutaona jinsi ambavyo mbinu zake zote zilishindwa, kwa sababu ‘kwa njia yenye nguvu, neno la Yehova lilizidi kukua na kusitawi.’ (Mdo. 19:20) Ni nini kilichowasaidia Wakristo hao kusimama imara? Ni kilekile kinachotusaidia leo. Bila shaka, hatutegemei nguvu zetu wenyewe, bali tunamtegemea Yehova. Hata hivyo, kama Wakristo wa karne ya kwanza, lazima tutimize sehemu yetu. Roho takatifu ya Yehova inaweza kutusaidia kukuza sifa zitakazotuwezesha kutimiza huduma yetu kwa mafanikio. Kwanza, acheni tuzungumzie mfano wa Apolo.
“Alikuwa . . . na Ujuzi Mwingi wa Maandiko” (Mdo. 18:24-28)
3, 4. Akila na Prisila walitambua nini kuhusu Apolo, nao walimsaidiaje?
3 Paulo alipoelekea Efeso, katika safari ya tatu ya umishonari, Myahudi anayeitwa Apolo aliwasili jijini humo. Alitoka katika jiji maarufu la Aleksandria, nchini Misri. Apolo alikuwa na sifa za pekee. Alikuwa mwenye ufasaha wa kuzungumza. Isitoshe, “alikuwa . . . na ujuzi mwingi wa Maandiko.” Pia, ‘alikuwa amewaka roho.’ Akiwa mwenye bidii, Apolo alizungumza kwa ujasiri mbele za Wayahudi waliokuwa katika sinagogi.—Mdo. 18:24, 25.
4 Akila na Prisila walimsikia Apolo akizungumza. Bila shaka walifurahi walipomwona ‘akifundisha kwa usahihi kumhusu Yesu.’ Mambo aliyosema kumhusu Yesu yalikuwa sahihi. Lakini, baada ya muda mfupi Akila na Prisila wakatambua kwamba kuna jambo muhimu ambalo Apolo haelewi. “Alifahamu ubatizo wa Yohana tu.” Wenzi hao, waliokuwa watengenezaji wa mahema, hawakumwogopa Apolo kwa sababu ya ufasaha na elimu yake. Badala yake, “wakamchukua na kumfafanulia kwa usahihi zaidi njia ya Mungu.” (Mdo. 18:25, 26) Mtu huyo mwenye ufasaha na elimu aliitikiaje? Alionyesha mojawapo ya sifa muhimu zaidi ambazo Mkristo anapaswa kusitawisha—sifa ya unyenyekevu.
5, 6. Ni nini kilichomsaidia Apolo kupata matokeo mazuri katika utumishi wa Yehova, nasi tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Apolo?
5 Kwa kuwa Apolo alikubali msaada wa Akila na Prisila, alipata matokeo mazuri katika utumishi wa Yehova. Alisafiri kwenda Akaya, na akiwa huko, “akawasaidia sana” waabudu wenzake. Pia, aliwahubiria Wayahudi waliokuwa katika eneo hilo ambao walidai kwamba Yesu si Masihi aliyeahidiwa. Luka anasema hivi: “Alithibitisha kikamili . . . kwa juhudi nyingi kwamba Wayahudi walikuwa wamekosea, na kuwaonyesha kwa Maandiko kuwa Yesu ndiye Kristo.” (Mdo. 18:27, 28) Apolo alisaidia sana kutaniko! Kwa kweli, alichangia kusitawi kwa “neno la Yehova.” Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Apolo?
6 Lazima Wakristo wasitawishe sifa ya unyenyekevu. Kila mmoja wetu ana vipawa mbalimbali—iwe ni uwezo wa asili, uzoefu, au ujuzi ambao tumepata. Hata hivyo, tunapaswa kutambuliwa kwa sababu ya unyenyekevu bali si vipawa vyetu. La sivyo, huenda vipawa vyetu vikatusababishia matatizo. Tunaweza kuanza kuwa na kiburi. (1 Kor. 4:7; Yak. 4:6) Ikiwa kwa kweli sisi ni wanyenyekevu, tutajitahidi kuwaona wengine kuwa bora kuliko sisi. (Flp. 2:3) Hatutakasirika tunaporekebishwa au kukataa tunapofundishwa na wengine. Hatutaendelea kushikilia maoni yetu kwa ushupavu tukijua kwamba hayapatani na mwongozo wa sasa wa roho takatifu. Tukiendelea kuwa wanyenyekevu, Yehova na Mwana wake wataendelea kututumia.—Luka 1:51, 52.
7. Paulo na Apolo walionyeshaje sifa ya unyenyekevu, na tunaweza kuwaiga kwa njia gani?
7 Pia, unyenyekevu huzuia roho ya mashindano. Bila shaka Shetani angependa Wakristo wa karne ya kwanza wawe na migawanyiko. Angefurahi sana ikiwa watu wawili mashuhuri kama vile Apolo na mtume Paulo wangeanza kushindana, huenda hata kuoneana wivu na kujaribu kutafuta wafuasi katika makutaniko! Jambo hilo lingeweza kutokea. Katika jiji la Korintho, Wakristo fulani walianza kusema, “Mimi ni wa Paulo,” huku wengine wakisema, “Lakini mimi ni wa Apolo.” Je, Paulo na Apolo walitaka ndugu na dada wawe na mgawanyiko? Hapana! Badala yake, Paulo alionyesha unyenyekevu kwa kutambua mchango wa Apolo katika kazi ya kuhubiri, na kumpa mapendeleo ya utumishi. Na Apolo alifuata maagizo ya Paulo. (1 Kor. 1:10-12; 3:6, 9; Tito 3:12, 13) Ndugu hao wawili walituwekea mfano mzuri sana wa kufanya kazi bega kwa bega!
“Kujadiliana kwa Ushawishi Kuhusu Ufalme” (Mdo. 18:23; 19:1-10)
8. Paulo alipitia njia gani ili kufika Efeso, na kwa nini?
8 Paulo aliahidi atarudi Efeso, naye alitimiza ahadi hiyo.a (Mdo. 18:20, 21) Hata hivyo, alirudi jinsi gani? Kwa kuwa alikuwa Antiokia ya Siria, angeweza kwenda Seleukia, apande meli, na kusafiri baharini hadi Efeso. Badala yake, alimua ‘kupitia bara.’ Inakadiriwa kwamba, safari ya Paulo inayozungumziwa katika Matendo 18:23 na 19:1, ilikuwa na urefu wa kilomita 1,600 hivi! Kwa nini Paulo aliamua kuzunguka? Kwa sababu lengo lake lilikuwa ‘kuwaimarisha wanafunzi wote.’ (Mdo. 18:23) Safari yake ya tatu ya umishonari, kama zile safari mbili za kwanza, haikuwa rahisi, hata hivyo, hakujuta. Waangalizi wa mzunguko na wake zao leo wanaonyesha roho hiyohiyo. Tunauthamini sana upendo wao wa kujidhabihu!
9. Kwa nini wanafunzi fulani walihitaji kubatizwa tena, na tunaweza kujifunza nini kutokana na kisa chao?
9 Alipofika Efeso, Paulo alikuta kikundi cha watu kumi na wawili hivi waliokuwa wanafunzi wa Yohana Mbatizaji. Walikuwa wamebatizwa ubatizo wa Yohana ambao haukuwa na maana tena. Isitoshe, hawakuelewa vizuri kazi ya roho takatifu. Paulo aliwasaidia kuelewa ni kwa nini wanapaswa kubatizwa katika jina la Yesu. Kama Apolo, walikuwa wanyenyekevu na wenye hamu ya kujifunza. Baada ya kubatizwa katika jina la Yesu, walipokea roho takatifu na zawadi fulani za kufanya miujiza. Kwa kweli, Yehova huwabariki wale ambao wako tayari kufuata mwongozo mpya unatolewa na tengenezo lake.—Mdo. 19:1-7.
