Je! Utii Unafaa, Sikuzote?
“UMESIKIA nilivyosema?” mama anapaaza sauti kwa Jioni mdogo anapopitia mlangoni kwenda nje. Kwa kufanya hivyo hawi akichunguza kama masikio ya Jioni yanafanya kazi. Yeye anahakikisha kwamba Jioni atamtii na kuwapo nyumbani wakati unaofaa.
Kweli kweli, kusikia na kutii ni mambo yanayohusiana kwa ukaribu. Basi, si ajabu kwamba katika zile lugha za asili za Biblia, maneno yanayoonyesha utii yanahusiana na kusikia. Lakini ni nani ambaye sisi tunapaswa kutegea sikio letu la usikilizaji? Je! tunapaswa kumpa utii kila mtu anayeudai? Na je! utii unafaa sikuzote?
Wakati Utii Unapofaa
Utii kwa Muumba wetu, Yehova Mungu, unafaa sikuzote. Akiwa ndiye Mfanyi na Chanzo cha uhai wetu, yeye ndiye anayestahili utii wa kwanza wa viumbe wake. (Zaburi 95:6, 7) Akiwa ndiye Mwenye Enzi aliye Mkuu Zaidi, Yehova anaweka itibari ya mamlaka yake kwa wengine ambao wanatimiza viwango vyake, na hiyo inafanya utii wetu kwao ufae. Anayetangulia kabisa miongoni mwa watu hao ni Yesu Kristo. Tangu 1914 yeye amekuwa Mfalme mwekwa-rasmi na Mungu wa Ufalme wa kimbingu, “kwamba jamii za watu, vikundi vya kitaifa na lugha zipaswe zote kutumikia hata yeye.” (Danieli 7:13, 14, NW) Zaidi ya hilo, akiwa ndiye Kichwa cha kundi la Kikristo, Yesu amewapa mamlaka wengine walio humo, hiyo ikifanya utii wetu kwa hao wachungaji-wadogo ufae.—Waebrania 13:17.
Yehova ameweka pia miongozo kuhusu lile jambo la utii ndani ya jamaa. Watoto wanaonywa kwa upole ‘watii wazazi wao katika muungano pamoja na Bwana,’ na wake wanaambiwa wawe katika ‘kujiweka chini ya waume zao kama kwa Bwana.’ (Waefeso 5:21–6:3, NW) Wakristo hata wanakumbushwa ‘wawe katika kujiweka chini na kuwa watii kwa serikali na mamlaka zilizo watawala.’ (Tito 3:1, NW) Hata hivyo, katika yote hayo, je! utii wetu unapasa kuwa kamili? Je! unafaa sikuzote?
Wakati Utii Unapokuwa Haufai
Bila shaka, kusikiliza wale ambao hawakupewa itibari ya mamlaka kutoka kwa Yehova kunaweza kutokeza msiba. Mwanadamu wa kwanza, Adamu, ‘alisikiliza’ sauti ya Hawa na akajiunga naye katika kula kutokana na ule mti wa maarifa ya kujua mema na mabaya. (Mwanzo 3:17, NW) Tokeo lilikuwa nini? “Kupitia ukosefu wa utii wa mwanadamu mmoja wengi walifanyizwa kuwa watenda dhambi.” (Warumi 5:19, NW) Ni tokeo lenye msiba kama nini kutokana na kusikiliza mtu asiyefaa.
Hata hivyo, inafaa sikuzote kusikiliza wale ambao wamepewa itibari ya vyeo vya mamlaka? Si ikiwa wao wanajaribu kutumia mamlaka yao katika njia isiyo ya kimungu. Mathalani, kupatana na kanuni ya kutii ‘mabwana-wakubwa katika maana ya kimnofu,’ sisi tungetii waajiri-kazi wetu. Lakini namna gani ikiwa wao wanatuagiza tutende jambo fulani linalohitilafiana na sheria za Mungu aliye mweza yote? Jambo ambalo Paulo alifuatisha kusema linaonyesha mwendo unaofaa kufuatwa: “Si kwa njia ya utumishi wa kujionyesha kama wapendeza wanadamu, bali kama watumwa wa Kristo, kwa kufanya mapenzi ya Mungu kwa nafsi yote.” (Waefeso 6:5, 6, NW) Katika pindi nyingine, Petro na mitume wale wengine walisema: “Ni lazima sisi tutii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29, NW.
