Njoni Kwenye “Lugha Iliyo Safi” Mkusanyiko wa Wilaya wa 1990
1 Mikusanyiko ya wilaya ya 1990 itakuwa na kichwa “Lugha Iliyo Safi,” nawe umealikwa kuhudhuria. Katika Afrika Mashariki mikusanyiko 10 imeratibiwa. Itaanza Novemba 1 na itamalizika mwishoni mwa Desemba.
2 Neno la kiunabii la Yehova kwenye Sefania 3:9 husema: “Maana hapo ndipo nitakapowarudishia mataifa lugha iliyo safi, wapate kuliitia jina la BWANA [Yehova, NW], wamtumikie kwa nia moja.” Mkusanyiko mwaka huu si kwamba tu utatambulisha hiyo “lugha iliyo safi” ni nini bali pia utatusaidia tuthamini kwa nini kujifunza hiyo na kuinena kwa ufasaha ni muhimu na jinsi uwezo wetu wa kuitumia huimarisha umoja wa udugu wa ulimwenguni pote.
3 WASILI MAPEMA: Tengenezo la Yehova linatualika tujilishe kwenye meza yake ya kiroho. Ni ishara ya staha na uthamini kuwasili kwa wakati. Kwa kweli, hiyo yamaanisha kwamba twapaswa kuwasili kila siku mapema na tuwe tumeketi kabla ya programu kuanza. Hiyo hutaka kuruhusu wakati wa kutosha kushughulikia mambo yanayohitaji kuangaliwa, kutia ndani kutafuta viti vinavyofaa kwa ajili ya familia yetu.—1 Kor. 14:40.
4 Wajumbe kwenye mikusanyiko ya Polandi mwaka jana walivutwa na ujitoaji kimungu, upendo, na umoja wa ndugu zao. Uthamini wenye kina kwa maandalizi ya kiroho ambayo yangeletwa na mkusanyiko yalikuwa wazi. Kila asubuhi, akina ndugu walikuwa kwenye mahali pa mkusanyiko mapema, wameketi na tayari kwa ajili ya wimbo na sala ya kufungua. Walibaki kwa ajili ya wimbo na sala ya kufunga, nao walikaa-kaa baada ya programu ili wapate ushirika pamoja na ndugu zao.
5 Utaratibu wa akina ndugu ulikuwa kielelezo kizuri. Walikuwa wamekuja kusikiliza na kujifunza. Hata mvua iliyokunya kwenye stediamu zilizo wazi katika Poznani na Chorzow haingeweza kukengeusha usikilizaji wao kutoka kwenye proramu. Wale wachanga zaidi waliokuwapo, kutia na watoto wachanga, walikuwa na nidhamu nzuri, wenye kimya, na wenye kusikiliza programu. Familia ziliketi pamoja. Walikuwa kielelezo kizuri katika kuonyesha staha yao yenye kina kwa ajili ya meza ya Yehova. Tunaweza kufaidikaje na kielelezo chao?
6 Ni jambo la Kimaandiko kuiga vielelezo vizuri vya wengine. (2 The. 3:7) Ingawa hali zetu za kibinafsi zaweza zikawa tofauti, sisi pia twataka kupata faida zote kutokana na mikusanyiko yetu. Ili kuzuia wasiwasi na mitamauko kwa sababu ya kuanza safari ya kuja kwenye mkusanyiko tukiwa tumechelewa, baadhi ya familia hulipata kuwa jambo lenye kunufaisha kuweka wakati wenye kupatana na akili nzuri wa kwenda kulala. Kwa kushikamana kabisa na ratiba, wanakuwa na uwezekano zaidi wa kupata usingizi mzuri usiku na kuwa tayari kwa ajili ya kuanza mapema kesho yake. Hilo huwaepusha kuwasili wakati programu inaendelea, jambo ambalo hukengeusha fikiria na laweza kuudhi wale ambao tayari wameketi. Ufikirio wetu katika habari hii ni wonyesho wa kicho na staha yetu kwa Yehova na upendo wetu na ufikirio kwa ndugu zetu.
