Kuongoza Mafunzo ya Biblia ya Familia Yenye Kujaa Maana
1 Mojapo utendaji wenye maana kupita wote ambao wazazi hufanya ni kufundisha watoto wao kweli. Ni jukumu kutoka kwa Yehova. (Kum. 6:6, 7) Watoto wahitaji mwelekezo na mwongozo ili watembee kwa unyofu katika ulimwengu usiomhofu Mungu. Wanahitaji kujifunza kumpenda Yehova na kupenda kweli na kuazimia kushikamana nayo. Mnara wa Mlinzi wa Agosti 1, 1988 ukurasa 11, ulitaarifu hivi: “Kujapokuwa na wajibu wowote mwinginewo ambao ninyi mnao au taabu mnazoelekeana nazo, kutumia wakati pamoja na watoto wenu kunahitaji kuwa utangulizo wa kwanza. Wakati unaotumiwa pamoja utawaruhusu ninyi mkaze kikiki maadili ya kiroho ambayo yatalinda salama mioyo ya watoto wenu na kuwaweka katika mwendo unaofaa.”
2 Ikiwa familia zitafuata miongozo iliyotolewa katika Neno la Mungu, lazima wakati utengwe kwa ukawaida kwa ajili ya funzo la familia. Vichwa vya familia wahitaji kutanguliza kutunza hali ya kiroho ya familia. Ikiwa mahitaji ya familia ya kiroho hayaangaliwi ifaavyo sasa, yaelekea sana wazazi watakuwa hawana budi kushughulikia matatizo mazito katika wakati ujao.
HABARI NA NJIA ZA KUJIFUNZA
3 Mjifunze nini? Kichwa cha familia yuko katika hali bora zaidi kujua yanayohitajiwa na familia. Aweza kuuliza wengine wanafikiri ni habari ipi itanufaisha na kufikiria madokezo yao. Kubadilikana kutafanya funzo la familia liwe lenye kutumika na lenye kuchochea. Familia nyingi huchagua kutayarisha somo la kila juma la Mnara wa Mlinzi. Hata hivyo, huenda ikahitajiwa nyakati fulani kuzungumza habari mahususi zinazohusu matatizo wanayokabili vijana shuleni. Habari iliyochapwa inayoshughulika na matembezi ya kimapenzi ya watu wa jinsia tofauti, utendaji wa baada ya masomo ya shule, michezo, na maelekeo yenye ukosefu wa adili zaweza kuzungumzwa kwa njia yenye kujenga na yenye kutia moyo. Ni jambo la maana kwamba kichwa cha familia achunguze-chunguze daima ni habari ipi inayohitajiwa na familia na jinsi ya kufikia vyema zaidi mioyo yao kwa habari hiyo.—Ona The Watchtower, Februari 15, 1971, kurasa 105-6.
4 Funzo lapasa kuongozwaje? Sitawisha mazingira yenye starehe na bado yenye staha. Epuka njia ya kufanya mambo kimashine, yenye hali ya kidarasani kupita kiasi. Uliza maswali ya ziada, na kutumia vielezi ili kuchochea kufikiri na kuhusisha wote. Misaada yenye kuonekana, kama vile ramani na chati, yaweza kutumiwa kuongezea habari. Migawo yaweza kutolewa ili kupata habari katika Fahirisi au mabuku ya Insight, kulingana na umri na uwezo wa watoto. Wahusishe watoto wachanga zaidi katika mazungumzo upesi iwezekanavyo wanapoweza kujibu. Waweza kuulizwa maswali rahisi yanayotaka majibu ya maneno machache tu. Usitumie wakati wa funzo kushutumu watoto. Badala ya hivyo, wasifu, onyesha uthamini kwa jitihada zao, na uwe mchangamfu katika kushiriki pamoja nao maoni ya kiroho.
5 Waweza kuwaje na uhakika kwamba unafikia moyo? Watie moyo wote watumie maneno yao wenyewe kujibu. Tumia kwa busara maswali ya maoni ili kujua maoni ya moyoni. Ungeweza kuuliza: “Watoto shuleni wahisije juu ya jambo hili? Je! nyinyi mnakuwa na shaka juu ya jambo hili wakati wowote? Uwe mwangalifu usiitikie kwa njia yenye kupita kiasi majibu wanayotoa watoto kwa maswali ya maoni, au sivyo huenda watoto wako wasijisikie huru kujieleza kwa unyofu. Wape wakati wa kunena. Kujua kwao kwamba wapendezwa nao na matatizo yao kutafanya jitihada zako za kufundisha ziwe rahisi zaidi.—Ona Mnara wa Mlinzi, Novemba 1, 1986, kurasa 23-5.
6 Kumbuka kwamba lengo kuu la funzo lenu la familia ni kukaza kikiki mawazo ya Yehova na si kupata jibu tu la kurudia kulijibu katika mkutano wa kundi. (Efe. 3:17-19) Hilo lamaanisha kufanya kazi ili kuingiza habari ndani ya mioyo. Ipe familia sababu kwa nini wapaswa watake kufanya mapenzi ya Mungu na kwa nini huo ndio mwendo bora zaidi maishani.
7 Funzo la Biblia la ukawaida la familia ni la muhimu katika kujenga hali ya kiroho ya familia. Linazoeza na kuwatayarisha watoto wawezane na matatizo ya maisha. Nyinyi wazazi mko katika hali bora zaidi kusaidia watoto wenu. Twaeni daraka hili ambalo mmepewa na Mungu. Hakika Yehova atabariki nyinyi ikiwa mtafanya kila jitihada mwe wenye ukawaida katika kuongoza funzo la Biblia la familia lenye kujaa maana.