Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 11/15 kur. 524-528
  • Sisi Hatukuahirisha Mambo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sisi Hatukuahirisha Mambo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KATIKA KASKAZI YENYE BARIDI NYINGI YA JAPAN
  • ZIARA ILIYOZAA MATUNDA
  • UTUMISHI KATIKA OKINAWA
  • MAKUSANYIKO YA KIJAPAN YALETA MAENDELEO
  • KAZI YA KUTAYARISHA KUSANYIKO YABARIKIWA
  • MAISHA YETU YA JAMAA JAPAN
  • MATATIZO KATIKA ELIMU YA JAPAN
  • MAISHA YENYE BARAKA
  • Wajapani Wapokea Zawadi Ambayo Hawakutarajia
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Kuacha Ibada ya Maliki na Kuanza Ibada ya Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1998
  • Mtu Aitapo, Je! Wewe Huitikia?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 11/15 kur. 524-528

Sisi Hatukuahirisha Mambo

Imesimuliwa na Leon Pettitt

“MWENYE kuuangalia upepo hatapanda; naye ayatazamaye mawingu hatavuna.” (Mhu. 11:4) Kukumbuka hivyo kumesaidia Daphne mke wangu, na mimi, kumtumikia Yehova wakati wote tukiwa “mapainia,” kwenda Gilead na kuelekea kwenye mgawo wa umisionari wa nchi ya kigeni​—na vile-vile kukaa hapa tukilea jamaa. Nilipokuwa Uingereza niliacha kufundishwa kazi baada ya miaka miwili ili niwe Shahidi “painia,” nitumie wakati wangu wote kueleza watu habari za ufalme wa Mungu. Naye mke wangu aliacha chuo kikuu kwa kusudi hilo hilo, akiwa amebaki na miaka miwili ya kumaliza masomo. Siku hizo hatukuwa tumekutana. Mwaka 1951, mimi nilihitimu katika Watchtower Bible School of Gilead mjini New York, kisha nikaja Japan. Daphne alikuja miaka minne baadaye, nasi tukaoana katika kiangazi cha 1957. Hatukuanza kuwa na jamaa mpaka mwaka 1968. Sisi tuna wavulana wawili, na yule mkubwa anakwenda katika shule ya Kijapan iliyo karibu.

Muda ambao sisi wawili tulikuwa na uwezo wa kutumia wakati wetu kutumikia kama wamisionari, tulijitoa tupewe mgawo wo wote ambao Watch Tower Society iliona unafaa. Tulikubali migawo tuliyopewa bila kuchagua-chagua, nasi tumepata baraka nyingi sana.

KATIKA KASKAZI YENYE BARIDI NYINGI YA JAPAN

Tulipokwisha oana, mgawo tuliopewa kwanza pamoja na wamisionari wengine wanne ni kufungua kazi katika Hokkaido. Haikuwa mara yetu ya kwanza kupatwa na baridi, lakini hatukuwa tumeishi mahali kama hapa penye baridi nyingi sana na pepo kali zenye theluji nyingi. Hata hivyo, baada ya muda mfupi tuliona kwamba vipindi hivyo virefu vya baridi vilitufungulia njia ya kujifunza Biblia na watu wengi nyumbani kwao, maana hawakuwa na kazi nyingi. Masika yalipofika wanafunzi wetu kadha walikuwa tayari kujiunga nasi katika utumishi wetu wa kutumia Biblia nyumba kwa nyumba.

Nilianza kujifunza na mwanafunzi wa chuo kikuu aliyetaka sana kuwa mwalimu mahali pa mbali ambako waalimu wengi hawakutaka kwenda. Miezi sita kabla hajahitimu, nilipanga kujifunza naye kila siku. Baada ya muda mfupi aliikubali kweli akaamua kufundisha watu Biblia nyakati zote badala ya kuwa mwalimu wa shule. Hata yeye hakuahirisha mambo (hakukawia-kawia). Alipakua theluji, akafyeka miti, akafanyia watu kazi nyumbani kwao na kufanya vibarua ili kujipatia riziki, hata mwishowe akapewa mapendeleo ya kuwa “painia wa pekee.” Leo, yeye pia ana jamaa na anaendelea kutumikia kwa uaminifu akiwa mzee katika mojawapo makundi 866 ya Japan, ya Mashahidi wa Yehova.

