Sababu gani Mungu wa upendo atalipa kisasi?
“Mungu ni upendo.”—1 Yohana 4:8.
1. Ni jambo gani litakalotuwezesha tufahamu kwamba maneno ya kichwa chetu yanapatana yajaposikika kutopatana?
KISASI? Kutoka kwa Mungu mwenye upendo? Hilo laweza kuwaje? Je! wazo la Mungu mwenye upendo akilipa kisasi si lenye kutopatana? Inaweza kuonekana hivyo. Walakini acheni tufikirie sifa za upendo anazoonyesha Muumba, ndipo tutafahamu wazi zaidi namna jambo hilo linavyohusiana na kisasi chake.
2. Ni kwa sababu gani tunaweza kusema kwamba upendo wa Mungu ni wa hali ya juu zaidi, nayo ni mipango gani mingine yake ya upendo ambayo kwayo twapaswa kushukuru? (Zab. 136:1-6)
2 Tunapozungumza juu ya upendo wa Mungu, twaweza kusema kwamba ni wa hali ya juu zaidi. Nao umeonyeshwa kwetu katika njia nyingi. Ebu ifikirie, kwa mfano, dunia ambayo juu yake tunaishi. Biblia yasema kwamba dunia ni ‘zawadi ya Mungu kwa wanadamu.’ (Zab. 115:16, NW) Ebu fikiria namna Mungu alivyoitayarisha sayari hii kwa njia yenye upendo kwa ajili yetu. Mungu aliiweka angani ili ipate kadiri inayofaa ya joto na mwangaza kutoka kwa jua, akaipamba kwa majani mabichi na maua yenye rangi rangi. Na kwa sababu ya upendo wake, Mungu aliipa dunia yetu wanyama, ndege na samaki wengi, naye akatoa wingi wa nafaka na namna nyingine za chakula.—Zab. 104:1, 13-15.
3. Mungu alionyeshaje upendo katika kutuumba sisi wanadamu?
3 Hata hivyo, upendo wa Mungu kwetu hauonyeshwi tu katika vitu alivyotuumbia; unaonyeshwa vilevile katika njia aliyotuumba sisi. Alituumba tupate kufurahia uumbaji wake. Mtunga zaburi huyo anaeleza vizuri jambo hilo anaposema: “Ee Yehova, . . . Nitakusifu wewe kwa sababu kwa njia yenye kutia hofu nimeumbwa kiajabu. Kazi zako ni za ajabu”! (Zab. 139:1, 14, NW) Kwa sababu ya ukarimu na upendo wake, Mungu alitupa macho tuone uzuri wa ulimwengu unaotuzunguka, masikio ya kufurahia sauti ya muziki na sauti za watu, pua za kunusa harufu ya chakula na harufu tamu ya maua. Na kilicho bora kuliko vyote ni akili ya kibinadamu, ambayo inafikiri, kukumbuka na kusawazisha utendaji wa mwili. Hakika, tunastaajabia namna Mungu alivyoiumba miili yetu akiipa kwa wingi sana viungo vilivyohitajiwa. Kweli kweli, “Mungu ni upendo.”—1 Yohana 4:8.
Upendo wa Mungu waenda kuokoa
4. Upendo wa Mungu ulionyeshwaje katika paradiso ya Edeni?
4 Mungu alipomwumba mtu wa kwanza, Adamu, alimweka katika paradiso yenye kupendeza sana ya Edeni. Adamu aliona furaha kama nini katika wingi wa mipango ya upendo wa Mungu iliyomzunguka! Baadaye, Mungu alimwumba Hawa naye akamleta kwa Adamu. Na Hawa alipendezwa kama nini, katika siku yake ya kwanza ya kuwa hai, kuunganishwa pamoja na mume na kichwa ambaye angemlinda na kumwongoza! Wakiwa pamoja wangetarajia kutimiza mapenzi ya Mungu katika kufanya dunia iwe nzuri na kuijaza, na kutawala kwa upendo viumbe wanyama. Loo! ni wakati ujao ulio bora kama nini ambao Mungu aliweka mbele yao!
