Fungu Lako Katika Kujenga kwa Ajili ya Wakati Ujao
1 Leo Wakristo wanaendelea kusimamia kazi ya ujenzi wa kiroho ambayo Yesu alianzisha yapata miaka 1,960 iliyopita wakati alipoanza kukusanya wanafunzi. (Mt. 4:17; 7:24, 25, 28; Yn. 7:46) Yehova amebariki kazi hiyo kwa wingi sana. (Mit. 10:22) Tuendeleapo na kazi yetu ya kutangaza Ufalme wa Mungu, sisi tunajenga pia ili kutunza ongezeko la wakati ujao.—Mhu. 11:6
2 Baadhi ya Majumba ya Ufalme ya zamani kidogo yanahitaji kutengenezwa. Ama baraza la wazee au halmashauri ya utunzaji wapaswa kuchunguza kuona kama kuta zahitaji kupakwa rangi upya, au kama paa lahitaji kutengenezwa. Namna gani sehemu ambazo fasihi na magazeti hupokewa? Je, vyoo vinafanya kazi vizuri? Hakikisheni kuweka Jumba la Ufalme katika hali nzuri. Majumba zaidi yahitajiwa ili makundi mapya yanayoundwa yawe na mahali pa kukutanikia. Mwaka jana makundi katika Afrika Mashariki yaliongezeka kwa 46. Fedha na pia wafanyakazi wa kujitolea wahitajiwa ili miradi hiyo ya ujenzi imalizwe kwa kufanikiwa. Maoni chanya ya akina ndugu yenye kusifika kuelekea kutimiza uhitaji huu yanabarikiwa sana.—Zab. 41:1; Mit. 19:17; Mhu. 11:1; Lk. 14:13, 14.
USAIDIZI WENYE UPENDO WATOLEWA NA WENGI
3 Sisi twaonyesha upendo kwa ajili ya ‘ushirika mzima wa akina ndugu’ kwa kuchanga katika kundi letu kwa ajili ya miradi ya ujenzi wa Jumba la Ufalme na Jumba la Kusanyiko. Sosaiti inaendelea kutegemeza miradi hiyo na kwa wakati wa sasa makundi 26 yanasaidiwa kupitia mikopo kutoka kwa Sosaiti. Kwa kuongezea, hesabu fulani ya makundi mengine yameweka hazina ya ujenzi kwa ajili ya miradi ya wakati ujao na baadhi ya makundi hukabidhi Sosaiti hazina yao iwawekee mpaka wanapokuwa tayari kujenga. Hakika kadiri kazi ya kukusanya inavyoongeza mwendo ndivyo na uhitaji wa Majumba ya Ufalme ya kutosha ili kuwe na nafasi kwa ukuzi huo. Sosaiti huonyesha uthamini wenye kina kwa umati wa watu mmoja mmoja na familia ambao huchangia kwa ukawaida utunzaji na udumishaji wa Majumba ya Ufalme yaliyopo na wanaotegemeza kwa ukarimu ujenzi wa majumba mapya katika eneo letu.—1 Pet. 2:17, NW.
4 Je, wewe una ustadi katika kazi ya ujenzi? ikiwa ndivyo, na ikiwa unapatikana kusaidia katika ujenzi wa Jumba la Ufalme, unaweza kujulisha wazee wa kundi lenu jambo hilo pamoja na mwangalizi wa mzunguko. Wafanyakazi stadi wa kujitolea wahitajiwa kotekote katika eneo. Kwa kweli, sisi huwauliza waangalizi wa mzunguko waweke orodha yenye habari ya karibuni zaidi ya mafundi stadi wote katika mzunguko wao pamoja na orodha ya vifaa vyovyote vya kazi ngumu ya ujenzi, kama vile, mashine za kuchanganya saruji, tinga-tinga, n.k., zinazoweza kupatikana kutumiwa katika mzunguko wenu.
5 Sosaiti, kwa msaada wa ndugu wenye ujuzi katika sehemu mbalimbali za eneo letu, iko tayari kutoa usaidizi katika hatua zote za kuchora ramani na kujenga. Sosaiti ina ramani ambazo zimekwisha chorwa zinazofaa njia za ujenzi za kwenu na ambazo hutoa madokezo na usaidizi wenye mafaa kwa kujenga Majumba ya Ufalme madogo kiasi na yenye kuvutia na pia kuokoa wakati na fedha. Katika maeneo mengi msaada unaweza kutolewa kwa wazee ili kukadiria kwa usahihi gharama za ujenzi na kupata vifaa vya ujenzi kwa bei nafuu.
6 Mapema vya kutosha kabla ya kununua kiwanja au kukubali kupewa kiwanja na wenye mamlaka au mchango wa kiwanja wa watu binafsi, ni jambo la hekima kushauriana na mwangalizi wa mzunguko au Sosaiti. Miongozo fulani yaweza kutolewa kusaidia kundi ili kuepuka magumu ambayo yangeweza kutokea katika kujipatia kiwanja. Katika visa fulani ambapo haiwezekani kupata hati ya umilikaji iliyoandikishwa na wenye mamlaka huenda ikahitajiwa kuwa na tangazo la udhamini kwa ajili ya kiwanja hicho kuonyesha kwamba kimetengwa kweli kweli kwa ajili ya matumizi ya kundi. Imetukia pia kwamba upaji wa sehemu ya kiwanja mahususi iliyotolewa na wenye mamlaka ilikuwa kubwa mno isiweze kusitawishwa vya kutosha kwa fedha lilizokuwa nazo kundi. Kushindwa kusitawisha kiwanja kilichotolewa na wenye mamlaka kwaweza kuongoza kwenye kukipoteza. Kwa hiyo, ni jambo la hekima kushauriana na mwangalizi wa mzunguko au Sosaiti kabla ya kukamilisha lolote la yaliyo juu kwa ajili ya miongozo kuhusu kupata hati ya umilikaji au kusitawisha kisehemu chochote cha kiwanja.
7 Wakati wa kuteua kiwanja kwa ajili ya ujenzi wa Jumba la Ufalme katika mji ambamo mna zaidi ya kundi moja, wazee wenyeji wapaswa kuzungumza jambo hilo pamoja na mwangalizi wa mzunguko, mwangalizi wa mji, na pengine wazee wa makundi ya karibu. Hilo laweza kusaidia wazee wenyeji katika kuchagua mahali ambapo patanufaisha makundi zaidi yanayohusika katika mradi huo wa sasa na pengine isaidie kupunguza msongamano katika Majumba ya Ufalme yaliyo jirani, wakati uo huo kuruhusu pia nafasi kwa ajili ya ukuzi wa wakati ujao katika eneo hilo. Katika baadhi ya maeneo ya mijini, mara nyingi Jumba la Ufalme moja hutumiwa na makundi matatu au zaidi. Hata katika maeneo yasiyo na idadi kubwa ya watu, mahali paweza kuteuliwa ambapo paweza kutumiwa na makundi mawili au zaidi.
8 Mpango wa kitengenezo na stadi walizojifunza katika miradi hii zimekuwa zenye kusaidia katika ujenzi wa Majumba ya Kusanyiko na katika kusaidia akina ndugu wajenge upya baada ya misiba ya kiasili, kama vile mafuriko ya hivi majuzi katika nchi moja katika eneo letu. Popote palipo na mradi, wazee watakumbuka umaana wa kujaribu kuratibu kazi na wenye kujitolea kwa wakati watakaohitajiwa hasa kwenye ujenzi hivi kwamba hawatakosa kushiriki katika mikutano na utendaji wa utumishi wa shambani wa kundi.
9 Wote waweza kudhihirisha tunda la fadhili katika kushirikiana na wale wanaosimamia utendaji wa ujenzi. Kwa njia hiyo kazi inayohitajiwa ‘inatimizwa kikamili’ na “kwa furaha wala si kwa kuugua.”—Mdo. 14:26; Ebr. 13:17.
KUTOA FEDHA KWA AJILI YA MIRADI YA UJENZI WA JUMBA LA UFALME
10 Mipango ya kutoa fedha zinazohitajiwa yapasa kufanywa mwanzoni kabisa. (Lk. 14:28-30) Wazee wapaswa kuamua uwezo wa kundi wa kulipia gharama zinazohusika kwa kufanya uchunguzi ili kuamua (1) ni kiasi gani kitakachochangwa mara moja cha kutosha ili kusaidia kununua kiwanja na gharama za ujenzi, (2) ni kiasi gani kinachoweza kukopeshwa na washiriki wa kundi lenu na ni kwa muda gani fedha hizo zitakopeshwa, na (3) wahubiri wanafikiria kuchanga kiasi gani kila mwezi ili kulipia mkopo wowote unaohitajiwa kuongezea kutimiza gharama za kawaida za mradi huo.
11 Kwa hiyo, wazee wa makundi yanayohitaji usaidizi wa kifedha kutoka kwa Sosaiti wapaswa kuzungumza na mwangalizi wa mzunguko juu ya mradi wanaokusudia na mahitaji ya kifedha, ambaye aweza kuwasaidia kwa kujulisha Sosaiti mahitaji yao na habari zaidi kuhusu mradi huo. Baada ya mwangalizi wa mzunguko kupelekea Sosaiti habari, barua zitapelekewa makundi yanayohusika moja kwa moja. Usaidizi wa kifedha unatolewa hatua kwa hatua kadiri fedha zinavyopatikana na kulingana na mahitaji.
DUMISHENI ROHO YA BIDII
12 Wote wastahili kupongezwa kwa ukarimu wao katika kutegemeza miradi ya ujenzi wa Majumba ya Ufalme. Uthamini mwingi ambao umeonyeshwa umepokewa kutoka kwa makundi yaliyosaidiwa. “Usawazisho” unatukia miongoni mwa makundi.—2 Kor. 8:14, 15, NW.
13 Wakati wa kujenga Jumba la Ufalme jipya, shauku, bidii, na roho chanya huchangia kufanikiwa kwa mradi huo. Roho iyo hiyo yapaswa iendelee tutafutapo kuleta watu wengi zaidi kwenye maarifa ya kweli na kuwatia moyo wakutane pamoja nasi kwenye Jumba la Ufalme. Bidii kama hiyo ni udhihirisho wa wonyesho wa uthamini ambao hutokeza maongezeko yenye kuonekana katika hudhurio la mikutano na katika ukuzi wa ujumla wa kundi.
14 Tuendeleapo kupanua huduma yetu, tukijitahidi wenyewe kwa bidii katika kazi iliyopo, bila shaka baraka ya Yehova itaendelea kuwa pamoja nasi. (Lk. 13:24) Sisi hatujui ni ukuzi na ongezeko gani latungojea wakati ujao. Lakini twapaswa kuwa tayari kukaribisha mmiminiko wowote wa waabudu wa wakati ujao. Hilo lataka kujitayarisha sasa upande wetu. Hivyo, twasali twendelee kupata baraka na mwelekezo wa Yehova. Katika kujenga kwa ajili ya wakati ujao, sisi sote na tuwe wafanyakazi pamoja na Yehova—kwa nguvu zetu za mwili, kwa vitu vya kimwili, na kiroho. Bila shaka yeye atatubariki tutunzapo ifaavyo wale wanaoharakisha kuingia katika tengenezo lake la Ufalme wakati wa hii sehemu ya kumalizia ya siku za mwisho.—Isa. 60:8, 10, 11, 22.