Miaka kumi na tisa imekwisha tangu tulipokuja Hokkaido kuanza kundi la kwanza katika Sapporo. Sasa eneo hili la kaskazini lina makundi 75. Baadaye, tulipewa mgawo mwingine kusini, tutembelee makundi ya Kijapan katika mzunguko mmoja. Baada ya kukaa miaka mitatu kaskazini, tuliona kwamba nyakati za baridi Tokyo ni sawa na nyakati za masika.

ZIARA ILIYOZAA MATUNDA

Mke wangu alipokuwa akiwapa watu ushuhuda pamoja na kundi moja la Tokyo, aliingia katika mkahawa mdogo karibu dakika mbili kabla ya saa sita ya adhuhuri. Alishangaa kuona mwenye mkahawa huyo akiandikisha awe akipokea Mnara wa Mlinzi, ingawa alikuwa na kazi nyingi na alielezwa machache tu. Mke wangu alikuja kujua kwamba mtu huyo alikuwa na wakati wa kupumzika alasiri, akarudi juma iyo hiyo pamoja na Shahidi wa hapo na kufanya mipango ya kujifunza naye Biblia. Tangu zamani mtu huyo alitaka sana kusaidia wanadamu wenzake, basi akapata nafasi ya kufanya hivyo alipojifunza kweli. Juma iyo hiyo alifika mkutanoni akiwa amevaa nguo zake nyeupe za kazi, na kila miezi minne tulipotembelea tena kundi hilo, tulimkuta akiwa amefanya maendeleo mengine. Wakati wa ziara moja alitupa mahali pa kulala. Miaka mingi sasa yeye na mke wake wamemtumikia Yehova Mungu wakati wote. Hata siku hizi tunamwona akiwa amevaa nguo zake nyeupe za kazi katika makusanyiko makubwa, anaposimamia kazi ya kupakua na kutayarisha vyakula vinavyoliwa na makumi ya maelfu ya wakusanyikaji. Mkewe na watoto wanafurahi kwamba yeye hakuahirisha mambo wakati mke wangu alipomfikia mara ya ya kwanza.

Baadaye, tulipewa kazi ya “wilaya.” Basi nikawa nitakuwa nikitayarisha makusanyiko makubwa ya Mashahidi wa Yehova kila juma ya pili na kuyahutubia. Sasa tulikuwa wasemaji wafasaha wa Kijapan. Wilaya yetu ilikuwa na zaidi ya nusu ya Japan pamoja na Okinawa.

UTUMISHI KATIKA OKINAWA

Maisha yalikuwa ya kujikokota Okinawa. Katika maeneo mengi, kabla hatujaweza kueleza watu kusudi la kuwatembelea, walikuwa wakituketisha mkekani kwa ukarimu huku tukiletewa chai ya kijani na vipande vya sukari nguru. Sisi tutafurahi daima tukumbukapo ukaribishaji wa Waokinawa wakarimu na upendo wa ndugu zetu wa huko.

Kabla Okinawa haijaunganishwa na Japan tena, mmojawapo dada zetu wa kiroho alikaribia kupoteza kazi yake ya ualimu kwa sababu watoto kadha wa shule yake waliokuwa wakijifunza naye Biblia kwa bidii walikataa kusalimu bendera ya Japan. Mume wake asiyeamini, aliyekuwa mwalimu wa masomo ya juu, alifaulu kumtetea mbele ya wakuu wa shule, kisha akawa mmoja wa Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya uchunguzi aliofanya akijitayarisha kumtetea mkewe. Tulitiwa moyo sana kwa kufanya naye kazi ya nyumba kwa nyumba. Baadaye akawa mzee, akasimamia ujenzi wa Jumba la Ufalme zuri katika Mji wa Koza.

MAKUSANYIKO YA KIJAPAN YALETA MAENDELEO

Kuhudhuria makusanyiko kunasaidia watu waione roho na ukuzi ulio kati ya watu wa Mungu. Siku za zamani wakati makusanyiko ya taifa yalipokuwa yakihudhuriwa na mamia machache tu ya watu, wakati tulipolalia vitanda vilivyokuwa vifupi mno kwa wageni wenye miguu mirefu, wakati tulipokuwa tukiamsha vinywa kwa kula mayai mabichi yaliyomwagwa juu ya wali uliopoa, hatukudhani kwamba kazi ya Yehova ingepanuka sana Japan kama ilivyo leo. Bila shaka makusanyiko yamesaidia kuleta ongezeko.

