Kutoa Utegemezo kwa Mapainia
1 Watu wa Mungu wanajulikana kwa bidii yao ya kushiriki katika huduma. Ingawa si wote walio na hali zinazowaruhusu kupainia, tunapaswa tujitahidi kukuza roho ya upainia, tukiwa wenye nafsi yote katika yale tufanyayo. Tunashangilia pamoja na kuwatia moyo wale wengi wanaoweza kuingia utumishi wa upainia.
2 Kuwa na kuendelea kuwa painia ni kazi kubwa. Mapainia huwa na sehemu kubwa ya kazi ya kuhubiri na kufundisha. Hiyo haitimizwi bila jitihada na kujidhabihu kwingi. Wengine wanaweza kutegemezaje na kutiaje moyo watumishi hao wa wakati wote wenye bidii?
3 Yale Yanayoweza Kufanywa: Mapainia wanahitaji utegemezo kutoka kwa wazee. Kitia-moyo kingi kinatolewa wakati wazee wafanyapo kazi pamoja na mapainia kundini. Wazee wengi hujaribu kuhubiri na kila painia kundini angalau mara moja kwa mwaka. Kwa njia hiyo wazee wanaweza kutoa pongezi kwa yale ambayo mapainia wanafanya na kuwasaidia kufanya maendeleo zaidi. Huenda mapainia wakahitaji kurekebisha ratiba yao ili wawe katika utumishi wakati ambao wazee waweza kupatikana. Pia, wazee wahakikishe kuwa eneo la kutosha lapatikana kwa ajili ya vikundi. Mikutano ya ziada kwa ajili ya utumishi wa shambani yaweza kupangwa alasiri au jioni ili kufaa ratiba za mapainia. Hilo lingefaa hasa wakati wa miezi ambapo kuna mapainia wasaidizi kadhaa.—Isa. 40:11.
4 Watumishi wa huduma wako katika hali bora ya kusaidia mapainia kwa kuwategemeza katika huduma na kwa kutunza mipango ya kundi kwa bidii. Akina dada mapainia huthamini ndugu wanaoongoza katika kupanga vikundi vya utumishi wa shambani. Wale wanaoshughulikia fasihi na magazeti wanaweza kuhakikisha kwamba kuna ugavi wa kutosha unaopatikana. Kutunza mambo kama hayo huwawezesha mapainia kukazia fikira huduma yao.
5 Kila Mtu Aweza Kusaidia: Wahubiri waweza kusaidia kwa kujitokeza mara nyingi zaidi kufanya kazi pamoja na mapainia. Mapainia huonea shangwe ushirika na utegemezo wa wahubiri wengine. Labda unaweza kupanga kuhubiri na mapainia mara moja kwa juma au mara mbili kwa mwezi. Vitu vya kimwili vyaweza kushirikiwa na mapainia, na ukarimu huo huthaminiwa sana na mapainia.—Flp. 4:14-19.
6 Familia zaweza kufanya mengi kusaidia washiriki wazo wanaopainia. Mara nyingi, kazi za nyumbani zaweza kupangwa upya kuruhusu mshiriki mmoja au zaidi wa familia kupainia. Dada mmoja mwenye watoto watatu huhubiri siku mbili kwa juma. Wana wake husaidia katika ununuzi na kazi nyingine za nyumbani. Binti yake husaidia na usafi na upishi. Tangu ahitimu, yeye pia ameanza kupainia, wakibadilishana na mama yake siku za mahubiri. Ushirikiano kama huo katika familia huwezesha wengi zaidi wapainie na huletea familia baraka.
7 Mapainia wenye bidii hujithibitisha kuwa baraka kwa kundi katika njia nyingi. Bidii na mfano wao hutia wengi moyo kufanya zaidi katika utumishi. Kweli kweli, tunapaswa kufanya yote tuwezayo kuwategemeza. Jitihada kama hizo za pamoja huletea wote shangwe na huleta sifa kwa Yehova.