Funzo Lina Faida
JE, UMEPATA kuona watu wakichagua tunda? Wengi hutazama rangi yake na ukubwa wake ili wajue kama limeiva. Wengine hulinusa. Wengine hulishika na hata kulifinya-finya. Wengine nao hupima uzito wake, wakibeba tunda moja kwenye mkono mmoja na tunda lingine kwenye mkono mwingine waone ni tunda gani lililo na maji mengi. Watu hao hufikiria nini? Wao huchunguza matunda hayo kwa makini, wakilinganisha tofauti zilizoko kati ya matunda waliyochagua kwanza na yale wanayoona sasa. Watapata faida kwa sababu wamefikiria uchaguzi wao kwa makini.
Bila shaka, kuna faida nyingi sana za kujifunza Neno la Mungu. Funzo linapokuwa jambo kuu katika maisha yetu, imani yetu huimarika, upendo wetu huongezeka, huduma yetu hupata matokeo mazuri, na maamuzi tunayofanya hudhihirisha kwamba tuna ufahamu na hekima ya Mungu. Kuhusu faida hizo, Mithali 3:15 linasema hivi: ‘Vyote uvitamanivyo havilingani nazo.’ Je, unapata faida hizo? Hiyo inategemea jinsi unavyojifunza.—Kol. 1:9, 10.
Tafakari
Funzo ni nini? Funzo si kusoma kijuu-juu tu. Funzo linahusisha kutumia akili kuchunguza habari kwa makini au kwa undani. Funzo linatia ndani kuchanganua habari unayosoma, ukiilinganisha na habari ambayo tayari unajua, na kuona sababu zinazounga mkono taarifa zinazotolewa. Unapojifunza, fikiria kwa uzito mambo yoyote yanayotajwa ambayo huenda yakawa mapya kwako. Fikiria pia jinsi wewe binafsi unavyoweza kutumia zaidi mashauri ya Maandiko. Kwa kuwa wewe ni Shahidi wa Yehova, inafaa ufikirie pia jinsi unavyoweza kutumia habari hiyo kuwasaidia wengine. Bila shaka, funzo hutia ndani kutafakari.
Kutayarisha Akili
Ili ufaidike kwa ukamili na funzo lako, tayarisha moyo wako
Unapofanya matayarisho ya kujifunza, unakusanya vitu kama Biblia, vichapo unavyotaka kutumia, kalamu ya risasi au kalamu ya wino, na labda kitabu cha kuandikia. Lakini, je, wewe hutayarisha moyo wako pia? Biblia inatuambia kwamba Ezra “alikuwa ameuelekeza [“ameutayarisha,” NW] moyo wake kuitafuta sheria ya BWANA, na kuitenda, na kufundisha maagizo na hukumu katika Israeli.” (Ezra 7:10) Kutayarisha moyo kunahusisha nini?
Sala hutuwezesha kuwa na maoni yanayofaa kuhusu funzo la Neno la Mungu. Tunataka moyo wetu upokee maagizo ambayo Yehova anatupatia. Mwanzoni mwa kila kipindi cha funzo, msihi Yehova ili roho yake ikusaidie. (Luka 11:13) Umwombe akusaidie kuelewa maana ya habari unayojifunza, jinsi inavyohusiana na kusudi lake, jinsi inavyoweza kukusaidia kutambua kati ya mema na mabaya, jinsi unavyoweza kutumia kanuni zake maishani mwako, na jinsi habari hiyo inavyochangia uhusiano wako na yeye. (Mit. 9:10) Unapojifunza, ‘fuliza kumwomba Mungu’ upate hekima. (Yak. 1:5) Jichunguze kwa unyofu ukitumia habari unayojifunza na umwombe Yehova akusaidie kuondosha mawazo mabaya au tamaa zenye kudhuru. Nyakati zote ‘tushukuru BWANA’ kwa mambo ambayo anafunua. (Zab. 147:7) Kujifunza hivyo kwa njia ya sala hutokeza uhusiano wa karibu na Yehova, kwa kuwa kunatuwezesha kufuata yale anayotuambia kupitia Neno lake.—Zab. 145:18.
Usikivu huo hutofautisha watu wa Yehova na watu wengine. Ni jambo la kawaida kwa watu wasiomcha Mungu kutilia shaka au kupinga mambo ambayo yameandikwa. Tusiwe na maoni kama hayo. Tumtumaini Yehova. (Mit. 3:5-7) Kama hatuelewi jambo fulani, tusikate kauli kimbelembele kwamba ni lazima jambo hilo ni kosa. Tunapoendelea kufanya utafiti na kuchunguza majibu, tumngojee Yehova. (Mika 7:7) Kama Ezra, tunataka kufuata mambo tunayojifunza na kuwafundisha wengine pia. Tukiwa na maoni hayo moyoni, funzo letu litatufaidi sana.