Kanuni hiyo hiyo inatumika ndani ya jamaa. Kwa kutothamini matakwa ya kimungu, huenda mume akakatalia kibali cha tamaa ya mke wake kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa ukawaida. Ingekuwaje kama yeye angetia mkazo juu yake, hata kugeukia kumtenda jeuri, kama ambavyo imekuwa nyakati fulani, ili amwachishe kwenda kwenye mikutano ya Kikristo. Inampasa mke huyo afanye nini? Kama yeye angekubali tu bila kujitetea, huenda akahatarisha hali yake mwenyewe ya kiroho, pia ile ya jamaa yake, na apoteze tumaini la uhai wa milele. Je! haingekuwa vizuri zaidi kutii Yehova, aking’amua kwamba hakuna binadamu ye yote, hata mume wake, ambaye amekabidhiwa mamlaka ya kutangua ile amri ya ‘kutoacha kujikusanya wenyewe pamoja’?—Waebrania 10:25, NW.
Mume wa Miyoko alikataa kwamba mshahara wake kuwa ‘ukitapanywa’ kwa ki hudhuria kwake mikutano ambayo yeye hakukubalia. Mwishowe, yeye aliacha kutoa pesa za utunzaji wa nyumba, na Miyoko akalazimika kutembea umbali wa saa moja kwenda kwenye Jumba la Ufalme.
Je! yeye alichoka na kuacha? Hapana. Alifikia Yehova katika sala na akachanganua hali yake. Kwa kung’amua sababu ya upinzani wa mume wake, Miyoko aliamua kuanza kazi ya kupelekea watu karatasi-habari. Mume wake alikubali, mradi yeye angempa mumeye nusu ya mapato yake.
Miyoko alisali tena ili apate watu wa hapo karibu wa kuzichukua karatasi-habari kwa ukawaida, ikiwa ni mapenzi ya Yehova. Kwa kawaida, inachukua mwaka mmoja hivi ili mtu apate anachotaka. Lakini, kwa kushangaza, katika muda wa majuma sita Miyoko alielekezewa toleo la kuwa akipelekea watu karatasi-habari pale pale karibu na nyumbani kwake. Kwa kutiwa moyo na fikira ya kwamba Yehova alisikia sala zake, yeye alifanya kazi kutoka saa 10:30 mpaka saa 12:00 kila asubuhi. Kuona hivyo, mwelekeo wa mume wake ulibadilika pole kwa pole akawa mwenye ushirikiano. Sawa na vile Miyoko, ambaye anatumikia kwa ukawaida akiwa painia-msaidizi, alivyofikiria hali yake na kuichanganua, akasali juu yayo kisha akatenda akiwa na mwelekeo chanya, wewe pia utapata kwamba hii itatokeza baraka ya Yehova.
Bila shaka, huenda kukawa na sababu za pekee zinazofanya mume asiyeitikadi aombe mke wake akose mkutano fulani wa Kikristo. Huenda yeye akafanya hivyo bila kusudio lo lote la kutaka kulegeza-legeza ibada na utumishi wake kwa Yehova Mungu. Kuelewa kanuni zinazohusika kutasaidia mwanamke Mkristo aamue kwa usahihi kulingana na ile hali mahususi inayomhusu yeye.
