“Maneno ya Kiroho” kwa Wenye Kutaabika Akilini
MATATIZO ya akilini yanasumbua hata watumishi fulani waaminifu wa Mungu. Na ingawa nyakati fulani huenda ikahitajiwa kabisa na ikafaa wenye kutaabika watafute msaada wa wenye ujuzi, wanaweza pia kupata manufaa kutokana na usaidizi na kitia-moyo cha kundi la Kikristo. Mathalani, wakati Epafrodito Mkristo mwaminifu alipokuja kushuka moyo vikali, waitikadi wenzake katika Filipi walihimilizwa wasipuuze taabu yake kubwa bali ‘wampe upokezi ule wa kidesturi katika Bwana kwa shangwe yote; na kuendelea kuwachukua watu wa jinsi hiyo kuwa wapendwa wanaothaminika.’—Wafilipi 2:25-29, NW.
Mashahidi wa Yehova leo wako vivyo hivyo chini ya wajibu wa ‘kuendelea kufarijiana’ na ‘kutegemeza walio dhaifu.’ (1 Wathesalonike 5:11, 14, NW) Wazee Wakristo wanapaswa kuchukua uongozi katika habari hiyo.—Isaya 32:2.
Bila shaka, kwa kawaida wazee hawana sifa za kuwastahilisha kutenda wakiwa watabibu wala kutumia mawazo na istilahi (maneno) ya udaktari wa akili. Kufanya hivyo kungekuwa ni kukosa moyo wa kiasi na labda kuwe hatari. (Mithali 11:2) Kama vile mtume Paulo, ni lazima wao ‘wanene, si kwa maneno yanayofundishwa kwa hekima ya kibinadamu, bali yale yanayofundishwa na roho, huku wakiunganisha mambo ya kiroho pamoja na maneno ya kiroho.’ (1 Wakorintho 2:13, NW) Hayo “maneno ya kiroho” yanatia ndani mawazo na kanuni zinazopatikana katika Biblia. Kwa kutumiwa kwa usahihi, yanaweza kufariji na kujenga sana watu wenye kutaabika sana.—2 Timotheo 3:16.
‘Wepesi wa Kusikia’
Ingawa hivyo, ni lazima kwanza wazee ‘wawe wepesi wa kusikia, bali si wepesi wa kusema.’ (Yakobo 1:19) ‘Kujibu kabla ya kusikia’ kunaweza kuwa na tokeo la kutoa ushauri usiofaa. (Mithali 18:13) Kwa kutoelewa vizuri kabisa hali ya kasoro ya ndugu fulani ya mshuko wa moyo, kikundi kimoja cha wazee kiliachilia mbali shauri lake kwa kumchukua kuwa dhaifu kiroho. “Sali kwa wingi zaidi,” wao wakamwambia—agizo ambalo yeye aliliona kuwa gumu kutumia kwa sababu ya hali yake ya mshuko wa akilini.
Basi, kabla ya kutoa shauri wazee wanapaswa kusikia kila jambo ambalo mtesekaji anataka kusema. Labda, kile anachohitaji ni msikilizaji mwema. Kupitia saburi na utambuzi, ‘tekeni’ yaliyo katika moyo wake. (Mithali 20:5) Ikiwa mwenye kutaabika ana ugumu wa kueleza hisia zake kwa maneno, kumbukeni jinsi Elkana alivyouliza maswali yenye fadhili lakini ya kutaja mambo wazi kuhusu huzuni ya mke wake. “Hana,” yeye akauliza, “unalilia nini? kwani huli chakula? kwa nini moyo wako una huzuni?” (1 Samweli 1:8) Maswali yenye hadhari, yenye kuulizwa kwa uanana, yanaweza mara nyingi kusaidia ndugu aliyeshuka moyo ataje wazi kabisa chanzo cha “ujalifu wa hangaiko” lake. (Mithali 12:25, NW) Mathalani, katika kisa kimoja matatizo ya ndoa yalithibitika kuwa ndicho kisababishi cha kushuka moyo kwa ndugu mmoja.
