-
Mashahidi wa Yehova Ni Nani?Mnara wa Mlinzi—2015 | Septemba 1
-
-
HABARI KUU
Mashahidi wa Yehova ni nani?
“Kwa miaka mingi nimemfahamu Mike. Ni Shahidi wa Yehova. Hata hivyo nimeshindwa kuielewa dini yake. Yehova ni nani? Kwa nini Mashahidi hawasherehekei sikukuu? Je, Mike alikuwa akijihusisha na dhehebu la ajabu?”—Becky, California, Marekani.
“Jirani zangu walipoanza kujifunza Biblia na Mashahidi wa Yehova, niliwaza hivi: ‘Jina Mashahidi wa Yehova linamaanisha nini? Jina la dini hiyo ni la ajabu sana!’”—Zenon, Ontario, Kanada.
“Mimi na mke wangu tulifikiri kwamba Mashahidi wa Yehova walitutembelea kwa kuwa hatukwenda kanisani siku hiyo. Tulifikiri pia kwamba ikiwa makanisa makubwa hayakuwa na kile tulichokuwa tunatafuta, dhehebu la ajabu la Mashahidi wa Yehova halitaweza.”—Kent, Washington, Marekani.
“Kusema kweli, sikujua wao ni nani na wanaamini nini.”—Cecilie, Esbjerg, Denmark.
Huenda umewaona wakihubiri nyumba kwa nyumba au hadharani, wakitoa machapisho yanayotegemea Biblia, na kuwafundisha watu Biblia bila malipo. Huenda umepewa gazeti hili na mmoja wao. Hata hivyo, bado unajiuliza, Mashahidi wa Yehova ni nani? Huenda una maoni kama ya watu walionukuliwa mwanzoni.
Utapata wapi majibu ya maswali hayo? Utaijuaje imani ya Mashahidi wa Yehova, jinsi huduma na majumba yao ya ibada yanavyogharimiwa, na kwa nini wao hukutembelea nyumbani kwako na kukuhubiria katika maeneo ya umma?
“Nilisoma mambo mengi kuhusu Mashahidi wa Yehova katika Intaneti. Nilisikia uvumi na kuwasikiliza watu wengi wakisema vibaya kuwahusu. Matokeo ni kwamba nilianza kuwa na maoni mabaya kuhusu Mashahidi wa Yehova,” anasema Cecilie. Hata hivyo, baada ya muda fulani alizungumza na Mashahidi wa Yehova na akapata majibu yenye kuridhisha.
Je, ungependa kupata majibu sahihi ya maswali yako kuhusu Mashahidi wa Yehova? Tunakutia moyo utafute majibu sahihi kutoka kwa Mashahidi wa Yehova, wachapishaji wa gazeti hili. (Methali 14:15) Tunatumaini kwamba makala zinazofuata zitakusaidia utufahamu sisi, imani yetu, na kazi tunayofanya.
-
-
Mashahidi wa Yehova Ni Watu wa Aina Gani?Mnara wa Mlinzi—2015 | Septemba 1
-
-
HABARI KUU | MASHAHIDI WA YEHOVA NI NANI?
Mashahidi wa Yehova ni watu wa aina gani?
Sisi ni tengenezo la kimataifa lisilokuwa na uhusiano wowote na vikundi vingine vya kidini. Ijapokuwa makao yetu makuu yako Marekani, idadi kubwa ya Mashahidi wa Yehova wanaishi katika nchi tofauti-tofauti. Mashahidi zaidi ya milioni nane hivi wanawafundisha watu Biblia katika nchi zaidi ya 230. Tunatii maneno haya ya Yesu: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote.”—Mathayo 24:14.
Bila kujali tunaishi wapi, sisi hutii sheria. Hata hivyo hatuungi mkono upande wowote wa siasa. Tunafanya hivyo kwa kuwa tunafuata agizo la Yesu kwa Wakristo la ‘kutokuwa sehemu ya ulimwengu.’ Hivyo, hatuungi mkono vita au kushiriki katika siasa. (Yohana 15:19; 17:16) Katika Vita vya Pili vya Ulimwengu, Mashahidi wa Yehova walifungwa gerezani, waliteswa, na kutendewa kikatili kwa sababu walikataa kulegeza msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote. Mwanamume mmoja kutoka Ujerumani aliyewahi kuwa askofu aliandika hivi: “Wana haki ya kusema kwamba wao ndio kikundi kikubwa cha dini ambacho, kwa sababu ya dhamiri, kilikataa kujiunga na vita wakati wa utawala wa Nazi.”
“[Mashahidi wa Yehova] ni watu wenye maadili. Tungewapa watu hao wasio na ubinafsi vyeo vikubwa vya kisiasa—lakini kamwe hawawezi kukubali. . . . Wanaheshimu mamlaka za serikali lakini wanaamini kwamba Ufalme wa Mungu tu ndio utakaoondoa matatizo yote ya mwanadamu.”—Gazeti la Nová Svoboda, Jamhuri ya Cheki.
Hata hivyo, hatujitengi na watu. Yesu alisali hivi kwa Mungu kuhusu wafuasi wake: “Ninakuomba, si kwamba uwatoe ulimwenguni.” (Yohana 17:15) Hivyo, huenda ukatuona tukifanya kazi, tukinunua bidhaa, na tukienda shule.
-
-
Mashahidi wa Yehova Wanaamini Nini?Mnara wa Mlinzi—2015 | Septemba 1
-
-
HABARI KUU | MASHAHIDI WA YEHOVA NI NANI?
Mashahidi wa Yehova wanaamini nini?
Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba “andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida.” (2 Timotheo 3:16) Tunatumia Biblia kujifunza kuhusu Muumba na inatusaidia kuishi maisha yenye kusudi.
Biblia inasema hivi: “Ili watu wajue kwamba wewe, ambaye jina lako ni Yehova, wewe peke yako ndiye Uliye Juu Zaidi, juu ya dunia yote.” (Zaburi 83:18) Hivyo, sisi tunamwabudu Yehova Mungu peke yake na tukiwa Mashahidi wake tunajitahidi kuwaambia wengine kuhusu jina lake.—Isaya 43:10-12.
Tukiwa Wakristo, tunaamini kwamba Yesu, “Mwana wa Mungu,”a alikuja duniani na kisha akawa Masihi. (Yohana 1:34, 41; 4:25, 26) Baada ya kufa, alifufuliwa na kwenda mbinguni. (1 Wakorintho 15:3, 4) Baadaye, akawa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. (Ufunuo 11:15) Ufalme huo ni serikali halisi itakayoleta Paradiso tena. (Danieli 2:44) Biblia inasema hivi: “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:11, 29.
“Wanapoisoma Biblia, wanaamini kwamba Mungu anazungumza nao. Kila mara wanapopata matatizo katika maisha yao, wao huchunguza Neno la Mungu ili kupata suluhisho. . . . Wanaamini kwamba Neno la Mungu bado liko hai.”—Kasisi Mkatoliki Benjamin Cherayath, gazeti la Münsterländische Volkszeitung, Ujerumani
Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba kanuni za Biblia zinaweza kuwanufaisha watu leo. (Isaya 48:17, 18) Hivyo, sisi hujitahidi sana kufuata kanuni hizo. Kwa mfano, sisi hatuvuti sigara au kutumia dawa za kulevya kwa sababu Biblia inasema tunapaswa kuepuka matendo yanayochafua akili na miili yetu. (2 Wakorintho 7:1) Pia, tunaepuka matendo yanayoshutumiwa na Biblia kama vile ulevi, uasherati, na wizi.—1 Wakorintho 6:9-11.
a Pia, Biblia inamtaja Yesu kuwa “Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu” kwa sababu ni yeye peke yake aliyeumbwa moja kwa moja na Yehova.—Yohana 3:18; Wakolosai 1:13-15.
-
-
Kazi Yetu Inagharimiwaje?Mnara wa Mlinzi—2015 | Septemba 1
-
-
HABARI KUU | MASHAHIDI WA YEHOVA NI NANI?
Kazi yetu inagharimiwaje?
Kila mwaka, tunachapisha na kugawanya mamilioni ya Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia. Tunajenga na kuendesha viwanda vya uchapishaji na ofisi za tawi ulimwenguni pote. Makutaniko mengi hukutana katika nyumba za ibada zinazoitwa Majumba ya Ufalme. Ni nani hulipia gharama hizo?