Jinsi ya Kujifunza
Badala ya kuanza moja kwa moja na fungu la 1 na kuendelea hadi mwisho, kwanza angalia funzo zima au sura nzima. Anza kwa kuchunguza maneno ya kichwa kikuu. Hilo ndilo jambo kuu la habari utakayojifunza. Kisha chunguza kwa makini jinsi vichwa vidogo vinavyohusiana na jambo kuu. Chunguza picha zozote zile, chati, au masanduku ya maswali ambazo zinaambatana na habari. Jiulize: ‘Nitarajie kujifunza nini kulingana na pitio hili la kimbele? Itanisaidia kwa njia gani?’ Kufanya hivyo hufanya funzo liwe na kusudi.
Fahamu vichapo vya kufanyia utafiti katika lugha unazofahamu
Sasa soma habari kamili. Funzo la Mnara wa Mlinzi na baadhi ya vitabu vina maswali yaliyochapishwa. Unaposoma kila fungu, inafaa kutia alama kwenye majibu. Hata kama hakuna maswali ya funzo, bado unaweza kutia alama mambo makuu ambayo unataka kukumbuka. Ukiona jambo ambalo ni jipya kwako, tumia muda zaidi kulichunguza ili uhakikishe umelielewa vizuri. Uwe macho kuona mifano au njia za kusababu ambazo zitakusaidia katika huduma ya shambani au ambazo unaweza kutumia katika hotuba utakayotoa. Fikiria watu fulani-fulani ambao imani yao inaweza kuimarishwa ukiwaeleza habari unayojifunza. Tia alama mambo ambayo unataka kutumia, na uyapitie tena unapomaliza kujifunza.
Unapojifunza, soma maandiko yaliyotajwa. Chunguza jinsi kila andiko linavyohusiana na mawazo ya fungu hilo.
Huenda ukapata mambo ambayo huyaelewi kwa urahisi au yale ambayo ungependa kuchunguza zaidi. Badala ya kuacha mambo hayo yakukengeushe, andika kifupi kwamba utayachunguza baadaye. Mara nyingi mambo hueleweka wazi unapoendelea kusoma habari hiyo. Kama sivyo, unaweza kufanya utafiti wa ziada. Unaweza kuandika mambo gani ili uyachunguze baadaye? Labda huelewi vizuri andiko fulani ambalo limenukuliwa. Au huenda usiweze kutambua mara moja jinsi linavyohusu habari inayozungumziwa. Labda unahisi kwamba unaelewa habari fulani lakini huielewi kwa kiasi cha kuweza kuwaelezea wengine. Badala ya kupuuza tu mambo hayo, huenda ikawa jambo la hekima kuyafanyia utafiti baada ya kumaliza kusoma.
Soma maandiko
Mtume Paulo alipowaandikia Wakristo Waebrania barua yenye mambo mengi, alitua katikati akasema: “Jambo kuu ni hili.” (Ebr. 8:1) Je, wewe hujikumbusha hivyo pindi kwa pindi? Ebu ona sababu iliyomfanya Paulo afanye hivyo. Katika sura zinazotangulia za barua yake iliyopuliziwa, tayari ameonyesha kwamba Kristo akiwa Kuhani wa Cheo cha Juu aliye mkuu ameingia katika mbingu yenyewe. (Ebr. 4:14–5:10; 6:20) Lakini kwa kutenga jambo kuu na kulikazia mwanzoni mwa sura ya 8, Paulo alitayarisha akili za wasomaji ili wafikirie kwa uzito jinsi jambo hilo linavyohusu maisha yao. Alitaja kwamba Kristo alikuwa ametokea mbele ya Mungu kwa niaba yao na alikuwa amewafungulia njia ya kuingia “mahali patakatifu” mbinguni. (Ebr. 9:24; 10:19-22) Uhakika wa tumaini lao ungesaidia kuwafanya watumie mashauri mengine ya barua hii ambayo yanahusu imani, uvumilivu, na mwenendo wa Kikristo. Vivyo hivyo, kukazia akili mambo makuu tunapojifunza kutatusaidia kutambua jinsi kichwa kinavyofafanuliwa na kuingiza akilini mwetu sababu nzuri za kutenda kwa kupatana nayo.
Je, funzo lako la binafsi litakuchochea utende? Swali hili ni muhimu. Unapojifunza jambo, jiulize: ‘Jambo hili linahusuje mtazamo wangu na miradi yangu maishani? Naweza kutumiaje habari hii kusuluhisha tatizo, kufanya uamuzi, au kufikia mradi fulani? Naweza kuitumiaje habari hii katika familia, katika huduma ya shambani, na kutanikoni?’ Yafikirie maswali haya kwa njia ya sala, ukitafakari hali halisi za maisha ambazo katika hizo unaweza kutumia ujuzi huo.
Baada ya kumaliza sura moja au makala moja, pitia kwa ufupi habari uliyosoma. Je, unaweza kukumbuka mambo makuu na sababu zinazotolewa kuyathibitisha. Hiyo itakusaidia kukumbuka habari hiyo ukaitumie wakati ujao.
Habari ya Kujifunza
Watu wa Yehova wana mengi ya kusoma. Lakini tuanzie wapi? Kila siku, ni vizuri kujifunza andiko na maelezo ya kitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku. Sisi huhudhuria mikutano ya kutaniko kila juma, na kuna faida kubwa sana ya kujifunza tunapotayarisha mikutano hiyo. Na zaidi, wengine wametumia wakati wao kwa hekima kujifunza baadhi ya vichapo vyetu vya Kikristo ambavyo vilichapishwa kabla ya wakati walipojifunza kweli. Wengine huchagua maandiko fulani ya usomaji wa Biblia wa kila juma na kuyafanyia utafiti kindani.
Namna gani kama hali hazikuruhusu kujifunza kwa makini habari zote ambazo zitashughulikiwa kwenye mikutano ya kutaniko ya kila juma? Epuka mtego wa kusoma habari mbio-mbio mradi tu umesoma, au vibaya zaidi, kutosoma chochote kabisa eti kwa sababu huwezi kutayarisha mambo yote. Badala yake, angalia kiasi ambacho unaweza kujifunza, na ujifunze vizuri. Fanya hivyo kila juma. Baada ya muda, jaribu kufanya hivyo na mikutano mingine.
“Jenga Nyumba Yako”
Yehova anatambua kwamba ni sharti wazazi watie bidii kuwapa wapendwa wao riziki. “Tengeneza kazi yako huko nje,” andiko la Mithali 24:27 linasema, “jifanyizie kazi yako tayari shambani.” Lakini usipuuze mahitaji ya kiroho ya familia yako. Kwa hiyo, mstari huo waendelea kusema: “Ukiisha, jenga nyumba yako.” Wazazi wanaweza kufanyaje hivyo? Mithali 24:3 linasema: “Kwa ufahamu [nyumba] huthibitika.”
Ufahamu unaweza kufaidije nyumba yako? Ufahamu ni uwezo wa akili kuelewa mambo yasiyoeleweka kwa urahisi. Kwa kweli inaweza kusemwa kwamba kuchunguza kwa makini hali ya familia yako ndiyo njia ya kwanza ya kuwa na funzo zuri la familia. Familia yako inaendeleaje kiroho? Sikiliza kwa makini unapozungumza nao. Je, kuna roho ya kulalamika au ya kinyongo? Je, jambo kuu katika familia ni kufuatia vitu vya kimwili? Mkiwa katika huduma ya shambani pamoja na watoto wako, je, wanajitambulisha kwa urahisi kwa vijana wenzao kwamba wao ni Mashahidi wa Yehova? Je, wanafurahia usomaji wa Biblia na funzo la familia? Je, kweli wanafuata njia ya Yehova maishani mwao? Ukiwa mzazi, uchunguzi wa makini utakuonyesha kile ambacho unahitaji kufanya ili kutia sifa za kiroho katika kila mmoja wa familia yako na kuzikuza.
Tafuta habari zinazozungumzia mahitaji fulani hususa katika Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Kisha ambia familia mapema makala mtakayosoma ili waifikirie mapema. Dumisha hali ya upendo wakati wa funzo. Kazia umuhimu wa habari mnayozungumzia, ukionyesha matumizi yake hususa katika familia yenu, bila kukaripia yeyote wala kumwaibisha. Husisha kila mmoja. Saidia kila mmoja aone kwamba Neno la Yehova ni “kamilifu” na linaandaa hasa kile kinachohitajika maishani.—Zab. 19:7.
Kupata Faida
Watu walio wepesi kuona mambo lakini wasio na ufahamu wa kiroho, wanaweza kuchunguza ulimwengu wote mzima, matukio ya ulimwengu, na hata kujichunguza wenyewe lakini washindwe kufahamu maana hasa ya mambo wanayoona. Kwa upande mwingine, kwa msaada wa roho ya Mungu, watu ambao hujifunza Neno la Mungu kwa ukawaida wanaweza kufahamu kwamba hizo ni kazi za Mungu, ni utimizo wa unabii wa Biblia, na ufunuo wa kusudi la Mungu la kuwabariki wanadamu watiifu.—Mk. 13:4-29; Rom. 1:20; Ufu. 12:12.
Ijapokuwa tuna pendeleo hilo la ajabu, tusiwe wenye kiburi kamwe. Badala yake, kuchunguza Neno la Mungu kila siku hutusaidia kuendelea kuwa wanyenyekevu. (Kum. 17:18-20) Pia kunatukinga na “nguvu ya udanganyifu ya dhambi” kwa sababu Neno la Mungu linapokuwa hai mioyoni mwetu, inaelekea sana azimio letu litashinda uvutio wa dhambi. (Ebr. 2:1; 3:13; Kol. 3:5-10) Kwa hiyo ‘tutatembea kwa kumstahili Yehova kwa madhumuni ya kumpendeza yeye kikamili tunapoendelea kuzaa matunda katika kila kazi njema.’ (Kol. 1:10) Ni kusudi letu kufanya hivyo tunapojifunza Neno la Mungu, na tunapata faida kubwa tunapolitimiza.