10. Kwa nini Paulo alihama kutoka katika sinagogi na kwenda katika ukumbi wa shule, na tunawezaje kumwiga katika huduma yetu?
10 Si hao tu, wengine pia walifanya maendeleo. Paulo alihubiri kwa ujasiri katika sinagogi kwa miezi mitatu. Ingawa “[alijadiliana] kwa ushawishi kuhusu Ufalme wa Mungu,” baadhi ya wasikilizaji wake walikataa kumsikiliza na kuanza kumpinga. Paulo aliamua kutoa hotuba katika ukumbi wa shule badala ya kupoteza wakati akizungumza na watu waliokuwa “wakizungumza vibaya kuhusu Ile Njia.” (Mdo. 19:8, 9) Watu waliotaka kufanya maendeleo ya kiroho walihitaji kutoka katika sinagogi na kwenda katika ukumbi huo. Kama Paulo, tunaweza kukatisha mazungumzo tunapotambua kwamba mwenye nyumba hataki kusikiliza au anataka tu kubishana. Bado kuna watu wengi walio mfano wa kondoo wanaohitaji kusikiliza ujumbe wetu wenye kutia moyo!
11, 12. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba Paulo alikuwa na bidii na alibadilika kulingana na hali? (b) Mashahidi wa Yehova wanaonyeshaje kwamba wana bidii na wako tayari kubadilika kulingana na hali wanapohubiri?
11 Inawezekana Paulo alizungumza katika ukumbi huo kuanzia saa tano asubuhi hadi saa kumi jioni. (Mdo. 19:9) Inaonekana kulikuwa na joto kali muda huo na watu wengi waliacha kazi zao ili wale chakula na kupumzika. Ikiwa Paulo alifanya hivyo kwa miaka miwili, basi alitumia zaidi ya saa 3,000 akifundisha.b Hiyo ni sababu nyingine iliyofanya neno la Yehova lizidi kukua na kusitawi. Paulo alikuwa mwenye bidii naye alibadilika kulingana na hali. Alibadili ratiba ya kuhubiri ili aweze kuwasaidia watu wengi zaidi. Alipata matokeo gani? “Wote walioishi katika mkoa wa Asia wakasikia neno la Bwana, Wayahudi na Wagiriki pia.” (Mdo. 19:10) Bila shaka alitoa ushahidi kikamili.
Sisi hujitahidi kuwahubiria watu popote wanapopatikana
12 Mashahidi wa Yehova leo huhubiri kwa bidii na kubadilika kulingana na hali. Tunajitahidi kuwafikia watu popote walipo na wakati wowote wanapoweza kupatikana. Tunawahubiria barabarani, sokoni, na katika maegesho ya magari. Tunawasiliana na watu kupitia simu au barua. Na tunapohubiri nyumba kwa nyumba, tunajitahidi kufanya hivyo wakati ambapo kuna uwezekano mkubwa wa kuwapata nyumbani.
Neno la Yehova ‘Lilikua na Kusitawi’ Licha ya Roho Waovu (Mdo. 19:11-22)
13, 14. (a) Yehova alimwezesha Paulo kufanya nini? (b) Wana wa Skewa walifanya kosa gani, na watu wengi leo katika dini zinazodai kuwa za Kikristo wanafanyaje kosa kama hilo?
13 Luka anatujulisha kwamba kwa muda fulani mambo yalikuwa shwari, na Yehova alimwezesha Paulo kufanya “matendo yenye nguvu yasiyo ya kawaida.” Hata nguo na vitambaa ambavyo Paulo alivaa vilichukuliwa na kupelekwa kwa wagonjwa, nao wakapona. Roho waovu walitolewa kwa njia hiyo pia.c (Mdo. 19:11, 12) Ushindi huo dhidi ya majeshi ya Shetani uliwashangaza watu wengi. Hata hivyo si watu wote waliofurahia jambo hilo.
14 “Baadhi ya Wayahudi waliosafiri huku na huku wakifukuza roho waovu” walijaribu kuiga miujiza ya Paulo. Baadhi yao walijaribu kufukuza roho waovu kwa kutumia jina la Yesu na Paulo. Luka anasema kwamba wana saba wa Skewa—kutoka katika familia ya kikuhani—walijaribu kufanya hivyo. Roho mwovu aliwaambia: “Ninamjua Yesu nami ninamfahamu Paulo; lakini ninyi ni nani?” Kisha mtu huyo aliyekuwa na roho mwovu, akawarukia na kuwashambulia matapeli hao kama mnyama mwitu, akawajeruhi na kuwatimua wakiwa uchi. (Mdo. 19:13-16) Huo ulikuwa ushindi mkubwa wa “neno la Yehova,” kwa sababu ilionekana wazi kwamba Yehova alimpatia Paulo nguvu nyingi lakini wale wafuasi wa dini za uwongo hawakuwa na nguvu kutoka kwa Yehova. Leo, mamilioni ya watu hufikiri kwamba kuliitia tu jina la Yesu, au kujiita “Mkristo” kunatosha. Hata hivyo, kama Yesu alivyosema, wale wanaofanya mapenzi ya Baba yake ndio tu walio na tumaini hakika la wakati ujao.—Mt. 7:21-23.
15. Tunawezaje kuwaiga Waefeso kuhusiana na mazoea ya kuwasiliana na roho, au vitu vinavyohusiana na mazoea hayo?
15 Ilipojulikana wazi kwamba wana wa Skewa hawana nguvu, watu wengi waliamua kuwa Wakristo na kuacha mazoea ya kuwasiliana na roho. Waefeso wengi waliamini mambo ya uchawi. Watu walifanya mambo ya uchawi na walikuwa na vitu na vitabu vingi vilivyohusiana na mambo hayo. Hivyo, Waefeso wengi walichochewa kutoa vitabu vyao vya uchawi na kuviteketeza hadharani. Kulingana na viwango vya leo, vitabu hivyo vilikuwa na thamani ya pesa nyingi sana.d Luka anasema: “Hivyo kwa njia yenye nguvu, neno la Yehova likazidi kukua na kusitawi.” (Mdo. 19:17-20) Ulikuwa ushindi mkubwa wa ile kweli dhidi ya uwongo na roho waovu! Watu hao waaminifu walituwekea mfano mzuri tunaoweza kuiga leo. Sisi pia tunaishi katika ulimwengu ambao watu wengi wana mazoea ya kuwasiliana na roho. Tukigundua kwamba tuna kitu fulani kinachohusiana na mazoea hayo, tunapaswa kufanya kama walivyofanya Waefeso—kukiharibu kabisa! Na tuepuke kabisa mazoea hayo yenye kuchukiza, hata ikiwa ni vigumu kufanya hivyo.
“Kukatokea Mvurugo Mkubwa” (Mdo. 19:23-41)
“Wanaume, mnajua vema kwamba tunapata mafanikio yetu kutokana na biashara hii.”—Matendo 19:25
16, 17. (a) Eleza jinsi Demetrio alivyoanzisha vurugu jijini Efeso. (b) Waefeso walionyeshaje wanashikilia kupita kiasi maoni ya dini yao?