Kutoa Msaada “Bila Kusuta”
Si sikuzote ambapo watu wenye kutaabika sana hutumia njia nzuri ya kufikiri kueleza jinsi wanavyohisi. Anaandika hivi mmoja aliyepatwa na ugonjwa wa akilini: “Wakati nilipokuja kuwa mgonjwa, sikuelewa hivyo na nyakati fulani nililaumu Yehova.” Hivyo wenye kusumbuka huenda wakatoa malalamiko yasiyo na msingi kwamba wametendwa vibaya au wakakataliwa na kundi. Wazee wanapaswa kuitikia jinsi gani?
Yehova huweka kielelezo kwa ‘kuwapa wote kwa ukarimu bila kusuta [wala hakemei, UV].’ (Yakobo 1:5, NW) Watesekaji hawapasi kufanywa wahisi kwamba ni wapumbavu au wajinga kwa sababu ya vile wanavyohisi. Hisia zao—ingawa huenda zikawa zisizo za kufikiri kuzuri—ni halisi kabisa kwao. Wao wanahitaji “hisia mwenzi,” si uchambuzi. (1 Petro 3:8, NW) Wazee wanapaswa kuwa waangalifu pia wasimwongezee mtesekaji himila ya kihisia-moyo kwa kumshtaki kuwa amefanya kosa. Mwanamume mwadilifu Ayubu alitaabika sana hata akaomboleza hivi: “Nafsi yangu inachoka [inakirihi, NW] na maisha yangu.” (Ayubu 10:1) Lakini waandamani wake watatu hawakumfariji. Mmoja wao hata alisema hivi: “Je! uovu wako si mkuu? Wala maovu yako hayana mwisho.”—Ayubu 22:5.
Hata hivyo, nyakati fulani mwenendo usiofaa ndio husababisha msukosuko wa hisia-moyo au ndio huchangia kuufanya uwe mkali. “Niliponyamaza [kuhusu ukosaji] mifupa yangu ilichakaa kwa kuugua kwangu mchana na usiku,” akasema mtunga zaburi Daudi. (Zaburi 32:3) Vivyo hivyo, ndugu mmoja aliteswa na hangaiko kali sana hata akawa hawezi tena kufanya kazi. Kisababishi cha taabu yake kubwa kilikuwa nini? Kitendo cha uzinzi alichokuwa ameficha. Kwa hiyo ikiwa kuna sababu ya kushuku kwamba kosa linahusika, wazee wanaweza kuchunguza-chunguza kama kuna uwezekano wa jambo hilo. Lakini wanapaswa kufanya hivyo kwa njia yenye fadhili, si kwa kumshtakia mtu yule kutenda kosa huku wakimsuta.
Kuponya kwa Ulimi Wenye Hekima
Baada ya wazee kuwa wamefanya wawezavyo ili kuamua tatizo la mtu ni la hali gani, inawapasa kutenda kupatana na Mithali 12:18, NW, inayosema: “Ulimi wa wenye hekima ni ponyo.” Wazee hawawezi kuponya ugonjwa wenyewe, hapana. Lakini kwa kutumia maneno yaliyochaguliwa kwa uangalifu, huenda wakaweza kuwaondolea wenye kutaabika sana akilini mzigo wa hangaiko na mkazo waliojitwika bila sababu. Wazee wangeweza kuanza kwa kuchagua makala za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! zinazohusu matatizo ya akilini na ya kihisia-moyo. Zinaweza kuzungumziwa pamoja na wenye kutaabika sana ili kuwasaidia waelewe hali yao vizuri zaidi. Mara nyingi wanahisi kuondokewa na mzigo kwa kujua kwamba tatizo lao ni tokeo la kutokamilika kimwili, wala si upotezo wa upendeleo wa Yehova.