Waume wengi wasioamini wanahudhuria makusanyiko. Wanashangaa kuona wafanya kazi wengi wenye jamaa kama wao wakihudhuria. Kawaida ya wanaume Wajapan ni kufanya kazi zao kwa bidii nyingi sana. Inakuwa lazima kazi za kampuni zifanywe kabla ya shughuli za jamaa na za mtu binafsi. Watu wengi wanadhani kwamba wakijifunza Biblia, waende mikutanoni, waache kucheza kamari na kuvuta sigareti kisha wafanye mabadiliko mengine, mwishowe watalazimika kuacha kazi zao pia. Wanapokwenda makusanyikoni wanawaona watu waliofanya mabadiliko hayo bila kubadili kazi zao.

Siku moja nilisikia mtu mmoja asiyeamini akimwuliza Shahidi Mjapan, “Lakini wewe ungefanyaje kampuni ikikuambia uiwakilishe katika maziko ya Kibuddha?” Ndugu alimweleza kwamba jambo hilo lilimpata. Badala ya kwenda mazikoni na kuiaibisha jamaa iliyofiwa kwa kutoingia katika ibada yao, yeye alikwenda nyumbani kwao usiku uliotangulia, akawaachia kadi yenye jina lake na zawadi iliyotolewa na kampuni kisha akawaeleza asingeweza kuhudhuria maziko kesho yake. Watu wasioamini wanapoonana hivyo na Mashahidi, wanajua kwamba wanaweza kufuata kanuni za Biblia bila kulazimika kubadili kazi zao za kimwili.

KAZI YA KUTAYARISHA KUSANYIKO YABARIKIWA

Wakati wa kutayarisha kusanyiko katika mji fulani, mke mmoja alimwomba mumewe asiyeamini apelekee wafanya kazi chakula cha mchana katika makao makuu ya kusanyiko. Makundi ya karibu yalikuwa yakipokezana zamu ya kufanya hivyo. Wafanya kazi walimkaribisha ale pamoja nao, na baada ya muda mfupi akapendezwa na mambo yaliyozungumzwa. Tatizo lililokuwa likizungumzwa ni jinsi ya kutengeneza miguu ya vijiti vya kutengeneza mbao za kukaliwa na watu 10,000. Mtu mmoja alipendekeza mitaimbo itumiwe, halafu mgeni huyo akawaeleza yeye ni mwuza mitaimbo na kwamba angewapa bure mitaimbo kadha. Mgeni huyo asiyetazamiwa alitatua tatizo la wafanya kazi hao wa kusanyiko, nayo hatua hiyo ikawa ndiyo mwanzo wa kubadili maisha yake mwenyewe. Sasa ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova.

Katika kusanyiko ilo hilo la mataifa yote ndipo dada “painia” alipomwandikia msimamizi wa kampuni kubwa zaidi ya Osaka inayotengeneza vifaa vya umeme, akamweleza tatizo la viti tulilokuwa nalo kwa sababu wakuu wa shule walikataa kuazima tengenezo letu la kidini viti. Msimamizi aliagiza mmoja wa maafisa wa kampuni achunguze jambo hilo, halafu kusanyiko likaazimwa maelfu kadha ya viti bila malipo. Barua hiyo ilimfikia msimamizi siku moja kabla hajajiuzulu.

Jambo hilo lilituonyesha kwamba malaika wanatusaidia sana katika makusanyiko yetu kuliko tunavyodhani.

Kwa mfano, wakati mmoja Mashahidi wenye bidii walimaliza kusafisha uwanja unaoitwa Expo ‘70 katika Osaka, kuutayarisha kwa ajili ya kusanyiko la taifa. Halafu tukapata habari kwamba sherehe kubwa ya muziki ilipangwa kufanywa hapo, jioni iliyotangulia kusanyiko letu. Tukajisikia kwamba sasa Shetani alikuwa ameanza kucheka akifurahi kwamba uwanja ungechafuliwa tena. Ndipo radio ilipotoa onyo kwamba tufani ilikuwa inakuja. Dhoruba hiyo ilikuwa ikiuelekea mji wa Osaka moja kwa moja. Ingeupiga uwanja wakati ule ule ambao wapenda muziki wangekuwa wakiendeleza sherehe zao. Waliamua upesi kusiwe na sherehe. Ikawaje? Kwa ghafula tufani ilibadili mwendo ikabaki kule kule katika bahari kuu ya Pacific.