7 MKUSANYIKO WA SIKU NNE: “Lugha Iliyo Safi” Mkusanyiko wa Wilaya utakuwa wa siku nne. Utaanza Alhamisi saa 7:30 alasiri na utamalizika saa 11:10 hivi alasiri Alhamisi, Ijumaa, na Jumamosi, na saa 10:00 alasiri Jumapili. Ijumaa hadi Jumapili programu itaanza saa 3:30 asubuhi. Kila siku itajawa na habari muhimu inayohusiana na kunena lugha iliyo safi. Kutakuwako hotuba, maonyesho, maono, hotuba mfululizo, na drama mbili.
8 Lifanye kuwa azimio lako kutokosa hata kipindi kimoja. Huenda hilo likataka dhabihu za kibinafsi na marekebisho katika ratiba yako. Huenda wengine wakaliona kuwa jambo linalohitajiwa kabisa kufanya mipango ya pekee na waajiri-kazi wao. Wengi hata huachilia manufaa za kifedha ili kuhudhuria vipindi vyote. Hata hivyo, fikiria yale ndugu zetu walidhabihu na kupatwa nayo ili wahudhurie mikusanyiko katika Polandi mwaka jana. Je! hilo halikuchochei zaidi uwepo kwenye mkusanyiko wenu kwa ajili ya kila kipindi? Bila shaka Yehova atabariki wale wanaofanya jambo hilo kuwa jambo la sala ya moyo mweupe na hutia jitihada yenye kuhisiwa moyoni ili wahudhurie.—Ebr. 10:24, 25.
9 SIKILIZA KWA MAKINI: Kwenye Zaburi 50:7 Yehova husema: “Sikieni, enyi watu wangu, nami nitanena.” Kwa hiyo, wakati wa programu ya mkusanyiko, usikengeushwe fikira na vitu unavyoona na sauti zisizohusiana na habari inayotolewa kutoka jukwaani. Tamaa yetu ya kunena lugha iliyo safi kwa ufasaha yapasa itusukume tutii kabisa ombi la Yehova kwenye Isaya 55:2: “Nisikilizeni kwa bidii.”
10 Habari yote itakayotolewa kwenye mkusanyiko huu ni kwa ajili ya masilahi yetu ya kiroho na itatumika kuimarisha azimio letu la kubaki tukiwa imara katika utumishi wetu kwa Yehova na tukiwa na umoja na ndugu zetu. Mkusanyiko utatuelewesha mahitaji ya karibuni zaidi na kutusaidia kwenda sambamba na tengenezo la Yehova. Kutosikiliza kutatutokezea kuachwa nyuma. Lazima tujiweke wenyewe tukiwa tumekaza fikira zetu katika programu ili tupate manufaa kamili kutokana nayo na baada ya hapo tujizoeze yale tutajifunza.—Yak. 1:25.
11 Je! lipo jambo tuwezalo kufanya ili tusikilize programu kwa makini zaidi na tukumbuke habari inayotolewa? Ndiyo, lipo. Wajumbe wengi wa mkusanyiko wamesitawisha zoea lenye mafaa la kuandika mambo wakati wa programu. Vifaa vinavyofaa vya kuandikia mambo vyapasa kutiwa pamoja na Biblia na vitabu vya nyimbo viwe vifaa vya kawaida wakati wa kuhudhuria mkusanyiko. Ikiwa wewe umekuwa na maoni yenye shaka juu ya kuandika mambo, sababu gani usijaribu kufanya hivyo wakati wa “Lugha Iliyo Safi” Mkusanyiko? Huenda ukapata kwamba ni njia nzuri ya kuweka usikilizaji wako ukiwa umekazwa juu ya yale yanayosemwa na kwamba hukuhami usiruhusu akili yako itanga-tange.
12 Mambo ya kuandikwa hayapasi kuwa mengi au yenye maelezo marefu. Kwa kawaida fungu la maneno machache linatosha kwa wazo kuu. Wazee huliona kuwa jambo lenye faida kuwa na mambo yaliyoandikwa kwa njia nadhifu kwa ajili ya kuongoza pitio lenye maana la programu ya mkusanyiko wakati wa Mkutano wa Utumishi. Baadaye waweza kuunganisha nyingi za habari zilizotolewa kwenye mkusanyiko katika kazi yao ya kufundisha na kufanya uchungaji.