5. (a) Wazazi wetu wa kwanza walikujaje kuwa wasiostahili upendo wa Mungu (b) Hata hivyo upendo wa Mungu ulionyeshwaje kwa wazao wao?
5 Hata hivyo, kwa kusikitisha, huo wakati ujao haungetokea, angaa kwa hao. Kiumbe wa roho mwasi alijiondoa katika upendo wa Mungu, akajifanya mwenyewe kuwa Shetani Ibilisi. Ibilisi huyo alimshawisha Hawa, na kupitia kwa Hawa, Adamu, ili ‘wafanye yao wenyewe.’ Hivyo, walichukua mwendo wa kichoyo, wa kutomtegemea Muumba wao. Lakini kwa kufanya hivyo, walijionyesha wenyewe kuwa hawastahili upendo wa Muumba wao. Kwa hiyo kwa kufaa Mungu alipitisha hukumu ya kifo kwa watenda dhambi hao wa kukusudia. Hata hivyo, kwa sababu ya upendo wake kwa wanadamu, yeye aliwaruhusu waendelee kuishi mpaka wakazaa watoto, kama sivyo sisi hatungekuwa hai hivi sasa. Zaidi ya hayo, ingawa jamii ya kibinadamu sasa ilikuwa imerithi dhambi na mauti kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza, Mungu mwenye upendo alitoa msingi wa tumaini.—3:16-23; Rum. 8:20, 21.
6. Ni matangazo gani katika Edeni yaliyoonyesha upendo wa Mungu, na kwa namna gani?
6 Katika njia gani? Mara tu uasi ulipotokea, Mungu alijulisha kwamba angetokeza “Uzao,” akimtuma Huyo kutoka kwa tengenezo lake la kimbinguni lenye ushikamanifu ili kuondoa uharibifu wote uliotokezwa na Ibilisi, na Adamu na Hawa. Hata hivyo, huko nyuma katika Edeni, Mungu wetu mwenye upendo alitangaza kwamba angelipa kisasi juu ya Shetani na wale wote ambao wangejifanya sehemu ya uzao wa Shetani kwa kuuacha upendo wa Mungu.—Mwa. 3:15; Ufu. 12:9.
MUNGU WA UPENDO, NA WA KISASI
7. Kupatana na Kumbukumbu la Torati 32:43, sisi tuna sababu gani ya kufurahi?
7 Basi, Mungu wa upendo alijitangaza pia kuwa Mungu wa kisasi. Lakini kulipa kisasi juu ya adui zake lingekuwa jambo lenye kufaa. Namna gani hivyo? Kwa sababu kufanya hivyo kungefungua njia ili watu wote wanaompenda Mungu wafurahi, washangilie. Bila shaka, twaweza kufurahi sasa kwa kuwa Mungu atafungua njia ili tufurahie mpango wake wa uzima wa milele. Ebu angalia vile Mungu alivyomwongoza Musa aseme: “Furahini, enyi mataifa, pamoja na watu wake, kwa kuwa atalipiza kisasi cha damu ya watumishi wake, naye atalipa kisasi juu ya adui zake.”—Kum. 32:43, NW.
8, 9. (a) Kwa sababu ya upendo wake, Mungu anakusudia kufanya mambo gani mawili? (b) Katika kuonyesha upendo wake, Mungu ametoa zawadi gani iliyo nzuri sana?
8 Ndiyo, Mungu wetu mwenye upendo anakusudia kutetea enzi yake kuu na kuokoa wale wanaompenda kutokana na adui zao. Kwani, hata atatuokoa na adui mkubwa, kifo, kinachotujia maishani mwetu kwa kukirithi kutoka kwa baba yetu wa kwanza, Adamu. (Rum. 5:12) Walakini atafanyaje jambo hilo? Biblia inatuambia kwamba yeye atafanya jambo hilo kupitia kwa zawadi yake iliyo bora zaidi, Mwanawe. “Mungu ni upendo. Katika hili pendo la Mungu lilionekana kwetu, kwamba Mungu amemtuma Mwanawe pekee ulimwenguni, ili tupate uzima kwa yeye. Hili ndilo pendo, si kwamba sisi tulimpenda Mungu, bali kwamba yeye alitupenda sisi, akamtuma Mwanawe kuwa kipatanisho kwa dhambi zetu.”—1 Yohana 4:8-10; 1 Kor. 15:25, 26.