Kazi yetu hutegemezwa kwa michango ya hiari. (2 Wakorintho 9:7) Katika mwaka wa 1879, toleo la pili la gazeti hili lilisema hivi: “Tunaamini kwamba gazeti ‘Zion’s Watch Tower’ [kama lilivyokuwa likiitwa gazeti hili wakati huo] linategemezwa na YEHOVA, na maadamu hivyo ndivyo ilivyo halitawaomba watu wala kuwasihi kamwe walitegemeze.” Bado tunaendelea na sera hiyo.
Michango hutumwa moja kwa moja katika mojawapo ya ofisi zetu za tawi au huwekwa katika sanduku la michango linalopatikana katika kila Jumba la Ufalme. Hata hivyo, hatutoi sehemu ya kumi, hatuchukui sadaka, au kulipisha watu kwa ajili ya huduma zetu au machapisho yetu. Hatulipwi pesa kwa sababu ya kazi ya kuhubiri, kufundisha katika kutaniko, au kusaidia kujenga majengo ya ibada. Yesu alisema hivi: “Mlipokea bure, toeni bure.” (Mathayo 10:8) Watumishi wote wanaofanya kazi katika ofisi za tawi na katika makao makuu, kutia ndani Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova, ni washiriki wa kikundi cha kidini wasiolipwa mshahara.
“Kama ilivyo katika utendaji wowote wa Mashahidi wa Yehova, shughuli za dini yao huendeshwa kwa michango ya hiari na kila mtu anaamua kiasi na kadiri atakavyotoa ‘michango’ yake.’”—Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu, 2011
Michango hutumiwa pia kusaidia wakati wa majanga ya asili. Wakristo wa mapema walifurahia kuwasaidia ndugu zao waliopatwa na matatizo. (Waroma 15:26) Sisi pia huwasaidia wale waliopatwa na maafa kwa kujenga tena nyumba zao na nyumba za ibada, kwa kuwapatia chakula, mavazi, na matibabu.
-
-
Kwa Nini Tunahubiri?Mnara wa Mlinzi—2015 | Septemba 1
-
-
HABARI KUU | MASHAHIDI WA YEHOVA NI NANI?
Kwa nini tunahubiri?
Tunatambuliwa sana kutokana na kazi yetu ya kuhubiri inayofanywa ulimwenguni pote katika nyumba za watu, hadharani, na popote ambapo watu wanapatikana. Kwa nini tunahubiri?
Mashahidi wa Yehova wanahubiri ili kumtukuza Mungu na kuwaambia watu jina lake. (Waebrania 13:15) Pia, tunamtii Kristo Yesu aliyeagiza hivi: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, . . . na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi.”—Mathayo 28:19, 20.
Zaidi ya hilo, tunahubiri kwa sababu tunawapenda jirani zetu. (Mathayo 22:39) Tunajua kwamba watu wengi wana imani zao na kwamba si kila mtu anapenda ujumbe wetu. Hata hivyo, tunaamini kwamba mafundisho ya Biblia yanaokoa uhai. Ndio maana tunaendelea “bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema juu ya Kristo,” kama walivyofanya Wakristo wa karne ya kwanza.—Matendo 5:41, 42.
Mtaalamu wa elimu ya jamii, Antonio Cova Maduro aliandika kuhusu “jitihada nyingi sana ambazo Mashahidi wa Yehova wanafanya . . . , ili neno takatifu lifike maeneo ya mbali zaidi duniani.”—Gazeti la Venezuela linaloitwa El Universal
Wasomaji wengi wa machapisho yetu si Mashahidi wa Yehova. Na watu wengi tunaowafundisha Biblia ni waumini wa dini nyingine. Hata hivyo, wanathamini Mashahidi wa Yehova wanapowatembelea.
Bila shaka, huenda ukawa na maswali mengine kuhusu Mashahidi wa Yehova. Tunakutia moyo utafute majibu ya maswali hayo kwa
Kumuuliza Shahidi wa Yehova.
Kutembelea tovuti yetu ya www.jw.org/sw.
Kuhudhuria mikutano yetu ambayo haina kiingilio na kila mtu anaalikwa.
-