Tusirudi Nyuma Kamwe Kwenye Uangamivu!
“Sisi si namna irudiyo nyuma kwenye uangamivu.”—WAEBRANIA 10:39.
1. Ni hali zipi zilizomfanya mtume Petro ashindwe na hofu?
NI LAZIMA mitume wawe walishtuka sana wakati Bwana-Mkubwa wao mpendwa, Yesu, alipowaambia kwamba hao wote wangetawanyika na kumwacha. Ingewezekanaje wamwache wakati huo ambapo angewahitaji zaidi? Petro alisisitiza: “Hata ikiwa wengine wote wakwazika, hata hivyo hakika mimi sitakwazika.” Kwa kweli Petro alikuwa mjasiri na shujaa. Lakini Yesu aliposalitiwa na kukamatwa, mitume—kutia ndani Petro—walitawanyika. Baadaye, Yesu alipokuwa akihojiwa katika nyumba ya Kuhani wa Cheo cha Juu, Kayafa, Petro alikuwa amekaa kwenye ua akiwa na wasiwasi. Usiku huo wenye baridi ulipozidi kuyoyoma, yaelekea Petro alianza kuhofu kwamba huenda Yesu angeuawa pamoja na mtu yeyote aliyeshirikiana naye. Watu wengine waliosimama kando walipomtambua Petro kuwa mmojawapo wa waandamani wa karibu wa Yesu, Petro akashikwa na hofu. Mara tatu akakataa kwamba hana uhusiano na Yesu. Petro akakana kwamba hata hamjui!—Marko 14:27-31, 66-72.
2. (a) Kwa nini mwenendo wa Petro wenye hofu ule usiku ambao Yesu alikamatwa haumaanishi kwamba alikuwa wa “namna irudiyo nyuma”? (b) Azimio letu lapaswa kuwa nini?
2 Huo ukawa wakati ambapo Petro alivunjika moyo sana katika maisha yake, wakati ambao yaelekea alijutia maisha yake yote. Lakini, je, mwenendo wa Petro usiku huo ulimaanisha kwamba yeye ni mwoga? Je, mwenendo huo ulimfanya awe mtu wa “namna” ambayo mtume Paulo alitaja baadaye alipoandika: “Sasa sisi si namna irudiyo nyuma kwenye uangamivu”? (Waebrania 10:39) Yaelekea wengi wetu wangekubali kwamba maneno ya Paulo hayamhusu Petro. Kwa nini? Kwa sababu hofu ya Petro ilikuwa ya muda tu, pindi fupi tu katika maisha yake yaliyojaa ujasiri na imani yenye kutokeza. Vivyo hivyo, kuna pindi fulani katika maisha yetu ambazo sisi hukumbuka na kuaibika kwa kadiri fulani, wakati ambapo tulishikwa na hofu kwa ghafula na kushindwa kutetea kweli kwa ujasiri kama ambavyo tungalipenda. (Linganisha Waroma 7:21-23.) Tuwe na hakika ya kwamba kupatwa na pindi kama hizo za muda tu hakumaanishi kwamba sisi ni namna irudiyo nyuma kwenye uangamivu. Lakini, bado twahitaji kuazimia tusiwe kamwe wa namna irudiyo nyuma. Kwa nini? Na twaweza kuepukaje kuwa watu wa aina hiyo?
Maana ya Kurudi Nyuma Kwenye Uangamivu
3. Manabii Eliya na Yona walishindwaje na hofu?
3 Paulo alipoandika juu ya “namna irudiyo nyuma,” yeye hakumaanisha wale ambao huenda wakapatwa na woga kwa muda mfupi. Kwa kweli Paulo alijua kisa cha Petro pamoja na visa vingine kama hivyo. Pindi moja Eliya, nabii jasiri na mwenye kusema wazi, alishindwa na hofu, akatoroka asiuawe kwa sababu Malkia mwovu Yezebeli alitisha kumwua. (1 Wafalme 19:1-4) Nabii Yona alishikwa na hofu mbaya hata zaidi. Yehova alimpa mgawo wa kwenda jiji la Ninewi lililojaa sana uovu na ujeuri. Mara moja Yona akapanda meli, akaelekea Tarshishi—iliyokuwa kilometa 3,500 upande tofauti! (Yona 1:1-3) Lakini wala manabii hawa wala mtume Petro hawawezi kwa kweli kusemwa kuwa wa namna irudiyo nyuma. Kwa nini?
