-
Mungu Ana Maoni Gani Kuhusu Vita?Mnara wa Mlinzi—2015 | Novemba 1
-
-
HABARI KUU
Mungu Ana Maoni Gani Kuhusu Vita?
Ungejibuje swali hilo? Wengi hufikiri kwamba Mungu huunga mkono vita. Wanasema kwamba aliwaamuru baadhi ya watumishi wake wa zamani wapigane vita; Biblia inathibitisha jambo hilo. Hata hivyo, wengine wanajua kwamba Yesu, Mwana wa Mungu, aliwafundisha wafuasi wake wawapende adui zao. (Mathayo 5: 43, 44) Kwa hiyo wanadai kwamba maoni ya Mungu kuhusu vita yamebadilika na sasa anachukia vita.
Unaonaje? Je, Mungu anaunga mkono vita? Ikiwa ni hivyo, anaunga mkono upande gani katika mizozano inayoendelea ulimwenguni? Majibu ya maswali hayo yatakusaidia uchunguze maoni yako kuhusu vita. Kwa mfano, ukijua kwamba Mungu anapenda vita na anaunga mkono upande unaopenda katika vita, huenda ukahisi vizuri na ukawa na uhakika kwamba mtashinda. Kwa upande mwingine, ungehisije ukijua kwamba Mungu anaunga mkono wapinzani wenu? Huenda ungefikiria kwa makini kuhusu msimamo wako.
Kuna jambo muhimu la kuzingatia. Kujua maoni ya Mungu kuhusu vita huenda kukabadili maoni yako kumhusu Mungu. Ikiwa wewe ni miongoni mwa watu wengi ambao wameteseka kwa sababu ya vita, huenda ungependa kupata jibu la swali, Je, Mungu anachochea watu wapigane ili wengine wateseke, au labda anakaa tu na hawajali wale wanaokandamizwa?
Huenda ukashangaa kujifunza kwamba jibu la Biblia linatofautiana sana na maoni hayo. Isitoshe, tangu zamani mpaka sasa maoni ya Mungu kuhusu vita hayajabadilika. Acheni tuone Biblia inasema nini kuhusu jinsi Mungu alivyoona vita katika nyakati za kale na katika karne ya kwanza Yesu alipokuwa duniani. Jambo hilo litatusaidia tujue jinsi Mungu anavyoona vita leo na ikiwa vita vitakwisha.
-
-
Maoni ya Mungu Kuhusu Vita Katika Nyakati za KaleMnara wa Mlinzi—2015 | Novemba 1
-
-
HABARI KUU | MUNGU ANA MAONI GANI KUHUSU VITA?
Maoni ya Mungu Kuhusu Vita Katika Nyakati za Kale
Watu walikuwa wakiteswa. Walisali mara nyingi kwa Mungu ili awasaidie, lakini hawakupata msaada. Watu hao walikuwa Waisraeli, watu wa Mungu katika nyakati za kale. Walikandamizwa na taifa lenye nguvu la Misri. (Kutoka 1:13, 14) Kwa miaka mingi, Waisraeli walisubiri Mungu awaondolee utawala wa mabavu wa Misri. Hatimaye, wakati wa Mungu kuchukua hatua uliwadia. (Kutoka 3:7-10) Biblia inaeleza kwamba Mungu alipigana vita na Wamisri. Aliwapiga Wamisri kwa mapigo kumi yenye kuangamiza, na kisha akamuua mfalme wa Misri na jeshi lake kwenye Bahari Nyekundu. (Zaburi 136:15) Yehova Mungu akathibitika kuwa “mtu wa vita” kwa ajili ya watu wake.—Kutoka 15:3, 4.
Kitendo cha Mungu kupigana vita na Wamisri kinaonyesha kwamba hapingi kila vita. Nyakati nyingine, aliwaruhusu Waisraeli wapigane vita. Mathalani, aliwaamuru wapigane vita na Wakanaani waliokuwa waovu sana. (Kumbukumbu la Torati 9:5; 20:17, 18) Alimwagiza Mfalme Daudi apigane vita na Wafilisti waliokuwa wakandamizaji. Hata alimpa Daudi mbinu za kupigana ambazo zingemsaidia ashinde.—2 Samweli 5:17-25.