16 Sasa, hila ya Shetani inaonekana wazi Luka anaposema kwamba “kukatokea mvurugo mkubwa kuhusu Ile Njia.” Ilikuwa hali ya hatari sana.e (Mdo. 19:23) Fundi fulani wa fedha anayeitwa Demetrio ndiye aliyeanzisha vurugu hizo. Aliwachochea mafundi wenzake kwa kuwakumbusha kwamba utajiri wao unatokana na kazi ya kuuza sanamu. Alidai kwamba ujumbe ambao Paulo alihubiri ungeharibu kazi yao, kwa sababu Wakristo hawaabudu sanamu. Kisha akijua kwamba Waefeso hao walijivunia jiji na taifa lao, akawaonya kwamba ikiwa watu watamsikiliza Paulo, mungu wao wa kike Artemi, na hekalu lao linalojulikana ulimwenguni pote, “litaonwa kuwa si kitu.”—Mdo. 19:24-27.
17 Njama ya Demetrio ilifanikiwa. Mafundi hao walikasirika na kuanza kupiga kelele “Artemi wa Waefeso ni mkuu!” Kisha vurugu ikatokea katika jiji hilo kama ilivyosimuliwa mwanzoni mwa sura hii.f Paulo alikuwa jasiri sana na alitaka kwenda kwenye uwanja huo ili azungumze na watu hao, lakini wanafunzi wakasisitiza asijihatarishe. Mtu fulani anayeitwa Aleksanda akasimama mbele ya umati huo na kujaribu kuzungumza. Kwa kuwa alikuwa Myahudi, huenda alitaka kueleza tofauti kati ya Wayahudi na Wakristo hao. Lakini watu hao hawakumsikiliza. Walipotambua kwamba ni Myahudi, walianza kumzomea, na kurudia tena na tena maneno yao “Artemi wa Waefeso ni mkuu!” kwa muda wa saa mbili hivi. Leo pia kuna watu wanaoshikilia sana maoni au itikadi zao za kidini, na si rahisi kuwafundisha.—Mdo. 19:28-34.
18, 19. (a) Karani wa jiji aliunyamazisha jinsi gani umati jijini Efeso? (b) Watu wa Yehova wamelindwa jinsi gani na wenye mamlaka, na wakati mwingine ulinzi huo unategemea nini?
18 Mwishowe, karani wa jiji akaunyamazisha umati huo. Ofisa huyo alikuwa na usawaziko. Kwanza aliwaambia watu hao wenye hasira kwamba Wakristo hawangeweza kuhatarisha hekalu lao na mungu wao wa kike. Pia aliwaambia kwamba Paulo na wenzake hawajafanya kosa lolote dhidi ya hekalu la Artemi. Na pia aliwaeleza kwamba kuna njia rasmi za kushughulikia mambo kama hayo. Huenda walinyamaza kabisa karani huyo alipowaambia kwamba wasipotulia, watashtakiwa chini ya sheria za Roma kwa kukusanyika kinyume cha sheria na kuanzisha vurugu. Kisha, akawaagiza waondoke. Maneno yenye usawaziko ya ofisa huyo yalituliza hasira za watu hao.—Mdo. 19:35-41.
19 Hiyo haikuwa mara ya kwanza kwa ofisa wa serikali mwenye usawaziko kuingilia kati na kuwalinda wafuasi wa Yesu, na wala haikuwa ya mwisho. Mtume Yohana aliona katika maono kwamba katika siku za mwisho, wenye mamlaka katika ulimwengu huu, wanaofananishwa na dunia, wangemeza maji ya mafuriko ya mateso ya Shetani dhidi ya wafuasi wa Yesu. (Ufu. 12:15, 16) Ndivyo ilivyo leo. Katika visa vingi, mahakimu wenye usawaziko wamelinda haki za Mashahidi wa Yehova za kukutana kwa ajili ya ibada na kuwahubiria wengine habari njema. Bila shaka, nyakati nyingine mwenendo wetu huchangia matokeo mazuri tunayopata. Mwenendo wa Paulo ulifanya apendwe na kuheshimiwa na maofisa fulani wa serikali huko Efeso, nao walitaka awe salama. (Mdo. 19:31) Sikuzote na tujiendeshe kwa unyoofu na heshima. Kufanya hivyo kunaweza kuwa na matokeo mazuri.
20. (a) Unahisije unapotafakari jinsi neno la Yehova lilivyositawi katika karne ya kwanza na linavyositawi leo? (b) Umeazimia kufanya nini kuhusiana na ushindi wa Yehova katika siku zetu?
20 Inasisimua kutafakari jinsi ‘neno la Yehova lilivyozidi kukua na kusitawi’ katika karne ya kwanza. Leo, pia, inasisimua kuona jinsi Yehova ametusaidia kupata ushindi mbalimbali. Je, ungependa kushiriki katika ushindi huo hata ikiwa ni kwa kiwango kidogo? Basi jifunze kutokana na mifano ambayo imezungumziwa. Endelea kuwa mnyenyekevu. Mwongozo wa tengenezo la Yehova unapotolewa, ufuate bila kukawia. Endelea kuwa na bidii. Epuka kabisa mazoea ya kuwasiliana na roho. Fanya kila uwezalo ili kutoa ushahidi kamili kupitia mwenendo wako wa unyoofu na heshima.
a Ona sanduku lenye kichwa “Efeso—Jiji Kuu la Asia.”
b Akiwa Efeso, Paulo aliandika barua ya kwanza kwa Wakorintho.
c Huenda “nguo” zinazotajwa ni vitambaa vya mkononi ambavyo Paulo alijifunga kichwani ili kuzuia jasho lisiingie machoni. Na “vitambaa” alivyojifunga vinadokeza kwamba alikuwa akiendelea na kazi yake ya kutengeneza mahema wakati ambapo hakuwa akihubiri, labda mapema asubuhi.—Mdo. 20:34, 35.
d Kulingana na Luka, vitabu hivyo viligharimu vipande 50,000 vya fedha. Ikiwa alikuwa akizungumzia dinari, basi mfanyakazi wa nyakati hizo angehitaji kufanya kazi kila siku kwa siku 50,000—miaka 137 hivi ili kupata pesa hizo.
e Watu fulani husema kwamba Paulo alikuwa akirejelea tukio hili alipowaambia Wakorintho “hatukuwa na uhakika hata kuhusu uhai wetu.” (2 Kor. 1:8) Hata hivyo, huenda alikuwa akizungumzia pindi nyingine iliyokuwa hatari zaidi. Paulo alipoandika kwamba ‘alipigana na wanyama wa mwituni huko Efeso,’ huenda alikuwa akizungumzia wanyama wakali katika uwanja fulani wa michezo au wanadamu wapinzani. (1 Kor. 15:32) Inawezekana alikabili hali hizo kihalisi au kwa njia ya mfano.
f Vyama au mashirika kama hayo ya wafanyakazi yanaweza kuwa na nguvu sana. Kwa mfano, karne moja hivi baadaye, chama cha waokaji kilichochea vurugu kama hizo jijini Efeso.
-
-
“Mimi Sina Hatia ya Damu ya Mtu Yeyote”“Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
-
-
SURA YA 21
“Mimi Sina Hatia ya Damu ya Mtu Yeyote”
Bidii ya Paulo katika huduma na ushauri wake kwa wazee
1-3. (a) Eleza matukio ya siku ambayo Eutiko alikufa. (b) Paulo afanya nini, na tukio hilo laonyesha nini kumhusu Paulo?
PAULO yuko katika chumba cha juu huko Troa. Chumba hicho kimejaa watu. Ana mazungumzo marefu pamoja na akina ndugu, kwa kuwa huu ndio usiku wa mwisho atakaokuwa pamoja nao. Ni usiku wa manane. Kuna taa nyingi zinazowaka chumbani, na kwa hiyo kuna joto jingi na moshi pia. Kijana mmoja anayeitwa Eutiko ameketi dirishani. Paulo anapozungumza, Eutiko analala usingizi mzito na kuanguka nje ya chumba hicho kilicho katika ghorofa ya tatu!