Kwa kuzungumzia jambo hili hatua moja zaidi, namna gani ikiwa , mume wake anamwambia asipeleke watoto wao kwenye mikutano ya Kikristo? Bila shaka, mke anajua kwamba j ingawa mume wake hakubali ukichwa wa Kristo, bado mume huyo ndiye kichwa cha jamaa. (1 Wakorintho 11:3) Na bado, mke anafikiria moyoni pia hali njema ya kiroho ya watoto, na pia tamaa yake mwenyewe kuwa mtii kwa Yehova. Kwa uhakika ni mtihani wa imani yake kuishi kulingana na —wajibu wake mbalimbali katika maeneo haya. Kupelekea Yehova sala ili kuomba hekima na utambuzi kungesaidia hakika. (Yakobo 1:5; Wafilipi 4:6, 7) Kuzungumza na mumeye kwa kumpa sababu za mambo na kuonyesha roho ya utulivu na upole, huenda pia kukasaidia katika kutatua muhali huo.—Wakolosai 4:6; 1 Petro 3:1-5.
Mwanamke mmoja Mkristo katika Yamato, Japani, alielekeana na hali hiyo wakati mume wake alipomkataza kupeleka watoto wao watatu kwenye mikutano. Yeye angeweza kufanya nini? Aliwafundisha kwa bidii watoto wake nyumbani, na wakati wao walipofikia umri wa kutosha kufanya maamuzi yao wenyewe, kila mmoja alichukua msimamo kwa ajili ya Yehova na kuanza kuhudhuria mikutano. Kwa kupatwa na hasira kali, mume aliwafukuza wote nyumbani mwake.
Mke huyo alipata kazi na akatulia kwa muda kwenye kijumba fulani cha jengo la dada mmoja. Lakini yeye hakuachia mambo hapo. Yeye alirudi kusafisha nyumba ya mume wake na kumtayarishia milo. Hatimaye, baada ya mwezi mmoja hivi, mume aliwarudisha na akaacha kuwapinga. Lo, thawabu kama nini kwa mwendo wa uaminifu wa mke huyo!
‘Zifanyieni Mtihani Semi Zilizovuviwa’
Namna gani juu ya mamlaka katika kundi la Kikristo? Kwa kuwa wale walio katika vyeo vya madaraka wamewekwa rasmi na utendaji wa roho takatifu na wanategemeza shauri na onyo lao la upole juu ya Neno la Mungu, sisi tunaweza kuwa na uhakika kwamba inafaa kutii mamlaka iliyowekwa rasmi katika kundi la Kikristo. (Matendo 20:28; Waebrania 13:17) Lakini hiyo haimaanishi kwamba sisi tutii mamlaka bila kufanya mfikirio upasao juu ya mambo yanayosemwa. Kwa sababu gani?
Mtume Yohana alitoa shauri hili: “Usiitikadi kila usemi uliovuviwa, bali zifanyie mtihani semi zilizovuviwa uone kama hizo zina asili ya kutoka kwa Mungu.” (1 Yohana 4:1, NW) Hiyo haimaanishi kwamba inatupasa sisi tuwe na tuhuma juu ya kila jambo ambalo wengine wanatuambia. Bali, tunazingatia katika akili zetu maneno ya Paulo kwenye Wagalatia 1:8, AW: “Hata ikiwa sisi au malaika kutoka mbinguni angewatangazia ninyi kuwa habari njema jambo fulani linalozidi lile ambalo sisi tuliwatangazia ninyi kuwa habari njema, acheni huyo awe mlaaniwa.”
Je! habari ambazo ziko mbele yetu ni tofauti na zile ambazo tumefundishwa kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye uangalifu”? Je! mtu ambaye anaeneza ujumbe huo ananena ili kuheshimu jina la Yehova, au anajaribu kujikweza yeye mwenyewe? Je! habari hizo zinapatana na mafundisho ya ujumla ya Biblia? Hayo ni maswali ambayo yatatusaidia katika ‘kufanyia mtihani’ jambo lo lote ambalo huenda likasikika kuwa la kutilika mashaka. Sisi tunaonywa kwa upole ‘tuhakikishe mambo yote; tushike sana yaliyo mema.’—Mathayo 24:45; 1 Wathesalonike 5:21, NW.