MAISHA YETU YA JAMAA JAPAN

Sasa turudiapo habari za matatizo yetu binafsi, nasema kwamba tuliona badiliko kubwa tulipolazimika kukaa mahali pamoja ili kulea jamaa. Sikuwa na kazi naye mke wangu alikuwa na wasiwasi wa kupata kitoto chake cha kwanza katika Japan. Ndugu mmoja wa Uingereza alinionyesha fadhili kwa kuniambia angenipa kazi tukirudi huko. Sasa tufanye nini? Ndugu mmoja Mkanada mwenye mke Mjapan alikuwa amefaulu sana kukaa huku akifundisha Kiingereza. Nikaona labda hata mimi ningeweza kufanya hivyo. Wakati huo, ndugu mdogo wa Daphne na jamaa yake walikuwa Uganda wakitumikia kwenye uhitaji mkubwa. Sisi pia tungeweza kufanya hivyo kwa kubaki tulipokuwa. Tukaamua kujaribu.

Watch Tower Society ilitushauri kwamba tungeweza kusaidia tukienda katika kundi moja la Nagoya. Ndugu walituonyesha fadhili nyingi wakatusaidia kuhama. Tulikaa katika nyumba ndogo yenye vyumba viwili tuliyokodi kwa dada “painia” tukiwa na zawadi nyingi tulizopewa, pamoja na vifaa vilivyotumika vya kuweka ndani, na godoro jipya. Kwa kuwa hatukuwa hata na kisu wala uma, tulifurahi sana tulipoonyeshwa ukarimu na upendo mwingi na ndugu zetu Wajapan.

Tulipolea jamaa yetu wenyewe tulianza kuyafahamu matatizo yanayowapata ndugu wa huku pamoja na watoto wao. Elimu ni jambo la maana sana kwa jamaa nyingi za Kijapan. Jirani zetu walikuwa na wasiwasi kwa sababu mtoto wetu hakwenda kwenye kishule cha watoto, kinachodhaniwa kuwa ndiyo hatua ya kwanza ya kufika chuo kikuu. Tulianza kujisikia tukitaka kufuata maneno yao. Mke wangu alipata nafasi nyingi za kuwapa jirani ushuhuda kwa sababu ya vile walivyopendezwa na mambo yetu.

Alikuwa akiwaeleza habari za mikutano, jinsi watoto wanavyojifunza kukaa na watu wengi muda wa saa mbili bila kupiga kelele na kujibu maulizo (katika kundi letu wanatumia vikuza-sauti wanapojibu), jinsi wanavyojifunza kuimba pamoja na watu wengi katika kitabu kilichoandikwa kwa herufi za Kijapan, ambazo watoto hawafundishwi mpaka wanapokuwa katika mwaka wao wa kwanza shuleni. Watoto wanaopokea elimu hiyo ya mapema katika Jumba la Ufalme, bila malipo yo yote, wanalindwa wasifundishwe mambo mabaya na watoto wanaokwenda kwenye vishule vidogo vya watoto. Mama mmoja kijana mwenye watoto watatu ameanza kuhudhuria mikutano kwa sababu ya kupokea ushuhuda huo wa vivi hivi katika uwanja wa watoto unaoelekea nyumba yetu. Mama mwingine jirani amekwisha kuwa dada yetu wa kiroho na anaongoza mafunzo yake mwenyewe.

MATATIZO KATIKA ELIMU YA JAPAN

Baadaye, tuliamua kumpeleka Ivan, kivulana wetu, kwenye shule ya msingi ya Kijapan ya hapo kwetu, aweze kupata elimu nzuri, hasa ya Kijapan. Inaonekana sasa wavulana wale wengine wamekwisha mzoea, ingawa mara ya kwanza walishangazwa na macho yake ya samawati (buluu) na nywele zake laini. Mwalimu wake wa kike pia anaonekana amekwisha jua kwamba yako mambo fulani ambayo kivulana wetu hawezi kuruhusiwa ayafanye na dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia.

Alipata tatizo la kwanza alipopewa nyama ya nyangumi, ambayo kwa kawaida haitolewi damu jinsi Maandiko yanavyosema, inayopakuliwa shuleni wakati wa vyakula vya mchana, basi yeye akaikataa. (Matendo 15:28, 29) Ndipo ilipofika sikukuu ya wavulana siku ya tano ya mwezi wa tano. Siku hiyo, desturi ni kwamba nyumba zenye wavulana zipeperushe kitambaa au plastiki iliyo mfano wa samaki ikiwa juu ya kijiti kirefu. Watoto shuleni waliombwa watengeneze samaki wa karatasi, kisha wawafunge katika kijiti na kuwapeleka nyumbani. Ivan alikataa, halafu mama yake akaagizwa aende shuleni kueleza sababu.