4, 5. (a) Muktadha watusaidiaje kujua alilomaanisha Paulo kwa neno “uangamivu” kwenye Waebrania 10:39? (b) Paulo alimaanisha nini aliposema: “Sisi si namna irudiyo nyuma kwenye uangamivu”?
4 Ebu tazama maneno yote ambayo Paulo alitumia: “Sasa sisi si namna irudiyo nyuma kwenye uangamivu.” Alimaanisha nini kwa neno “uangamivu”? Nyakati nyingine neno la Kigiriki alilotumia lahusu uharibifu wa milele. Ufafanuzi huo wapatana na muktadha wa maneno hayo. Paulo alikuwa ametoka tu kutoa onyo hili: “Tukizoea dhambi kwa kusudi baada ya kuwa tumepokea ujuzi sahihi juu ya kweli, hakuna tena dhabihu yoyote iliyoachwa kwa ajili ya dhambi, lakini kuna taraja fulani lenye hofu la hukumu na kuna wivu wenye moto utakaowala kabisa wale walio katika upinzani.”—Waebrania 10:26, 27.
5 Kwa hiyo Paulo alipowaambia waamini wenzake, “Sisi si namna irudiyo nyuma kwenye uangamivu,” alimaanisha kwamba yeye pamoja na Wakristo waaminifu waliosoma barua yake waliazimia kwamba hawatamwacha Yehova kamwe wala hawataacha kumtumikia. Kufanya hivyo kungesababisha uangamivu wa milele. Yudasi Iskariote alirudi nyuma kwenye uangamivu huo, na vilevile maadui wengine wa ile kweli ambao walipinga kimakusudi roho ya Yehova. (Yohana 17:12; 2 Wathesalonike 2:3) Watu hao wako miongoni mwa “waoga” ambao wataharibiwa milele katika ziwa la moto la mfano. (Ufunuo 21:8) Hatutaki kamwe kuwa wa namna hiyo!
6. Shetani Ibilisi anataka tuwe na mwenendo wa aina gani?
6 Shetani Ibilisi anataka turudi nyuma kwenye uangamivu. Kwa kuwa yeye ni stadi wa “matendo yenye hila,” anajua kwamba mwenendo wenye kudhuru kama huo huanza kwa mambo madogo-madogo. (Waefeso 6:11, kielezi-chini katika New World Translation of the Holy Scriptures—With References) Shetani akishindwa kufaulu kwa mnyanyaso wa moja kwa moja, yeye hujaribu kudhoofisha imani ya Wakristo wa kweli kupitia njia zenye hila zaidi. Yeye hutaka Mashahidi wa Yehova wajasiri na wenye bidii wanyamazishwe. Ebu tuone mbinu alizotumia dhidi ya Wakristo Waebrania ambao Paulo aliwaandikia.
Jinsi Wakristo Walivyosongwa Warudi Nyuma
7. (a) Kutaniko lililokuwa Yerusalemu lilikuwa limepatwa na nini? (b) Baadhi ya watu waliosoma barua ya Paulo walikuwa katika hali zipi za kiroho?
