Kutangaza Habari Njema—Kwa Kutoa Maandikisho kwa Ujasiri
1 Mnara wa Mlinzi bila shaka ndilo gazeti bora zaidi la kujifunza Biblia usoni pa dunia! Je! wewe unasadiki hiyo ni kweli? Ikiwa ndivyo, je! kila mtu hapaswi kupewa fursa ya kuliandikisha?
2 Wewe binafsi umesaidiwaje kwa kusoma Mnara wa Mlinzi? Yaelekea sisi sote tungeweza kusimulia njia ambazo gazeti hilo limetusaidia. Huenda wengine wakasema limekuwa njia ya msingi ya kutufanya chonjo juu ya umaana wa nyakati tunamoishi. Au limetuwezesha tujifunze maana ya kweli ya “ishara za nyakati” zinazovuruga aina-binadamu leo. (Mt. 16:3, NW) Wengine wangesema kwamba wamefarijiwa na habari njema kwamba Ufalme wa Mungu karibuni utaangamiza wale wanaoonea wanadamu wenzao. Mnara wa Mlinzi umetetea wazo hilo tangu mwanzo walo miaka zaidi ya 110 iliyopita. Bila shaka sisi sote tungesema kwamba jarida hilo la kutokeza la Biblia limetusaidia kujenga imani katika uandalizi wa ukombozi unaowapa binadamu wasiokamilika fursa ya kupata uhai wa milele. Wengine wanahitaji kujifunza kweli hizo.
UWE CHANYA KATIKA MAONI YAKO
3 Hekima ya Mungu na wala si kusababu kwa kibinadamu ndiyo inakaziwa katika Mnara wa Mlinzi. (Isa. 55:8, 9) Hekima hiyo inahitajiwa sana na kila mtu leo. Inaweza kufanya maisha yawe bora zaidi na kusaidia kusitawisha nia zinazofaa. Hilo ni la lazima ili ‘kuendelea kuishi.’ (Mit. 9:1-6, NW) Tukiwa tumesadikishwa hivyo, tutatoa andikisho hilo na mtazamo chanya, tukitambua kwamba tuna ambacho wengine wanahitaji. Kwa uangalifu chunguza kila toleo ili kupata taarifa ambazo unaamini zaweza kuwasaidia wenye nyumba. Matayarisho hayo ya kimbele yatakusaidia kuonyesha roho chanya wakati wa kuyatoa magazeti haya katika huduma.
4 Huenda wengine wakaelekea kuwa hasi (wenye maoni yasiyofaa) juu ya kutoa maandikisho. Huenda wakamwingiza mwenye nyumba katika mazungumzo, hata kuongea juu ya Kichwa cha Mazungumzo, halafu kutoa magazeti mawili badala ya kutoa andikisho. Kwa nini? Ni gharama? Ikiwa ndivyo, huko si kuwaza kuzuri. Ingawa gharama ya andikisho ni ya chini ikilinganishwa na vichapo vya kilimwengu, inapolinganishwa na thamani yake kwa msomaji bei yake haipimiki. Kwa hiyo uwe chanya na kutoa andikisho la Mnara wa Mlinzi au kuutoa pamoja na jenzile Amkeni!
5 Dada mmoja aliazimia kuangusha maandikisho, kwa maana aliweka mradi wa 50 kwa kipindi cha miezi miwili. Alipata maandikisho 31 mwezi wa kwanza na jumla ya 50 kwa kipindi hicho cha miezi miwili. Alisema kwamba wakati wengine hawakuwa na hela lakini walitaka andikisho, alirudi safari tatu au nne kabla mwenye nyumba hajaweza kukusanya hela hizo. (yb89, kur. 60-1; ona pia 1990 Yearbook, kurasa 47-9) Katika Japani, ambako gharama ya ada ya kuandikisha ni sawa kama dola 14 za Kimarekani, akina ndugu waliangusha maandikisho zaidi ya 71,600 katika Oktoba, kilele kipya na ongezeko la asilimia 57 zaidi ya mwezi uo huo mwaka mmoja uliopita.
ENDELEA KWA UJASIRI
6 Tuna kila sababu ya kuwa wajasiri katika huduma yetu—tuna tegemezo la Yehova. (Mdo. 14:3) Kimoja cha vyombo vikuu ambavyo Yehova anatumia kueneza habari njema leo ni Mnara wa Mlinzi. Tukiangusha maandikisho na halafu kufuatia kwa kitia-moyo cha kusoma magazeti hayo, jitihada yetu ya bidii huenda ikaokoa maisha za watu. Kwa hiyo na tutoe maandikisho kwa idili na kwa bidii kwa wote tunaowajua na kwa wale tunaowakuta katika huduma ya shambani.