2 Kwa kuwa ni daktari, huenda Luka ndiye wa kwanza kufika nje ili kuona hali ya kijana huyo. Eutiko ‘anaokotwa akiwa amekufa.’ (Mdo. 20:9) Hata hivyo, muujiza watokea. Paulo akajitupa juu ya kijana huyo na kuuambia umati: “Acheni kupiga kelele, kwa maana yuko hai.” Paulo amemfufua Eutiko!—Mdo. 20:10.
3 Tukio hilo linaonyesha nguvu za roho takatifu ya Mungu. Paulo hakusababisha kifo cha Eutiko. Hata hivyo, hakutaka kifo cha kijana huyo kivuruge pindi hiyo muhimu au kumkwaza mtu yeyote kiroho. Kwa kumfufua Eutiko, Paulo aliliacha kutaniko likiwa limefarijiwa na likiwa tayari kuendeleza huduma yao. Ni wazi kwamba Paulo alithamini uhai wa wengine. Kumbuka alivyosema: “Mimi sina hatia ya damu ya mtu yeyote.” (Mdo. 20:26) Acheni tuone jinsi mfano wa Paulo unavyoweza kutusaidia.
“Akaanza Safari Yake ya Kwenda Makedonia” (Mdo. 20:1, 2)
4. Paulo alikabili hali gani yenye kuogopesha?
4 Kama tulivyoona katika sura ya 20, Paulo alikuwa amekabili hali yenye kuogopesha. Huduma yake katika jiji la Efeso ilisababisha mvurugo. Mafundi wa fedha ambao biashara yao ilitegemea ibada ya Artemi ndio waliochochea mvurugo huo! “Baada ya ghasia kutulia,” andiko la Matendo 20:1 linasema, “Paulo akatuma watu wawaite wanafunzi, akawatia moyo na kuwaaga, kisha akaanza safari yake ya kwenda Makedonia.”
5, 6. (a) Huenda Paulo alikaa Makedonia kwa muda gani, na aliwafanyia nini akina ndugu huko? (b) Paulo aliwaonaje waamini wenzake?
5 Alipokuwa akielekea Makedonia, Paulo alifika katika bandari ya Troa na kukaa huko kidogo. Paulo alitazamia kukutana na Tito, aliyekuwa ametumwa Korintho. (2 Kor. 2:12, 13) Hata hivyo, alipoona kwamba Tito hafiki, Paulo akaenda Makedonia, ambako yaelekea alikaa kwa mwaka mmoja hivi na “kuwatia moyo kwa maneno mengi.”a (Mdo. 20:2) Mwishowe, Tito alijiunga na Paulo huko Makedonia, na kumweleza habari njema kuhusu jinsi Wakorintho walivyoitikia barua ya kwanza ya Paulo. (2 Kor. 7:5-7) Hilo lilimchochea Paulo kuwaandikia barua nyingine, ambayo leo twaijua kama Barua ya Pili kwa Wakorintho.
6 Luka anatumia maneno “akawatia moyo,” na “kuwatia moyo,” anapofafanua ziara ya Paulo kwa akina ndugu wa Efeso na Makedonia. Maneno hayo yanaonyesha vizuri jinsi Paulo alivyowaona waamini wenzake! Tofauti na Mafarisayo, waliowadharau watu, Paulo aliwaona kondoo hao kuwa wafanyakazi wenzake. (Yoh. 7:47-49; 1 Kor. 3:9) Paulo alikuwa na maoni hayo sikuzote, hata wakati ambapo alilazimika kuwapa shauri kali.—2 Kor. 2:4.
7. Wazee Wakristo wanaweza kuigaje mfano wa Paulo?
7 Leo, wazee wa kutaniko na waangalizi wa mzunguko hujitahidi kuiga mfano wa Paulo. Hata wanapotoa karipio, lengo lao ni kuwatia nguvu wale wanaohitaji msaada. Wazee na waangalizi huwahangaikia wengine na kujitahidi kuwatia moyo badala ya kuwashutumu. Mwangalizi mmoja wa mzunguko alisema hivi: “Ndugu na dada zetu wengi wanataka kufanya yaliyo sawa, lakini mara nyingi wao huvunjika moyo, huogopa na huhisi kwamba hawajui jambo la kufanya.” Wazee wanaweza kuwatia nguvu waamini wenzao wanaokabili hali kama hizo.—Ebr. 12:12, 13.
‘Walitunga Hila Dhidi Yake’ (Mdo. 20:3, 4)
8, 9. (a) Ni nini kilichokatiza safari ya Paulo kuelekea Siria? (b) Huenda ni nini kilichochochea chuki ya Wayahudi dhidi ya Paulo?
8 Alipotoka Makedonia, Paulo alienda Korintho.b Baada ya kukaa miezi mitatu huko, alitamani kwenda Kenkrea, ambapo angepanda mashua hadi Siria. Akiwa huko angeweza kwenda Yerusalemu na kuwapa msaada ndugu wenye uhitaji.c (Mdo. 24:17; Rom. 15:25, 26) Lakini, mambo yasiyotazamiwa yalibadili mipango yake. Andiko la Matendo 20:3 linasema hivi: “Wayahudi walikuwa wametunga hila dhidi yake”!
9 Si ajabu kwamba Wayahudi walimchukia Paulo kwa kuwa walimwona kuwa mwasi imani. Mwanzoni, Paulo alipohubiri Korintho, alimsaidia Krispo kuwa mwamini. Krispo alikuwa kiongozi katika sinagogi. (Mdo. 18:7, 8; 1 Kor. 1:14) Pindi nyingine, Wayahudi waliokuwa Korintho walimshtaki Paulo kwa Galio, liwali wa Akaya. Hata hivyo, Galio aliyatupilia mbali mashtaka hayo na kusema kwamba hayana msingi. Uamuzi huo uliwakasirisha sana adui za Paulo. (Mdo. 18:12-17) Huenda Wayahudi waliokuwa Korintho walijua au walidhani kwamba karibuni Paulo angesafiri kutoka Kenkrea, hivyo wakapanga njama ya kumvamia. Paulo angefanya nini?
10. Eleza kwa nini Paulo hakutenda kwa woga alipoamua kutoenda Kenkrea.
10 Akihangaikia usalama wake—na ili kuhakikisha kwamba michango aliyokabidhiwa iko salama—Paulo aliamua kurudi Makedonia badala ya kwenda Kenkrea. Ni kweli kwamba kusafiri barabarani kulikuwa na hatari nyingi. Mara nyingi wezi waliwaibia watu barabarani. Hata nyumba za wageni hazikuwa salama. Hata hivyo, Paulo aliamua kwamba yote hayo ni afadhali kuliko yaliyokuwa yakimsubiri huko Kenkrea. Jambo zuri ni kwamba hakusafiri peke yake. Katika safari hiyo ya umishonari, aliandamana na Aristarko, Gayo, Sekundo, Sopatro, Timotheo, Trofimo, na Tikiko.—Mdo. 20:3, 4.
11. Ni kwa njia gani Wakristo leo huchukua hatua zinazohitajika ili kujilinda, na Yesu aliwawekea mfano mzuri jinsi gani?