Kielelezo cha kupendeza katika habari hii ni kile cha Mwamuzi Gideoni. Ili ahakikishe kwamba Yehova angekuwa pamoja naye, Gideoni alinuia kwamba mtihani fulani ufanywe: “Tazama, nitaweka ngozi ya kondoo katika kiwanja cha kupuria,” yeye akasema kwa Yehova. “Kama ukiwapo umande juu ya ngozi tu, na nchi yote ikiwa kavu, basi, hapo ndipo nitakapojua ya kuwa utawaokoa Israeli kwa mkono wangu.” Yehova aliposababisha hilo litukie sawa na takwa lililoombwa, Gideoni alitaka uhakikisho zaidi: “Sasa ngozi tu na iwe kavu, na uwe umande juu ya nchi yote.”—Waamuzi 6:37-39.
Je! Gideoni alikuwa mwenye nadhari au tuhuma kupita kiasi? Haionekani hivyo, kwa sababu Yehova alikubali takwa aliloomba mara zote mbili, na akafanya sawa na vile alivyoomba. Gideoni alitaka kuwa na uhakika kwamba msimamo wake ulifaa. Kwa kuwa hakuwa na Neno la Mungu lililoandikwa kama sisi tulivyo nalo, hiyo ilikuwa ndiyo njia yenye matokeo mazuri kwa Gideoni ‘kuhakikishia’ jambo hilo. Hata hivyo, mara alipokwisha kupokea uhakikisho, yeye alitii kabisa kabisa maagizo kutoka kwa Yehova, ingawa kusukuma wanaume 300 dhidi ya jeshi la adui 135,000 kungeonekana kama kuwafanya wakajiue wenyewe tu, kulingana na maoni ya kibinadamu. (Waamuzi 7:7; 8:10) Je! sisi tunaonyesha mwelekeo huo huo kwa kutafuta-tafuta katika Neno la Mungu mapenzi ya Yehova ni nini hasa, kisha kushikamana nayo?
Uchaguzi Ulio wa Hekima Zaidi
Yehova hatutazamii tuonyeshe itikadi ya kukubali-kubali mambo kwa upofu. Yeye hataki kutoka kwetu utii wa aina ambayo mzoezaji anapata kutoka kwa mnyama kwa kutumia lijamu au kiboko. Hiyo ndiyo sababu yeye aliambia Daudi: “Msijifanye wenyewe kuwa kama farasi au nyumbu asiye na uelewevu, ambaye uchangamfu wake wa roho ni wa kuzuiliwa hata kwa lijamu au kisimamishaji.” (Zaburi 32:9, NW) Badala ya hivyo, Yehova ametupa sisi uwezo wa kufikiri na utambuzi kwamba, kwa kutegemea uelewevu, sisi tuweze kuchagua kumtii yeye.
Katika Kijapani, neno kiku (sikia) linatia ndani maana, si ya kusikiliza na kutii tu, bali pia ya kuhukumu kama jambo ni jema au baya. Wakati mtu fulani anaposema kwa sisi, ni vema kusikiliza katika maana hiyo ili tunapotii, tuwe tunafanya hivyo si kwa kukubali-kubali mambo bila msingi, bali kwa uchaguzi wetu. Wakati Baba yetu wa kimbingu, Yehova Mungu, anaponena, iwe ni kupitia Neno lake, Biblia, au kupitia tengenezo lake la kidunia, ni jambo la maana hata zaidi tusikilize na kutii, hivyo tukithibitisha kwamba sisi ni waabudu watii, ambao hawapuuzi kikumbusha hiki chenye upendo: “Umesikia nilivyosema?”
[Picha katika ukurasa wa 29]
Mimi napaswa kusikiliza nani?
[Picha katika ukurasa wa 31]
Gideoni alitafuta-tafuta mapenzi ya Yehova na akamtii yeye