Takwa la Kufanya Ziara za Kurudia
1 Tukiwa wahudumu wa habari njema, tumeamuriwa kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Hilo linatia ndani kufanya ziara za kurudia. Je! wewe una maoni yanayofaa kuhusu sehemu hii muhimu sana ya huduma yetu ya Kikristo? Kuwa wastadi katika kufanya ziara za kurudia kwaweza kuwa jambo lenye kuchochea.—Mit. 22:29.
2 Kila Mkristo aliyejiweka wakfu apaswa ahisi akiwa na jukumu la kushiriki katika kazi ya kufanya wanafunzi. Huenda hilo likataka tuweke kando mambo yanayoweza kutufurahisha ili tushiriki tumaini la Ufalme na wengine. Ziara za kurudia hutupatia fursa ya kusaidia watu wanyoofu watosheleze mahitaji yao ya kiroho.
3 Fuatia Wote Wanaopendezwa: Ziara za kurudia zapaswa zifanywe kwa wote wanaoonyesha kupendezwa na ujumbe wa Ufalme, hata ingawa huenda wasichukue vichapo vyetu. Kuna watu wengi wanaoonyesha kupendezwa kwa kutaka tuzungumze habari za Biblia pamoja nao. Yesu na mitume walionyesha jinsi kupendezwa na ujumbe wa Ufalme kwaweza kusitawishwa kwa kuzungumza na watu habari hususa za Kimaandiko.—Mk. 10:21; Mdo. 2:37-41.
4 Kusudi letu la kurudi lapaswa liwe kuanzisha funzo la Biblia. Huenda tukaweza kumwonyesha mwenye nyumba jinsi funzo la Biblia huongozwa. Unaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atajibu sala yako ya kuomba msaada katika kumpata mtu mwenye moyo mnyoofu wa kufundisha. Yehova atabariki jitihada zako nyingi katika utumishi wake. Kwa nini usitafute msaada wa Yehova na uwe na mradi wa kuanzisha funzo la Biblia?
5 Tumia Trakti Ifaavyo: Trakti zaweza kutumiwa kwa matokeo katika kuanzisha funzo la Biblia. Wengi wamefanikiwa kuanzisha mazungumzo kwa kuzungumzia tu picha iliyo kwenye jalada. Soma pamoja na mwenye nyumba fungu moja baada ya nyingine. Swali linapoulizwa, tua na kumwalika mwenye nyumba atoe jibu. Soma maandiko na uonyeshe jinsi yanavyotumika. Halafu mazungumzo yanaweza kuelekezwa kwenye kichapo ambacho funzo laweza kuongozwa kwacho.
6 Tumia Kitabu Kutoa Sababu: Ziara za kurudia zenye matokeo zaweza kufanywa kwa kutumia kitabu Kutoa Sababu. Kupitia orodha ya habari kuu au faharisi kwaweza kukusaidia kuchagua habari inayofaa ya kuzungumzia unapoendeleza mazungumzo ya wakati uliopita. Sehemu ya “Maandiko Ambayo Mara Nyingi Hutumiwa Kimakosa” yaweza kusaidia katika kushughulika na vipingamizi vinavyoweza kuzuka. Mapainia wanaripoti mafanikio mengi katika kuanzisha mafunzo ya Biblia kwa kutumia habari kama ile iliyo katika kitabu Kutoa Sababu ukurasa 184 chini ya “Mashahidi wa Yehova hutumia njia gani ya kueleza Biblia?” Wao humwonyesha mtu anayependezwa jinsi tunavyoacha Biblia ijieleze yenyewe. Hilo hufanikiwa na limetokeza kuanzishwa kwa hesabu fulani ya mafunzo ya Biblia.
7 Kama vile Yesu na mitume, tunahitaji kuonyesha kupendezwa na kondoo za Yehova kwa moyo mweupe. (Lk. 9:11) Upendo kwa watu utatusaidia kuwafikia na kweli za Ufalme. (2 Kor. 2:17) Tunapoweka mkazo mwingi juu ya kujitoa wenyewe kwa ajili ya hali njema ya kiroho ya wengine, tunaweza kutimiza takwa la kufanya ziara za kurudia.