11 Kama alivyofanya Paulo, Wakristo leo huchukua hatua zinazohitajika ili kujilinda wanapokuwa katika huduma. Katika maeneo fulani, wao huhubiri wakiwa vikundi—au angalau wawili—badala ya kwenda peke yao. Namna gani mateso? Wakristo wanatambua kwamba hawawezi kuepuka mateso. (Yoh. 15:20; 2 Tim. 3:12) Hata hivyo, hawajiweki katika hali ya hatari. Fikiria mfano wa Yesu. Pindi moja, wapinzani wake katika jiji la Yerusalemu walipookota mawe ili wampige, ‘Yesu alijificha na kuondoka hekaluni.’ (Yoh. 8:59) Baadaye, Wayahudi walipopanga njama ya kumuua, “Yesu hakutembea tena hadharani kati ya Wayahudi, bali alienda katika eneo lililo karibu na nyika.” (Yoh. 11:54) Yesu alichukua hatua zinazohitajika ili kujilinda, maadamu kufanya hivyo hakukupingana na mapenzi ya Mungu. Wakristo pia hufanya hivyo leo.—Mt. 10:16.
“Wakafarijika Sana” (Mdo. 20:5-12)
12, 13. (a) Ufufuo wa Eutiko ulikuwa na matokeo gani kutanikoni? (b) Ni tumaini gani linalopatikana katika Biblia ambalo huwafariji wale wanaofiwa leo?
12 Baada ya kupita Makedonia, Paulo na wenzake waligawanyika na kwenda sehemu tofauti. Yaonekana kwamba kikundi hicho kilikutana tena Troa.d Masimulizi yanasema: “Siku tano baadaye tukawafikia huko Troa.”e (Mdo. 20:6) Wakiwa Troa ndipo yule kijana Eutiko alipofufuliwa, kama tulivyosoma mwanzoni mwa sura hii. Wazia jinsi akina ndugu walivyohisi walipomwona mwenzao Eutiko akifufuliwa! Masimulizi hayo yanasema kwamba ‘walifarijika sana.’—Mdo. 20:12.
13 Bila shaka, miujiza kama hiyo haitokei leo. Hata hivyo, wale ambao wamefiwa ‘hufarijiwa sana’ na tumaini la ufufuo linalopatikana katika Biblia. (Yoh. 5:28, 29) Fikiria hili: Kwa kuwa Eutiko hakuwa mkamilifu, alikufa tena baadaye. (Rom. 6:23) Hata hivyo, watakaofufuliwa katika ulimwengu mpya wa Mungu wana tumaini la kuishi milele! Isitoshe, wale wanaofufuliwa wakatawale pamoja na Yesu huko mbinguni huvikwa kutoweza kufa. (1 Kor. 15:51-53) Wakristo leo—iwe ni watiwa mafuta au ni “kondoo wengine”—wana sababu nzuri ya ‘kufarijiwa sana.’—Yohana 10:16.
“Hadharani na Nyumba kwa Nyumba” (Mdo. 20:13-24)
14. Paulo aliwaambia nini wazee wa Efeso walipokutana naye huko Mileto?
14 Paulo na wenzake walisafiri kutoka Troa hadi Aso, kisha wakaenda Mitilene, Kio, Samo, na Mileto. Paulo alikusudia kufika Yerusalemu kabla ya Sherehe ya Pentekoste. Kwa kuwa alikuwa na haraka ya kurudi Yerusalemu kabla ya Pentekoste, huenda ndiyo sababu aliamua kutopitia Efeso. Hata hivyo, kwa kuwa Paulo alitaka kuongea na wazee wa Efeso, aliwaomba wakutane naye Mileto. (Mdo. 20:13-17) Walipofika, Paulo aliwaambia hivi: “Mnajua vema jinsi nilivyotenda kati yenu tangu siku ya kwanza niliyokanyaga mkoa wa Asia, nilivyomtumikia Bwana kwa unyenyekevu wote na machozi na majaribu yaliyonipata kupitia hila za Wayahudi, nami sikuepuka kuwaambia ninyi jambo lolote lenye faida na kuwafundisha hadharani na nyumba kwa nyumba. Lakini nilitoa ushahidi kikamili kwa Wayahudi na Wagiriki kuhusu toba kwa Mungu na kuwa na imani katika Bwana wetu Yesu.”—Mdo. 20:18-21.
15. Kwa nini sisi huhubiri nyumba kwa nyumba?
15 Leo, kuna njia nyingi za kuwahubiria watu habari njema. Kama alivyofanya Paulo, sisi hujitahidi kwenda mahali ambapo watu wanapatikana, iwe ni katika vituo vya mabasi, barabara zenye watu wengi, au sokoni. Hata hivyo, njia kuu inayotumiwa na Mashahidi wa Yehova ni kuhubiri nyumba kwa nyumba. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba kuhubiri nyumba kwa nyumba huwapa watu wote nafasi ya kutosha kuusikia ujumbe wa Ufalme kwa ukawaida, na hilo huonyesha wazi kwamba Mungu hana ubaguzi. Pia, tunapohubiri nyumba kwa nyumba, tunaweza kuwasaidia kibinafsi watu wanaopendezwa na ujumbe wetu. Tena, kufanya hivyo hutusaidia kuimarisha imani yetu na kusitawisha sifa ya uvumilivu. Wakristo wa kweli wanajulikana kwa bidii yao katika kuhubiri “hadharani na nyumba kwa nyumba.”
16, 17. Paulo alionyesha ujasiri wake jinsi gani, na Wakristo leo wanawezaje kufuata mfano wake?
16 Paulo aliwaeleza wazee wa Efeso kwamba hajui hatari ambazo angepata baada ya kurudi Yerusalemu. Aliwaambia hivi: “Hata hivyo, sioni uhai wangu kuwa muhimu kwangu, mradi tu nimalize mwendo wangu na huduma niliyopokea kutoka kwa Bwana Yesu, kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema ya fadhili zisizostahiliwa za Mungu.” (Mdo. 20:24) Paulo hakuogopa wala kuruhusu hali yoyote—iwe ni afya mbaya au upinzani mkali—imzuie kutimiza mgawo wake.
17 Leo pia, Wakristo huvumilia hali nyingi ngumu. Katika nchi fulani wamepigwa marufuku na kuteswa. Wengine hupambana kwa ujasiri na magonjwa ya kimwili au kihisia. Vijana Wakristo hushinikizwa na marafiki shuleni. Vyovyote vile, Mashahidi wa Yehova huonyesha ushikamanifu, kama alivyofanya Paulo. Wameazimia “kutoa ushahidi kamili kuhusu habari njema.”
“Jiangalieni Wenyewe na Kundi Lote” (Mdo. 20:25-38)
18. Paulo aliepuka hatia ya damu jinsi gani, nao wazee wa Efeso wangeweza kufuata mfano wake kwa njia gani?
18 Paulo aliwahimiza wazee wa Efeso, akitumia mfano wake mwenyewe. Kwanza aliwaambia kwamba huenda hawatamwona tena. Kisha akasema: “Mimi sina hatia ya damu ya mtu yeyote, kwa maana sikukosa kuwaambia mashauri yote ya Mungu.” Wazee wa Efeso wangeweza kufuata mfano wa Paulo kwa kuepuka hatia ya damu jinsi gani? Paulo aliwaambia: “Jiangalieni wenyewe na kundi lote, ambalo kati yake roho takatifu imewaweka ninyi rasmi muwe waangalizi, mlichunge kutaniko la Mungu, ambalo alilinunua kwa damu ya Mwana wake mwenyewe.” (Mdo. 20:26-28) Paulo alionya kwamba “mbwamwitu wenye kukandamiza” wangeingia kutanikoni na “kusema mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” Wazee hao walipaswa kufanya nini? Paulo aliwahimiza hivi: “Endeleeni kukesha, na kukumbuka kwamba kwa miaka mitatu, usiku na mchana, sikuacha kumwonya kila mmoja kwa machozi.”—Mdo. 20:29-31.
19. Ni uasi imani gani uliotokea kufikia mwishoni mwa karne ya kwanza, nao ulitokeza nini katika karne zilizofuata?
19 “Mbwamwitu wenye kukandamiza” walianza kutokea mwishoni mwa karne ya kwanza. Mwaka wa 98 hivi W.K., mtume Yohana aliandika: “Hata sasa wapinga-Kristo wengi wametokea . . . Waliondoka miongoni mwetu, lakini hawakuwa wa namna yetu; kwa maana kama wangekuwa wa namna yetu, wangebaki pamoja nasi.” (1 Yoh. 2:18, 19) Kufikia karne ya tatu, uasi imani ulitokeza makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, na katika karne ya nne, Maliki Konstantino akaidhinisha rasmi “Ukristo” huo bandia. Viongozi wa dini ‘walisema mambo yaliyopotoka’ kwa kuchukua mazoea ya kipagani na kuyafanya yaonekane kuwa ya “Kikristo.” Hata leo hii, matokeo ya uasi imani huo yanaonekana katika mafundisho na desturi ya dini zinazodai kuwa za Kikristo.
20, 21. Paulo alionyeshaje roho ya kujidhabihu, nao wazee Wakristo wanaweza kufuata mfano wake kwa njia gani leo?
20 Maisha ya Paulo yalikuwa tofauti kabisa na ya wale ambao baadaye walilitumia kundi vibaya. Alifanya kazi ya kimwili na kujitegemeza ili asiwe mzigo kutanikoni. Paulo aliwatumikia ndugu zake na hakutarajia kupata pesa kutoka kwao. Aliwahimiza wazee wa Efeso waonyeshe roho ya kujidhabihu. Aliwaambia hivi: “Lazima mwasaidie walio dhaifu, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, aliposema: ‘Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.’”—Mdo. 20:35.
21 Kama alivyofanya Paulo, wazee Wakristo hujidhabihu. Tofauti na makasisi wa dini zinazodai kuwa za Kikristo, wanaofilisi makundi yao, wale walio na jukumu la ‘kulichunga kutaniko la Mungu’ hufanya hivyo bila ubinafsi. Watu wenye kiburi na wanaojitakia makuu hawana nafasi yoyote katika kutaniko la Kikristo. Wale wanaotafuta ‘utukufu wao wenyewe’ mwishowe wataambulia patupu. (Met. 25:27) Sikuzote, kimbelembele huleta aibu.—Met. 11:2.
“Wote wakalia sana.”—Matendo 20:37
22. Kwa nini wazee wa Efeso walimpenda sana Paulo?
22 Kwa kuwa Paulo aliwapenda akina ndugu kikweli, ndugu hao walimpenda sana. Kwa kweli, wakati wake wa kuondoka ulipofika, ‘wote walilia sana, nao wakamkumbatia Paulo na kumbusu kwa upendo.’ (Mdo. 20:37, 38) Wakristo huwathamini na kuwapenda ndugu ambao, kama alivyofanya Paulo, hujitoa wenyewe bila ubinafsi kwa manufaa ya kundi. Unapotafakari mfano mzuri wa Paulo, je, hukubali kwamba hakuwa akijisifu wala kutilia chumvi aliposema: “Mimi sina hatia ya damu ya mtu yeyote”?—Mdo. 20:26.
a Ona sanduku lenye kichwa “Barua Ambazo Paulo Aliandika Alipokuwa Makedonia.”
b Inawezekana Paulo aliandika barua yake kwa Waroma alipokuwa Korintho.
c Ona sanduku lenye kichwa “Paulo Apeleka Misaada.”
d Maneno ya Luka katika Matendo 20:5, 6 yanadokeza kwamba Luka aliungana tena na Paulo huko Filipi. Mapema Paulo alimwacha Luka huko.—Mdo. 16:10-17, 40.
e Safari ya kutoka Filipi hadi Troa iliwachukua siku tano. Yawezekana kwamba kulikuwa na upepo mkali, kwa sababu awali safari hiyo iliwachukua siku mbili tu.—Mdo. 16:11.
-
-
“Mapenzi ya Yehova na Yatendeke”“Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
-
-
SURA YA 22
“Mapenzi ya Yehova na Yatendeke”
Akiwa ameazimia kufanya mapenzi ya Mungu, Paulo anaenda Yerusalemu
1-4. Kwa nini Paulo anaenda Yerusalemu, na nini kinachomngojea huko?
WATU wengi wamehuzunika baada ya Paulo kuondoka huko Mileto. Si rahisi kwa Paulo na Luka kuachana na wazee wa Efeso, waliowapenda sana! Wamishonari hao wawili wamesimama kwenye sitaha. Mizigo yao ina vitu wanavyohitaji kwa ajili ya safari. Pia wamebeba michango iliyokusanywa kwa ajili ya Wakristo wenye uhitaji huko Yudea nao wanakusudia kuwasilisha salama zawadi hizo.
2 Upepo mwanana unajaza matanga na meli yang’oa nanga. Wanaume hao wawili, na wengine saba wanaosafiri pamoja nao, wanawatazama ndugu zao wenye huzuni waliobaki ufuoni. (Mdo. 20:4, 14, 15) Wasafiri hao wanaendelea kupunga mikono mpaka wanapokuwa mbali wasiweze tena kuwaona rafiki zao.
3 Kwa miaka mitatu hivi, Paulo amekuwa akifanya kazi pamoja na wazee wa Efeso. Lakini sasa, akiongozwa na roho takatifu, anaelekea Yerusalemu. Kwa kiasi fulani, anajua yatakayompata. Awali, aliwaambia wazee hao hivi: “Nikiwa nimefungwa katika roho, ninasafiri kwenda Yerusalemu, ingawa sijui mambo yatakayonipata huko, isipokuwa kutoka jiji mpaka jiji roho takatifu inanitolea ushahidi tena na tena, ikisema kwamba nitafungwa gerezani na kupatwa na dhiki.” (Mdo. 20:22, 23) Licha ya hatari anazokabili, Paulo anahisi kwamba ‘amefungwa katika roho,’ yaani anawajibika na yuko tayari kufuata mwongozo wa roho wa kwenda Yerusalemu. Anathamini uhai wake, hata hivyo, kufanya mapenzi ya Mungu ndilo jambo kuu zaidi maishani mwake.
4 Je, unahisi hivyo? Tulipojiweka wakfu kwa Yehova, tuliahidi kwamba tutatanguliza mapenzi yake maishani mwetu. Tunaweza kunufaika kwa kuchunguza mfano mzuri wa mtume Paulo.
Kukiacha Nyuma “Kisiwa cha Kipro” (Mdo. 21:1-3)
5. Paulo na wenzake walipitia njia gani kwenda Tiro?
5 Meli ambayo Paulo na wenzake walipanda ‘ilienda moja kwa moja.’ Hilo linamaanisha kwamba kulikuwa na upepo mzuri uliovuma, na meli haikushusha matanga hadi walipofika Kosi siku hiyo. (Mdo. 21:1) Inaonekana kwamba meli hiyo ilitia nanga huko usiku kucha kabla ya kuelekea Rode na Patara. Walipofika Patara, katika pwani ya kusini ya Asia Ndogo, ndugu hao walipanda meli kubwa ya shehena, iliyowapeleka moja kwa moja hadi Tiro, Foinike. Wakiwa njiani, walikiacha nyuma “kisiwa cha Kipro . . . upande wa kushoto.” (Mdo. 21:3) Kwa nini Luka, aliyeandika kitabu cha Matendo, anataja jambo hilo?
6. (a) Kwa nini yawezekana kwamba Paulo alitiwa moyo alipokiona kisiwa cha Kipro? (b) Unapotafakari jinsi Yehova amekubariki na kukusaidia, unafikia mkataa gani?
6 Huenda Paulo aliwaonyesha wasafiri wenzake kisiwa hicho na kusimulia mambo aliyojionea alipokuwa huko. Katika safari yake ya kwanza ya umishonari, miaka tisa hivi iliyopita, Paulo, pamoja na Barnaba na Yohana Marko, walikutana na Elima mlozi, aliyepinga kazi yao ya kuhubiri. (Mdo. 13:4-12) Paulo aliimarishwa kukabiliana na mambo yaliyokuwa mbele yao baada ya kukiona kisiwa hicho na kutafakari yaliyotokea. Sisi pia tunaweza kunufaika kwa kutafakari jinsi Yehova ametubariki na kutusaidia kuvumilia majaribu. Tukitafakari kwa njia hiyo tunaweza kuchochewa kusema kama Daudi: “Mwadilifu ana matatizo mengi, lakini Yehova humwokoa kutoka katika matatizo hayo yote.”—Zab. 34:19.
‘Tukawatafuta Wanafunzi na Tukawapata’ (Mdo. 21:4-9)
7. Paulo na wenzake walifanya nini walipofika Tiro?
7 Paulo alithamini sana ushirika wa Kikristo naye alipenda kuwa pamoja na waamini wenzake. Walipofika Tiro, Luka anaandika, ‘tukawatafuta wanafunzi na tukawapata.’ (Mdo. 21:4) Wakijua kwamba kuna Wakristo wenzao Tiro, wasafiri hao waliwatafuta na huenda walikaa pamoja nao. Mojawapo ya baraka kubwa za kujua kweli ni kwamba popote tunapoenda, tunaweza kupata waabudu wenzetu ambao watatukaribisha. Waabudu wa Mungu wa kweli wana marafiki ulimwenguni pote.
8. Andiko la Matendo 21:4 linamaanisha nini?
8 Akieleza kuhusu siku saba walizokaa Tiro, Luka anataja jambo ambalo mwanzoni linaonekana kuwa lenye kushangaza: “Kupitia roho [akina ndugu wa Tiro] wakamwambia Paulo tena na tena asikanyage Yerusalemu.” (Mdo. 21:4) Je, Yehova alikuwa amebadili nia yake? Je, sasa alikuwa akimzuia Paulo asiende Yerusalemu? Hapana. Roho ilionyesha kwamba Paulo angeteswa Yerusalemu, bali si kwamba asiende huko. Inaonekana kwamba kupitia roho takatifu, ndugu wa Tiro walikuwa sahihi kwamba Paulo angepatwa na matatizo Yerusalemu. Hivyo, wakimhangaikia Paulo, walimhimiza asiende huko. Hangaiko lao la kutaka kumlinda Paulo asipatwe na hatari zilizokuwa zikimngojea linaeleweka. Hata hivyo, akiwa ameazimia kufanya mapenzi ya Yehova, Paulo aliendelea na safari yake hadi Yerusalemu.—Mdo. 21:12.
9, 10. (a) Aliposikia mahangaiko ya ndugu zake huko Tiro, inawezekana Paulo alikumbuka hali gani inayofanana na hiyo? (b) Ni maoni gani ambayo yameenea sana ulimwenguni leo, nayo yanatofautiana jinsi gani na maneno ya Yesu?
9 Aliposikia mahangaiko ya akina ndugu, huenda Paulo alikumbuka kwamba wanafunzi wa Yesu pia, walijaribu kumzuia alipowaambia ataenda Yerusalemu, ateswe, na kuuawa. Akisukumwa na hisia, Petro alimwambia Yesu: “Bwana jihurumie; hutapatwa kamwe na mambo hayo.” Yesu alimjibu: “Nenda nyuma yangu, Shetani! Wewe ni kikwazo kwangu, kwa sababu hufikirii mawazo ya Mungu, bali ya wanadamu.” (Mt. 16:21-23) Yesu aliazimia kuishi maisha ya kujidhabihu, jambo ambalo Mungu alikuwa amemtuma afanye. Paulo alihisi hivyo pia. Bila shaka, kama mtume Petro, ndugu wa Tiro walikuwa na nia nzuri, hata hivyo, hawakutambua mapenzi ya Mungu.
Ili kuwa mfuasi wa Yesu, lazima mtu awe na roho ya kujidhabihu
10 Watu wengi leo hupenda kujitendea kwa fadhili au kuishi maisha ya starehe. Kwa ujumla watu hutafuta dini ambayo haidai mengi ili wastarehe. Hata hivyo, Yesu aliwahimiza wafuasi wake wawe na maoni tofauti kabisa. Aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe, aubebe mti wake wa mateso na aendelee kunifuata.” (Mt. 16:24) Ni jambo la hekima na linalofaa kumfuata Yesu. Hata hivyo, si rahisi kufanya hivyo sikuzote.
11. Wanafunzi wa Tiro walionyesha jinsi gani upendo wao kwa Paulo na kwamba wanamuunga mkono?
11 Punde si punde, wakati wa Paulo, Luka, na wenzao kuondoka ukafika. Mambo yaliyotokea wanapoondoka yanagusa moyo sana. Yanaonyesha jinsi akina ndugu wa Tiro walivyompenda Paulo na walivyounga mkono kabisa huduma yake. Wanaume, wanawake, na watoto walimsindikiza Paulo na wenzake hadi ufuoni. Walipiga magoti na kusali pamoja kisha wakaagana. Baadaye, Paulo, Luka, na wenzao wakapanda meli na kuendelea na safari yao hadi Tolemai, ambako waliwakuta akina ndugu na kukaa pamoja nao kwa siku moja.—Mdo. 21:5-7.
12, 13. (a) Filipo alikuwa na rekodi ya aina gani ya kutumikia kwa uaminifu? (b) Akina baba Wakristo leo, wanaweza kuiga jinsi gani mfano wa Filipo?
12 Kisha, Luka anaripoti kwamba Paulo na wasafiri wenzake wakaelekea Kaisaria. Walipofika huko, ‘wakaingia katika nyumba ya Filipo mweneza-injili.’a (Mdo. 21:8) Lazima walifurahi sana kumwona Filipo. Miaka 20 hivi iliyopita huko Yerusalemu, Filipo alikuwa amewekwa rasmi na mitume asaidie kugawanya chakula katika kutaniko jipya la Kikristo. Filipo alikuwa mhubiri mwenye bidii kwa muda mrefu. Kumbuka kwamba wanafunzi walipotawanyika kwa sababu ya mateso, Filipo alienda Samaria na kuanza kuhubiri. Baadaye, alimhubiria na kumbatiza towashi Mwethiopia. (Mdo. 6:2-6; 8:4-13, 26-38) Alikuwa na rekodi nzuri sana ya kutumikia kwa uaminifu!
13 Filipo hakupunguza bidii yake katika huduma. Akiwa Kaisaria, bado alikuwa na bidii katika kazi ya kuhubiri, kama Luka anavyoonyesha kwa kumwita “mweneza-injili.” Pia, tunaambiwa kwamba alikuwa na binti wanne waliokuwa wakitoa unabii, jambo linaloonyesha kwamba walifuata mfano wa baba yao.b (Mdo. 21:9) Hivyo, lazima Filipo alikuwa amefanya mengi ili kuijenga nyumba yake kiroho. Akina baba Wakristo wanapaswa kufuata mfano wake, kwa kuwa na bidii katika huduma na kuwasaidia watoto wao waipende kazi ya kuhubiri.
14. Ziara za Paulo zilitokeza nafasi ya nini, nasi tuna nafasi gani kama hizo leo?
14 Popote alipoenda, Paulo aliwatafuta waabudu wenzake na kukaa pamoja nao. Akina ndugu walikuwa tayari kumkaribisha mmishonari huyo na wenzake. Bila shaka, ziara hizo zilikuwa pindi za ‘kutiana moyo.’ (Rom. 1:11, 12) Kuna nafasi nyingi kama hizo leo. Unaweza kupata baraka nyingi kwa kumkaribisha mwangalizi wa mzunguko na mke wake nyumbani kwako, hata ikiwa hauna vitu vingi vya kimwili.—Rom. 12:13.
