Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • rs uku. 265-uku. 269
  • Serikali

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Serikali
  • Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
  • Habari Zinazolingana
  • Namna Ufalme wa Mungu Unavyoweza Kukufaidi Wewe
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Masuala Yanayoamua Wakati Ujao Wetu Utakavyokuwa
    Kuokolewa Kuingia Katika Dunia Mpya
  • Utawala wa Ulimwengu Unabadilika
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Ufalme
    Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
Pata Habari Zaidi
Kutoa Sababu kwa Kutumia Maandiko
rs uku. 265-uku. 269

Serikali

Maana: Mpango wa kutunga na kutekeleza sheria. Mara nyingi serikali hutofautishwa kulingana na chanzo na mamlaka yake. Yehova Mungu ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, anayewapa wengine mamlaka kulingana na mapenzi na kusudi lake. Hata hivyo, Shetani Ibilisi, mwasi mkuu wa enzi kuu ya Yehova, ndiye “mtawala wa ulimwengu”—Mungu amemruhusu atawale kwa kipindi kifupi. Biblia inafananisha mfumo wa duniani pote wa utawala wa kisiasa na mnyama-mwitu na inasema kwamba “yule joka mkubwa [Shetani Ibilisi] akampa huyo mnyama nguvu zake na kile kiti chake cha ufalme na mamlaka kubwa.”—Yoh. 14:30; Ufu. 13:2; 1 Yoh. 5:19.

Je, wanadamu wanaweza kuanzisha serikali ambayo kwa kweli italeta furaha yenye kudumu?

Historia ya wanadamu inaonyesha nini?

Mhu. 8:9: “Mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” (Hali imekuwa hivyo hata ingawa serikali na watawala fulani wameanza wakiwa na makusudio mazuri.)

“Kila ustaarabu ambao umepata kuwako mwishowe umeanguka. Historia inaonyesha kwamba jitihada za mwanadamu zimeshindwa, au miradi yake haikutimia. . . . Kwa hiyo, mwanahistoria analazimika kuishi akijua kwamba msiba hauwezi kuepukika.”—Henry Kissinger, mwanasayansi wa kisiasa na profesa wa serikali, kama alivyonukuliwa katika The New York Times, Oktoba 13, 1974, uku. 30B.

Ni nini kinachofanya serikali za wanadamu zisifaulu?

Yer. 10:23: “Ninajua vema, Ee Yehova, kwamba njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.” (Mungu hakuwapa wanadamu mamlaka ya kujiongoza wenyewe bila kumtegemea Mungu.)

Mwa. 8:21: “Mwelekeo wa moyo wa mwanadamu ni mbaya tangu ujana wake na kuendelea.” (Watawala pamoja na wale wanaotawaliwa wote wamezaliwa katika dhambi, wakiwa na maelekeo ya ubinafsi.)

2 Tim. 3:1-4: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wasiotaka makubaliano yoyote, . . . wenye kujivuna kwa kiburi.” (Matatizo yanayowakabili wanadamu leo hayawezi kutatuliwa daima na taifa moja tu; yanataka ushirikiano kamili wa kimataifa. Lakini faida za ubinafsi zinazuia hilo na pia zinazuia sana ushirikiano wowote wa kweli kati ya mashirika mbalimbali yaliyo katika mataifa.)

Biblia pia inafunua kwamba viumbe fulani vyenye nguvu kuliko wanadamu vinaongoza kwa hila mambo ya wanadamu. “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1 Yoh. 5:19) “Tuna kushindana mweleka, si juu ya damu na mwili, bali juu ya . . . watawala wa ulimwengu wa giza hili, juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” (Efe. 6:12) “Maneno yanayoongozwa na roho waovu . . . yanakwenda kwa wafalme wa dunia nzima inayokaliwa, ili kuwakusanya pamoja kwa vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote.”—Ufu. 16:14.

Watu wanaweza kupataje kitulizo cha kudumu kutoka katika ufisadi na ukandamizaji wa serikali?