Masimulizi hayo ya Biblia yanaonyesha kuwa Waisraeli walipokuwa katika hatari ya kuonewa au kutendewa uovu, Mungu aliruhusu vita ili kulinda watu wake na ibada ya kweli. Lakini ona mambo matatu yafuatayo yanayohusu vita hivyo vilivyokubaliwa na Mungu.
MUNGU NDIYE ALIYEAMUA NANI ANGEPIGANA VITA. Pindi moja, Mungu aliwaambia Waisraeli: “Hamtahitaji kupigana katika kisa hiki.” Kwa nini? Kwa sababu Mungu angepigana vita kwa niaba yao. (2 Mambo ya Nyakati 20:17; 32:7, 8) Alifanya hivyo mara nyingi, kama katika kisa kilichotajwa mwanzoni mwa makala hii. Nyakati nyingine, Mungu aliwaamuru watu wake katika Israeli la kale wapigane vita ambavyo aliruhusu, yaani, vile ambavyo vilihusisha kuchukua na kulinda Nchi yao ya Ahadi.—Kumbukumbu la Torati 7:1, 2; Yoshua 10:40.
MUNGU NDIYE ALIYEAMUA LINI VITA HIVYO VINGEPIGANWA. Watumishi wa Mungu walihitaji kusubiri hadi wakati ambapo Mungu aliwaruhusu wakapigane vita ili kuondoa ukandamizaji na uovu uliowazunguka. Hawakupaswa kupigana kabla ya wakati huo kufika. Walipoamua kupigana bila ruhusa, walikosa kibali cha Mungu. Isitoshe, Biblia inaonyesha kwamba Waisraeli walipoamua kupigana vita bila kuruhusiwa na Mungu, matokeo yalikuwa mabaya.a
Ingawa Mungu alipigana na Wakanaani, hakuwaangamiza baadhi yao kama vile Rahabu na familia yake
MUNGU HAPENDI WANADAMU WAFE HATA KAMA NI WAOVU. Yehova Mungu ni chanzo cha uhai na Muumba wa wanadamu. (Zaburi 36:9) Kwa hiyo, hapendi kuona watu wakifa. Hata hivyo, kwa kusikitisha kuna watu hupanga kuwatesa na hata kuwaua wenzao. (Zaburi 37:12, 14) Ili kukomesha uovu huo, nyakati fulani Mungu huruhusu vita vipiganwe dhidi ya waovu. Pamoja na hayo, miaka yote ambayo aliwaruhusu Waisraeli wapigane, aliendelea kuwa mwenye “rehema” na hakuwa “mwepesi wa hasira” kuelekea wale waliowakandamiza Waisraeli. (Zaburi 86:15) Kwa mfano, aliagiza kwamba kabla Waisraeli hawajavamia jiji, walipaswa ‘kulitangazia masharti ya amani,’ ili kuwapa wakazi wa jiji hilo fursa ya kubadili njia zao na kuepuka vita. (Kumbukumbu la Torati 20:10-13) Kwa kufanya hivyo, Mungu alionyesha ‘anapendezwa, si na kifo cha mwovu, bali kwamba mtu mwovu ageuke na kuiacha njia yake na kwa kweli aendelee kuishi.’—Ezekieli 33:11, 14-16.b
Kutokana na mambo tuliyochunguza tumeona kwamba katika nyakati za kale, Mungu aliona vita kuwa njia halali ya kukomesha uonevu na uovu. Lakini, Mungu—wala si wanadamu—ndiye aliyeamua wakati na wale ambao wangepigana vita. Je, Mungu alifurahia kupigana vita ili aone umwagaji wa damu? Hapana. Kwa kweli, anachukia jeuri. (Zaburi 11:5) Je, maoni ya Mungu kuhusu vita yalibadilika Mwana wake, Yesu Kristo, alipoanza huduma yake katika karne ya kwanza?
a Kwa mfano, nyakati fulani, Waisraeli walishindwa vita walipoamua kupigana na Waamaleki na Wakanaani baada ya Mungu kuwakataza kufanya hivyo. (Hesabu 14:41-45) Miaka mingi baadaye, Mfalme Yosia mwaminifu alipigana vita bila ruhusa ya Mungu na uamuzi huo ulimfanya apoteze uhai wake.—2 Mambo ya Nyakati 35:20-24.
b Waisraeli hawakuwatangazia Wakanaani masharti ya amani kabla ya kupigana nao. Kwa nini? Kwa sababu Wakanaani walipewa miaka 400 ya kurekebisha matendo yao maovu. Kufikia wakati ambapo Waisraeli walipigana nao, Wakanaani walikuwa waovu sana. (Mwanzo 15:13-16) Hivyo, walipaswa kuangamizwa kabisa. Hata hivyo, Wakanaani waliobadilika waliokolewa.—Yoshua 6:25; 9:3-27.