7 Uthibitisho waonyesha kwamba Paulo aliwaandikia Waebrania barua wapata mwaka wa 61 W.K. Kutaniko lililokuwa Yerusalemu lilikuwa limepatwa na mvurugo sana. Baada ya kifo cha Yesu, mnyanyaso mkali uliibuka, ukiwalazimisha Wakristo wengi waliokuwa jijini humo kutawanyika. Hata hivyo, kipindi cha amani kikafuata, na kufanya Wakristo waongezeke. (Matendo 8:4; 9:31) Kadiri miaka ilivyopita, minyanyaso na magumu mengine yakatokea pindi kwa pindi. Inaonekana kwamba kufikia wakati Paulo alipowaandikia Waebrania barua, kutaniko lilikuwa limepata tena amani kwa kadiri fulani. Lakini bado kulikuwa na mikazo mingine. Miongo mitatu hivi ilikuwa imepita tangu Yesu alipotabiri uharibifu wa Yerusalemu. Yaelekea kulikuwa na watu waliohisi kwamba mwisho ulikuwa umekawia kupita kiasi na huenda mwisho huo usingekuja wakiwa wangali hai. Wengine, hasa wapya katika imani, bado hawakuwa wamejaribiwa na mnyanyaso mkali na hawakujua uhitaji wa kuvumilia wanaponyanyaswa. (Waebrania 12:4) Kwa kweli Shetani alijaribu kutumia hali kama hizo. Alitumia “matendo [gani] yenye hila”?
8. Wayahudi wengi walikuwa na maoni gani juu ya kutaniko changa la Kikristo?
8 Wayahudi waliokuwa Yerusalemu na Yudea walilidharau kutaniko changa la Kikristo. Kutokana na mambo yaliyoandikwa katika barua ya Paulo, twapata ufahamu fulani kuhusu dhihaka ambazo viongozi wa dini ya Kiyahudi wenye kiburi na wafuasi wao walikuwa wakiwafanyia Wakristo. Huenda walisema: ‘Tuna lile hekalu kuu Yerusalemu, na limekuwapo kwa karne nyingi! Tuna kuhani mashuhuri wa cheo cha juu anayetumikia huko, pamoja na makuhani wa cheo cha chini. Dhabihu zinatolewa kila siku. Tuna Sheria, ambayo malaika walimpa Musa nayo ilianzishwa kwa ishara kuu kwenye Mlima Sinai. Hili farakano jipya, Wakristo hawa, ambao wameasi Dini ya Kiyahudi, hawana mambo kama haya!’ Je, dhihaka kama hizo zilifaulu? Inaonekana kwamba baadhi ya Wakristo Waebrania walisumbuliwa na mashambulio hayo. Barua ya Paulo ya kuwasaidia ikawajia kwa wakati ufaao kabisa.
Sababu Iliyofanya Wasirudi Nyuma Kamwe Kwenye Uangamivu
9. (a) Ni habari gani inayoenea kote katika barua kwa Waebrania? (b) Ni kwa njia gani Wakristo walitumikia katika hekalu bora kuliko lile la Yerusalemu?
9 Ebu tuchunguze sababu mbili ambazo Paulo aliwapa ndugu zake na dada zake waliokuwa Yudea ili wasirudi nyuma kamwe kwenye uangamivu. Kwanza—ubora wa ibada ya Kikristo—waenea kote katika barua aliyoandikia Waebrania. Kote katika barua yake, Paulo alifafanua ubora huo. Hekalu katika Yerusalemu lilikuwa igizo la kitu halisi ambacho ni kikuu zaidi, hekalu kuu la kiroho la Yehova, jengo “ambalo halikufanywa kwa mikono.” (Waebrania 9:11) Wakristo hao walikuwa na pendeleo la kutumikia katika mpango huo wa kiroho wa ibada safi. Wao walitumikia chini ya agano bora zaidi, agano jipya lililoahidiwa zamani, ambalo Mpatanishi wake, Yesu Kristo, ni bora kuliko Musa.—Yeremia 31:31-34.
10, 11. (a) Kwa nini ukoo wa Yesu haukumfanya asistahili kutumikia akiwa Kuhani wa Cheo cha Juu katika hekalu la kiroho? (b) Ni katika njia zipi Yesu alikuwa Kuhani wa Cheo cha Juu aliye bora kuliko yule aliyekuwa akitumikia kwenye hekalu la Yerusalemu?