13 WIMBO NA SALA: Sisi tunamheshimu Yehova kwa kuimba sifa zake. Ni sehemu ya ibada yetu. Yehova anapendezwa pia wakati watu wake wanapomfikia kwa sala ya bidii. (Mit. 15:8b) Mikusanyiko ya wilaya hutupa fursa isiyo na kifani ili tuungane pamoja na maelfu ya ndugu na dada zetu katika kusifu Yehova katika wimbo na sala pia. Hata hivyo, wengine wameonyesha ukosefu wa staha kwa sehemu hizi za maana sana za ibada yetu. Jinsi gani? Kwa kufika isivyohitajiwa kwenye mkusanyiko wakati wa wimbo na sala ya kufungua au baadaye. Kwa nini? Katika pindi chache huenda kukawa na sababu nzuri za kufanya hivyo. Hata hivyo, je! staha na uthamini unaofaa unaonyeshwa kwa meza Yehova baadhi yetu wanapoacha pendeleo la kuimba na kujiunga katika sala ili tu waweze kuanza kwenda mapema kwenye mahali pao pa kulala au kula?—Mt. 6:33.
14 Lazima uangalifu utolewe kwamba kwa kufuatia mafaa ya kibinafsi, tusiruhusu mtazamo wa kilimwengu wa mimi kwanza na vitabia visivyo vya kimungu kama vile choyo na ubinafsi vizuie maendeleo yetu ya kiroho. Na tuonyeshe roho ile ile ya uthamini kwa ajili ya vitu vitakatifu kama ndugu zetu walivyofanya kwenye mikusanyiko katika Polandi mwaka jana, sisi na tutembee kwa nia moja nao kwa kuonyesha staha inayofaa kwa ajili ya sehemu tukufu za ibada yetu, yaani, sala na kumwimbia Yehova sifa.—Zab. 69:30.
15 ADABU ZETU ZA KIKRISTO: Kwa muda mrefu adabu zetu za Kikristo na sura yetu kwenye mikusanyiko vimetuletea sifa njema tukiwa Mashahidi wa Yehova. Hii ni kwa sababu kwa kufaa tunaiona ibada yetu kwa Yehova kwa uzito na kwa sababu hatuoni kuhudhuria mikusanyiko yetu kuwa vikusanyiko vya tafrija ya kirafiki vya familia kwenda nje tu. Tunapokuwa tukija pamoja kwa pindi hizo za pekee, yatupasa kudumisha adhama ya Kikristo na akili timamu ya kiroho tukijiendesha nyakati zote kama wahudumu.—1 Kor. 10:31-33.
16 Lakini, ni jambo lenye kuhuzunisha kuona kwamba wachache wenye kuhudhuria mikusanyiko wamekuwa wazembe mno katika mtazamo, mavazi, msemo, na mwenendo wao. Ni jambo gani linaloweza kufanywa wakati mambo kama hayo yanapoonekana wazi katika kundi la kwenu au kwenye mkusanyiko? Wale walio na sifa za kiroho wanapaswa kutoa ushauri wenye upendo kwa kusudi la kuwarekebisha upya. (Gal. 6:1; Efe. 4:11, 12) Kunena lugha iliyo safi kwapasa kutuchochea tutegemeze sifa yetu njema na viwango vya juu vya mwenendo.
17 Mgeni kwenye mmojapo mikusanyiko aliacha barua fupi ifuatayo ndani ya sanduku la michango: “Mimi nilionea shangwe sana sana programu yenu. Sasa mimi nitajifunza Biblia na mmoja wa akina ndugu. Hii ilikuwa ndiyo ziara yangu ya kwanza kwa lolote ya mikusanyiko yenu. Nilipanga kuja Jumamosi peke yake, kwa kuwa Jumapili ni siku ya kanisa langu. Lakini nilivutwa sana hivi kwamba nilikuja leo na nikaja na familia yangu yote. Lakini nilitamaushwa na watu wazima wakiongea kwa sauti kubwa wakati mnenaji alipokuwa akinena.”