-
-
Maoni ya Mungu Kuhusu Vita Katika Karne ya KwanzaMnara wa Mlinzi—2015 | Novemba 1
-
-
HABARI KUU | MUNGU ANA MAONI GANI KUHUSU VITA?
Maoni ya Mungu Kuhusu Vita Katika Karne ya Kwanza
Watu walinyanyaswa. Kama mababu zao, Wayahudi wa karne ya kwanza walimwomba Mungu mara nyingi awakomboe kutoka katika Milki ya Roma iliyokuwa ikiwakandamiza. Kisha wakasikia kumhusu Yesu. Je, ndiye Masihi aliyeahidiwa? Si ajabu, watu wengi ‘walitumaini kwamba mtu huyo ndiye angekomboa Israeli’ kutoka kwa Waroma wakandamizaji. (Luka 24:21) Lakini hawakupata msaada. Badala yake, katika mwaka wa 70 W.K., majeshi ya Roma yalikuja na kuharibu Yerusalemu na hekalu lake.
Ni nini kilichotokea? Kwa nini Mungu hakuwapigania Wayahudi kama alivyofanya wakati uliopita? Au kwa nini hakuwaruhusu wapigane vita ili kujikomboa kutoka kwa wale wanaowakandamiza? Je, maoni ya Mungu kuhusu vita yalibadilika? Hapana. Lakini mtazamo wa Wayahudi ulibadilika. Walimkataa Mwana wa Mungu, Yesu, kuwa Masihi. (Matendo 2:36) Kwa hiyo, wakiwa taifa walipoteza uhusiano wao wa pekee na Mungu.—Mathayo 23:37, 38.
Mungu aliacha kuwalinda Wayahudi na Nchi yao ya Ahadi hivyo wasingeweza tena kudai kwamba wanapigana vita kwa msaada wa Mungu. Kama Yesu alivyotabiri, baraka zilizotokana na kupata kibali cha Mungu ziliondolewa kutoka katika taifa la asili la Israeli na kupewa taifa jipya, taifa la kiroho, ambalo baadaye Biblia ililiita kuwa “Israeli wa Mungu.” (Wagalatia 6:16; Mathayo 21:43) Kutaniko la Wakristo watiwa-mafuta lilithibitika kuwa Israeli wa kiroho wa Mungu. Waliambiwa hivi katika karne ya kwanza: “Sasa ninyi ni watu wa Mungu.”—1 Petro 2:9, 10.
Kwa kuwa Wakristo wa karne ya kwanza walikuwa “watu wa Mungu,” je, Mungu alipigana kwa niaba yao, ili kuwakomboa kutoka kwa Waroma wakandamizaji? Au je, Mungu aliwaruhusu wapigane na wale waliokuwa wakiwakandamiza? Hapana, hakufanya hivyo. Kwa nini? Katika vita ambavyo Mungu ameruhusu, Mungu pekee ndiye anayeamua lini vita hivyo vipiganwe, kama makala iliyopita ilivyoonyesha. Mungu hakupigana vita kwa ajili ya Wakristo wa karne ya kwanza wala hakuwaruhusu wapigane vita. Ni wazi kwamba, karne ya kwanza haukuwa wakati wa Mungu kupigana ili kukomesha uovu na uonevu.
Hivyo, kama watumishi wa Mungu wa nyakati za kale, Wakristo hao wa karne ya kwanza walihitaji kusubiri mpaka wakati wa Mungu wa kukomesha uovu na ukandamizaji ufike. Kabla kufika kwa wakati huo, hawakuruhusiwa na Mungu kupigana na maadui zao. Yesu Kristo alionyesha wazi jambo hilo katika mafundisho yake. Kwa mfano, hakuwaagiza wafuasi wake kupigana vita badala yake aliwaambia: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa.” (Mathayo 5:44) Akitabiri kuhusu wakati ambapo jiji la Yerusalemu la karne ya kwanza lingevamiwa na majeshi ya Roma, Yesu hakuwaagiza wafuasi wake wabaki na kupigana bali aliwaambia wakimbie, nao walifanya hivyo.—Luka 21:20, 21.