“Niko Tayari . . . Kufa” (Mdo. 21:10-14)
15, 16. Agabo alileta habari gani, nazo zilikuwa na matokeo gani kwa wale waliozisikia?
15 Paulo alipokuwa akikaa na Filipo, mgeni mwingine aliyeheshimiwa akafika. Jina lake ni Agabo. Waliokuwa wamekusanyika nyumbani kwa Filipo walijua kwamba Agabo ni nabii; alikuwa ametabiri njaa kubwa wakati wa utawala wa Klaudio. (Mdo. 11:27, 28) Huenda walianza kujiuliza: ‘Kwa nini Agabo amekuja? Ana ujumbe gani?’ Walipokuwa wakimtazama kwa makini, alichukua mshipi wa Paulo—kitambaa kirefu ambacho kingeweza kubeba pesa na vitu vingine, nacho kilikuwa kikifungwa kiunoni. Agabo akafunga miguu na mikono yake. Kisha akaanza kuzungumza. Ujumbe wake ulikuwa mzito: “Hivi ndivyo roho takatifu inavyosema, ‘Wayahudi kule Yerusalemu watamfunga hivi mwanamume ambaye mshipi huu ni wake, nao watamtia mikononi mwa watu wa mataifa.’”—Mdo. 21:11.
16 Kulingana na unabii huo, ni wazi kwamba Paulo angeenda Yerusalemu. Pia, unabii huo ulionyesha kwamba baadaye Wayahudi wangemtia “mikononi mwa watu wa mataifa.” Unabii huo uliwahangaisha sana wale waliokuwako. Luka anaandika: “Tuliposikia hayo, sisi na wale waliokuwa hapo tukaanza kumsihi Paulo asipande kwenda Yerusalemu. Kisha Paulo akasema: ‘Kwa nini mnalia na kujaribu kunivunja moyo? Muwe na hakika kwamba niko tayari si kufungwa tu bali pia kufa huko Yerusalemu kwa ajili ya jina la Bwana Yesu.’”—Mdo. 21:12, 13.
17, 18. Paulo alionyesha azimio lake jinsi gani, na akina ndugu walitendaje?
17 Wazia hali hiyo. Akina ndugu, kutia ndani Luka, wanamsihi Paulo asiende. Baadhi yao wanalia. Akichochewa na hangaiko lao lenye upendo kwake, Paulo anasema kwa upole kwamba ‘wanajaribu kumvunja moyo,’ au kama tafsiri fulani zinavyosema, ‘wanaudhoofisha moyo wangu.’ Hata hivyo, azimio lake ni thabiti, na kama vile ilivyokuwa alipokutana na ndugu wa Tiro, hatakubali sihi zao au machozi yao yamfanye akengeuke. Badala yake, anawaeleza kwa nini lazima aende. Alikuwa ameazimia na alionyesha ujasiri! Kama alivyofanya Yesu, Paulo ameazimia kabisa kwenda Yerusalemu. (Ebr. 12:2) Paulo hakutaka kufa kimakusudi kwa sababu ya imani yake, lakini ikiwa angeuawa, angeona kuwa ni jambo la heshima kufa akiwa mfuasi wa Kristo Yesu.
18 Akina ndugu walitendaje? Waliheshimu msimamo wake. Tunasoma hivi: “Tuliposhindwa kumshawishi, tukaacha kumkataza, tukasema: ‘Mapenzi ya Yehova na yatendeke.’” (Mdo. 21:14) Waliojaribu kumshawishi Paulo asiende Yerusalemu hawakushikilia maoni yao. Walimsikiliza Paulo na kukubali maoni yake, wakitambua na kukubali mapenzi ya Yehova yatendeke, ingawa haikuwa rahisi kwao. Paulo alikuwa ameanza safari ambayo baadaye ingeweza kusababisha kifo chake. Mambo yangekuwa rahisi zaidi kwa Paulo ikiwa ndugu zake wapendwa wasingejaribu kumshawishi asiende.
19. Tunajifunza jambo gani muhimu kutokana na mambo yaliyompata Paulo?
19 Tunajifunza jambo muhimu kutokana na mambo yaliyompata Paulo: Hatupaswi kamwe kuwavunja moyo wengine wasiishi maisha ya kujidhabihu katika utumishi wao kwa Mungu. Tunaweza kutumia kanuni hiyo katika hali nyingi, si wakati tu ambapo uhai uko hatarini. Kwa mfano, ingawa wazazi wengi Wakristo huhuzunika watoto wao wanapoondoka nyumbani na kwenda kumtumikia Yehova katika nchi za kigeni, wameazimia kutowavunja moyo. Phyllis, anayeishi Uingereza, anakumbuka jinsi alivyolia sana wakati binti yake wa pekee alipoenda kutumikia akiwa mmishonari barani Afrika. Phyllis anasema hivi: “Nilihuzunika sana. Haikuwa rahisi kwangu kukubali kwamba atakuwa mbali sana. Nilihuzunika, lakini pia nilimwonea fahari. Nilisali sana. Hata hivyo, ulikuwa uamuzi wake, nami sikujaribu kamwe kuubadili. Sikuzote nilikuwa nimemfundisha kutanguliza Ufalme! Ametumikia katika nchi za kigeni kwa miaka 30, nami humshukuru Yehova kila siku kwa sababu ya uaminifu wake.” Ni jambo zuri sana tunapowatia moyo waabudu wenzetu wanaojidhabihu!
Ni vizuri kuwatia moyo waabudu wenzetu wanaojidhabihu
“Akina Ndugu Wakatukaribisha kwa Furaha” (Mdo. 21:15-17)
20, 21. Tunajuaje kwamba Paulo alipenda kuwa pamoja na ndugu zake, na kwa nini alipenda kuwa pamoja na waabudu wenzake?
20 Matayarisho yalifanywa, naye Paulo akaendelea na safari yake, akisindikizwa na akina ndugu ambao kwa kufanya hivyo walimhakikishia kwamba wanamuunga mkono. Kila mahali walipopita katika safari yao kuelekea Yerusalemu, Paulo na wenzake walishirikiana na ndugu na dada zao Wakristo. Katika jiji la Tiro, walipata wanafunzi na kukaa nao siku saba. Walipokuwa Tolemai, waliwasalimu dada na ndugu zao na kukaa huko siku moja. Kaisaria, walikaa siku kadhaa katika nyumba ya Filipo. Kisha, baadhi ya wanafunzi kutoka Kaisaria wakamsindikiza Paulo na wenzake hadi Yerusalemu, ambapo walikaa kwa Mnasoni, mwanafunzi wa awali. Hatimaye, wasafiri hao walipofika Yerusalemu, Luka anaripoti kwamba ‘akina ndugu waliwakaribisha kwa furaha.’—Mdo. 21:17.
21 Ni wazi kwamba Paulo alipenda kuwa pamoja na waabudu wenzake. Mtume huyo alitiwa moyo na ndugu na dada zake, kama ilivyo leo. Bila shaka, baada ya Paulo kutiwa moyo na kuimarishwa na akina ndugu, angeweza kukabiliana na wapinzani wenye hasira waliotaka kumuua.
a Ona sanduku lenye kichwa “Kaisaria—Jiji Kuu la Mkoa wa Yudea.”
b Ona sanduku lenye kichwa “Je, Wanawake Wanaweza Kuwa Wahudumu Wakristo?.”
-