18 Imeonwa pia kwamba kwenye baadhi ya mikusanyiko matineja wachache huketi katika sehemu za juu au sehemu zilizo mbali za jumba, wakipitisha vikaratasi vyenye maandishi, wakinong’onezeana, na kwa ujumla hawasikilizi programu. Mwenendo wa namna hii hudokeza kwamba wao wangali wanahitaji usimamizi wa wazazi na wapaswa kuketi pamoja na familia. Wazazi wenye kutunza madaraka wataangalia mambo hayo na kuandaa mwongozo unaohitajiwa na watoto wao. (Efe. 6:4) Akina ndugu, akina dada, na walio wachanga wapaswa kuthamini kwamba wakati programu inapoendelea, ni wakati wa kusikiliza, si kuongea.—Kum. 31:12.
19 Eneo jingine ambapo ufikirio na adabu nzuri zapasa kuonyeshwa ni kuhusiana na mahali petu pa kulala. Tunapata mahali pazuri pa kulala kwa bei iliyopunguzwa sana. Twapaswa kuonyesha uthamini na ufikirio kwa wafanya kazi na ndugu zetu katika idara ya mahali pa kulala tuwe na adabu nzuri na si wenye kudai mno. (Gal. 6:10) Ushauri mzuri umetolewa kwa habari ya mwenendo unaofaa kwenye hoteli au mahali penginepo pa kulala palipokodishwa na katika makao ya ndugu zetu. Tafadhali fuateni kwa uangalifu maagizo kuhusu makatazo yoyote juu ya kupika na kusafisha nguo katika mahali pa kulala pa kukodishwa. Kwa kuwa hatutaki kuacha mahali hapo katika hali isiyofaa tuondokapo twajua kila mmoja atashirikiana na mipango ya kusafisha iliyopangiwa kila mahali pa kulala hususa. Usafi na ufikirio wapasa kudhihirishwa si katika mavazi na mwenendo wetu tu bali pia katika njia ambayo twashughulikia mali za wengine. Je! kuna sababu yoyote kwa nini chumba kilichokodishwa hakipasi kuachwa kikiwa nadhifu na safi? Bila shaka, ni hali moja na mahali pa kulala palipopatikana katika makao ya ndugu zetu. Tabia isiyoonyesha kuwafikiria wengine huharibu jina letu zuri. Wakati wa mikusanyiko ya wilaya ijayo, acheni sisi sote tujitahidi kujiendesha kwa njia ‘itakayopamba mafundisho ya Mwokozi wetu Mungu katika mambo yote.’—Tito 2:10.
20 KWA WAZAZI: Watoto wachanga na matineja wako miongoni mwa wale wanaoalikwa kwenye “Lugha Iliyo Safi” Mkusanyiko wa Wilaya. Lazima wao pia wanene lugha iliyo safi kwa ufasaha. Ni vema kama nini kuona wachanga ambao wamejifunza kusikiliza kwa makini kwenye mikutano yote ya Kikristo na ambao wanapendezwa sana na programu ya mkusanyiko! (Zab. 148:12, 13) Lakini mengi yategemea kielelezo na usimamizi wa wazazi. Wachanga wengi wamezoezwa vizuri sana kuandika habari. Endapo wewe ukiwa mzazi bado hujawafunza watoto wako kuandika habari, mbona usitumie wakati unaobaki kabla ya mkusanyiko wenu ufanye hivyo? Hata walio wachanga sana wanaweza kutiwa moyo kuandika mitajo ya Maandiko na maneno ya msingi yanayohusiana na wanayosikia yakisemwa na wasemaji. Wazazi fulani hupanga kupitia habari kuu kutoka programu ya siku baada ya kurudi mahali pao pa kulala au wanaposafiri kwenda nyumbani.
21 Bila shaka, wazazi walio wengi wanathamini kwamba mbetuko wa asili wa watoto ni kucheza. Hawana maarifa maishani, nao hawajakomaa. Basi, wanapaswa kufundishwa wakati wa kuelekeza fikira na jinsi ya kujiendesha wenyewe kwenye mikutano. Hili linataka usimamizi mzuri wa wazazi wao. Wazazi fulani wamelegea katika sehemu hii. Nyakati nyingine, ingawa huenda wazazi wakawa wanamwonyesha Yehova kicho kinchofaa wakati wa sala, watoto wao wanacheza na kukengeusha fikira za wengine. Wazazi wanapaswa kujua watoto wao wanafanya nini hata wakati wa sala. Pia wanafanya nini wanapoondoka kwenye viti vyao wakati wa programu? Je! watoto wanaachwa bila usimamizi wakati na baada ya programu ya mkusanyiko?—Mit. 29:15.
22 Katika visa fulani watoto wameachwa bila usimamizi katika mahali pao pa kulala huku wazazi wakijihusisha katika utendaji mwingine. Hili halifai. Baadhi ya watoto wametenda katika njia ya ukosefu wa nidhamu na yenye utukutu na hata wamekuwa bila staha kwa akina ndugu na dada wenye umri mkubwa zaidi waliojaribu kuwasahihisha kwa njia ya fadhili. Utukutu huo na mwenendo usiowafaa Wakristo mara nyingi huwa ni tokeo la uendekevu na ukosefu wa nidhamu nyumbani. Hakika wapasa kusahihishwa. Wazazi wote Wakristo wapaswa kuwapa watoto wao usimamizi wa karibu nyakati zote ‘wanapowalea katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.’—Efe. 6:4, NW.
23 Ushirikiano wenu kamili unaombwa kwa habari ya kuhifadhi viti. Tafadhali kumbukeni kwamba VITI VINAWEZA KUHIFADHIWA KWA AJILI YA WASHIRIKI WA FAMILIA YAKO PEKE YAO NA WOWOTE AMBAO HUENDA WAKAWA WANASAFIRI PAMOJA NAWE. Tafadhali msihifadhi viti kwa ajili ya wengine. Nyakati fulani, viti vya ziada haviwekewi mtu fulani hasa. Hili ni jambo la kutoonyesha upendo na linawapotosha wakaribishaji na wengine wanaotafuta viti vilivyo wazi. Kupatana na ushauri wa Biblia, tunapaswa kujitahidi kuonyesha shauku ya kidugu na ushirikiano kamili na mpango unaokubaliwa kwa ajili ya kuhifadhi viti.—2 Pet. 1:5-8.
24 Inadokezwa kwamba uchaguzi mzuri ufanywe kwa habari ya kuleta vitu vya kibinafsi kwenye mahali pa mkusanyiko. Wakati uliopita, watu fulani wameleta mizigo mikubwa ambayo haiwezi kuwekwa chini ya viti. Hii iliwekwa kwenye vijia au juu ya viti. Jambo hili linafanya wengine wanyimwe viti. Tunahitaji kuonyesha ufikirio katika mambo haya.
25 Matumizi ya kamera za vidio na vifaa vya kunasia sauti yanaruhusiwa kwenye mahali pa mkusanyiko. Hata hivyo, wale wanaotumia vifaa hivyo wanapaswa kuwa waangalifu waepuke kusumbua-sumbua au kukengeusha fikira za wengine. Vifaa kama hivyo havipaswi kuwekwa kwenye vijia au kwenye miingilio. Vifaa hivyo havipaswi kuunganishwa na mfumo wa kuhutubia watu wote au matundu ya umeme. Taa zenye mwangaza mwingi hazitaruhusiwa. Wale ambao wanakengeusha fikira au kupuuza yoyote ya miongozo iliyo juu wanapaswa warekebishe jambo hilo bila kukawia wanapoombwa kufanya hivyo. Wakaribishaji na wengine wanaosimamia mambo watakuwa macho kurekebisha uvunjaji wowote wa miongozo hiyo, nao wanapaswa kupata ushirikiano kamili wa wale wanaotumia vyombo hivyo.
26 Kwa hakika, watu wa Yehova huthamini kuweza kukutana pamoja kwenye vifaa hivi vizuri kila mwaka ili kunufaishwa na programu ya kiroho yenye kupendeza ambayo imetayarishwa. Pia sisi tunathamini utumishi mwingi na manufaa yanayoandaliwa kwenye vikusanyiko hivyo. Kwa uangalifu mwingi na kwa gharama kubwa kwa Sosaiti, mipango hufanywa kwa ajili ya viti vyenye kutosha, kuweka mifumo ya sauti yenye gharama sana, kuendesha utumishi wa chakula wenye mafanikio, na kushughulikia hesabu fulani ya mipango mingine na utumishi mbalimbali ambao hufanya kuhudhuria mikusanyiko kuwe jambo la kuonewa shangwe na lenye kuburudisha kiroho.
27 Gharama hizo hulipwa kwa michango yenu ya hiari katika kutegemeza kazi ya ulimwenguni pote ya Sosaiti. Kwa manufaa yenu, masanduku ya michango yenye maandishi yaliyo wazi huwekwa kote kote katika vifaa vya mkusanyiko. Michango yote huthaminiwa sana sana, na Sosaiti yataka kuwashukuru kimbele kwa utegemezo wenu na ukarimu wenye umoja wa masilahi ya Ufalme katika njia hii. Sisi tuna hakika kwamba wote watasukumwa wahisi daraka lao mmoja mmoja kwa habari ya mabadiliko yaliyotajwa hapa na kushirikiana kikamili kwa kushiriki kwa kadiri hali zenu zinavyowaruhusu.—Lk. 6:38.
28 NJONI KWENYE “LUGHA ILIYO SAFI” MKUSANYIKO WA WILAYA: Kwa kuhudhuria “Lugha Iliyo Safi” Mkusanyiko wa Wilaya na kusikiliza programu kwa makini, utathamini kwa ukamili hata zaidi kwa nini Yehova ametupa lugha iliyo safi na kwa nini lazima sikuzote tulinde dhidi ya mielekeo yoyote ya ubinafsi ambayo ingeweza kuharibu umoja wetu na ndugu zetu. Fanya mipango yako sasa uwepo kwa ajili ya wimbo wa kufungua na kuhudhuria vipindi vyote mpaka sala ya kumalizia Jumapili alasiri.
[Sanduku katika ukurasa wa 10]
Vikumbusho vya Mkusanyiko wa Wilaya
MAHALI PA KULALA: Mipango kwa mwaka huu, kwa sehemu iliyo kubwa, itafuata kiolezo cha miaka iliyotangulia. Mikusanyiko iliyo mingi hutumia vyumba vya kulala au vifaa vilivyo mahali pa mkusanyiko ili wote wanaohudhuria wapate mahali pa kulala. Huenda kukawa na mahali pa kulala katika nyumba za watu binafsi. Hata hivyo, tafadhali kumbukeni kwamba, si jambo linalofaa wajumbe wachukue kivivi hivi tu ukaribishaji-wageni wa ndugu zao na kutazamia wawakaribishe siku za ziada ili waweze kuzuru sehemu fulani wakati wa likizo au kufanya mambo mengine kabla au baada ya mkusanyiko. Vyumba hivi ni kwa ajili ya wakati wa mkusanyiko tu. Wale wanaopata mahali kama hapo pa kulala wapaswa wahakikishe kwamba wao na watoto wao wanatenda kwa njia yenye staha kuelekea nyumba ya mkaribishaji wao na wasiharibu kitu chochote au kupekua-pekua mali au sehemu za faragha za nyumba hiyo. Wenye nyumba wakiwa na matatizo yoyote kuhusiana na jambo hili wanapaswa kujulisha Idara ya Mahali pa Kulala mara moja kwenye mkusanyiko, na ndugu waliopo watafurahi kusaidia. Mnaweza kupeleka fomu ya maombi ya mahali pa kulala iliyojazwa kupitia msawazishaji wa mkusanyiko katika kundi lenu.
UBATIZO: Wale wanaotaka kubatizwa wanapaswa wajitahidi kuwa kwenye viti vyao katika sehemu iliyoonyeshwa kabla ya programu kuanza Jumamosi asubuhi. Mavazi yenye kiasi na taulo yanapaswa kuletwa na kila mmoja anayepanga kubatizwa. Akina dada hasa watataka kuchunguza kimbele waone kama mavazi wanayopanga kuvaa yanaonyesha uchi yanapolowa maji. (Ona Huduma ya Ufalme, Novemba 1987, ukurasa 3, fungu 6) Baada ya hotuba ya ubatizo na sala itakayotolewa na mnenaji, mwenyekiti wa kipindi hicho atawatolea wanaobatizwa maagizo mafupi kisha ataomba wimbo uimbwe. Mstari wa mwisho uanzapo, wakaribishaji watawaelekeza wenye kubatizwa kwenye mahali pa uzamisho au kwenye magari yatakayowapeleka hapo, huku wasikilizaji wale wengine wakimaliza kuimba wimbo. Kwa kuwa ubatizo kwa kufananisha kujiweka wakfu kwa mtu ni jambo la usiri na la kibinafsi kati ya mtu na Yehova, hakuna uandalizi kwa ule unaoitwa eti ubatizo wa shirika ambao watu wawili au zaidi wanaotaka kubatizwa wanakumbatiana au kushikana mikono wanapobatizwa.
KITAMBULISHO CHA MAPAINIA: Mapainia wote wa kawaida na wa Pekee, na waangalizi wasafirio pia watahitaji kuleta kadi yao ya Utambulisho na Mgawo kwenye mkusanyiko. Mapainia ambao watakuwa wamekuwa kwenye orodha kwa miezi sita tangu waanze upainia wakati wa mkusanyiko wa wilaya watakaouhudhuria wanaweza kupokea tikiti za chakula za mkusanyiko wakionyesha kitambulisho chao kwenye mkusanyiko huu mmoja tu. Hivyo, tunza kadi hiyo kama vile ungetunza pesa. Huwezi kupata nyingine kwenye mkusanyiko. Vichapo vyovyote vitakavyotolewa kama zawadi au vingine kwa bei ya painia vitapatikana kwa mapainia katika chumba cha vitabu tu, kwa kuonyesha kitambulisho chao. Wale walio katika utumishi wa Betheli wanaweza kupokea maandalizi yayo hayo kwa kuonyesha kitambulisho chao cha Betheli.
UTUMISHI WA KUJITOLEA: Msaada wa kujitolea unahitajiwa ili mkusanyiko wa wilaya uendeshwe vizuri. Hata kama unaweza kufanya kazi kwa sehemu fulani tu ya mkusanyiko, utumishi wako utathaminiwa. Ikiwa unaweza kusaidia, tafadhali piga ripoti kwenye Idara ya Utumishi wa Kujitolea unapowasili kwenye mkusanyiko. Watoto wa umri ulio chini ya miaka 16 waweza kuchangia pia kufanikiwa kwa mkusanyiko, wanatakwa wafanye kazi pamoja na mzazi au mtu mwingine mzima mwenye kujali daraka.
KADI ZA BEJI ZA SHAVU LA KOTI: Tafadhali vaa kadi ya beji ya shavu la koti iliyotayarishwa kipekee kwenye mkusanyiko na pia unaposafiri kwenye na kutoka mahali pa mkusanyiko. Mara nyingi hii inatuwezesha tutoe ushahidi mzuri tunaposafiri. Unapaswa upokee kadi ya beji ya shavu la koti kupitia kundi lako kwa sababu hazitapatikana kwenye mkusanyiko.
TAHADHARI: Hata uwe unaegesha wapi, unapaswa ufunge gari lako wakati wote na usiache ndani kitu chochote kinachoonekana. Fungia mizigo yako yote nyuma ya gari, ikiwezekana. Pia, ujilinde dhidi ya wevi na wakwepuzi wa mifuko wanaovutiwa na mikusanyiko mikubwa. Hii inatia ndani kutoacha kitu chochote chenye thamani bila mtu wa kukitunza katika viti kwenye mikusanyiko. Tafadhali iweni waangalifu.