9 Kwa hiyo Mungu alimtoa Mwanawe Yesu Kristo ili atukomboe kutokana na kifo kinachotujia sisi kwa sababu ya dhambi iliyorithiwa kutoka kwa Adamu. Ndiyo, kama vile isemavyo Biblia katika Timotheo wa Kwanza 2:6, NW, Kristo “alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi unaolingana kwa ajili ya wote” ambao wangeonyesha imani katika yeye. Kwa hiyo Yesu aliweza kusema hivi kuhusu wafuasi wake wenye mfano wa kondoo: “Mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele,” ndiyo, uzima wa milele.—Yohana 10:10.
10. (a) Ni kwa sababu gani ‘Mungu wa upendo’ vile-vile ni Mungu wa “kisasi”? (b) Sababu gani ni Jambo la maana sana leo kwamba tumjue na kumtii Mungu?
10 Hata hivyo, kwa kurudia-rudia, Biblia inatuambia kwamba ‘Mungu wa upendo’ vilevile ni ‘Mungu wa kisasi.’ Kwa sababu gani? Kwa sababu upendo wa Mungu hauwezi kuvumilia uovu milele. (Nah. 1:2; Kum. 32:35, 41) Ndiyo sababu mtume Paulo anaandika juu ya “kufunuliwa kwake Bwana Yesu kutoka mbinguni pamoja na malaika wa uweza wake; katika mwali wa moto; huku akiwalipiza kisasi wao wasiomjua Mungu, na wao wasioitii Injili ya Bwana Yesu.” (2 The. 1: 6-9) Basi, ni jambo la maana kama nini kwamba tupate ‘kumjua Mungu!’ Katika ulimwengu huu uliovurugika wenye dini nyingi sana mbalimbali, ni jambo lenye maana kama nini, ‘kumtafuta Mungu wa kweli na kumpata kweli kweli’ kama isemavyo Biblia!—Matendo 17: 27, NW.
KUSAWAZISHA KISASI NA UPENDO
11, 12. (a) Ni hali gani iliyotokea mapema katika historia ya wanadamu, ikahitaji tendo gani kwa upande wa Mungu? (b) Kisasi cha Mungu wakati huo kilisawazishwaje na upendo wake?
11 Hata hivyo, ebu turudi kwenye mianzo ya historia ya wanadamu. Kufanya hivyo kutatusaidia kuelewa vizuri uhusiano kati ya upendo wa Mungu na kisasi chake. Kwa upendo, Mungu alikuwa ameruhusu uzao wa Adamu uongezeke, walakini wanadamu waliopotoka hawakuitikia upendo huo. Kwa hiyo, baada ya kama miaka 500, Yehova alimtuma nabii wake Henoko atangaze hukumu ya kimungu juu ya wanadamu waovu kwa sababu ya matendo yao ya kutomwogopa Mungu na mambo ya kuogopesha ambayo waliyasema juu ya Mungu. (Yuda 14, 15) Miaka mingine elfu ikapita, nao ulimwengu huo wa kale ukafikia kilele chake cha uasherati na jeuri. Kwa hiyo, Neno la Mungu lasema, “dunia ikaharibika mbele za Mungu, dunia ikajaa dhuluma. Mungu akaiona dunia, na tazama, imeharibika.—Mwa. 6:11,12.
12 Sasa, Mungu angefanyaje? Je! Mungu angelipa kisasi? Ndiyo! Na hata katika jambo hilo sifa yake ya upendo ikaonekana. Kwa nini tunasema hivyo? Wakati huo, kulikuwako jamaa moja tu juu ya dunia iliyokuwa imejitoa kufanya mapenzi ya Mungu. Ilikuwa jamaa ya Noa, mwanamume ambaye katika Biblia anaitwa “mhubiri wa haki.” Kwa upendo, Yehova alimwagiza Noa atengeneze safina “apate kuokoa nyumba yake.” Kisha ikaja gharika ya duniani pote ikafutilia mbali jirani waovu wa Noa. (2 Pet. 2:5, NW; Ebr. 11:7) Dunia yote ilisafishwa isiwe tena na jeuri yenye kuharibu pamoja na uasherati, hata ikawa tena mahali panapofaa jamaa ya wanadamu ipate kuongezeka tena.—Mwa. 6:9, 22; 7:21-23; 8:15-17.
13. Je! hukumu ya Yehova juu ya Sodoma na Gomora ilikuwa kukosa kuonyesha upendo, na sababu gani wajibu hivyo?
13 Hata hivyo, maelekeo ya dhambi yaliyorithiwa kutoka kwa Adamu yalibaki na upesi wanadamu wasiomwogopa Mungu wakaanza kuonyesha tabia mbaya tena. (Zab. 51:5) Chukua, kwa mfano, watu wa Sodoma na Gomora, walioishi katika wilaya ambayo wakati mmoja ilikuwa “kama bustani ya [Yehova].” Biblia inatuambia kwamba watu wa Sodoma walikuwa wabaya [sana], wenye kufanya dhambi nyingi sana juu ya [Yehova].” Watu wa namna moja walikuwa wanalalana, na kufanya jeuri katika kutosheleza tamaa zao. (Mwa. 13:13; 19:11) Mungu mwenye upendo, Yehova, aliazimia kuharibu miji hiyo, ili kwamba Abrahamu mwenye haki na mpwa wake Loti wasitaabishwe tena na jirani hao wabaya. Kama vile linavyosema Mwanzo 18:25, NW, “hakimu wa dunia yote,” Yehova, alifanya ‘yaliyokuwa haki.’ Alimwokoa Loti na binti zake wawili, bali akanyesha moto yenye kuharibu juu ya Sodoma na Gomora, akisafisha wilaya yote hiyo.—Luka 17:29; Yuda 7.
14, 15. (a) Wakanaani walikuwa wasio na hatia kadiri gani? (b) Je! Mungu alikuwa na haki ya kulipa kisasi Juu yao?
14 Miaka mingi baadaye, kwa mara nyingine tena Yehova alifanya “yaliyo haki,” kwa watu wake, Israeli. Namna gani? Kwa kufanya mpango wa kuwafukuza Wakanaani kutoka katika Nchi ya Ahadi.(Kum. 18:9-12) ‘Lakini je! hiyo haikuwa kuwatendea isivyofaa Wakanaani hao wasio na hatia? ’ mtu fulani aweza kuuliza. Wakanaani wasio na hatia? Hawakuwa bila hatia hata kidogo! Wakanaani hao walikuwa wamekuwa wenye kuchukiza sana katika kufanya ngono kwa watu wa jamaa moja, uzinzi, kutoa dhabihu watoto wao, kulalana kwa watu wa namna moja pamoja na kulala na wanyama. Kwa mfano, katika kuiabudu miungu yao ya uongo walikuwa wakiwatoa watoto wao kuwa dhabihu kwa kuwatupa katika moto wakiwa hai. Vilevile walikuwa na makahaba wanaume na wanawake mahekaluni mwao.a Kwa hiyo, Yehova aliwaagiza watu wake hivi: “Msijitie unajisi katika mambo hayo hata mojawapo; kwa maana hizo taifa nitakazozitoa mbele zenu zimekuwa najisi kwa mambo hayo yote; na hiyo nchi imekuwa najisi; kwa ajili ya hayo naipatiliza uovu wake juu yake, na hiyo nchi yatapika wenyeji wake na kuwatoa.”—Law. 18:1-25.
15 Kwa mara nyingine, ilikuwa kwa sababu ya kuwapenda watu wake mwenyewe kwamba Yehova aliwaamuru Israeli wawafagilie mbali wakosaji hao. Njia yao chafu ya maisha ilihatirisha watu wake. Ilikuwa kama vile inavyosema Biblia “jambo lenye kuchukiza kwa Yehova.” Kwa haki, basi, kisasi cha Mungu kiliwaka juu yao.—Zab. 106:34-40; Kum. 18:12, NW.
16. Israeli walionyeshwaje upendo na subira ya Mungu?
16 Kwa upande mwingine, Mungu alishughulikaje na watu wa Israeli? Yehova aliwaonyesha upendo mwingi sana. Musa analieleza jambo hilo kwa maneno haya mazuri sana katika Kumbukumbu la Torati 32:11 na 12, ZSB: “Kama tai anayeshutusha kioto chake, na kupigapiga mabawa yake juu ya watoto wake, akanyosha mabawa yake, akawatwaa, akawachukua juu ya mabawa yake: [Yehova] tu akamwongoza, wala mungu mugeni hakuwa pamoja naye.” Walakini, ole wao! Muda si muda miungu ya kigeni ilipenyeza katika Israeli, hata kwamba Mungu ambaye alikuwa ametangaza kwamba angelipa kisasi juu ya adui zao akalazimika kulipa kisasi juu ya watu wake mwenyewe. Walakini Yehova alikuwa mwenye subira kwa Israeli kama nini! Kwa miaka 900 alivumilia upotovu wao. Katika wakati huo wote Yehova aliwaonyesha rehema. “Sikufurahii kufa kwake mtu mwovu,” akatangaza Yehova Mungu, “bali aghairi mtu mwovu, na kuiacha njia yake mbaya, akaishi. Ghairini, ghairini, mkaache njia zenu mbaya; mbona mnataka kufa, Enyi nyumba ya Israeli?”—Eze. 33:11.
17. (a) Israeli walipewa onyo gani na Mungu? (b) Kisasi ambacho Mungu alilipa juu ya Israeli kilichanganywaje na upendo wake?
17 Kwa upendo, Mungu aliwaonya mara nyingi juu ya matokeo ya ibada yao ya sanamu, uasherati wao na kumwaga damu isiyo na hatia. Hata hivyo, mwishowe, Yehova alilazimika kulipa kisasi juu ya Israeli kwa kumruhusu Mfalme Nebukadreza wa Babeli aharibu Yerusalemu na hekalu lake. Waokokaji walichukuliwa mpaka Babeli. Hata hivyo, baada ya miaka 70 Mungu aliongoza kupinduliwa kwa Babeli ili mabaki wenye kuthamini ya Waisraeli yaweze kurudi kwenye nchi yao na kuanza tena ibada safi huko.—2 Fal. 24:3, 4; 2 Nya. 36:12-21; Ezra 1:1-3; Ebr. 12:6.
YESU HUSEMA JUU YA UPENDO NA KISASI
18. Yesu alisema nini kuhusu (a) upendo wa Mungu, na (b) kisasi chake?
18 Yesu Kristo alikuwa na jambo gani la kusema juu ya upendo na kisasi cha Mungu? Yeye alisema kwa uchangamfu sana juu ya upendo wa Babaye, hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu [wa wanadamu], hata akamtoa Mwanawe pekee, ili kila mtu amwaminiye asipotee, bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Lakini je! yeye alisita kusema juu ya kisasi cha Mungu? Hata kidogo! Kwa kuwa Biblia husema kwamba Yesu, kama vile Babaye, ‘alipenda haki, akachukia uasi.’ (Ebr. 1:9; Zab. 11:5, 7) Yesu hakupunguza uzito wa maneno hata wakati mmoja alipozungumza na viongozi wa kidini Wayahudi wa siku zake au alipozungumza juu yao. Mara tatu katika Mahubiri ya Mlimani yake aliwaita “wanafiki.” (Mt. 6:2, 5, 16) Aliwaambia hivi hao viongozi wa kidini: “Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi,” hivyo akawashirikisha na ‘uzao wa nyoka.’ (Yohana 8:44; Mwa. 3:15) Kisha, siku tatu tu kabla hajauawa, Yesu aliwakanusha viongozi hao wa kidini Wayahudi mbele ya watu wote, akisema: “Enyi nyoka, wana wa majoka, mtaikimbiaje hukumu ya jehanum?”—Mt. 23:13-33.
19. (a) Ni kwa sababu gani maoni ya Yesu yalikuwa yenye upendo sana na vilevile ujumbe wake wenye onyo? (b) Lakini kwa haki Yehova alitendaje?
19 Je! hiyo ilimaanisha kwamba Yesu hakuwa akionyesha upendo? Sivyo, hata kidogo. Kwa kuwa, ijapokuwa Yesu alijua kwamba Wayahudi hao walikuwa karibu kuongeza hatia yao ya damu kwa kumwua yeye, hata hivyo, yeye aliendelea kusema hivi katika Mathayo sura ya 23: “Ee Yerusalemu, Yerusalemu, uwauaye manabii, na kuwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwako! Ni mara ngapi nimetaka kuwakusanya pamoja watoto wako, kama vile kuku avikusanyavyo pamoja vifaranga vyake chini ya mabawa yake, lakini hamkutaka! Angalieni, nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.” (Mt. 23:37, 38; Matendo 3:13-15) Miaka 37 baadaye, jeshi la Rumi chini ya jemadari Tito liliteka nyara Yerusalemu na kuharibu hekalu lake. Huo ulikuwa msiba ambao katika huo watu wake waasi 1,100,000 walikufa! Ndipo, wakati huo, maneno ya unabii wa Yesu yakaonekana wazi wazi katika nguvu zake zote. Kwa haki, Yehova alikuwa amelipa kisasi!
20. Kwa habari ya upendo na kisasi, ni mambo gani yenye kupendeza yanayopatikana katika Isaya 61:1, 2
20 Karne nyingi zilizopita, Isaya, mmojawapo wa manabii anayeripotiwa kuwa aliuawa katika Yerusalemu wa kale, alisema maneno haya: “Roho ya Bwana Yehova Mwenye Enzi Kuu i juu yangu, kwa sababu Yehova amenitia mafuta nisimulie habari njema kwa wapole . . . kutangaza mwaka wa nia njema upande wa Yehova na siku ya kisasi upande wa Mungu wetu; kufariji wote waombolezao’’—Isa. 61:1, 2, NW.
21. (a) Ni nini inayoweza kuwa sababu ya Yesu ya kutaja sehemu tu ya Isaya 61:1, 2? (b) Ni ulizo gani linalotokea kuhusu Isaya 2:2-5?
21 Yesu alisoma sehemu ya unabii wakati wa mwanzo wa huduma yake, naye akautumia juu yake akiwa Mtiwa Mafuta Mkuu wa Yehova. (Luka 4:18-21) Hata hivyo, wakati Yesu alipotaja maneno hayo ya Isaya yeye hakutaja siku ya Mungu ya kisasi. Sababu gani? Kwa wazi mkazo mkubwa juu ya kutangaza siku ya Mungu ya kisasi ungekuja “katika siku za mwisho,” kama vile Isaya sura ya 2 inavyosema. Je! sisi sasa tumefika wakati huo?
[Maelezo ya Chini]
a Angalia pia kitabu Aid to Bible Understanding, kurasa 76, 145 na 287, chini ya “Anathi,” “Ashtorethi” na “Kanaani, Mkanaani.”
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
“Ee Yehova, kazi zako ni nyingi kama nini! Vyote umevifanya kwa hekima. Dunia imejaa uumbaji wako. . . . Mbariki Yehova, Ee nafsi yangu. Msifuni Yah, enyi watu!”—Zab. 104:24, 25, NW.
[Sanduku katika ukurasa wa 4]
ZAWADI KUU ZAIDI YA UPENDO WA MUNGU
Kwa sababu ya upendo wake mwingi kwa wanadamu wenye kuteseka, Mungu alikuwa na nia ya kutoa mali yake ya thamani zaidi, mwenzi wake wa karibu zaidi, “stadi wa kazi” pamoja naye katika uumbaji, yeye aliyekuwa ‘furaha yake kila siku” awe dhabihu. Alikuwa tayari kumtuma Mwanawe mzaliwa wa kwanza wa kimbinguni aje chini katika dunia hii, apatwe na masuto yote, kuvunjiwa heshima na ukatili ambao Ibilisi na watumishi wake wangemwonyesha. Akiwa chini ya jaribu, Mwana huyo angethibitisha kwamba, akiwa mwanadamu mkamilifu, angeweza kushikilia enzi kuu ya Mungu chini ya majaribu makali zaidi, hata kufa kwenyewe. Zaidi ya hayo, kwa njia hiyo angetoa “nafsi yake iwe [ukombozi] kwa wengi” kwa ajili ya wengi wa wanadamu wenye dhambi ambao wangemwamini. (Mit. 8:30; Mt. 20:28) Kwa hiyo Yesu aliweza kusema hivi kwa habari ya wafuasi wake wenye mfano wa kondoo, wale wa “kundi dogo” na “kondoo wengine” wake: “Nami nawapa uzima wa milele; wala hawatapotea kamwe.” Wengi wao wangeupata uzima huo kwa kufufuliwa kutoka kwa wafu. (Luka 12:32; Yohana 10:16, 28; 5:28, 29) Hizo ni fadhili zisizostahilika kama nini, walizooyeshwa wanadamu wasiojiweza! Tukiudharau mpango huo wa upendo, hakika tungestahili kupatwa na hasira ya kisasi cha Mungu!
[Sanduku katika ukurasa wa 5]
UZIMA WETU UNAITEGEMEA!
Watu wengi wanazaliwa katika dini. Walakini je! hiyo inamaanisha kwamba wanaabudu Mungu wa kweli? Badala yake, je! dini ya wengi si jambo linalotokana tu na kuzaliwa? Walakini uzima wetu unategemea ‘kumjua Mungu na kuzitii habari njema juu ya Bwana Yesu,’ aliyemtuma ili atukomboe sisi kutoka kwa dhambi na mauti. (2 The. 1:8; Marko 10:45) Ni wazi kabisa kwamba ulimwengu unaotuzunguka ‘haumjui Mungu.’ Biblia inasema waziwazi kwamba kuna “Mungu mmoja, naye ni Baba wa wote.” (Efe. 4:6) Hata hivyo, wamegawanyika katika kuabudu miungu mingi ya kidini. Kuna mabuddha, miungu ya mababu ya dini ya Shinto na dini ya Confucius, Allah wa Waislamu, pia, Brahma, Vishnu na Siva—utatu wa Mabanyani—na utatu wa Jumuiya ya Wakristo wa Baba, Mwana na “Roho Mtakatifu.” Watu wengi hata wanaabudu watu mashuhuri, walio hai au waliokufa, kama vile mabingwa na kucheza “rumba,” mabingwa wa michezo na viongozi wa mapinduzi ya kisiasa.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
YALIYOVUMBULIWA NA UBUKUZI WA MAMBO YA KALE KATIKA KANAANI:
“Wakanaani waliabudu, kwa kufanya uasherati sana, kama sherehe ya kidini, mbele ya miungu yao; kisha, kwa kuwaua watoto wao wazaliwa wa kwanza, wawe dhabihu kwa miungu iyo hiyo. Inaelekea kwamba, kwa kadiri kubwa sana, nchi ya Kanaani ilikuwa kama Sodoma na Gomora katika taifa zima. . . . Je! watu wenye ukatili mchafu na wenye kuchukiza namna hiyo walikuwa na haki tena ya kuendelea kuwako? . . . Wabukuzi wa mambo ya kale ambao hubukua magofu ya miji ya Wakanaani wanashangaa kwamba Mungu hakuwaharibu mapema kuliko wakati ule alipowaharibu.”—“Halley’s Bible Handbook,” H. H. Halley, Uku. 161.
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
SIFA YA YEHOVA ILIYO BORA ZAIDI YA REHEMA
Hata alipoadhibisha kwa ukali sana taifa la Israeli lenye kuasi, Yehova alionyesha rehema, akasema hivi kupitia kwa nabii wake Yeremia: “Kwa kuwa [Yehova] hatamtupa mtu hata milele. Maana ajapomhuzunisha atamrehemu, kwa kadiri ya wingi wa huruma zake. Maana moyo wake hapendi kuwatesa wanadamu. Wala kuwahuzunisha.”—Omb. 3:31-33.