Pia, mtume Paulo akiongozwa na roho ya Mungu aliandika hivi: “Msijilipizie kisasi, . . . kwa maana imeandikwa: ‘Kisasi ni changu; mimi nitalipa,’ asema Yehova.” (Waroma 12:19) Paulo alikuwa akinukuu jambo alilosema Mungu karne nyingi mapema kama ilivyoandikwa katika Mambo ya Walawi 19:18 na Kumbukumbu la Torati 32:35. Kama ilivyoonyeshwa katika makala iliyotangulia, njia moja ambayo Mungu aliwalipizia kisasi watu wake katika nyakati za kale ilikuwa ni kwa kuwasaidia walipopigana vita na maadui zao. Hivyo maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba maoni ya Mungu kuhusu vita hayajabadilika. Hata katika karne ya kwanza, bado Mungu aliona vita kama njia halali ya kuwalipizia kisasi watumishi wake na kukomesha uovu na ukandamizaji. Hata hivyo, kama ilivyokuwa wakati uliopita, Mungu pekee ndiye anayeamua lini vita vingepiganwa na nani ambaye angepigana vita hivyo.
Hivyo, ni wazi kwamba Mungu hakuwaruhusu Wakristo katika karne ya kwanza wapigane vita. Vipi wakati huu? Je, Mungu ameruhusu kikundi fulani cha watu kipigane vita? Au, je, huu ni wakati wa Mungu kuingilia kati na kupigana vita kwa niaba ya watumishi wake? Mungu ana maoni kuhusu vita vinavyopiganwa leo? Majibu ya maswali hayo yanapatikana katika makala ya mwisho ya mfululizo huu.
-
-
Maoni ya Mungu Kuhusu Vita LeoMnara wa Mlinzi—2015 | Novemba 1
-
-
HABARI KUU | MUNGU ANA MAONI GANI KUHUSU VITA?
Maoni ya Mungu Kuhusu Vita Leo
Watu wengi leo wanakandamizwa. Wengi wao wanamwomba Mungu kila siku awasaidie na wanajiuliza ikiwa kweli atawasaidia. Je, Mungu anasikia vilio vyao vya kuomba msaada? Vipi kuhusu wale wanaopigana vita ili kuondoa ukandamizaji? Je, Mungu anaunga mkono jitihada zao na kuona vita vyao kuwa halali?
Har–Magedoni itakomesha vita vyote
Kwanza kabisa, utafarijika ukijua ukweli huu: Mungu anayaona mateso yote wanayokabili watu ulimwenguni na anapanga kuchukua hatua. (Zaburi 72:13, 14) Katika Neno lake, Biblia, Mungu ametoa ahadi kwamba wale wote ‘wanaopata dhiki, watapata kitulizo.’ Wakati gani? “Wakati wa ufunuo wa Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika zake wenye nguvu . . . anapoleta kisasi juu ya wale wasiomjua Mungu na wale wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu.” (2 Wathesalonike 1:7, 8) Ufunuo huo wa Yesu utatimizwa wakati ujao unaoitwa na Biblia kuwa “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote,” au Har–Magedoni.—Ufunuo 16:14, 16.
Katika vita hivyo vya wakati ujao, Mungu hatatumia wanadamu kupigana vita na waovu bali atamtumia Mwana wake, Yesu Kristo, pamoja na viumbe wa roho wenye nguvu. Jeshi hilo la mbinguni litakomesha ukandamizaji wote.—Isaya 11:4; Ufunuo 19:11-16.
Mpaka sasa, maoni ya Mungu kuhusu vita hayajabadilika. Bado anaona vita kuwa njia halali ya kukomesha ukandamizaji na uovu. Hata hivyo, kama historia inavyoonyesha, Mungu pekee ndiye mwenye haki ya kuamua wakati na wale watakaopigana vita. Kama tulivyoona, Mungu amepanga kwamba vita vya kukomesha uovu na kulipiza kisasi kwa wapinzani wake vipiganwe wakati ujao na Mwana wake, Yesu Kristo. Hilo linamaanisha kwamba Mungu haungi mkono vita vinavyoendelea duniani leo hata kama kuna sababu nzuri ya kupigana.
Kwa mfano: Fikiria watoto wawili wanaoanza kupigana baada ya baba yao kuondoka nyumbani. Wanaacha kupigana kwa muda mfupi na kumpigia simu baba yao. Mtoto mmoja analalamika kuwa mwenzake ndiye chanzo cha ugomvi na yule mwingine anadai kwamba ameonewa. Wote wawili wanapeleka malalamiko kwa baba yao na kila mmoja anatumaini ataungwa mkono. Hata hivyo, baada ya kuwasikiliza, baba yao anawaambia waache kupigana na wamsubiri arudi ili atatue tatizo hilo. Watoto hao wanasubiri kwa muda fulani. Lakini baada ya muda mfupi wanaanza kupigana tena. Baba yao anaporudi anawaadhibu wote wawili kwa sababu hawakutii.
Mara nyingi mataifa yanapopigana humwomba Mungu awasaidie. Lakini Mungu haungi mkono upande wowote wa mapigano hayo. Badala yake, katika Neno lake, Biblia, anaeleza waziwazi kwamba: “Msimlipe yeyote uovu kwa uovu,” na “Msijilipizie kisasi wenyewe.” (Waroma 12:17, 19) Zaidi ya hayo, ameonyesha kwamba wanadamu wanapaswa “kumngojea kwa kutamani” ili achukue hatua, naye atafanya hivyo katika vita vya Har–Magedoni. (Zaburi 37:7) Mungu hukasirika sana mataifa yanaposhindwa kumngojea na kuonyesha kimbelembele kwa kuamua kupigana. Hivyo, katika Har–Magedoni, Mungu ataonyesha hasira yake na kumaliza migogoro yote ya mataifa kwa ‘kukomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.’ (Zaburi 46:9; Isaya 34:2) Kwa kweli, vita vya Har–Magedoni vitakomesha vita vyote.
Kukomeshwa kwa vita ni mojawapo ya baraka nyingi za Ufalme wa Mungu. Alipokuwa akizungumzia serikali hiyo katika sala hii inayojulikana sana, Yesu alisema hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Ufalme wa Mungu hautakomesha vita tu, bali pia utakomesha chanzo cha vita yaani uovu.a (Zaburi 37:9, 10, 14, 15) Ndiyo sababu wafuasi wa Yesu walitazamia kwa hamu baraka za Ufalme wa Mungu.—2 Petro 3:13.
Hata hivyo, tutasubiri Ufalme wa Mungu kwa muda gani hadi utakapokuja kukomesha mateso, ukandamizaji, na uovu? Utimizo wa unabii mwingi wa Biblia unaonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho” za mfumo huu wa mambo. (2 Timotheo 3:1-5)b Hivi karibuni, Ufalme wa Mungu utakomesha siku hizi za mwisho kwa vita vya Har–Magedoni.
Kama ilivyotajwa mwanzoni, wale “wasiotii habari njema juu ya Bwana wetu Yesu” wataangamizwa katika vita hiyo ya mwisho. (2 Wathesalonike 1:8) Lakini kumbuka, Mungu hapendezwi na kifo cha mtu yeyote, kutia ndani waovu. (Ezekieli 33:11) Kwa kuwa “hataki yeyote aangamizwe” katika vita hiyo ya mwisho, anahakikisha kwamba habari njema kumhusu Bwana wetu Yesu ‘inahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote’ kabla ya mwisho kuja. (2 Petro 3:8, 9; Mathayo 24:14; 1 Timotheo 2:3, 4) Naam, kupitia kazi ya kuhubiri inayofanywa ulimwenguni pote na Mashahidi wa Yehova, watu wanapata fursa ya kumjua Mungu, kutii habari njema kumhusu Yesu, na kutarajia kuishi wakati ambapo vita havitakuwapo tena.
a Ufalme wa Mungu utakomesha kifo ambacho ni adui ya wanadamu. Kama ilivyoelezwa katika makala “Majibu ya Maswali ya Biblia” ya toleo hili, Mungu atawafufua watu wengi, kutia ndani wale waliouawa kwa sababu ya vita.
b Ili kupata habari zaidi kuhusu siku za mwisho, soma sura ya 9 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
-