Wasaidieni Watoto Wamtumikie Yehova Kutoka Moyoni
1 Sulemani alijulisha kwamba “wana ni urithi kutoka kwa Yehova.” (Zab. 127:3-5, NW) Kwa kweli, wao ni urithi wenye thamani kubwa sana. Wazazi wana daraka walilopewa na Mungu la kuwafunza, kuwazoeza, na kuwatia nidhamu watoto wao. Hilo latia ndani kuwazoeza katika huduma, kuwatia moyo watoto kuzungumza kutoka moyoni kuhusu Yehova na Ufalme.—Efe. 6:4.
2 Wazazi wanapaswa kuanza mazoezi hayo katika umri gani? Jibu la Biblia ni wazi: Yapasa iwe kuanzia utoto. (2 Tim. 3:14, 15) Kadiri mazoezi hayo yaanzavyo mapema, ndivyo inavyoelekea zaidi kwamba watoto watasitawisha msingi imara katika kweli na kufanya huduma iwe kazi-maisha yao. Mazoezi hayo ya mapema yatatumika pia kuwalinda wasiwe na mafikira na mitazamo ya kilimwengu.
3 Wengi ambao bado hawajaanza shule wameonyesha uwezo mkubwa wa kuzoelea stadi zilizo ngumu. Uwezo huo wa kujifunza katika umri mchanga wapaswa uelekezwe kwenye kuwazoeza katika stadi zinazoleta kibali cha Yehova. (w88-SW 8/1 uku. 15; w89-SW 12/1 uku. 31) Wengi walio wachanga wamefanya maendeleo kufikia kuwa wahubiri wasiobatizwa. Watoto wengine hujitoa wakfu na kubatizwa kabla ya kuingia miaka ya utineja. Hilo limewafungulia njia kutumika wakiwa mapainia wasaidizi na hata mapainia wa kawaida kabla ya kumaliza shule. Ili kutimiza miradi hiyo, wanahitaji kufundishwa kuzungumza na watu kuhusu habari mbalimbali za Biblia.
4 Baadhi ya watu wazima wenye mbetuko wa kuona vijana wa leo kwa ujumla kuwa wajeuri na wasio na staha huenda wasipendezwe kuzungumza na kijana anayebisha mlangoni pao. Mhubiri kijana anaweza kusema nini mlangoni ili kushinda kizuizi hicho na kupata kusikilizwa na mwenye nyumba aliye mtu mzima? Mhubiri mmoja kijana alitumia jambo kama hili: “Habari ya asubuhi, jina langu ni ________. Ninawazuru majirani wangu leo kwa sababu wengi wanahangaika kuhusu wakati ujao. Ukiwa mtu mzima, kwa hakika wewe una ujuzi mwingi zaidi kuhusu maisha zaidi yangu. Hata hivyo, hapa pana andiko ambalo ni lenye kutufariji sisi sote.” Baada ya kusoma Ufunuo 21:3, 4, mazungumzo yaweza kukazia trakti Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani.
5 Dokezo jingine ni: “Jambo, jina langu ni ________. Ninafanya ziara fupi katika ujirani kwa sababu ninajua watu wengi wazima wanahangaika kuhusu mwelekeo ambao vijana wanaonekana wakifuata leo. Nyakati nyingine vijana huonyesha mtazamo usio na staha, hata wenye uasi. Lakini ninashiriki andiko fulani linaloonyesha jinsi siku fulani kila mtu atajifunza kuishi pamoja kwa amani.” Halafu soma Zaburi 37:11 na utoe maelezo ifaavyo. Wenye nyumba walio watu wazima wasikiapo maelezo hayo manyoofu ya wahubiri wetu vijana, kwa hakika wengi wao watavutiwa kwa njia ifaayo.
6 Maelfu ya wahubiri wachanga wanaendelea kushiriki vema katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Wao wanastahili kupongezwa kwa uchangamfu. Vijana waliozoezwa kutoka uchanga na wazazi wenye kumhofu Mungu huitikia kwa utayari kitia-moyo cha kweli kuwa wajitahidi kuwa na ushiriki kamili zaidi katika sehemu zote za huduma. Wale walio shuleni wana fursa ya kipekee ya kutoa ushahidi kwa wanafunzi wenzi na pia walimu. Wengi wamefurahia mambo yaliyoonwa yenye kuridhisha wakitoa ushahidi katika eneo hilo la kipekee.
7 Kwa hiyo saidieni wahubiri wachanga katika kundi lenu watumie kwa faida fursa ya kumtumikia Yehova wakiwa na idili ya ujana, wakimsifu kutoka moyoni.—Mhu. 12:1.