10 Wakristo hao pia walikuwa na Kuhani wa Cheo cha Juu aliye bora zaidi, Yesu Kristo. Yeye hakuwa wa ukoo wa Haruni. Badala yake, yeye alikuwa Kuhani wa Cheo cha Juu “kwa mfano wa Melkizedeki.” (Zaburi 110:4) Melkizedeki ambaye ukoo wake haukuandikwa, alikuwa mfalme wa Salemu la kale na vilevile kuhani wake wa cheo cha juu. Basi akawa mfano unaofaa wa kiunabii wa Yesu, ambaye ukuhani wake haukutegemea ukoo wowote ule wa wanadamu ambao hawajakamilika, bali ulitegemea jambo bora zaidi—kiapo cha Yehova Mungu mwenyewe. Kama Melkizedeki, Yesu anatumikia akiwa Kuhani wa Cheo cha Juu na vilevile akiwa Mfalme, ambaye hatakufa kamwe.—Waebrania 7:11-21.
11 Na zaidi, Yesu hakuhitaji kutoa dhabihu kila mwaka tofauti na kuhani wa cheo cha juu kwenye hekalu la Yerusalemu. Dhabihu yake ilikuwa uhai wake mwenyewe mkamilifu, ambao alitoa mara moja kwa wakati wote. (Waebrania 7:27) Dhabihu zote hizo zilizotolewa katika hekalu zilikuwa mifano tu, zikionyesha kile Yesu alichotoa. Dhabihu yake kamilifu iliandaa msamaha wa kweli kwa dhambi za wote wanaodhihirisha imani. Maneno ya Paulo yaliwachangamsha pia kwa sababu yalionyesha kwamba huyu Kuhani wa Cheo cha Juu ndiye yule Yesu asiyebadilika ambaye Wakristo katika Yerusalemu walikuwa wamemfahamu. Alikuwa mnyenyekevu, mwenye fadhili, na mtu awezaye “kushiriki hisia za udhaifu wetu mbalimbali.” (Waebrania 4:15; 13:8) Wakristo hao watiwa-mafuta walitazamia kutumikia wakiwa makuhani wa Kristo wa cheo cha chini! Basi ingewezekanaje hata wafikirie kurudi nyuma kwenye mambo “yaliyo dhaifu na yasiyo na maana” ya Dini ya Kiyahudi yenye ufisadi?—Wagalatia 4:9.
12, 13. (a) Paulo alitaja sababu gani ya pili ya kutorudi nyuma? (b) Kwa nini rekodi iliyopita ya uvumilivu ya Wakristo Waebrania ingewatia moyo wasirudi nyuma kamwe kwenye uangamivu?
12 Kana kwamba uthibitisho huo hautoshi, Paulo aliwapa Waebrania sababu ya pili ya kutorudi nyuma kwenye uangamivu—rekodi yao wenyewe ya uvumilivu. Aliandika: “Fulizeni kukumbuka siku za hapo zamani ambazo katika hizo, baada ya nyinyi kutiwa nuru, mlivumilia shindano kubwa chini ya mateso.” Paulo aliwakumbusha kwamba walikuwa ‘wakifunuliwa wazi kama katika mahali pa michezo’ kwa mashutumu na dhiki. Wengine walikuwa wamefungwa gerezani; wengine walikuwa wamewahurumia wale waliokuwa wamefungwa gerezani na kuwategemeza. Ndiyo, walikuwa wameonyesha mfano mzuri sana wa imani na uvumilivu. (Waebrania 10:32-34) Lakini, kwa nini Paulo aliwaomba ‘wafulize kukumbuka’ mambo kama hayo yenye kuumiza? Je, hilo halingewavunja moyo?
13 Badala yake, ‘kukumbuka siku za hapo zamani’ kungewakumbusha Waebrania jinsi ambavyo Yehova aliwategemeza wakati wa majaribu. Kwa msaada wake, tayari wao walikuwa wamekinza mashambulio mengi ya Shetani. Paulo aliandika: “Mungu si asiye mwadilifu ili asahau kazi yenu na upendo mlioonyesha kwa ajili ya jina lake.” (Waebrania 6:10) Ndiyo, Yehova alikumbuka kazi zao zote zenye uaminifu, akiziweka katika kumbukumbu yake isiyo na mwisho. Twakumbushwa himizo la Yesu la kuweka hazina zetu mbinguni. Hakuna mwizi awezaye kuiba hazina hizo; nondo hawawezi kuzila wala kutu kuziharibu. (Mathayo 6:19-21) Kwa hakika hazina hizi zinaweza kuharibiwa ikiwa tu Mkristo arudi nyuma kwenye uangamivu. Kurudi nyuma kungeharibu hazina zozote ambazo Mkristo ameweka mbinguni. Paulo aliwapa Wakristo Waebrania sababu zenye nguvu kama nini za kutofuatia mwenendo huo! Kwa nini wapoteze miaka yao yote ya utumishi mwaminifu? Lingekuwa jambo linalofaa na bora kabisa kuendelea kuvumilia.
Sababu Inayofanya Tusirudi Nyuma Kamwe Kwenye Uangamivu
14. Tunakabili magumu gani ambayo yanafanana na yale ambayo Wakristo wa karne ya kwanza walikabili?
14 Wakristo wa kweli leo vilevile wana sababu zenye nguvu za kutorudi nyuma. Kwanza, tukumbuke kwamba tumebarikiwa sana kwa sababu tuna ibada safi ambayo Yehova ametuandalia. Kama Wakristo wa karne ya kwanza, sisi twaishi katika wakati ambapo wafuasi wa dini zilizo mashuhuri zaidi wanatudharau na kutudhihaki, wakionyesha kwa kiburi majengo yao makubwa ya kidini yenye kuvutia na mapokeo yao ya kale. Lakini Yehova anatuhakikishia kwamba yeye amekubali ibada yetu. Sisi tuna baraka leo ambazo hata Wakristo wa karne ya kwanza hawakupata. Huenda ukajiuliza, ‘Kwa njia gani?’ Kwani, hao waliishi wakati hekalu la kiroho lilipoanza kutenda kazi. Kristo akawa Kuhani wake wa Cheo cha Juu alipobatizwa mwaka wa 29 W.K. Baadhi yao walikuwa wamemwona Mwana wa Mungu aliyefanya miujiza. Hata baada ya kifo chake, kulikuwa na miujiza zaidi. Lakini kama ilivyotabiriwa, zawadi hizo zikakoma hatimaye.—1 Wakorintho 13:8.
15. Wakristo wa kweli leo wanaishi wakati wa utimizo wa unabii gani, na hilo linamaanisha nini kwetu?
15 Lakini, sisi twaishi katika wakati wa utimizo muhimu wa unabii wenye mambo mengi sana unaohusu hekalu katika Ezekieli sura ya 40-48.a Basi tumeona kurejeshwa kwa mpango wa Mungu wa ibada safi. Hekalu hilo la kiroho limetakaswa na kuondolewa aina zote za uchafu wa kidini na ibada ya sanamu. (Ezekieli 43:9; Malaki 3:1-5) Ebu fikiria manufaa tunazopata kutokana na utakasaji huo.
16. Wakristo wa karne ya kwanza walipatwa na hali gani yenye kuvunja moyo?
16 Katika karne ya kwanza, wakati ujao haukuonekana kuwa mzuri kwa kutaniko la Kikristo lililokuwa limepangwa kitengenezo. Yesu alikuwa ametabiri kwamba hali ingekuwa kama shamba ambalo limetoka tu kupandwa ngano kisha likapandwa magugu mengi, na kufanya iwe vigumu sana kutofautisha baina ya ngano na magugu. (Mathayo 13:24-30) Na ndivyo ilivyokuwa. Kufikia mwisho wa karne ya kwanza, mtume Yohana aliyezeeka alipokuwa kizuizi cha mwisho dhidi ya ufisadi, tayari uasi-imani ulikuwa unasitawi. (2 Wathesalonike 2:6; 1 Yohana 2:18) Muda usio mrefu baada ya mitume kufa, jamii ya kipekee ya makasisi ikaibuka, ikanyanyasa kundi na kuvalia mavazi ya kipekee. Uasi-imani ukaenea sana. Wakristo waaminifu walivunjika moyo kama nini! Waliona mpango mpya uliowekwa kwa ajili ya ibada safi ukishindwa kabisa na ibada iliyofisidika. Hayo yalitokea kwa kipindi kinachopungua nusu karne baada ya Kristo kuanzisha kutaniko.
17. Ni katika maana gani kutaniko la Kikristo la wakati huu limedumu kwa muda mrefu kuliko lile la karne ya kwanza?
17 Sasa ebu ona tofauti iliyopo. Leo, ibada safi tayari imedumu kwa muda mrefu kuliko vile ilivyodumu katika kipindi cha kabla ya vifo vya mitume. Tokea wakati toleo la kwanza la gazeti hili lilipochapishwa mwaka wa 1879, Yehova ametubariki kwa ibada ambayo huzidi kutakaswa. Yehova na Kristo Yesu waliingia katika hekalu la kiroho mwaka wa 1918 kwa ajili ya kulitakasa. (Malaki 3:1-5) Tangu mwaka wa 1919, mpango wa kuabudu Yehova Mungu umesafishwa hatua kwa hatua. Tumeendelea kuuelewa vizuri zaidi unabii wa Biblia pamoja na kanuni zake. (Mithali 4:18) Ni nani astahiliye sifa? Si wanadamu tu wasiokamilika. Ni Yehova pekee, pamoja na Mwana wake aliye Kichwa cha kutaniko, ndiye awezaye kulinda watu Wake kutokana na ufisadi katika nyakati hizi zenye ufisadi. Basi, tusikose kamwe kumshukuru Yehova kwa kuturuhusu tushiriki katika ibada yake safi leo. Na tuazimie kabisa kutorudi nyuma kamwe kwenye uangamivu!
18. Tuna sababu zipi za kutorudi nyuma kamwe kwenye uangamivu?
18 Kama Wakristo hao Waebrania, tuna sababu ya pili ya kukataa mwenendo wenye woga wa kurudi nyuma—rekodi yetu wenyewe ya uvumilivu. Tuwe tumeanza kumtumikia Yehova katika miaka ya karibuni au tumekuwa tukifanya hivyo kwa uaminifu kwa miongo mingi, tuna rekodi nzuri ya kazi njema za Kikristo. Wengi wetu wamewahi kunyanyaswa, iwe ni kufungwa gerezani, kupigwa marufuku, kutendwa kikatili, au kupoteza mali. Wengi zaidi wamekabili upinzani, madharau, dhihaka, na ubaridi wa familia. Sisi sote tumevumilia, tukiendelea na utumishi wetu mwaminifu kwa Yehova japo magumu na majaribu ya maisha. Kwa kufanya hivyo, tumeweka rekodi ya uvumilivu ambayo Yehova hatasahau, akiba ya hazina mbinguni. Basi, kwa hakika huu si wakati wa kurudi nyuma kwenye mfumo wa kale wenye ufisadi ambao tuliacha! Kwa nini tuharibu kazi yetu yote ya bidii? Na hasa leo, wakati ambapo ni “muda kidogo sana” ubakio kabla ya mwisho.—Waebrania 10:37.
19. Ni nini litakalozungumziwa katika makala yetu ifuatayo?
19 Ndiyo, na tuazimie kwamba “sisi si namna irudiyo nyuma kwenye uangamivu”! Badala yake, na tuwe “namna iliyo na imani.” (Waebrania 10:39) Tunawezaje kuwa na hakika ya kwamba sisi ni watu wa namna hiyo, na tunawezaje kuwasaidia Wakristo wenzetu pia wawe wa namna hiyo? Makala yetu ifuatayo itazungumzia jambo hilo.
[Maelezo ya Chini]
Je, Wakumbuka?
◻ Inamaanisha nini kurudi nyuma kwenye uangamivu?
◻ Ni misongo gani iliyokuwa ikiwapata Wakristo Waebrania ambao Paulo aliwaandikia barua?
◻ Paulo aliwapa Waebrania sababu zipi za kutorudi nyuma kwenye uangamivu?
◻ Tuna sababu zipi za kuazimia kutorudi nyuma kamwe kwenye uangamivu?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Hofu iliyompata Petro haikumfanya awe wa “namna irudiyo nyuma kwenye uangamivu”