Shule ilikubali kwamba asili ya sikukuu hiyo ni ibada za utakaso za Washinto, lakini ikasisitiza kwamba siku hizi desturi hiyo si ya kidini. Ilidaiwa kwamba samaki huyo wa maji baridi, anayejulikana sana kwa sababu anaweza kuogelea apande juu ya poromoko la maji, alikuwa mfano tu wa tamaa ambayo wazazi wanakuwa nayo wakitaka wavulana wao wawe wenye nguvu. Walipoelezwa kwamba huo ni ushirikina walikataa, lakini mwishowe wakakubali Ivan atumie wakati huo kuchora na kukata kitu cha namna nyingine.

Krismasi ilipofika, mwalimu alishangazwa na jambo jingine. Krismasi imekuwa ikizoewa sana na Wajapan walio wafuasi wa Buddha, pamoja na karamu za kusherehekea siku za kuzaliwa, Siku ya Valetine, kula mandazi ya Pasaka na desturi nyingine za nchi za Uzunguni zinazofaidi sana wafanya biashara. Watoto wa darasa lao walipoombwa wachore picha kwa ajili ya Krismasi, Ivan, aliyekuwa kivulana wa pekee Mkristo, aliomba ruhusa achore kitu tofauti. Alikuwa tayari kueleza sababu gani Krismasi haihusiani na Yesu Kristo, lakini mwalimu wake hakujishughulisha kumwuliza sababu.

Alikuwa ameona kwamba Ivan hakujiunga na watoto wale wengine kuuimba wimbo wa taifa wa Japan, akadhani kwamba hakufanya hivyo kwa sababu hiyo si nchi yake. Baadaye alijua kwamba Ivan hakuimba hata wimbo wa taifa wa Uingereza. Jambo hilo lilimpa mke wangu nafasi ya kueleza habari za kutokuwamo na umoja wa mashahidi Wakristo wa Yehova ulimwenguni pote. Ivan aendeleapo kuwa mkubwa atakabiliwa na matatizo mengine kama kujifunza kupigana na watu, kufanya judo na kupigana kwa kutumia panga, kwa maana hayo ni mambo ambayo watoto wanafundishwa yakisemekana kuwa michezo. Tuna hakika kwamba atafanya maamuzi mazuri juu ya mambo hayo, kama alivyofanya mengine.

Tunaona kwamba kitabu Kumsikiliza Mwalimu Mkuu kimemsaidia sana katika kusudi hilo. Njia iliyotumiwa katika kitabu hicho kufundisha watoto kanuni fulani na kuihusianisha na matatizo wanayopata inafaa kabisa. Tunalishukuru sana tengenezo la Yehova kwa sababu ya kifaa hicho kilichotolewa kwa wakati wake.

MAISHA YENYE BARAKA

Mojawapo matatizo ya Daphne limekuwa kusikitika kwa sababu hayuko karibu na nchi ya kwetu. Anajua kwamba tunaweza kusaidia sana watu tukikaa hapa, hata hivyo limekuwa si jambo jepesi kwake kuacha kufikiria nyumbani kwetu. Baada ya kutafuta miaka mingi njia ya kummalizia masikitiko hayo, inaonekana sasa tumeipata. Zaidi ya kufanya kazi inayomfurahisha ya kusaidia watu wajifunze kweli ya Biblia, Daphne aliamua kutumia asubuhi moja kwa juma akijifunza kuchora michoro ya Kijapan. Kazi hiyo anayofanya mara kwa mara inamfurahisha na kumpunguzia sana tatizo lake.

Kwa sasa nina kazi nyingi zinazonifurahisha, maana mimi ni mzee katika mojawapo makundi kumi na manne ya Nagoya, tena natafutia jamaa riziki. Nafurahia kujifunza Biblia na waume wasioamini, nami nayafahamu zaidi matatizo yao kwa sababu sasa nakutana na wanaume wa namna zote kazini. Sisi tunafurahi sana kwa sababu tumeitumia kila nafasi mpya ya kumtolea Yehova utumishi mtakatifu kwa nguvu zote! Sisi tunawaambia wengine. Msiahirishe mambo. Hakuna anayejua baraka tutakazopata kesho.

[Picha of Daphne and Leon Pettitt katika ukurasa wa 524]

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki