Sura ya 22
Sehemu ya 3—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
Ripoti ya duniani pote ya kazi ya kuhubiri ujumbe wa Ufalme tokea 1935 hadi 1945 imeonyeshwa katika kurasa 444 hadi 461. Mwaka 1935 ni wa maana sana kwa sababu wakati huo ile halaiki kubwa, au umati mkubwa, wa Ufunuo 7:9 ulipata kutambulishwa. Kuhusiana na kukusanywa kwa kikundi hicho, Mashahidi wa Yehova walianza kutambua kwamba Biblia iliweka mbele yao kazi ya kadiri kubwa zaidi ya yoyote iliyoitangulia. Waliifanyaje wakati mataifa yalipojizamisha katika Vita ya Ulimwengu 2 na nchi nyingi zilipowapiga marufuku au zikaharamisha fasihi zao za Biblia?
MASHAHIDI WA YEHOVA waliposhiriki katika huduma yao wakati wa miaka ya 1930, lengo lao lilikuwa kufikia watu wengi kadiri ilivyowezekana kwa ujumbe wa Ufalme. Ikiwa walitambua kupendezwa kusiko kwa kawaida, baadhi yao walikuwa wakikaa sehemu kubwa ya usiku wakieleza juu ya kweli za Biblia na kujibu maswali ili kutosheleza wenye njaa kiroho. Lakini katika visa vingi, Mashahidi walitumia tu utoaji mfupi uliokusudiwa kuchochea kupendezwa kwa wenye nyumba, na kisha waliacha fasihi au mihadhara ya Biblia ya watu wote itimize ile kazi iliyobaki. Kazi yao ilikuwa kuarifu watu, kupanda mbegu za kweli ya Ufalme.
Jitihada Nyingi ya Kufikia Watu Wengi kwa Habari Njema
Kazi ilifanywa kwa hima. Kwa kielelezo, mapema katika miaka ya 1930, wakati Armando Menazzi, katika Córdoba, Argentina, aliposoma ufafanuzi wenye kueleweka wazi wa kweli ya Biblia katika vijitabu Hell na Where Are the Dead?, alitenda kwa njia yenye kukata maneno. (Zab. 145:20; Mhu. 9:5; Mdo. 24:15) Akisukumwa na yale aliyojifunza, na kuchochewa na bidii iliyokuwa ikionyeshwa na Nicolás Argyrós, aliuza gereji lake la kurekebishia magari ili ajitoe mwenyewe kwa kazi ya kuhubiri kweli akiwa painia. Halafu, katika miaka ya mapema ya 1940, kwa kitia-moyo chake, Mashahidi katika Córdoba walinunua basi kuukuu, wakajenga vitanda ndani, na kulitumia kupeleka wahubiri kumi au zaidi kwenye safari za kuhubiri zilizochukua juma moja, majuma mawili, au hata miezi mitatu. Safari hizo zilipokuwa zikipangwa, ndugu na dada tofauti-tofauti kutanikoni walipewa fursa ya kwenda. Kila mmoja katika kikundi hicho alipewa mgawo wa kufanya kazi—kufanya usafi, kupika, au kuvua samaki na kuwinda ili kupata chakula. Katika angalau mikoa kumi ya Argentina, kikundi hicho chenye bidii kilihubiri nyumba hadi nyumba, kikieneza miji pamoja na vijiji na kujitahidi kufikia mashamba yaliyotawanyika.
Roho kama hiyo ilidhihirishwa katika shamba la Australia. Kazi nyingi ya kutoa ushahidi ilifanywa katika majiji ya pwani yenye idadi kubwa ya watu. Lakini Mashahidi walijitahidi pia kufikia watu walioishi katika maeneo yaliyo mbali. Hivyo, katika Machi 31, 1936, ili kufikia watu katika mashamba ya kufuga kondoo na ng’ombe yaliyotawanyika kotekote katika sehemu za mashambani, Arthur Willis na Bill Newlands walianza safari iliyowapeleka jumla ya kilometa 19,710. Katika sehemu iliyo kubwa ya safari yao, hakukuwa na barabara—ila vijia tu vya porini kupitia jangwa lisilo na miti lenye joto kali na dhoruba kali za vumbi. Lakini walisonga mbele. Kokote kupendezwa kulikoonyeshwa, walipiga rekodi za santuri zenye mihadhara ya Biblia na kuacha fasihi. Katika pindi nyingine, John E. (Ted) Sewell alienda pamoja nao; kisha akajitolea kutumikia katika Kusini-Mashariki mwa Asia.
Eneo lililosimamiwa na tawi la Sosaiti la Australia lilifika mbali sana nje ya Australia yenyewe. Lilitia ndani China na vikundi vya visiwa na mataifa yaliyoenea kuanzia Tahiti upande wa mashariki hadi Burma (sasa ni Myanmar) upande wa magharibi, umbali wa kilometa 13,700. Ndani ya eneo hilo zilikuwamo sehemu kama vile Hong Kong, Indochina (sasa ni Kambodia, Laos, na Vietnam), Indies Mashariki ya Uholanzi (kutia na visiwa kama Sumatra, Java, na Borneo), New Zealand, Siam (sasa ni Thailand), na Maleya. Lilikuwa jambo la kawaida kwa mwangalizi wa tawi, Alexander MacGillivray, Mscotland, kumwalika painia kijana mwenye bidii katika ofisi yake, na kumwonyesha ramani ya eneo la tawi na kumwuliza: ‘Je, ungependa kuwa mishonari?’ Kisha, akielekeza kwenye eneo ambalo ni kazi ndogo sana ya kuhubiri imefanywa, alikuwa akiuliza: ‘Je, ungependa kufungua kazi katika eneo hili?’
Wakati wa miaka ya mapema ya 1930, baadhi ya mapainia hao walikuwa wamefanya kazi nyingi katika Indies Mashariki ya Uholanzi (sasa ni Indonesia) na Singapore. Katika 1935, Frank Dewar, mwenyeji wa New Zealand, alisafiri pamoja na kikundi cha mapainia hao ndani ya Lightbearer mbali sana hadi Singapore. Kisha kabla tu ya mashua hiyo kusonga mbele hadi pwani ya kaskazini-magharibi mwa Maleya, Kapteni Eric Ewins akasema: “Basi, Frank, tumefika. Hapa ndipo tuwezapo kukufikisha. Ulichagua kwenda Siam. Basi, shuka ushike njia!” Lakini Frank alikuwa karibu amesahau habari za Siam. Alikuwa akifurahia utumishi pamoja na kikundi hicho ndani ya mashua. Sasa alikuwa peke yake.
Alitua katika Kuala Lumpur mpaka aweze kuchuma pesa za kutosha kuendelea na safari, lakini, alipokuwa huko, alipatwa na aksidenti ya gari—lori lilimgonga na kumwangusha kutoka baiskeli yake. Baada ya kupata nafuu, akiwa na dola tano tu katika mfuko wake, alipanda garimoshi lililokuwa likisafiri kutoka Singapore hadi Bangkok. Lakini akiwa na imani katika uwezo wa Yehova wa kuruzuku, akaanza kazi. Claude Goodman alikuwa amehubiri huko kifupi katika 1931; lakini wakati Frank alipowasili katika Julai 1936, hakukuwa na Mashahidi wa kumlaki. Hata hivyo, wakati wa miaka michache iliyofuata, wengine waliishiriki kazi—Willy Unglaube, Hans Thomas, na Kurt Gruber kutoka Ujerumani na Ted Sewell kutoka Australia. Waligawanya fasihi nyingi, lakini sehemu kubwa yayo ilikuwa katika Kiingereza, Kichina, na Kijapani.
Wakati barua ilipopelekwa kwenye makao makuu ya Sosaiti ikisema kwamba ndugu walihitaji fasihi katika lugha ya Thai lakini hawakuwa na mtafsiri, Ndugu Rutherford alijibu hivi: “Mimi simo Thailand; ni nyinyi mmo humo. Iweni na imani katika Yehova na kufanya kazi kwa bidii, nanyi mtapata mtafsiri.” Nao walimpata. Chomchai Inthaphan, aliyekuwa hapo kwanza mwalimu mkuu wa Shule ya Wasichana ya Kipresbiteri katika Chiang Mai, alikubali kweli, na kufikia 1941 alikuwa akitafsiri fasihi za Biblia katika lugha ya Thai.
Juma moja baada ya Frank Dewar kuanza kazi ya kuhubiri katika Bangkok, Frank Rice, ambaye alikuwa ameanzisha kazi ya Ufalme katika Java (sasa ni sehemu ya Indonesia), alipitia Thailand akiwa njiani kwenda kwenye mgawo mpya katika ile iliyokuwa wakati huo Indochina ya Ufaransa. Kama vile alivyokuwa amefanya katika eneo lake la mapema zaidi, alihubiria wale waliosema Kiingereza alipokuwa akijifunza lugha ya wenyeji. Baada ya kueneza Saigon (sasa ni Jiji la Ho Chi Minh), alifundisha Kiingereza ili aweze kununua gari kuukuu ambalo angeweza kutumia kufikia sehemu ya kaskazini ya nchi. Hangaiko lake halikuwa vitu vya kimwili vya starehe bali masilahi ya Ufalme. (Ebr. 13:5) Akitumia gari hilo alilonunua, alitoa ushahidi katika miji na vijiji na makao yaliyo peke yayo mwendo wote hadi Hanoi.
Utangazaji wa Ujasiri
Ili kuamsha kupendezwa katika ujumbe wa Ufalme na kuwajulisha watu uhitaji wa kuchukua hatua ya kukata maneno, njia zenye kutazamisha zilitumiwa na Mashahidi katika nchi nyingi. Kuanzia 1936 katika Glasgow, Scotland, Mashahidi walitangaza hotuba za mkusanyiko kwa kuvaa mabango yaliyoangikwa mabegani, mbele na nyuma, na kwa kugawanya vikaratasi vya ukaribishaji katika maeneo ya maduka. Miaka miwili baadaye, katika 1938, kuhusiana na mkusanyiko katika London, Uingereza, sehemu nyingine yenye kutazamisha iliongezwa. Nathan H. Knorr na Albert D. Schroeder, waliotumikia pamoja baadaye katika Baraza Linaloongoza, waliongoza gwaride ya Mashahidi karibu elfu moja kupitia sehemu kuu ya kibiashara katika London. Kila mpiga-miguu wa pili alivalia mabango yaliyotangaza hotuba ya watu wote “Yakabili Mambo ya Hakika,” ambayo yangetolewa na J. F. Rutherford katika jumba Royal Albert Hall. Wale waliokuwa katikati walichukua mkononi ishara zenye kusomeka “Dini Ni Mtego na Hila.” (Wakati huo walielewa dini kuwa ibada yote isiyopatana na Neno la Mungu, Biblia.) Baadaye katika juma hilo, ili kupunguza uhasama wa baadhi ya umma, ishara zenye kusomeka “Mtumikie Mungu na Kristo Mfalme” zilipachikwa katikati ya zile za mapema kidogo. Utendaji huo haukuwa rahisi kwa wengi kati ya Mashahidi wa Yehova, lakini waliuona kuwa njia nyingine ya kumtumikia Yehova, mtihani mwingine wa uaminifu-mshikamanifu wao kwake.
Si kila mtu aliyependezwa na utangazaji wa ujasiri ambao Mashahidi wa Yehova walitoa kwa ujumbe wao. Makasisi katika Australia na New Zealand walikaza mameneja wa vituo vya redio wakandamize utangazaji wote wa redio uliodhaminiwa na Mashahidi wa Yehova. Katika Aprili 1938, wakati Ndugu Rutherford alipokuwa njiani kwenda Australia ili kutoa hotuba ya redio, maofisa wa umma walijiruhusu wenyewe washurutishwe na makasisi kufuta mipango iliyokuwa imefanywa ili atumie Sydney Town Hall na vifaa vya redio. Upesi uwanja wa Sydney Sports Ground ulikodiwa, na kwa sababu ya utangazaji mkubwa wa magazeti kuhusu upinzani kwa ziara ya Ndugu Rutherford, umati mkubwa hata zaidi ulikuja kusikia hotuba yake. Katika pindi nyinginezo, wakati Mashahidi walipokatazwa kutumia vifaa vya redio, waliitikia kwa kutangaza sana mikutano ambayo hotuba za Ndugu Rutherford zilizorekodiwa zilitolewa kwa kutumia kinanda.
Makasisi katika Ubelgiji walituma watoto wakawatupie Mashahidi mawe, nao mapadri walikuwa wakienda wao binafsi kwenye makao ya watu ili kukusanya fasihi zilizokuwa zimegawanywa. Lakini baadhi ya wanavijiji walipenda yale waliyokuwa wakijifunza kutoka kwa Mashahidi wa Yehova. Mara nyingi walikuwa wakisema: “Nipe vijitabu vyenu kadhaa; padri ajapo, naweza kumpa kimoja ili kumridhisha na kubaki na vile vingine nivisome!”
Hata hivyo, miaka iliyofuata iliongoza kwenye upinzani wenye nguvu hata zaidi kwa Mashahidi wa Yehova na ujumbe wa Ufalme waliokuwa wakitangaza.
Kuhubiri Katika Ulaya Ujapokuwa Mnyanyaso wa Wakati wa Vita
Kwa sababu hawangeweza kuacha imani yao na kazi yao ya kuhubiri, maelfu ya Mashahidi wa Yehova katika Austria, Ubelgiji, Ufaransa, Uholanzi, na Ujerumani walitiwa gerezani au wakapelekwa kwenye kambi za mateso za Nazi. Humo kutendwa kinyama kulikuwa jambo la kawaida sana. Wale waliokuwa bado kutiwa gerezani waliendelea na huduma yao kwa tahadhari. Mara nyingi walifanya kazi kwa kutumia Biblia pekee na kutoa fasihi nyingine wakati tu walipokuwa wakifanya ziara za kurudia kwa watu wenye kupendezwa. Ili kuepuka kukamatwa, Mashahidi walikuwa wakizuru nyumba moja katika ghorofa na kisha labda kwenda kwenye jengo jingine, au baada ya kuzuru nyumba moja tu wangeenda kwenye barabara nyingine kabla ya kuzuru nyumba nyingine. Lakini hawakuwa na woga hata kidogo wa kutoa ushahidi.
Katika Desemba 12, 1936, miezi michache tu baada ya Gestapo kukamata maelfu ya Mashahidi na watu wengine wenye kupendezwa katika jitihada ya taifa zima ya kukomesha kazi yao, Mashahidi walifanya kampeni yao wenyewe. Kwa mwendo kama wa umeme walitia makumi ya maelfu ya nakala za azimio lililochapwa katika masanduku ya posta na chini ya milango ya watu kotekote katika Ujerumani. Maazimio hayo yalipinga jinsi ndugu na dada zao Wakristo walivyokuwa wakitendewa. Katika muda wa saa moja baada ya ugawanyaji huo kuanza, polisi walikuwa wakienda huku na huku wakijaribu kukamata wagawanyaji, lakini waliweza kuwakamata kama kumi hivi tu nchini mwote.
Maofisa walishtuka kwamba kampeni kama hiyo ingeweza kufanywa baada ya yote ambayo serikali ya Nazi ilikuwa imefanya ili kukandamiza kazi. Zaidi ya hilo, walikuja kuwaogopa raia. Kwa nini? Kwa sababu wakati polisi na wakuu wengine waliovalia kirasmi walipozuru makao ya watu na kuwauliza kama walikuwa wamepokea kikaratasi kama hicho, wengi wao walikana jambo hilo. Kwa kweli, wengi wao hawakuwa wamekipokea. Nakala zilikuwa zimeachiwa familia mbili au tatu tu katika kila jengo. Lakini polisi hawakujua hivyo. Walidhani kwamba nakala iliachwa kwenye kila mlango.
Wakati wa miezi iliyofuata, wakuu wa Nazi walikataa katakata mashtaka yaliyofanywa katika azimio hilo lililochapwa. Kwa hiyo, katika Juni 20, 1937, Mashahidi waliokuwa wangali huru waligawanya ujumbe mwingine, barua iliyoandikiwa wakuu katika magazeti ya umma ambayo ilifichua wazi mambo mengi kwa urefu juu ya mnyanyaso huo, hati hiyo ilitaja majina ya maofisa na tarehe na mahali pa mnyanyaso. Mshangao ulikuwa mkuu miongoni mwa Gestapo juu ya mfichuo huo na juu ya uwezo wa Mashahidi wa kufanya ugawanyaji kama huo.
Mambo mengi yaliyoipata familia ya Kusserow, iliyotoka Bad Lippspringe, Ujerumani, yalidhihirisha nia hiyohiyo ya kutoa ushahidi. Kielelezo kimoja chahusu jambo lililotukia baada ya Wilhelm Kusserow kuuawa hadharani katika Münster na serikali ya Nazi kwa sababu ya kukataa kwake kuridhiana imani yake. Hilda, mama yake Wilhelm, alienda gerezani mara hiyo na kusihi sana apewe mwili ili ukazikwe. Aliambia familia yake hivi: “Tutatoa ushahidi mwingi kwa watu waliomjua.” Kwenye mazishi, Franz, baba ya Wilhelm, alitoa sala iliyoonyesha imani katika uandalizi wenye upendo wa Yehova. Kaburini, Karl-Heinz, ndugu mdogo wa Wilhelm alisema maneno ya kufariji kutoka katika Biblia. Kwa kufanya hivyo waliadhibiwa, lakini kwao jambo lililokuwa la maana lilikuwa kumheshimu Yehova kwa kutoa ushahidi kuhusu jina na Ufalme wake.
Kadiri mikazo ya wakati wa vita ilivyoongezeka katika Uholanzi, kwa hekima Mashahidi huko walirekebisha mipango yao ya mikutano. Sasa ilifanywa katika vikundi vya watu kumi au wachache zaidi katika makao ya watu binafsi. Mahali pa mikutano palibadilishwa mara nyingi. Kila Shahidi alihudhuria pamoja na kikundi chake tu, na hakuna yeyote angetoboa siri ya mahali pa funzo, hata kwa rafiki mwenye kutumainiwa. Katika pindi hiyo ya historia, wakati idadi nzimanzima za watu zilipokuwa zikifukuzwa kutoka makao yao kama tokeo la vita, Mashahidi wa Yehova walijua kwamba watu walihitaji sana ujumbe wenye kufariji upatikanao tu katika Neno la Mungu, nao waliushiriki pamoja nao bila woga. Lakini barua moja kutoka ofisi ya tawi iliwakumbusha akina ndugu juu ya tahadhari ambayo Yesu alionyesha katika pindi mbalimbali alipokabiliwa na wapinzani. (Mt. 10:16; 22:15-22) Kama tokeo, walipokutana na mtu aliyeonyesha uhasama, waliandika nambari ya nyumba kwa uangalifu ili tahadhari za pekee ziweze kuchukuliwa wakati wa kufanya kazi katika eneo hilo wakati ujao.
Katika Ugiriki wakazi walipatwa na mateso yenye kuenea sana wakati wa kukaliwa na Ujerumani. Hata hivyo, kutendwa vibaya sana kulikowapata Mashahidi wa Yehova kulikuja kama tokeo la kusingiziwa kikatili na makasisi wa Kanisa Orthodoksi la Kigiriki, waliosisitiza kwamba polisi na mahakama ziwachukulie hatua. Mashahidi wengi walitiwa gerezani au wakafukuzwa kutoka miji ya kwao na kupelekwa kwenye vijiji vya mbali au kufungwa chini ya hali mbaya sana katika visiwa visivyo na kitu. Hata hivyo, wao waliendelea kutoa ushahidi. (Linganisha Matendo 8:1, 4.) Mara nyingi jambo hilo lilifanywa kwa kuongea na watu katika bustani za umma, kwa kuketi kwenye mabenchi pamoja nao na kuwaambia juu ya Ufalme wa Mungu. Wakati kupendezwa kwa kweli kulipopatikana, mtu huyo aliazimwa fasihi fulani ya Biblia yenye thamani kubwa. Fasihi hiyo ilirudishwa baadaye ili itumiwe tena na tena. Wengi wapendao kweli walikubali kwa shukrani msaada uliotolewa na Mashahidi na hata wakajiunga pamoja nao katika kushiriki habari njema na wengine, ingawa kufanya hivyo kuliwaletea mnyanyaso mkali.
Jambo la maana katika ujasiri na ustahimilivu wa Mashahidi lilikuwa kujengwa kwao na chakula cha kiroho. Ingawa ugavi wa fasihi ya kugawiwa wengine hatimaye ilipata kupungua sana katika sehemu nyingine za Ulaya wakati wa vita, walifaulu kueneza miongoni mwao habari yenye kujenga imani iliyokuwa imetayarishwa na Sosaiti kwa ajili ya funzo la Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote. Kwa kuhatirisha maisha zao, August Kraft, Peter Gölles, Ludwig Cyranek, Therese Schreiber, na wengine wengi walishiriki kazi ya kurudufisha na kugawanya habari ya funzo iliyoingizwa katika Austria kisirisiri kutoka Chekoslovakia, Italia, na Uswisi. Katika Uholanzi, ni mlinzi wa gereza mwenye fadhili aliyesaidia kwa kupata Biblia kwa ajili ya Arthur Winkler. Ijapokuwa tahadhari yote iliyochukuliwa na maadui, maji ya kweli ya Biblia yenye kuburudisha kutoka kwa Mnara wa Mlinzi yalifika hata ndani ya kambi za mateso za Ujerumani na kuenezwa miongoni mwa Mashahidi humo.
Kufungiwa gerezani na katika kambi za mateso hakukuzuia Mashahidi wa Yehova wasiwe mashahidi. Wakati mtume Paulo alipokuwa gerezani katika Roma, aliandika hivi: “Ninavumilia uovu kufikia hatua ya vifungo vya gereza . . . Hata hivyo, neno la Mungu halifungwi.” (2 Tim. 2:9, NW) Ilithibitika kuwa vivyo hivyo kwa habari ya Mashahidi wa Yehova katika Ulaya wakati wa Vita ya Ulimwengu 2. Walinzi waliona mwenendo wao; baadhi yao waliuliza maswali, na wachache wao wakawa waamini wenzao, hata ingawa hiyo ilimaanisha kupoteza uhuru wao wenyewe. Wafungwa wengi waliofungwa pamoja na Mashahidi walikuwa wametoka nchi mbalimbali kama vile Urusi, ambako ni kazi ndogo sana ya kuhubiri habari njema ilikuwa imefanywa. Baada ya vita baadhi yao walirudi nchi za kwao wakiwa Mashahidi wa Yehova, wakiwa na hamu ya kueneza ujumbe wa Ufalme humo.
Mnyanyaso wa kinyama na athari za vita kamili havikuweza kuzuia ile kazi iliyotabiriwa ya kukusanya watu kwenye nyumba kuu ya kiroho ya Yehova kwa ajili ya ibada. (Isa. 2:2-4) Kuanzia 1938 hadi 1945, nchi nyingi za Ulaya zilionyesha maongezeko makubwa ya idadi ya waliokuwa wakishiriki hadharani katika ibada hiyo kwa kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu. Katika Finland, Ufaransa, Uingereza, na Uswisi, Mashahidi walipata maongezeko ya karibu asilimia 100. Katika Ugiriki, kulikuwa ongezeko la karibu mara saba. Katika Uholanzi, lilikuwa mara 12. Lakini kufikia mwisho wa 1945, habari kamili haikuwa imefika kutoka Ujerumani au Rumania, na ripoti ambazo hazikuwa zimekamilika zilitoka katika nchi nyingine chache.
Nje ya Ulaya Wakati wa Miaka Hiyo ya Vita
Katika nchi za Mashariki vilevile, vita ya ulimwengu ilitokeza magumu makubwa sana kwa Mashahidi wa Yehova. Katika Japani na Korea, walikamatwa na kupigwa na kuteswa kwa sababu walitetea Ufalme wa Mungu na hawakuabudu maliki wa Japani. Hatimaye mawasiliano yote na Mashahidi katika zile nchi nyingine yalikatwa kabisa. Kwa wengi wao, fursa pekee za kutoa ushahidi zilikuwapo wakati walipohojiwa au waliposhtakiwa mahakamani. Kufikia mwisho wa vita, huduma ya hadharani ya Mashahidi wa Yehova katika nchi hizo ilikuwa ni kama imekoma.
Wakati vita ilipofika Filipino, Mashahidi huko walitendwa vibaya na pande zote mbili kwa sababu wao hawakuunga mkono ama Wajapani ama wakinzani. Ili kuepuka kukamatwa, Mashahidi wengi waliacha makao yao. Lakini walipokuwa wakihamahama walihubiri—na kuwaazima wengine fasihi wakati zilipokuwa zinapatikana, na baadaye kwa kutumia Biblia pekee. Wakati vita viliposonga mbali, hata walitayarisha mashua kadhaa ili kusafirisha vikundi vikubwa vya Mashahidi kwenye visiwa ambavyo hakuna ushahidi uliokuwa umetolewa.
Katika Burma (sasa ni Myanmar), mkazo kutoka kwa makasisi Waanglikana, Wamethodisti, Wakatoliki wa Roma, na Wabaptisti Waamerika uliotumiwa juu ya maofisa wa kikoloni ndio uliosababisha kupigwa marufuku kwa fasihi za Mashahidi wa Yehova katika Mei 1941 wala si uvamizi wa Japani. Mashahidi wawili waliokuwa wakifanya kazi katika ofisi ya kebo waliona telegramu iliyowajulisha ni jambo gani lililokaribia kutukia, hivyo ndugu waliondoa haraka fasihi katika depo ya Sosaiti ili kuepuka isinyakuliwe na maofisa. Halafu jitihada ilifanywa ya kuipeleka China kupitia nchi kavu.
Wakati huo serikali ya Marekani ilikuwa ikisafirisha kwa malori kiasi kikubwa cha vifaa vya vita kupitia Barabara ya Burma ili kuunga mkono serikali ya Kitaifa ya China. Ndugu walijaribu kupata nafasi katika mojawapo malori hayo lakini wakakataliwa vikali. Jitihada za kupata gari kutoka Singapore zilishindwa pia. Hata hivyo, wakati Mick Engel, aliyekuwa msimamizi wa depo ya Sosaiti ya Rangoon (sasa ni Yangon), alipomwendea ofisa wa cheo cha juu wa Marekani, alipewa ruhusa ya kusafirisha fasihi hizo kwa malori ya kijeshi.
Hata hivyo, baada ya hapo wakati Fred Paton na Hector Oates walipomwendea ofisa aliyesimamia msafara uliokuwa ukienda China na kumuuliza awape nafasi, alipandwa sana na hasira! “Eti nini?” akapaaza sauti. “Nawezaje kuwapa nafasi yenye thamani sana katika malori yangu kwa ajili ya trakti zenu duni hali mimi sina nafasi hata kidogo kwa ugavi wenye kuhitajiwa sana wa kijeshi na kitiba unaoharibikia hapa nje?” Fred alitua, akatia mkono katika mkoba wake, akamwonyesha ile barua ya ruhusa, na kutaja kwamba lingekuwa jambo la hatari sana kupuuza mwelekezo uliotolewa na maofisa katika Rangoon. Si kwamba tu msimamizi huyo wa msafara alipanga kusafirisha tani mbili za vitabu bali pia aliwapa ndugu hao lori jepesi pamoja na dereva na ugavi wa mahitaji walitumie. Walielekea kaskazini-mashariki kupitia njia hiyo hatari ya milimani ya kwenda China wakiwa na shehena yao yenye thamani kubwa. Baada ya kutoa ushahidi katika Pao-shan, walisonga mbele hadi Chungking (Pahsien). Maelfu ya fasihi mbalimbali yenye kusema juu ya Ufalme wa Yehova iligawanywa wakati wa mwaka mmoja waliotumia katika China. Miongoni mwa wale waliotolea ushahidi binafsi alikuwa Chiang Kai-shek, rais wa serikali ya Kitaifa ya China.
Wakati huohuo, kadiri Burma ilivyozidi kushambuliwa kwa mabomu, Mashahidi wote isipokuwa watatu tu waliondoka nchini, wengi wao wakielekea India. Bila shaka, utendaji wa hao watatu waliobaki ulikuwa mdogo. Hata hivyo waliendelea kutoa ushahidi ki-vivi-hivi, na jitihada zao zilizaa matunda baada ya vita.
Katika Amerika Kaskazini vilevile, Mashahidi wa Yehova walikabiliwa na vizuizi vikubwa wakati wa vita. Jeuri ya wafanyaghasia yenye kuenea na matumizi yaliyo kinyume cha katiba ya sheria za mahalimahali vilileta mkazo juu ya kazi ya kuhubiri. Maelfu walitiwa gerezani kwa sababu ya kuchukua msimamo wao wakiwa Wakristo wasiokuwamo. Hata hivyo, jambo hilo halikupunguza huduma ya nyumba hadi nyumba ya Mashahidi. Zaidi ya hilo, kuanzia na Februari 1940, lilikuwa jambo la kawaida kuwaona barabarani katika wilaya za kibiashara wakitoa Mnara wa Mlinzi na Consolation (sasa ni Amkeni!). Bidii yao ikawa yenye nguvu hata zaidi. Ingawa walikuwa wakipatwa na mnyanyaso mkali usiopata kuonwa katika sehemu hiyo ya ulimwengu, Mashahidi waliongezeka zaidi ya mara mbili katika Marekani na Kanada pia tokea 1938 hadi 1945, na wakati waliotumia katika huduma yao ya hadharani uliongezeka mara tatu.
Katika nchi nyingi zilizohusiana na Jumuiya ya Madola ya Uingereza (katika Amerika Kaskazini, Afrika, Asia, na visiwa vya Karibea na vya Pasifiki) ama Mashahidi wa Yehova ama fasihi zao zilipigwa marufuku na serikali. Mojawapo nchi hizo ni Australia. Tangazo la serikali lililotangazwa huko katika Januari 17, 1941, kwa mwelekezo wa gavana mkuu, lilifanya iwe kinyume cha sheria kwa Mashahidi wa Yehova kukutana kwa ajili ya ibada, kueneza yoyote ya fasihi zao, au hata kuwa nayo. Chini ya sheria iliwezekana kupinga marufuku hiyo mahakamani, na jambo hilo lilifanywa mara moja. Lakini ilikuwa zaidi ya miaka miwili kabla Bw. Justice Starke wa Mahakama Kuu kujulisha kwamba kanuni ambazo marufuku hiyo ilitegemea zilikuwa “matumizi mabaya ya mamlaka, kinyume cha sheria, na yenye uonevu.” Washiriki wote wa Mahakama Kuu waliiondoa marufuku hiyo. Kwa wakati huohuo Mashahidi wa Yehova walifanya nini?
Kwa kuiga mitume wa Yesu Kristo, ‘walimtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’ (Mdo. 4:19, 20; 5:29, NW) Waliendelea kuhubiri. Vijapokuwa vizuizi vingi, hata walipanga kuwa na mkusanyiko katika Hargrave Park, karibu na Sydney, Desemba 25-29, 1941. Wakati serikali ilipokataa kusafirisha baadhi ya wajumbe kwa reli, kikundi kimoja kutoka Australia Magharibi kilitia katika magari yao vifaa vyenye kutokeza gesi vyenye kutumia makaa na kuanza safari ya siku 14 ya kuvuka nchi, iliyotia ndani kutumia juma moja wakivuka ile Tambarare ya Nullarbor iliyo kavu sana. Waliwasili salama nao wakafurahia programu pamoja na wajumbe wengine elfu sita. Mwaka uliofuata, kusanyiko lingine lilifanywa, lakini wakati huu liligawanywa kuwa vikundi vidogo 150 katika majiji saba makubwa kotekote nchini, wasemaji wakisafiri toka mahali pamoja hadi pengine.
Kadiri hali katika Ulaya zilivyozorota katika 1939, baadhi ya wahudumu mapainia wa Mashahidi wa Yehova walijitolea kutumikia katika mashamba mengine. (Linganisha Mathayo 10:23; Matendo 8:4.) Mapainia watatu kutoka Ujerumani walitumwa kutoka Uswisi hadi Shanghai, China. Idadi fulani yao walienda Amerika Kusini. Miongoni mwa wale waliohamishwa kwenda Brazili alikuwa Otto Estelmann, aliyekuwa amekuwa akitembelea na kusaidia makutaniko katika Chekoslovakia, na Erich Kattner, aliyekuwa ametumikia kwenye ofisi ya Watch Tower Society katika Prague. Mgawo wao mpya haukuwa rahisi. Walipata kwamba, katika sehemu fulani za mashamba, Mashahidi walikuwa wakiamka mapema na kuhubiri hadi saa 1:00 asubuhi na kisha kufanya utumishi zaidi wa shambani wakati wa jioni sana. Ndugu Kattner akumbuka kwamba alipokuwa akitembea toka mahali pamoja hadi pengine, mara nyingi alilala nje, akitumia mkoba wake wa fasihi kama mto.—Linganisha Mathayo 8:20.
Wote wawili Ndugu Estelmann na Ndugu Kattner walikuwa wakiwindwa daima na polisi wa siri wa Nazi katika Ulaya. Je, kuhamia kwao Brazili kuliwaokoa na mnyanyaso? Kinyume cha hivyo, baada ya mwaka mmoja tu, walijipata wakiwa wamezuiliwa nyumbani na kufungwa kwa muda mrefu kwa uchochezi wa maofisa ambao kwa wazi walikuwa marafiki wa Nazi! Upinzani kutoka kwa makasisi Wakatoliki ulikuwa wa kawaida pia, lakini Mashahidi waliendelea na kazi yao waliyopewa na Mungu. Walijitahidi daima kufikia majiji na miji katika Brazili ambayo ujumbe wa Ufalme ulikuwa haujahubiriwa.
Pitio la hali ya dunia hufunua kwamba katika nchi nyingi ambako Mashahidi wa Yehova walikuwa wakati wa Vita ya Ulimwengu 2, serikali ilipiga marufuku ama tengenezo lao ama fasihi zao. Ingawa walikuwa wamekuwa wakihubiri katika nchi 117 katika 1938, katika miaka ya vita (1939-1945) ama tengenezo lao au fasihi zao zilipigwa marufuku, au wahudumu wao wakarudishwa kwenye nchi zao, katika zaidi ya nchi 60 kati ya hizo. Hata mahali ambako hakukuwa na marufuku, walikabiliwa na umati wenye ghasia na walikamatwa mara nyingi. Yajapokuwa yote hayo, kazi ya kuhubiri habari njema haikukoma.
Umati Mkubwa Waanza Kujidhihirisha Katika Amerika ya Latin
Katikati ya miaka ya vita, katika Februari 1943, wakipanga kwa ajili ya kazi ambayo ingefanywa wakati wa baada ya vita, Watch Tower Society ilianzisha Shule ya Gileadi katika Jimbo la New York ili kuzoeza wamishonari kwa ajili ya utumishi katika nchi za kigeni. Kabla ya mwisho wa mwaka, 12 kati ya wamishonari hao walikuwa tayari wameanza kutumikia katika Kuba. Shamba huko lilithibitika kuwa lenye kuzaa sana.
Mapema sana kama 1910, mbegu za kweli ya Biblia zilikuwa zimefika Kuba. C. T. Russell alikuwa ametoa hotuba moja huko katika 1913. J. F. Rutherford alikuwa amehutubu kwa redio katika Havana katika 1932, nayo habari hiyo ilikuwa imetangazwa tena katika Kihispania. Lakini ukuzi ulikuwa wa polepole. Kutojua kusoma na kuandika kulienea sana katika wakati huo na uadui wa kidini ulikuwa mwingi. Mwanzoni watu wasemao Kiingereza waliotoka Jamaika na mahali pengine ndio sanasana walioonyesha kupendezwa. Kufikia 1936 kulikuwa wapiga-mbiu wa Ufalme 40 tu katika Kuba. Lakini ndipo kazi ya kupanda na kutilia maji mbegu za kweli ya Ufalme ikaanza kuzaa matunda zaidi.
Katika 1934 Wakuba wa kwanza walikuwa wamebatizwa; wengine wakafuata. Kuanzia 1940, matangazo ya kila siku ya redio pamoja na kutoa ushahidi kwa ujasiri barabarani kuliongezea nguvu huduma ya nyumba hadi nyumba huko. Hata kabla ya wamishonari waliozoezwa Gileadi kuwasili katika 1943, katika Kuba mlikuwamo 950 waliokuwa wamekubali habari njema nao walikuwa wakiihubiri kwa wengine, ingawa si wote waliokuwa wakishiriki kwa ukawaida. Wakati wa miaka miwili kufuatia kuwasili kwa wamishonari, hesabu iliongezeka kwa kasi hata zaidi. Kufikia 1945, Mashahidi wa Yehova katika Kuba walikuwa 1,894. Ijapokuwa wengi wao walikuwa wametoka katika dini iliyofundisha kwamba wategemezaji wote waaminifu wa kanisa wangeenda mbinguni, wengi wa wale waliopata kuwa Mashahidi wa Yehova walikubali kwa hamu taraja la uhai wa milele duniani katika paradiso iliyorudishwa. (Mwa. 1:28; 2:15; Zab. 37:9, 29; Ufu. 21:3, 4) Ni asilimia 1.4 tu kati yao waliodai kuwa ndugu za Kristo watiwa-mafuta kwa roho.
Kwa njia nyingine, msaada ulitolewa kwa shamba la Amerika ya Latin na makao makuu ya Sosaiti. Mapema katika 1944, N. H. Knorr, F. W. Franz, W. E. Van Amburgh, na M. G. Henschel walitumia siku kumi katika Kuba kuimarisha ndugu kiroho humo. Katika pindi hiyo mkusanyiko ulifanywa katika Havana, na mipango ilitolewa kwa ajili ya kuratibu vizuri zaidi kazi ya kuhubiri. Pia safari hiyo iliwapeleka Ndugu Knorr na Ndugu Henschel hadi Kosta Rika, Guatemala, na Mexico ili kusaidia Mashahidi wa Yehova katika nchi hizo.
Katika 1945 na 1946, N. H. Knorr na F. W. Franz walifanya safari zilizowawezesha kusema na kufanya kazi pamoja na Mashahidi katika nchi 24 katika eneo hilo la kuanzia Mexico hadi ncha ya kusini mwa Amerika Kusini pamoja na Karibea. Walitumia binafsi miezi mitano katika sehemu hiyo ya ulimwengu, wakitoa msaada na mwelekezo wa upendo. Katika baadhi ya sehemu hizo walikutana na watu wachache tu wenye kupendezwa. Ili kuwe na mipango ya ukawaida kwa ajili ya mikutano na utumishi wa shambani, walisaidia kibinafsi katika kupanga kitengenezo makutaniko ya kwanza katika Lima, Peru, na Caracas, Venezuela. Mahali popote ambapo tayari mikutano ya kutaniko ilikuwa ikifanywa, waliihudhuria, na pindi kwa pindi, walitoa shauri juu ya jinsi ya kufanya maendeleo katika thamani yayo yenye kutumika kuhusiana na kazi ya kueneza evanjeli.
Ilipowezekana, mipango ilifanywa ili hotuba za watu wote za Biblia zitolewe wakati wa ziara hizo. Hotuba hizo zilitangazwa sana kwa kutumia mabango yaliyovaliwa na Mashahidi na kwa kugawanya barabarani vikaratasi vya ukaribishaji. Kama tokeo, wale Mashahidi 394 katika Brazili walifurahia kuwa na watu 765 kwenye mkusanyiko wao katika São Paulo. Katika Chile, ambako kulikuwa na wapiga-mbiu wa Ufalme 83, watu 340 walikuja kusikia hotuba iliyokuwa imetangazwa kipekee. Katika Kosta Rika wale Mashahidi wenyeji 253 walifurahia kuwa na jumla ya watu 849 kwenye mikusanyiko yao miwili. Hizo zilikuwa pindi za ushirika wenye uchangamfu miongoni mwa akina ndugu.
Hata hivyo, lengo halikuwa tu kuwa na mikusanyiko yenye kukumbukwa. Wakati wa safari hizo wawakilishi kutoka makao makuu waliweka mkazo wa pekee juu ya umaana wa kufanya ziara za kuwarudia watu wenye kupendezwa na kuongoza mafunzo ya Biblia nyumbani pamoja nao. Ikiwa watu wangepata kuwa wanafunzi halisi, walihitaji maagizo ya ukawaida kutoka kwa Neno la Mungu. Kama tokeo, idadi ya mafunzo ya Biblia nyumbani yaliongezeka kasi katika sehemu hiyo ya ulimwengu.
Wakati Ndugu Knorr na Ndugu Franz walipokuwa wakifanya safari hizo za utumishi, wamishonari zaidi waliozoezwa Gileadi walikuwa wakiwasili katika migawo yao. Kufikia mwisho wa 1944, baadhi yao walikuwa wakitumikia katika Kosta Rika, Mexico, na Puerto Riko. Katika 1945, wamishonari wengine walikuwa wakisaidia kupanga kitengenezo vizuri zaidi kazi ya kuhubiri katika Barbados, Brazili, Honduras ya Uingereza (sasa ni Belize), Chile, Kolombia, El Salvador, Guatemala, Haiti, Jamaika, Nikaragua, Panama, na Uruguai. Wakati wamishonari wawili wa kwanza walipowasili katika Jamhuri ya Dominika katika 1945, walikuwa ndio Mashahidi pekee katika nchi hiyo. Matokeo ya huduma ya wamishonari hao wa mapema yalihisiwa upesi. Trinidad Paniagua alisema hivi kuhusu wamishonari wa kwanza waliotumwa Guatemala: “Hilo ndilo tulilohitaji hasa—walimu wa Neno la Mungu ambao wangetusaidia kuelewa jinsi ya kufanya kazi.”
Hivyo msingi ulikuwa ukiwekwa kwa ajili ya upanuzi katika sehemu hiyo ya shamba la ulimwengu. Katika visiwa vya Karibea, kulikuwa wapiga-mbiu wa Ufalme 3,394 kufikia mwisho wa 1945. Katika Mexico, walikuwa 3,276, na wengine 404 katika Amerika ya Kati. Katika Amerika Kusini, 1,042. Kwa sehemu hii ya ulimwengu hiyo inawakilisha ongezeko la asilimia 386 wakati wa miaka saba iliyopita, pindi yenye msukosuko sana ya historia ya kibinadamu. Lakini ulikuwa ni mwanzo tu. Ukuzi wa kadiri yenye kutokeza kikweli ulikuwa ungali mbele! Biblia ilikuwa imetabiri kwamba “umati mkubwa . . . kutoka katika mataifa yote na makabila na vikundi vya watu na lugha” ungekusanywa wakiwa waabudu wa Yehova kabla ya dhiki kubwa.—Ufu. 7:9, 10, 14, NW.
Wakati Vita ya Ulimwengu 2 ilipoanza katika 1939, kulikuwa Mashahidi wa Yehova 72,475 tu wakihubiri katika nchi 115 (zikihesabiwa kulingana na mipaka ya kitaifa ya miaka ya mapema ya 1990). Ujapokuwa mnyanyaso mkali walioupata duniani pote, waliongezeka kuwa zaidi ya mara mbili katika hesabu kufikia mwisho wa vita hiyo. Hivyo, ripoti ya mwaka wa 1945 ilionyesha Mashahidi 156,299 wenye kutenda katika zile nchi 107 ambazo ripoti imeweza kujumlishwa. Hata hivyo, kufikia wakati huo, kwa kweli nchi 163 zilikuwa zimefikiwa kwa ujumbe wa Ufalme.
Ushahidi uliotolewa wakati wa miaka ya kuanzia 1936 hadi 1945 ulikuwa wenye kustaajabisha kwelikweli. Wakati wa mwongo huo wa msukosuko wa ulimwengu, Mashahidi wa Yehova hao wenye bidii walitumia jumla ya saa 212,069,285 kupiga mbiu kwa ulimwengu kwamba Ufalme wa Mungu ndio tumaini pekee kwa wanadamu. Pia waligawanya vitabu, vijitabu, na magazeti 343,054,579 ili kusaidia watu waelewe msingi wa Kimaandiko wa uhakika huo. Ili kusaidia wenye kupendezwa kikweli, kwa wastani, katika 1945 walikuwa wakiongoza mafunzo ya Biblia nyumbani 104,814, bila malipo.
[Blabu katika ukurasa wa 455]
Ingawa hali za wakati wa vita ziliwalazimisha kutoroka, wao waliendelea kuhubiri
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 451-453]
Walikataa Kuacha Kutoa Ushahidi Hata Ingawa Walitiwa Gerezani
Walioonyeshwa hapa ni baadhi tu ya maelfu ya wale walioteseka kwa ajili ya imani yao katika magereza na kambi za mateso wakati wa Vita ya Ulimwengu 2
1. Adrian Thompson, New Zealand. Alifungwa katika 1941 nchini Australia; maombi yake ya kusihi asitiwe kwenye orodha ya wanajeshi yalikataliwa wakati Australia ilipopiga marufuku Mashahidi wa Yehova. Baada ya kuachiliwa kwake, akiwa mwangalizi asafiriye, aliimarisha makutaniko katika huduma yayo ya hadharani. Alitumikia akiwa mishonari na mwangalizi asafiriye wa kwanza katika Japani baada ya vita; aliendelea kuhubiri kwa bidii hadi kifo chake katika 1976.
2. Alois Moser, Austria. Alifungwa katika magereza na kambi saba za mateso. Yeye angali Shahidi mwenye bidii katika 1992 akiwa na umri wa miaka 92.
3. Franz Wohlfahrt, Austria. Kuuawa kwa babaye na nduguye hakukumzuia Franz. Alifungwa katika Kambi ya Rollwald katika Ujerumani kwa miaka mitano. Alikuwa angali akitoa ushahidi katika 1992 akiwa na umri wa miaka 70.
4. Thomas Jones, Kanada. Alifungwa katika 1944, kisha akafungwa katika kambi mbili za kazi ngumu. Baada ya miaka 34 ya utumishi wa wakati wote, aliwekwa katika 1977 kuwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi inayosimamia kazi ya kuhubiri katika Kanada yote.
5. Maria Hombach, Ujerumani. Alifungwa mara kwa mara; katika kifungo cha peke yake kwa miaka mitatu na nusu. Akiwa tarishi, alihatirisha maisha yake kupeleka fasihi za Biblia kwa Mashahidi wenzi. Katika 1992, yeye alikuwa mshiriki mwaminifu wa familia ya Betheli akiwa na umri wa miaka 90.
6. Max na Konrad Franke, Ujerumani. Baba na mwanaye, wote wawili wakifungwa mara kwa mara, na kwa miaka mingi. (Mke wa Konrad, Gertrud, alikuwa pia gerezani.) Wote waliendelea kuwa waaminifu-washikamanifu, watumishi wa Yehova wenye bidii, na Konrad alikuwa katika mstari wa mbele wa kuanzisha upya kazi ya kuhubiri ya Mashahidi katika Ujerumani ya baada ya vita.
7. A. Pryce Hughes, Uingereza. Alihukumiwa kifungo cha miaka miwili katika Wormwood Scrubs, London; pia amepata kufungwa kwa sababu ya imani yake wakati wa Vita ya Ulimwengu 1. Alikuwa katika mstari wa mbele katika kazi ya kuhubiri Ufalme katika Uingereza hadi kufikia kifo chake katika 1978.
8. Adolphe na Emma Arnold pamoja na binti yao Simone, Ufaransa. Baada ya Adolphe kufungwa, Emma na Simone waliendelea kutoa ushahidi, na pia kugawia Mashahidi wengine fasihi. Alipokuwa gerezani, Emma, alifungwa peke yake kwa sababu ya kuendelea kutolea wafungwa wengine ushahidi. Simone alipelekwa kwenye shule ya kurekebishia tabia. Wote waliendelea kuwa Mashahidi wenye bidii.
9. Ernst na Hildegard Seliger, Ujerumani. Wote wawili wamekuwa katika magereza na kambi za mateso kwa miaka zaidi ya 40 kwa ajili ya imani yao. Hata wakiwa gerezani waliendelea kushiriki na wengine kweli za Biblia. Walipoachiliwa huru walitumia wakati wao wote wakihubiri habari njema. Ndugu Seliger alikufa akiwa mtumishi wa Mungu mwaminifu-mshikamanifu katika 1985; Dada Seliger, alikufa katika 1992.
10. Carl Johnson, Marekani. Miaka mwili baada ya kubatizwa, alifungwa pamoja na mamia ya Mashahidi wengine katika Ashland, Kentucky. Ametumikia akiwa painia na akiwa mwangalizi wa mzunguko; katika 1992, alikuwa angali akiongoza katika huduma ya shambani akiwa mzee.
11. August Peters, Ujerumani. Akitenganishwa na mke wake na watoto wanne, alifungwa katika 1936-1937, pia katika 1937-1945. Baada ya kuachiliwa, badala ya kupunguza wakati wa mahubiri, aliuongeza, katika utumishi wa wakati wote. Katika 1992, akiwa na umri wa miaka 99, yeye alikuwa angali akitumikia akiwa mshiriki wa familia ya Betheli na alikuwa ameona idadi ya Mashahidi wa Yehova katika Ujerumani ikikua hadi kufikia 163, 095.
12. Gertrud Ott, Ujerumani. Alifungwa katika Lodz, Poland, kisha katika kambi ya mateso ya Auschwitz, kisha katika Gross-Rosen na Bergen-Belsen katika Ujerumani. Baada ya vita alitumikia kwa bidii akiwa mishonari katika Indonesia, Iran, and Luxembourg.
13. Katsuo Miura, Japani. Miaka saba baada ya kukamatwa na kufungwa kwake katika Hiroshima, sehemu kubwa ya gereza alimokuwa amefungiwa iliharibiwa na bomu la atomi lililofanya jiji kuwa ukiwa. Hata hivyo, madaktari hawakupata ithibati yoyote kwamba aliathiriwa na minururisho. Alitumia miaka ya mwisho ya maisha yake akiwa painia.
14. Martin na Gertrud Poetzinger, Ujerumani. Miezi michache baada ya kufunga ndoa, walikamatwa na kutenganishwa kwa miaka tisa. Martin alipelekwa Dachau and Mauthausen; Gertrud, alipelekwa Ravensbrück. Wajapotendwa kikatili, imani yao haikuyumbayumba. Baada ya kuachiliwa walitoa jitihada zao zote kwa utumishi wa Yehova. Kwa miaka 29 alitumikia akiwa mwangalizi asafiriye kotekote katika Ujerumani; kisha, akawa mshiriki wa Baraza Linaloongoza hadi kifo chake katika 1988. Katika 1992, Gertrud aliendelea kuwa mweneza-evanjeli mwenye bidii.
15. Jizo na Matsue Ishii, Japani. Baada ya kugawanya fasihi za Biblia kotekote katika Japani kwa mwongo mmoja, wakafungwa. Ingawa kazi ya Mashahidi wa Yehova katika Japani ilikomeshwa wakati wa vita, Ndugu na Dada Ishii walitoa ushahidi tena kwa bidii baada ya vita. Kufikia 1992, Matsue Ishii alikuwa ameona idadi ya Mashahidi watendaji katika Japani imeongezeka kuwa zaidi ya 171,000.
16. Victor Bruch, Luxembourg. Alifungwa katika Buchenwald, Lublin, Auschwitz, na Ravensbrück. Akiwa na umri wa miaka 90, angali anatenda akiwa mzee wa Mashahidi wa Yehova.
17. Karl Schurstein, Ujerumani. Mwangalizi asafiriye kabla ya Hitler kupata mamlaka. Alifungwa kwa miaka minane, kisha akauawa na SS katika Dachau katika 1944. Hata ndani ya kambi, aliendelea kujenga wengine kiroho.
18. Kim Bong-nyu, Korea. Alifungwa kwa miaka sita. Akiwa na umri wa miaka 72, angali anawaambia wengine kuhusu Ufalme wa Mungu.
19. Pamfil Albu, Rumania. Baada ya kutendwa kikatili, alipelekwa kwenye kambi ya kazi ngumu katika Yugoslavia kwa miaka miwili unusu. Baada ya vita alifungwa mara mbili tena, kwa miaka mingine 12. Hakuacha kusema juu ya kusudi la Mungu. Kabla ya kifo chake alisaidia maelfu katika Rumania kutumikia pamoja na tengenezo la duniani pote la Mashahidi wa Yehova.
20. Wilhelm Scheider, Poland. Alikuwa katika kambi za mateso za Nazi katika 1939-1945. Katika magereza ya Wakomunisti katika 1950-1956, pia 1960-1964. Hadi kifo chake katika 1971, alitoa nishati zake bila kuyumbayumba katika kupiga mbiu ya Ufalme wa Mungu.
21. Harald na Elsa Abt, Poland. Wakati na baada ya vita, Harald alitumia miaka 14 gerezani na katika kambi za mateso kwa sababu ya imani yake lakini aliendelea kuhubiri huko pia. Elsa alitenganishwa na binti yao mdogo na kisha akazuiwa katika kambi sita katika Poland, Ujerumani, na Austria. Kujapokuwa na marufuku ya miaka 40 juu ya Mashahidi wa Yehova katika Poland hata baada ya vita, wote waliendelea kuwa watumishi wa Yehova wenye bidii.
22. Ádám Szinger, Hungaria. Wakati wa kusikizwa kwa kesi mara sita, alihukumiwa kifungo cha miaka 23, ambacho alitumikia miaka 8 1/2 gerezani na kambi za kazi ngumu. Alipoachiliwa, alitumikia akiwa mwangalizi asafiriye kwa jumla ya miaka 30. Yeye angali mzee wa kutaniko aliye mwaminifu-mshikamanifu akiwa na umri wa miaka 69.
23. Joseph Dos Santos, Filipino. Alikuwa ametumia miaka 12 akiwa mpiga-mbiu ya ujumbe wa Ufalme kwa wakati wote kabla ya kufungwa katika 1942. Alifufua utendaji wa Mashahidi wa Yehova katika Filipino baada ya vita na akaendelea katika utumishi wa painia hadi kifo chake katika 1983.
24. Rudolph Sunal, Marekani. Alifungwa katika Mill Point, West Virginia. Baada ya kuachiliwa alitumia wakati wote kueneza ujuzi wa Ufalme wa Mungu—akiwa painia, mshiriki wa familia ya Betheli, na mwangalizi wa mzunguko. Alikuwa angali akipainia katika 1992, akiwa na umri wa miaka 78.
25. Martin Magyarosi, Rumania. Alipotoka gerezani, katika 1942-1944, aliendelea kutoa mwelekezo kwa kazi ya kuhubiri habari njema katika Transylvania. Alipoachiliwa alisafiri mahali pengi ili kutia moyo Mashahidi wenzi katika kuhubiri kwao na yeye mwenyewe alikuwa Shahidi mwenye ujasiri. Alifungwa tena katika 1950, alikufa katika kambi ya kazi ngumu katika 1953, akiwa mtumishi mwaminifu-mshikamanifu wa Yehova.
26. R. Arthur Winkler, Ujerumani na Uholanzi. Alipelekwa kwanza katika kambi ya mateso ya Esterwegen; aliendelea kuhubiri kambini. Baadaye, katika Uholanzi, alipigwa na Gestapo hadi akawa hatambuliki. Mwishowe akapelekwa Sachsenhausen. Alikuwa Shahidi mwaminifu-mshikamanifu mwenye bidii hadi kifo chake katika 1972.
27. Park Ock-hi, Korea. Alifungwa miaka mitatu katika Gereza la Sodaemun, Seoul; aliteswa vibaya sana. Katika 1992, akiwa na umri wa miaka 91, yeye alikuwa angali akitoa ushahidi kwa bidii, akiwa painia wa pekee.
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 446]
Alexander MacGillivray, akiwa mwangalizi wa tawi la Australia, alisaidia kupanga safari za kuhubiri katika nchi na visiwa vingi
[Ramani]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
AUSTRALIA
NEW ZEALAND
TAHITI
TONGA
FIJI
NEW GUINEA
JAVA
BORNEO
SUMATRA
BURMA
HONG KONG
MALEYA
SIAM
INDOCHINA
CHINA
BAHARI YA PASIFIKI
Majina ya Mahali Ni Yale Yaliyokuwa Yakitumika Wakati wa Miaka ya 1930
[Ramani/Picha katika ukurasa wa 460]
Kufikia mwishoni-mwishoni mwa 1945, wamishonari kutoka Shule ya Gileadi walikuwa tayari wameanza utumishi katika nchi 18 katika sehemu hii ya ulimwengu
Charles na Lorene Eisenhower
Kuba
John na Adda Parker
Guatemala
Emil Van Daalen
Puerto Riko
Olaf Olson
Kolombia
Don Burt
Kosta Rika
Gladys Wilson
El Salvador
Hazel Burford
Panama
Louise Stubbs
Chile
[Ramani]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
BARBADOS
BELIZE
BOLIVIA
BRAZILI
CHILE
KOLOMBIA
KOSTA RIKA
KUBA
JAMHURI YA DOMINIKA
EL SALVADOR
GUATEMALA
HAITI
JAMAIKA
MEXICO
NIKARAGUA
PANAMA
PUERTO RIKO
URUGUAI
[Picha katika ukurasa wa 444]
Baadhi ya makolpota waliangusha vibweta vingi vya fasihi; wenye nyumba walipokea mahubiri mengi ya Biblia katika kila kitabu
[Picha katika ukurasa wa 445]
Armando Menazzi (katikati mbele) pamoja na kikundi chenye furaha kilichosafiri pamoja naye katika safari ya kuhubiri wakiwa katika “gari lililokuwa makao ya mapainia”
[Picha katika ukurasa wa 445]
Arthur Willis, Ted Sewell, na Bill Newlands—watatu waliopeleka ujumbe wa Ufalme kwenye sehemu za mashambani za Australia
[Picha katika ukurasa wa 447]
Frank Dewar (anayeonyeshwa hapa akiwa na mke wake na mabinti wao wawili) alienda Thailand katika 1936 akiwa painia peke yake na alikuwa angali painia wa pekee katika 1992
[Picha katika ukurasa wa 447]
Chomchai Inthaphan alitumia uwezo wake akiwa mtafsiri ili kufikia watu wa Thai kwa habari njema zipatikanazo katika Biblia
[Picha katika ukurasa wa 448]
Katika Ujerumani, Mashahidi wa Yehova walieneza sana hadharani barua hii iliyoandikiwa maofisa kupitia magazeti ya habari katika 1937, hata ingawa ibada yao ilikuwa chini ya marufuku ya serikali
[Picha katika ukurasa wa 449]
Familia ya Franz na Hilda Kusserow—kila mmoja wao Shahidi wa Yehova mwaminifu ingawa wote katika familia (isipokuwa mwana mmoja aliyekuwa amekufa katika aksidenti) walitiwa ndani ya kambi za mateso, magereza, au shule za kurekebishia tabia kwa sababu ya imani yao
[Picha katika ukurasa wa 450]
Wengine katika Austria na Ujerumani waliohatirisha maisha zao kwa kurudufisha au kugawanya habari yenye thamani ya funzo la Biblia, kama ile iliyoonyeshwa katika mandhari ya nyuma
Therese Schreiber
Peter Gölles
Elfriede Löhr
Albert Wandres
August Kraft
Ilse Unterdörfer
[Picha katika ukurasa wa 454]
Mashahidi kwenye mkusanyiko katika Shanghai, China, katika 1936; tisa katika kikundi hiki walibatizwa katika pindi hiyo
[Picha katika ukurasa wa 456]
Ijapokuwa marufuku juu ya kazi yao, Mashahidi hawa walifanya mkusanyiko katika Hargrave Park, karibu na Sydney, Australia, katika 1941
[Picha katika ukurasa wa 458]
Mashahidi Wakuba kwenye mkusanyiko katika Cienfuegos katika 1939
[Picha katika ukurasa wa 459]
N. H. Knorr (kushoto) kwenye mkusanyiko wa São Paulo katika 1945, Erick Kattner akiwa mkalimani