Je, kuwapa watu wengine mamlaka kutasuluhisha tatizo hilo?

Je, si kweli kwamba mahali ambapo pana uchaguzi huru watu walio mamlakani mara nyingi huondolewa baada ya miaka michache? Kwa nini? Watu wengi hawaridhiki na kazi yao.

Zab. 146:3, 4: “Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, wala katika mtu wa udongo, ambaye hana wokovu wowote. Roho yake hutoka, naye hurudi kwenye udongo wake; siku hiyo mawazo yake hupotea.” (Mipango yoyote ya kuboresha mambo ambayo watawala huanzisha huanguka upesi mikononi mwa wengine na mara nyingi huachiliwa mbali.)

Hata mtawala awe ni nani, bado yeye ni sehemu ya ulimwengu huu ulio katika nguvu za Shetani.—1 Yoh. 5:19.

Je, mapinduzi ya kutumia nguvu ndiyo suluhisho?

Hata watawala wafisadi wakipinduliwa na sheria zisizo za haki kutupiliwa mbali, serikali mpya itakuwa na wanadamu wasiokamilika na bado watakuwa sehemu ya mfumo wa kisiasa ambao Biblia inasema waziwazi kwamba uko chini ya uongozi wa Shetani.

Mt. 26:52: “Rudisha upanga wako mahali pake, kwa maana wale wote wanaouchukua upanga wataangamia kwa upanga.” (Yesu alimwambia hayo mmoja wa mitume wake wakati ambapo mamlaka ya serikali ilikuwa ikitumiwa isivyo haki dhidi ya Mwana wa Mungu mwenyewe. Je, hiyo haingekuwa sababu nzuri zaidi ya mtu kupigana, ikiwa hilo lingekuwa jambo zuri la kufanya?)

Met. 24:21, 22: “Mwanangu, mwogope Yehova na mfalme. Usishirikiane na watu wanaotaka badiliko. Kwa maana msiba wao utakuja ghafula, hivi kwamba ni nani anayejua juu ya kuangamizwa kwa watu wanaotaka badiliko?”

Basi suluhisho ni nini kwa matatizo ya ufisadi na ukandamizaji?

Dan. 2:44: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme [serikali] ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.”

Zab. 72:12-14: “[Yesu Kristo, mfalme aliyewekwa na Yehova] atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataziokoa nafsi za maskini. Ataikomboa nafsi yao kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri, nayo damu yao itakuwa na thamani machoni pake.” (Jinsi alivyowahangaikia watu hao alipokuwa duniani—alivyowaponya, alivyolisha umati wa watu, hata kutoa uhai wake kwa ajili yao—huonyesha kwamba yeye kwa kweli ndiye mtawala aliyetabiriwa katika unabii huo.)

Ona pia ukurasa wa 313-318, chini ya kichwa “Ufalme.”

Kwa nini tunapaswa kufikiria kwa uzito yale ambayo Biblia inasema kuhusu wakati ujao wa serikali?

Watawala wa kibinadamu hawatoi yale ambayo wanadamu wanahitaji kwa haraka

Fikiria mambo haya ambayo watu kila mahali wanahitaji, ambayo serikali za kibinadamu hazitoi lakini ambayo Mungu ameahidi: (1) Maisha katika ulimwengu usio na tisho la vita.—Isa. 2:4; Zab. 46:9, 10. (2) Chakula cha kumtosha kila mtu.—Zab. 72:16. (3) Nyumba nzuri kwa kila mtu.—Isa. 65:21. (4) Kazi ya kuridhisha kwa wote wanaoihitaji, ili waweze kujiruzuku wenyewe na familia zao.—Isa. 65:22. (5) Maisha yasiyoharibiwa na magonjwa na maradhi.—Ufu. 21:3, 4. (6) Haki; uhuru bila ubaguzi wa kidini, wa rangi, wa kiuchumi, na wa kikabila na kitaifa.—Isa. 9:7; 11:3-5. (7) Kuwa na usalama, bila wahalifu kuhatarisha maisha ya watu au mali zao.—Mika 4:4; Met. 2:22. (8) Ulimwengu ambamo sifa zenye kuthaminiwa zaidi zitatia ndani upendo, fadhili, watu kuhangaikiana, na ukweli.—Zab. 85:10, 11; Gal. 5:22, 23.