Ni kweli kwamba watu wenye kusumbuka fikira wanaweza kuwa wagumu kushughulika nao, huku wengine wao wakifadhaika kwa hasira. Hata hivyo, mzee mwenye hekima hukumbuka kwamba “jawabu la upole hugeuza hasira.” (Mithali 15:1) Kuhakikisha kwamba matamko yake ni yenye neema sikuzote humzuia asikoroge hali ile iwe mbaya zaidi isivyohitajiwa. (Wakolosai 4:6) Mathalani, ndugu mwenye ugonjwa wa skizofrenia (kutenda-tenda mambo ya kiajabu-ajabu kwa mwenendo usio wa akili timamu) huenda akasisitiza kwamba yeye husikia sauti-sauti.a Dakt. E. Fuller Torrey anaonelea hivi: ‘Kujaribu kubishana na wagonjwa wa skizofrenia ili kuwatoa katika itikadi zao za kuona mambo yasiyo ya kweli ni njia isiyo na matokeo mazuri. Mara nyingi majaribio ya kufanya hivyo hutokeza kutoelewana na hasira. Badala ya kubishana, sema tu kitaarifa cha kwamba huafikiani na jambo hilo.’ Ndiyo kusema, wazee wanaweza kueleza kwa saburi kwamba ingawa sauti-sauti hizo zinasikika kama kwamba ni halisi, inaelekea kuwa akili ya mtu huyo inamfanyizia tu viini-macho.
Utumizi wenye matokeo mazuri wa Biblia unaweza pia kutokeza matokeo mazuri sana. (Waebrania 4:12) Mathalani, ikiwa mtu mgonjwa anaeleza ana hofu za kwamba Mungu amemwachilia mbali, kwa fadhili onyesha huruma kuhusu hofu zake. Hata hivyo, wakati ule ule mkumbushe kwa saburi juu ya nguvu za ukombozi, ukitumia maandiko kama vile Zaburi 103:8-14 na 1 Yohana 2:1, 2. Petro wa Kwanza 5:6, 7 na Warumi 8:26, 27 huenda yakamsaidia kuthamini kwamba Mungu ‘hujishughulisha sana kwa mambo yake’ na husikia sala zake, hata ikiwa ana ugumu wa kueleza hisia zake kwa maneno. Kwa kufuata kanuni iliyo kwenye Yakobo 5:14, ndipo wazee wanapoweza kusali pamoja na mtu huyo mwenye kutaabika sana.
Namna gani ikiwa mtesekaji ana elekeo la kufanyiza-fanyiza matata makubwa juu ya mambo madogo sana? Anaweza kukumbushwa juu ya shauri la Biblia juu ya kutokuwa na “haki kupita kiasi.” (Mhubiri 7:16) Huenda mwingine akapata manufaa kutokana na kitia-moyo kilicho kwenye Wafilipi 4:8, ambacho kinaweza kumsaidia apigane na fikira za kukosa adili. Na bado huenda mwingine akawa hakubali ni mwenye mapungukiwa ya kutoweza mambo fulani na huenda akawa amevunjika moyo kwa sababu ugonjwa wake unamwekea mipaka ya utendaji wake wa Kikristo. Maandiko kama vile Mathayo 13:23 na Luka 21:1-4 yanaweza kutumiwa kumsaidia athamini kwamba ingawa huenda mastakimu zetu zikatuwekea mipaka juu ya mambo tuwezayo kufanya, Yehova huthamini jitihada zetu kwa kina kirefu.
Ndiyo, wakiwa na kifaa cha ulimi uliozoezwa na Biblia, wazee wanaweza kufanya mengi wasaidie na kufariji waitikadi wenzao wenye kutaabika sana. Dada mmoja aliyepatwa na matatizo ya kiakili anasema hivi: “Mimi nathamini kikweli yale ambayo Isaya 32:2 inasema juu ya wazee katika kundi. Wao walikuwapo sikuzote wakiwa na ushauri wenye mafaa wakati nilipowahitaji.”
Mikutano na Utumishi wa Shambani
Mtu mwenye kutaabika sana akilini angali ana mahitaji ya kiroho. (Mathayo 5:3) Kweli kweli, kubaki mwenye imara kiroho ndiko kumefanyizia watu fulani tofauti ya kuwa hai badala ya kufa. Irene, aliyeteseka kwa sababu ya ugonjwa wa skizofrenia kwa miaka 30, anakumbuka hivi: “Nyakati fulani, mimi nilivurugika sana. Lakini sikuzote ukweli ulikuwa katika akili yangu—ukiwa imara madhubuti kama bamba la zege. Uliendelea kunizuia nisijiondolee uhai!”
Kwa hiyo, kwa kadiri inayofaa, mtu yule mwenye kuugua anapasa kutiwa moyo ashiriki katika kazi ya kuhubiri na kuhudhuria mikutano, ‘asijitenge na wenzake.’ (Mithali 18:1) Hivi ndivyo dada mmoja alivyohisi kwa sababu ya ugonjwa wa akilini: ‘Mimi nilisadiki kwamba nilikuwa nimetenda dhambi dhidi ya Mungu wetu, Yehova, kwa kadiri isiyosameheka. Tokeo ni kwamba, mimi niligeuza kila jambo nililosikia mikutanoni kwa kulichukulia kuwa limesemwa kwa njia isiyofaa. Lolote lililokuwa la kushutumu, nililitumia hilo kuwa lanihusu mimi mwenyewe.’ Lakini yeye alizidi tu kuhudhuria mikutano na mwishowe akasikia hotuba iliyomsaidia kushinda maono yake yasiyo ya kweli kwamba alikataliwa na Mungu.
Ingawa hivyo, namna gani mtu aliye mgonjwa vikali akifadhaika kwa hasira na kuvuruga mikutano ya kundi au utumishi wa shambani? Inaelekea kuwa mtesekaji huyo hana nia ya ukorofi bali ameudhika tu kwa sababu ya fikira iliyovurugika. Na bado, jambo hilo linaweza kuwa na ujaribu kwa wote wanaohusika. Ikiwa usumbuaji ule ni mdogo au usio wa mara nyingi, inaelekea kuwa kundi litaonyesha ustahimilivu. (Wakolosai 3:12, 13) Ama sivyo, huenda ikahitajiwa kabisa kudokeza kwamba mtesekaji aketi mahali ambapo uvurugaji ule utaondosha fikira kwa kadiri ndogo zaidi. Mipango yenye upendo inaweza kufanywa kusaidia mtu huyo awe mtendaji katika kazi ya kuhubiri, labda kuhakikisha kwamba mhubiri mkomavu, mwenye utambuzi, anaandamana naye sikuzote au kwamba anaketi katika mafunzo ya Biblia ya kimaskani mahali ambako hali yake inaeleweka na kuvumiliwa.
Ingawa hivyo, nyakati fulani mwenendo wa mtu unakuwa wa kushtusha, wenye suto, au ulio hatari kwa kutoweza kudhibitiwa. Labda mtu yule ameacha kutumia dawa alizoandikiwa na anahitaji kitia-moyo imara arudie kawaida yake ya kitiba. Lakini ikiwa hakuna itikio au vitendo vya uvurugaji wa mtu huyo vinaendelea, huenda ikahitajiwa kabisa kumzuia asiwe kwenye mikutano na utumishi wa shambani ili kudumisha utaratibu. (1 Wakorintho 14:40) Wazee wanapaswa wamwambie kwa fadhili mtu huyo mwenye kuugua kwamba yeye hahukumiwi kuwa asiyeaminika bali ni ugonjwa wake tu unaomwekea mipaka ya mambo awezayo kufanya. ‘Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yake,’ na Yeye anaelewa mipaka ya kupungukiwa kwake. (Waebrania 6:10) Ziara za uchungaji wa ukawaida zitasaidia mtu yule kudumisha hali yake ya kiroho mpaka apate nafuu.
Kusaidia Jamaa Zao
Ugonjwa wa akilini huziletea jamaa mvurugiko mkubwa. “Imetufanya tuwe hoi,” anasema ndugu mmoja ambaye mwana wake aliye mtu mzima ni mgonjwa vikali katika akili. “Siku baada ya siku huoni kitulizo,” mke wake anaongezea. “Hiyo imeathiri ndoa yetu, kwa kuwa nyakati fulani tunajikuta tukizozana sisi kwa sisi.” Wazia, pia, lile umivu la kuona mwenzi wa ndoa akipatwa na ugonjwa wa akilini. Ndugu mmoja anasema: “Mke wangu amebandikwa jina la kuwa ‘mskizofrenia wa maono bandia.’ Yeye husikia sauti-sauti na kukataa dawa kwa sababu anaitikadi ‘itamtia sumu.’ Haitikadi kwamba mimi ni mume wake na hukataa kwenda katika utumishi au mikutanoni.” Sisi tunaweza kusaidia jinsi gani jamaa za wenye kusumbuliwa?
Paulo alisema: “Neneni kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo.” (1 Wathesalonike 5:14, NW) Ungekuwa ukatili kuepuka au kupuuza Wakristo wenzetu wanaofanya kazi ya jasho kutunza mshiriki wa jamaa aliye mgonjwa akilini. “Mkaribishane ninyi kwa ninyi,” akasema Paulo. (Warumi 15:7) Mikutano ya Kikristo inatoa fursa ya kufanya hivyo kwa uchangamfu na kuonyesha upendo na uthamini kwa wale ‘wanaozoea bidii ya kujitolea Mungu katika nyumba zao.’—1 Timotheo 5:4, NW.
Katika ziara za uchungaji, wazee wanaweza kuwatia moyo zaidi watu hao kuendeleza funzo la jamaa, kuhudhuria mikutano, na kubaki wakiwa wahubiri Ufalme walio watendaji. Hata hivyo, kwa habari ya mahitaji yao ya kimwili na ya vitu vya kuwafaa, kundi linapasa kufanya mengi zaidi ya kusema tu, “Mkaote moto na kushiba.” (Yakobo 2:16) Labda jamaa inahitaji usaidizi katika kufika mikutanoni. Watu fulani mmoja mmoja huenda wakawa wanaweza kusaidia gharama zao za kitiba zinazoendelea kuongezeka. (1 Yohana 3:17, 18) Hangaikio hilo lenye upendo linathaminiwa kama nini! Mume wa dada mmoja aliye mgonjwa akilini anasema hivi: “Kundi linajua tatizo letu, nao huonyesha kwa upendo sana kwamba wanajali.”
Kushika Ukamilifu
“Viumbe vyote pia vinaugua pamoja, navyo vina utungu pamoja hata sasa,” akasema Paulo. (Warumi 8:22) Na mtaabiko wa akilini ni moja la mambo ya urithi wa kutokamilika. Huenda madaktari wakatoa kitulizo cha kadiri fulani. Lakini wengi ambao wametafuta msaada wao wamejionea kama mwanamke yule katika siku ya Yesu ambaye ‘aliteswa mengi kwa mikono ya matabibu wengi, akigharimiwa vitu vyote alivyo navyo, kusimfae hata kidogo, bali hali yake ilizidi kuwa mbaya.’—Marko 5:26.
Basi, wengi lazima wajifunze kuishi pamoja na matatizo yao, wakitazamia kupata kitulizo halisi katika ulimwengu mpya wa Mungu. (Ufunuo 21:3, 4) “Umhimidi BWANA [Yehova, NW], . . . akuponya magonjwa yako yote,” ndivyo mtunga zaburi akapaaza sauti. (Zaburi 103:2, 3) Kwa sasa, hangaikio tunalopasa kukazia fikira zaidi lazima liwe ni kuthibitisha ukamilifu wetu, si kuwa na afya kamilifu ya kiakili au kimwili. (Zaburi 26:11; linganisha 1 Wakorintho 7:29-31.) Kuteseka kutokana na kasoro ya akilini huenda kukafanya hilo liwe jambo gumu. Lakini watumishi wengi wa Mungu, kama Paulo, wametumikia kwa uaminifu wakiwa na “mwiba katika mwili.” (2 Wakorintho 12:7) “Mimi nimejifunza kwamba hakuna daktari yeyote, wala hata akina ndugu, anayeweza kuniponya,” anasema mmoja aliye na ugonjwa wa akilini. “Lakini nimejifunza kutegemea Yehova.” Watu wenye kutaabika sana akilini wanaweza pia kutegemea ndugu na dada wenye upendo ambao wananena kwa saburi “maneno ya kiroho” ili kuwapa faraja na utegemezo.
[Maelezo ya Chini]
a Makala “Mtaabiko wa Akilini—Wakati Unaposumbua Mkristo” katika Mnara wa Mlinzi wa Oktoba 15, 1988, ilitoa miongozo ya kushughulikia hali ambazo zina shuku ya kwamba kuna uvutano wa roho wabaya.
[Picha katika ukurasa wa 21]
“Maneno ya kiroho” kutoka kwa wazee wenye upendo yanaweza kusaidia sana watu wenye kutaabika