Kwa maelfu ya miaka, watawala wa kisiasa wamekuwa wakiwaahidi watu wao hali zilizo bora. Kukiwa na matokeo gani? Ijapokuwa watu katika mataifa mengi wana mali nyingi zaidi, si wenye furaha zaidi, nayo matatizo yanayowakabili ni mengi kuliko zamani.

Unabii wa Biblia umekuwa wenye kutegemeka kabisa

Karne moja mapema neno la Mungu lilitabiri cheo cha Babiloni cha kutawala ulimwengu, pia jinsi ambavyo mamlaka yake yangevunjwa mwishowe, na uhakika wa kwamba, ikiisha kuharibiwa, jiji lake kuu halingekaliwa tena kamwe. (Isa. 13:17-22) Karibu karne mbili mapema, hata kabla Koreshi hajazaliwa, Biblia ilitabiri kumhusu kwa kumtaja jina na pia daraka lake katika mambo ya kimataifa. (Isa. 44:28; 45:1, 2) Kabla Umedi na Uajemi hazijawa mamlaka ya ulimwengu, kuinuka kwake, ukiwa muungano wa mamlaka mbili, na jinsi ambavyo ungekoma, yote hayo yalitabiriwa. Zaidi ya karne mbili mapema mwendo wa milki ya ulimwengu ya Ugiriki chini ya mfalme wake wa kwanza ulitabiriwa, pia mgawanyiko wa baadaye wa milki hiyo kuwa sehemu nne.—Dan. 8:1-8, 20-22,

Biblia ilitabiri kirefu hali za ulimwengu za wakati wetu, na inatupasha habari kwamba serikali zote za kibinadamu zitakomeshwa mikononi mwa Mungu na kwamba Ufalme wa Mungu mikononi mwa Mwanawe, Yesu Kristo, utawatawala wanadamu wote.—Dan. 2:44; 7:13, 14.

Je, si jambo la hekima kutii chanzo cha habari ambacho kimetegemeka sana bila kugeuka-geuka?

Serikali ya Mungu ndiyo suluhisho pekee la kweli kwa matatizo ya wanadamu

Matatizo yanayohitaji kusuluhishwa yanataka nguvu, uwezo, na sifa ambazo wanadamu hawana. Mungu anaweza kuwaweka huru wanadamu kutoka katika uvutano wa Ibilisi na roho wake waovu, na Mungu ameahidi kufanya hivyo, lakini hakuna mwanadamu anayeweza kufanya hivyo. Mungu amefanya uandalizi wa kufanya yale ambayo sayansi ya tiba haiwezi kamwe kutimiza—kuondoa dhambi, hivyo kukomesha magonjwa na kifo na kufanya iwezekane watu wawe jinsi wanavyotaka kuwa kikweli. Muumba ana ujuzi unaohitajiwa (kuhusu dunia na taratibu zote za uhai) ili kusuluhisha matatizo ya uzalishaji wa chakula na kuzuia uchafuzi hatari, lakini mara nyingi jitihada za wanadamu huleta matatizo zaidi. Neno la Mungu tayari linageuza maisha ya watu hivi kwamba wale wanaoitikia uongozi wake wanakuwa wenye fadhili, watu wenye upendo na maadili bora, jamii ya watu wanaokataa kutumia silaha dhidi ya wanadamu wenzao na wanaoishi kwa amani na undugu wa kweli ijapokuwa wanatoka katika mataifa, rangi, na makabila yote.

Ufalme wa Mungu utaondoa wakati gani mfumo wa ulimwengu uliopo sasa? Ona vichwa “Vipindi vya Wakati” na “Siku za Mwisho.”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki